Tuesday, February 03, 2026

WMA YAFUNGA MTAMBO WA KISASA UNAOHAKIKI DIRA ZA MAJI DODOMA

Mtambo wa kisasa unaotumika kuhakiki dira za maji. Mtambo huu wa kidijitali umefungwa katika Jengo la Makao Makuu ya Wakala wa Vipimo (WMA), Dodoma.

Sehemu ya Mtambo wa kisasa unaotumika kuhakiki dira za maji. Mtambo huu wa kidijitali umefungwa katika Jengo la Makao Makuu ya Wakala wa Vipimo (WMA), Dodoma.

Jengo lenye mitambo ya kuhakiki dira za maji, lililopo katika Kituo cha Uhakiki Vipimo Misugusugu, Mkoa wa Pwani.

Afisa Vipimo kutoka Wakala wa Vipimo (WMA), akihakiki dira za maji.

 Veronica Simba - WMA 

Wakala wa Vipimo (WMA) umesimika mtambo wa kisasa wa kidijitali wa kuhakiki dira za maji katika jengo la makao yake makuu lililopo jijini Dodoma.

Meneja Uhakiki wa Vipimo na Viwango wa WMA Makao Makuu, Magesa Biyani amesema usimikaji mtambo huo uliogharimu takribani shilingi milioni 400, utawezesha uidhinishaji na uhakiki wa dira za maji kwa muda mfupi na kwa usahihi zaidi kupitia miradi mingi ya maji inayoendelea kutekelezwa nchini ikiwemo Mkoa wa Dodoma na mikoa mingine jirani.

Akizungumza na wanahabari wa WMA Februari 3, 2026, Biyani amesema kuwa “Mtambo huu umekuja kwa wakati mwafaka kuwezesha wafanyabiashara pamoja na Mamlaka za Maji kuzingatia kwamba dira za maji zote ambazo wanawafungia wateja katika maeneo yao ziwe zimehakikiwa na WMA ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma kulingana na thamani ya fedha wanazolipa.”

Akifafanua zaidi, amesema kuwa mtambo huo una uwezo wa kuhakiki dira za maji nyingi zaidi kwa wakati mmoja kwa kutumia muda mfupi zaidi tofauti na mitambo ya awali ambayo ni ya ki-makenikali (Mechanical Test Bench) yenye uwezo wa kuhakiki dira za maji 10 kwa wakati mmoja ikitumia dakika 20 hadi 30.

Amesema kuwa mtambo huo pamoja na mingine miwili ya aina hiyo iliyoko katika Kituo cha Uhakiki Vipimo, Misugusugu mkoani Pwani, kwa pamoja imeleta faida kubwa ikiwemo kupima dira za maji nyingi zaidi, kwa usahihi zaidi na kwa muda mfupi tofauti na awali kabla ya uwepo wake.

Akitoa mfano, Biyani amesema mathalani kwa Kituo cha Misugusugu ambako mitambo ya aina hiyo ilitangulia kusimikwa kabla ya Dodoma, dira za maji kati ya laki mbili hadi laki tatu zimekuwa zikipimwa kwa mwaka kutegemea na uhitaji kutokana na kuongezeka kwa miradi ya kimkakati.

“Kwahiyo imeleta faida kubwa sana na kusaidia thamani ya fedha iweze kuonekana kwa wateja/wananchi, Mamlaka za Maji na wafanyabiashara na hata kwa uchumi wa nchi,” ameeleza Biyani.

 Akidadavua zaidi namna WMA inavyohusika katika uidhinishaji na uhakiki wa dira za maji, ameeleza kuwa hilo ni mojawapo ya majukumu yake ya uhakiki wa vipimo vya aina mbalimbali nchini kwa lengo la kumlinda mlaji.

