Tuesday, June 16, 2026

MAMA NEEMA MWIGULU AHIMIZA TAASISI KUUNGA MKONO JUHUDI ZA SERIKALI KUPITIA UWAJIBIKAJI KWA JAMII







Mwenza wa Waziri Mkuu, Mama Neema Mwigulu Nchemba, amehimiza taasisi za umma na binafsi kuendelea kuunga mkono juhudi za Serikali katika kuboresha huduma za kijamii kupitia utekelezaji wa programu za uwajibikaji kwa jamii (CSR).

Mama Neema amesema hayo leo Jumanne, Juni 16, 2026 katika hafla ya kukabidhi vifaa vya hospitali vilivyotolewa na Shirika la Viwango Tanzania (TBS) katika Hospitali ya Wilaya ya Chamwino, Mkoa wa Dodoma, ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya miaka 50 ya shirika hilo.

Mama Neema ambae alikuwa mgeni rasmi katika hafla hiyo, amesema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imefanya uwekezaji mkubwa katika sekta ya afya kupitia ujenzi wa miundombinu ya kutolea huduma za afya, ajira kwa wataalamu wa afya, upatikanaji wa dawa na vifaa tiba pamoja na kuimarisha huduma za kibingwa na ubingwa bobezi.

“Tunashuhudia maboresho makubwa katika sekta ya afya kutokana na uwekezaji unaoendelea kufanywa na Serikali. Leo tunajivunia huduma nyingi ambazo hapo awali zilikuwa zinapatikana nje ya nchi kupatikana hapa nchini,” amesema.

Mama Neema amewapongeza viongozi wa Shirika la Viwango Tanzania kwa kuendelea kutekeleza kwa vitendo sera ya uwajibikaji kwa jamii na kuchangia ustawi wa wananchi kupitia sekta ya afya pamoja na makundi mbalimbali yenye mahitaji maalum.

Amesema vifaa vilivyotolewa vitasaidia kuboresha utoaji wa huduma katika Hospitali ya Wilaya ya Chamwino na kuongeza ustawi wa mama na mtoto.

Vifaa hivyo vinajumuisha vitimwendo 20, vitanda vya kujifungulia vitano, vitanda vya kufanyia uchunguzi vitano, vitanda vitano vya kulaza wagonjwa, machela moja ya kisasa, makabati matatu ya kuhifadhia vifaa tiba pamoja na mabeseni yenye vifaa mbalimbali kwa ajili ya akinamama 30 waliojifungua.

Awali, akimkaribisha mgeni rasmi kuzungumza katika hafla hiyo, Waziri wa Viwanda na Biashara, Judith Kapinga amesema Serikali itaendelea kuhimiza taasisi zake kutekeleza kwa vitendo sera ya uwajibikaji kwa jamii ili kuchangia kuboresha huduma za kijamii na maisha ya wananchi.

Amesema msaada uliotolewa na Shirika la Viwango Tanzania (TBS) katika Hospitali ya Wilaya ya Chamwino ni sehemu ya mchango wa taasisi za umma katika kuunga mkono jitihada za Serikali za kuimarisha huduma za afya nchini pamoja na kuendelea kuyaishi maono ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuboresha ustawi wa wananchi.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Viwango Tanzania (TBS), Dkt. Ashura Katunzi amesema shirika hilo limeendelea kutekeleza miradi mbalimbali ya kijamii katika sekta ya afya, elimu na makundi maalum ikiwa ni sehemu ya mchango wake kwa maendeleo ya jamii.

Amesema TBS itaendelea kushirikiana na Serikali na wadau mbalimbali katika kuboresha maisha ya wananchi kupitia programu zake za uwajibikaji kwa jamii.

