Thursday, April 09, 2026

TUTABORESHA BAJETI YA ELIMU – WAZIRI MKUU




▪️Asema Serikali itaimarisha vitengo vya tathmini na ufuatiliaji kila wizara

Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba amesema Serikali itaendelea kuboresha bajeti ya elimu wakati ikitekeleza mtaala mpya wa elimu ili kuziba mianya ya mahitaji shuleni.

“Kwa kuwa tunaenda katika mtaala mpya wa elimu, tutaendelea kuboresha bajeti. Tutaendelea kuboresha bajeti kwa sababu mahitaji yanaongezeka kila wakati katika kumfanya mtoto asome vizuri,” amesema.

Waziri Mkuu ametoa kauli hiyo Bungeni jijini Dodoma, leo (Alhamisi, Aprili 9, 2026) wakati akijibu swali la Mbunge wa Segerea, Agnesta Lambert Kaiza, kwenye kipindi cha maswali ya papo kwa papo kwa Waziri Mkuu ambaye alitaka kujua kauli ya Serikali juu ya kukomesha michango holela inayotozwa shuleni.

Dkt. Mwigulu amesema Serikali haina shida na michango ya chakula ambayo imekuwa ikitolewa shuleni lakini akasisitiza kuwa endapo kutatokea michango mingine yoyote, ni lazima ifuate miongozo ya serikali na ipate baraka za Wakuu wa Mikoa husika.

Akitoa mfano wa michango ambayo haikubaliki, Waziri Mkuu amesema akiwa ziarani mkoani Katavi, alipokea malalamiko ya Mama mmoja ambaye mwanaye alizuiwa kujiunga na shule ya sekondari hadi atoe sh. 50,000/- ya dawati.

“Nilielekeza yule mtoto arudishwe shuleni na nimpongeze Mkuu wa Mkoa ambaye amenijulisha kuwa yule mtoto amesharudi shuleni. Lakini pia nilielekeza yule mwalimu mkuu naye aitwe na mamlaka za nidhamu, ahojiwe kwa uzembe wa kuona mtoto anakosa masomo kwa miezi miwili na wao wakaendelea na maisha kana kwamba hakuna jambo lililotokea,” amesema.

Mbali na changamoto hiyo, Waziri Mkuu amewapongeza walimu nchini kwa kujitoa bila kuchoka ili kuhakikisha watoto wa Kitanzania wanapata elimu bora. “Sote tunatambua kuwa walimu wengi wamejitoa sana katika baadhi ya maeneo. Licha ya wingi watoto na uchache wa walimu, kwa juhudi zao wamehakikisha wanakamilisha syllabus zao ili watoto wetu wapate elimu bora.”

Akielezea kuhusu uwepo wa walimu wa kujitolea katika baadhi ya shule, Waziri Mkuu amesema alishatoa maelekezo kwamba malipo ya walimu wa aina hiyo yatoke kwenye mapato ya ndani ya Halmashauri husika badala ya kuwataka wazazi wachangie malipo yao.

“Wazo la kuwa na walimu wa kujitolea ni jema, na sisi wakati tunasoma tulipata mafunzo ya ziada (tuition) kwa walimu wa aina hii. Wazo la kuwa na walimu wanaojitolea ni jema lakini malipo yao yasilipwe na wazazi, badala ya kwenda kwenye michango, Mamlaka za Serikali za Mitaa watumie mapato ya ndani.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu amesema Serikali itaendelea kuimarisha vitengo vya tathmini na ufuatiliaji katika kila wizara ili viweze kufanya kazi kwa ufanisi zaidi. “Kwenye kila wizara, kuna hivi vitengo vya ufuatiliaji na tathmini. Tunapanga kuongeza bajeti zao ili viweze kutimiza wajibu wao katika ufuatiliaji wa miradi na shughuli zote za Serikali.

Alikuwa akijibu swali la Mbunge wa Monduli, Isack Joseph Copriano aliyetaka kujua  Serikali ina mkakati gani wa kuimarisha timu ya tathmini na ufuatiliaji ili kuharakisha majibu ya wananchi na hususan kero zao. 

Alisema katika kuimarisha mawasiliano na wananchi, Serikali imeanzisha kituo cha kupokea simu (Call Centre) yenye namba 190 ambapo mwananchi mwenye shida yoyote anaweza kupiga simu na kutoa kero yake na kwamba atajulishwa majibu yake kupitia kituo hicho.

