Thursday, April 16, 2026

SAMIA AZINDUA MKUTANO WA KIMATAIFA WA WFNS, ATEMBELEA MAONESHO YA SEKTA YA AFYA






Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, akitembelea mabanda ya maonesho ya wadau wa Sekta ya Afya kabla ya kufungua rasmi Mkutano wa Pili wa Kimataifa wa Shirikisho la Dunia la Madaktari Bingwa wa Upasuaji wa Ubongo na Mishipa ya Fahamu (WFNS).

Mkutano huo unafanyika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC), jijini Dar es Salaam, tarehe 16 Aprili 2026.

Makamu wa Rais wa Zimbabwe akutana na CP Kaganda kuimarisha ushirikiano wa kidiplomasia.




Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Zimbabwe, Mhe. Kembo Mohadi, amekutana na Balozi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nchini humo, Kamishna wa Polisi (CP) Suzan Kaganda, ikiwa ni juhudi za kuimarisha ushirikiano wa kidiplomasia kati ya nchi hizo mbili.

Mazungumzo hayo yaliyofanyika tarehe 15 Aprili 2026 katika Ofisi Ndogo za Makamu wa Rais nchini Zimbabwe, yalilenga kuendeleza na kuimarisha mahusiano ya kihistoria yaliyopo kati ya Zimbabwe na Tanzania.

Katika kikao hicho, Mhe. Mohadi alimshukuru Balozi Kaganda kwa mchango wake katika kuimarisha uhusiano kati ya mataifa hayo mawili kupitia kazi za ubalozi huku akieleza kuwa ushirikiano huo unaendelea kukua, ukichochewa na ziara za viongozi wa ngazi za juu na mawasiliano ya karibu ya kidiplomasia.

 Alisisitiza umuhimu wa kufanyika kwa Mkutano wa Tisa wa Tume ya Pamoja ya Kudumu (JPC), ambao utatoa fursa ya kutathmini utekelezaji wa makubaliano yaliyopita pamoja na kuweka mikakati mipya ya kuendeleza ushirikiano wa pande mbili.

Aidha akizungumzia masuala ya kiuchumi, Mhe. Mohadi alibainisha nafasi ya miundombinu ya usafiri katika kukuza biashara, akitolea mfano wa reli ya TAZARA, ambayo ina uwezo mkubwa wa kurahisisha usafirishaji wa bidhaa, hususan nafaka, kutoka Tanzania kwenda Zambia na baadae Zimbabwe.

Kwa upande wake, Balozi (CP) Kaganda amemshukuru Makamu wa Rais kwa muda wake na kujadili kwa kina masuala ya ushirikiano wa pande mbili ambapo alithibitisha utayari wa Serikali ya Tanzania kuandaa Mkutano wa Tisa wa Joint Permanent Commission (JPC) ambalo ni jukwaa rasmi la ushirikiano kati ya nchi mbili linalotumika kujadili, kupanga na kufuatilia utekelezaji wa makubaliano ya maendeleo kiuchumi, na kidiplomasia huku lengo likiwa ni kuimarisha zaidi mahusiano hayo.

Amefafanua zaidi kuwa ubalozi unaendelea kuratibu mafunzo ya lugha ya Kiswahili nchini Zimbabwe, ambapo washiriki wengi ni maafisa wa  vyombo vya ulinzi na usalama, hatua inayochangia kukuza mawasiliano na ushirikiano wa kikanda.

TANZANIA NA BRAZIL ZAJIZATITI KUENDELEZA USHIRIKIANO WA KIDIPLOMASIA









Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Ngwaru Maghembe (Mb.) ameongoza ujumbe wa Tanzania kwenye Mkutano wa Pili wa Mashauriano ya Kisiasa kati ya Tanzania na Brazili uliofanyika jijini Brasilia, Brazili Aprili 15, 2026. 

Ujumbe wa Brazili katika mkutano huo uliongozwa na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje, Mhe. Balozi Sobral Duerte Carlos Sergio Sobral Duerte. 

Katika Mkutano huo, Tanzania na Brazili zimejadili na kukubaliana mikakati mbalimbali ya kukuza uhusiano na Ushirikiano wa Kidiplomasia baina ya Tanzania na Brazili katika sekta mbalimbali. 

Baadhi ya sekta hizo ni pamoja na umuhimu wa viongozi wa nchi hizi mbili kuendelea kutembeleana na kubadilisha mawazo kuhusu masuala mbalimbali ya ushirikiano ya uwili na kimataifa; Kukuza Ushirikiano katika sekta ya elimu na mafunzo ambapo Brazili itaendelea kutoa ufadhili wa masomo kwa wanafunzi kutoka Tanzania.