TANESCO YAKAMILISHA MIRADI YA KUIMARISHA UPATIKANAJI WA UMEME DODOMA







📌 Itanufaisha wilaya za Kongwa,Gairo, Mpwapwa, na Chamwino 

📌 Waziri Ndejembi azindua Kituo cha Kubadilishia Njia za Usambazaji Umeme na Transfoma ya Kudhibiti Umeme

📌 Serikali yawekeza zaidi ya Shilingi Bilioni 10.5 kuimarisha huduma ya umeme

Na Mwandishi Wetu, Kongwa

Wananchi wa Wilaya za Gairo, Mpwapwa, Kongwa, Chamwino na Kiteto wanatarajiwa kunufaika na huduma ya umeme wa uhakika zaidi kufuatia kukamilika kwa miradi ya kuimarisha mfumo wa usambazaji wa umeme iliyotekelezwa na Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) kwa gharama ya zaidi ya Shilingi bilioni 10.5.

Miradi hiyo inahusisha Kituo cha Kubadilishia Njia za Usambazaji Umeme (Switching Station), Transfoma ya Kudhibiti Umeme (Automatic Voltage Regulator – AVR) yenye uwezo wa MVA 20 pamoja na njia ya kusafirisha umeme ya msongo wa kilovoti 33 kutoka Kituo cha Kupokea na Kupoza Umeme cha Zuzu hadi Mbande yenye urefu wa kilomita 92.

Akizindua miradi hiyo Juni 16, 2026 katika eneo la Mbande, Wilaya ya Kongwa, Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi, alisema uwekezaji huo ni sehemu ya juhudi za Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, za kuhakikisha wananchi wanapata huduma ya umeme wa uhakika kwa ajili ya shughuli za kijamii na kiuchumi.

Alisema miradi hiyo imeleta maboresho makubwa katika mfumo wa usambazaji wa umeme katika ukanda huo, ambapo hapo awali hitilafu zilizokuwa zikitokea katika eneo moja zilisababisha wananchi wa maeneo mengine kukosa huduma ya umeme kwa muda.

“Kituo hiki kimeimarisha upatikanaji wa umeme wa uhakika. Tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa uwekezaji mkubwa uliofanyika. Hapo awali changamoto zilikuwa kubwa, hususan wakati wa mvua ambapo hitilafu katika wilaya moja ziliathiri huduma katika wilaya nyingine. Leo tunashuhudia matokeo ya uwekezaji huu kwa manufaa ya wananchi wetu,” alisema Mhe. Ndejembi.

Waziri huyo alibainisha kuwa Serikali itaendelea kuwekeza katika sekta ya nishati kupitia miradi mbalimbali ya kimkakati inayolenga kuimarisha uzalishaji, usafirishaji na usambazaji wa umeme nchini ili kuendana na kasi ya maendeleo ya Taifa na mahitaji ya wananchi.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, Mhe. Subira Mgalu, alisema utekelezaji wa miradi ya umeme unaendelea kuleta matokeo chanya kwa wananchi na kuchangia kufanikisha agenda ya maendeleo ya Serikali.

“Tunafarijika kuona kazi kubwa inayofanywa na TANESCO kuhakikisha Watanzania wanapata umeme wa uhakika. Hapo nyuma kulikuwa na changamoto za kukatika kwa umeme mara kwa mara katika maeneo haya, lakini Serikali ya Awamu ya Sita imefanya uwekezaji mkubwa kupitia TANESCO na matokeo yake yanaonekana wazi,” alisema Mhe. Mgalu.

Naye Mkuu wa Wilaya ya Kongwa, Mhe. Mayeka Simon Mayeka, aliwataka wananchi na wawekezaji kutumia fursa ya upatikanaji wa umeme wa uhakika kuanzisha shughuli mbalimbali za uzalishaji mali ikiwemo viwanda vya usindikaji, biashara na shughuli nyingine za kiuchumi zitakazochochea maendeleo ya eneo hilo.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO, Bw. Lazaro Twange, alisema kwa muda mrefu wananchi wa Kongwa na maeneo jirani walitegemea njia moja ya umeme ya msongo wa kilovoti 33 kutoka Dodoma Mjini, hali iliyokuwa ikisababisha changamoto za upatikanaji wa umeme wa uhakika kutokana na ongezeko la mahitaji ya huduma hiyo.

Alisema kukamilika kwa miradi hiyo kumeimarisha mfumo wa usambazaji wa umeme katika ukanda huo na kupunguza kwa kiasi kikubwa changamoto zilizokuwa zikiathiri upatikanaji wa huduma.