Amesema kuwa, WMA huidhinisha na kuhakiki vipimo kwa niaba ya Serikali ambapo kwa upande wa dira za maji, mfanyabiashara yeyote binafsi au kampuni kabla ya kuagiza au kuzalisha bidhaa hizo anatakiwa awasilishe sampuli yake WMA ili kuhakiki muundo wake na baada ya kuidhinishwa anatakiwa kuziwasilisha bidhaa zote alizoagiza au kuzalisha ili zihakikiwe kwa kila moja kujiridhisha kuhusu usahihi wake.

Biyani amefafanua zaidi kuwa zoezi hilo hulenga kuzilinda pande zote mbili yaani mteja na muuzaji ili yeyote kati yao asipunjwe. Dira za maji zilizohakikiwa humuwezesha mteja kulipia kiwango stahiki kulingana na matumizi yake ilhali kwa upande wa muuzaji humwezesha kupata malipo stahiki kulingana na huduma anayotoa.

Akijibu swali la mwandishi kuhusu mipango ya WMA kufikisha huduma hiyo nchi nzima, Biyani ameeleza kuwa Mpango Mkakati wa Wakala wa miaka mitano ijayo kuanzia mwaka huu wa 2026 ni kusimika mitambo ya aina hiyo katika Kanda zote zilizosalia nchini ambazo amezitaja kuwa ni Kanda ya Kaskazini, Kanda ya Ziwa, Kanda ya Magharibi pamoja na Kanda ya Kusini.

Hata hivyo, ameweka bayana kuwa kutokuwepo kwa mitambo ya kisasa katika Kanda tajwa haimaanishi kuwa kazi hiyo haifanyiki katika maeneo hayo, la hasha, inafanyika kwa kutumia mitambo ya ki-makenikali pamoja na ile midogo inayobebeka (Portable Test Kit) ambayo amesema Maafisa Vipimo kote nchini huibeba mikononi na kwenda nayo katika maeneo mbalimbali kuhakiki dira za maji.

Katika hatua nyingine, Biyani ametoa hamasa kwa wadau wa vipimo mkoani Dodoma na mikoa ya jirani hususani katika sekta ya maji kutumia fursa ya uwepo wa mtambo huo wa kisasa kupeleka dira za maji WMA zikahakikiwe na kuidhinishwa.

Biyani ameonya kwamba ni kosa kisheria kwa mtu yeyote kufunga na/au kutumia dira ya maji ambayo haijahakikiwa na Wakala wa Vipimo huku akibainisha kuwa adhabu yake huanzia kutozwa faini ya shilingi laki moja hadi milioni 20 kwa kosa la kwanza na shilingi milioni 20 hadi milioni 50 kwa kosa la pili kutegemea na aina ya kosa.

Ametaja gharama za kuhakiki dira za maji kwa mujibu wa sheria kuwa ni shilingi elfu kumi tu kwa kila moja na kwa uidhinishaji wa muundo ni shilingi elfu hamsini.

Sheria ya Vipimo, Sura Namba 340 kupitia kanuni zake mbalimbali inaielekeza WMA kuhakiki dira za maji walau mara moja kila mwaka lakini pia Wakala hufanya kaguzi mbalimbali za kushtukiza ili kubaini endapo kuna udanganyifu na kuchukua hatua.

Wakala imeendelea kutoa elimu kwa wadau wa vipimo na umma kwa ujumla katika maeneo mbalimbali ikiwemo namna ya kutambua kipimo ambacho kimehakikiwa ambapo kwa upande wa dira za maji, utambuzi kuwa dira husika imehakikiwa ni kwa kuona lakiri iliyofungwa pamoja na muhuri wa WMA ukionesha tarehe, mwezi na muda ambao kifaa hicho kimehakikiwa. Dira yoyote ambayo haina lakiri na muhuri wa WMA inamaanisha kuwa haijahakikiwa.

DKT. MWIGULU AKUTANA NA NAIBU MKURUGENZI WA FAO






WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba amefanya mazungumzo na Naibu Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa (FAO), Bi. Beth Bechdol jijini Dar es salaam leo tarehe 3 Februari, 2026.