Pia kukuza ushirikiano katika sekta ya kilimo na ufugaji hususan katika matumizi ya teknolojia na mbinu za kisasa za kilimo na ufugaji; pamoja na kuimarisha uhusiano wa kiuchumi kwa kukuza viwango vya biashara, uwekezaji na utalii baina ya nchi hizi mbili. 

Aidha, Tanzania na Brazili zimekubaliana kukamilisha majadiliano ya rasimu za makubaliano ya ushirikiano katika sekta husika ili ziweze kusainiwa na utekelezaji wake uanze mara moja.

Vilevile, Tanzania na Brazili zimebadilishana mawazo kuhusu masuala mbalimbali ya kikanda na kimataifa yenye maslahi kwa pande zote, ikiwemo athari za migogoro ya kisiasa na vita ulimwenguni, mchakato wa Mageuzi ya Mifumo Ulimwenguni kama vile Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa.

SERIKALI YAJIPANGA KUZIFANYIA UKARABATI SHULE ZOTE KONGWE NCHINI - PROF. SHEMDOE








Na OWM – TAMISEMI, Dodoma

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu - TAMISEMI, Mhe. Prof. Riziki Shemdoe, amesema Serikali kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu - TAMISEMI imeandaa andiko la mradi unaoitwa SIFA yaani (School Infrastructure Facelifting Programme) na kuliwasilisha Wizara ya Mipango, ili kuwezesha upatikanaji wa fedha za kufanyia ukarabati wa shule zote kongwe za awali, msingi na sekondari nchini.

Prof. Shemdoe amesema hayo Aprili 15, 2026 wakati akijibu hoja za Waheshimiwa Wabunge walizoziwasilisha wakati wa kujadili Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka 2026/27.

“Namshukuru Mheshimiwa Prof. Kitila Mkumbo na timu yake ya Wizara ya Mipango kwa kulipokea andiko tulilowasilisha ili tupate fedha za kutekeleza mradi wa ukarabati wa shule kongwe nchi nzima,” amesema Prof. Shemdoe.

Prof. Shemdoe amefafanua kuwa, tathmini iliyofanyika imebaini ukarabati unahitajika kwenye shule za msingi ikihusisha vyumba vya madarasa ni 42,716 na nyumba za walimu 31,813 na kwa upande wa shule za sekondari inajumuisha vyumba vya madarasa 6,889, nyumba za walimu 3,518, maktaba 91 na mabweni 309. 

Prof. Shemdoe ameanisha kuwa, Serikali imekuwa ikitoa fedha kwa ajili ya kufanya ukarabati kwa awamu ambapo kati ya mwaka 2021/22 hadi 2025/26, Serikali imetumia shilingi bilioni 237.9 kwa ajili ya ukarabati na ujenzi wa miundombinu mipya ya shule za msingi na Sekondari kongwe na chakavu nchini.

Wednesday, April 15, 2026

RAIS SAMIA AKUTANA NA MJUMBE MAALUM WA JUMUIYA YA MADOLA IKULU DAR ES SALAAM






Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, leo tarehe 15 Aprili 2026, amekutana na kufanya mazungumzo na Mjumbe Maalum wa Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Madola (Commonwealth), ambaye pia ni Rais wa zamani wa Jamhuri ya Malawi, Mhe. Dkt. Lazarus McCarthy Chakwera, Ikulu Jijini Dar es Salaam.

Mazungumzo yao yamejikita katika kuimarisha ushirikiano wa kimataifa, kukuza maendeleo ya kijamii na kiuchumi, pamoja na kuendeleza ajenda za pamoja ndani ya Jumuiya ya Madola.

Mkutano huo unaakisi dhamira ya Tanzania kuendelea kujenga mahusiano imara ya kidiplomasia na washirika wa kimataifa, sambamba na kuimarisha nafasi yake katika jukwaa la kimataifa.

#SamiaSuluhuHassan #Tanzania #Commonwealth #Diplomasia #Maendeleo

TRC YASAFIRISHA ABIRIA 5,512,995

 

Shirika la Reli Tanzania (TRC) lilianza kutoa huduma ya usafirishaji abiria kutumia reli ya kiwango cha kimataifa (SGR) mnamo mwezi Juni 2024, toka kipindi hicho mpaka Machi 2026, abiria 5,512,995, wamesafiri kwa kutumia treni za SGR.  