“Awali kulikuwa na njia moja ya kusambaza umeme inayopita katika wilaya tano tofauti. Kuongezeka kwa mahitaji ya umeme pamoja na fursa za uwekezaji kulianza kuleta changamoto katika utoaji wa huduma. Tangu miradi hii ilipoanza kufanya kazi, tumeshuhudia maboresho makubwa na changamoto zilizokuwa zikiathiri huduma zimepungua kwa zaidi ya asilimia 90,” alisema Bw. Twange.

Kukamilika kwa miradi hiyo kunatarajiwa kuimarisha zaidi upatikanaji wa huduma ya umeme, kuongeza fursa za uwekezaji, kukuza shughuli za kiuchumi na kuboresha utoaji wa huduma za kijamii katika Wilaya za Gairo, Mpwapwa, Kongwa, Chamwino na Kiteto.

Friday, June 12, 2026

CGP. KATUNGU AWATAKA MAAFISA USTAWI KUELIMISHA WAFUNGWA HAKI NA WAJIBU WAO


 Na. Ssgt Mawazo Mtondo – Dodoma.

Mkuu wa Jeshi la Magereza, CGP Jeremiah Yoram Katungu, amewataka Maafisa Ustawi wa Jamii wa Jeshi la Magereza kuhakikisha wanawaelimisha wafungwa na mahabusu kuhusu haki na wajibu wao mara wanapopokelewa magerezani pamoja na taratibu zinazopaswa kufuatwa katika kipindi chote wanaposhikiliwa gerezani.

CGP Katungu ametoa maelekezo hayo leo Juni 12, 2026 wakati akifunga rasmi Mafunzo ya Maafisa Ustawi wa Jamii kuhusu Mwongozo wa Utekelezaji wa Programu za Urekebishaji yaliyofanyika kwa siku tatu katika Ukumbi wa Rugimbana, Msalato jijini Dodoma.

Amesema mafunzo hayo ni sehemu ya jitihada za Jeshi la Magereza za kuendelea kuboresha huduma za urekebishaji kwa wafungwa sambamba na kutekeleza maelekezo ya Serikali na mapendekezo ya Tume ya Kuboresha Vyombo vya Haki Jinai.

Akizungumza na washiriki wa mafunzo hayo, CGP Katungu alisema mwongozo huo umebainisha maeneo muhimu yanayopaswa kuzingatiwa katika utekelezaji wa jukumu la urekebishaji, ikiwemo maadili ya kazi, dhana ya urekebishaji wa wafungwa, haki za binadamu katika utekelezaji wa programu za urekebishaji pamoja na matumizi sahihi ya nyaraka na fomu mbalimbali za kazi.

Aliwataka washiriki kutumia maarifa waliyojifunza kwa weledi na ufanisi ili kuleta mageuzi chanya katika utekelezaji wa jukumu la msingi la Jeshi la Magereza la kuwarekebisha wafungwa. Aidha, aliwahimiza kushirikiana na Wakuu wa Magereza kuanzisha na kuimarisha shughuli zinazolenga kuwapatia wafungwa elimu, maarifa na ujuzi wa kujitegemea.

Vilevile, aliwataka maafisa na askari wote wa Jeshi la Magereza kutekeleza majukumu yao kwa kuzingatia haki za wafungwa na mahabusu bila kuathiri usalama wao na wa magereza kwa ujumla. Alisisitiza umuhimu wa kudumisha upendo, mshikamano na umoja miongoni mwa watumishi wa Jeshi la Magereza ili kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa majukumu na kuendelea kulitumikia Taifa kwa ufanisi.

Awali akimkaribisha Mkuu wa Jeshi la Magereza, Kamishna wa Sheria na Uendeshaji wa Magereza, CP Nicodemus Tenga, alimshukuru kwa kuridhia kufanyika kwa mafunzo hayo yaliyolenga kuwajengea uwezo, maarifa na stadi za kiutendaji Maafisa Ustawi wa Jamii.

CP Tenga alisema mafunzo hayo pia yalitoa fursa kwa washiriki kubadilishana uzoefu na kujifunza mbinu mbalimbali za kuboresha utendaji wao katika maeneo ya kazi kwa lengo la kuimarisha huduma za urekebishaji ndani ya Jeshi la Magereza.











