Monday, April 14, 2025

MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI AWAONGOZA MAWAKILI WA SERIKALI KATIKA MKUTANO MKUU WA MAWAKILI










Mwanasheria Mkuu wa Serikali na Mlezi wa Chama cha Mawakili wa Serikali Tanzania, Mhe. Hamza S. Johari amewaongoza Mawakili wa Serikali kushiriki katika Mkutano Mkuu wa Mwaka wa Chama cha Mawakili wa Serikali unaofanyika  Jijini, Dodoma tarehe 14 hadi 15 Aprili, 2025.

Akizungumza katika Mkutano huo, Mwanasheria Mkuu wa Serikali amewataka Mawakili wa Serikali kuutumia mkutano katika kujadili kwa kina masuala mbalimbali yanayohusu Chama cha Mawakili wa Serikali pamoja na Sekta ya Sheria kwa ujumla.

“Wote tunafahamu lengo la mkutano huu ni kutoa fursa kwa wanachama kujadili mambo mbalimbali yanayohusu chama chetu.”

Katika hatua nyingine, Mhe. Johari amewakumbusha Mawakili wa Serikali kuendelea kutekeleza majukumu yao vizuri ili kuweza kuifikia Dira ya Taifa ya Maendeleo ya mwaka  2050, kwa kuzingatia na kuiishi kauli mbiu ya mkutano huo inayosema “Utawala wa Sheria katika utekelezaji wa majukumu ya Serikali, ni nguzo muhimu katika kufikia malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050”. 

“Kauli mbiu yetu ya Mwaka huu imejielekeza kwenye Dira ya Taifa ya Mwaka 2050 na ili tuifikie dira hii tunatakiwa kuwa na proper legal framework na sisi tunataka kuwa facilitator wa kulifikisha taifa huko.”

Awali, akimkaribisha Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Mhe. Samwel M. Maneno amewahakikishia Mawakili wa Serikali kuwa Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali itaendelea kuhakikisha kuwa Mawakili wa Serikali wanaendelea kutekeleza majukumu yao kwa ujasiri na ulinzi mkubwa bila kutetereka.

“Tutahakikisha kila Mwanasheria kule aliko anatekeleza  majukumu yake kwa niaba ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, na milango ya Ofisi ya Mwanasheria Mkuu iko wazi wakati wowote tutawasikiliza.”

Kwa upande wake, Naibu Mwanasheria Mkuu wa Zanzibar, Ndg. Shaaban Ramadhan Abdalla ameishukuru Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali na Chama cha Mawakili wa Serikali Tanzania kwa kuialika Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Zanzibar kuja kuhudhuria Mkutano huo huku akikipongeza Chama cha Mawakili wa Serikali kwa kuendelea kuwasimamia vizuri Mawakili wa Serikali.

Mkutano Mkuu wa Chama cha Mawakili wa Serikali umeanza tarehe 14 Aprili, 2025 kwa Mawakili wa Serikali kupokea taarifa mbalimbali zinazohusu chama hicho na Mkutano utaendelea hadi tarehe 15 Aprili, 2025 ambapo Mgeni Rasmi anatarajiwa kuwa Mhe. Dkt. Doto Mashaka Biteko, Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati.

Aidha, kupitia mkutano huo Mawakili hao watapata fursa ya kufanya uchaguzi kwa kuwachagua viongozi mbalimbali wa kukiongoza  Chama cha Mawakili wa Serikali kwa kipindi cha mwaka mmoja

WAZIRI MAVUNDE AINGILIA KATI UTEKELEZAJI WA MIRADI YA CSR MKOANI GEITA

 










▪️Ataka taarifa kamili ndani ya siku tatu ya mpango wa utekelezaji CSR

▪️Miradi ya 2018-2021 kukamilishwa

▪️Fedha zilizotengwa na GGM kwa miradi kutumika zote

▪️RC Shigela ahimiza ushirikiano wa karibu wa GGM na Serikali

Waziri wa Madini, Mh. Anthony Mavunde, ameongoza kikao cha kujadili utekelezaji wa miradi ya Mpango wa Uwajibikaji wa Mmiliki wa Leseni kwa Jamii (CSR) inayotekelezwa na Kampuni ya Geita Gold Mining Limited (GGML) katika Mkoa wa Geita.

