Tuesday, March 31, 2026

VIONGOZI WAUNGANA KUAGA MWILI WA MAREHEMU MHE. WILLIAM LUKUVI IRINGA

 










Iringa, Machi 31, 2026 — Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba, amewasili nyumbani kwa aliyekuwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu) na Mbunge wa Jimbo la Isimani, Marehemu Mhe. William Lukuvi, kilichopo Kijiji cha Idodi mkoani Iringa, kuongoza mamia ya waombolezaji katika shughuli za maziko zilizofanyika leo.

Ujio wa kiongozi huyo umeambatana na viongozi mbalimbali wa Serikali, wabunge, viongozi wa vyama vya siasa pamoja na wananchi kutoka maeneo tofauti ya nchi waliojitokeza kutoa heshima zao za mwisho kwa kiongozi huyo aliyekuwa na mchango mkubwa katika utumishi wa umma.

Akizungumza katika shughuli hiyo, Mhe. Dkt. Nchemba alieleza kuwa taifa limepoteza kiongozi mwenye uzoefu, aliyekuwa mstari wa mbele kusimamia sera, uratibu wa shughuli za Serikali na utetezi wa masuala ya watu wenye ulemavu. Alisisitiza kuwa mchango wa Marehemu Lukuvi utaendelea kukumbukwa na kuthaminiwa na vizazi vya sasa na vijavyo.

Marehemu Mhe. William Lukuvi alifariki dunia tarehe 25 Machi, 2026 katika Hospitali ya Benjamin Mkapa jijini Dodoma alipokuwa akipatiwa matibabu. Enzi za uhai wake, alitumikia nafasi mbalimbali za uongozi serikalini kwa weledi na uzalendo mkubwa, akijijengea heshima ndani na nje ya Bunge.

Maziko hayo yamefanyika katika kijiji chake cha nyumbani cha Idodi, huku yakihudhuriwa na umati mkubwa wa wananchi waliokusanyika kumlaki na kumuaga kiongozi wao kwa heshima na majonzi makubwa.

Taifa linaendelea kuungana na familia, ndugu, jamaa na wananchi wa Jimbo la Isimani katika kipindi hiki kigumu cha maombolezo. Mwenyezi Mungu ailaze roho ya Marehemu mahali pema peponi.

TARURA YATEKELEZA UJENZI WA KM 56 ZA BARABARA ZA LAMI ILALA KUPITIA DMDP II






‎Serikali kupitia Wakala ya Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) imeanza kutekeleza ujenzi wa barabara zaidi ya Kilomita 56 kwa kiwango cha lami na zege kupitia mradi wa Uendelezaji Jiji la Dar es Salaam Awamu ya Pili (DMDP II) katika Halmashauri ya Manispaa ya Ilala mkoani humo.

‎Akiwa katika ziara ya ukaguzi wa miradi hiyo Kaimu Meneja wa TARURA wilaya ya Ilala, Mhandisi Grayson Nzunda amesema kuwa miradi inayojengwa ni barabara za lami na zege, mifereji ya maji ya mvua, makalavati, njia za waenda kwa miguu, uwekaji wa taa za barabarani pamoja na kuweka alama za barabarani ambapo mradi unagharimu shilingi Bilioni 138.

‎“Hapa tulipo ni maeneo ya Kivule tupo kukagua ujenzi wa barabara zenye urefu wa Kilomita 12, barabara ya Kivule-Majohe Junction Km 2.79 inajengwa kwa kiwango cha zege na barabara ya Kitunda-Kivule-Msongola Km 9.95 inajengwa kwa kiwango cha lami, mradi umegharimu shilingi Bilioni 30 kati ya Bilioni 138 za wilaya nzima ya Ilala”, alisema.

‎Ameeleza kuwa barabara hizo zilikuwa na changamoto kubwa hivyo kukamilika kwake zitasaidia wananchi kufikia huduma mbalimbali kwa urahisi na kupunguza gharama za usafiri na usafirishaji, pia barabara hizo zinatumika kama ‘bypass’ kwa wanaokwenda Chanika au Majohe kama barabara kubwa ikiwa na foleni.

‎Naye, Bi. Vicky Shayo mkazi wa Kitunda amesema kuwa wamekuwa wakikosa wateja katika biashara zao kutokana na changamoto ya barabara hasa kipindi cha mvua kutokana na maji mengi na matope ambapo inapelekea watu kuanguka kwasababu ya udongo kuteleza, lakini barabara ikikamilika itawasaidia kufanya biashara zao na kipato kitaongezeka.

