Wednesday, June 10, 2026

WAZIRI WA FEDHA: BAJETI YA 2026/27 KUIJENGA TANZANIA YA DIRA YA 2050




 Na Eva Valerian, WF, Dodoma

Serikali imesema Bajeti Kuu ya mwaka wa fedha 2026/27 ni ya kipekee kwa kuwa ndiyo bajeti ya kwanza itakayotumika kutekeleza Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, Mpango wa Nne wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano (2026/27–2030/31) pamoja na Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ya mwaka 2025.

Hayo yamesemwa na Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu mwelekeo wa Bajeti Kuu ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2026/27, katika Ukumbi wa Kambarage, Treasury Square jijini Dodoma, Bajeti ambayo itasomwa Bungeni Dodoma Siku ya Alhamisi, tarehe 11 juni 2026.

Mhe. Balozi Omar alisema kuwa, Serikali inatarajia kutumia jumla ya shilingi trilioni 62.3 katika mwaka wa fedha 2026/27, ambapo sehemu kubwa ya fedha hizo itaelekezwa katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo ya kimkakati inayochochea ukuaji wa uchumi wa Taifa.

“Fedha hizi zitaelekezwa katika kuendelea na ujenzi wa Reli ya Kisasa (SGR), kuboresha mtandao wa barabara, kuimarisha huduma za maji, kuendeleza miradi ya nishati pamoja na uwekezaji katika rasilimali watu na maendeleo ya ujuzi,” alisema Mhe. Balozi Omar. 

Aidha, alisema kuwa bajeti hiyo imeandaliwa kwa lengo la kuharakisha maendeleo ya kiuchumi na kijamii, kuongeza ajira, kuvutia uwekezaji na kuimarisha ustawi wa wananchi na Serikali inatarajia kukusanya mapato ya ndani ya shilingi trilioni 46.8 ili kugharamia sehemu kubwa ya matumizi yaliyopangwa katika bajeti hiyo.

Mhe. Balozi Omar aliongeza kuwa, kabla ya kuwasilisha makadirio ya mapato na matumizi ya mwaka 2026/27, Serikali itatoa tathmini ya utekelezaji wa Bajeti ya mwaka 2025/26, akibainisha kuwa ukusanyaji wa mapato ya ndani umeendelea kufanya vizuri na kufikia malengo yaliyowekwa. 

Aliongeza kuwa, Serikali imeendelea kushirikisha wadau mbalimbali katika mchakato wa maandalizi ya bajeti kupitia Kamati ya Wataalam wa Maboresho ya Kodi (Task Force on Tax Reforms) pamoja na Kamati ya Ushauri ya Ngazi ya Juu ya ‘Think Tank’, hatua ambayo imeongeza uwazi na ushirikishwaji katika maamuzi ya sera za kodi.

“Upande wa maboresho ya kodi, Serikali imepokea jumla ya mapendekezo 727 kutoka kwa wadau mbalimbali wakiwemo sekta binafsi, taasisi za elimu, jumuiya za wafanyabiashara, mashirika yasiyo ya kiserikali na wananchi binafsi, ambapo kati ya mapendekezo hayo, 125 yalikubaliwa kama yalivyowasilishwa, 121 yalifanyiwa maboresho na kukubaliwa, huku 295 yakikataliwa baada ya kufanyiwa uchambuzi wa kina” alisema Mhe. Balozi Omar 

Mhe Balozi Omar aliongeza kuwa, Lengo la maboresho hayo ni kukuza uchumi, kuongeza ajira, kupanua wigo wa kodi kwa kuvutia uwekezaji zaidi na wakati huo huo kupunguza mzigo wa kodi kwa walipakodi. 

Mhe. Balozi Omar, alitumia fursa hiyo kuwapongeza waandishi wa habari kwa mchango wao mkubwa katika kuhabarisha umma kuhusu masuala ya maendeleo na kusisitiza umuhimu wa wananchi kuendelea kutimiza wajibu wao wa kulipa kodi kwa hiari na kwa wakati. 

“Tunajenga Taifa letu kwa pamoja. Serikali itaendelea kuhakikisha fedha zinazokusanywa zinatumika kwa ufanisi na kuleta matokeo chanya kwa wananchi,” alisema Mhe. Balozi Omar.

