Friday, October 17, 2025

CHUO KIKUU MZUMBE CHAPOKEWA MSAADA WA VITABU KUTOKA ACCA

 




Chuo Kikuu Mzumbe kimepokea vitabu 69 vya kufundishia na kujifunzia kutoka Association of Chartered Certified Accountants (ACCA) kupitia ofisi yake ya Tanzania.

Vitabu hivyo vinahusu masomo ya uhasibu na fedha, na vinatarajiwa kusaidia walimu na wanafunzi katika kukuza maarifa ya kitaaluma na kiutendaji, hususan katika maeneo yanayohusiana na ushughulikiaji wa biashara, fedha, na mahitaji ya soko la ajira la kisasa.

Akizungumza katika hafla ya makabidhiano iliyofanyika Oktoba 17, 2025, katika Ndaki ya Dar es Salaam, Prof. Omary Swalehe, Naibu Rasi wa Chuo Kikuu Mzumbe, ameishukuru ACCA kwa msaada huo, akisema utachangia kwa kiasi kikubwa kuinua kiwango cha elimu ya uhasibu na fedha.

“Huu ni msaada mkubwa sana na utasaidia katika kuendeleza maarifa ya masomo ya uhasibu na fedha kwa walimu na wanafunzi wetu,” amesema Prof. Swalehe.

Kwa upande wake, Bw. Jenard Lazaro, Meneja wa ACCA Tanzania, amesema ACCA imekuwa mshirika wa muda mrefu wa Chuo Kikuu Mzumbe katika nyanja mbalimbali, ikiwemo ujenzi wa uwezo wa walimu na usaidizi wa kitaaluma kwa wanafunzi.

“Tukio la leo ni mwendelezo wa ushirikiano wetu, na lengo kuu ni kuhakikisha wanafunzi wanapata vifaa bora vya kujifunzia vitakavyowawezesha kufanikiwa katika safari yao ya ACCA na taaluma zao za baadaye,” amesema Bw. Lazaro.

Hafla hiyo ilihudhuriwa pia na wawakilishi wa chuo, akiwemo Dkt. Daudi Pascal Ndaki, aliyemwakilisha Mkuu wa Skuli ya Biashara ya Chuo Kikuu Mzumbe Kampasi Kuu Morogoro, pamoja ,  Dkt. Joshua Mwakujonga, Mkuu wa Idara ya Masomo ya Biashara, Ndaki  ya Dar es Salaam pamoja na Bw. Elias Ntobi, Mkuu wa Kitengo cha Huduma za Maktaba Ndaki ya Dar es Salaam.

Uchangiaji huo unaakisi dhamira ya ACCA ya kuwezesha wataalamu wa fedha wa kizazi kijacho, kupitia kuimarisha ushirikiano kati ya sekta ya elimu na taaluma, sambamba na kuinua ubora wa elimu ya uhasibu nchini Tanzania.

TANZANIA KUNUFAIKA NA PROGRAM YA BENKI YA DUNIA YA KUENDELEZA KILIMO

 

Tanzania inatarajiwa kunufaika na mpango wa Benki ya Dunia wa kuboresha mnyororo wa thamani wa sekta ya kilimo katika Bara la Afrika, kupitia program yake mpya ya kuendeleza kilimo ya AgroConnect, itakayogharimu dola bilioni 9 za Marekani. 


Hayo yamesemwa na Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Dunia, anayesimamia Kundi la Kwanza la nchi za Kanda ya Afrika (Africa Group 1 Constituency), Dkt. Zarau Wendeline Kibwe, alipokutana na kufanya mazungumzo na Ujumbe wa Tanzania ukiongozwa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha, Dkt. Natu El-maamry Mwamba, Makao Makuu ya Benki hiyo Jijini Washington D.C, nchini Marekani.

Dkt. Kibwe ambaye ni Mtanzania anayeshikilia nafasi hiyo kubwa katika Benki ya Dunia, alisema kuwa program hiyo itahusisha kuwasaidia wakulima kuboresha kilimo kwa kuongeza thamani ya mazao yao na kuwaunganisha na masoko ya uhakika.

