Monday, July 28, 2025

WAZIRI MKUU MAJALIWA KUFUNGUA CHAN2024 KWA MKAPA

 






 Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika  ufunguzi wa mashindano ya CHAN 2024, yanayotarajiwa kuanza rasmi Agosti 02, 2025 katika  Uwanja wa Benjamin Mkapa Dar es Salaam.

Amebainisha hayo Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo na Msemaji Mkuu wa Serikali  Gerson Msingwa Julai 28, 2025 jijini Dar es Salaam  wakati akikagua  maandalizi ya Ufunguzi huo.

Amesema kuwa, nchi 5 za Afrika ambazo ni Burkinafaso, Algeria, Jamuhuri ya Afrika ya Kati, Maurtania, Madagascar tayari zimeanza kuwasili kuanzia  Julai 28,2025.

"Kabla ya uzinduzi huo, uwanja  utapambwa na burudani za  Mziki ambazo zitahusisha wasanii wa Singeli (CHAN SINGELI FEST) ambalo litafanyika nje ya Uwanja wa Benjamin Mkapa, bila kiingilio,  kuanzia Julai 30 hadi 31, 2025" alisema Msigwa.  

Ameongeza  kuwa, mashindano hayo ni moja ya maandalizi  ya kuelekea kuwa wenyeji wa AFCON 2027,  hivyo  ni nafasi nzuri ya kufanya maandalizi ikiwemo kuwakaribisha wageni kwani njia za kuingia  nchini zimerahisishwa.

Mwenyekiti wa CCM Taifa, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan Aongoza Kikao cha Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya CCM Jijini Dodoma












Dodoma, 28 Julai 2025 – Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi (CCM) Taifa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, leo ameongoza kikao cha Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya CCM Taifa, kilichofanyika jijini Dodoma kwa madhumuni ya kujadili masuala muhimu ya chama na ustawi wa taifa kwa ujumla.

Kikao hicho cha juu cha uongozi wa CCM kimewakutanisha viongozi hao waandamizi wa chama kujadili majina ya watia nia. Aidha, kikao hicho kimeangazia pia mipango ya chama kuelekea uchaguzi wa serikali za mitaa na maandalizi ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2025.

Mwenyekiti wa CCM, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika hotuba yake ya ufunguzi wa kikao, amesisitiza umuhimu wa viongozi wa chama kuendelea kuwa karibu na wananchi, kuhakikisha utekelezaji wa ahadi zilizotolewa wakati wa kampeni unaendelea kwa kasi na ufanisi. Amesisitiza pia dhamira ya chama kuendeleza utulivu wa kisiasa, mshikamano wa kitaifa na maendeleo jumuishi.

“Ni wajibu wetu kama viongozi wa CCM kuhakikisha kuwa tunasimamia kikamilifu utekelezaji wa Ilani yetu ya uchaguzi, kwa kuwa ndiyo mkataba kati ya chama na wananchi. Tunatakiwa kuwa na chama kinachoishi na kuishi na watu,” alisema Mhe. Dkt. Samia.

Viongozi mbalimbali waliotoa michango yao katika kikao hicho wameelezea mafanikio ya Serikali chini ya uongozi wa CCM, huku wakipendekeza maeneo ya kuboresha zaidi huduma za jamii, miundombinu, elimu, afya na uwezeshaji wa vijana na wanawake.

Kikao hiki cha Kamati Kuu ni sehemu ya mfululizo wa mikutano ya ndani ya chama inayolenga kuimarisha utekelezaji wa majukumu ya CCM kama chama tawala, pamoja na kuhakikisha kuwa masuala ya msingi yanashughulikiwa kwa mujibu wa dira na misingi ya chama.

Mwisho wa kikao, wajumbe walieleza kuridhishwa na maelekezo ya Mwenyekiti na kuweka mikakati ya pamoja ya kusimamia kwa karibu utekelezaji wa maazimio yaliyopitishwa.

