Thursday, March 20, 2025

WIZARA YA MADINI KUANZA UTOAJI HUDUMA NDANI YA JENGO JIPYA KUANZIA MEI 15

 










* Kamati ya Bunge Yasema ina matumaini Makubwa na Hatua iliyofikiwa, Wapongeza Serikali kutoa fedha


* Ujenzi Wafikia Asilimia 92.8


📍 Dodoma

Waziri wa Madini Mhe. Anthony Mavunde ameiambia Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na  Madini kwamba, ifikapo Mei 15, 2025, Huduma zote za Wizara Makao Makuu, zitaanza kutolewa katika Jengo Jipya la Wizara Mji wa Serikali- Mtumba baada ya michakato yote kukamilishwa.

Amesema hayo leo Machi 20, 2025, wakati wa ziara ya Kamati hiyo ilipotembelea kukagua maendeleo ya mradi huo ambapo ujenzi wake umefikia asilimia 92.8, huku kazi chache zilizobaki zikihusisha ukamilishaji wa masuala ya mifumo ya TEHAMA, zimamoto, rangi na samani za ndani ambapo tayari Wizara imekwisha kutangaza zabuni ya samani hizo.

‘’Mhe. Mwenyekiti, kukamilika kwa jengo hili kutaiwezesha Wizara kuwahudumia watanzania na wageni kutokea eneo moja na hivyo  kutoa huduma kwa urahisi kuliko ilivyo sasa ambapo baadhi ya watumishi wako kwenye maeneo mengine ikiwemo katika eneo la ilipo Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini Tanzania (GST) na hapa Mtumba,’’ amesema Mhe. Mavunde.

Ametumia fursa hiyo kuishukuru Serikali kwa kwa kuweka nguvu ili kukamilisha mradi wa Mji wa Serikali na kuweza kutoa kiasi cha shilingi bilioni 300 kwa ajili ya ujenzi wa mji huo na kueleza kuwa, uwepo wa mji huo utasaidia kurahisisha utoaji huduma kwa Serikali na kuongeza kwamba, umeongeza mwonekano  mzuri  wa mji  wa Dodoma huku akitolea mfano wa Nchi ya Malaysia kuwa na mfumo kama Mtumba.

Naye, Mwenyekiti wa Kamati hiyo Mhe. Dkt. David Mathayo amesema kwamba Kamati hiyo ina matumiani makubwa kutokana na hatua iliyofikiwa ya ujenzi wa jengo hilo na hivyo kutoa pongezi kwa Serikali kwa kutoa fedha kukamilisha majengo yaliyopo katika mji huo na kusema kwamba  uwepo wa Wizara zote katika mji huo utarahisisha utoaji huduma kwa wawekezaji na watanzania  kama ilivyo kwa nchi ya Brazil.

Katika hatua nyingine, Mhe. Dkt. Mathayo ameumwagia sifa uongozi wa Wizara ya Madini kutokana na namna wanavyosimamia shughuli za Sekta ya Madini na kueleza kuwa, kitendo hicho kinatoa ahueni kwa kamati hiyo ambayo inasimamia Wizara za Madini na Nishati.

‘’Tunawafahamu namna mnavyochapa kazi, kamati yetu tuna furahi tuna viongozi walionyooka, ni viongozi, wazoefu na wachapakazi. Hatuna shaka kama kamati tunafurahi kwasaabu mnaisimamia wizara vizuri,’’ amesema Dkt. Mathayo.

Awali, Mkurugenzi wa Idara ya Utawala na Rasilimali Watu Wizara ya Madini, Festus Mbwilo akisoma taarifa ya maendeleo ya mradi, ameieleza kamati kuwa Wizara imeendelea kusimamia kwa karibuni utekelezaji wa mradi huo ulioanzamwaka 2021 ili ukamilike kwa wakati ikiwemo kuchukua hatua za kukabiliana na changamoto zinazojitokeza

Mkandarasi wa jengo la Wizara ya Madini ni Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) na linajengwa kwa gharama ya shilingi bilioni 22.8 na Mshauri Elekezi ni Wakala wa Majengo Tanzania (TBA



MAJALIWA: HAKIKISHENI BIDHAA ZINAZOZALISHWA NCHINI ZINAKIDHI VIWANGO








WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa ameziagiza taasisi za kudhibiti viwango nchini zihakikishe uzalishaji wa bidhaa  zote zinazozalishwa zikiwemo za afya zinakidhi ubora unaotakiwa na kuweza kushindana katika masoko ya kimataifa.

