Wednesday, August 27, 2025

Dkt. Samia Suluhu Hassan Awasilisha Fomu za Kugombea Urais 2025

 











Mgombea wa nafasi ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Ndugu Dkt. Samia Suluhu Hassan, ametimia hatua nyingine muhimu katika mchakato wa uchaguzi wa 2025 kwa kurejesha rasmi fomu zake za kugombea nafasi ya urais.

Fomu hizo zimewasilishwa katika Ofisi za Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC) zilizopo Njedengwa, Jijini Dodoma, ikiwa ni ishara ya dhamira yake ya kuendelea kuongoza taifa kwa kuzingatia taratibu rasmi za kikatiba na kisheria.

Hatua hii ni muhimu kisiasa na kisheria, ikionyesha uwajibikaji wa mgombea wa ngazi ya juu na kuimarisha uwazi wa mchakato wa uchaguzi. 

Tukio hili limevutia hisia mchanganyiko za wananchi, wanasiasa, na wadau wa maendeleo, kwani linaashiria mwanzo rasmi wa mchakato wa uchaguzi unaosubiriwa kwa hamu, na kutoa fursa kwa wananchi kuona nia ya mgombea wa kuendeleza miradi ya kitaifa na sera za maendeleo endelevu.

TANZANIA KUNUFAIKA NA FURSA LUKUKI KUPITIA USHIRIKIANO WA AFRIKA NA SINGAPORE









* Miongoni mwa maeneo ya ushirikiano ni masoko ya mazao ya kilimo, elimu na mafunzo kwa vijana, nishati jadidifu, na uchumi wa kidijitali

Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imeshiriki hafla ya ufunguzi wa Mkutano wa Tano wa Mawaziri wa Mambo ya Nje wa Nchi za Afrika na Singapore (SAMEV), uliofanyika tarehe 26 Agosti 2025 jijini Singapore.

Ujumbe wa Tanzania katika mkutano huo umeongozwa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo.

Akifungua mkutano huo, Waziri wa Mambo ya Nje wa Singapore, Mhe. Dkt. Vivian Balakrishnan, alibainisha kuwa Mkutano huo unajadili mbinu za kuimarisha ushirikiano wa kidiplomasia, uchumi na maendeleo endelevu kati ya Singapore na nchi za Afrika. Alisisitiza kuwa ushirikiano huo unapaswa kuwa nguzo ya pamoja kukabiliana na changamoto mpya za uchumi na biashara duniani.

“Tunaishi katika nyakati zenye misukosuko mikubwa inayosababisha kudorora kwa ukuaji wa uchumi na biashara duniani. Vikwazo vya kibiashara, mabadiliko ya sera, ongezeko la ushuru usio wa kawaida, majanga ya asili na migogoro ya kisiasa vimeathiri kwa kiasi kikubwa mfumo wa uchumi wa kimataifa. Huu ni wakati muafaka wa kuweka mikakati ya pamoja ili tuweze kuhimili changamoto hizi na kuendelea kukua kiuchumi,” alisema Dkt. Balakrishnan.

Katika hotuba yake, Dkt. Balakrishnan alitaja maeneo ya kimkakati ambayo yataimarishwa kupitia ushirikiano wa Afrika na Singapore, na ambayo Tanzania itanufaika nayo moja kwa moja kuwa ni Fursa za masoko ya bidhaa za kilimo na madini zinazozalishwa nchini, Uwekezaji katika teknolojia na nishati jadidifu, Ufadhili wa masomo na mafunzo ya ufundi kwa vijana, Mapambano dhidi ya mabadiliko ya tabianchi, Ukuaji wa uchumi wa kidijitali na uchumi wa buluu na Uwekezaji katika sekta ya viwanda na biashara.

Aidha, Waziri Balakrishnan alieleza kuwa Singapore imeamua kuimarisha uhusiano wake na Afrika kutokana na mabadiliko makubwa ya kiuchumi na kisiasa duniani, hali inayohitaji mshikamano wa kimataifa. Alisisitiza kuwa Afrika na Asia ya Kusini-Mashariki zina nafasi ya kipekee ya kushirikiana kwa kuzingatia rasilimali tele, ukuaji wa kasi wa idadi ya watu, na ukubwa wa masoko.

Akiainisha sababu zinazovutia Singapore kuelekeza mikakati ya maendeleo Afrika, alibainisha mambo kadhaa muhimu ikiwemo idadi kubwa ya watu barani Afrika (takribani bilioni 1.3), ardhi kubwa na yenye rutuba, nafasi nzuri ya kijiografia, nguvu kazi yenye vijana walio chini ya miaka 30 wanaokaribia asilimia 70 ya idadi ya watu, hali ya amani na usalama, kasi ya ukuaji wa uchumi, na upatikanaji wa malighafi.