Amesema Serikali inataka kurejesha utaratibu wa kila kiongozi kubeba hoja za wananchi kupitia rejesta ambazo zitakuwa zinatumika kwenye ofisi za viongozi kurekodi kero za wananchi na kutoa mrejesho serikalini kila mwisho wa mwezi.

“Utaratibu wa kupokea kero siyo wa kwenye ziara tu, kila mwezi viongozi watapaswa kutoa taarifa ya idadi ya wananchi waliowahudumia na majibu waliyowapa wakionesha hoja zipi walipokea, namba za simu za wananchi waliohudumiwa na hizo hoja zimetatuliwa vipi.” 

“Tunataka kurejesha utaratibu wa kila kiongozi kubeba hoja za wananchi na siyo kuacha wananchi waende kutafuta majibu kwa viongozi,” alisisitiza.


Wednesday, April 08, 2026

RAIS SAMIA ASHIRIKI DUA MAALUM KUMUENZI HAYATI KARUME, MIAKA 54 BAADA YA KUUAWA KWAKE











Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, jana tarehe 07 Aprili 2026 aliungana na viongozi mbalimbali pamoja na wananchi katika dua maalum ya kumuombea aliyekuwa Rais wa kwanza wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Hayati Abeid Amani Karume, ikiwa ni kumbukizi ya miaka 54 tangu kuuawa kwake.

Dua hiyo ilifanyika katika Afisi Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) Kisiwandui, Zanzibar, mahali penye historia kubwa katika harakati za kisiasa na mapinduzi ya Zanzibar. 

Tukio hilo limeambatana pia na zoezi la uwekaji wa shada la maua katika kaburi la hayati Karume, kama ishara ya heshima, kumbukumbu na kutambua mchango wake mkubwa katika kuijenga Zanzibar ya kisasa.

Katika tukio hilo lenye uzito wa kihistoria na kiimani, viongozi wa dini waliongoza dua maalum ya kumuombea marehemu Karume, wakisisitiza umuhimu wa kuendeleza amani, mshikamano na uzalendo aliouasisi. 

Viongozi wa serikali, chama na wananchi waliohudhuria walipata fursa ya kutafakari mchango wake katika kuimarisha misingi ya Mapinduzi ya Zanzibar na kuleta maendeleo ya kijamii na kiuchumi.

Hayati Karume anakumbukwa kama kiongozi shupavu aliyesimamia mageuzi makubwa baada ya Mapinduzi ya Zanzibar ya mwaka 1964, akijenga misingi ya usawa, haki na maendeleo kwa wananchi wa Zanzibar. Urithi wake unaendelea kuenziwa na viongozi wa sasa pamoja na vizazi vipya, kama sehemu ya historia muhimu ya Taifa.

Maadhimisho haya yanaendelea kuwa chachu ya kuwakumbusha Watanzania umuhimu wa kulinda amani, umoja na mshikamano wa kitaifa—misingi ambayo hayati Karume aliisimamia kwa dhati katika uongozi wake.

Friday, April 03, 2026

TANZANIA NA URUSI ZAIMARISHA USHIRIKIANO WA KIMKAKATI KATIKA SEKTA YA UCHUKUZI

Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Shirikisho la Urusi zimeingia hatua mpya ya ushirikiano wa maendeleo baada ya kusaini hati ya makubaliano katika sekta ya uchukuzi, ikiwa ni sehemu ya jitihada za kukuza miundombinu ya kisasa na kuongeza ufanisi wa usafirishaji nchini.

Makubaliano hayo yalisainiwa tarehe 03 Aprili 2026 jijini St. Petersburg, Urusi, pembezoni mwa Mkutano wa Kimataifa wa Uchukuzi na Usafirishaji, yakihusisha Wizara ya Uchukuzi ya Tanzania na Wizara ya Uchukuzi ya Shirikisho la Urusi.

Kwa upande wa Urusi, Waziri wa Uchukuzi, Mhe. Andrey Nikitin, alieleza kuwa nchi yake ipo tayari kuendeleza ushirikiano wa karibu na Tanzania, akisisitiza kuwa hatua hiyo ni utekelezaji wa maazimio ya Mkutano wa Russia–Africa 2023. Alibainisha kuwa ushirikiano huo utahusisha uwekezaji katika miundombinu ya kisasa, msaada wa kiufundi, pamoja na ushiriki katika miradi ya kimkakati yenye tija kwa pande zote mbili.

