Thursday, February 26, 2026

MHE. NDEJEMBI AITAKA PURA KUWAJENGEA UWEZO WATANZANIA KUSHIRIKI MRADI WA LNG

Na Mwandishi Wetu, Morogoro

Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratous Ndejembi, ameitaka Mamlaka ya Udhibiti Mkondo wa Juu wa Petroli (PURA) kuimarisha mipango yake katika ukusanyaji wa data sahihi, tathmini ya vitalu vya utafiti, na maandalizi ya Watanzania kushiriki kikamilifu katika miradi mikubwa ya kimkakati, ikiwemo mradi wa kuchakata gesi asilia kuwa kimiminika (LNG).

Mhe. Ndejembi ameyasema hayo wakati wa Kikao cha Tano cha Mkutano wa Pili wa Baraza la Wafanyakazi la PURA kilichofanyika mkoani Morogoro leo Februari 26, 2026.

 Amesisitiza kwamba sekta ya nishati ina nafasi ya kipekee katika kufanikisha malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, hivyo PURA inatakiwa kuhakikisha mipango yake inaendana na maono hayo.

“Sekta ya Nishati imetambuliwa kama moja ya vichocheo muhimu vya uchumi wa taifa. Taasisi zilizo chini ya Wizara ya Nishati zina wajibu mkubwa kuhakikisha upatikanaji endelevu, salama na wa uhakika wa rasilimali za mafuta na gesi asilia,” amesema Mhe. Ndejembi.

Aidha, Mhe. Ndejembi amewataka PURA kuongeza juhudi katika ukusanyaji na usimamizi wa data za kijiolojia na kufanya tafiti za awali, hasa ikizingatiwa kwamba maeneo makubwa ya nchi bado hayajafanyiwa utafiti wa kina.

“Takwimu sahihi ni msingi wa kuvutia uwekezaji na kuongeza ugunduzi wa rasilimali. Hatuwezi kuendeleza sekta bila taarifa za kutosha na tafiti madhubuti,” amesisitiza.

Waziri huyo pia ameagiza PURA kufanya tathmini ya kina katika vitalu vilivyopo, hususan katika ukanda wa Tanga, Ruvu, na maeneo mengine, ili kubaini iwapo wamiliki wa vitalu wanafanya shughuli za utafutaji kama inavyotakiwa.

 Ameongeza kuwa si vyema kwa vitalu kukaa mikononi mwa wawekezaji wasioendeleza shughuli za utafutaji, na mamlaka za udhibiti zinapaswa kuchukua hatua pale inapobainika hakuna maendeleo yanayofanyika kwa manufaa ya Taifa.

Akizungumzia mradi wa LNG, Mhe. Ndejembi amewataka PURA kuanza mapema kuandaa mkakati wa kujenga uwezo wa kitaasisi katika kusimamia mradi huo. 

Sambamba na hilo, amewahimiza kuandaa Watanzania kushiriki kikamilifu katika mnyororo wa thamani wa LNG, badala ya kusubiri utekelezaji wa mradi kuanza.

Awali katika kikao hicho, Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati anayeshughulikia Mafuta na Gesi Asilia, Dkt. James Mataragio, amewataka PURA kusimamia majukumu yake ya msingi kama yanavyoainishwa katika malengo ya kuanzishwa kwa taasisi hiyo.











MGODI WA ITRACOM WACHANGIA SHILINGI BILIONI 1.29 MAPATO YA SERIKALI MANYARA









📍Manyara

MGODI wa Itracom Fertilizer Limited unaojihusisha na uchimbaji na uchakataji wa madini ya phosphate uliopo  katika eneo la Vilima Vitatu, Wilayani Babati mkoani Manyara, umechangia Shilingi Bilioni 1.29 katika mapato ya Serikali tangu kuanza kwa shughuli zake mwaka 2023.

