Monday, February 16, 2026

DKT. POSSI: VIONGOZI NI TASWIRA YA TAASISI NA SERIKALI KWA JAMII


Bi. Alice Mtulo, Naibu Wakili Mkuu wa Serikali akizungumza na Menejimenti ya Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali wakati wa kikao cha faragha kilichofanyika jijini Dodoma.
Ndugu Kadari Singo, Mtendaji Mkuu wa Taasisi ya Uongozi akitoa mada kuhusu Ugawaji wa Majukumu na Usimamizi wa Muda kwa wajumbe wa Menejimenti ya Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali wakati wa kikao cha faragha kilichofanyika jijini 

Ndugu Camilius Ruhinda, Mkurugenzi wa Idara ya Usimamizi wa Mashauri na Udhibiti Ubora wa Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali akizungumza wakati wa kikao cha faragha kwa wajumbe wa menejimenti ya Ofisi hiyo kilichofanyika jijini Dodoma
Ndugu Godwin Gonde, Mhadhiri wa Chuo cha Diplomasia akitoa mada kuhusu Kanuni za Msingi za Itifaki na Maadili kwa Viongozi wakati wa kikao cha faragha kwa wajumbe wa Menejimenti ya Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali kilichofanyika jijini Dodoma.


Dkt. Ally Possi, Wakili Mkuu wa Serikali (aliyesimama katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na wakufunzi baada ya kufungua kikao cha faragha kwa wajumbe wa Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali kilichofanyika jijini Dodoma.
Bi. Alice Mtulo, Naibu Wakili Mkuu wa Serikali (aliyesimama katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na wakufunzi baada ya ufunguzi wa kikao cha faragha kwa wajumbe wa Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali kilichofanyika jijini Dodoma.

Baadhi ya wajumbe wa Menejimenti ya Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali wakichangia mada kuhusu Ugawaji wa Majukumu na Usimamizi wa Muda wakati wa kikao cha faragha kwa viongozi hao kilichofanyika jijini Dodoma.

Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali imeendesha mafunzo kwa viongozi wa taasisi hiyo na menejimenti yake ambayo yamefanyika jijini Dodoma mwishoni mwa wiki ambapo pamoja na mafunzo hayo viongozi hao wamejitathmini utendaji kazi wao wa kila siku, wamepatiwa mafunzo ya uongozi ikiwemo usimamizi na mgawanyo wa majukumu, usimamizi wa muda, itifaki na ustaarabu.

Wakili Mkuu wa Serikali, Dkt. Ally Possi alifungua mafunzo hayo na kuwaeleza wajumbe wa menejimenti ya Ofisi hiyo kuwa viongozi ni taswira ya taasisi na Serikali kwa ujumla ambapo amewaeleza kuwa kiongozi yeyote awe Mkuu wa Idara au Mkuu wa Kitengo atambue kuwa anabeba taswira ya taasisi anayofanyia kazi na Serikali kwa ujumla popote alipo, iwe kazi au unapoishi, hivyo ni muhimu kuzingatia sheria, taratibu, kanuni, maadili ya uongozi, mila na desturi za uongozi.

“Kila mmoja ajitambue wadhifa alionao na bendera anayopeperusha kwa niaba ya Serikali na kwa wale tunaowaongoza. Tuwe walezi kwa kuzingatia kuwa muda mwingi tupo mahali pa kazi kuliko familia zetu, watu tunaofanya nao kazi wafurahie kufanya kazi na wewe badala ya kukasirika, tujitathmini na kutafakari utendaji kazi wetu ili kuwa na matokeo mazuri mahali pa kazi na kujipa muda wa kujisahihisha huku tukifanya kazi kwa kuzingatia sheria, taratibu na kanuni, tuwe wabunifu na tufanye ufuatiliaji wa majukumu,” amesisitiza Dkt. Possi.

Naye Naibu Wakili Mkuu wa Serikali, Bi. Alice Mtulo amesema kuwa kikao hicho cha faragha na mafunzo hayo ni muhimu kwa wajumbe wa menejimenti wa Ofisi hiyo ili kupata muda wa kutathmini utendaji kazi na ana amini kuwa mafunzo hayo yataleta mabadiliko katika taasisi, kuwawezesha kuwafahamu na kuwasimamia vizuri wasaidizi wao, kumiliki kazi zao, kufanya maamuzi kwa wakati na kuzingatia muda katika utekelezaji wa majukumu.