Naye Waziri wa Uchukuzi wa Tanzania, Mhe. Prof. Makame Mbarawa, alisema makubaliano hayo yanaendana kikamilifu na mkakati wa Serikali wa kuimarisha sekta ya uchukuzi kwa kushirikiana na mataifa yenye uzoefu mkubwa na teknolojia ya hali ya juu.

Alifafanua kuwa kupitia ushirikiano huo, Tanzania itanufaika na ubadilishanaji wa utaalamu, mafunzo kwa wataalamu, pamoja na uhamishaji wa teknolojia utakaosaidia kuongeza ufanisi, ubora na ushindani wa miundombinu ya uchukuzi. Aidha, alisisitiza kuwa hatua hiyo itaiwezesha Tanzania kujijengea nafasi imara kama kitovu cha usafirishaji na biashara katika ukanda wa Afrika Mashariki na kati.

Kwa mtazamo mpana, makubaliano haya yanafungua ukurasa mpya wa fursa za uwekezaji, utafiti na ubunifu, huku yakichochea maendeleo ya rasilimali watu na kuimarisha zaidi uhusiano wa kidiplomasia na kiuchumi kati ya Tanzania na Urusi.

#Tanzania #Urusi #Uchukuzi #Maendeleo #Uwekezaji #Diplomasia #Miundombinu #HabariZaLeo








UPATIKANAJI WA DAWA WAIMARIKA NCHINI

 OWM-TAMISEMI

Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa  (OWM– TAMISEMI) anayeshughulikia masuala ya Afya, Mhe. Dkt. Jafari Seif, amesema kuwa hali ya upatikanaji wa bidhaa za afya katika ngazi ya huduma za afya ya msingi nchini imeendelea kuimarika na kufikia kiwango cha kuridhisha ikilinganishwa na miaka iliyopita.

Akizungumza Aprili 2, 2026 jijini Dar es Salaam, katika kikao kazi kilichoongozwa na Waziri wa Afya, Mhe.Mohamed Mchengerwa, pamoja na wadau wa sekta ya afya, katika ofisi za Bohari ya Dawa (MSD), Mhe. Dkt. Seif amesema kuwa tathmini ya mwaka 2026 inaonesha hali ya upatikanaji wa dawa imefikia asilimia 89 katika hospitali, asilimia 88 katika vituo vya afya, na asilimia 88 katika zahanati.

Ameongeza kuwa katika mwaka wa fedha 2024/25, vituo vya kutolea huduma za afya ngazi ya msingi vilikusanya takribani Shilingi Bilioni 108, huku makusanyo hayo yakitarajiwa kuongezeka hadi kufikia Shilingi Bilioni 192 katika mwaka 2025/26.   

Kwa upande wake, Waziri wa Afya, Mhe. Mohamed Mchengerwa, amemuelekeza Katibu Mkuu wa wizara hiyo kushirikiana kwa karibu na Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI kuandaa na kusimamia miongozo, taratibu na miundo ya usimamizi wa vituo vya kutolea huduma za afya. Lengo la hatua hiyo ni kuhakikisha kuwa wafamasia kote nchini wanakuwa sehemu muhimu ya timu za menejimenti katika vituo hivyo, ili kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma za afya.




MAKAMU WA PILI WA RAIS ZANZIBAR AUNGANA NA WAUMINI IJUMAA PEMBA, ASISITIZA UMOJA NA MAADILI






Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Alhajj Hemed Suleiman Abdulla, leo ameungana na Waumini wa Dini ya Kiislamu katika ibada ya Sala ya Ijumaa iliyofanyika katika Msikiti wa Al-Tawfiiq, uliopo Jundamiti Kiwani, Wilaya ya Mkoani, Mkoa wa Kusini Pemba.

Mara baada ya ibada hiyo, Alhajj Hemed alipata fursa ya kuwasalimia waumini na kubadilishana nao salamu za amani, upendo na mshikamano, akionesha ukaribu wa dhati kati ya uongozi na wananchi. Tukio hilo liligubikwa na hali ya furaha na heshima, huku waumini wakionesha kuthamini uwepo wa kiongozi huyo miongoni mwao.

Katika mazungumzo yake, alisisitiza umuhimu wa kudumisha maadili mema, kuheshimiana na kuendeleza umoja kama nguzo muhimu ya ustawi wa jamii na maendeleo endelevu. Amesema mshikamano wa kijamii na kiroho ni msingi imara unaoweza kuijenga jamii yenye amani na utulivu.

