Wednesday, July 08, 2026

MBUNGE WA BUNGE LA NORWAY AVUTIWA NA VIVUTIO VYA SERENGETI, AIKARIBISHA DUNIA KUTEMBELEA TANZANIA


Mbunge wa Bunge la Norway, Mhe. Himanshu Gulati, akiongozana na mwenyeji wake, Mbunge wa Jimbo la Buchosa, Mhe. Eric Shigongo, ametembelea Hifadhi ya Taifa Serengeti na kujionea vivutio vya kipekee vya utalii, wanyamapori mbalimbali pamoja na mandhari ya kuvutia inayoifanya Tanzania kuwa miongoni mwa nchi zinazoongoza kwa utalii duniani.

Akizungumza baada ya ziara hiyo, Mhe. Gulati alisema amefurahishwa na ubora wa vivutio vya utalii nchini pamoja na juhudi kubwa zinazofanywa na Serikali ya Tanzania katika kuhifadhi rasilimali za asili na wanyamapori kwa manufaa ya vizazi vya sasa na vijavyo.

Aidha, amewahamasisha wananchi wa Norway na mataifa mengine duniani kuitembelea Tanzania ili kujionea uzuri wa Hifadhi za Taifa, urithi wa asili na uzoefu wa kipekee unaopatikana katika vivutio vya utalii vya nchi hii.

"Tanzania ni nchi yenye vivutio vya kipekee na mazingira ya kuvutia. Kila mtu anapaswa kupata nafasi ya kuitembelea na kujionea uzuri wake," alisema Mhe. Gulati.

WAZIRI MKUU AKUTANA NA MAKAMU WA RAIS WA KAMPUNI YA ALSTOM




▪️Yaonesha nia ya kushirikiana na Serikali katika usafiri ya Mijini.

▪️Dkt. Mwigulu awahakikishia mazingira bora ya uwekezaji

WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba, amekutana na Makamu wa Rais wa Kampuni ya ALSTOM ya nchini Ufaransa, Philippe Deller ambapo wamejadiliana kuhusu fursa za uwekezaji katika sekta ya miundombinu ya usafiri nchini Tanzania.

Katika mazungumzo hayo, Dkt. Mwigulu Nchemba aliikaribisha ALSTOM kuwekeza nchini, akieleza kuwa Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan inaendelea kuweka mazingira wezeshi kwa wawekezaji na kutekeleza mageuzi yanayolenga kuifanya Tanzania kuwa kitovu cha biashara, usafiri na uwekezaji katika ukanda wa Afrika Mashariki.

Kwa Upande wake Bw. Phillepe alieleza nia ya kampuni hiyo kushirikiana na Serikali ya Tanzania katika utekelezaji wa miradi ya kimkakati ya usafiri wa mijini.

Kampuni hiyo imeonesha utayari wa kuwekeza katika ujenzi wa mifumo ya usafiri wa haraka na miundombinu ya kisasa yenye lengo la kupunguza msongamano wa magari katika Jiji la Dar es Salaam, huku ikitazama pia fursa za utekelezaji wa miradi kama hiyo katika majiji ya Mwanza, Mbeya na Arusha.

Miradi hiyo inatarajiwa kuongeza ufanisi wa usafiri wa mijini, kupunguza muda wa safari, kuimarisha shughuli za biashara na uwekezaji, pamoja na kuchochea ukuaji wa uchumi na kuboresha maisha ya wananchi kupitia matumizi ya teknolojia za kisasa.

Mazungumzo hayo ni sehemu ya jitihada za Serikali za kuimarisha ushirikiano na kampuni kubwa za kimataifa ili kuleta teknolojia, utaalamu na mitaji inayochochea maendeleo ya miundombinu na uchumi wa Taifa.

Kampuni ya ALSTOM, ina uzoefu mkubwa katika kubuni, kujenga na kuendesha mifumo ya kisasa ya usafiri wa umma ikiwemo reli za kisasa, treni za mwendo kasi, metro, tram na teknolojia za usimamizi wa usafiri.