Akitoa mada kuhusu uongozi na mgawanyo wa majukumu kwa wajumbe hao, Afisa Mtendaji Mkuu wa Taasisi ya Uongozi, ndugu Kadari Singo, amewapongeza viongozi wa Ofisi hiyo kwa kuandaa na kushiriki mafunzo hayo na ametoa rai kwao kujenga utaratibu wa kuwajenga wasaidizi wao ili wanapoondoka kwenye nafasi zao wawe na watu wa kuhakikisha mifumo inafanya kazi.

Aidha, Mhadhiri wa Chuo cha Diplomasia, ndugu Godwin Gonde Amani, aliwafundisha wajumbe wa menejimenti hiyo mada kuhusu itifaki na ustaarabu ambayo ilijikita kwenye masuala ya muonekano wa mtu, mavazi, mawasiliano, tabia, mienendo, matumizi ya akili ya kuzaliwa, kuheshimu mamlaka na madaraka ya kiongozi, kutambua, kujali na kuthamini uwepo wa kiongozi.

“Iitifaki ni jambo muhimu Serikalini na katika uongozi kwa kuwa ni jambo nyeti lina athari chanya na hasi baina yako binafsi na mtu mwingine katika muonekano wa mavazi, salamu, mazungumzo na mawasiliano,” amesisitiza Mhadhiri Amani.

Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali imekuwa na utaratibu wa kuendesha mafunzo kwa viongozi wa Ofisi hiyo, kufanya kikao cha faragha kwa ajili ya kutathmini utendaji kazi na utekelezaji wa majukumu mara moja kwa mwaka.

Sunday, February 15, 2026

SERIKALI KUONGEZA NGUVU KUPAMBANA NA WANYAMAPORI WAKALI TANGA








Na Sixmund Begashe, Tanga

Wizara ya Maliasili na Utalii inaendelea kutumia mbinu na teknolojia mbalimbali za kupambana na Wanyamapori wakali na waharibifu sambamba na kufungua fursa za uhifadhi na Utalii kupitia sekta za Maliasili na Utalii, kwa Watanzania ikiwemo Wilaya ya Mkinga iliyoko Mkoa wa Tanga. 

Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji (Mb), ameyasema hayo kwenye Mkutano wa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Mwigulu Lameki Nchemba (Mb) na Wananchi wa Mkinga katika hafla ya uwekaji jiwe la msingi chuo Kikuu Mzumbe tawi la Tanga.

Dkt. Kijaji amesema kuwa, ni dhamira ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe.Dkt. Samia Suluhu Hassan ambaye ndiye Mhifadhi namba moja nchini,  kuhakikisha wananchi wananufaika na uhifadhi wakiwa salama na wenye furaha. 

"Vituo vya Askari wa kuzuia Wanyamapori wakali na waharibifu (PAC) vitajengwa  katika eneo la vijiji vya Mwanyumba na Mavovo Wilayani Mkinga kwa sababu ndio eneo lenye changamoto kubwa ya tembo kwani ni mapito ya tembo kuelekea misitu ya mtoni bombo". Alisema Dkt. Kijaji.

Akizungumza kwa niaba ya wanamkinga, Mbunge wa Jimbo la Mkinga Mhe.Twaha Mwakihoja (Mb) ameipongeza Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kazi kubwa ya uhifadhi na mapambano dhidi ya Wanyamapori wakali na waharibifu, nakuomba juhudi hizo ziongezeke zaidi sambamba na kufungua fursa zaidi ya kiuchumi kwa wananchi kupitia swkta ya Utalii.

Dkt. Kijaji yupo Mkoani Tanga, kwenye ziara ya kikazi ya  Waziri Mkuu Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba, pamoja naye ameambatana na baadhi ya wajumbe wa  Menejimenti ya Wizara hiyo, pamoja na wataalam mbalimbali.

JAB YAJIPANGA KUENDELEA KUTOA MAFUNZO KWA WAANDISHI, WAMILIKI WA VYOMBO VYA HABARI




Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) imejipanga kuendelea kutoa mafunzo kwa waandishi wa habari pamoja na wamiliki wa vyombo vya habari ili kuongeza uelewa wa sheria, maadili ya taaluma na umuhimu wa ithibati katika utendaji kazi wa kila siku.

Sambamba na hilo, Bodi imebainisha haja ya kufanya mapitio ya haraka ya Sera na Sheria ya Huduma za Habari nchini ili kuendana na kasi kubwa ya mabadiliko ya teknolojia ya kidijitali.