Vilevile, alitambua juhudi za nchi za Afrika katika kujenga uchumi wake kupitia utekelezaji wa Eneo Huru la Biashara la Afrika (AfCFTA) pamoja na uwepo wa Jumuiya za Kikanda za Afrika Mashariki (EAC) na Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC). 

Alibainisha kuwa Singapore iko tayari kushirikiana na jumuiya hizo kwa njia zitakazokubaliwa ili kuongeza kasi ya maendeleo kwa pande zote mbili.

Mkutano wa SAMEV hufanyika kila baada ya miaka miwili, ambapo kwa mara ya kwanza ulifanyika mwaka 2014. Ufunguzi wa mkutano wa mwaka huu pia ulihudhuriwa na Rais wa Jamhuri ya Ghana, Mhe. John Dramani Mahama

Tuesday, August 26, 2025

WAZIRI MKUU ALIPONGEZA SOKO LA HISA LA DAR ES SALAAM





_Ni baada ya kuongeza thamani na kufikia shilingi trilioni 21, Julai 2025_

_Pamoja na kuongeza ukuaji wa hisa kwa zaidi ya asilimia 246_

_Asema hatua hiyo ni ishara ya ukuaji imara wa sekta ya mitaji nchini_

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amelipongeza Soko la Hisa la Dar es Salaam (DSE) kwa kuongezeka kwa thamani ya soko hilo na kufikia shilingi trilioni 21.0 katika kipindi cha kufikia julai 2025.

Amesema kuwa pia soko hilo limeongeza ukuaji wa mauzo ya hisa kwa zaidi ya asilimia 246 pamoja na ongezeko la idadi ya wawekezaji hadi zaidi ya akaunti 683,000 ikiwa ni ishara ya ukuaji imara wa sekta ya mitaji nchini

Amesema hayo leo Jumanne (Agosti 26, 2025) alipotembelea Ofisi za soko hilo zilizopo Morocco, jijini Dar es Salaam.

Mheshimiwa Majaliwa amesema katika kipindi hicho mauzo ya hatifungani yaliyofikia zaidi ya shilingi trilioni 3 pamoja na hatifungani zenye maudhui ya kusaidia mazingira na jamii. “Hiki ni kielelezo cha ubunifu na mchango wa DSE katika kuendeleza uchumi jumuishi na endelevu wa Taifa letu, hii hatuwezi acha ikapita ni lazima tuwapongeze”.

Akizungumza katika mkutano huo, Mheshimiwa Majaliwa ametangaza kununua hisa zenye thamani ya shilingi milioni 100 katika soko la hisa la Dar es Salaam.

“Watanzania wekeni kipaumbele cha kufanya uwekezaji kupitia Soko la Hisa la Dar es Salaam kwa njia ya kidigitali ili kupata fursa ya kuwa sehemu ya kumiliki makampuni na kupata fedha kupitia faida inayotengenezwa na kampuni na kuchochea ukuaji wa uchumi wa Taifa letu.”

Waziri Mkuu ameiagiza Wizara ya Fedha iendelee kushirikiana na DSE katika kutoa elimu ya fedha kwa wananchi wote ili kuhakikisha fursa zinazotolewa na soko hilo zinanufaisha Watanzania wengi zaidi.

Naye, Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Fedha, Elijah Mwandumbya, amesema ili kufanikisha malengo ya dira Taifa ya Maendeleo ya 2050 Serikali imeweka mpango wa kuendeleza bidhaa mpya za kifedha kama vile hati fungani, kuimarisha mifumo ya kidijitali katika soko la DSE ili kuwafikia Watanzania wengi zaidi wakiwemo Diaspora.

Amesema eneo lingine ni kuendeleza ushirikiano na sekta binafsi na wadau wa kikanda, kuongeza ushiriki wa wawekezaji wa ndani na nje ya nchi ili kuongeza ukuaji wa soko la DSE.

Kwa upande wake, Kaimu Mtendaji Mkuu wa Mamlaka ya Masoko ya Mitaji na Dhamana (CMSA) Charles Shirima amesema ili kuwezesha ushiriki wa wananchi wengi mijini na vijijini katika uwekezaji wa masoko ya mitaji, mamlaka hiyo imehimiza matumizi ya mifumo bunifu katika uuzaji na ununuzi wa dhamana za masoko ya mitaji kwa kutumia Teknolojia ya Habari na Mawasiliano ikiwa ni pamoja na simu za mikononi na intaneti.