Alitumia fursa hiyo kuwataka Watanzania kufuatilia kwa makini uwasilishaji rasmi wa Bajeti Kuu ya Serikali ya mwaka 2026/27 utakaofanyika Bungeni jijini Dodoma Juni 11, 2026, akisema bajeti hiyo imeandaliwa kwa kuzingatia matarajio ya wananchi na mahitaji ya maendeleo ya taifa.

MAHUNDI AIELEZA DUNIA HATUA ZA TANZANIA KATIKA KULINDA HAKI ZA WATU WENYE ULEMAVU

Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Mhe. Mhandisi Maryprisca MahundI akitoa taarifa ya nchi Mkutano wa 19 wa Nchi Wanachama wa Mkataba wa Haki za Watu Wenye Ulemavu (COSP19) unaofanyika katika Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa, Jijini New York, Marekani.




Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Mhe. Mhandisi Maryprisca Mahundi akiwa na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Wakili Amon Mpanju katika Mkutano wa 19 wa Nchi Wanachama wa Mkataba wa Haki za Watu Wenye Ulemavu (COSP19) unaofanyika katika Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa, Jijini New York, Marekani.

Baadhi ya washiriki wakiwa katika Mkutano wa 19 wa Nchi Wanachama wa Mkataba wa Haki za Watu Wenye Ulemavu (COSP19) unaofanyika katika Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa, Jijini New York, Marekani. Picha zote na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini-WMMJWM
 Mganga Mkuu wa Serikali Dkt. Grace Maghembe akiwa katika Mkutano wa 19 wa Nchi Wanachama wa Mkataba wa Haki za Watu Wenye Ulemavu (COSP19) unaofanyika katika Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa, Jijini New York, Marekani.

Na Jackline Minja, New York, Marekani

Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Mhe. Mhandisi Maryprisca Mahundi, ameieleza Jumuiya ya Kimataifa hatua kubwa zinazochukuliwa na Serikali ya Tanzania katika kulinda na kuendeleza haki za watu wenye ulemavu, wakati aliposhiriki Mkutano wa 19 wa Nchi Wanachama wa Mkataba wa Haki za Watu Wenye Ulemavu (COSP19) unaofanyika katika Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa, Jijini New York, Marekani.

Mhe. Mahundi, ambaye amemuwakilisha Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Sera, Bunge na Uratibu  na Wenye Ulemavu, Mhe. Profesa Palamagamba John Kabudi, amesema Tanzania imeendelea kuimarisha mifumo ya kisheria, kisera na kiutendaji ili kuhakikisha watu wenye ulemavu wanapata haki, fursa na huduma stahiki kama wananchi wengine.

Akiwasilisha taarifa ya nchi, Mhe. Mahundi amesema Tanzania imepiga hatua kubwa kupitia Sheria ya Watu Wenye Ulemavu Na. 9 ya mwaka 2010 kwa Tanzania Bara pamoja na Sheria Na. 8 ya mwaka 2022 ya Zanzibar, ambazo zimeweka msingi imara wa kulinda haki na ustawi wa watu wenye ulemavu.

 “Masuala ya ulemavu yamejumuishwa katika Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 na mipango mbalimbali ya maendeleo ili kuhakikisha hakuna anayebaki nyuma katika safari ya maendeleo ya taifa na kusema kuwa Serikali imeendelea kupanua upatikanaji wa elimu jumuishi, huduma za afya, huduma za urekebishaji na tiba, teknolojia saidizi, programu za uwezeshaji kiuchumi pamoja na huduma za hifadhi ya jamii kwa watu wenye ulemavu” amesema Mhe. Mahundi

Aidha  Mhe. Mahundi amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa uongozi wake madhubuti na dhamira ya dhati ya kuhakikisha watu wenye ulemavu wanapata huduma bora na fursa zinazowawezesha kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya nchi.

“Serikali ya Tanzania itaendelea kushirikiana na nchi wanachama, Umoja wa Mataifa, asasi za kiraia na watu wenye ulemavu wenyewe katika kuharakisha utekelezaji wa Mkataba wa Haki za Watu Wenye Ulemavu na kujenga jamii jumuishi inayoheshimu usawa, utu na haki za kila mtu,” amesema Mhe. Mahundi

Mkutano huo wa 19 wa Nchi Wanachama wa Mkataba wa Haki za Watu Wenye Ulemavu umebeba kaulimbiu inayosema “CRPD at 20: Celebrating and Consolidating Achievements and Shaping the Next Phase of Implementation in a Changing World,” ukilenga kutathmini mafanikio yaliyopatikana katika kipindi cha miaka 20 tangu kuanzishwa kwa mkataba huo na kuweka mikakati ya kuendeleza utekelezaji wake duniani. 