Kikao hicho kimefanyika leo, Aprili 14, 2025 jijini Dodoma, kikihusisha viongozi kutoka Wizara ya Madini, Tume ya Madini, uongozi wa Mkoa wa Geita,Wabunge wa Geita pamoja na wawakilishi wa GGML kwa lengo la kupata muafaka kuhusu changamoto za utekelezaji wa miradi ya CSR na kuweka mikakati madhubuti ya kuhakikisha wananchi wa Geita wananufaika ipasavyo na rasilimali za madini.

Akizungumza katika kikao hicho, Waziri Mavunde amesisitiza kuwa wananchi wa Geita wanatamani kuona matokeo ya moja kwa moja ya uwepo wa mgodi huo kwa kupitia miradi ya maendeleo.

"Nimeitisha kikao hiki kwa lengo la kutafuta njia bora ya kutekeleza miradi ya CSR, kutatua changamoto zilizopo, na kuhakikisha wananchi wa Geita wananufaika na rasilimali zinazochimbwa katika maeneo yao.

Kuna umuhimu wa kukamilisha utekelezaji wa miradi ya nyuma ya kuanzia mwaka 2018-2021 ili kuwezesha uanzishwaji wa miradi mipya yenye tija kwa jamii.

Ninatoa agizo la siku tatu kwa GGML kukutana na Wakurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Geita na Halmashauri ya Wilaya ya Geita, kwa lengo la kuandaa na kuwasilisha taarifa ya utekelezaji wa miradi ya nyuma”Alisema Mavunde

Makamu wa Rais wa Anglo-Gold Ashanti, Simon Shayo, amesema kwamba Kampuni ya GGM ipo tayari kushirikiana na uongozi wa Mkoa wa Geita kuhakikisha wananchi wa Geita wananufaika na miradi ya CSR ambayo kwa sasa kwa ujumla wake imetengewa kiasi cha Tsh 21bn kwa ajili ya utekelezaji wake na hivyo kuleta matokea chanya kwenye. maendeleo ya mkoa wa Geita

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Geita, Mhe. Martin Shigella, ameisisitiza GGML kuhakikisha miradi iliyosainiwa inatekelezwa kwa wakati na kwa mujibu wa makubaliano, akisisitiza umuhimu wa ushirikiano baina ya Mgodi na Uongozi wa Mkoa kwa manufaa ya wana Geita.

Wakichangia kwenye kikao hicho wabunge wa Mkoa wa Geita Mh. Constantine Kanyasu,Mh. Joseph Kasheku Msukuma na Mh. Tumaini Magesa wameitaka Kampuni ya GGM kuhakikisha inakamilisha miradi ya CSR kwa wakati na kwa ubora wa juu utakaoendana na gharama zilizotumika ili wananchi wa Geita wayaone matunda ya uwepo wa Mgodi huo.

Kwa sasa, GGML huchangia kiasi cha Shilingi bilioni 9.2 kila mwaka kama sehemu ya CSR Mkoani Geita

WANAWAKE WACHANGIA 35% YA PATO LA TAIFA




📌 Dkt. Biteko afungua Mkutano wa TAWiFA

📌 Dkt. Biteko awataka wanawake kuwekeza katika teknolojia kufikisha huduma vijijini

📌 Uwekezaji kwa wanawake si hisani ni kimkakati kwa maendeleo ya Taifa

Ofisi ya Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati

Wanawake nchini Tanzania wametajwa kuwa na mchango mkubwa katika Pato la Taifa ambapo takwimu zinaonesha kuwa asilimia 35 ya uchumi wa Tanzania unatokana na juhudi za wanawake ambao wanachangia asilimia 70 ya nguvu kazi ya kilimo ni wanawake hasa katika mazao ya chakula.

Mchango wa mwingine wa wanawake unajidhihirisha katika biashara, viwandani na katika huduma za kifedha kupitia utafiti uliofanywa na Chama cha Mabenki Tanzania (TBA) mwa ka 2022 umeonesha wanawake ni 47% ya wafanyakazi wote wa sekta ya fedha. Pia wanashika 10% ya nafasi za kufanya maamuzi. Vile vile, 18% wakiwa wajumbe katika bodi za wakurugenzi sawa na wastani wa wanawake wawili katika kila bodi.

