Friday, February 20, 2026

Oryx Gas Waja na Promosheni Maalum ya Mfungo

 

NA MWANDISHI WETU, DAR ES SALAAM


KATIKA kuendelea kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia, Kampuni ya Oryx Gas imezindua kampeni ya msimu wa mwezi wa Ramadhan na Kwaresma inayoitwa Pishi la Kibabe ikiwa ni sehemu pia kurejesha shukrani kwa wateja wao.

Akizungumza leo Februari 20,2026 jijini Dar es Salaam wakati wa uzinduzi huo Meneja Masoko na Mauzo wa Oryx Gas Tanzania Shaban Fundi amesema huu ni mwezi wa kujitafakari ,kushirikiana ,kujitolea na zaidi ya yote kuunganisha watu wote.

“Ili kuunga mkono wateja wetu katika kipindi hiki maalum tunatoa bei ya promosheni kwenye mitungi yetu mipya ya kilo sita itauzwa kwa Sh.37000 nchi nzima hadi Zanzibar.”amesema Fundi

Pia amesema mbali ya kupunguza bei katika kipindi hiki cha Ramadhan na Kwaresma wateja wao watakaonunua au kujaza gesi kwenye maduka maalum ya Oryx na Mangi Shop watapokea zawadi ya futari papo kama ishara ya shukrani yao kwao.

Akizungumza kuhusu gharama za mtungi wa kilo sita amesema mpaka unafika nchini Tanzania gharama yake haipungui Sh.80,000 lakini Oryx katika soko mtungi huo unapatikana kwa Sh.40000 na kwa sasa tumetoa promosheni mpaka Sh.37000.

“Oryx Gas tunashusha bei kwa ajili ya kuiwezesha jamii iweze kutumia nishati safi ya kupikia.Pia tunaishukuru Serikali kwa mfano sasa hivi tunamsamaha wa kodi katika mitungi pamoja na jitihada nyingine wanazochukua.

-“Hata hivyo tunaomba Serikali iendelee kuangalia katika maeneo mengine ili kuhakikisha kwamba gesi pamoja na mtungi bei yake inakuwa chini ili wananchi waweze kupata kwa bei nafuu.Kwafanya hivyo Oryx Gas kwa kushirikiana na Serikali tunaweza kufanikisha matumizi ya nishati safi kwa wananchi wengi zaidi.”

“Kuhusu gharama ukilinganisha mkaa na kuni bei yake iko juu zaidi ya nishati safi ya kupikia kwani kwa familia ya kawaida kwa siku moja inatumia kopo moja la mkaa ambalo linauzwa Sh.2000 hivyo kwa mwezi ni Sh.60,000 wakati mtungi wa gesi ya oryx wa kilo 6 ni Sh.40,000.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa Oryx Gas Tanzania Benoit Araman amesema lengo la kampeni iliyozinduliwa kwa ajili ya Mfungo wa Mwezi wq Ramadhan na Kwaresma ni muendelezo wa kuhamasisha matumizi ya nishati safi nchini ikiwa ni kuunga mkono juhudi za Serikali za kuhimiza wananchi kutumia nishati safi ya kupikia.

“Oryx Gas lengo letu kubwa ni kuendelea kuhamasisha nishati safi ya kupikia na mimi na timu yangu tumejipanga vema kuhakikisha tunaendelea kufanya kampeni za kuwezesha wananchi kutumia nishati safi ya kupikia.Wakati huu wa Ramadhan na Kwaresma tunawatakia mfungo mwema lakini wakati huo huo tukihamasisha matumizi ya nishati safi.”

Wakati huo huo Mkuu wa Idara ya Mauzo ya Gesi kwa Ujumla Carloline Msokwa amesema kipindi hiki Waislamu na Wakristo wanaungana pamoja kuomba toba na ni kipindi ambacho familia zinakaa kufanya ibada na kuomba toba lakini pia ni wakati wa kupika chakula kizuri kwa ajili ya kufuturu.

“Kwahiyo Oryx Gas tumekuja na kampeni ya Pishi la kibabe ambapo familia zitakaa na kupika pamoja lakini pia Oryx tumetoa punguzo la bei ili kuwezesha wananchi kutumia gesi.Pia nitoe rai huu ni wakati wa Watanzania kuwa wamoja na tuliombee taifa letu.”