Hayo yamebainishwa na Mjiolojia, Waziri Mkupe, akizungumza kwa niaba ya Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Manyara, Godfrey Nyanda, ambapo amesema mapato hayo yametokana na mrabaha na ada ya ukaguzi wa madini.

Amesema tangu kuanza kwa uzalishaji, mgodi huo umezalisha jumla ya tani 69,929 za madini ya phosphate zenye thamani ya Shilingi Bilioni 36.99, ambazo zimeuzwa katika soko la ndani na nje ya nchi, hususan Nala mkoani Dodoma na nchini Burundi.

Kwa mujibu wa Mkupe, mchango huo umeimarisha ukusanyaji wa maduhuli ya Serikali na kuchochea maendeleo ya jamii inayozunguka mgodi kupitia utekelezaji wa miradi ya Uwajibikaji kwa Jamii (CSR).

Ameeleza kuwa tangu kuanza kwa shughuli zake, mgodi huo umechangia utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo ikiwemo ujenzi wa Shule ya Msingi Vilima Vitatu, nyumba za walimu, na upo katika hatua za awali za ujenzi wa bweni la shule ya sekondari ya wasichana.

Akifafanua kuhusu mauzo ya ndani, amesema kuanzia Desemba 16, 2023 hadi Februari 24, 2026, jumla ya tani 22,686 zenye thamani ya Shilingi bilioni 9.07 ziliuzwa kwenda Nala, Dodoma. Katika mauzo hayo, Serikali ilikusanya Shilingi milioni 90.74 kama mrabaha na kiasi kama hicho kama ada ya ukaguzi.

Kuhusu mauzo ya nje, amesema vibali 13 vilitolewa kwa ajili ya kusafirisha tani 47,243 za madini ya phosphate kwenda Burundi zenye thamani ya Shilingi Bilioni 27.92. Katika kipindi cha Septemba 4, 2024 hadi Februari 24, 2026, Serikali ilikusanya Shilingi milioni 837.64 kama mrabaha na Shilingi milioni 279.21 kama ada ya ukaguzi.

“Mgodi wa Itracom Fertilizer Limited umeendelea kudhihirisha kuwa sekta ya madini ya phosphate ni kichocheo muhimu cha ukuaji wa uchumi wa Mkoa wa Manyara kwa kuongeza mapato ya Serikali, kutoa ajira na kuimarisha maendeleo ya jamii,” amesema Mkupe.

Aidha, amewahimiza Watanzania kuchangamkia fursa za uwekezaji zilizopo mkoani humo, akibainisha kuwa pamoja na madini ya phosphate, Mkoa wa Manyara una rasilimali nyingine zikiwemo dhahabu, moonstone, green tourmaline, amethyst, green aventurine, limestone, azurite, chumvi, muscovite mica, feldspar na quartz crystal.

BARABARA YA MLIMA KITONGA KUWA NJIA NNE

 
📌Lengo ni kupunguza foleni, usalama

📌Ni Maelekezo ya Rais Samia

📌Waziri Ulega aagiza manunuzi yaanze mara moja

SERIKALI iko katika hatua za mwisho za kuanza upanuzi wa barabara ya Kitonga mkoani Iringa ambayo sasa itakuwa ya njia nne na yenye taa za barabarani. 

Waziri wa Ujenzi, Abdallah Ulega, amesema kuwa hatua hiyo ni uamuzi wa Rais Samia Suluhu Hassan ili kupunguza foleni na kuboresha usalama wa watumiaji barabara katika njia hiyo inayotumiwa na magari mengi. 

Waziri Ulega aliyekuwa katika ziara ya ukaguzi wa eneo la zaidi ya kilomita saba linalopaswa kupanuliwa, alisema barabara hiyo ni ya kimkakati kwa uchumi wa nchi kwa sababu inatumiwa pia na magari yanayokwenda katika nchi zinazotumia bandari ya Dar wa Salaam kubeba mizigo yao. 

