Thursday, February 13, 2025

Spika wa Bunge, Mhe. Dkt. Tulia Ackson, Aongoza Kikao cha Maandalizi cha Mkutano wa 6 wa Maspika Duniani





New York, Marekani – Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Rais wa Umoja wa Mabunge Duniani (IPU), Mhe. Dkt. Tulia Ackson, ameongoza Kikao cha Kamati ya Maandalizi cha Mkutano wa 6 wa Maspika Duniani, unaotarajiwa kufanyika mwezi Julai 2025 mjini Geneva, Uswisi.

Kikao hicho kimefanyika tarehe 12 Februari 2025 katika ukumbi wa Umoja wa Mataifa (UN) jijini New York, Marekani, kikiwaleta pamoja viongozi mashuhuri wa mabunge kutoka mataifa mbalimbali duniani. 

Mkutano huo ulihudhuriwa na Mwakilishi wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Katibu Mkuu wa IPU, pamoja na Maspika, Manaibu Spika, na Wakuu wa Misafara wa Mabunge kutoka China, Uingereza, Nigeria, Hispania, Bahamas, Malta, Azerbaijan, Ivory Coast, Mexico, Uswisi, Algeria, Malawi, Canada, na Qatar.

Katika kikao hicho, washiriki walijadili maandalizi ya mkutano huo mkubwa wa viongozi wa mabunge duniani, wakitilia mkazo masuala muhimu ya ushirikiano wa mabunge, demokrasia, na maendeleo ya kimataifa. 

Uongozi wa Mhe. Dkt. Tulia Ackson katika kikao hiki unaendelea kuonesha nafasi muhimu ya Tanzania katika masuala ya kidiplomasia na ushirikiano wa kimataifa kupitia Bunge.

Mkutano wa 6 wa Maspika Duniani unatarajiwa kuwa jukwaa muhimu la kujadili changamoto na fursa za mabunge katika kusimamia maendeleo endelevu, amani, na utawala bora duniani.

No comments:

SAMIA AZINDUA MKUTANO WA KIMATAIFA WA WFNS, ATEMBELEA MAONESHO YA SEKTA YA AFYA

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, akitembelea mabanda ya maonesho ya wadau wa Sekta ya Afya kabla ya k...