Alisema kuwa hatua hiyo si tu kwamba itaongeza usalama wa upatikanaji wa chakula, bali pia utaongeza upatikanaji wa ajira na kukuza uchumi jumuishi katika nchi wanachama wa Benki ya Dunia.


Alisema kuwa Benki ya Dunia inathamini ushirikiano mkubwa uliopo kati ya Benki yake na Tanzania na kwamba itaendeleza ushirikiano huo kupitia mwelekeo mpya wa kisera ambapo msisitizo mkubwa umewekwa katika maeneo matano yenye kuziwezesha nchi wanachama hususan zilizoko katika Ukanda wa Kusini mwa Jangwa la Sahara, kuwekeza kwenye miradi itakayochangia kukuza ajira, kupitia sekta za kilimo biashara, ujenzi wa miundombinu ikiwemo reli, nishati, afya, utalii na uzalishaji viwandani vitakavyo changia kuongeza thamani ya bidhaa.

Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha, Dkt. Natu El-maamry Mwamba, pamoja na kuishukuru Benki ya Dunia kwa kuendelea kutoa fedha zinazotumika kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo, alionesha furaha yake kwa Benki ya Dunia kuonesha utayari wake wa kusaidia ujenzi wa mradi mkubwa wa kimkakati wa Reli ya Kisasa (SGR), sekta ya madini, kilimo, elimu na ujenzi wa miundombinu mbalimbali. 


Dkt. Mwamba alisema kuwa mpango wa Benki ya Dunia wa kuboresha sekta ya kilimo Barani Afrika unakwenda sambamba na vipaumbele vya Serikali ya   Tanzania kuendeleza sekta hiyo kupitia Dira ya Taifa ha Maendeleo ya 2050.

Uwekezaji wa Benki ya Dunia katika utekelezaji wa miradi mbalimbali ya kiuchumi na kijamii nchini Tanzania umefikia dola za Marekani bilioni 10.9 ambapo miradi 38 ya maendeleo ya kitaifa na kikanda inatekelezwa katika sekta mbalimbali ikiwemo afya, maji, elimu, nishati, ujenzi wa miundombinu ya barabara, na huduma za kijamii ikiwemo masoko na kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi.

Kikao hicho kilihudhuriwa pia na Katibu Mkuu, Fedha na Mipango kutoka Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, Dkt. Juma Malik Akil na Kamishna Msaidizi wa Fedha za Nje, Wizara ya Fedha, Bw. Robert Mtengule.

DKT. KIKWETE NA MAKAMU WA RAIS DKT. MPANGO WASHIRIKI KUAGA MWILI WA RAILA ODINGA NAIROBI









Rais mstaafu wa Tanzania, Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, pamoja na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Philip Mpango, wameshiriki kushiriki kuaga mwili wa Waziri Mkuu Mstaafu wa Kenya, Mhe. Raila Amolo Odinga, aliyefariki akiwa Nchini India tarehe 15 Oktoba 2025. Mazishi hayo ya kitaifa yamefanyika leo tarehe 17 Oktoba 2025, katika Uwanja wa Nyayo, Jijini Nairobi.

Katika hafla hiyo, Dkt. Mpango alimfariji Rais wa Kenya, Mhe. Dkt. William Ruto, kufuatia msiba mkubwa uliogusa mioyo ya Wakenya na wananchi wa Afrika Mashariki. Kwa upande wake, Dkt. Kikwete ni miongoni mwa waombolezaji waliokusanyika kushiriki kumuaga Odinga, akionesha heshima ya dhati kwa marehemu ambaye hakuwa tu mwanasiasa, bali pia mshirika wa dhati katika juhudi za kudumisha amani, demokrasia na mshikamano barani Afrika.