“Barabara hii sasa itakuwa ya njia nne – mbili za kwenda na mbili za kurudi ambapo sasa ni njia mbili tu zinatumika. Na tutafunga taa kote ili kuhakikisha muda wote barabara inapitika muda wote, “ alisema Ulega. 

Akitoa picha ya ongezeko la uhitaji wa upanuzi wa barabara hiyo, Mbunge huyo wa Jimbo la Mkuranga alisema idadi ya magari yanayopita katika Barabara Kuu ya TANZAM imeongezeka kutoka magari 1,700 hadi 3,400 kwa siku, hali inayopelekea barabara hiyo kuzidiwa na wingi wa magari.

“Nimepokea mapendekezo kutoka kwa Meneja wa TANROADS Iringa ya kuhakikisha tunaondoa msongamano wa magari katika mlima Kitonga, na nimeelekeza kwa wataalamu wetu kupanua hii barabara kwa kilometa 7. Kwa sasa hivi barabara ina njia mbili kwa hiyo tutatanua na kuwa njia nne”, amesema Ulega.

Waziri Ulega ameongeza kuwa ni maelekezo ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwamba kila mradi wa barabara uende sambamba na uwekaji wa taa za barabarani ili kuhakikisha usalama wa watumiaji ikiwemo wananchi, wafanyabiashara na madereva pamoja na kuweka kingo pembezoni mwa barabara ili kuzuia magari yasianguke kwenye makorongo.

“Ninaagiza manunuzi yaanze mara moja ili kuhakikisha kwamba barabara hii inatanuliwa kwani ina umuhimu mkubwa katika uchumi wa nchi hivyo hatuwezi kuiacha katika hali hii na kutimiza pia maelekezo ya Mheshimiwa Rais kutatua changamoto zote”, ameongeza Waziri Ulega. 

Naye Mbunge wa Jimbo la Kilolo, Ritha Kabati, amesema barabara hiyo ni ya uchumi wa kimataifa hivyo ikitengenezwa itainua zaidi uchumi wa mkoa wa Iringa na Taifa kwa ujumla pamoja na kuwasaidia wananchi ambao hupata changamoto ya kufuata huduma za kijamii ikiwemo matibabu Iringa mjini. 

Kwa upande wake Meneja wa TANROADS mkoa wa Iringa Eng. Yudas Msangi amesema gharama ya upanuzi wa kilometa 7 wa njia mbili katika barabara hiyo ni bilioni 59.2 na ukarabati wa njia mbili zilizopo ni bilioni 16.2.







Wednesday, February 25, 2026

WAZIRI SANGU: MAHUSIANO MEMA MSINGI WA UMOJA WA TAIFA







✅ Ahimiza Mshikamano katika kujenga Tanzania Imara

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano, Mhe. Deus Clement Sangu amesisitiza umuhimu wa kudumisha mahusiano mema ili kuimarisha umoja wa Taifa na kuchochea maendeleo endelevu nchini.

‎Mhe. Sangu amesema hayo wakati wa ufunguzi wa Kikao cha Wadau wa Mahusiano kilichofanyika tarehe Februari 24, 2026 katika Halmashauri ya Sumbawanga mkoani Rukwa.

Aidha, amesema kuwa uwepo wa mahusiano imara miongoni mwa Watanzania ni nguzo muhimu ya kudumisha amani, umoja na mshikamano wa Taifa.

‎Ameongeza kuwa, Serikali itaendelea kuratibu na kuimarisha mahusiano baina yake na makundi mbalimbali ya kijamii ili kuhakikisha nchi inaendelea kuwa kielelezo cha utulivu barani Afrika.