RAIS SAMIA AIPONGEZA BOT KWA KUKUSANYA DHAHABU YA THAMANI YA TSH TRILIONI 10, ATOA MAELEKEZO MAPYA KUHUSU MIKOPO KWA WANANCHI

 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye picha na Waziri wa Fedha Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar pamoja na Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania Bw. Emmanuel Tutuba kwenye Maadhimisho ya cha miaka 60 ya Benki Kuu ya Tanzania yaliyofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC), Jijini Dar es Salaam tarehe 12 Juni, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akipokea zawadi ya Kitabu cha picha za matoleo ya noti kuanzia mwaka 1966-2026, pamoja na Sarafu ya kumbukumbu ya miaka 60 ya Benki Kuu ya Tanzania kutoka kwa Gavana wa Benki hiyo Bw. Emmanuel Tutuba katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC), Jijini Dar es Salaam tarehe 12 Juni, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akipokea zawadi ya Kitabu cha picha za matoleo ya noti kuanzia mwaka 1966-2026, pamoja na Sarafu ya kumbukumbu ya miaka 60 ya Benki Kuu ya Tanzania kutoka kwa Gavana wa Benki hiyo Bw. Emmanuel Tutuba katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC), Jijini Dar es Salaam tarehe 12 Juni, 2026.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akipokea Tuzo Maalum kutoka Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania Bw. Emmanuel Tutuba kwenye Maadhimisho ya cha miaka 60 ya Benki hiyo yaliyofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC), Jijini Dar es Salaam tarehe 12 Juni, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, ameipongeza Benki Kuu ya Tanzania (BoT) kwa mafanikio makubwa ya kukusanya tani 27.05 za dhahabu zenye thamani ya zaidi ya Shilingi trilioni 10, hatua aliyoitaja kuwa ya kimkakati katika kuimarisha uchumi wa Taifa na kulinda thamani ya Shilingi ya Tanzania.

Rais Samia ametoa pongezi hizo leo Juni 12, 2026, wakati akihutubia kilele cha Maadhimisho ya Miaka 60 ya Benki Kuu ya Tanzania yaliyofanyika katika Ukumbi wa Kimataifa wa Mikutano wa Julius Nyerere (JNICC), jijini Dar es Salaam.

"Nipongeze Benki Kuu kwa mpango wa ununuzi wa dhahabu ya ndani. Hadi mwezi Mei mwaka huu tumefanikiwa kukusanya tani 27.05 za dhahabu zenye thamani ya shilingi trilioni 10. Hapa tulipofika si haba," amesema Rais Samia huku akisisitiza umuhimu wa kuendelea kuimarisha akiba ya Taifa.

Ameeleza kuwa mkakati wa kununua dhahabu kutoka ndani ya nchi umeiwezesha Tanzania kuongeza uwezo wa kukabiliana na misukosuko ya uchumi wa dunia huku ukiimarisha akiba ya fedha za kigeni na kuongeza uthabiti wa mfumo wa kifedha.

Katika hotuba yake, Rais Samia ameitaka Benki Kuu kuendelea kusimamia kwa karibu sekta ya fedha ili kuhakikisha mfumuko wa bei unaendelea kudhibitiwa na uchumi wa nchi unaendelea kukua kwa manufaa ya wananchi wote.

Aidha, amesisitiza umuhimu wa matumizi ya teknolojia na ubunifu wa kidijitali katika sekta ya fedha ili huduma za kifedha ziweze kuwafikia Watanzania wengi zaidi, hususan waliopo maeneo ya vijijini na pembezoni.

Katika hatua nyingine, Rais Samia ametoa maelekezo muhimu kwa Benki Kuu na taasisi za fedha nchini kutafuta njia mbadala za kuwawezesha wananchi kupata mikopo hata kama hawana dhamana za kawaida kama nyumba, viwanja au magari.

Amesema wananchi wenye biashara zinazoonekana, historia nzuri ya mauzo pamoja na rekodi za miamala wanapaswa kupewa nafasi ya kupata mikopo kwa kuzingatia kiwango chao cha uaminifu na uwezo wa kurejesha fedha.