Kumbukumbu za kihistoria zinaonesha jinsi Rais Kikwete alivyojenga uhusiano wa karibu na Kenya, hususan mwaka 2008 alipokuwa Mwenyekiti wa Umoja wa Afrika, wakati Kenya ilikumbwa na mgogoro wa kisiasa uliosababisha vifo na machafuko makubwa. Wakati huo, Dkt. Kikwete, akiwa sambamba na Hayati Kofi Annan na Hayati Benjamin Mkapa, alishiriki moja kwa moja katika mchakato wa usuluhishi wa kisiasa uliomleta pamoja Rais Mwai Kibaki na Raila Odinga, hatua iliyorejesha amani na kuzaliwa kwa Serikali ya Maridhiano.

Akizungumza kwa niaba ya Serikali ya Tanzania, Dkt. Mpango alieleza kuwa marehemu Raila Odinga alikuwa kiongozi shupavu, mzalendo na mtetezi wa haki za watu, ambaye mchango wake utaendelea kukumbukwa katika historia ya ukombozi wa kisiasa na maendeleo ya bara la Afrika.

Mazishi hayo yameakisi umoja, heshima na ujirani mwema uliopo kati ya Tanzania na Kenya, huku ujumbe wa amani, mshikamano na upendo ukitawala hafla hiyo ya kihistoria.

#RailaOdinga #DktKikwete #DktPhilipMpango #WilliamRuto #KenyaTanzaniaUnity #UjiraniMwema #AfricaPeace #UmojaWaAfrika

DC Magoti Aongoza Mazoezi ya Afya Kisarawe, Ahamasisha Jamii Kujikinga na Magonjwa Yasiyo ya Kuambukiza 🌿

 





Mkuu wa Wilaya ya Kisarawe, Mhe. Petro Magoti, ameongoza wajumbe wa Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya katika mazoezi ya pamoja yaliyolenga kuimarisha afya na ustawi wa mwili. Mazoezi hayo yamefanyika kwa lengo la kujikinga dhidi ya magonjwa yasiyo ya kuambukiza kama vile presha, kisukari, unene uliopitiliza (obesity) na mengineyo yanayotokana na kukosa mazoezi ya mara kwa mara.

Akizungumza baada ya mazoezi hayo, Mhe. Magoti amesisitiza umuhimu wa viongozi na wananchi kwa ujumla kujenga utamaduni wa kufanya mazoezi angalau mara tatu kwa wiki ili kudumisha afya njema, kuongeza ufanisi kazini, na kupunguza gharama za matibabu.

Amesema kuwa afya bora huanza na maamuzi madogo ya kila siku, na kwamba kufanya mazoezi ni njia rahisi, ya bure na yenye manufaa makubwa kwa maisha ya kila mtu.

Mazoezi hayo yamepambwa na hamasa kubwa kutoka kwa washiriki, yakidhihirisha mshikamano na dhamira ya pamoja ya kujenga jamii yenye afya bora na yenye tija.

#MazoeziNiAfya #Kisarawe #DCMagoti #AfyaBoraKwaWote #PamojaTunaweza

DKT. ABBAS: ONGEZEKO LA WATALII KICHOCHEO CHA UWEKEZAJI HIFADHINI.








Katibu Mkuu Wizara ya Maliasili na Utalii Mhe. Dkt. Hassan Abbas leo Oktoba 17, 2025 ametembelea Hifadhi ya Taifa Mkomazi na kukagua mradi wa faru Mbula ikiwa ni moja ya ahadi alizozitoa Septemba 30, 2025 mara baada ya kukabidhi vitendea kazi katika kituo cha udhibiti wa wanyamapori waharibifu Goha wilayani Korogwe mkoani Tanga. 

Katika ziara hiyo Dkt. Abbas alieleza kuwa zao la utalii ni matokeo chanya ya uhifadhi inayofanywa na maafisa na askari. Akiongea na TANAPA katika kikao kifupi Dkt. Abbas alisema,

"Ongezeko la Utalii ni matokeo ya Uhifadhi mnaufanya, tuzidi kushirikiana tusiishie tulipo, twende mbali zaidi kwa kutumia rasilimali zilizopo. Tuwekeze kwenye kujitangaza katika vivutio tulivyonavyo na siyo kujifungia ndani tukisubiri watalii waje ndipo wajifunze kujua mazao tuliyonayo. Tuwekeze kwenye maeneo ambayo tukiulizwa ndani ya miaka mitano au kumi ijayo ithibitishe uwekezaji tulioufanya umeleta tija na mapinduzi ya sekta ya utalii na uchumi kwa ujumla".