‎Amesema kuwa, sifa ya Mtanzania ambayo ni miongoni mwa sifa kuu zinazomtambulisha ni mahusiano mazuri yanayobebwa na misingi mikuu mitatu, msingi wa kwanza ni mila na desturi za nchi, ambapo, Nchi yetu ina historia ndefu ya ushirikiano na utani kati ya makabila mbalimbali, mifumo ya kisera, kisheria na miongozo mbalimbali ya mahusiano na , umoja na mshikamano ulioachwa na waasisi wa Taifa.

‎Vilevile, amesisitiza kuwa ni wajibu wa kila kundi la kijamii kuheshimu na kutekeleza sera na sheria hizo kwa vitendo ili kuendeleza mshikamano wa Taifa.

‎Kikao hicho cha Mahusiano kililenga kukutana na wadau mbalimbali wa kijamii ili kujengeana uelewa wa pamoja kuhusu dhana ya mahusiano na kutoa fursa kwa wadau kutoa maoni na mapendekezo ya kuimarisha mahusiano nchini

Tuesday, February 24, 2026

TRENI YA MWENDOKASI KUFIKA MWANZA 2028

 



Waziri wa Uchukuzi, Profesa Makame Mbarawa (wa pili kutoka kulia),akizungumza baada ya kukagua daraja la kupitisha magari chn ya reli, leo.

Na Baltazar Mashaka, Mwanza

WAZIRI wa Uchukuzi, Makame Mbarawa, ameridhishwa na kasi ya ujenzi wa mradi wa reli ya kisasa (SGR) kipande cha Mwanza–Isaka chenye urefu wa kilomita 341, unaotarajiwa kukamilika mwaka 2028.

Akizungumza katika eneo la Fella, wilayani Misungwi, leo Februari 24, 2026, baada ya kukagua maendeleo ya mradi huo, Profesa Mbarawa alisema ujenzi wa mradi huo umefikia asilimia 68 na unaendelea vizuri.

Alisema mradi huo wa kimkakati unaogharimu dola za Marekani bilioni 1.326 (takribani shilingi trilioni 3.06), ni mkubwa na kielelezo cha kujivunia, huku akimshukuru Rais Dk.Samia Suluhu Hassan kwa kusimamia utekelezaji wake, akieleza kuwa wakati anaingia madarakani mradi ulikuwa hatua sifuri sasa umefikia hatua kubwa.

Kwa mujibu Profesa Mbarawa, jengo la stesheni kuu ya Mwanza lenye uwezo wa kuchukua abiria 900 pamoja na majengo mawili ya biashara ujenzi unaendelea vyema, miundombinu ikiwemo madaraja ikifikia takribani asilimia 90, huku ulazaji wa mataruma ukiwa asilimia 53.

Alisisitiza kuwa serikali itaendelea kutoa fedha ili kuhakikisha mradi huo unakamilika kwa viwango vya kimataifa na kwa kuzingatia thamani ya fedha, una uwezo wa kuhimili changamoto mbalimbali ikiwemo matetemeko ya ardhi.

Profesa Mbarawa aliwashukuru wananchi wa Mwanza kwa shughuli za maendeleo na kuunga mkono mradi huo, akibainisha kuwa eneo lililosalia na changamoto ni Mkuyuni ambako kuna makazi yanayochelewesha ulipuaji wa miamba.

Hata hivyo, alisema kuwa, mkandarasi ameahidi kukamilisha kazi hiyo ifikapo Agosti mwaka huu na kuanza uwekaji wa njia ya reli huku akionya waliopata kazi katika mrad huo wasifanye mambo ya ovyo ikiwemo wizi wa malighafi ya saruji, nondo na vyuma, wataakuwa wanawaiba Watanzania si mkandarasi.

Alisema kukamilika kwa mradi huo kutafungua fursa mbalimbali zikiwemo ujenzi wa Bandari Kavu ya kuhifadhi mizigo kutoka Bandari ya Dar es Salaam, kubadilisha vichwa vya treni na mabehewa, na kuchochea shughuli za kiuchumi katika eneo la Misungwi, aliwataka wananchi kutunza mali za mradi na kuepuka vitendo vya wizi wa vifaa vya ujenzi.