Thursday, February 19, 2026

UHUSIANO WA TANZANIA NA KOREA KUSINI WAZIDI KUIMARIKA

 Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha, Dkt. Natu El-Maamry Mwamba akiagana na Balozi wa Korea Kusini nchini Tanzania, Mhe. Eunje Ahn, baada ya mkutano kati yao kuhusu ushirikiano wa maendeleo, uliofanyika Ofisi Ndogo za Wizara ya Fedha, Jijini Dar es Salaam.

Balozi wa Korea Kusini nchini Tanzania, Mhe. Eunje Ahn, akiongoza ujumbe wa Korea Kusini katika kikao chake na Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha, Dkt. Natu El-Maamry Mwamba (hayupo pichani), kilichofanyika katika Ofisi Ndogo za Wizara ya Fedha,  Jijini Dar es Salaam. (Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini Wizara ya Fedha)
Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha, Dkt. Natu El-Maamry Mwamba, akiongoza ujumbe wa Tanzania katika kikao chake na Balozi wa Korea Kusini nchini Tanzania, Mhe. Eunje Ahn (hayupo pichani), kushoto ni Naibu Katibu Mkuu, Wizara ya Fedha, Bi. Amina Khamis Shaaban na kulia ni Kamishna Msaidizi, Idara ya Fedha za Nje, Wizara ya Fedha, Bw. Melckzedeck Mbise, kilichofanyika Ofisi Ndogo za Wizara ya Fedha, Jijini Dar es Salaam.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha, Dkt. Natu El-Maamry Mwamba akiongoza kikao kati yake na Balozi wa Korea Kusini nchini, Mhe. Eunje Ahn, kuhusu kuimarisha ushirikiano wa maendeleo kati ya mataifa hayo mawili, kilichofanyika Ofisi Ndogo za Wizara ya Fedha,  Jijini Dar es Salaam.

Balozi wa Korea Kusini nchini Tanzania, Mhe. Eunje Ahn, akiahidi kuendeleza ushirikiano wa kimkakati katika nyanja za maendeleo, wakati wa kikao na Katibu Mkuu Wizara ya Fedha, Dkt. Natu El-Maamry Mwamba, kilichofanyika Ofisi Ndogo za Wizara ya Fedha, Jijini Dar es Salaam.
Katibu Mkuu Wizara ya Fedha, Dkt. Natu El-Maamry Mwamba, akiipongeza Korea Kusini kwa mchango wake katika sekta za maendeleo nchini, wakati wa kikao na Balozi wa Korea Kusini nchini, Mhe. Eunje Ahn,  kilichofanyika Ofisi Ndogo za Wizara ya Fedha, Jijini Dar es Salaam.
………..

Na. Josephine Majura na Peter Haule, WF, Dar es Salaam

Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha, Dkt. Natu El-Maamry Mwamba, amesema kuwa Serikali ya Tanzania inatambua na kuthamini mchango mkubwa wa Korea Kusini katika sekta mbalimbali, kupitia nafasi yake kama mshirika wa maendeleo na rafiki wa karibu.

Dkt. Mwamba amesema hayo alipokutana na kufanya mazungumzo na Balozi wa Korea Kusini nchini Tanzania, Mhe. Eunje Ahn, katika Ofisi Ndogo za Wizara ya Fedha, Jjini Dar es Salaam, ambapo  mazungumzo hayo yalihusu namna ya kuendeleza na kuimarisha ushirikiano wa maendeleo kati ya mataifa hayo mawili.

Aidha, aliishukuru Serikali ya Korea Kusini kwa msaada wa kifedha kupitia mikopo nafuu na ruzuku, ambazo zimekuwa chachu ya utekelezaji wa miradi ya miundombinu na maendeleo nchini.

Katika mazungumzo hayo, Dkt. Mwamba pia alitoa salamu kutoka kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, akisisitiza dhamira ya Serikali ya Tanzania ya kuimarisha zaidi ushirikiano wa pande mbili kwa manufaa ya wananchi wa mataifa haya mawili.

Kwa upande wake, Balozi wa Korea Kusini nchini Tanzania Mhe. Eunje Ahn, aliahidi kuwa Serikali yake  itaendelea kushirikiana na Serikali ya Tanzania katika miradi ya kimkakati, ili kuhakikisha maendeleo ya kijamii na kiuchumi yanapatikana kwa manufaa ya wananchi wa mataifa hayo.