‎Bi. Maria Petro mkazi wa Kivule ameishukuru serikali kwa uboreshaji wa miundombinu ya barabara kwani walikuwa wanapata changamoto kwenda hospitalini lakini sasa hivi usafiri umekuwa rahisi kufika mpaka Banana.

‎Aidha, Mwenyekiti wa mtaa wa Karume Bw. Hajibu China amemshukuru Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwani anaiona Ilala inakwenda kubadilika kutokana na maboresho ya barabara kwani wananchi wanajenga nyumba zao, pia kutakuwa na taa za barabarani zitakazopendezesha mji na kuongeza ulinzi na usalama.

Friday, March 27, 2026

TBC Yawajengea Uwezo Washitiri Uzalishaji wa Vipindi

Kaimu Mkurugenzi wa Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC), Bw. Gwakisa Mlawa akizungumza wakati wa kufunga Mkutano wa 110 wa wadau wa elimu kwa umma (Washitiri), uliofanyika  katika ukumbi wa PAPU, Jijini Arusha, Machi 27, 2026

Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano LATRA, Bw. Salum Pazzy, akitoa salamu za shukrani kwa TBC kwa niaba ya washitiri wengine wakati wa kufunga Mkutano wa 110 wa wadau wa elimu kwa umma uliofanyika  katika ukumbi wa PAPU, Jijini Arusha, Machi 27, 2026.
Baadhi ya Washitiri walioshiriki Mkutano wa 110 wa wadau wa elimu kwa umma uliofanyika  katika ukumbi wa PAPU, Jijini Arusha, Machi 23 - 27, 2026.

Adelina Johnbosco na Timothy Mwakyenda – MAELEZO

Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC) limetoa mafunzo ya uandaaji bora wa vipindi kwa washitiri wa taasisi za umma nchini ili kuwajengea uwezo wa kutoa elimu kwa umma.

Washitiri hao kutoka vitengo vya mawasiliano vya wizara, taasisi, idara, mamlaka na mashirika ya umma wanahusika na utoaji wa taarifa za Serikali na utekelezaji wa shughuli na miradi mbalimbali ya maendeleo ya wananchi.

Akizungumza wakati wa kufunga mafunzo hayo, Kaimu Mkurugenzi wa TBC, Bw. Gwakisa Mlawa, amesema ana imani mafunzo hayo yataongeza ujuzi na ufanisi kwa washiriki katika majukumu yao ya kila siku ya mawasiliano.

Amesema mafunzo hayo pia yatakuwa chachu ya maboresho ya maudhui yanayozalishwa, kutokana na maarifa waliyopata kupitia wataalamu waliobobea katika nyanja tofauti.

Mafunzo hayo yamejumuisha mada mbalimbali zikiwemo uongozi bora, uandaaji wa vipindi, matumizi ya akili unde (AI) pamoja na mbinu za utatuzi wa migogoro kazini.

“Mawasiliano siyo suala la kutoa na kupokea taarifa tu, bali ni kujenga taswira nzuri ya taasisi na taifa kwa ujumla,” alisema Bw. Mlawa.

Aidha, amesema TBC inaendelea kuwekeza katika teknolojia za kisasa ili kuboresha utoaji wa huduma za habari na mawasiliano kwa wananchi akiwakaribisha wadau na wananchi kuendelea kuitumia TBC kama chombo muhimu cha utangazaji nchini.

Kwa upande wake Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano wa Mamlaka ya Udhibiti wa Usafiri Ardhini (LATRA), Bw. Salum Pazzy, akizungumza kwa niaba ya washiriki wenzake ameipongeza TBC kwa kuandaa mafunzo hayo, akieleza kuwa yamekuwa na manufaa makubwa kwa washitiri wote.

Amesema mafunzo hayo yamewajengea uwezo wa kuzalisha vipindi vya elimu kwa umma kwa weledi na uzalendo. 

TANZANIA NA ZAMBIA ZAIMARISHA USHIRIKIANO WA NISHATI KATIKA KUKUZA UCHUMI NA RASILIMALI ZA TAIFA









Katika kuendeleza ajenda ya kimkakati ya kukuza uchumi kupitia rasilimali za taifa, Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi, amekutana na kufanya mazungumzo na Waziri wa Nishati wa Zambia, Mhe. Makozo Chikote, tarehe 27 Machi 2026 jijini Lusaka, Zambia.