Saturday, July 26, 2025

Tanzania na Rwanda Zaimarisha Ushirikiano kwa Kusaini Hati Mbili za Makubaliano











Mkutano wa 16 wa Tume ya Kudumu ya Pamoja ya Ushirikiano (JPC) kati ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Jamhuri ya Rwanda umefungwa rasmi jijini Kigali leo tarehe 26 Julai 2025, baada ya mawaziri wa pande zote mbili kusaini hati mbili za makubaliano ya ushirikiano ikiwemo ya kilimo na uanzishwaji wa Ofisi ya Mamlaka ya Bandari ya Tanzania (TPA) jijini Kigali, kama sehemu ya hatua za kuimarisha uhusiano wa karibu na kukuza maendeleo ya pamoja baina ya nchi hizo mbili.

Hati hizo zimesainiwa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki wa Tanzania, Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo (Mb.), na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Balozi Olivier Nduhungirehe ikilenga kuimarisha ushirikiano wa kimkakati kati ya Tanzania na Rwanda kwa manufaa ya wananchi wa mataifa haya mawili. Kupitia makubaliano ya sekta ya kilimo, pande zote zimekusudia kubadilishana uzoefu, teknolojia, utaalamu na taarifa muhimu ili kuongeza uzalishaji, usalama wa chakula na fursa za biashara ya mazao ya kilimo. 

Aidha, uanzishwaji wa Ofisi ya Mamlaka ya Bandari ya Tanzania (TPA) jijini Kigali unalenga Kurahisisha upatikanaji wa huduma za Bandari nchini Rwanda, kupunguza gharama za bidhaa, kuimarisha na kuongeza matumizi ya Bandari za Tanzania kama lango kuu ka kupitisha mizigo na shehena za Rwanda

Akizungumza wakati wa hafla ya kufunga mkutano, Waziri Kombo amesisitiza umuhimu wa utekelezaji wa makubaliano yote yaliyoafikiwa katika mkutano huo na kuwataka wataalamu na viongozi wa serikali kuhakikisha kuwa mipango na maazimio ya JPC yanatekelezwa kwa wakati. 

Kwa upande wake, Waziri Nduhungirehe ameipongeza Tanzania kwa ushirikiano mzuri na kusisitiza kuwa Rwanda itaendelea kushirikiana kwa karibu na nchi jirani ili kuhakikisha maridhiano ya kweli yanapatikana kupitia utekelezaji wa maazimio yaliyofikiwa. Ameeleza kuwa makubaliano kama hayo ni nyenzo muhimu ya kukuza uchumi, kuboresha usalama wa chakula, na kuimarisha mshikamano wa kidiplomasia na kijamii kati ya mataifa hayo mawili.

Mkutano wa 16 wa JPC umejadili masuala mbalimbali ya ushirikiano ikiwemo biashara, ulinzi na usalama, miundombinu, afya, elimu, nishati, na kilimo. Mazungumzo hayo yamekuwa na tija kubwa na kufanikisha hatua za pamoja za kuendeleza mahusiano ya kidiplomasia na kiuchumi baina ya Tanzania na Rwanda.

WAZIRI KOMBO AFUNGUA MILANGO MIPYA YA USHIRIKIANO KATI YA TANZANIA NA RWANDA KUPITIA MKUTANO WA JPC KIGALI

 








Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo (Mb.), amefungua rasmi Mkutano wa 16 wa Tume ya Kudumu ya Pamoja ya Ushirikiano (JPC) kati ya Tanzania na Rwanda, uliofanyika tarehe 26 Julai 2025 jijini Kigali, Rwanda.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mkutano huo, Waziri Kombo ametoa salamu za kindugu kutoka kwa Serikali na Wananchi wa Tanzania kwa Serikali ya Jamhuri ya Rwanda, huku akitoa shukrani za dhati kwa mapokezi ya ukarimu na mazingira mazuri ya mkutano huo.

Waziri Kombo amebainisha kuwa miradi ya pamoja ya kimkakati inayotekelezwa na nchi hizo mbili, ikiwemo Mradi wa Umeme wa Rusumo, kituo cha pamoja cha forodha cha Rusumo (OSBP), pamoja na reli ya kisasa (Standard Gauge Railway – SGR), kuwa ni vielelezo vya mafanikio ya ushirikiano wa muda mrefu.