Kikao hicho kilihudhuriwa na Naibu Katibu Mkuu, Wizara ya Fedha, Bi. Amina Khamis Shaaban, Kamishna Msaidizi, Idara ya Fedha za Nje, Wizara ya Fedha Bw. Melckzedeck Mbise na mwakilishi kutoka Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki.

BELEKO: TUKISHINDWA KUPANGA, TUNAPANGA KUSHINDWA




Naibu Kamishna wa Uhifadhi anayeshughulikia Masoko na Matumizi Endelevu ya Rasilimali za Misitu wa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS), Salehe Beleko, amewataka viongozi na makamanda wa vituo vya wakala huo kuimarisha nidhamu ya mipango, uwazi wa mapato na utoaji wa huduma kwa kuzingatia misingi ya “Kazi na Utu”.

Akizungumza leo Februari 19, 2026 katika siku ya pili ya Mkutano wa Nne wa Viongozi na Makamanda wa Vituo vya TFS unaoendelea katika Ukumbi wa Hoteli ya Cate, Morogoro, Beleko alisisitiza kuwa mafanikio ya uhifadhi yanategemea ubora wa mipango na utekelezaji wake.

“Tunapoandaa mpango mkakati na mpango wa kibiashara, tuzingatie rasilimali tulizonazo. Fedha ni haba lakini mahitaji ni mengi, hivyo lazima tuweke vipaumbele vitakavyotupeleka moja kwa moja katika kuimarisha uhifadhi,” alisema.

Alionya kuwa ongezeko la carry overs na reallocations ni dalili ya udhaifu katika upangaji wa bajeti na mtiririko wa fedha (cash flows), akitahadharisha kuwa taasisi isipopanga vizuri, hujiandalia mazingira ya kushindwa.

Kwa upande wa leseni na matumizi ya rasilimali, Beleko alieleza kuwa kumekuwapo na tofauti kati ya kiasi kilichopangwa kuvunwa na kile kinachovunwa katika baadhi ya maeneo, huku malengo ya mapato yakifikiwa kupitia mifumo isiyo sahihi.

“Hakikisheni huduma zinatolewa kwa wateja waliopitia taratibu zote za kisheria—kamati za uvunaji za wilaya, vyeti vya mgao na leseni halali. Tusikusanye mapato nje ya mfumo,” alisisitiza.

Aidha, alikemea matumizi holela ya mashine za kuchakatia na misumeno ya moto ndani ya hifadhi bila vibali maalum, akitaka taratibu zifuatwe kikamilifu ili kulinda rasilimali na mapato ya serikali.

Katika kuboresha uwajibikaji, alihimiza matumizi ya teknolojia za kisasa katika upimaji wa rasilimali za misitu ili kuzuia upotevu wa mapato na mianya ya udanganyifu.

Hata hivyo, pamoja na msisitizo wa nidhamu ya kifedha na kiutendaji, alirejea kaulimbiu ya “Kazi na Utu”, akitaka wahifadhi na watumishi wote kutoa huduma kwa heshima na kuwachukulia wateja kama wadau, si wahalifu.

“Tuwahudumie kwa heshima. Wapo wanaokengeuka, lakini tuna wajibu wa kuwabadilisha kuwa wateja wazuri. Huduma bora inaleta tabasamu kwa Watanzania,” alisema.

Mkutano huo unaendelea kujadili mikakati ya kuimarisha uhifadhi, kuongeza mapato halali na kuboresha usimamizi wa mashamba na hifadhi za misitu nchini.

DKT. MATARAGIO AZUNGUMZA NA NBC DODOMA



📌Waweka mikakati ya kuwawezesha wawekezaji wazawa katika sekta ya Mafuta na Gesi.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati anayeshughulikia Mafuta na Gesi Asilia, Dkt. James Mataragio, amefanya kikao na uongozi wa Benki ya Taifa ya Biashara (NBC) leo tarehe 19 Februari 2026 jijini Dodoma. 

Kikao hicho kililenga kujadili namna ambavyo Wizara ya Nishati na NBC wanavyoweza kushirikiana katika kuwawezesha wawekezaji wazawa, hususan katika sekta ya mafuta na gesi.

Dkt. Mataragio ameipongeza NBC kwa utayari wake wa kuwainua wawekezaji wazawa, akisema hatua hiyo ni muhimu katika kukuza uchumi wa nchi, hasa kupitia sekta ya nishati. Ameeleza kuwa wapo wadau wengi wazawa wenye nia ya kuwekeza katika mafuta na gesi, lakini wanakumbwa na changamoto mbalimbali, ikiwemo ukosefu wa mitaji wezeshi ya kutekeleza miradi hiyo.