Tukio hilo limeendelea kudhihirisha dhamira ya viongozi kuwa karibu na wananchi pamoja na kuimarisha uhusiano unaojenga mshikamano na maelewano katika jamii.

Imetolewa na Kitengo cha Habari (OMPR)
Leo, tarehe 03 Aprili 2026.

#Zanzibar #Pemba #Ijumaa #Uongozi #Mshikamano #Amani #Maendeleo #OMPR #HabariZaLeo

TAIFA GAS IMETANGAZA KUWA HAITAPANDISHA BEI YA GESI YA MAJUMBANI (LPG) LICHA YA ONGEZEKO LA BEI KATIKA SOKO LA KIMATAIFA

 

Picha ni ya AI

Taifa Gesi haitapandisha bei ya gesi ya majumbani (LPG) licha ya ongezeko la takribani asilimia 43 ya bei ya gesi hiyo duniani. Hatua hii ni sehemu ya juhudi za kampuni hiyo kuendeleza upatikanaji nafuu wa nishati hiyo pamoja na kupunguza za athari za mabadiliko ya soko la kimataifa kwa wateja wake.

Katika taarifa yake kwa vyombo vya habari, Taifa Gas imeeleza kuwa soko la kimataifa la gesi ya kupikia limekumbwa na ongezeko kubwa la bei katika wiki za hivi karibuni na hivyo kusababisha kuongezeka kwa gharama za ununuzi katika minyororo ya ugavi na usambazaji duniani.

Alieleza kuwa katika wiki za hivi karibuni, soko la kimataifa la gesi ya kupikia limekumbwa na ongezeko kubwa la bei, hali iliyosababisha kupanda kwa gharama katika minyororo ya ugavi na usambazaji duniani.

“Katika mazingira haya ya sasa, tunayo dhamira ya dhati ya kuwasaidia wateja wetu kwa kubeba athari za ongezeko la gharama ya nishati ya kupikia kwa kutokuongeza bei huku tukihakikisha upatikanaji endelevu wa gesi safi na ya kuaminika,” alisema Deogratius.

Aliongeza kuwa kipaumbele cha kampuni hiyo kwa sasa ni kuhakikisha utulivu wa bei unaendelea ili kusaidia shughuli za kiuchumi, akibainisha kuwa gesi ya kupikia ni nishati muhimu kwa kaya nyingi pamoja na biashara ndogo ndogo nchini.

“Tunatambua kuwa gesi ya kupikia ni nishati muhimu kwa Watanzania wengi na lengo letu ni kuhakikisha kwamba inapatikana kwa bei nafuu huku tukidumisha usambazaji wa uhakika kote nchini,” alisisitiza.

Kwa upande wa usambazaji, kampuni hiyo imeeleza kuwa itaendelea kuhakikisha upatikanaji wa gesi kupitia mtandao wake wa maghala 25 yaliyosambaa nchini, hatua inayolenga kufikisha huduma hiyo katika maeneo ya mijini na vijijini.

Deogratius alibainisha kuwa Tanzania ni nchi kubwa yenye mahitaji tofauti ya nishati, hivyo uwekezaji katika miundombinu ya usambazaji umezingatiwa ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma hiyo kwa urahisi zaidi.

Aidha, kampuni hiyo imeeleza kuwa inaendelea kuunga mkono vipaumbele vya kitaifa vya nishati pamoja na Malengo ya Maendeleo Endelevu (SDGs), kwa kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia.

Ilieleza kuwa matumizi ya gesi ya kupikia yanachangia kuboresha afya za wananchi kwa kupunguza athari za moshi wa kuni na mkaa, sambamba na kulinda mazingira na kuchochea ushiriki wa wananchi katika shughuli za kiuchumi.

Thursday, April 02, 2026

UTEKELEZAJI WA DIRA 2050 UANZE - DKT. MWIGULU





WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba ameagiza kuanza utekelezaji wa Dira 2050 kupitia Mpango na Bajeti iliyoandaliwa na kuendelea kuishirikisha sekta binafsi na wadau wa maendeleo katika kuharakisha utekelezaji wake ili kujenga uchumi jumuishi, shindani na unaotegemea uzalishaji wenye tija.

Aidha, Waziri Mkuu ameilekeza Tume ya Mipango kuendelea kutoa elimu kwa umma kuhusu Dira 2050 ili kuwezesha kushiriki kikamilifu katika utekelezaji wake kwa sababu suala hilo litawezekana ikiwa wadau wote watakuwa na ufahamu wa kutosha kuhusu vipaumbele vilivyoainishwa katika Dira 2050.