Pamoja na mambo mengine, Viongozi hao wameahidi kuendeleza ushirikiano uliopo baina ya Tanzania na FAO ili kukuza na kuimarisha sekta ya Kilimo nchini.

 

RAIS SAMIA AANZA ZIARA YA KIKAZI DUBAI, AONGEZA KASI YA DIPLOMASIA YA KIUCHUMI NA UWEKEZAJI


Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ameanza rasmi ziara ya kikazi nchini Dubai, Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE), akilenga kuimarisha diplomasia ya kiuchumi, kupanua wigo wa ushirikiano wa kimataifa na kuvutia uwekezaji wa moja kwa moja nchini Tanzania.

Katika ratiba ya leo, Rais Samia anafanya mazungumzo ya ngazi ya juu na Mheshimiwa Gaston Browne, Waziri Mkuu wa Antigua and Barbuda, ikiwa ni sehemu ya kuimarisha uhusiano wa kidiplomasia na kiuchumi kati ya Tanzania na nchi rafiki. 

Aidha, Rais Samia anakutana na Bi. Shaikha Al Nuwais, Katibu Mkuu wa Shirika la Utalii la Umoja wa Mataifa (UN Tourism), kwa mazungumzo ya pande mbili yanayolenga kuendeleza sekta ya utalii kama nguzo muhimu ya uchumi na kichocheo cha uwekezaji.

Jioni ya leo, Rais Samia anatarajiwa kushiriki uzinduzi wa Global Africa Investment Summit (GAIS), jukwaa mahsusi la uwekezaji linalolenga kuoanisha miradi iliyo tayari kuwekezeka barani Afrika na wawekezaji wa kimataifa. Ushiriki wa Tanzania katika GAIS unaakisi dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita ya kugeuza fursa kuwa matokeo halisi ya kiuchumi.

GAIS ni mpango wa kimkakati unaoendeshwa sambamba na majadiliano ya sera ya World Governments Summit (WGS), ukiwa na lengo la kubadili mijadala ya sera kuwa uwekezaji wenye tija, unaochochea ukuaji wa uchumi, ajira na maendeleo endelevu barani Afrika.

Wananchi wanaendelea kushauriwa kufuatilia taarifa zaidi kupitia akaunti rasmi za Ikulu Mawasiliano, kwa maendeleo ya ziara hii muhimu kwa mustakabali wa uchumi wa Taifa.

KATAMBI AKUTANA NA BALOZI WA UINGEREZA



Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi,Patrobas Katambi amekutana na Balozi wa Uingereza nchini,Marianne Young ambae aliambatana na Mkuu wa Usalama na Sheria,Alex Beck pamoja na Mkuu wa Ofisi ya Dodoma,Godfrida Magubo.

Katika kikao hicho mambo mbalimbali yalijadiliwa chini ya mwamvuli wa kusimamia na kuhakikisha Amani,Utii wa Sheria,Usalama wa Raia na Mali.

Kikao hicho kimefanyika Makao Makuu ya wizara,Mtumba jijini Dodoma.

DKT. KIJAJI: LENGO LA RAIS SAMIA NI WATANZANIA WANUFAIKE NA RASILIMALI ZAO.







Na Sixmund Begashe, Dodoma 

Waziri wa Maliasili na Utalii Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji amesema lengo la Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan ni kuhakikisha watanzania wananufaika zaidi na rasilimali zao hivyo Wizara anayoiongoza itaendelea kushirikiana na wadau katika usimamizi wa urithi wa Maliasili na Utalii ili kufikia lengo hilo.

Dkt. Kijaji ameyasema hayo jijini Dodoma kwenye kikao chake na wadau wa Uwindaji Wenyeji na Bucha za Nyamapori kwa lengo la kupata uelewa wa pamoja wa sekta hizo muhimu kwa uchumi wa nchi na wananchi kwa ujumla.