Monday, July 06, 2026

RAIS SAMIA AMTEMBELEA PACOME, AMPATIA POLE NA KUMTAKIA AFYA NJEMA

 



Dar es Salaam – Mchezaji wa klabu ya Yanga, Pacome Zouzoua, amepata faraja ya kipekee baada ya kutembelewa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, alipokuwa akipatiwa matibabu katika Hospitali ya Aga Khan, jijini Dar es Salaam.

Rais Samia alikuwa hospitalini hapo kwa ajili ya kumjulia hali Sheikh Rashid Hamad Othman, lakini alipojulishwa kuwa Pacome amelazwa katika chumba jirani akipatiwa matibabu kufuatia majeraha aliyoyapata kwenye mchezo wa Ligi Kuu ya NBC dhidi ya JKT Tanzania, alitumia fursa hiyo kumtembelea na kumpa pole.

Hatua hiyo imeonesha moyo wa upendo na kujali kwa viongozi wakuu wa Taifa kwa wanamichezo, ikisisitiza nafasi muhimu ambayo michezo inaendelea kuwa nayo katika kuunganisha Watanzania.

Mashabiki wa soka nchini wanaendelea kumuombea Pacome apone haraka na kurejea uwanjani kuendelea kuonesha kipaji chake na kuiburudisha Yanga pamoja na wapenzi wa soka kwa ujumla.

Tunamtakia Pacome Zouzoua nafuu ya haraka na kurejea uwanjani akiwa imara zaidi. 💚⚽

RAIS MWINYI ATOA SH. MILIONI 200 KWA KITUO CHA IRSHAAD LUSHOTO, ARIDHIA MAOMBI YA PROF. SHEMDOE

 










Na OWM – TAMISEMI, Lushoto

Rais wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, ametoa Shilingi Milioni 200 kwa ajili ya kuendeleza Kituo cha Elimu ya Kiislamu Irshaad (Irshaad Islamic Centre) kilichopo Lushoto, Mkoa wa Tanga, kufuatia ombi lililotolewa na Mbunge wa Jimbo la Lushoto na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, Mhe. Prof. Riziki Shemdoe.

Msaada huo utasaidia kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo katika kituo hicho, ikiwemo kuboresha Chuo cha Ufundi, kujenga madrasa ya kisasa, nyumba za walimu, hospitali, ukumbi wa mikutano, jengo la wageni pamoja na bustani ya kisasa, hatua inayotarajiwa kuongeza ubora wa elimu na huduma za kijamii kwa wananchi wa Lushoto na maeneo jirani.

Prof. Shemdoe aliwasilisha ombi hilo wakati wa Sherehe ya Maulidi ya Kumswalia Mtume Muhammad (S.A.W.) zilizofanyika Julai 5, 2026 katika Kituo cha Irshaad Islamic Centre, ambapo Mhe. Dkt. Hussein Mwinyi alikuwa Mgeni Rasmi.

Katika tukio hilo, Rais Mwinyi pia alikubali ombi la Sheikh Sharrif Hussein Ahmad Badawiyy la kuwa Mlezi wa Kituo cha Irshaad Islamic Centre, akiahidi kuendelea kushirikiana na viongozi na wadau mbalimbali katika kukiendeleza ili kiwe kitovu cha elimu bora, maadili mema na maendeleo ya jamii.

Aidha, Rais Mwinyi aliridhia ombi la kutambua mchango wa Hayati Alhaji Ali Hassan Mwinyi kwa kuruhusu bustani itakayojengwa ndani ya Chuo cha Ufundi cha kituo hicho kuitwa jina lake, ikiwa ni sehemu ya kuenzi mchango wake mkubwa katika maendeleo ya taasisi hiyo.

Wito wa Prof. Shemdoe uliungwa mkono na viongozi mbalimbali waliochangia kwa hiari yao, akiwemo yeye mwenyewe aliyetoa Shilingi Milioni 20, Mkuu wa Mkoa wa Tanga Dkt. Batilda Burian (Milioni 5), Mkuu wa Mkoa wa Morogoro Mhe. Adam Malima (Milioni 5), Mbunge wa Bumbuli Mhandisi Ramadhani Hamza (Milioni 5), Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Tanga Bw. Rajab Abdallah (Milioni 3) na Mbunge wa Afrika Mashariki Dkt. Abdullah Makame (Milioni 5), na kufanya jumla ya michango kufikia Shilingi Milioni 248.

