Wednesday, March 11, 2026

USIPIME KIWANJA UACHE PORI! DODOMA YAWAVAA WAMILIKI WALIOLEGEZA

Halmashauri ya Jiji la Dodoma imesema itafuta umiliki wa viwanja vyote ambavyo havijaendelezwa ndani ya muda uliowekwa kisheria, na kuvitwaa kwa ajili ya kuvigawa au kuviuza kwa wahitaji wengine kwa mujibu wa taratibu za sheria.

Kauli hiyo imetolewa Machi 11, 2026 na Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini wa Halmashauri hiyo, Ndugu Dennis Godwe, ambaye amesema lengo ni kuwakumbusha wananchi na taasisi zinazomiliki viwanja ndani ya Jiji la Dodoma kutekeleza wajibu wao wa kuendeleza maeneo hayo kwa wakati.

Ameeleza kuwa kwa mujibu wa Sheria ya Ardhi namba 4 ya mwaka 1999 (Sura ya 113), mmiliki wa kiwanja anatakiwa kukiendeleza ndani ya kipindi kisichozidi miezi 36 tangu tarehe ya kupewa umiliki. Kushindwa kufanya hivyo ni ukiukwaji wa masharti ya umiliki na kunaweza kusababisha kufutwa kwa hati.

Hata hivyo, Halmashauri imebaini kuwapo kwa matukio ya watu wasiokuwa waadilifu kuvamia viwanja ambavyo havijaendelezwa, kuondoa bikoni na kuanza kufanya maendeleo bila kuwa wamiliki halali. Vitendo hivyo vimesababisha migogoro ya ardhi na usumbufu kwa wamiliki halali pamoja na Halmashauri, huku baadhi ya wananchi wakilazimika kufika ofisini kufuatilia maeneo yao yaliyovamiwa.

Aidha, imeonya dhidi ya tabia ya kuanza ujenzi wa kudumu bila kibali cha ujenzi kutoka Halmashauri, ikisisitiza kuwa hatua hiyo ni kinyume cha sheria. Ujenzi wowote unaofanywa bila kibali utachukuliwa hatua za kisheria, ikiwemo kubomolewa.

Katika kusimamia utekelezaji wa masharti hayo, Halmashauri inaongozwa na Sheria ya Mipangomiji namba 8 ya mwaka 2007, inayosimamia upangaji na maendeleo ya maeneo ya mijini.

TANZANIA YASHIRIKI MKUTANO, UWEZESHAJI WANAWAKE RIKA ZOTE









Tanzania imeshiriki mkutano uliohusu kufanikisha usawa wa kijinsia na kuwawezesha wanawake wa rika zote wakiwemo wazee.

Mkutano huo uliofanyika Machi 10, 2025 ni sehemu ya mkutano wa 70 wa Hali ya Wanawake Duniani (CSW 70) ulioanza Machi 09 hadi Machi 19, 2026 jijini New York nchini Marekani.

Lengo la Mkutano huo ni kuieleza dunia mafaniko ya Uwezeshaji Wanawake katika Sekta mbalimbali hasa upatikanaji wa Haki na huduma za Sheria.

Siku ya Pili ya Mkutano huo ujumbe wa Tanzania umeongozwa na Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Felister Mdemu.



BARAZA LA WAFANYAKAZI PBPA LAHIMIZWA KUWA NA UADILIFU KATIKA KUWAKILISHA MASLAHI YA WATUMISHI





📍Kibaha, Pwani – Machi 11, 2026

Wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi wa Wakala wa Uagizaji Mafuta kwa Pamoja (PBPA) wametakiwa kuzingatia uadilifu, uwazi na weledi katika kuwasilisha na kushughulikia changamoto za watumishi wanaowawakilisha, ili kuongeza ufanisi na tija katika utendaji kazi wa taasisi.

Wito huo umetolewa leo Machi 11, 2026 na Meneja wa Fedha na Mipango wa PBPA, Bw. Kedron Mbwilo, alipokuwa akizungumza kwa niaba ya Mtendaji Mkuu wa PBPA wakati wa ufunguzi wa Kikao cha Pili cha Baraza la Wafanyakazi kilichofanyika katika ukumbi wa Chuo cha Uongozi cha Mwalimu Nyerere, Kibaha mkoani Pwani.

Amesema Baraza la Wafanyakazi ni jukwaa muhimu linalounganisha menejimenti na watumishi, hivyo wajumbe wanapaswa kutekeleza majukumu yao kwa uadilifu na uwajibikaji mkubwa ili kuhakikisha masuala ya watumishi yanawasilishwa na kutatuliwa ipasavyo.

“Baraza la Wafanyakazi ni kiunganishi muhimu kati ya menejimenti na watumishi. Ni wajibu wa wajumbe kuwa waadilifu na kuwawakilisha watumishi wenzao kwa weledi mkubwa ili kuongeza tija na ufanisi katika taasisi,” amesisitiza Bw. Mbwilo.