Amebainisha kuwa, Serikali chini ya Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ipo bega kwa bega na wadau wa sekta binafsi hivyo uongozi wa Wizara hiyo hautakuwa na muhali kwa mtumishi yeyote atakaye kwamisha juhudi hizo za kuendelea kuwaletea watanzania tabasamu kwa kuwainua kiuchumi kupitia sekta ya Maliasili na Utalii. 

Pamoja na kuwapongeza wadau hao kwa uzalendo wao, amewataka kuendelea kushikamana na Wizara hiyo ambayo imekuwa na mchango mkubwa katika  uchumi wa nchi na wa mtu mmoja mmoja ili kufungua fursa zaidi za uwekezaji na ajira  hususani kwa vijana. 

Akizungumza kwa niaba ya Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Maliasi na Utalii anaeshughulika na Utalii, Bw. Nkoba Mabula, amewahakikishia wadau hao kuwa, ofisi yake itasimamia kikamilifu utekelezaji wa maelekezo yote yaliyotolewa na Mhe. Dkt. Kijaji ambayo yametokana na maono mbalimbali waliyotoa.

Monday, February 02, 2026

RAIS SAMIA AONDOKA DAR AWASILI DUBAI KUSHIRIKI MKUTANO WA DUNIA WA SERIKALI NA JUHUDI ZA UWEKEZAJI AFRIKA


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiondoka nchini kuelekea Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) leo tarehe 02 Februari, 2026, ambapo atashiriki kwenye mkutano wa World Government Summit (WGS 2026) na uzinduzi wa Global Africa Investment Summit (GAIS).

Ushiriki wa Tanzania katika WGS 2026 unaakisi utekelezaji wa DIRA 2050 na Sera Mpya ya Mambo ya Nje, zinazoweka diplomasia ya kiuchumi kama nguzo ya mahusiano ya kimataifa.

Lengo ni kuoanisha sera, ushirikiano na mitaji ya uwekezaji kwa maendeleo ya taifa.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwasili katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Al Maktoum (DWC) Dubai, Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE), tarehe 02 Februari, 2026. 

Rais Mhe. Dkt. Samia atashiriki kwenye Mkutano wa Dunia wa Serikali (World Governments Summit – WGS) 2026pamoja na kushiriki Jukwaa la Kimataifa wa Uwekezaji Afrika (GAIS).

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye mazungumzo na Waziri wa Sheria wa Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) Abdullah bin Sultan bin Awad al Nuaimi mara baada ya kuwasili katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Al Maktoum (DWC) Dubai, Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE), tarehe 2 Februari, 2026. 

Rais Mhe. Dkt. Samia atashiriki kwenye Mkutano wa Dunia wa Serikali (World Governments Summit – WGS) 2026 pamoja na kushiriki Jukwaa la Kimataifa wa Uwekezaji Afrika (GAIS).

MAKAMU WA RAIS AMWAKILISHA RAIS DKT. SAMIA KATIKA MAADHIMISHO YA SIKU YA SHERIA NCHINI








Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi amesema kwa kutambua umuhimu wa Mahakama katika ujenzi wa Taifa, Serikali imeendelea kuchukua hatua za makusudi katika kuimarisha uhuru wa Mahakama ili kuiwezesha kutekeleza wajibu wake kikamilifu na kuchochea ustawi na maendeleo ya Taifa.

Makamu wa Rais amesema hayo, wakati alipomwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan katika Maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini yaliyofanyika Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania, Tambukareli, Jijini Dodoma.

 Amesema Serikali itaendelea kushirikiana na Mahakama katika ujenzi wa miundombinu ya Mahakama, kuimarisha rasilimali watu, kuboresha maslahi ya watumishi wa Mahakama, na kusogeza huduma za utoaji haki karibu zaidi na wananchi, hususan kupitia mpango wa ujenzi wa Mahakama za Mwanzo kwa Kata zote nchini zisizo na  Mahakama za Mwanzo.