"Tusimnyime mtu mkopo kwa sababu hana mali tulizozizoea wakati ana historia inayoonesha wazi kuwa anaaminika. Uaminifu ni mali kubwa kuliko hata mali inayoonekana," amesisitiza Rais Samia.

Kauli hiyo imepokelewa kwa matumaini makubwa na wadau wa uchumi na biashara, ikitarajiwa kufungua fursa zaidi kwa wajasiriamali wadogo na wa kati ambao mara nyingi hukosa mikopo kutokana na kutokuwa na dhamana za jadi zinazotakiwa na taasisi za fedha.

Maadhimisho ya miaka 60 ya Benki Kuu ya Tanzania yamekuwa fursa ya kutafakari mchango wa taasisi hiyo katika maendeleo ya uchumi wa Taifa huku yakifungua ukurasa mpya wa mageuzi yanayolenga kujenga mfumo wa kifedha unaojumuisha wananchi wengi zaidi na kuchochea ukuaji wa uchumi unaogusa maisha ya kila Mtanzania.

Wednesday, June 10, 2026

WAZIRI WA FEDHA: BAJETI YA 2026/27 KUIJENGA TANZANIA YA DIRA YA 2050




 Na Eva Valerian, WF, Dodoma

Serikali imesema Bajeti Kuu ya mwaka wa fedha 2026/27 ni ya kipekee kwa kuwa ndiyo bajeti ya kwanza itakayotumika kutekeleza Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, Mpango wa Nne wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano (2026/27–2030/31) pamoja na Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ya mwaka 2025.

Hayo yamesemwa na Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu mwelekeo wa Bajeti Kuu ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2026/27, katika Ukumbi wa Kambarage, Treasury Square jijini Dodoma, Bajeti ambayo itasomwa Bungeni Dodoma Siku ya Alhamisi, tarehe 11 juni 2026.

Mhe. Balozi Omar alisema kuwa, Serikali inatarajia kutumia jumla ya shilingi trilioni 62.3 katika mwaka wa fedha 2026/27, ambapo sehemu kubwa ya fedha hizo itaelekezwa katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo ya kimkakati inayochochea ukuaji wa uchumi wa Taifa.

“Fedha hizi zitaelekezwa katika kuendelea na ujenzi wa Reli ya Kisasa (SGR), kuboresha mtandao wa barabara, kuimarisha huduma za maji, kuendeleza miradi ya nishati pamoja na uwekezaji katika rasilimali watu na maendeleo ya ujuzi,” alisema Mhe. Balozi Omar. 

Aidha, alisema kuwa bajeti hiyo imeandaliwa kwa lengo la kuharakisha maendeleo ya kiuchumi na kijamii, kuongeza ajira, kuvutia uwekezaji na kuimarisha ustawi wa wananchi na Serikali inatarajia kukusanya mapato ya ndani ya shilingi trilioni 46.8 ili kugharamia sehemu kubwa ya matumizi yaliyopangwa katika bajeti hiyo.

Mhe. Balozi Omar aliongeza kuwa, kabla ya kuwasilisha makadirio ya mapato na matumizi ya mwaka 2026/27, Serikali itatoa tathmini ya utekelezaji wa Bajeti ya mwaka 2025/26, akibainisha kuwa ukusanyaji wa mapato ya ndani umeendelea kufanya vizuri na kufikia malengo yaliyowekwa. 

Aliongeza kuwa, Serikali imeendelea kushirikisha wadau mbalimbali katika mchakato wa maandalizi ya bajeti kupitia Kamati ya Wataalam wa Maboresho ya Kodi (Task Force on Tax Reforms) pamoja na Kamati ya Ushauri ya Ngazi ya Juu ya ‘Think Tank’, hatua ambayo imeongeza uwazi na ushirikishwaji katika maamuzi ya sera za kodi.