Akizungumza baada ya hafla hiyo, Prof. Shemdoe alimshukuru Rais Mwinyi kwa kukubali ombi hilo, akieleza kuwa msaada huo utakuwa chachu ya kuimarisha elimu, kukuza ustawi wa jamii na kuboresha huduma zinazotolewa na Kituo cha Irshaad.

Wananchi na viongozi waliohudhuria hafla hiyo walimpongeza Rais Mwinyi kwa uamuzi huo, wakieleza kuwa utaacha alama ya kudumu katika maendeleo ya elimu, ujuzi na huduma za kijamii kwa vizazi vya sasa na vijavyo katika Wilaya ya Lushoto.

Saturday, July 04, 2026

UCHUMI WA TAIFA UNATEGEMEA UHIFADHI ASEMA MCHECHU AKIZINDUA GREAT RUAHA MARATHON 2026










RUAHA, IRINGA – Msajili wa Hazina na Mlezi wa Great Ruaha Marathon, Bw. Nehemiah Mchechu, ambaye alimwakilisha Mgeni Rasmi, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mwigulu Nchemba, amesema kuwa uhifadhi wa mazingira ni nguzo muhimu ya ukuaji wa uchumi wa Taifa na ustawi wa wananchi.

Akizindua rasmi Great Ruaha Marathon 2026 leo Julai 4, 2026 katika Hifadhi ya Taifa Ruaha, Bw. Mchechu alisema Mto Ruaha Mkuu ni moja ya vyanzo muhimu vya uhai nchini, ukiwezesha shughuli za kilimo, ufugaji, uzalishaji wa umeme pamoja na kuhifadhi mfumo wa ikolojia wa Hifadhi ya Taifa Ruaha.

Alisisitiza kuwa kulinda mazingira na vyanzo vya maji si jukumu la Serikali pekee, bali ni wajibu wa kila Mtanzania kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.

"Tunataka Watanzania wengi zaidi watembelee hifadhi zetu, wajivunie urithi tulionao na wawe mabalozi wa utalii wa nchi yao," amesema Mchechu.

Kwa upande wake, Kamishna wa Uhifadhi wa TANAPA, Massana Gibril Mwishawa, amesema utalii wa michezo umeendelea kuwa nyenzo muhimu ya kuitangaza Tanzania duniani, kuvutia watalii na wawekezaji, pamoja na kukuza biashara na uchumi wa Taifa.

Ameeleza kuwa TANAPA imejipanga kuendeleza utalii wa michezo kama zao jipya la kimkakati litakaloongeza mchango wa sekta ya utalii katika maendeleo ya nchi.

Naye Mratibu wa Great Ruaha Marathon, Hamim Kilahama, amesema mbio hizo si mashindano ya riadha pekee bali ni jukwaa la kuhamasisha jamii kulinda mazingira, kuhifadhi vyanzo vya maji vya Mto Ruaha Mkuu na kuitangaza Kanda ya Kusini kama kitovu cha utalii.

Amebainisha kuwa kwa mwaka wa tano mfululizo, Great Ruaha Marathon imeendelea kufungua fursa mpya za kuitangaza Hifadhi ya Taifa Ruaha kupitia utalii wa michezo, huku ikichochea maendeleo ya jamii na uchumi wa maeneo yanayozunguka hifadhi hiyo.

Hifadhi ya Taifa Ruaha, ambayo ni miongoni mwa hifadhi kubwa zaidi barani Afrika, inaendelea kuwa hazina ya kipekee ya utalii ikiwa na wanyamapori wengi wakiwemo tembo, simba, chui, mbwa mwitu wa porini, twiga, nyati na mamia ya aina za ndege wanaovutia wageni kutoka duniani kote.

Great Ruaha Marathon imeendelea kuthibitisha kuwa michezo, uhifadhi na utalii vinaweza kwenda sambamba katika kujenga uchumi imara, kulinda rasilimali za Taifa na kuitangaza Tanzania kimataifa.

 

MAKAMU WA RAIS DKT. NCHIMBI AMTEMBELEA JAJI MSTAAFU JOSEPH WARIOBA, AMJULIA HALI

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi amemtembelea na kumjulia hali, aliyewahi kuwa Waziri Mkuu na Makamu wa Kwanza wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Jaji. Joseph Sinde Warioba, katika makazi yake, Mbezi Juu Jijini Dar es Salaam.



Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi amemtembelea na kumjulia hali, aliyewahi kuwa Waziri Mkuu na Makamu wa Kwanza wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Jaji. Joseph Sinde Warioba, katika makazi yake, Mbezi Juu Jijini Dar es Salaam.

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi, amemtembelea na kumjulia hali aliyekuwa Waziri Mkuu na Makamu wa Kwanza wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Jaji Mstaafu Joseph Sinde Warioba, katika makazi yake yaliyopo Mbezi Juu, jijini Dar es Salaam.

Ziara hiyo imeonesha heshima na kuthamini mchango mkubwa wa viongozi wastaafu walioitumikia nchi kwa uadilifu na uzalendo. Katika mazungumzo yao, viongozi hao walipata fursa ya kubadilishana mawazo kuhusu masuala mbalimbali yanayohusu maendeleo ya Taifa na ustawi wa wananchi.

Hatua ya Makamu wa Rais kumtembelea Jaji Mstaafu Warioba imepokelewa kama ishara ya kuenzi utumishi wa viongozi walioweka msingi imara wa uongozi na utawala nchini, huku ikidhihirisha umuhimu wa kuendelea kuwajali na kuwathamini wazee wa Taifa kwa mchango wao katika kujenga Tanzania ya leo.


Wednesday, July 01, 2026

RAIS DKT. SAMIA AONGOZA MAADHIMISHO YA MIAKA 30 YA TRA

 
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye Maadhimisho ya miaka 30 ya kuanzishwa kwa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) katika ukumbi wa Mlimani City Jijini Dar es Salaam.



Viongozi, wafanyabiashara pamoja na wageni mbalimbali wakiwa kwenye Maadhimisho ya miaka 30 Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) katika ukumbi wa Mlimani City Jijini Dar es Salaam, tarehe 01 Julai, 2026



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akisikiliza historia ya miaka 30 ya Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) baada ya kuwasili katika ukumbi wa Mlimani City Jijini Dar es Salaam, tarehe 01 Julai, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, leo Julai 1, 2026, ameongoza Maadhimisho ya Miaka 30 ya kuanzishwa kwa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) yaliyofanyika katika Ukumbi wa Mlimani City, jijini Dar es Salaam.

Mara baada ya kuwasili katika ukumbi huo, Rais Samia alitembelea maonesho maalumu yaliyoandaliwa na TRA na kupata maelezo kuhusu historia ya mamlaka hiyo, mafanikio yaliyopatikana katika kipindi cha miaka 30 pamoja na mchango wake katika kuongeza mapato ya Serikali na kuchochea maendeleo ya kiuchumi nchini.

Maadhimisho hayo yamewakutanisha viongozi wa Serikali, taasisi za umma na binafsi, wadau wa kodi pamoja na washirika wa maendeleo kwa lengo la kuadhimisha mafanikio ya TRA tangu kuanzishwa kwake na kujadili mikakati ya kuendelea kuimarisha ukusanyaji wa mapato kwa maendeleo endelevu ya Taifa.

Kwa kipindi cha miaka 30, TRA imeendelea kuwa mhimili muhimu katika ukusanyaji wa mapato ya ndani, hatua iliyowezesha Serikali kugharamia utekelezaji wa miradi mikubwa ya maendeleo katika sekta mbalimbali zikiwemo elimu, afya, miundombinu, maji na huduma nyingine za kijamii.

Maadhimisho hayo pia yametoa fursa ya kutafakari mafanikio yaliyofikiwa, changamoto zilizopo na kuweka mikakati ya kuifanya TRA iendelee kuwa taasisi imara, bunifu na inayotoa huduma bora kwa walipakodi, sambamba na kuimarisha uchumi wa Taifa.

MBUNGE WA BUNGE LA NORWAY AVUTIWA NA VIVUTIO VYA SERENGETI, AIKARIBISHA DUNIA KUTEMBELEA TANZANIA

Mbunge wa Bunge la Norway, Mhe. Himanshu Gulati , akiongozana na mwenyeji wake, Mbunge wa Jimbo la Buchosa, Mhe. Eric Shigongo , ametembelea...