Sunday, March 22, 2026

UWEKEZAJI USAFIRI KANDA YA ZIWA KUCHOCHEA UCHUMI, WAWEKEZAJI WAHIMIZWA KUTUMIA FURSA


 Na Baltazar Mashaka, Mwanza

Serikali imesema uwekezaji mkubwa unaoendelea kufanywa katika sekta ya usafiri na usafirishaji Kanda ya Ziwa utachochea ukuaji wa uchumi wa Tanzania na nchi jirani za Ukanda wa Maziwa Makuu, huku ikiwahimiza wawekezaji wa sekta binafsi kutumia fursa zinazojitokeza katika eneo hilo.

 Kauli hiyo ilitolewa leo, jijini Mwanza na Msemaji Mkuu wa Serikali na Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Gerson Msigwa, alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari kuhusu maendeleo ya miradi mbalimbali ya serikali.

Msigwa alisema ujenzi wa meli kubwa ya kisasa ya New MV Mwanza ni sehemu ya juhudi za serikali kuboresha miundombinu ya usafiri katika Ziwa Victoria, hatua itakayofungua fursa mpya za kiuchumi hususan katika sekta ya utalii na biashara.

Alisisitiza kuwa serikali imeweka mazingira wezeshi kwa wawekezaji, hivyo wadau wa utalii wanapaswa kujitokeza kuwekeza ili kunufaika na ongezeko la shughuli za kiuchumi katika Kanda ya Ziwa.

Msemaji Mkuu huyo wa Serikali alisema, meli hiyo yenye uwezo wa kubeba abiria 1,200 na tani 400 za mizigo itakuza biashara na uchumi, itaimarisha usafiri wa majini kati ya Mwanza na miji ya Jinja na Port Bell nchini Uganda pamoja na Kisumu nchini Kenya.

Kwa mujibu wa Msigwa, hatua hiyo itaongeza mzunguko wa biashara na kukuza uchumi wa bidhaa mbalimbali zikiwemo pamba, madini, samaki, nyama na maziwa, huku akionya kuwa serikali haitaridhika kuona uwekezaji huo mkubwa unakosa tija.

Akizungumzia mradi wa reli ya kisasa ya kiwango cha kimataifa (SGR), Msigwa alisema ni uwekezaji mkubwa wenye thamani ya dola za Marekani bilioni 12 unaolenga kuimarisha uchumi wa taifa na nchi jirani.

Alieleza kuwa ujenzi unaendelea katika vipande mbalimbali, huku lengo likiwa ni kufikisha reli hiyo Mwanza ifikapo mwaka 2028 ili kurahisisha usafirishaji wa mizigo na kuongeza ufanisi wa biashara za kikanda.

Aidha, alisema serikali inaendelea na mipango ya kujenga reli ya kisasa inayotumia umeme yenye uwezo wa kusafirisha tani 10,000 za mizigo kutoka Bandari ya Dar es Salaam pamoja na meli nyingine ya mizigo katika Ziwa Victoria na Ziwa Tanganyika.

Alibainisha kuwa uwekezaji huo wa kimkakati utaongeza matumizi ya reli, kukuza biashara na kuchochea mageuzi ya kiuchumi kwa wananchi, huku Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 ikilenga kufikia pato la mtu mmoja mmoja la dola 7,000 kwa mchango mkubwa wa sekta binafsi.

MAKAMU WA RAIS AONGOZA KILELE CHA WIKI YA MAJI 2026, ATOA WITO KUIMARISHA ULINZI WA VYANZO VYA MAJI NCHINI











Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Emmanuel Nchimbi, ametoa wito kwa mamlaka husika pamoja na wananchi wote kuweka kipaumbele katika utunzaji na ulinzi wa vyanzo vya maji, akisisitiza kuwa rasilimali hiyo ni msingi wa maendeleo endelevu na urithi muhimu kwa vizazi vijavyo.

Makamu wa Rais aliyasema hayo alipomwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, katika Maadhimisho ya Kilele cha Wiki ya Maji 2026 sambamba na Siku ya Maji Duniani, yaliyofanyika katika Viwanja vya Mkwawa mkoani Morogoro tarehe 22 Machi 2026.

Amesisitiza umuhimu wa kufanya uwekezaji wa kimkakati unaolenga kulinda na kuongeza vyanzo vya maji ili kuhakikisha upatikanaji endelevu wa huduma hiyo muhimu kwa wananchi wote. Aidha, ametoa rai kwa wizara na taasisi za umma kujenga ushirikiano thabiti utakaowezesha kukabiliana kwa pamoja na changamoto zinazoikabili sekta ya maji nchini.