Mazungumzo hayo yamejikita katika kuimarisha ushirikiano wa sekta ya nishati, hususan mafuta na gesi, ambayo ni mhimili muhimu katika kuchochea maendeleo ya sekta nyingine za uzalishaji ikiwemo madini. Viongozi hao walisisitiza umuhimu wa kuunganisha nguvu za kikanda ili kuongeza thamani ya rasilimali, kuboresha miundombinu ya nishati na kuhakikisha upatikanaji wa nishati ya uhakika kwa shughuli za kiuchumi.

Katika muktadha wa sera ya madini ya Tanzania, nishati imeendelea kuwa nyenzo muhimu katika kuongeza ufanisi wa uchimbaji na uchakataji wa madini, hivyo ushirikiano huu unatarajiwa kuongeza kasi ya uwekezaji na tija katika sekta hiyo. Uimarishaji wa miundombinu ya mafuta na gesi unatoa msingi imara wa kukuza viwanda vinavyotegemea rasilimali za madini, na hivyo kuongeza mchango wa sekta hiyo katika pato la taifa.

Kikao hicho kilihudhuriwa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati anayeshughulikia Mafuta na Gesi, Dkt. James Mataragio, Balozi wa Tanzania nchini Zambia, Luteni Jenerali Mathew Edward Mkingule pamoja na wataalam kutoka Wizara ya Nishati na taasisi zake, wakionesha dhamira ya dhati ya pande zote mbili katika kuendeleza ushirikiano huo.

Historia ya ushirikiano kati ya Tanzania na Zambia inaendelea kudhihirishwa kupitia mradi wa kimkakati wa Bomba la Mafuta la TAZAMA, ambalo limekuwa mhimili wa usafirishaji wa mafuta kutoka Bandari ya Dar es Salaam kwenda Zambia. Mradi huo sio tu umeimarisha usalama wa nishati bali pia umefungua fursa za kiuchumi na uwekezaji katika ukanda wa Kusini mwa Afrika.

Kwa ujumla, hatua hii inaashiria mwelekeo mpya wa ushirikiano unaolenga kuunganisha sekta ya nishati na maendeleo ya madini, sambamba na utekelezaji wa sera za kitaifa zinazolenga kuongeza thamani ya rasilimali za ndani na kukuza uchumi shindani.

#Nishati #Madini #Ushirikiano #Tanzania #Zambia #TAZAMA #Uwekezaji #Maendeleo #Rasilimali #EnergySector #MiningPolicy

WANAWAKE WAJENGEWA UWEZO KATIKA UTATUZI WA MIGOGORO KWA NJIA MBADALA (ADR)

Mkurugenzi wa Idara ya Usuluhishi wa Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali, ndugu Saddy Sevingi akizungumza wakati akifunga mafunzo kuhusu ushirikishwaji wa wanawake kwenye utatuzi wa migogoro kwa njia mbadala yaliyofanyika Jijini Dar es Salaam.
Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Usuluhishi Tanzania, Bi. Madeline Kimei akitoa mada kuhusu fursa mbalimbali zilizopo kwenye utatuzi wa migogoro kwa njia mbadala wakati wa mafunzo kuhusu ushirikishwaji wa wanawake kwenye utatuzi wa migogoro kwa njia mbadala yaliyofanyika Jijini Dar es Salaam.
Wakili wa Serikali wa Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali, Bi. Lydia Thomas akitoa mada kuhusu mbinu za utatuzi wa migogoro ya kibiashara kwa njia mbadala (ADR) wakati wa mafunzo kuhusu ushirikishwaji wa wanawake kwenye utatuzi wa migogoro kwa njia mbadala yaliyofanyika Jijini Dar es Salaam.
Wakili wa Serikali Mwandamizi wa Wizara ya Katiba na Sheria, Bi. Aveline Ombock akitoa maelezo kuhusu namna ya kujisajili kupia mfumo wakati wa mafunzo kuhusu ushirikishwaji wa wanawake kwenye utatuzi wa migogoro kwa njia mbadala yaliyofanyika Jijini Dar es Salaam.