Friday, June 05, 2026

KIPANGULA: WAHITIMU WA HABARI WATAFAIDIKA NA MABORESHO YA KANUNI





 Na Mwandishi Wetu

Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB), Wakili Patrick Kipangula, amewashauri Waandishi wa Habari nchini kuipa thamani na heshima taaluma ya habari kwa kuzingatia nadhifu ya mavazi na mienendo yao wanapotekeleza majukumu ya kitaaluma.

Wakili Kipangula ametoa ushauri huo leo Juni 5, 2026 wakati akiwasilisha mada kuhusu “Uhuru wa Vyombo vya Habari katika Enzi ya Kidijiti: Wajibu wa Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari” kwenye Kongamano la Uhuru wa Vyombo vya Habari lililoandaliwa na Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) kupitia Idara ya Sanaa na Taaluma za Habari.

Amesema uandishi wa habari ni taaluma muhimu inayotambulika kama muhimili wa nne usio rasmi katika jamii, hivyo ni wajibu wa waandishi wenyewe kuhakikisha wanaijengea heshima kupitia mwenendo, maadili na namna wanavyojiwasilisha mbele ya jamii.

Wakili Kipangula amesema mwonekano wa mwandishi wa habari unaweza kuwa sehemu ya kujenga imani kwa jamii na vyanzo vya habari vinavyotoa taarifa mbalimbali kwa vyombo vya habari.

“Kwa hiyo hata mtu unavyoenda kumhoji mtu akikuona jinsi ulivyo anajua huyu mtu ataeleza kitu cha msingi na huyu mtu anaeleweka na ni wa maana,” amesema Wakili Kipangula.

Amesisitiza kuwa pamoja na kuzingatia maadili, sheria na weledi katika ukusanyaji na uchakataji wa habari, Waandishi wa Habari wanapaswa kutambua kuwa taswira wanayoijenga mbele ya jamii ni sehemu muhimu ya kuimarisha hadhi ya taaluma hiyo na kuongeza imani ya wananchi kwa vyombo vya habari.

Samia Aitangaza Tanzania kama Kitovu cha Uwekezaji Afrika katika Kongamano la Biashara Tanzania na Urusi

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza katika Kongamano la Biashara na Uwekezaji kati ya Tanzania na Urusi lililofanyika Jijini St. Petersburg nchini Urusi tarehe 05 Juni, 2026. Kongamano hilo limewakutanisha Wafanyabiashara, Wawekezaji pamoja na Taasisi za kukuza Uwekezaji kutoka Tanzania na Urusi.





Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, ameendelea kuitangaza Tanzania kama kitovu cha fursa za biashara na uwekezaji barani Afrika kwa kuwasilisha maono ya nchi katika Kongamano la Biashara na Uwekezaji kati ya Tanzania na Urusi lililofanyika jijini St. Petersburg nchini Urusi tarehe 05 Juni, 2026.

Akizungumza mbele ya viongozi wa serikali, wafanyabiashara wakubwa, wawekezaji na taasisi za kukuza uwekezaji kutoka Tanzania na Urusi, Rais Samia alieleza mafanikio makubwa ambayo Tanzania imeyapata katika kuboresha mazingira ya biashara, kuimarisha miundombinu ya kimkakati na kufungua milango kwa wawekezaji wa ndani na nje ya nchi.

Rais Samia alisisitiza kuwa Tanzania imeendelea kuwa moja ya nchi zenye mazingira rafiki zaidi ya uwekezaji katika ukanda wa Afrika Mashariki kutokana na utulivu wa kisiasa, sera zinazovutia uwekezaji, pamoja na uwekezaji mkubwa unaoendelea kufanywa katika sekta za usafirishaji, nishati, makazi, utalii, kilimo na viwanda.

Kongamano hilo limekuwa jukwaa muhimu la kuimarisha ushirikiano wa kiuchumi kati ya Tanzania na Urusi kwa kuwakutanisha wadau mbalimbali wa biashara na uwekezaji wenye lengo la kuchochea ushirikiano mpya, kuongeza mtiririko wa mitaji, teknolojia na ujuzi utakaosaidia kukuza uchumi wa pande zote mbili.