Ametoa agizo hilo leo (Alhamisi, Machi 20, 2025) baada ya kuweka jiwe la msingi la ujenzi wa mitambo ya kuzalisha oksijeni kwa matumizi ya hospitali, ambapo amesisitiza kuwa soko linatakiwa liwe na bidhaa salama, bora, na zinazokubalika kimataifa. Mitambo hiyo inajengwa katika ofisi za TOL Gases, Temeke Dar es Salaam.

Amesema mradi huo utakapokamilika utazalisha lita milioni 4.1 za oksijeni ya matibabu kwa mwaka kuanzia mwaka 2026. “Hatua hii itaboresha upatikanaji wa oksijeni katika hospitali na vituo vya afya, pamoja na kupunguza gharama za oksijeni ya matibabu kwa asilimia 35 katika hospitali na vituo vya afya kote nchini, hivyo kuimarisha huduma za afya kwa wananchi”.

Aidha, Waziri Mkuu amesema mradi huu unaunga mkono juhudi endelevu za Serikali za kuhakikisha oksijeni kwa ajili ya matibabu inapatikana kwa urahisi katika kila kituo cha huduma za afya nchini. 

“Mradi huu utaongeza upatikanaji wa oksijeni katika hospitali na zahanati nchini na kupunguza vifo vitokanavyo na magonjwa ya kupumua ikiwa ni pamoja na kupunguza vifo vya akina mama na kuokoa ya watoto wa Taifa hili.”

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Afya, Dkt. Godfrey Mollel amesema mradi huo ni muhimu kwa sababu oksijeni inayozalishwa kwa njia hiyo inakuwa na viwango vya ubora, hivyo itasaidia kuimarisha huduma za afya zitolewazo nchini pamoja na kupunguza vifo.

Awali, Mkurugenzi Mtendaji wa TOL Gases, Daniel Warungu ametumia fursa hiyo kuipongeza Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kujidhatiti katika kuboresha utoaji wa huduma za afya kwa Watanzania.

Amesema kampuni ya TOL inajivunia kushirikiana na Serikali katika miradi mbalimbali ya kuboresha huduma za afya, hususani upatikanaji na usambazaji wa gesi ya oksijeni kwa ajili ya matibabu ukiwemo mradi wa shilingi bilioni 9.8 wa ufungaji wa mifumo ya usambazaji gesi wodini katika vituo 129 vya huduma za afya nchini kote

MHE. RAIS DKT. SAMIA SULUHU HASSAN AKUTANA NA MJUMBE MAALUM WA RAIS WA MISRI






Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, amekutana na kufanya mazungumzo na Mjumbe Maalum wa Rais wa Misri, Mhe. Badr Abdelatty, ambaye pia ni Waziri wa Mambo ya Nje, Uhamiaji na Wamisri Waishio Nje wa Jamhuri ya Kiarabu ya Misri, tarehe 20 Machi 2025, katika Ikulu Ndogo ya Tunguu, Zanzibar.

Mazungumzo haya yamejikita katika kuimarisha uhusiano wa kihistoria na ushirikiano wa kimkakati kati ya Tanzania na Misri, hususan katika nyanja za biashara, uwekezaji, nishati, kilimo, miundombinu, na maendeleo ya sekta ya maji.

🌍 Ushirikiano wa Kidiplomasia na Kimaendeleo
Mkutano huu umeendeleza dhamira ya Mataifa haya mawili kushirikiana kwa karibu katika kukuza uchumi, kuimarisha amani na usalama wa kikanda, pamoja na kuhamasisha maendeleo endelevu kwa manufaa ya wananchi wa Tanzania na Misri.

Mhe. Badr Abdelatty ameeleza dhamira ya Serikali ya Misri kuendelea kuwekeza Tanzania na kushirikiana katika miradi mbalimbali inayolenga kuinua sekta za kimkakati, hususan kupitia uwekezaji wa moja kwa moja (FDI), ushirikiano wa kiufundi, na mipango ya maendeleo ya pamoja.

Kwa upande wake, Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan amepongeza ushirikiano wa muda mrefu kati ya Tanzania na Misri na kueleza kuwa Serikali yake itaendelea kuimarisha mazingira rafiki kwa uwekezaji na biashara baina ya mataifa haya mawili.