Baadhi ya washiriki wa mafunzo kuhusu ushirikishwaji wa wanawake kwenye utatuzi wa migogoro kwa njia mbadala wakimsikiliza Mkurugenzi wa Usuluhishi wa Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali, ndugu Saddy Sevingi wakati akifunga mafunzo kuhusu ushirikishwaji wa wanawake kwenye utatuzi wa migogoro kwa njia mbadala yaliyofanyika Jijini Dar es Salaam.

&&&&&&&&&&&&&&&&&&&

Jijini Dar es Salaam kumeshuhudiwa hatua muhimu katika kuimarisha ushiriki wa wanawake kwenye sekta ya sheria, kufuatia kufanyika kwa mafunzo maalum kuhusu ushirikishwaji wa wanawake katika utatuzi wa migogoro kwa njia mbadala (ADR).

Akifunga mafunzo hayo, Mkurugenzi wa Idara ya Usuluhishi wa Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali, ndugu Saddy Sevingi, alisisitiza umuhimu wa kuwajengea wanawake uwezo na ujasiri wa kushiriki kikamilifu katika mifumo ya utatuzi wa migogoro, akieleza kuwa ADR ni nyenzo muhimu inayochochea upatikanaji wa haki kwa haraka, nafuu na kwa ufanisi zaidi.

Katika mafunzo hayo, wataalamu mbalimbali walitoa mada zenye kujenga uelewa mpana kwa washiriki. Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Usuluhishi Tanzania, Bi. Madeline Kimei, aliwasilisha mada kuhusu fursa zilizopo katika sekta ya ADR na namna wanawake wanavyoweza kuzitumia kujenga taaluma na kuchangia maendeleo ya jamii.

Kwa upande wake, Wakili wa Serikali, Bi. Lydia Thomas, alielezea mbinu za kisasa za utatuzi wa migogoro ya kibiashara kwa njia mbadala, akisisitiza umuhimu wa weledi na uadilifu katika kushughulikia migogoro hiyo. Naye Wakili wa Serikali Mwandamizi kutoka Wizara ya Katiba na Sheria, Bi. Aveline Ombock, alitoa mwongozo wa kina kuhusu namna ya kujisajili kupitia mfumo husika, hatua inayolenga kurahisisha ushiriki wa wadau wengi zaidi katika huduma za usuluhishi.

Washiriki wa mafunzo hayo walionesha hamasa kubwa kwa kufuatilia kwa makini mada mbalimbali zilizowasilishwa, hatua inayoashiria mwitikio chanya na utayari wa wanawake kushiriki kikamilifu katika kuimarisha mifumo ya haki mbadala nchini.

Mafunzo haya yanaendelea kuwa chachu ya mabadiliko, yakifungua milango ya fursa kwa wanawake katika sekta ya sheria na kuchangia ujenzi wa jamii yenye usawa, haki na maendeleo endelevu.

#ADR #Wanawake #Uwezeshaji #Usuluhishi #Sheria #Migogoro #Maendeleo #DarEsSalaam #LegalEmpowerment #GenderEquality

SAMIA AENDELEA KUIPEPERUSHA VYEMA TANZANIA KATIKA MAJUKWAA YA KIMATAIFA

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, ambaye pia ni Makamu wa Pili wa Mwenyekiti wa Umoja wa Afrika (AU), akishiriki Kikao cha Baraza la Uongozi la Umoja wa Afrika (African Union Bureau of Assembly) kilichofanyika kwa njia ya mtandao, tarehe 26 Machi, 2026, Ikulu Ndogo ya Tunguu, Zanzibar. 

Kikao hicho kiliongozwa na Mwenyekiti wa Umoja wa Afrika (AU) Rais wa Jamhuri ya Burundi Mhe. Évariste Ndayishimiye.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, ameendelea kuimarisha nafasi ya Tanzania katika majukwaa ya kimataifa kwa kushiriki kikao muhimu cha Baraza la Uongozi la Umoja wa Afrika (African Union Bureau of Assembly), kilichofanyika kwa njia ya mtandao tarehe 26 Machi 2026.

Kikao hicho kilichofanyika kutoka Ikulu Ndogo ya Tunguu, Zanzibar, kiliwakutanisha viongozi wakuu wa Bara la Afrika kujadili masuala ya kimkakati yanayolenga kuimarisha mshikamano, kukuza uchumi na kuleta maendeleo endelevu kwa wananchi wa Afrika. 