Kupitia diplomasia ya uchumi inayoongozwa na Rais Samia, Tanzania inaendelea kujijengea nafasi ya kipekee katika ramani ya uwekezaji duniani, huku ikiwavutia wawekezaji wengi zaidi kuja kutumia fursa zilizopo katika sekta mbalimbali za maendeleo. Ushiriki wa Tanzania katika kongamano hilo unaonesha dhamira thabiti ya Serikali ya Awamu ya Sita ya kuendelea kufungua milango ya ushirikiano wa kimataifa, kuongeza biashara na kuharakisha maendeleo ya uchumi kwa manufaa ya wananchi.

Kongamano hilo linatarajiwa kuibua fursa mpya za ushirikiano wa kibiashara na uwekezaji kati ya Tanzania na Urusi, na kuimarisha zaidi mahusiano ya muda mrefu yaliyopo kati ya mataifa hayo mawili.

DKT.NCHIMBI ATOA MAELEKEZO MAPYA YA UHIFADHI WA MAZINGIRA, AZINDUA PROGRAMU YA MAGEUZI YA MIAKA MITANO

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi akihutubia wakati Maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani, yaliyofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Jakaya Kikwete Mkoani Dodoma, tarehe 05 Juni 2026.


Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi akimkabidhi tuzo Waziri wa Maliasili na Utalii Dkt. Ashatu Kijaji, iliyotolewa na Ofisi ya Makamu wa Rais kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kutambua Uongozi wake Mahiri na dhamira ya dhati ya kuimarisha Ajenda ya Uhifadhi wa Mazingira. Tuzo hiyo imetolewa wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani yaliyofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Jakaya Kikwete mkoani Dodoma, leo tarehe 05 Juni 2026.
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi akimkabidhi tuzo Mkurugenzi wa Mamlaka ya Udhibiti na Usimamizi wa Mazingira – Zanzibar Bw. Sheha Mjaja Juma, iliyotolewa na Ofisi ya Makamu wa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi kwa kutambua Uongozi wake Mahiri na mchango wa kipekee katika kuimarisha Ajenda ya Uhifadhi wa Mazingira. Tuzo hiyo imetolewa wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani yaliyofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Jakaya Kikwete mkoani Dodoma, leo tarehe 05 Juni 2026.

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi akiwa katika picha ya pamoja na wanafunzi mbalimbali, ambao wanashiriki katika program ya utunzaji wa mazingira ya Eco School, mara baada ya kuhitimisha Maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani, yaliyofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Jakaya Kikwete mkoani Dodoma, leo tarehe 05 Juni 2026.

Na Alex Sonna,Mzalendo blog-DODOMA 

Serikali imeweka mkazo mpya katika mapambano dhidi ya uharibifu wa mazingira na athari za mabadiliko ya tabianchi kwa kuzindua Programu ya Mageuzi ya Kimkakati ya Mazingira Endelevu Tanzania itakayotekelezwa kwa kipindi cha miaka mitano kuanzia mwaka 2026 hadi 2030.

Hayo yamesemwa  na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi akimwakilisha Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika kilele cha Maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani mwaka 2026 ,leo Juni 5,2026 jijini Dodoma.

Dkt.Nchimbi  amesema mazingira ni nguzo muhimu ya maendeleo ya taifa kwani yanachangia ukuaji wa uchumi, ustawi wa wananchi na upatikanaji wa rasilimali muhimu zinazohitajika kwa maendeleo ya sasa na ya baadaye.

Ameeleza kuwa Tanzania yenye zaidi ya wananchi milioni 67 kwa sasa inatarajiwa kuwa na zaidi ya watu milioni 118 ifikapo mwaka 2050, hali inayoongeza umuhimu wa kuhifadhi rasilimali za mazingira kama maji, ardhi yenye rutuba, misitu na vyanzo vya nishati ili kukidhi mahitaji ya idadi hiyo kubwa ya watu.

” Serikali imejumuisha masuala ya mazingira na ustahimilivu wa mabadiliko ya tabianchi katika Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, ikilenga kuhakikisha ukuaji wa uchumi unaenda sambamba na matumizi endelevu ya rasilimali za asili.”amesema Dkt.Nchimbi

Amesema maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani yanapaswa kuwa chachu ya kuimarisha ushirikiano kati ya Serikali, sekta binafsi, mashirika ya kiraia na wananchi katika kuhifadhi mazingira na kutumia rasilimali zilizopo kwa uangalifu mkubwa.

