
Na. Meleka Kulwa- Fullshangwe Blog, Dodoma
Waziri
wa Madini, Mhe. Anthony Mavunde, amesema kuwa Serikali inaendelea
kuonesha dhamira ya dhati ya kuifanya sekta ya madini kuwa injini muhimu
ya kukuza uchumi wa Taifa kwa kuwekeza zaidi katika mnyororo wa thamani
wa madini mkakati na kuhamasisha uwekezaji katika uongezaji thamani.
Ameyabainisha
hayo Aprili 27, 2026 Jijini Dodoma, wakati akiwasilisha bajeti ya
Wizara kwa mwaka wa fedha 2026/2027, amesema kuwa madini mkakati
yakiwemo lithium, graphite, nickel, cobalt na rare earth elements yana
nafasi kubwa katika maendeleo ya teknolojia za kisasa hususan nishati
safi. Aidha amebainisha kuwa mwelekeo wa dunia kutumia teknolojia rafiki
kwa mazingira unaongeza mahitaji na thamani ya madini hayo katika soko
la kimataifa.
Pia
ameongeza kuwa Serikali imejipanga kuimarisha uwekezaji katika utafutaji
na uchimbaji wa madini hayo ili kuongeza uzalishaji pamoja na mapato ya
Taifa. Amesema kuwa tafiti za masoko mapya zitafanyika ili kupanua wigo
wa biashara huku taratibu za utoaji leseni zikirahisishwa kwa
wawekezaji.
Amesema
kuwa lengo kuu ni kuhakikisha Watanzania wananufaika moja kwa moja
kupitia ajira, mapato na maendeleo ya viwanda vinavyotokana na
rasilimali hizo.
Aidha
amebainisha kuwa Serikali imeweka mkakati wa kuhamasisha ujenzi wa
viwanda vya uchenjuaji, uyeyushaji na usafishaji wa madini ili kuongeza
thamani kabla ya kusafirishwa nje ya nchi. Amesema hatua hiyo inalenga
kupunguza usafirishaji wa madini ghafi na kuongeza mapato kupitia bidhaa
zilizoboreshwa.
Pia
ameongeza kuwa eneo la Buzwagi wilayani Kahama limetengwa kwa ajili ya
uwekezaji wa viwanda vya kuongeza thamani madini, hatua inayotarajiwa
kuvutia wawekezaji na kuongeza ajira kwa wananchi.
Aidha
amebainisha kuwa Serikali inaendelea kushirikiana na wadau kuhakikisha
viwanda vya usafishaji wa dhahabu vinapata ithibati ya kimataifa ili
kuongeza ushindani wa bidhaa za Tanzania katika soko la dunia.
Amesema
kuwa Tanzania inatarajia kuandaa mkutano wa saba wa kimataifa wa
uwekezaji katika sekta ya madini utakaofanyika Dar es Salaam mwezi
Novemba 2026, ambapo wadau mbalimbali watakutana kujadili fursa na
changamoto za sekta hiyo.
Kwa
upande wa utekelezaji wa bajeti ya mwaka 2025/2026, amesema kuwa Wizara
imepiga hatua kubwa ikiwemo kuvuka malengo ya ukusanyaji wa mapato na
kuimarisha usimamizi wa rasilimali madini.
Aidha
amebainisha kuwa Bunge liliidhinisha shilingi bilioni 224.98 kwa ajili
ya Wizara, ambapo kati ya hizo shilingi bilioni 100.38 zilitengwa kwa
matumizi ya kawaida na shilingi bilioni 124.60 kwa miradi ya maendeleo.
Amesema kuwa hadi Machi 2026, Wizara ilikuwa imepokea shilingi bilioni
82.90.
Pia ameongeza
kuwa katika ukusanyaji wa maduhuli, Wizara ilipangiwa kukusanya shilingi
trilioni 1.41 lakini hadi Machi 2026 tayari ilikuwa imekusanya shilingi
trilioni 1.03, sawa na asilimia 114.94 ya lengo la kipindi husika.
Amesema
kuwa mafanikio hayo yametokana na kuimarishwa kwa ukaguzi katika maeneo
ya uchimbaji, masoko ya madini, vituo vya ununuzi pamoja na mipaka ya
nchi ili kudhibiti upotevu wa mapato.
Aidha
amebainisha kuwa thamani ya biashara ya madini imeongezeka na kufikia
shilingi trilioni 4.90 katika kipindi cha Julai 2025 hadi Machi 2026
ikilinganishwa na shilingi trilioni 2.82 kwa kipindi kama hicho mwaka
uliopita.
Pia
ameongeza kuwa Serikali imeendelea kudhibiti utoroshaji wa madini ambapo
madini yenye thamani ya shilingi bilioni 3.31 yalikamatwa katika
matukio 55 na wahusika kuchukuliwa hatua za kisheria.
Amesema
kuwa mapato ya fedha za kigeni yameongezeka ambapo mauzo ya madini nje
ya nchi yalifikia dola milioni 5,401.9 mwaka 2025 kutoka dola milioni
4,119.9 mwaka 2024.
Aidha
amebainisha kuwa mchango wa sekta ya madini katika Pato la Taifa
umeongezeka kutoka asilimia 9.1 mwaka 2023 hadi asilimia 10.1 mwaka 2024
na kufikia wastani wa asilimia 11.9 katika robo tatu za mwaka 2025