🤝 Tanzania na Misri Zinaimarisha Uhusiano wa Kihistoria!
Mazungumzo haya yameongeza msukumo mpya katika ajenda za maendeleo kati ya Tanzania na Misri, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuhakikisha mataifa haya mawili yanajenga mahusiano thabiti na endelevu kwa ustawi wa wananchi wake.

#DiplomasiaYaUchumi 🇹🇿🇪🇬 #TanzaniaNaMisri #UshirikianoImara #TunajengaMataifaYet

TAZARA SASA KUENDESHWA NA WACHINA MIAKA 30



KITWE, Zambia MAMLAKA ya Reli ya Tanzania na Zambia (TAZARA) imetangaza kuwa Kampuni ya China Civil Engineering Construction Corporation (CCECC) itachukua usimamizi na uendeshaji wa reli hiyo kwa kipindi cha miaka 27. 

Makubaliano haya, yenye thamani ya Dola bilioni 1.4 yatatoa fursa ya kurekebisha miundombinu ya reli na kuboresha ufanisi wake.

Mkurugenzi Mtendaji wa TAZARA, Mhandisi Bruno Ching'andu amesema sehemu ya uwekezaji utajumuisha ukarabati wa reli, pamoja na ununuzi wa vichwa vipya na mabehewa. Hatua hii inatarajiwa kuboresha usalama na kupanua uwezo wa usafirishaji wa abiria na mizigo.

Mkataba huu wa miaka 30 utalenga kutoa huduma bora zaidi na kudumisha operesheni za TAZARA. Serikali za Tanzania na Zambia zinatarajia kuwa mradi huu utaongeza biashara na kuimarisha usafiri kati ya nchi hizi mbili.

Kampuni ya CCECC itasimamia uendeshaji wa reli hiyo kwa miaka 27 ijayo, huku TAZARA ikifanya kazi kwa karibu kuhakikisha utekelezaji mzuri wa mradi huu.

SOURCE: HABARILEO | KITWE, Zambia MAMLAKA: ya Reli ya Tanzania na Zambia (TAZARA) imetangaza kuwa Kampuni ya China Civil Engineering Construction Corporation... | Instagram

Monday, March 17, 2025

RAIS SAMIA AIMWAGIA SIFA WIZARA YA ARDHI KWA KUSIMAMIA USTAWI WA WATANZANIA

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan, Ameishukuru Wizara ya ardhi, nyumba na maendeleo ya makazi chini ya Waziri wake Mhe. Deogratius Ndejembi, kwa kusimamia na kuratibu vyema maandalizi ya sera ya ardhi, akiipongeza pia kwa kubadilika kiutendaji na kuwa kinara katika utatuzi wa changamoto za ardhi na maendeleo ya watu.

Rais Samia ametoa pongezi hizo mapema leo Jumatatu Machi 17, 2025 Jijini Dodoma, wakati akizindua sera ya ardhi ya mwaka 1995 toleo la mwaka 2023, sera ambayo inatajwa kuwa muarobaini wa changamoto mbalimbali za ardhi pamoja na silaha muhimu katika uongezaji wa thamani ya ardhi kwa maendeleo ya watanzania.

RAIS DKT. SAMIA AZINDUA SERA MPYA YA ARDHI NA MFUMO WA e-ARDHI JIJINI DODOMA




Dodoma, Machi 17, 2025 – Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, leo amehutubia viongozi wa ngazi mbalimbali, wawakilishi wa taasisi za umma na binafsi, pamoja na wananchi kabla ya kuzindua rasmi Sera ya Taifa ya Ardhi ya mwaka 1995 Toleo la 2023 na Mfumo wa e-Ardhi. Hafla hiyo imefanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Jakaya Kikwete, jijini Dodoma, ikiwa ni sehemu ya jitihada za serikali kuboresha sekta ya ardhi nchini.

Katika hotuba yake, Rais Dkt. Samia amesisitiza kuwa maboresho katika sera ya ardhi yanatokana na mahitaji halisi ya wananchi, maendeleo ya kijamii na kiuchumi, pamoja na umuhimu wa kuendana na mabadiliko ya teknolojia.

"Marekebisho haya ya sera yanahakikisha kuwa kila Mtanzania anapata haki yake ya kumiliki ardhi kwa haki na uwazi zaidi. Tumejifunza kutokana na changamoto zilizokuwepo katika utekelezaji wa sera ya awali, na sasa tunaleta mfumo unaoendana na mazingira ya sasa ili kuondoa migogoro ya ardhi na urasimu," alisema Rais Dkt. Samia.