Katika hatua za kuimarisha usafi wa mazingira, Dkt.Nchimbi amesisitiza umuhimu wa kubadili mtazamo wa jamii kuhusu taka kwa kuziona kama fursa za kiuchumi badala ya mzigo. Amesema taka zinaweza kutumika kuzalisha mbolea, chakula cha mifugo na bidhaa nyingine zenye thamani ya kiuchumi huku zikichangia kupunguza uchafuzi wa mazingira.

Pia amepongeza mafanikio ya utekelezaji wa Mkakati wa Taifa wa Matumizi ya Nishati Safi ya Kupikia, akibainisha kuwa matumizi ya nishati hiyo yameongezeka kutoka asilimia 6.9 mwaka 2021 hadi asilimia 28.6 mwaka 2025.

“Tunakwenda katika mwelekeo sahihi wa kufikia lengo la zaidi ya asilimia 80 ya Watanzania kutumia nishati safi ya kupikia ifikapo mwaka 2034,” amesema.

Katika kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi, Serikali imeendelea kuimarisha utekelezaji wa mikakati mbalimbali ya kisekta inayolenga kujenga uchumi wenye uzalishaji mdogo wa gesi joto pamoja na kuimarisha uwezo wa jamii kustahimili athari za mabadiliko hayo.

Aidha, Serikali imeeleza kuwa biashara ya kaboni ni miongoni mwa fursa muhimu zinazoweza kuongeza mapato ya ndani huku zikichochea juhudi za uhifadhi wa mazingira. Hivyo, wizara na taasisi mbalimbali zimeagizwa kujumuisha fursa hizo katika mipango, miradi na programu zao za maendeleo.

Katika maelekezo mahsusi kwa taasisi za Serikali, Dkt.Nchimbi ameagiza majiji na manispaa nchini kuanzisha na kutunza bustani za kijani, huku mamlaka zinazotoa vibali vya ujenzi zikihakikisha kila kibali kinaambatana na sharti la kupanda miti isiyopungua mitano.

Pia ameitaka Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania kuhakikisha upatikanaji wa miche ya miti ya kutosha kwa ajili ya kuendeleza kampeni za upandaji miti nchini, sambamba na kuimarisha ulinzi wa maeneo yote yanayopandwa miti.

Kwa upande wa usimamizi wa taka, Serikali imezielekeza mamlaka za serikali za mitaa kuanzisha vituo vya kuchakata taka ili kupunguza mzigo wa taka katika madampo na kuongeza shughuli za urejelezaji ambazo zitasaidia kulinda mazingira na kufungua fursa mpya za ajira.

Kadhalika, Ofisi ya Waziri Mkuu (TAMISEMI), Wizara ya Maliasili na Utalii pamoja na Wizara ya Maji zimeagizwa kuimarisha usimamizi wa maeneo ya ardhi oevu ambayo ni muhimu kwa uzalishaji wa chakula, maji na nishati.

Dkt.Nchimbi pia amezitaka taasisi za utafiti nchini kufanya tafiti za kina kuhusu mimea na viumbe vamizi vinavyoendelea kuathiri mifugo, mazao na mifumo ya ikolojia katika maeneo mbalimbali ya Tanzania.

Hata hivyo  amesisitiza kuwa suala la uhifadhi wa mazingira halina mbadala kwa kuwa mazingira ndiyo msingi wa maisha na uchumi wa taifa.

“Mazingira yetu ndiyo uhai wetu na uchumi wetu. Kila mmoja wetu anapaswa kuwajibika katika kulinda, kutunza na kuhakikisha usafi wa mazingira ili kupunguza athari za mabadiliko ya tabianchi na kuacha urithi bora kwa vizazi vijavyo,” amesema.

Kwa upande wake Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira, Mhandisi Hamad Yusuf Masauni, amesema  katika maadhimisho hayo mwaka huu shughuli nyingi zimefanyika za utoaji elimu ya utunzaji wa mazingira.

Amesema shughuli nyingine zilizofanyika ni pamoja na upandaji miti katika maeneo korofi na kuratibiwa kwa kongamano la wadau wa mazingira.