Aidha Dkt. Abbas aliongeza kuwa  Wizara kupitia Jeshi la Uhifadhi  linaendelea na mkakati wa kukusanya fedha kupitia Mfuko wa Uhifadhi wa Wanyamapori (TWDF) pamoja na Mfuko wa maendeleo ya utalii (TDl) itokanayo na mapato ya utalii mahifadhini na kutolewa kwa asilimia 3% hadi 6% kuilinda mifuko hiyo kwaajili ya kukuza utalii na uhifadhi. Pia amesema kuwa serikali imeongeza nguvu kwa kugawa vifaa na kuboresha miundombinu ili kutatua changamoto zinazokwamisha shughuli za uhifadhi. 

Naye, Mkuu wa Kanda ya Kaskazini Naibu Kamishna wa Uhifadhi Steria Ndaga, alimkaribisha Katibu Mkuu na kumshukuru kwa jitihada zote zinazofanyika kuunga mkono maendeleo ya sekta ya uhifadhi na utalii yenye mchango mkubwa katika ongezeko la pato la Taifa nchini. 

Akiwasilisha taarifa fupi ya Hifadhi Kamishna Msaidizi wa Uhifadhi Emmanuel Moirana alitoa takwimu na kuonesha kuwa Hifadhi ya Taifa Mkomazi inapiga hatua katika ongezeko kubwa la watalii toka idadi ya watalii 489 kwa mwaka 2015/2016 na hadi kufikia idadi ya 10991 kwa mwaka 2024/2025. 

Mara baada ya kikao hicho Dkt. Abbas alipata nafasi ya kutembelea mradi wa Faru Mbula wenye Kilometa za mraba 13 na kujionea faru 9 kati ya 13 waliomo katika mradi huo.

Saturday, October 11, 2025

UTAFITI MIAMBA BONDE LA EYASI WEMBERE WATHIBITISHA UWEZEKANO WA UPATIKANAJI MAFUTA














📌 *Dkt Mataragio akagua shughuli za utafiti na kutoa maelekezo kwa TPDC/AGS* 

📌 *Awamu ya  pili ya utafiti kukamilika Aprili 2026.* 

 *📌Asilimia 90 ya wanaotekeleza mradi ni watanzania* 

Utafiti unaofanyika katika  mradi wa kimkakati wa  Eyasi Wembere unaolenga kutafuta mafuta na gesi katika bonde la ufa la Afrika  Mashariki umeonesha matumaini makubwa ya kupatikana kwa Mafuta na Gesi katika bonde hilo.

Hayo yamebainika wakati Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati, Dkt. James Mataragio alipofanya ziara ya kukagua maendeleo ya utekelezaji wa  mradi huo mkoani Arusha wilaya ya Karatu

 “Kazi za utafiti wa mradi huu zimeanza mwaka 2015,  tumekuwa tukikusanya data mbalimbali zinazohusiana na uwepo wa mafuta na gesi ambapo baada ya ukusanyaji,  data hizo zilitumika kubainisha miamba tabaka ambayo ina mafuta na tukajiridhisha kwamba katika eneo hili la bonde  ipo miamba ambayo inaweza ikahifadhi mafuta”.Amesema Dkt. Mataragio.

 Dkt. Mataragio ameeleza kuwa, data za awali za utafiti zilizoanza 2015 kwa njia ya ndege na uchorongaji visima vifupi ambpo ziligharimu takribani shilingi bilioni nane. 

Aliendelea kufafanua kuwa data za awamu ya kwanza kwa njia ya mitetemo  zenye urefu wa kilometa 260  ziligharimu takribani shilingi bilioni 10.