Aidha, amewahimiza watumishi wa PBPA kuendelea kufanya kazi kwa ushirikiano na kujituma ili kuunga mkono jitihada za Serikali katika kufikia Dira ya Taifa ya Maendeleo ya 2050, ambayo kwa upande wa sekta ya nishati inalenga kuhakikisha Tanzania inakuwa na upatikanaji wa uhakika wa nishati ya mafuta, miundombinu imara ya mafuta pamoja na usimamizi bora wa rasilimali za petroli.

Kwa upande wake, Kaimu Meneja wa Rasilimali Watu wa PBPA, Bw. Matiko Sanawa, amewahimiza wajumbe wa baraza hilo kutumia kikao hicho kama fursa ya kujadili kwa uwazi maoni, mapendekezo na changamoto mbalimbali zitakazochangia kuimarisha uendeshaji wa taasisi.

Amefafanua kuwa kikao hicho cha Baraza la Wafanyakazi kinafanyika kwa mujibu wa matakwa ya kisheria na kwamba, pamoja na mambo mengine, kitajadili taarifa ya utekelezaji wa Mpango Kazi na Bajeti kwa kipindi cha Julai 2025 hadi Desemba 2026, pamoja na kuwasilishwa kwa rasimu ya Mpango Kazi wa PBPA kwa kipindi cha 2026/2027 hadi 2030/2031 na rasimu ya Bajeti ya PBPA kwa mwaka wa fedha 2026/2027.

RAIS SAMIA AMUASILI MTOTO MCHANGA ALIYETELEKEZWA NZEGA

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, amemuasili mtoto mchanga wa kike leo tarehe 11 Machi, 2026, katika makazi yake, Ikulu Chamwino, mkoani Dodoma.

Mtoto huyo aliyepewa jina la Grace Samia Suluhu Hassan alitelekezwa mjini Nzega, mkoani Tabora, na amekabidhiwa kwa Rais Dkt. Samia na Mkuu wa Wilaya ya Nzega, Mhe. Naitapwaki Tukai.

Akizungumza wakati wa kumkabidhi mtoto huyo, Mkuu wa Wilaya Tukai alisema mtoto huyo aliokotwa tarehe 17 Januari, 2026 akiwa ametelekezwa katika eneo jirani na nyumba ya wageni ya Kasulu, Nzega Mjini. 

Alieleza kuwa baada ya kupokea taarifa hizo, alishirikiana na Jeshi la Polisi kumchukua mtoto huyo na kumpeleka hospitalini kwa uchunguzi na uangalizi, huku juhudi za kumtafuta mama yake zikiendelea bila mafanikio.

Rais Dkt. Samia amemkaribisha mtoto huyo katika familia yake na kuahidi kumpatia malezi, ulinzi na huduma zote muhimu ili akue katika mazingira salama na yenye upendo.

“Wanaotupa watoto hawajui wanalolifanya. Kuliko kumtupa mtoto ni afadhali ukamkabidhi katika mamlaka za kisheria au kituo cha kulelea watoto. Kila mtoto aliyezaliwa ni hazina, na hatuijui kesho yake,” alisema Rais Dkt. Samia.

WIZARA YA NISHATI YAPOKEA TRIL. 1.15/- ZA MIRADI YA MAENDELEO







 📌Ni asilimia 61 ya bajeti ya 2025/26

Na Mwandishi Wetu, Dodoma

WIZARA ya Nishati imepokea Sh. trilioni 1.150 kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo katika kipindi cha Julai 2025 hadi Februari 2026, sawa na asilimia 61 ya bajeti ya maendeleo iliyoidhinishwa kwa mwaka wa fedha 2025/26.

Taarifa hiyo imetolewa Machi 10, 2026 na Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi, wakati akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa miradi ya sekta ya nishati kwa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini inayoongozwa na Mwenyekiti wake, Mhe. Subira Mgalu, katika Ukumbi wa Bunge jijini Dodoma.

Mhe.Ndejembi amesema katika mwaka wa fedha 2025/26 wizara imeendelea kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo inayolenga kuimarisha uzalishaji, usafirishaji na usambazaji wa umeme nchini.

Amesema katika fedha zilizopokelewa hadi sasa, Sh. bilioni 410.04 ni fedha za ndani na Sh. bilioni 740.30 ni fedha za nje ambazo zimeendelea kusaidia utekelezaji wa miradi mbalimbali ya sekta ya nishati.

Ameongeza kuwa miradi hiyo inajumuisha upelekaji wa umeme vijijini na vitongojini, utafutaji na uendelezaji wa mafuta na gesi asilia, ujenzi wa miundombinu ya usafirishaji na uhifadhi wa bidhaa za mafuta ya petroli pamoja na kukuza matumizi ya nishati safi ya kupikia.