“Vilevile Mheshimiwa Makamu wa Rais, katika hafla hii tutakuomba utuzindulie Programu ya Mageuzi ya Usimamizi wa Mazingira Kuelekea Dira 2050 itakayotekelezwa kwa kipindi cha miaka mitano (2026–2030),” amesema 

Mhandisi Masauni amesema programu hiyo inalenga kuchochea matokeo makubwa na ya haraka katika kurejesha uoto wa asili, kuimarisha ustawi wa mifumo ikolojia pamoja na huduma za kiikolojia ambazo ni msingi muhimu wa uzalishaji katika sekta mbalimbali za uchumi.

Amesema hatua hizo zitachangia kwa kiasi kikubwa katika kufanikisha malengo ya Dira ya 2050, ambayo inalenga kuifanya Tanzania kuwa miongoni mwa nchi kumi barani Afrika zenye ustawi wa mazingira na ustahimilivu mkubwa dhidi ya mabadiliko ya tabianchi.

NAIBU WAZIRI WA MAJI APONGEZA JUHUDI ZA TFS KULINDA VYANZO VYA MAJI

 




Na Mwandishi Wetu, Dodoma

Naibu Waziri wa Maji, Eng. Kundo Mathew, amepongeza juhudi zinazofanywa na Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) katika kuhifadhi misitu na kulinda vyanzo vya maji nchini, akieleza kuwa uhifadhi wa misitu ni msingi muhimu wa upatikanaji endelevu wa maji kwa wananchi na shughuli za maendeleo.

Eng. Kundo alitoa pongezi hizo Juni 4, 2026, alipotembelea banda la TFS na Idara ya Misitu na Nyuki katika Maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani yanayoendelea jijini Dodoma.

Akipokea maelezo kutoka kwa Afisa Uhifadhi Mwandamizi wa TFS, Filipo Mwampamba, Naibu Waziri huyo alitaka kufahamu kwa kina namna TFS inavyoshirikiana na Wizara ya Nishati pamoja na taasisi zinazohusika na usimamizi wa mabonde ya maji katika kuhifadhi vyanzo vya maji vinavyotegemewa kwa matumizi ya nyumbani, kilimo, uzalishaji wa umeme na shughuli nyingine za kiuchumi.

Akijibu, Mwampamba alisema TFS imekuwa ikitekeleza programu mbalimbali za kuhifadhi misitu ya vyanzo vya maji kwa kushirikiana na mamlaka za mabonde ya maji, serikali za mitaa na wadau wa maendeleo.

Alisema ushirikiano huo unajumuisha upandaji miti, urejeshaji wa maeneo yaliyoharibiwa, kudhibiti shughuli za kibinadamu zinazochangia uharibifu wa mazingira pamoja na utoaji wa elimu ya uhifadhi kwa jamii zinazozunguka hifadhi za misitu.

“Misimu mingi ya mvua na upatikanaji wa maji hutegemea uwepo wa misitu yenye afya. Misitu mingi inayosimamiwa na TFS ndiyo chanzo cha mito na chemchemi zinazolisha mabonde makubwa ya maji nchini,” alisema Mwampamba.

Aliongeza kuwa TFS pia ina jukumu la kusimamia na kuhifadhi hifadhi za misitu, kuendeleza ufugaji nyuki na biashara ya mazao ya nyuki, pamoja na kusimamia utalii ikolojia na maeneo ya urithi wa kihistoria yaliyopo ndani ya hifadhi za misitu.

Akizungumza baada ya kutembelea banda hilo, Eng. Kundo alisema Serikali inatambua mchango mkubwa wa TFS katika kulinda mazingira na kuhakikisha vyanzo vya maji vinaendelea kuwa salama kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.

“Uhifadhi wa misitu ni sehemu muhimu ya uhifadhi wa rasilimali za maji. Bila misitu imara, upatikanaji wa maji ya uhakika kwa wananchi, viwanda na miradi ya uzalishaji wa umeme unaweza kuathirika. Tunapongeza kazi kubwa inayofanywa na TFS katika kuhakikisha vyanzo vya maji vinaendelea kulindwa,” alisema.

Aidha, alisisitiza umuhimu wa kuimarisha ushirikiano kati ya taasisi za serikali, sekta binafsi na wananchi katika kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi ambazo zimeendelea kuathiri mifumo ya ikolojia na upatikanaji wa maji katika maeneo mbalimbali nchini.

Maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani mwaka huu yameendelea kuwa jukwaa la kuelimisha umma kuhusu umuhimu wa kuhifadhi mazingira, kupunguza uharibifu wa misitu na kuhamasisha matumizi endelevu ya rasilimali asilia kwa maendeleo ya taifa.

Karibu-KiliFair Yaendelea Kuinua Hadhi ya Utalii Tanzania Kimataifa







Na Calvin Katera, Arusha

Maonesho ya Kimataifa ya Utalii ya Karibu-KiliFair 2026 yameendelea kuthibitisha nafasi yake kama jukwaa muhimu la kukuza utalii wa Tanzania kwa kuwakutanisha wadau wa ndani na nje ya nchi, huku yakichangia kuongezeka kwa watalii, uwekezaji na fursa za kiuchumi zinazotokana na sekta hiyo.

Akifungua rasmi maonesho hayo Juni 5, 2026 katika Viwanja vya Magereza jijini Arusha kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, Mkurugenzi wa Utalii Dkt. Thereza Mugobi alisema kuwa Karibu-KiliFair si maonesho ya kawaida bali ni uwekezaji wa kimkakati unaoendelea kuijenga Tanzania kama kitovu cha utalii barani Afrika.

Alisema kupitia maonesho hayo, mahusiano ya kibiashara yanayojengwa kati ya wadau wa sekta ya utalii kutoka mataifa mbalimbali yamekuwa chachu ya kuongeza idadi ya watalii wanaoingia nchini, kuvutia uwekezaji, kuzalisha ajira na kuboresha maisha ya jamii zinazozunguka maeneo ya utalii.

"Karibu-KiliFair ni zaidi ya maonesho; ni uwekezaji wa kimkakati katika mustakabali wa utalii wa Tanzania. Serikali itaendelea kuwekeza katika miundombinu ya utalii ikiwemo malazi, viwanja vya ndege na barabara ili kuboresha uzoefu wa watalii na kuwafikisha kwa urahisi katika vivutio mbalimbali vya utalii," alisema Dkt. Mugobi.

Aidha, alibainisha kuwa Wizara itaendelea kutumia majukwaa ya kidijitali kutangaza vivutio vya utalii vya Tanzania katika masoko mbalimbali duniani ili kuongeza ushindani wa nchi katika soko la utalii la kimataifa.

Kwa upande wake, mwakilishi wa Chama cha Waendeshaji wa Utalii Tanzania (TATO), Wilbard Chambulo, alisema maonesho hayo yameendelea kuwa daraja muhimu linalowaunganisha mawakala wa utalii, waongoza watalii na wawekezaji wa ndani na wale kutoka masoko ya kimataifa, hatua inayofungua fursa mpya za biashara na ushirikiano.

Naye Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Uhifadhi na Mkuu wa Kanda ya Kaskazini TANAPA, Dkt. Beatrice Kessy, akizungumza kwa niaba ya Kamishna wa Uhifadhi TANAPA, alisema ushiriki wa TANAPA katika Karibu-KiliFair unalenga kuimarisha ushirikiano wa kimataifa, kujifunza mwenendo wa masoko ya utalii na uwekezaji pamoja na kupanua wigo wa fursa zinazopatikana katika Hifadhi za Taifa.

"Kupitia mikutano na majadiliano ya kibiashara yanayofanyika katika maonesho haya, TANAPA hujenga mahusiano mapya na wadau wa sekta ya utalii duniani, huku ikiendelea kutangaza vivutio vya kipekee vilivyopo katika Hifadhi za Taifa za Tanzania," alisema Dkt. Kessy.

Karibu-KiliFair imeendelea kuwa moja ya majukwaa makubwa ya utalii Afrika Mashariki, ikiiwezesha Tanzania kuonesha utajiri wake wa vivutio vya asili, kuimarisha ushirikiano na wadau wa sekta hiyo na kuvutia watalii pamoja na wawekezaji zaidi kutoka sehemu mbalimbali duniani.

WAZIRI WA FEDHA: BAJETI YA 2026/27 KUIJENGA TANZANIA YA DIRA YA 2050

  Na Eva Valerian, WF, Dodoma Serikali imesema Bajeti Kuu ya mwaka wa fedha 2026/27 ni ya kipekee kwa kuwa ndiyo bajeti ya kwanza itakayot...