Hayo yamebainishwa leo Aprili 14, 2025 jijini Dodoma na Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Mhe. Dkt. Doto Biteko wakati aliposhiriki katika ufunguzi wa Mkutano wa mwaka wa Chama cha Wanawake katika Sekta ya Fedha (TAWiFA).

Pamoja na mafaniko hayo, Dkt. Biteko ametaja changamoto zinawakabili wanawake katika sekta ya fedha kuwa ni uhaba wa upatikanaji wa mikopo yenye riba nafuu, elimu duni ya masuala ya kifedha na uchache wa nafasi za kushiriki katika maamuzi ya Sera za Fedha.

Amewanawake nchini kuzingatia misingi ya malezi kwa watoto wao kwa kuwapa nafasi sawa watoto wa kike na wa kiume ili kukabili changamoto zinazotokana na mila, desturi utamaduni.

“Kwa kushirikiana na wadau wengine Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,  Mhe.  Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kuchukua hatua za makusudi ili kutatua changamoto zinazomkabili mwanamke na hivyo kuchochea maendeleo" amesema Dkt. Biteko.

Amebainisha baadhi ya hatua hizo kuwa  ni kuwaamini na kuwapa wanawake nafasi za juu za uongozi na maamuzi, kufanya Mapitio na Tathmini ya Utekelezaji wa Sera ya Taifa ya Jinsia na Maendeleo ya Wanawake ya mwaka 2000,  kuandaa miongozo mbalimbali ikiwemo  Mwongozo wa Ulinzi na Usalama wa Wanawake na Vijana Vyuoni uliozinduliwa mwaka 2023 na kutoa fursa nyingine mbalimbali za kifedha na kiuchumi kwa wanawake.

Amesisitiza kuwa wanawake wanatakiwa kuwekeza zaidi katika mifumo ya kidigitali ili kuendana na mabadiliko ya kidigitali "Naomba hapa nitoe rai kwenu kuwa, mkiwa mnaendelea kutekeleza majukumu yenu, msisahau kuhusu kuwekeza katika teknolojia. Maana Dunia ya sasa inazidi kwenda zaidi katika maisha ya kidigitali. Hii itasaidia kurahisisha biashara na kufikisha huduma kwa wepesi hususan katika maeneo ya vijijini,”

Fauka ya hayo, Dkt. Biteko amesema kupitia mijadala na maazimio yatakayotolewa katika mkutano huo, zitapatikana  mbinu mpya za kuongeza ushiriki wa wanawake katika sekta ya fedha na uchumi wa nchi kwa ujumla kupitia mabenki, kampuni za bima, masoko ya mitaji. Pamoja na mbinu na njia mbalimbali za fedha mtandao zinazotatua changamoto zinazomkabili mwanamke katika sekta ya fedha.

Naibu Waziri wa Wizara ya Fedha, Mhe. Hamad Chande amewapongeza wanawake nchini kwa kuanzisha Chama hicho kinacholenga kusaidia wanawake kiuchumi.

Amewahakikishia kuwa Serikali imeandaa mazingira rafiki kwa wanawake katika ukuzaji wa uchumi “ Serikali imeweka mazingira wezeshi kwa kutunga sera na sheria za kiuchumi ili wanawake na makundi mbalimbali yaweze kuimarika kupitia taasisi na vyama kama hivi. Aidha, Serikali itaendelea kushirikiana nanyi ili kuimarisha TAWiFA ili kuhakikisha nafasi ya mwanamke inazidi kuwa juu katika jamii.”

Rais wa Chama cha Wanawake katika Sekta ya Fedha (TAWiFA), Fikira Ntomola amesema kuwa wanawake nchini wameendelea kujishughulisha ili kuhakikisha sekta ya fedha nchini inakuwa. Aidha, jamii inapaswa itambue uwekezaji kwa wanawake si hisani bali ni uwekezaji wa kimkakati kwa maendeleo ya Taifa.

“ Tunaahidi kufikisha elimu ya fedha kwa wanawake katika maeneo mbalimbali nchini kwa kuandaa mafunzo na warsha kwa lengo la kuongeza uwezo wa kusimamia masuala yao ya fedha na biashara,” amesema Bi. Ntomola.

Ameongeza kuwa TAWiFA imedhamiria kuleta mabadiliko chanya kuhusu ushiriki wa wanawake katika sekta ya fedha, aidha wameishukuru Serikali kwa kuendelea kuweka sera na sheria zinazochochea uchumi jumuishi  na uwepo wa usawa wa kijinsia kiuchumi na kijamii.