Hatua hiyo inalenga kuhakikisha kuwa sheria hiyo, iliyotungwa mwaka 2016 kabla ya ukuaji wa sasa wa mitandao ya kijamii, inatoa tafsiri pana itakayowawezesha bloga na watengeneza maudhui ya mtandaoni kutambulika na kusimamiwa kisheria.

Kutokana na mazingira ya sasa, JAB inaona kuna umuhimu wa kufanya mapitio hayo ili kuyaingiza katika mfumo makundi hayo mapya yanayochipukia kwa kasi katika tasnia ya habari.

Katika wasilisho lililotolewa na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa JAB, Wakili Patrick Kipangula, katika mkutano wa mwaka wa utangazaji 2026 jijini Dodoma, imeelezwa kuwa mfumo rasmi wa ithibati umewekwa kwa mujibu wa Sheria ya Huduma za Habari, Sura ya 229, kwa lengo la kulinda maslahi ya umma na kuimarisha maadili ya kitaaluma.

Kwa sasa, JAB inasimamia utambuzi wa wataalamu wa habari kupitia mfumo wa kidijitali wa TAI-HABARI, ambapo waandishi waliokidhi vigezo hupatiwa vitambulisho (Press Cards) vyenye uhalali wa miaka miwili. Hadi kufikia Januari 2026, takwimu zinaonyesha kuwa zaidi ya maombi 3,200 yameidhinishwa, huku maombi mengine yakiendelea kufanyiwa kazi.

Licha ya mafanikio hayo, Bodi imetaja kuwepo kwa changamoto ya mtazamo hasi miongoni mwa baadhi ya wadau ambao wanaiona ithibati kama chombo cha kudhibiti badala ya nyenzo ya kuimarisha ubora wa uandishi.

Aidha, uelewa mdogo wa sheria umekuwa ukisababisha baadhi ya waandishi kuwasilisha maombi yasiyokidhi vigezo vya kitaaluma, ikiwemo hitaji la kuwa na angalau Stashahada au Shahada ya Uandishi wa Habari. JAB imesisitiza kuwa mwandishi asiye na ithibati hukosa uhalali wa kisheria na anaweza kuchukuliwa hatua kali, huku ikionya kuwa hali hiyo inadhoofisha uaminifu wa habari nchini.

Wakili Kipangula amesema kuwa Bodi itaendelea kushirikiana na mamlaka nyingine ikiwemo Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) pamoja na taasisi za elimu, kuhakikisha ithibati inatumika kama nyenzo ya kumlinda mwandishi katika utekelezaji wa majukumu yake, kumpatia ulinzi wa kitaaluma dhidi ya vitisho, na kuhakikisha jamii inapata habari sahihi na za kweli.

RAIS DKT. SAMIA REJEA TANZANIA BAADA YA KUSHIRIKI MKUTANO WA AU ETHIOPIA

 









Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, leo tarehe 15 Februari 2026 ameondoka katika Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Bole, jijini Addis Ababa, kurejea nchini baada ya kukamilisha ziara ya kikazi ya siku nne nchini Ethiopia. 

Katika ziara hiyo, Rais Dkt. Samia alishiriki Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Umoja wa Afrika (AU) uliofanyika tarehe 14 na 15 Februari 2026, mkutano uliowakutanisha viongozi wa bara la Afrika kujadili masuala ya amani, usalama, maendeleo ya uchumi na ushirikiano wa kikanda. 

Ushiriki wa Tanzania katika mkutano huo umeendelea kudhihirisha nafasi ya nchi katika diplomasia ya kimataifa na mchango wake katika ajenda za pamoja za bara la Afrika, hususan katika kuimarisha mshikamano, biashara baina ya nchi za Afrika na utekelezaji wa miradi ya kimkakati ya maendeleo. 

Baada ya kuondoka Addis Ababa, Rais Dkt. Samia aliwasili katika Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Abeid Amani Karume, Zanzibar, ambako alipokelewa na viongozi mbalimbali wa Serikali na Chama. Mapokezi hayo yaliashiria hitimisho la ziara yenye umuhimu wa kidiplomasia na kiuchumi kwa Taifa.

 Ziara hiyo ya siku nne imeimarisha mahusiano ya Tanzania na Ethiopia pamoja na nchi nyingine wanachama wa AU, huku ikiendeleza msimamo wa Tanzania katika kushiriki kikamilifu mijadala na maamuzi yanayolenga ustawi wa bara la Afrika. 