Licha ya mafanikio hayo, Mhe. Kombo amesisitiza kuwa bado kuna nafasi kubwa ya kuendeleza ushirikiano huo, hasa katika maeneo ya biashara, uwekezaji, kilimo, afya, teknolojia ya habari na mawasiliano (TEHAMA), nishati, utalii na miundombinu.

Kwa upande wake, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa wa Rwanda, Mhe. Balozi Olivier Nduhungirehe, ameeleza kuwa uhusiano kati ya Rwanda na Tanzania una historia ya kina inayojengwa juu ya maadili ya pamoja, undugu wa karibu, na maono ya maendeleo ya pamoja.

Waziri Nduhungirehe pia amesisitiza mchango mkubwa wa Tanzania kama mshirika wa kimkakati wa biashara na maendeleo ya Rwanda, akieleza kuwa zaidi ya asilimia 70 ya mizigo ya Rwanda husafirishwa kupitia Bandari ya Dar es Salaam. Aidha, amepongeza hatua ya kufunguliwa kwa Ofisi ya Mamlaka ya Bandari ya Tanzania (TPA) mjini Kigali.

RAIS SAMIA AKUTANA NA RAIS WA K-FINCO KUIMARISHA USHIRIKIANO WA KIMAENDELEO

 













Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, amekutana na kufanya mazungumzo na Rais wa Shirika la Fedha na Ujenzi la Korea (Korea Infrastructure Finance Corporation - K-FINCO), Dkt. Eun-Jae Lee, leo tarehe 26 Julai 2025, Ikulu Chamwino, Dodoma.

Katika mazungumzo hayo, viongozi hao wamejadili fursa mbalimbali za ushirikiano baina ya Tanzania na Korea ya Kusini, hususan katika nyanja za miundombinu, fedha, na uwekezaji. Ujumbe wa Dkt. Lee umeonesha nia thabiti ya kushirikiana na Serikali ya Tanzania katika kutekeleza miradi mikubwa ya maendeleo ikiwemo ya barabara, bandari, makazi na miundombinu ya kijamii.

Rais Samia amesisitiza dhamira ya Serikali kuendelea kushirikiana na wadau wa kimataifa wanaoonesha utayari wa kuisaidia Tanzania katika kukuza uchumi, kutoa ajira, na kuboresha maisha ya Watanzania.

Mazungumzo haya ni hatua muhimu katika kuimarisha uhusiano wa kidiplomasia na kiuchumi kati ya Tanzania na Korea ya Kusini, na yanatarajiwa kufungua milango ya ushirikiano zaidi katika sekta mbalimbali.

#TanzaniaYaViwanda
#UwekezajiTanzania
#SamiaSuluhu
#KFincoTanzania
#Dodoma2025
#MiundombinuNaMaendeleo

Thursday, July 24, 2025

*KAMISHNA KUJI AKAGUA ENEO LA KOGATENDE SERENGETI ASISITIZA MAAFISA NA ASKARI UHIFADHI KUENDELEA KUSIMAMIA SHERIA ZA HIFADHI ILI KUIMARISHA SHUGHULI ZA UTALII












Na. Philipo Hassan - Serengeti

Kamishna wa Uhifadhi, Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA) CPA Musa Nassoro Kuji, leo Julai 24, 2025 amefanya ukaguzi katika eneo la vivuko vya nyumbu (Kogatende) ndani ya Hifadhi ya Taifa Serengeti. Katika ukaguzi huo alielekeza Maafisa na Askari Uhifadhi kusimamia sheria ipasavyo, taratibu na miongozo mbalimbali ya Hifadhi za Taifa ili kuboresha shughuli za utalii endelevu usioharibu mazingira.