Aidha, alieleza kuwa kuzinduliwa kwa Mfumo wa e-Ardhi ni hatua kubwa inayolenga kurahisisha huduma za ardhi kwa kutumia teknolojia ya kidijitali. Mfumo huo utawezesha wananchi kupata huduma mbalimbali kwa njia ya mtandao, kama vile kuomba hati miliki, kulipia kodi ya ardhi, na kufuatilia maendeleo ya maombi yao bila kulazimika kwenda ofisi za ardhi.

"Mfumo huu utahakikisha kuwa wananchi wanapata huduma kwa haraka, kwa uwazi, na kwa gharama nafuu. Tunataka kila Mtanzania awe na uwezo wa kumiliki ardhi yake kihalali bila kuhangaika na urasimu wa muda mrefu," alisisitiza Rais.

Mageuzi Katika Sekta ya Ardhi

Akizungumzia sera mpya ya ardhi, Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Mhe. Deogratius Ndejembi, alieleza kuwa marekebisho ya sera ya ardhi yamezingatia masuala mbalimbali, ikiwa ni pamoja na kuongeza uwazi katika umilikaji wa ardhi, kuboresha usimamizi wa ardhi za vijiji, na kuweka utaratibu mzuri wa upangaji miji.

"Kupitia sera hii mpya, tumeimarisha mifumo ya upatikanaji wa ardhi kwa wote, kuhakikisha kwamba haki ya ardhi inalindwa na kwamba kila mwananchi anapata huduma stahiki kwa wakati," alisema Waziri Ndejembi.

Aidha, alisema kuwa mfumo wa e-Ardhi utaondoa urasimu uliokuwa ukisababisha ucheleweshaji wa huduma na migogoro mingi ya ardhi.

"Tumeanzisha mfumo huu wa kidijitali ili kuwezesha wananchi kutumia huduma za ardhi kwa njia rahisi zaidi. Hakutakuwa na haja ya kufanya safari ndefu kwenda ofisi za ardhi, kwani huduma zote zitapatikana mtandaoni," aliongeza Waziri.

Mwitikio wa Wananchi na Wadau wa Sekta ya Ardhi

Wadau mbalimbali wa sekta ya ardhi, wakiwemo wawakilishi wa mashirika ya serikali na binafsi, walieleza kuwa hatua hii ni mapinduzi makubwa katika sekta ya ardhi nchini.

Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Nyumba la Taifa (NHC), Bw. Nehemia Mchechu, alisema kuwa mfumo wa e-Ardhi utaongeza ufanisi katika upangaji wa makazi na maendeleo ya miji.

"Uwazi na ufanisi katika sekta ya ardhi ni muhimu kwa maendeleo ya sekta ya makazi. Mfumo huu mpya utasaidia wananchi na wawekezaji kupata taarifa muhimu kwa haraka na kwa njia ya uwazi," alisema Bw. Mchechu.

Wananchi waliohudhuria hafla hiyo pia walionesha furaha yao kwa uzinduzi huu, wakieleza kuwa mfumo wa e-Ardhi utawasaidia sana kupunguza gharama na muda wa kupata hati miliki za ardhi.

"Nilihangaika kwa muda mrefu kupata hati ya ardhi yangu, lakini kwa mfumo huu mpya, naamini itakuwa rahisi zaidi. Tunaishukuru serikali kwa kuleta mageuzi haya," alisema Bw. Juma Hassan, mkazi wa Dodoma.

Uzinduzi huu umehitimishwa kwa maonesho ya sekta ya ardhi, ambapo taasisi mbalimbali, zikiwemo Shirika la Nyumba la Taifa (NHC), Tume ya Mipango ya Matumizi Bora ya Ardhi, na Mamlaka ya Udhibiti wa Sekta ya Ardhi (LRRA), zilipata fursa ya kuonyesha miradi na huduma zao.

Kwa ujumla, kuzinduliwa kwa Sera ya Taifa ya Ardhi ya mwaka 1995 toleo la 2023 na Mfumo wa e-Ardhi ni hatua muhimu kuelekea usimamizi bora wa ardhi, utatuzi wa migogoro, na kuleta maendeleo ya kijamii na kiuchumi nchini.

Mwisho.