Aidha Makamu wa Rais ametoa rai kwamba, uhuru wa Mahakama usitumike kama sehemu ya kuficha uzembe, upendeleo au vitendo visivyo vya haki. Amesema uhuru huo ni dhamana ya kutenda haki kwa uadilifu, uwazi na kwa kuzingatia Katiba na Sheria za nchi.

Makamu wa Rais amesema Mahakama ina wajibu muhimu wa kulinda utawala wa sheria, kusimamia utekelezaji wa mikataba, kulinda rasilimali za Taifa, na kuhakikisha kuwa maendeleo yanayopatikana yanawanufaisha Watanzania wote kwa usawa.

Ameongeza kwamba Mahakama ina mchango mkubwa katika utekelezaji wa Dira ya Taifa ya 2050 kwa Kuendelea kulinda haki na misingi ya Katiba, Kuhakikisha migogoro ya kiuchumi, kibiashara na kijamii inatatuliwa kwa haraka na kwa haki, Kujenga imani ya wananchi na wawekezaji katika mfumo wa kisheria wa nchi, Kukuza uwajibikaji na nidhamu katika utumishi wa umma na sekta binafsi pamoja na Kudumisha amani na mshikamano wa Kitaifa, ambao ni msingi wa maendeleo endelevu.

Pia amesema ni muhimu Mahakama, Kuzuia migogoro inayoweza kuwa chanzo cha migawanyiko ya kijamii au kisiasa, Kuharakisha utekelezaji wa sera na mipango ya maendeleo kwa kutoa tafsiri ya kisheria iliyo wazi na thabiti, Kujenga na kuimarisha utamaduni wa kuheshimu sheria, haki na taasisi za umma, Kuchangia katika mapambano dhidi ya rushwa na matumizi mabaya ya madaraka pamoja na Kuwezesha wananchi kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya Taifa kwa kuwahakikishia ulinzi wa haki zao za kisheria.

Katika hatua nyingine, Makamu wa Rais amewaasa viongozi, wanasiasa, wanaharakati na wananchi mbalimbali kuheshimu tume iliyoundwa na Rais ya kuchunguza matukio ya uvunjifu wa amani baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29, 2025 kwa kuacha kuongelea masuala hayo nje ya mfumo wa kisheria. 

 Makamu wa Rais ametoa kauli hiyo kufuatia maombi ya Rais wa Chama Cha Wanasheria Tanganyika (TLS) Wakili Boniface Mwabukusi ambaye aliomba Viongozi kuacha kuzungumzia suala hilo ambalo limekuwa likiwaumiza wananchi.

Kwa upande wake Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. George Masaju amesema Mahakama inaendeleza na kuimarisha matumizi ya TEHAMA katika shughuli za Mahakama ili kuimarisha ufanisi. Amesema kwa sasa Mahakama inajenga mfumo unaotumia Akili Unde (AI) kwaajili ya kurekodi mwenendo wa kumbukumbu za mashauri na hukumu Mahakamani.

Amesema katika mfumo huo, Jaji, Hakimu, Wakili na Shahidi wanapozungumza mahakamani mfumo huo utatafsiri lugha iliyotumika na kuiandika kwa lugha iliyokuwa imechaguliwa kuandika kwa wakati huo huo.

 Ameongeza kwamba mfumo huo utakapoanza kutumika utaimarisha ufanisi wa utendaji wa Mahakama kwani kuchukua kumbukumbu za mwenendo wa mashauri Mahakamani kwa kuandika kwa mkono au kompyuta kunachelewesha na wakati mwingine kupotosha.

 


WMA YAFUNGA MTAMBO WA KISASA UNAOHAKIKI DIRA ZA MAJI DODOMA

Mtambo wa kisasa unaotumika kuhakiki dira za maji. Mtambo huu wa kidijitali umefungwa katika Jengo la Makao Makuu ya Wakala wa Vipimo (WMA),...