“Tumekuwa tukiwajengea uwezo wanawake wa kuendesha biashara zao kiufanisi, kukuza biashara zao na kupanua  wigo wao kuhusu sekta ya fedha,” amebainisha Bi. Ntomola.

Amewaomba wadau mbalimbali nchini kufungua milango ya fursa kwa wanawake, na kuwa TAWiFA ipo tayari kushirikiana nao kwa ajili ya kutoa elimu ya fedha kwa umma, pamoja na tafiti za kuendeleza miradi ya kusaidia wanawake ili kujenga sekta ya fedha iliyo jumuishi.

Makamu wa Rais wa Chama cha Wanawake katika Sekta ya Fedha (TAWIFA), Nangi Massawe amesema kuwa Chama hicho kinakutanisha wanawake katika sekta ya fedha ili kujenga sekta yenye usawa kwa manufaa ya Taifa.

TAWiFA kina jumla ya wanachama 204 na kimeendelea kuhakikisha wanawake wanashiriki katika sekta hiyo ili kuchochea maendeleo.





Sunday, April 13, 2025

UBUNIFU NA TEKNOLOJIA: MSINGI WA USIMAMIZI BORA WA MISITU NA NYUKI

 




Na Mwandishi Wetu, Arusha

Kamishna wa Uhifadhi kutoka Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS), Prof. Dos Santos Silayo, amewataka Maafisa na Askari wa uhifadhi nchini kuhakikisha wanazingatia mafunzo ya uongozi waliyopata, huku wakiongeza ubunifu na kutumia teknolojia za kisasa katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku.

Prof. Silayo aliyasema hayo Aprili 12, 2025, wakati akifunga rasmi mafunzo ya uongozi kwa wahifadhi 481 katika Chuo cha Misitu (Olmotonyi), Jijini Arusha. 

Alisisitiza kuwa elimu waliyoipata inapaswa kuwa chachu ya mabadiliko chanya ya utendaji kazi ili kufanikisha malengo ya taasisi kwa wakati na kwa ufanisi.

“Ni muhimu kila mmoja akasimamia vyema eneo lake la kazi alilokasimiwa. Hii italeta matokeo bora na kusaidia taasisi kufikia malengo yake kwa wakati,” alisema Prof. Silayo.

Aidha, Kamishna huyo alihimiza matumizi ya teknolojia mpya kama matumizi ya drone katika kusimamia maeneo ya hifadhi, akisema teknolojia hiyo itarahisisha utambuzi wa matukio ya uhalifu kwa haraka, hivyo kuongeza ufanisi wa operesheni za uhifadhi.

“Taasisi yetu inatekeleza majukumu mengi muhimu kama upandaji miti, uvunaji wa malighafi, ufugaji nyuki, na utalii wa ikolojia. 

Tunapaswa kuhakikisha jamii inazifahamu shughuli hizi ili kuongeza uelewa wa masuala ya uhifadhi,” aliongeza.

Aliwahimiza wahifadhi kuondokana na utendaji kazi wa kimazoea na badala yake kuonyesha ubunifu unaoleta matokeo chanya katika ulinzi na usimamizi wa rasilimali za misitu na nyuki.

Katika kuhitimisha, Prof. Silayo aliwakumbusha wahitimu hao umuhimu wa kuzingatia utawala wa sheria, nidhamu, na ushirikiano kazini, akisema haya ni msingi wa utendaji bora na mafanikio ya Jeshi la Uhifadhi.

Awali, Mkuu wa Chuo cha Misitu Olmotonyi, Dkt. Joseph Makero, aliwapongeza wahitimu kwa nidhamu, ukakamavu na weledi waliouonyesha wakati wote wa mafunzo, akisema sifa hizo ni muhimu katika kutekeleza majukumu ya kitaifa ya uhifadhi.

Naye Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Uhifadhi na Meneja wa Utawala wa TFS, Erasto Luoga, aliwasilisha taarifa ya mafunzo hayo na kusema kuwa jumla ya wahifadhi 481 wamehitimu kwa mafanikio makubwa.