Takwimu hiyo ina ujumbe mkubwa sana kimkakati kuhusu ubora na mafanikio ya huduma ya SGR, na ina maana zifuatazo:

Kwanza ni Kukubalika kwa Huduma (High public acceptance)

Abiria zaidi ya milioni 5.5 ndani ya muda mfupi inaonyesha kuwa, Wananchi wameikubali kwa kiwango cha juu kabisa, huduma ya SGR kwani mejenga imani kubwa kwa watumiaji. Ukiachana na hilo, SGR imekuwa chaguo kuu la usafiri ukilinganisha na njia nyingine na usafiri na usafirishaji, lakini kubwq zaidi hii ni ishara ya market penetration yenye mafanikio makubwa.

Pili inadhihirisha Ufanisi wa Utoaji Huduma (Service Efficiency), na kwa muktadha huo, idadi hii inaashiria kuwa, huduma inapatikana kwa uhakika na ratiba zinazingatiwa , katika kipindi chote hicho uendeshaji umekuwa ni wa kuaminika (reliable), hili la pili lina maanisha kwamba ,TRC imefanikiwa kusimamia miundombinu na uendeshaji kwa ufanisi.

Tatu, ni kudhihirika kwa Ubora wa Huduma (Customer Experience), abiria kuendelea kutumia huduma hiyo kunamaanisha, wanaridhika na usalama, mwendo na faraja aidha kuna uzoefu mzuri wa safari (customer satisfaction), la tatu lina maanisha kwamba huduma hii mpya katika sekta ndogo ya reli nchini, imeleta thamani halisi kwa mtumiaji.

Nne, Mchango wa Kiuchumi na Kijamii, huduma hii ya treni za SGR, inachochea ukuaji wa uchumi (biashara, ajira na utalii) pia inarahisisha muunganiko wa mikoa (kati ya Dar es Salaam, Morogoro na Dodoma) hili la nne linajipambanua kuwa kusafiri na treni za SGR, kunapunguza gharama na muda wa usafiri kwa wananchi.

Tano, haya ni Mafanikio ya Uwekezaji wa Serikali, na kwamba takwimu hizo za abiria katika kipindi cha muda mfupi wa huduma ya treni za SGR, inaonyesha kuwa, Uwekezaji wa Serikali kwenye SGR umeanza kuzaa matunda, kwa kuongeza huu ni mradi wenye tija (value for money) na unatekeleza dira ya maendeleo ya Taifa 2050 sambamba na Ilani ya Chama cha Mapinduzi ya mwaka 2025/30, ambayo moja ya malengo yake ni kuimarisha miundombinu ya kisasa ya usafiri na usafirishaji

Hitimisho, idadi ya abiria zaidi ya milioni 5.5 waliotumia SGR ndani ya kipindi kifupi tangu kuanza kwa huduma inaonyesha kiwango kikubwa cha kukubalika kwa huduma hiyo, ufanisi wa uendeshaji, na mchango wake muhimu katika kurahisisha usafiri, kukuza uchumi na kuboresha maisha ya wananchi. 



RAIS SAMIA AKUTANA NA RAIS WA KAMPUNI YA GRUPA ZENITH YA POLAND








Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan amekutana na kufanya mazungumzo na Rais wa Kampuni ya Grupa Zenith kutoka nchini Poland, Dkt. Aleksander Joseph Widuchi, tarehe 14 Aprili, 2026 Ikulu Dar es Salaam.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan amekutana na kufanya mazungumzo na Rais wa Kampuni ya Grupa Zenith kutoka nchini Poland, Dkt. Aleksander Joseph Widuchi, tarehe 14 Aprili, 2026 Ikulu Dar es Salaam. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiangalia kitabu kinachoelezea masuala ya Mazingira, Nishati na masuala mbalimbali ya Poland wengine pichani ni Rais wa Kampuni ya Grupa Zenith kutoka nchini Poland, Dkt. Aleksander Joseph Widuchi pamoja na Mkurugenzi Mtendaji Bi. Aleksandra Stephania Widuchi, tarehe 14 Aprili, 2026 Ikulu Dar es laam.


SAMIA AZINDUA MKUTANO WA KIMATAIFA WA WFNS, ATEMBELEA MAONESHO YA SEKTA YA AFYA

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, akitembelea mabanda ya maonesho ya wadau wa Sekta ya Afya kabla ya k...