Amesema jitihada hizi zimewezesha kuanzishwa kwa mifumo kadhaa ikiwepo ya Sim Invest, Hisa Kiganjani, WekezaWHI na M-Wekeza ambayo inatumika kurahisisha upatikanaji wa huduma za masoko ya mitaji kwa wananchi wengi zaidi mijini na vijijini.

"Kwa mfano asilimia 24.33 ya mauzo ya hisa kwa mwaka 2024, yalipitia katika mfumo wa teknolojia ya habari yakiwa yameongezeka kutoka asilimia 4.84 mwaka 2023."

Awali, Afisa Mtendaji Mkuu wa Soko la Hisa la Dar es Salaam (DSE), Peter Situmbeko amesema tangu kuanzishwa kwake, soko hilo limeendelea kuongezeka thamani ya mauzo ya hisa pamoja na hamasa kwa wawekezaji.

Amesema thamani ya mauzo ya hisa ilifikia shilingi bilioni 369.4 sawa na ongezeko la asilimia 246 ikilinganishwa na kipindi kama hichi mwaka jana.

"Kiasi cha hisa zilizouzwa zilifikia milioni 272 ambalo ni ongezelo la asilimia 108 ikilinganishwa na kipindi kama hichi mwaka jana, hatifungani za Serikali pamoja na makampuni binafsi zilifikia jumia ya mauzo ya zaidi ya shilingi trilioni 3 katika kipindi kama hichi mwaka jana mauzo haya yalifikia shilingi trillioni 1.9"

KASI YA UJENZI WA VIWANDA VYA KUONGEZA THAMANI MADINI YAONGEZEKA NCHINI TANZANIA




📍Dodoma, Tanzania 

Serikali imeendelea kuthibitisha dhamira yake ya kuhakikisha rasilimali za madini zinawanufaisha Watanzania kupitia uongezaji thamani ndani ya nchi ikiwa ni sehemu ya jitihada za kuifanya Tanzania kuwa kitovu cha uchumi wa kijani (green economy)  hususan katika utengenezaji wa magari ya umeme, betri za magari, nishati safi na vifaa vya kielektroniki.

Hayo yamewekwa wazi leo Agosti 26, 2025 na Waziri wa Madini, Mhe. Anthony  Mavunde, wakati akiweka jiwe la msingi la Kiwanda cha kusafisha na kusindika Madini ya Nikeli na Shaba kinachojengwa na Kampuni ya Zhongzhou Mining Co. Ltd, eneo la Zamahero, Wilaya ya Bahi, mkoani Dodoma.

Amesema kuwa, Mradi huo utekelezaji wa maelekezo ya Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwamba madini yanayochimbwa hapa nchini yaongezewe thamani ndani ya nchi na kuuza bidhaa ya mwishyabadala ya madini ghafi.

“Ujenzi wa kiwanda hiki ni uthibitisho kuwa dhamira ya kuongeza thamani madini nchini, tunataka kuona Tanzania ikibadilika na kuwa taifa linalozalisha bidhaa zenye thamani kubwa kwenye soko la dunia la bidhaa teknolojia.” amesema Mavunde 

Waziri Mavunde ameeleza kuwa mradi huo wenye thamani ya dola za kimarekani milioni 15 utakapokamilika utazalisha takribani tani 200,000 za nikeli na shaba kwa mwaka, kuajiri zaidi ya Watanzania 200 hadi 230, na kuchangia kodi na mapato mengine ya Serikali.

“Uwekezaji huu ni kielelezo cha mafanikio ya Serikali katika kufanikisha dira ya uchumi wa viwanda na uongezaji thamani madini kama ilivyoelekezwa na Ilani ya uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi (CCM) ya mwaka 2020–2025," amesisitiza Mavunde. 

Amebainisha kuwa, pia Sera ya Madini ya mwaka 2009 inaelekeza kuyaongezea thamani madini yetu ndani ya nchi na kuongeza kuwa “hivi sasa Tanzania tuna viwanda vinane vya kusafisha madini ya dhahabu (gold refinery) lakini viwanda vya kuongezea thamani Madini ya metali tunavyo 9, mkoa wa Dodoma peke yake tunavyo vitano”  ameongeza Mavunde. 

Kwa upande wake, Kamishna wa Madini, Dkt. AbdulRahman Mwanga amesema kuwa, kwa kuwekeza kwenye miradi ya kuongeza thamani, Tanzania inajenga msingi imara wa ajira, mapato, na uchumi shindani kimataifa na kufikia lengo la ujenzi wa Tanzania ya uchumi.