“Ujio na ushirikiano wenu utasaidia kuwainua wawekezaji wazawa ili waweze kumudu na kuwekeza kikamilifu hapa nchini,” amesisitiza Dkt. Mataragio.

Aidha, ameongeza kuwa Serikali inatamani kuona wawekezaji wazawa wanajenga viwanda, kuanzisha biashara, na kuajiri vijana ili kupunguza changamoto ya ukosefu wa ajira nchini. Pia alibainisha kuwa sekta ya nishati inapaswa kuwa na mchango mkubwa zaidi katika uchumi wa taifa, huku wawekezaji wazawa wakichukua nafasi muhimu katika maendeleo ya sekta hiyo.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa NBC anayeshughulikia wateja wakubwa na Serikali, Bw. Elvis Ndunguru, amesema benki hiyo imekuwa ikitoa mikopo kwa wawekezaji wadogo na wakubwa ili kusaidia kukuza biashara zao.

Benki ya Taifa ya Biashara  imekuwa ikishirikiana na Serikali na taasisi mbalimbali kutoa huduma za kifedha kwa wawekezaji, hasa katika sekta za kilimo, uvuvi na ufugaji. Sisi kama NBC tupo tayari kushirikiana na Wizara ili kufikia malengo ya Serikali ya kuwawezesha wawekezaji, hususan wazawa,” amesema Ndunguru.

Wizara ya Nishati na NBC zimekubaliana kufanya kazi kwa pamoja ili kuwainua wawekezaji wazawa katika sekta ya nishati kwa lengo la kukuza uwekezaji wa ndani, kutengeneza ajira na kuchangia ukuaji wa uchumi nchini. 

Ushirikiano huo unatarajiwa kuleta matokeo chanya katika maendeleo ya sekta ya nishati nchini na kusaidia utekelezaji wa malengo ya Serikali ya kukuza uchumi na kuboresha maisha ya wananchi kwa ujumla.

RAIS MWINYI ASHIRIKI FUTARI ILIYOANDALIWA NA RAIS SAMIA IKULU TUNGUU–ZANZIBAR

 












Tunguu, Unguja – 19 Februari 2026

Mwezi mtukufu wa Ramadhani umeendelea kuunganisha viongozi na wananchi, ambapo Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, alijumuika kwenye futari iliyoandaliwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika Viwanja vya Ikulu Ndogo ya Tunguu, Mkoa wa Kusini Unguja.

Hafla hiyo iliwakutanisha viongozi wa Serikali, vyombo vya ulinzi na usalama, viongozi wa vyama vya siasa, viongozi wa dini pamoja na wananchi kutoka maeneo mbalimbali ya Zanzibar, katika mazingira yaliyojaa mshikamano, heshima na maombi ya pamoja.

Akizungumza katika tukio hilo, Rais Samia alisisitiza umuhimu wa Ramadhani kama kipindi cha kuimarisha umoja wa kitaifa, mshikamano wa kijamii na uwajibikaji katika utumishi wa umma. Alitoa wito kwa viongozi na wananchi kuendelea kudumisha amani, upendo na mshikamano kama tunu kuu za Taifa.

Kwa upande wake, Rais Mwinyi alieleza shukrani kwa mwaliko huo na kupongeza juhudi za kuendeleza utamaduni wa kukutana na wananchi katika matukio ya kiroho yanayolenga kuimarisha mshikamano wa kitaifa. Alibainisha kuwa futari ya pamoja ni ishara ya umoja na ushirikiano kati ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Futari hiyo ilipambwa na dua maalum za kuliombea Taifa, viongozi wake na wananchi kwa ujumla, huku washiriki wakisisitiza umuhimu wa kuendeleza maadili mema yanayohimizwa katika mwezi wa Ramadhani — ikiwemo uvumilivu, huruma na kusaidiana.

Tukio hilo limeonesha kwa vitendo mshikamano wa viongozi wakuu wa nchi na wananchi, likiwa ni sehemu ya kuimarisha umoja na kuendeleza maadili ya kitaifa katika kipindi hiki muhimu cha kiimani.

