RUAHA, IRINGA – Msajili wa Hazina na Mlezi wa Great Ruaha Marathon, Bw. Nehemiah Mchechu, ambaye alimwakilisha Mgeni Rasmi, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mwigulu Nchemba, amesema kuwa uhifadhi wa mazingira ni nguzo muhimu ya ukuaji wa uchumi wa Taifa na ustawi wa wananchi.
Akizindua rasmi Great Ruaha Marathon 2026 leo Julai 4, 2026 katika Hifadhi ya Taifa Ruaha, Bw. Mchechu alisema Mto Ruaha Mkuu ni moja ya vyanzo muhimu vya uhai nchini, ukiwezesha shughuli za kilimo, ufugaji, uzalishaji wa umeme pamoja na kuhifadhi mfumo wa ikolojia wa Hifadhi ya Taifa Ruaha.
Alisisitiza kuwa kulinda mazingira na vyanzo vya maji si jukumu la Serikali pekee, bali ni wajibu wa kila Mtanzania kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.
"Tunataka Watanzania wengi zaidi watembelee hifadhi zetu, wajivunie urithi tulionao na wawe mabalozi wa utalii wa nchi yao," amesema Mchechu.
Kwa upande wake, Kamishna wa Uhifadhi wa TANAPA, Massana Gibril Mwishawa, amesema utalii wa michezo umeendelea kuwa nyenzo muhimu ya kuitangaza Tanzania duniani, kuvutia watalii na wawekezaji, pamoja na kukuza biashara na uchumi wa Taifa.
Ameeleza kuwa TANAPA imejipanga kuendeleza utalii wa michezo kama zao jipya la kimkakati litakaloongeza mchango wa sekta ya utalii katika maendeleo ya nchi.
Naye Mratibu wa Great Ruaha Marathon, Hamim Kilahama, amesema mbio hizo si mashindano ya riadha pekee bali ni jukwaa la kuhamasisha jamii kulinda mazingira, kuhifadhi vyanzo vya maji vya Mto Ruaha Mkuu na kuitangaza Kanda ya Kusini kama kitovu cha utalii.
Amebainisha kuwa kwa mwaka wa tano mfululizo, Great Ruaha Marathon imeendelea kufungua fursa mpya za kuitangaza Hifadhi ya Taifa Ruaha kupitia utalii wa michezo, huku ikichochea maendeleo ya jamii na uchumi wa maeneo yanayozunguka hifadhi hiyo.
Hifadhi ya Taifa Ruaha, ambayo ni miongoni mwa hifadhi kubwa zaidi barani Afrika, inaendelea kuwa hazina ya kipekee ya utalii ikiwa na wanyamapori wengi wakiwemo tembo, simba, chui, mbwa mwitu wa porini, twiga, nyati na mamia ya aina za ndege wanaovutia wageni kutoka duniani kote.
Great Ruaha Marathon imeendelea kuthibitisha kuwa michezo, uhifadhi na utalii vinaweza kwenda sambamba katika kujenga uchumi imara, kulinda rasilimali za Taifa na kuitangaza Tanzania kimataifa.






















.jpeg)

.jpeg)

.jpeg)
.jpeg)