Ziara ya Kamishna Kuji ni muendelezo wa ziara zake za kikazi kukagua shughuli za maendeleo na utekelezaji wa miongozo mbalimbali iliyowekwa na Wizara ya Maliasili na Utalii ili kuwa na uhifadhi endelevu ambao ndio kiini cha utalii tunaoushuhudia leo ukilipatia Shirika na Taifa mapato na fedha za kigeni ambazo zimeendelea kuchagiza katika uchumi wa Taifa letu.

Akizungumza katika ziara hiyo Kamishna Kuji alitoa maagizo kwa Maafisa na Askari Uhifadhi wanaosimamia shughuli za utalii katika Hifadhi ya Taifa Serengeti kuendelea kusimamia sheria, kanuni na taratibu zilizotungwa na Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ili kuboresha huduma bora kwa watalii na kuwakumbusha kuzifuata ili kuondoa mkanganyiko wa mara kwa kwa mara. 

Aidha, Kamishna Kuji alisema, “Endeleeni kuchukua tahadhari na kuendelea kusimamia taratibu na sheria za hifadhi zilizowekwa kwa ajili ya kudhibiti vitengo vya uvunjifu wa sheria na miongozo ya hifadhi iliyowekwa. Kuweni imara kudhibiti matendo yanayokiuka taratibu zote za kiuhifadhi zinazofanywa na waongoza utalii wasio na weledi kama vile kushusha watalii kwenye  magari maeneo yasiyoruhusiwa ambayo ni hatari kwa watalii na waongoza watalii pia”.

Vilevile, CPA Kuji aliongeza, Simamieni na kuthibiti magari yanayotumia njia zisizo halali na rasmi  “Offroading”, kutupa taka hifadhini, mwendokasi na tabia ya kulisha wanyamapori, kwa wale watakaokengeuka na kutotii sheria na taratibu hizo, sheria ichukue mkondo wake”.  

Naye, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Uhifadhi Stephano Msumi ambaye ni Mkuu wa Hifadhi ya Taifa Serengeti akitoa taarifa ya tukio lililotokea Julai 21, 2025 ambapo picha jongefu na mnato zilionekana katika mitandao ya kijamii zikionesha watalii wakiwa wameshuka kutoka kwenye magari

katika eneo la Kogatende kivuko namba nne wameshajulikana na taratibu za adhabu zinaendelea kuchukuliwa kwa kufuata miongozo na hatutamuonea mtu wala kumfumbia mtu macho.

“ Hata hivyo, Afande Kamishna, kama hifadhi hii mama na yenye watalii wengi tumeshachukua hatua kali za kisheria kutokana na tukio hilo ambapo kampuni zote zilizohusika kuvunja sheria na taratibu kwa kushusha watalii kutoka kwenye magari yao katika maeneo ambayo hayaruhusiwi tayari zimeanza kuchukuliwa”, alisema Mhifadhi Msumi.

Kamishna Msumi aliongeza kuwa “Ni jukumu la kila mmoja wetu kwa maana ya TANAPA, waongoza watalii, madereva pamoja na wadau wote wa utalii kuhakikisha kuwa tunafuata sheria, taratibu na miongozo iliyowekwa tuwapo hifadhini ili kuendelea kutunza maliasili zetu ambazo ni chanzo cha kuleta watalii kutoka maeneo mbalimbali duniani.  Na watalii hao hukuza uchumi wa watanzania pamoja na kuchangia kuongeza pato la Taifa.

Katika kuhitimisha ziara yake Kamishna Kuji ametoa maelekezo kwa uongozi wa Kanda ya Magharibi na Hifadhi ya Taifa Serengeti kuongeza nguvu katika kuimarisha shughuli za ulinzi na usalama katika eneo la Nyatwali Wilayani Bunda ambalo Shirika limekabidhiwa kwa ajili ya kulijumuisha kuwa sehemu ya Hifadhi ya Taifa Serengeti kwa manufaa ya shughuli za uhifadhi na utalii hapa nchini. ‎

WAZIRI MKUU MAJALIWA KUFUNGUA CHAN2024 KWA MKAPA

   Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika  ufunguzi wa mashindano ya CHAN 2...