Naye, Mkurugenzi wa Kampuni ya Zhongzhou Mining Lee Zhong LIANG amemuhakikishia Waziri Mavunde kuwa Kampuni itaendeleza uhusiano mwema na Serikali pamoja wananchi wanaozunguka mradi huo.

Pia, Katibu Tawala Wilaya ya Bahi , Mwanamvua Muyongo ameeleza kuwa uwepo wa kiwanda hicho utasaidia kuiweka Wilaya hiyo katika ramani ya wazalishaji wa bidhaa muhimu za kiteknolojia pamoja na kuboresha maisha ya watu wa hapa kupitia ajira rasmi na zisizo za moja kwa moja.

*#Value Addition

For Socio- Economic Development*

#Uongezaji Thamani Madini kwa  Maendeleo ya Kiuchumi na Kijamii

Makamu wa Rais Dkt. Mpango Awasili Kigoma kwa Ziara ya Kiserikali






Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Philip Mpango, amewasili katika Uwanja wa Ndege wa Kigoma leo, tarehe 26 Agosti 2025, ambapo alipokelewa kwa heshima kubwa na Viongozi mbalimbali wa Serikali, Chama na Taasisi za Umma.

Ziara ya Makamu wa Rais mkoani humo inalenga kuimarisha jitihada za Serikali katika kusogeza huduma karibu zaidi na wananchi na kuchochea maendeleo ya kiuchumi katika ukanda wa magharibi mwa nchi.

Kesho, tarehe 27 Agosti 2025, Dkt. Mpango anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika hafla ya ufunguzi wa Tawi jipya la Benki ya CRDB katika Wilaya ya Buhigwe. Ufunguzi huo ni sehemu ya mkakati wa benki hiyo wa kupanua huduma zake nchini, huku ukiendana na dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita ya kusogeza huduma za kifedha kwa wananchi wote, hususan waliopo vijijini na maeneo ya mipakani.

Wananchi wa Mkoa wa Kigoma na wilaya jirani wanatarajiwa kunufaika kwa kiasi kikubwa na upatikanaji wa huduma za kibenki, jambo litakalowezesha biashara ndogo, za kati na kubwa kukua, kuongeza fursa za ajira, na kuimarisha mzunguko wa fedha katika maeneo hayo.

Ziara hii pia inatarajiwa kutoa fursa kwa Makamu wa Rais kusikiliza na kujadiliana na wananchi kuhusu masuala ya maendeleo ya jamii, kilimo, biashara, na miundombinu, kwa lengo la kuendelea kuboresha ustawi wa wananchi wa Kigoma na taifa kwa ujumla.

#MakamuWaRais #PhilipMpango #Kigoma #CRDBBuhigwe #MaendeleoKwaWote #HudumaZaKifedha

Rais Samia Aapisha Viongozi Wapya Ikulu Chamwino















Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, tarehe 26 Agosti 2025 ameongoza hafla ya uapisho wa viongozi wapya katika Ikulu ya Chamwino, jijini Dodoma. Hafla hii ilihudhuriwa na viongozi wa Serikali, watumishi wa umma, viongozi wa dini pamoja na ndugu na jamaa wa viongozi walioteuliwa.

Miongoni mwa walioteuliwa na kuapishwa na Rais Samia ni:

  • Ndugu Hassan Omari Kitenge – Kamishna wa Tume ya Utumishi wa Umma.

  • Ndugu Salama Aboud Twalib – Kamishna wa Tume ya Utumishi wa Umma.

  • Dkt. Deo Osmund Mwapinga – Balozi.

  • Dkt. Laurean Josephat Ndumbaro – Kamishna wa Tume ya Utumishi wa Umma.

Akizungumza katika hafla hiyo, Rais Samia aliwakumbusha viongozi walioteuliwa kwamba dhamana waliyopewa ni kubwa na inalenga kuwatumikia Watanzania kwa uadilifu, weledi na moyo wa kizalendo. Aidha, alisisitiza umuhimu wa kuimarisha ufanisi wa utendaji ndani ya taasisi za umma na kuhakikisha kila mmoja anachangia kikamilifu katika kuleta maendeleo ya taifa.

Kwa hatua hii, Serikali ya Awamu ya Sita inaendelea kuimarisha safu ya uongozi kwa kuwapa nafasi viongozi wenye uwezo na uzoefu, ili kuhakikisha Tanzania inasonga mbele katika mageuzi ya kiuchumi, kijamii na kidiplomasia.

#RaisSamia #IkuluChamwino #Uapisho2025 #UongoziBora #Uwajibikaji

Dkt. Samia Suluhu Hassan Awasilisha Fomu za Kugombea Urais 2025

  Mgombea wa nafasi ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Ndugu Dkt. Samia Suluhu Hassan, a...