RAIS DKT. SAMIA AZINDUA SERA YA TAIFA YA ARDHI TOLEO LA 2023 NA MFUMO WA e-ARDHI JIJINI DODOMA














Dodoma, Machi 17, 2025 – Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, leo amezindua rasmi Sera ya Taifa ya Ardhi ya mwaka 1995 toleo la 2023 pamoja na Mfumo wa e-Ardhi katika hafla iliyofanyika kwenye Ukumbi wa Mikutano wa Jakaya Kikwete, jijini Dodoma.

Kabla ya uzinduzi huo, Rais Dkt. Samia alitembelea mabanda ya maonesho yaliyopo nje ya ukumbi huo, ambapo wadau mbalimbali wa sekta ya ardhi walikuwa wakionyesha shughuli na miradi yao inayolenga kuboresha usimamizi wa ardhi nchini. Miongoni mwa taasisi zilizoshiriki ni Shirika la Nyumba la Taifa (NHC), Mamlaka ya Udhibiti wa Sekta ya Ardhi (LRRA), Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, pamoja na taasisi nyingine za serikali na sekta binafsi.

Katika hotuba yake, Rais Dkt. Samia alisisitiza umuhimu wa sera mpya ya ardhi, akieleza kuwa maboresho yaliyofanyika yanalenga kuongeza ufanisi katika usimamizi wa ardhi, kupunguza migogoro ya ardhi, na kurahisisha upatikanaji wa hati miliki kwa wananchi.

"Sera hii mpya inaleta mageuzi makubwa katika sekta ya ardhi nchini. Tumejifunza kutoka changamoto zilizopita na sasa tunaweka misingi imara kwa ajili ya kizazi cha sasa na kijacho. Mfumo wa e-Ardhi ni hatua kubwa katika kuhakikisha kuwa huduma za ardhi zinapatikana kwa uwazi na kwa haraka zaidi," alisema Rais Dkt. Samia.

Mfumo wa e-Ardhi, ambao pia umezinduliwa rasmi leo, ni mfumo wa kidijitali unaolenga kurahisisha upatikanaji wa huduma za ardhi kwa njia ya mtandao. Mfumo huu utawezesha wananchi kuomba na kufuatilia hati miliki, kulipa kodi ya ardhi, na kupata taarifa za umiliki wa ardhi bila kulazimika kufika ofisi za ardhi.

Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Mhe. Deogratius Ndejembi, alieleza kuwa mfumo huu utaongeza uwazi, kupunguza urasimu, na kudhibiti changamoto za rushwa katika sekta ya ardhi.

"Kupitia mfumo wa e-Ardhi, tutahakikisha kuwa wananchi wanapata huduma kwa haraka na kwa ufanisi mkubwa. Tunataka kufikia wakati ambapo mtu anaweza kupata hati yake ya ardhi bila kulazimika kupoteza muda mwingi kufuatilia ofisini," alisema Waziri Ndejembi.

Shirika la Nyumba la Taifa (NHC), kama mdau mkubwa wa sekta ya ardhi, liliwasilisha miradi yake mikubwa inayoendelea kutekelezwa, ikiwemo Morocco Square, 711 Kawe, na Samia Housing Scheme Kawe. Miradi hii inadhihirisha dhamira ya serikali ya kuboresha sekta ya makazi kwa Watanzania.

Wananchi waliohudhuria uzinduzi huu walionesha furaha yao kuhusu maboresho haya makubwa katika sekta ya ardhi. Bi. Neema John, mkazi wa Dodoma, alisema kuwa mfumo wa e-Ardhi utasaidia kupunguza changamoto zilizopo katika kupata hati miliki.

"Awali, ilikuwa vigumu sana kupata hati miliki bila kuhangaika na urasimu. Tunashukuru kwa mfumo huu wa kidijitali kwani utarahisisha mambo na kupunguza gharama," alisema Bi. Neema.

Kwa ujumla, uzinduzi wa Sera ya Taifa ya Ardhi ya mwaka 1995 toleo la 2023 na Mfumo wa e-Ardhi ni hatua muhimu katika kuhakikisha kwamba sekta ya ardhi inakuwa ya kisasa zaidi, inawafikia wananchi wengi, na inachangia maendeleo ya taifa kwa ufanisi mkubwa.

WIZARA YA MADINI KUANZA UTOAJI HUDUMA NDANI YA JENGO JIPYA KUANZIA MEI 15

  * Kamati ya Bunge Yasema ina matumaini Makubwa na Hatua iliyofikiwa, Wapongeza Serikali kutoa fedha * Ujenzi Wafikia Asilimia 92.8 📍 Dodo...