Kwa ujumla, ushiriki wa Rais Dkt. Samia katika Mkutano wa AU na ziara yake nchini Ethiopia umeendelea kuweka Tanzania katika nafasi thabiti ya uongozi na ushirikiano wa kikanda na kimataifa.      #RaisSamia #Tanzania #AU2026 #DiplomasiaYaAfrika #MahusianoYaKikanda #MaendeleoYaAfrika

KIWANDA CHA NGUZO ZA ZEGE TCPM – TABORA CHA SERIKALI SIO TISHIO KWA SEKTA BINAFSI: NDEJEMBI








Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi amesema ujenzi wa Kiwanda cha Kutengeneza Nguzo za Zege cha TCPM Tabora kinachomilikiwa na Shirika la Umeme Tanzania - TANESCO kupitia kampuni tanzu ya TCPM haukusudii kuathiri wala kudhoofisha uwekezaji wa sekta binafsi bali unaongeza uzalishaji wa nguzo za zege ili kukidhi mahitaji yaliyopo ambayo bado hayajatosheleza uhitaji wa nguzo hizo nchini.

Ameeleza hayo Februari 15, 2026 wakati akikagua mradi wa ujenzi wa Kiwanda cha Kutengeneza Nguzo za Zege cha TCPM Tabora, ambao umefikia asilimia 95 ya utekelezaji. Kiwanda hicho kitakuwa na uwezo wa kuzalisha wastani wa nguzo za zege 120 kwa siku.

“Kiwanda hiki si tishio kwa sekta binafsi; kinakuja kuongeza nguvu katika kazi ambazo tayari zilikuwa zinafanywa na sekta binafsi ya kuzalisha nguzo za zege,” amesema Ndejembi.

Ndejembi amefafanua kuwa TANESCO kwa mwaka 2025 ilikuwa na uhitaji wa nguzo za zege 80,000, lakini zilizopatikana kupitia sekta binafsi ni nguzo 40,000 jambo lililosababisha kutokufikiwa kwa malengo ya mahitaji hayo.

Ameeleza kuwa pamoja na Serikali kujenga kiwanda hicho, bado kuna fursa kwa sekta binafsi kuwekeza katika viwanda vya nguzo za umeme kutokana na mpango wa TANESCO wa kuendelea kufanya maboresho kwa kuondoa nguzo za miti na kutumia nguzo za zege katika usambazaji wa umeme nchini.

Aidha, Ndejembi ameitaka Bodi na Menejimenti ya TANESCO kusimamia kikamilifu ukamilishaji wa kiwanda hicho ili mitambo itakapowashwa iweze kufanya kazi kwa ufanisi na ubora kulingana na mpango na malengo ya Kiwanda hicho.

Kadhalika, amewataka wafanyakazi waliopata ajira na watakaoajiriwa kutunza miundombinu na mitambo ya kiwanda hicho pamoja na kuweka mpango madhubuti na endelevu wa uendeshaji ili kuepusha hasara zinazoweza kujitokeza.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO, Lazaro Twange amesema utekelezaji wa mradi wa kiwanda hicho cha nguzo za zege, kinachomilikiwa na Serikali kwa asilimia 100, hadi kukamilika kwake utagharimu Shilingi bilioni 7.9.

Twange ameeleza kuwa ujenzi wa kiwanda hicho upo katika hatua za mwisho za ukamilishaji, ambapo kufikia tarehe 20 Februari 2026 mkandarasi atakuwa amekamilisha kazi zote, tayari kwa kuanza uzalishaji.

RAIS SAMIA AKUTANA NA NAIBU KATIBU MKUU WA UMOJA WA MATAIFA ADDIS ABABA, ATOA MSUKUMO DIPLOMASIA YA MAENDELEO



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, amekutana na kufanya mazungumzo na Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Bi. Amina Mohammed, tarehe 15 Februari 2026 jijini Addis Ababa, Ethiopia.

Katika mazungumzo hayo, viongozi hao walijadili masuala ya ushirikiano kati ya Tanzania na Umoja wa Mataifa, hususan katika maeneo ya maendeleo endelevu, uwekezaji katika rasilimali watu, mabadiliko ya tabianchi, pamoja na juhudi za kukuza amani na utulivu barani Afrika. Rais Dkt. Samia alisisitiza dhamira ya Tanzania kuendelea kushirikiana kwa karibu na taasisi za kimataifa katika kufanikisha Ajenda ya Maendeleo Endelevu ya 2030, sambamba na vipaumbele vya kitaifa vinavyolenga ustawi wa wananchi.