Mbunge wa Misungwi, Silvery Salvatory (CCM), alisema reli ya SGR itaongeza usafirishaji wa mizigo ya ndani na kutoka nchi jirani, hivyo kuchochea uchumi jumuishi kama ilivyoainishwa katika Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, alitoa wito kwa wananchi kujipanga kunufaika na fursa zitakazotokana na miradi hiyo.

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Misungwi, Johari Samizi, alisema miradi ya SGR, Bandari Kavu na Daraja la JPM itaimarisha uchumi wa wilaya hiyo na kuwataka wananchi kupanga matumizi bora ya ardhi ili kuepuka migogoro na madai ya fidia baadaye.

Naye Mkuu wa Wilaya ya Nyamagana, Amina Makilagi, kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Said Mtanda, alisema kukamilika kwa reli ya SGR kutaufungua mkoa wa Mwanza kiuchumi na kuongeza fursa za uwekezaji.

Awali, Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Reli Tanzania (TRC), Mhandisi Machibya Masanja, alisema eneo la Misungwi limepangwa kuwa kitovu cha shughuli za kilojistiki, na kuwataka wawekezaji kuchangamkia fursa za kuwekeza katika Bandari Kavu, ambayo serikali imeiachia sekta binafsi kuendesha.

Alisisitiza kuwa lengo ni kuhakikisha ifikapo mwaka 2028 treni ya SGR inasafiri kutoka Dar es Salaam hadi Mwanza ikiwa na mizigo na abiria, na hivyo kuimarisha uchumi wa taifa.







REA YAANZA USAMBAZAJI WA MAJIKO BANIFU 6,692 KATIKA MKOA WA SINGIDA

 Ilongero-Singida

Wakala wa Nishati Vijijini imeanza utekelezaji wa mpango mkakati wa kitaifa wa nishati safi ya kupikia ili kufikia lengo la zaidi ya asilimia themanini 80% ya watanzania ifikapo mwaka 2034 wawe wanatumia nishati safi ya kupikia nishati ambayo ni salama kwa mtumiaji na rafiki kwa mazingira.

Akizungumza wakati wa ugawaji wa majiko katika Kata na Tarafa ya Irongero katika Wilaya ya Singida leo tarehe 24 Februari 2026 Mhandisi wa miradi ya REA Mkoani Singida, Mha.Nathan Msanze amesema kuwa Wakala ya Nishati Vijijini-REA katika mkoa huo umeanza usambazaji wa majiko banifu 6,692.

Amesema kuwa majiko hayo yatagawiwa kwa wananchi kwa bei ya ruzuku katika wilaya zote na Halmashauri za mkoa huo ambazo ni Ikungi majiko 1,116, Iramba 1,116, Itigi 1,115, Manyoni 1,115, Mkalama 1,115 na Singida 1,115.

Mhandisi Nathan amesema kuwa mradi huo unahusisha usambazaji wa majiko banifu yanayotumia kuni na mkaa kidogo ili kupunguza matumizi ya vyanzo hivyo vya nishati pamoja na athari za moshi zitokanazo na matumizi katika majiko ya kawaida. Katika mkakati huo Wakala wa Nishati Vijijini umeandaa mpango wa uuzwaji wa majiko banifu 200,000 kwa bei ya ruzuku yenye ufanisi mkubwa katika utumiaji wake.

Amesema kuwa mikataba hiyo ilisainiwa tarehe 9 Mei , 2025 na itatekelezwa ndani ya miezi 15. Gharama ya mradi ni TZS 340,288,200 kwa mkoa wa Singida na ruzuku inayotolewa na Wakala wa Nishati Vijijini ni TZS 289,230,508.47 sawa na asilimia 85 ya gharama ya mradi. Wananchi wanachangia TZS 51,057,691.53 sawa na asilimia 15 ya gharama ya mradi.