Aidha, shughuli za utafiti katika awamu ya pili zitahusisha eneo la kilomita  914  zitagharimu shillingi bilioni 43 ambapo kilomita 430 ndio zimekamilika sawa na asilimia 47.

Akizungumzia faida zitakazopatikana nchi ikipata mafuta kutoka eneo hilo ni pamoja na uhakika wa uwepo wa mafuta na kupunguza gharama za ununuaji wa mafuta nje ya nchi.

 “Tutaweza pia kutunza akiba ya fedha za kigeni ambazo zinatumika  kwa ajili ya kuagiza mafuta nje ya Nchi”. Ameongeza  Dkt. Mataragio

Katika hatua nyingine, Dkt. Mataragio amesema kuwa kutoka kuanza kwa mradi  mwaka 2015 takribani  asilimia 90 ya wanaotekeleza mradi ni watanzania. 

Baada ya ukaguzi wa mradi huo,  Dkt. Mataragio ameliagiza Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC)  pamoja na Mkandarasi kampuni ya AGS  kuhakikisha kuwa wanakamilisha mradi kabla ya mwezi Aprili na kazi ziendelee hata kipindi cha mvua.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Utafutaji Uendelezaji na uzalishaji Mafuta na Gesi kutoka TPDC, Mjiolojia Paschal Njiko amesema TPDC  inafanya utafiti katika bonde hilo kwa kushirikiana na Mkandarasi mzawa kampuni ya  African Geographical Services (AGS).

 Njiko amesema TPDC imepokea maagizo yaliyotolewa na Naibu Katibu Mkuu na itahakikisha inamsimamia Mkandarasi ili kuhakikisha utafiti wa awamu ya pili unakamilika kwa wakati.

Naye, Mwenyekiti wa kampuni ya AGS ambayo ni Mkandarasi anayesimamia utafiti katika Bonde la Eyasi Wembere, Salum Haji amesema wanatambua unuhimu wa mradi huo kwa kwa taifa hivyo  watahakikisha utafiti unakamilika kwa wakati kama ilivyopangwa. 

Kwa upande wake, mmoja wa wanufaika wa  mradi wa Bonde la Eyasi Wembere, Biru Benjamini amesema "kupitia mradi huu sisi vijana tuliokuwa mtaani tumenufaika na ajira na pia kupata ujuzi."

Friday, October 10, 2025

ABSA WAJIONEA MAAJABU YA MIRADI YA NHC DAR ES SALAAM

Mkurugenzi Mtendaji wa ABSA Tanzania, Bw. Obedi Laiser akikaribishwa na Bw. Deogratious BatakanwaMeneja wa Mauzo na Masoko wa NHC kwenye mradi wa Kawe 711 jijini Dar es Salaam.

Injinia Grace Musita, Meneja Miradi wa NHC, akitoa maelezo kuhusu maendeleo ya mradi wa Samia Housing Scheme – Kijichi kwa maafisa wa Benki ya Absa Tanzania.


Timu ya wataalamu kutoka Benki ya ABSA Tanzania ikiwa katika ziara maalum katika mradi wa Samia Housing Scheme – Kijichi jijini Dar es Salaam.


Timu ya Benki ya ABSA Tanzania ikiwa katika picha ya pamoja kwenye mradi wa Kawe 711 jijini Dar es Salaam.





Mkurugenzi Mtendaji wa ABSA Tanzania, Bw. Obedi Laiser akiongozana na Bw. Deogratious BatakanwaMeneja wa Mauzo na Masoko wa NHC kwenye mradi wa Kawe 711 jijini Dar es Salaam.

Afisa Mkuu wa Mauzo na Masoko wa NHC, Emmanuel Lyimo akiwaeleza jambo Wataalamu wa Benki ya ABSA walipokuwa kwenye majengo ya Samia Housing Scheme Kawe.