MSIPORE ARDHI ZA WANANCHI KWA KIGEZO CHA UWEKEZAJI-DKT. MWIGULU







Asema msimamo wa Rais Dkt. Samia ni maendeleo na uwekezaji

WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba amewataka watendaji wa Serikali wasipore ardhi za wananchi kwa kigezo cha uwekezaji kwani msimamo wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ni kuwa kinara katika maendeleo na uwekezaji

“Rais Dkt. Samia anasema watendaji Serikalini, kwenye maeneo ya mikoa, wilayani msipore ardhi za watu kwa kigezo cha uwekezaji au maendeleo. Kila mtu apewe haki yake, msitumie ubabe kupora maeneo ya watu; Naibu Waziri - TAMISEMI andikeni barua inayotoa maelekezo hayo,” amesema.

Amesema hayo leo (Alhamisi, Februari 19, 2026) wakati akizungumza na wakazi wa Mkuu, mara baada ya kuweka jiwe la msingi kwenye jengo la utawala la Halmshauri ya Wilaya ya Rombo, mkoani Kilimanjaro.

Mheshimiwa Dkt. Mwigulu amesema kuwa Rais Dkt. Samia anafanya kazi kubwa inayoleta heshima kwa Tanzania. “Kuna mambo yalikuwa yanaleta aibu kuyasema, lakini leo hii ndani ya kipindi cha miaka minne, Rais Dkt. Samia ameyatekeleza.”

Amesema kuwa katika kipindi cha miaka minne, Rais Dkt. Samia amejenga majengo ya utawala katika halmashauri 143 ambazo hazikuwa na majengo yenye hali ya kuridhisha. “Pia amejenga hospitali 119 kwenye wilaya zote ambazo hazikuwa na hospitali za wilaya.”

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu amemuagiza Kamanda wa TAKUKURU mkoa wa Kilimanjaro afuatilie tuhuma kwenye mradi wa mabwawa ya samaki uliopo eneo la Mraokeryo, Wilaya ya Rombo mkoani Kilimanjaro ambao umejengwa chini ya kiwango na kupunguza ukubwa wa bwawa lililotakiwa kujengwa.

Kwa upande wake, Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, Reuben Kwagiilwa amewaagiza Wakurugenzi wote wa Halmashauri kuhakikisha kuwa kila mmoja anamsimamia aliye chini yake ili kuongeza uwajibikaji katika kutoa huduma kwa wananchi.

JKCI yaiweka Tanzania kwenye ramani ya Afrika kwa upasuaji wa Moyo wa kisasa

Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge akimkabidhi zawadi  Mwenyekiti mpya wa Bodi ya Wadhamini ya Taasisi hiyo Dkt. Hassan Mahmoud Mshinda alipotembelea JKCI kwa mara ya kwanza leo kwaajili ya kuona utendaji kazi pamoja na kukutana na viongozi.
Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge akimweleza utendaji kazi wa taasisi hiyo  Mwenyekiti mpya wa Bodi ya Wadhamini ya JKCI  Dkt. Hassan Mahmoud Mshinda alipotembelea taasisi hiyo  kwa mara ya kwanza leo kwaajili ya kuona utendaji kazi pamoja na kukutana na viongozi.

 Uongozi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) umepongezwa kwa maono ya mbali na uthubutu mkubwa katika kuanzisha na kuendeleza upasuaji wa moyo wa aina mbalimbali, hatua iliyoiwezesha Tanzania kuwa kitovu cha huduma za kibingwa na bobezi za matibabu ya moyo katika Ukanda wa Afrika Mashariki na Kati.

Pongezi hizo zimetolewa na Mwenyekiti mpya wa Bodi ya Wadhamini ya taasisi hiyo, Dkt. Hassan Mahmoud Mshinda wakati wa ziara yake ya kwanza JKCI kwaajili ya kuona utendaji kazi pamoja na kukutana na viongozi wa taasisi hiyo.

Dkt. Mshinda alisema ameridhishwa na kasi ya maendeleo, ubunifu na uthubutu uliofanywa na taasisi hiyo katika kuboresha huduma za moyo nchini.

“Nimejionea kwa macho yangu ubora wa huduma na mipango mikubwa ya maendeleo inayoendelea kutekelezwa. Si rahisi kwa taasisi nyingi kuwa na ujasiri wa kujaribu na kuwekeza katika teknolojia za kisasa kama ilivyofanywa hapa, haya ni mafanikio yanayostahili pongezi,” alisema Dkt. Mshinda.