Mtoa huduma ni Tango Energy Limited ambapo jumla ya majiko banifu 6,692 yatauzwa kwa wananchi kwa bei ya ruzuku. Gharama ya jiko moja ni TZS 50,847.46 lakini serikali imetoa ruzuku ya asilimia 85 hivyo mwananchi atanunua kwa gharama ya TZS 7,600

Kwa upande wao wananchi ambao wamenufaika na majiko hayo katika kata ya Ilongero wakiongozwa na Diwani wa Kata hiyo Mhe Issa Mwiru kwa kauli moja wamempongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe Dkt Samia Suluhu Hassan kwa kuamua kutoa majiko bunifu kwa bei ya ruzuku ambayo itawanufaisha wananchi wote.







PROF. SHEMDOE APIGA MARUFUKU UHAMISHO WA WATUMISHI WENYE CHANGAMOTO ZA KINIDHAMU

 


Na OWM – TAMISEMI, Muheza

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu -TAMISEMI Mhe. Prof. Riziki Shemdoe, amewaelekeza Makatibu Tawala wa Mikoa na Wakurugenzi wa Halmashauri kutowahamisha au kuwaombea uhamisho watumishi wanaobainika kuwa na changamoto za kinidhamu katika Mamlaka za Mikoa na Serikali za Mitaa, na badala yake kuchukua hatua kwa kuwafungulia mashauri ya kinidhamu.

Prof. Shemdoe ametoa maelekezo hayo hivi karibuni akiwa katika kikao kazi na watumishi wa Muheza kilicholenga kuhimiza uwajibikaji katika usimamizi na matumizi ya fedha za miradi ya maendeleo, ikiwa ni utekelezaji wa maelekezo ya Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba, ambaye wakati wa ziara yake wilayani Muheza alibaini ubadhirifu wa fedha katika Mradi wa Jengo la Utawala na kumuelekeza Prof. Shemdoe na Waziri wa Ofisi ya Rais UTUMISHI na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete kuchukua hatua.

Aidha, Prof. Shemdoe amewaeleleza viongozi hao, kutotumia fedha au vifungu vya bajeti ya maendeleo kufanya malipo ya stahiki za watumishi, na kwamba fedha za mapato ya ndani zinazotengwa na Halmashauri kwa ajili ya miradi ya maendeleo zitumike kwenye shughuli zilizopangwa na si vinginevyo.

Sanjali na hayo, Prof. Shemdoe amewataka Wakurugenzi wa Halmashauri kuendelea kusimamia kikamilifu upatikanaji wa rasilimali fedha na matumizi sahihi ya rasilimali hizo ili kuwaletea wananchi maendeleo endelevu na tabasamu la kudumu.

Vivile, amewataka Makatibu Tawala wa Mikoa kufanya uchambuzi wa matumizi wa fedha za miradi ya maendeleo, pamoja na zinazotoka Serikali kuu na za mapato ya ndani katika kipindi cha kuanzia mwaka wa fedha 2024/25 hadi sasa, “Kama ikibainika kuna Halmashauri yoyote ina ubadhilifu na kuna watuhumiwa wa ubadhirifu huo mimi na Mhe. Ridhiwani Kikwete tutachukua hatua,” amesisitiza Prof. Shemdoe.

Hatua hiyo ya Prof. Shemdoe ni sehemu ya jitihada za kuunga mkono kwa vitendo azma ya Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kutaka fedha za miradi ya maendeleo kutumika katika kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi kupitia ujenzi wa miundombinu bora afya, elimu na barabara.


MHE. NDEJEMBI AITAKA PURA KUWAJENGEA UWEZO WATANZANIA KUSHIRIKI MRADI WA LNG

Na Mwandishi Wetu, Morogoro Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratous Ndejembi, ameitaka Mamlaka ya Udhibiti Mkondo wa Juu wa Petroli (PURA) kuimar...