“Upande wa maboresho ya kodi, Serikali imepokea jumla ya mapendekezo 727 kutoka kwa wadau mbalimbali wakiwemo sekta binafsi, taasisi za elimu, jumuiya za wafanyabiashara, mashirika yasiyo ya kiserikali na wananchi binafsi, ambapo kati ya mapendekezo hayo, 125 yalikubaliwa kama yalivyowasilishwa, 121 yalifanyiwa maboresho na kukubaliwa, huku 295 yakikataliwa baada ya kufanyiwa uchambuzi wa kina” alisema Mhe. Balozi Omar 

Mhe Balozi Omar aliongeza kuwa, Lengo la maboresho hayo ni kukuza uchumi, kuongeza ajira, kupanua wigo wa kodi kwa kuvutia uwekezaji zaidi na wakati huo huo kupunguza mzigo wa kodi kwa walipakodi. 

Mhe. Balozi Omar, alitumia fursa hiyo kuwapongeza waandishi wa habari kwa mchango wao mkubwa katika kuhabarisha umma kuhusu masuala ya maendeleo na kusisitiza umuhimu wa wananchi kuendelea kutimiza wajibu wao wa kulipa kodi kwa hiari na kwa wakati. 

“Tunajenga Taifa letu kwa pamoja. Serikali itaendelea kuhakikisha fedha zinazokusanywa zinatumika kwa ufanisi na kuleta matokeo chanya kwa wananchi,” alisema Mhe. Balozi Omar.

Alitumia fursa hiyo kuwataka Watanzania kufuatilia kwa makini uwasilishaji rasmi wa Bajeti Kuu ya Serikali ya mwaka 2026/27 utakaofanyika Bungeni jijini Dodoma Juni 11, 2026, akisema bajeti hiyo imeandaliwa kwa kuzingatia matarajio ya wananchi na mahitaji ya maendeleo ya taifa.

MAHUNDI AIELEZA DUNIA HATUA ZA TANZANIA KATIKA KULINDA HAKI ZA WATU WENYE ULEMAVU

Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Mhe. Mhandisi Maryprisca MahundI akitoa taarifa ya nchi Mkutano wa 19 wa Nchi Wanachama wa Mkataba wa Haki za Watu Wenye Ulemavu (COSP19) unaofanyika katika Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa, Jijini New York, Marekani.




Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Mhe. Mhandisi Maryprisca Mahundi akiwa na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Wakili Amon Mpanju katika Mkutano wa 19 wa Nchi Wanachama wa Mkataba wa Haki za Watu Wenye Ulemavu (COSP19) unaofanyika katika Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa, Jijini New York, Marekani.

Baadhi ya washiriki wakiwa katika Mkutano wa 19 wa Nchi Wanachama wa Mkataba wa Haki za Watu Wenye Ulemavu (COSP19) unaofanyika katika Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa, Jijini New York, Marekani. Picha zote na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini-WMMJWM
 Mganga Mkuu wa Serikali Dkt. Grace Maghembe akiwa katika Mkutano wa 19 wa Nchi Wanachama wa Mkataba wa Haki za Watu Wenye Ulemavu (COSP19) unaofanyika katika Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa, Jijini New York, Marekani.

Na Jackline Minja, New York, Marekani

Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Mhe. Mhandisi Maryprisca Mahundi, ameieleza Jumuiya ya Kimataifa hatua kubwa zinazochukuliwa na Serikali ya Tanzania katika kulinda na kuendeleza haki za watu wenye ulemavu, wakati aliposhiriki Mkutano wa 19 wa Nchi Wanachama wa Mkataba wa Haki za Watu Wenye Ulemavu (COSP19) unaofanyika katika Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa, Jijini New York, Marekani.

Mhe. Mahundi, ambaye amemuwakilisha Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Sera, Bunge na Uratibu  na Wenye Ulemavu, Mhe. Profesa Palamagamba John Kabudi, amesema Tanzania imeendelea kuimarisha mifumo ya kisheria, kisera na kiutendaji ili kuhakikisha watu wenye ulemavu wanapata haki, fursa na huduma stahiki kama wananchi wengine.

Akiwasilisha taarifa ya nchi, Mhe. Mahundi amesema Tanzania imepiga hatua kubwa kupitia Sheria ya Watu Wenye Ulemavu Na. 9 ya mwaka 2010 kwa Tanzania Bara pamoja na Sheria Na. 8 ya mwaka 2022 ya Zanzibar, ambazo zimeweka msingi imara wa kulinda haki na ustawi wa watu wenye ulemavu.