*SANAA NI UCHUMI-MAJALIWA

 





Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amesema Serikali imejidhatiti kuendelea kukuza na kuimarisha sanaa nchini ikiwa ni moja ya sekta rasmi ya kiuchumi.

Ametoa kauli hiyo leo Jumapili (Aprili 13, 2025) katika Kongamano la Chama cha Wafawidhi wa Matukio Tanzania, linalofanyika Olasiti Garden, Mkoani Arusha. Ambapo amesema fani ya ushereheshaji ni uchumi.

Amesema kuwa kwa kutambua umuhimu huo, Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan aliridhia kaunzisha Mfuko wa Utamaduni na Sanaa ambao unakopesha hadi shilingi Milioni 100 kwa wasanii wakiwemo washereheshaji ili waweze kujiimarisha kimitaji na vitendea kazi.

“Pia kupitia maboresho ya Sheria ya Hakimiliki na Hakishiriki ya mwaka 1999 yaliyofanyika mwaka 2022, Serikali imeanzishwa tozo ya hakimiliki (copyright levy) ambapo asilimia 60 ya makusanyo inakuja kwenu moja kwa moja na asilimia nyingine 10 inakuja kwenu kupitia Mfuko”

Katika hatua nyingine, Mheshimiwa Majaliwa amesema kuwa Serikali inatarajia kujenga Ukumbi wa Kimataifa ya Sanaa na Michezo ‘Arts and Sports Arena’ kwa shilingi bilioni 300. “Haya yote ni maono ya Rais wetu Dkt. Samia Suluhu Hassan”

Pia, Mheshimiwa Majaliwa ameaigiza Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kupitia Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA) kushirikiana chama cha Kisima cha Mafanikio katika kuandaa miongozo, mafunzo ya kitaaluma, na mfumo wa urasimishaji wa washereheshaji nchini.

“Baraza la Kiswahili la Taifa (BAKITA) endeleeni kushirikiana na Kisima cha Mafanikio katika kukuza matumizi sahihi ya Kiswahili kwenye majukwaa mbalimbali”.

Kadhalika Mheshimiwa Majaliwa amesema Serikali inatambua kazi ya Chama cha Kisima cha Mafanikio. “Hakika kazi yenu ni ya msingi, nyeti na yenye mchango mkubwa kwa Taifa”.

Kwa Upande wake, Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Prof. Palamagamba Kabudi amemshukuru Rais Dkt. Samia kwa uongozi wake mahiri na kwa kutoa fursa kwa watanzania kukuza vipaji vyao na kuendeleza stadi za kazi na taaluma katika tasnia mbalimbali ikiwemo ya ushereheshaji na upangaji wa matukio.

Hakika Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan amekuwa katika mstari wa mbele wa kulea vipaji vyote na kuvipa nafasi kuweza kuonekana na kutenda kazi zao kama ilivyokwenu watu wa Kisima cha Mafanikio”.

Kwa Upande wake Mwenyekiti wa Chama hicho Ester Kimweri ameipongeza Serikali ya awamu ya Sita inayoomgozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kusimamia uzalendo nchini.

“Sisi wadau wa sekta hii tunapenda kuonesha nia yetu ya dhati kuendelea kuunga mkono juhudi hizi kwa vitendo kwa kuuelimisha, kuuhamasisha, kuburudisha na kufundisha na sisi tutaendelea kuheshimu sheria, kulinda rasilimali, mali za umma, kushiriki shughuli za maendeleo ya jamii”

*TANAPA YASHIRIKI MAADHIMISHO YA MIAKA 103 YA KUZALIWA KWA MWL. NYERERE – DODOMA





Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA), likiongozwa na Kamishna wa Uhifadhi Musa Nassoro Kuji, limeshiriki hafla ya Maadhimisho ya Kumbukizi ya Miaka 103 ya kuzaliwa kwa Baba wa Taifa, Mwalimu Julius K. Nyerere, leo Aprili 13, 2025, yanayofanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Dkt. Jakaya Kikwete, jijini Dodoma.

Hafla hiyo imehudhuriwa na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Philip Isdori Mpango, pamoja na viongozi mbalimbali wa Wizara ya Maliasili na Utalii wakiongozwa na Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Danstan Kitandula (Mb).