Alisisitiza kuwa Bodi ya Wadhamini itatoa ushirikiano wa karibu kwa uongozi wa taasisi hiyo ili kuhakikisha malengo ya kuimarisha huduma za moyo yanatimia kwa ufanisi na kwa manufaa ya Watanzania wote.

Akigusia uzoefu wake binafsi, Dkt. Mshinda alisema aliwahi kupatiwa matibabu katika taasisi hiyo na kushuhudia viwango vya juu vya huduma vinavyolingana na vya mataifa yaliyoendelea.

“Nimewahi kutibiwa hapa. Naweza kusema bila kusita kuwa huduma za hapa na za Switzerland hazina tofauti kubwa. Hata wenzetu wa huko walishangaa kusikia kuwa Tanzania ina taasisi ya kiwango hiki”, aliongeza.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa JKCI, Dkt. Peter Kisenge alisema tangu kuanzishwa kwa taasisi hiyo imechangia kwa kiasi kikubwa kupunguza rufaa za wagonjwa wa moyo waliokuwa wakipelekwa nje ya nchi kwa matibabu maalum jambo lililookoa fedha nyingi za Serikali na kupunguza adha kwa wagonjwa na familia zao.

Alifafanua kuwa taasisi hiyo imepanua wigo wa huduma kwa kuanzisha matawi sita katika maeneo mbalimbali ya nchi, hatua iliyosaidia kupunguza msongamano wa wagonjwa katika makao makuu na kuongeza ufanisi wa utoaji huduma.

“Mbali na huduma za ana kwa ana, tumeanza pia kutoa huduma kwa njia ya mtandao hususan kwa wagonjwa wa shinikizo la damu ili kurahisisha ufuatiliaji wa matibabu na kupunguza gharama na muda wa safari”, alisema Dkt. Kisenge.

Alibainisha kuwa JKCI ni miongoni mwa taasisi chache barani Afrika zenye uwezo wa kufanya upasuaji wa moyo kwa kutumia teknolojia ya kisasa ya tundu dogo, pamoja na kumiliki mtambo wa Carto 3 kwaajili ya matibabu ya umeme wa moyo ambao ni wa kipekee katika Ukanda wa Afrika Mashariki na Kati.

Dkt. Kisenge alimshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan,kwa kuendelea kuiunga mkono taasisi hiyo na kwa kumteua Dkt. Mshinda kuiongoza Bodi ya Wadhamini huku akieleza akieleza kuwa uzoefu wake katika utafiti utaongeza nguvu katika eneo la tafiti za magonjwa ya moyo.

Katika ziara hiyo  Mwenyekiti huyo wa Bodi ya Wadhamini ya JKCI alitembelea pia JKCI Hospitali ya Dar Group ambapo  Mkurugenzi wa Hospitali hiyo Dkt. Tulizo Shemu, alisema tangu hospitali hiyo ilipokabidhiwa kwa JKCI mwishoni mwa mwaka 2022 imefanya maboresho makubwa ya miundombinu na utoaji wa huduma.

Dkt. Shemu alieleza kuwa idadi ya wagonjwa wa nje imeongezeka kutoka wastani wa 200 hadi kufikia 650 pia wamefanya ujenzi wa chumba cha kisasa cha upasuaji, wameboresho eneo la OPD, ujenzi wa jengo la VIP, pamoja na ongezeko la vifaa tiba na uwepo wa wataalamu mabingwa wa magonjwa mbalimbali.

Dkt. Shemu alisema Hospitali ya Dar Group inatoa huduma za matibabu ya magonjwa mbalimbali ikiwemo matibabu za moyo, huduma za upasuaji, matibabu ya magonjwa ya wanawake na watoto, matibabu ya afya ya kinywa na meno, matibabu ya macho, huduma za mazoezi tiba, matibabu ya mifupa, pamoja na huduma za dharura. 

“Hospitali ya Dar Group ilianzishwa na Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere kupitia azimio maalumu la mwaka 1981 na kusajiliwa na Wakala wa usajili wa Biashara na Leseni (BRELA) mwaka 1997 chini ya sheria ya makampuni ya mwaka 1967 ikihusishwa na dhamana isiyo mtaji”, alisema Dkt. Shemu.

Oryx Gas Waja na Promosheni Maalum ya Mfungo

  NA MWANDISHI WETU, DAR ES SALAAM KATIKA kuendelea kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia, Kampuni ya Oryx Gas imezindua kampeni...