Waziri Mkuu ametoa maagizo hayo leo (Jumatano, Aprili 1, 2026) wakati akiwasilisha hotuba yake kuhusu Mapitio na Mwelekeo wa Kazi za Serikali na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na Ofisi ya Bunge kwa Mwaka 2026/2027 Bungeni jijini Dodoma.

Amesema Dira 2050 iliyozinduliwa na Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan mnamo tarehe 17 Julai, 2025, itaongoza mipango ya maendeleo katika miaka 25 ijayo inalenga kujenga Taifa jumuishi, lenye ustawi kwa wote, lenye haki na linalojitegemea.

 “Nitoe rai kwa viongozi wa Serikali, Dini, Sekta Binafsi, Asasi za Kiraia na Wadau wa Maendeleo kuhakikisha kwamba mipango yao inawiana na vipaumbele vya Dira 2050 na kuiunga mkono katika utekelezaji wake”.

Amesema utekelezaji wa Dira hiyo, utawezesha Taifa kuwa na uchumi wenye thamani ya dola za Marekani trilioni moja na wastani wa pato la mtu mmoja mmoja kuwa dola za Marekani 7,000 kwa mwaka ifikapo 2050. “Nguzo muhimu za kutuwezesha kufikia malengo hayo ni pamoja na utawala bora, amani, usalama na utulivu.”

Vilevile, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu amewaagiza viongozi wa kila sekta wahakikishe rasilimali zote za Taifa zinaelekezwa katika maeneo yenye tija na matokeo makubwa ili kupunguza utegemezi kutoka nje.

Amesema kuwa Dira 2050 imejengwa na nguzo kuu tatu ambazo ni uchumi imara jumuishi na shindani; uwezo wa watu na maendeleo ya jamii; na uhifadhi wa mazingira na ustahimilivu wa mabadiliko ya tabianchi.

Amesema katika hatua za kutekeleza Dira hiyo kwa vitendo, Serikali kwa kushirikiana na wadau imeweka mikakati mbalimbali ya utekelezaji, ambayo ni pamoja na kuchagiza ubia kati ya sekta ya umma na binafsi.

Waziri Mkuu ameongeza kuwa mikakati mingine ni pamoja na matumizi yenye tija ya rasilimali za Taifa kupitia utekelezaji wa programu za kimkakati na kukuza utamaduni wa kuweka akiba kwa ajili ya uwekezaji.

Amesema Mpango na Bajeti itakayopitishwa na Bunge hilo ni hatua ya kwanza ya utekelezaji wa Mpango wa Nne wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano 2026/2027 - 2030/2031 na Dira 2050,huku dhima ya mpango huo ni “Mageuzi katika Kukuza Uchumi na Kuzalisha Ajira.”

Amesema mipango hiyo inawezesha Taifa kuelekeza rasilimali katika vipaumbele vya kimkakati vyenye matokeo makubwa kwa ajili ya ukuaji wa uchumi na ustawi wa wananchi.

Aidha, Waziri Mkuu amesema kwa kutambua umuhimu wa Dira hiyo, Serikali itaendelea kuimarisha mfumo wa ufuatiliaji na tathmini pamoja na kuhimiza uwajibikaji, ili kuhakikisha tunafikia malengo tuliyojiwekea.

Waziri Mkuu ameliomba Bunge liidhinishe jumla ya shilingi trilioni 12.50 kati ya fedha hizo, shilingi trilioni 8.73 ni kwa ajili ya matumizi ya kawaida na shilingi trilioni 3.76 ni kwa ajili ya matumizi ya maendeleo. Fedha hizo ni kwa ajili ya Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake kwa mwaka 2026/2027.

Vilevile, Waziri Mkuu ameliomba Bunge liidhinishe jumla ya shilingi 225,021,780,000 kwa ajili ya Mfuko wa Bunge. Kati ya fedha hizo, shilingi 207,992,798,000 ni kwa ajili ya matumizi ya kawaida na shilingi 17,028,982,000 ni kwa ajili ya matumizi ya maendeleo.

TUTABORESHA BAJETI YA ELIMU – WAZIRI MKUU

▪️Asema Serikali itaimarisha vitengo vya tathmini na ufuatiliaji kila wizara Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba amesema Serikali itaendelea ku...