Sherehe hizo zimeandaliwa na Taasisi ya Kumbukumbu ya Mwl. J.K. Nyerere, ambapo TANAPA ni Mdhamini Mkuu wa Maadhimisho hayo. Kaulimbiu ya Maadhimisho haya ni: “Chagua Viongozi Bora kwa Ustawi wa Jamii na Maendeleo Endelevu ya Taifa.”

Katika kuenzi misingi ya uongozi wa Mwalimu Nyerere na Azimio la Arusha ambalo lililenga kujenga jamii yenye misingi ya uadilifu, usawa, uwajibikaji na uzalendo limekuwa likienziwa hivyo kupitia maadhimisho hayo, Watanzania wamehimizwa kuendeleza maono ya Baba wa Taifa kwa kusimamia rasilimali za nchi kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho, sambamba na kuchagua viongozi bora watakaoendeleza misingi hiyo kwa maendeleo endelevu ya Taifa.

Aidha, TANAPA imetumia jukwaa hilo kuhamasisha Watanzania kupigia kura Hifadhi za Taifa kumi (10) zilizoingia katika vipengele vinane (8) katika kuwania Tuzo kubwa za Utalii Duniani, maarufu kama World Travel Awards, ili kuendelea kuitambulisha Tanzania kimataifa jambo linalotarajiwa kuchochea ongezeko la watalii na mapato yatokanayo na shughuli za utalii.

Saturday, April 12, 2025

SERIKALI YATOA WITO KWA DIASPORA KUWEKEZA NYUMBANI

















Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. David Cosato Chumi (Mb) kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo ametoa wito kwa Watanzania waishio nje ya nchi (diaspora) kuchangamkia fursa ya kuwekeza nyumbani, akisema kuwa mchango wao ni nguzo muhimu ya maendeleo ya taifa.

Mhe. Chumi ametoa kauli hiyo jijini Dar es Salaam wakati wa hafla ya uzinduzi wa Akaunti ya Mzawa, huduma maalum ya kifedha kwa diaspora iliyozinduliwa na Benki ya Absa Tanzania.

Akizungumza kwenye hafla hiyo, Mhe. Chumi ameipongeza Benki ya Absa kwa ubunifu wa huduma hiyo ambayo inalenga kupunguza changamoto wanazokutana nazo Watanzania wanaoishi ughaibuni, hususan katika kupata huduma za kifedha, kutuma fedha, na kushiriki katika uwekezaji wa ndani.

“Akaunti hii ni suluhisho la changamoto za kifedha kwa diaspora. Inawaruhusu kufungua akaunti, kutuma fedha, kuwekeza, na kutumia sarafu 5 tofauti wakiwa popote duniani.

Amefafanua kuwa mchango wa diaspora umekuwa ukiongezeka kila mwaka, akitaja kuwa mwaka 2022 pekee, Watanzania waishio nje walituma nchini fedha za kigeni zenye thamani ya zaidi ya Shilingi trilioni 1.4. Amesema fedha hizo zimechangia maendeleo ya sekta mbalimbali kama elimu, afya, biashara, na ujenzi wa makazi.

“Serikali inatambua nafasi muhimu ya diaspora. Ndiyo maana tumekamilisha mapitio ya Sera ya Mambo ya Nje inayojumuisha masuala ya diaspora, tumeanzisha mfumo wa kidijitali wa usajili wa diaspora, tumepitisha hadhi maalum kwa Watanzania wasio raia, na kuanzisha vitengo mahsusi serikalini vya kushughulikia masuala yao,” ameongeza Mhe. Chumi

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Absa Tanzania, Bw. Obedi Laizer, amesema huduma hiyo imebuniwa kwa kuzingatia maoni ya Watanzania waishio nje, na kwamba benki hiyo itaendelea kushirikiana na Serikali katika kukuza uwekezaji wa ndani na biashara jumuishi. 

Hafla hiyo pia imehudhuriwa na Mkurugenzi wa Idara ya Diaspora katika Wizara ya Mambo ya Nje, Bw. Salvatory Mbilinyi, mabalozi wastaafu, na wadau mbalimbali wa sekta ya kifedha na uwekezaji.

MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI AWAONGOZA MAWAKILI WA SERIKALI KATIKA MKUTANO MKUU WA MAWAKILI

Mwanasheria Mkuu wa Serikali na Mlezi wa Chama cha Mawakili wa Serikali Tanzania, Mhe. Hamza S. Johari amewaongoza Mawakili wa Serikali kush...