Tarehe 10 Oktoba 2025, timu ya wataalamu kutoka Benki ya ABSA Tanzania imefanya ziara maalum katika miradi mikubwa ya makazi inayotekelezwa na Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) jijini Dar es Salaam — ikiwemo Samia Housing Scheme – Kijichi na Kawe 711 Housing Project.

Lengo la ziara hiyo lilikuwa ni kuwajengea uelewa maafisa wa ABSA kuhusu utekelezaji wa miradi ya NHC, kuonyesha fursa za ununuzi wa nyumba, na kuimarisha ushirikiano katika kusaidia Watanzania kumiliki makazi bora kupitia mikopo ya nyumba.

Ziara hiyo iliongozwa na Mkurugenzi Mtendaji wa ABSA Tanzania, Bw. Obedi Laiser, ambaye hakuficha furaha yake baada ya kujionea kazi kubwa inayofanywa na NHC katika kubadilisha sura ya makazi nchini.

“Tumepata fursa nzuri ya kujifunza na kujionea kazi kubwa inayofanywa na NHC. Nyumba hizi ni za kisasa, zenye ubora wa juu na zitachangia kwa kiasi kikubwa kupunguza changamoto ya uhaba wa makazi nchini. Tunawapongeza NHC kwa ubunifu na ufanisi mkubwa katika utekelezaji wa miradi hii,” alisema Bw. Laiser.

Aidha, alisisitiza kuwa ubora wa miradi ya NHC unaendana kikamilifu na falsafa ya chapa ya ABSA inayosema “Hadithi yako ina thamani”, akifafanua kuwa nyumba hizo zinaakisi maisha halisi ya Watanzania na ndoto zao za kumiliki makazi bora.

Kwa upande wa NHC, Meneja Miradi, Injinia Grace Musita, aliyeongoza maelezo kwa niaba ya Shirika, alieleza kuwa miradi ya Samia Housing na Kawe 711 ni sehemu ya utekelezaji wa dira ya Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan.

“NHC imejipanga kuhakikisha kila Mtanzania anapata makazi bora, salama na ya kisasa. Miradi hii inajengwa kwa kutumia teknolojia za kisasa, ubora wa hali ya juu na kwa kuzingatia mazingira rafiki,” alisema Injinia Musita.

Naye Bw. Deogratious Batakanwa, Meneja wa Mauzo na Masoko wa NHC, aliishukuru Benki ya ABSA kwa ushirikiano wa muda mrefu katika kusaidia ujenzi na mauzo ya nyumba za Shirika.

“Tunathamini ushirikiano wa ABSA kwa kutuwezesha kifedha katika ujenzi wa miradi yetu, na pia kwa kuwasaidia wateja wetu kupata mikopo ya nyumba. Ushirikiano huu ni mfano bora wa taasisi za kifedha na sekta ya makazi kufanya kazi kwa pamoja kwa manufaa ya Watanzania,” alisema Bw. Batakanwa.

Ziara hiyo imetajwa kuwa ni mwanzo wa hatua mpya ya ushirikiano wa kimkakati kati ya NHC na ABSA Tanzania, ikilenga kuendeleza jitihada za kuhakikisha Watanzania wengi zaidi wanapata makazi bora, yenye hadhi na ya gharama nafuu.

Kupitia miradi kama Samia Housing Scheme – Kijichi na Kawe 711, NHC inaendelea kuthibitisha uwezo wake wa kubadilisha mandhari ya miji ya Tanzania na kuwa nguzo muhimu katika ujenzi wa Taifa lenye ustawi wa makazi bora kwa wote.

🏠 NHC – Tunajenga Taifa, Tunakuza Ndoto.
#NHC #ABSA #Kawe711 #SamiaHousing #MakaziBora #UshirikianoWaMaendeleo #TunajengaTaifa #DarEsSalaam

 

CHUO KIKUU MZUMBE CHAPOKEWA MSAADA WA VITABU KUTOKA ACCA

  Chuo Kikuu Mzumbe kimepokea vitabu 69 vya kufundishia na kujifunzia kutoka Association of Chartered Certified Accountants (ACCA) kupitia o...