Kwa upande wake, Bi. Amina Mohammed alieleza utayari wa Umoja wa Mataifa kuendeleza ushirikiano na Tanzania katika miradi ya kimkakati inayogusa sekta za afya, elimu, nishati safi na uwezeshaji wa wanawake na vijana kiuchumi.

Rais Dkt. Samia yupo nchini Ethiopia kwa ziara ya kikazi ya siku nne, ambapo pamoja na shughuli nyingine, alishiriki Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Umoja wa Afrika (AU) uliofanyika tarehe 14 na 15 Februari 2026. Mkutano huo umejadili ajenda pana za maendeleo ya bara, ikiwemo kuimarisha biashara ya ndani ya Afrika, usalama wa chakula na mageuzi ya kiuchumi.

Ziara hiyo inaendelea kudhihirisha nafasi ya Tanzania katika majukwaa ya kimataifa na kikanda, huku Rais Samia akiendeleza diplomasia ya uchumi na maendeleo kwa manufaa ya Taifa.

Saturday, February 14, 2026

RAIS SAMIA AONGOZA MJADALA WA MAJI NA MAENDELEO AFRIKA, AKUTANA NA WAZIRI MKUU WA ETHIOPIA ADDIS ABABA

 











Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, ameendeleza diplomasia ya kimkakati kwa kushiriki Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Umoja wa Afrika unaofanyika jijini Addis Ababa tarehe 14 Februari, 2026, sambamba na kufanya mazungumzo ya kando na Waziri Mkuu wa Ethiopia, Mheshimiwa Abiy Ahmed.

Katika mazungumzo hayo ya pembezoni mwa mkutano, viongozi hao wamejadili kuimarisha ushirikiano wa pande mbili katika sekta za maji, nishati, miundombinu na biashara, wakitambua umuhimu wa rasilimali maji kama mhimili wa maendeleo ya kiuchumi na ustawi wa jamii. Tanzania na Ethiopia zimeonesha utayari wa kuendeleza ushirikiano wa kiufundi na kubadilishana uzoefu katika usimamizi wa rasilimali maji, hasa katika kukabiliana na changamoto za mabadiliko ya tabianchi.

Mkutano wa mwaka huu unaongozwa na kaulimbiu isemayo: “Kuhakikisha Upatikanaji Endelevu wa Maji na Huduma Salama za Usafi wa Mazingira ili Kufikia Malengo ya Ajenda 2063.” Kaulimbiu hiyo inaakisi dhamira ya bara la Afrika ya kuweka kipaumbele katika usalama wa maji, afya ya umma na ujenzi wa mifumo himilivu ya huduma za kijamii kwa mujibu wa dira ya maendeleo ya muda mrefu ya Afrika, Ajenda 2063.

Akichangia katika mjadala wa wakuu wa nchi, Rais Samia amesisitiza umuhimu wa uwekezaji katika miundombinu ya maji safi na usafi wa mazingira, akieleza kuwa upatikanaji wa maji salama si suala la kijamii pekee bali ni kichocheo cha uzalishaji, viwanda, kilimo na maendeleo ya rasilimali watu. Amehimiza nchi wanachama kuimarisha ushirikiano wa kikanda katika usimamizi wa vyanzo vya maji vinavyovuka mipaka, ili kuhakikisha matumizi endelevu na yenye manufaa kwa kizazi cha sasa na kijacho.

Ushiriki wa Tanzania katika mkutano huo unaonesha msimamo wake wa kuendelea kuwa mdau hai katika ajenda za maendeleo za bara, huku ikiunganisha diplomasia ya kimataifa na vipaumbele vya ndani vya kuboresha huduma za maji na usafi wa mazingira kwa wananchi.

Kwa hatua hiyo, Tanzania inaendelea kujenga taswira ya taifa linalochangia kikamilifu katika majadiliano ya kimkakati ya bara, likisisitiza mshikamano, uwajibikaji na utekelezaji wa pamoja katika kufanikisha malengo ya Ajenda 2063.

DKT. POSSI: VIONGOZI NI TASWIRA YA TAASISI NA SERIKALI KWA JAMII

Bi. Alice Mtulo, Naibu Wakili Mkuu wa Serikali akizungumza na Menejimenti ya Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali wakati wa kikao cha faragha ki...