Mheshimiwa Dkt. Samia, ambaye pia ni Makamu wa Pili wa Mwenyekiti wa Umoja wa Afrika (AU), alishiriki kikamilifu katika majadiliano hayo, akisisitiza umuhimu wa ushirikiano wa kikanda na maendeleo jumuishi.

Mkutano huo uliongozwa na Mwenyekiti wa Umoja wa Afrika, Rais wa Jamhuri ya Burundi Mheshimiwa Évariste Ndayishimiye, ambapo ajenda kuu zilihusu kuharakisha utekelezaji wa miradi ya maendeleo, kuimarisha amani na usalama, pamoja na kukuza uchumi wa bara kwa manufaa ya wote.

Ushiriki wa Mheshimiwa Dkt. Samia unaendelea kudhihirisha dhamira ya Tanzania ya kuwa sehemu muhimu ya ujenzi wa Afrika yenye umoja, nguvu na ustawi wa pamoja.

#SamiaSuluhuHassan #Tanzania #AfricanUnion #AU #Diplomasia #Uongozi #Maendeleo #Afrika #Ushirikiano #GlobalLeadership

Wednesday, March 25, 2026

KIKWETE ATEULIWA KUWA MWAKILISHI WA NGAZI YA JUU WA MWENYEKITI WA KAMISHENI YA AU


Mwenyekiti wa Kamisheni ya Umoja wa Afrika (AUC), Mhe. Mahmoud Ali Youssouf, amemteua Rais Mstaafu wa Tanzania, Mhe. Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, kuwa Mwakilishi wa Ngazi ya Juu wa Mwenyekiti wa AUC katika eneo la Pembe ya Afrika na Bahari ya Shamu.

Uteuzi huo uliotangazwa rasmi leo, Machi 25, 2026, unalenga kuimarisha juhudi za Umoja wa Afrika katika kushughulikia changamoto za kisiasa, amani, na masuala ya kiusalama yanayoikabili kanda hiyo.

Kufuatia uteuzi huo, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan amempongeza Dkt. Kikwete na kueleza kuwa ni heshima kubwa kwake na kwa Tanzania. Aidha, amemtakia majukumu mema katika kuimarisha Umoja wa Afrika na kupata suluhu ya amani ya kudumu kwa manufaa ya Afrika na ulimwengu wote. 

Katika nafasi hiyo, Dkt. Kikwete atakuwa na jukumu la kuunga mkono jitihada za AU kupitia: kuendeleza diplomasia ya kuzuia migogoro na kuratibu mazungumzo jumuishi ya kisiasa. Aidha, kujenga uaminifu miongoni mwa wadau mbalimbali wa kikanda na kuimarisha ushirikiano wa kikanda unaolenga kukuza amani na utulivu wa kudumu.

Mhe. Dkt. Kikwete, kama Mwakilishi wa Ngazi ya Juu, atafanya kazi kwa uratibu wa karibu na AU na washirika muhimu wa kikanda na kimataifa, ikiwa ni pamoja na Mamlaka ya Kiserikali ya Maendeleo (IGAD), Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), Umoja wa Nchi za Kiarabu, na Umoja wa Mataifa (UN) ili kujenga amani na utulivu wa kudumu.

Ushirikiano huo ni muhimu kutokana na nafasi ya kimkakati ya Pembe ya Afrika na Bahari ya Shamu kwa biashara ya kimataifa na utulivu wa Bara la Afrika kwa ujumla.

Mhe. Youssouf ameeleza kuwa na imani kubwa na uzoefu, uongozi, na hekima za Dkt. Kikwete, na kwamba atatoa mchango mkubwa katika kuzisaidia nchi za kanda hiyo kukabiliana na changamoto zilizopo, kukuza ustawi pamoja na amani ya kudumu.

Uteuzi huu unakuja wakati ambapo eneo la Pembe ya Afrika na Bahari ya Shamu linaendelea kuhitaji ushirikiano wa karibu wa kidiplomasia ili kuhakikisha usalama wa kanda na ulinzi wa njia kuu za biashara duniani.




VIONGOZI WAUNGANA KUAGA MWILI WA MAREHEMU MHE. WILLIAM LUKUVI IRINGA

  Iringa, Machi 31, 2026 — Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba, amewasili nyumbani kwa aliyekuwa Wazir...