Kwa mujibu wa Ndejembi, katika mwaka wa fedha 2025/26 Wizara ya Nishati iliidhinishiwa kutumia jumla ya Sh trilioni 1.965, ambapo Sh trilioni 1.886 sawa na asilimia 95.97 zilitengwa kwa ajili ya miradi ya maendeleo huku Sh bilioni 79.23 sawa na asilimia 4.03 zikiwa kwa matumizi ya kawaida.

Amefafanua kuwa kati ya fedha za maendeleo zilizoidhinishwa, Sh trilioni 1.466 ni fedha za ndani na Sh bilioni 420.49 ni fedha za nje.

Ndejembi ameishukuru Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kwa miongozo na maelekezo ambayo imekuwa ikitoa na kuchangia mafanikio katika utekelezaji wa miradi hiyo.

Amesisitiza kuwa wizara itaendelea kupokea ushauri na maoni ya kamati hiyo pamoja na kutoa ushirikiano unaostahili ili kuimarisha maendeleo ya sekta ya nishati nchini

PROF. KABUDI AKUTANA NA NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NJE WA CANADA






Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Kazi Maalum), Prof. Palamagamba Kabudi, amefanya mazungumzo na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Canada, Mhe. Robert Oliphant.

Mazungumzo hayo yamefanyika jijini London, Uingereza, pembezoni mwa Mkutano wa 26 wa Mawaziri wa Mambo ya Nje wa Jumuiya ya Madola uliofanyika Machi 8, 2026, ambapo viongozi hao wamejadili namna ya kuimarisha ushirikiano wa kimataifa kati ya Tanzania na Canada pamoja na kuendeleza uhusiano wao ndani ya Jumuiya ya Madola kwa kuzingatia misingi na tunu za jumuiya hiyo katika kukuza ushirikiano na maendeleo ya pamoja.

Viongozi hao wamebainisha kuwa uhusiano kati ya Tanzania na Canada umejengwa juu ya msingi wa urafiki wa kihistoria, ushirikiano wa kiuchumi pamoja na uanachama wao ndani ya Jumuiya ya Madola, hali inayofungua fursa zaidi za kupanua ushirikiano katika nyanja za biashara, uwekezaji na kubadilishana uzoefu katika sekta mbalimbali za maendeleo.

Aidha, viongozi hao wameangazia mchango wa diaspora wa Tanzania na Canada katika kuchochea maendeleo ya kiuchumi na kijamii katika nchi zao. 

Walieleza kuwa kupitia uhusiano wao ndani ya Jumuiya ya Madola, diaspora imeendelea kuwa kiungo muhimu kinachoimarisha uhusiano wa watu kwa watu na kufungua fursa zaidi za ushirikiano kati ya mataifa hayo mawili.

Katika mazungumzo hayo, Prof. Kabudi aliambatana na Mshauri wa Rais katika Masuala ya Diplomasia, Balozi Lazaro Nyalandu; Balozi wa Tanzania nchini Uingereza, Mhe. Mbelwa Kairuki; pamoja na Mkurugenzi wa Idara ya Ushirikiano wa Kimataifa katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Noel Kaganda.

WAZIRI KATAMBI MBELE YA KAMATI YA MAMBO YA NJE ULINZI NA USALAMA

Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Patrobas Katambi, amewasilisha Taarifa ya Utekelezaji wa Miradi inayotekelezwa na Vyombo vya Usalama vilivyo chini ya wizara yake mbele ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama.

Uwasilishaji huo umefanyika leo jijini Dodoma, ikiwa ni sehemu ya utaratibu wa kamati hiyo kupokea na kujadili taarifa za utekelezaji wa miradi iliyotengewa fedha na Serikali kwa lengo la kuhakikisha uwajibikaji, ufanisi na thamani ya fedha katika matumizi ya rasilimali za umma.

Katika taarifa yake, Waziri Katambi alieleza hatua zilizofikiwa katika utekelezaji wa miradi mbalimbali, ikiwa ni pamoja na maendeleo ya miundombinu, ununuzi wa vifaa, pamoja na maboresho yanayolenga kuimarisha utendaji wa vyombo vya usalama nchini. 

Aidha, alifafanua namna ambavyo wizara inaendelea kusimamia utekelezaji huo ili kuendana na malengo ya Serikali ya kuimarisha amani, usalama na ustawi wa taifa.

Kamati ilipokea na kujadili taarifa hiyo kwa lengo la kupata ufafanuzi wa kina kuhusu maendeleo ya miradi, changamoto zilizojitokeza pamoja na mikakati ya kuhakikisha miradi hiyo inakamilika kwa wakati na kwa viwango vinavyotarajiwa.







USIPIME KIWANJA UACHE PORI! DODOMA YAWAVAA WAMILIKI WALIOLEGEZA

Halmashauri ya Jiji la Dodoma imesema itafuta umiliki wa viwanja vyote ambavyo havijaendelezwa ndani ya muda uliowekwa kisheria, na kuvitwa...