 “Masuala ya ulemavu yamejumuishwa katika Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 na mipango mbalimbali ya maendeleo ili kuhakikisha hakuna anayebaki nyuma katika safari ya maendeleo ya taifa na kusema kuwa Serikali imeendelea kupanua upatikanaji wa elimu jumuishi, huduma za afya, huduma za urekebishaji na tiba, teknolojia saidizi, programu za uwezeshaji kiuchumi pamoja na huduma za hifadhi ya jamii kwa watu wenye ulemavu” amesema Mhe. Mahundi

Aidha  Mhe. Mahundi amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa uongozi wake madhubuti na dhamira ya dhati ya kuhakikisha watu wenye ulemavu wanapata huduma bora na fursa zinazowawezesha kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya nchi.

“Serikali ya Tanzania itaendelea kushirikiana na nchi wanachama, Umoja wa Mataifa, asasi za kiraia na watu wenye ulemavu wenyewe katika kuharakisha utekelezaji wa Mkataba wa Haki za Watu Wenye Ulemavu na kujenga jamii jumuishi inayoheshimu usawa, utu na haki za kila mtu,” amesema Mhe. Mahundi

Mkutano huo wa 19 wa Nchi Wanachama wa Mkataba wa Haki za Watu Wenye Ulemavu umebeba kaulimbiu inayosema “CRPD at 20: Celebrating and Consolidating Achievements and Shaping the Next Phase of Implementation in a Changing World,” ukilenga kutathmini mafanikio yaliyopatikana katika kipindi cha miaka 20 tangu kuanzishwa kwa mkataba huo na kuweka mikakati ya kuendeleza utekelezaji wake duniani. 




Friday, June 05, 2026

KIPANGULA: WAHITIMU WA HABARI WATAFAIDIKA NA MABORESHO YA KANUNI





 Na Mwandishi Wetu

Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB), Wakili Patrick Kipangula, amewashauri Waandishi wa Habari nchini kuipa thamani na heshima taaluma ya habari kwa kuzingatia nadhifu ya mavazi na mienendo yao wanapotekeleza majukumu ya kitaaluma.

Wakili Kipangula ametoa ushauri huo leo Juni 5, 2026 wakati akiwasilisha mada kuhusu “Uhuru wa Vyombo vya Habari katika Enzi ya Kidijiti: Wajibu wa Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari” kwenye Kongamano la Uhuru wa Vyombo vya Habari lililoandaliwa na Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) kupitia Idara ya Sanaa na Taaluma za Habari.

Amesema uandishi wa habari ni taaluma muhimu inayotambulika kama muhimili wa nne usio rasmi katika jamii, hivyo ni wajibu wa waandishi wenyewe kuhakikisha wanaijengea heshima kupitia mwenendo, maadili na namna wanavyojiwasilisha mbele ya jamii.

Wakili Kipangula amesema mwonekano wa mwandishi wa habari unaweza kuwa sehemu ya kujenga imani kwa jamii na vyanzo vya habari vinavyotoa taarifa mbalimbali kwa vyombo vya habari.

“Kwa hiyo hata mtu unavyoenda kumhoji mtu akikuona jinsi ulivyo anajua huyu mtu ataeleza kitu cha msingi na huyu mtu anaeleweka na ni wa maana,” amesema Wakili Kipangula.

Amesisitiza kuwa pamoja na kuzingatia maadili, sheria na weledi katika ukusanyaji na uchakataji wa habari, Waandishi wa Habari wanapaswa kutambua kuwa taswira wanayoijenga mbele ya jamii ni sehemu muhimu ya kuimarisha hadhi ya taaluma hiyo na kuongeza imani ya wananchi kwa vyombo vya habari.

MAMA NEEMA MWIGULU AHIMIZA TAASISI KUUNGA MKONO JUHUDI ZA SERIKALI KUPITIA UWAJIBIKAJI KWA JAMII

Mwenza wa Waziri Mkuu, Mama Neema Mwigulu Nchemba, amehimiza taasisi za umma na binafsi kuendelea kuunga mkono juhudi za Serikali katika kub...