Katika hatua ya kuimarisha sekta hiyo, Makamu wa Rais amezitaka mamlaka za maji kubuni vyanzo mbadala vya mapato ili kuongeza ufanisi wa utekelezaji wa miradi. Ameipongeza Mamlaka ya Maji Tanga kwa kutumia mfumo wa hati fungani (bonds) kugharamia miradi ya maji, akieleza kuwa ubunifu huo ni mfano wa kuigwa kitaifa.

Vilevile, amesisitiza umuhimu wa sekta binafsi kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya miradi ya maji, akieleza kuwa ushirikiano kati ya serikali na wadau binafsi ni nguzo muhimu ya kufanikisha upatikanaji wa huduma bora na endelevu.

Makamu wa Rais pia ameelekeza juhudi zaidi katika utekelezaji wa Mpango wa Gridi ya Taifa ya Maji, akibainisha kuwa kukamilika kwake kutakuwa suluhisho la kudumu la changamoto ya maji nchini. Aidha, ameitaka Wizara ya Maji kuhakikisha ufungaji wa mita za maji unaimarishwa ili kudhibiti upotevu na kuongeza uwajibikaji kwa watumiaji.

Akizungumzia dira ya maendeleo ya taifa, amesema kuwa Dira ya Maendeleo 2050 inalenga kuifanya Tanzania kuwa nchi ya kipato cha kati ngazi ya juu, huku ikikabiliwa na ongezeko la idadi ya watu litakalofikia takriban milioni 118. Alisisitiza kuwa hali hiyo inahitaji mipango madhubuti ya kuhakikisha upatikanaji wa huduma muhimu za kijamii ikiwemo maji safi na salama.

Kwa mujibu wa takwimu za Sera ya Taifa ya Maji ya Mwaka 2002 (Toleo la 2025), upatikanaji wa maji umeendelea kuimarika ambapo huduma hiyo imefikia wastani wa asilimia 85.2 vijijini na asilimia 92.5 mijini. Jumla ya vijiji 10,758 tayari vimefikiwa na huduma hiyo, huku jitihada maalum zikiendelea kuhakikisha vijiji vilivyosalia vinaunganishwa na huduma ya maji.

Kwa upande wake, Waziri wa Maji, Jumaa Aweso, alimshukuru Rais kwa kuwezesha utekelezaji wa miradi ya maji kwa ufanisi, akiahidi kuwa wizara hiyo itaendelea kuhakikisha wananchi wanapata huduma ya maji safi na salama bila vikwazo.

Katika kuimarisha matumizi ya teknolojia, Makamu wa Rais alizindua Mfumo wa Utabiri wa Kiasi cha Maji katika mito nchini, katika eneo la Bwawa la Mindu mjini Morogoro. Mfumo huo unatarajiwa kuboresha upatikanaji wa taarifa sahihi za kiwango cha maji na kusaidia kupanga matumizi na uhifadhi wake kwa ufanisi zaidi.

Kama sehemu ya maadhimisho hayo, Makamu wa Rais pia alipanda miti rafiki wa maji katika eneo la chanzo hicho, akihamasisha utunzaji wa mazingira kama nguzo muhimu ya kulinda rasilimali za maji.

Maadhimisho ya mwaka huu yalibebwa na kaulimbiu “Maji na Usawa wa Kijinsia,” ikilenga kuangazia uhusiano kati ya upatikanaji wa maji safi na usawa wa kijinsia katika jamii. Ripoti mbalimbali zinaonesha kuwa ukosefu wa maji safi na huduma bora za usafi wa mazingira unaathiri kwa kiasi kikubwa uchumi wa nchi nyingi barani Afrika, hususan Kusini mwa Jangwa la Sahara.

Kwa ujumla, maadhimisho hayo yamekuwa jukwaa muhimu la kuimarisha uelewa, kuongeza ushirikiano na kuhamasisha hatua za pamoja katika kuhakikisha Tanzania inafikia malengo ya kuwa na upatikanaji wa maji safi, salama na endelevu kwa wananchi wote.

MSIGWA: SERIKALI IMEWEKEZA ZAIDI YA TRILIONI 1 USAFIRI WA MAJINI


Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo na Msemaji Mkuu wa Serikali, Ndg, Gerson Msigwa, akizungumza na waandishi wa habari kuhusu miradi ya maendeleo inayotekelezwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika Mkoa wa Mwanza, leo Machi 22, 2026, katika Bandari ya Mwanza South, jijini Mwanza

Na. Fullshangwe Blog, Mwanza

Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo ambaye pia ni Msemaji Mkuu wa Serikali, Bw. Gerson Msigwa, amesema kuwa Serikali ya Awamu ya Sita inaendelea kutekeleza miradi ya usafiri na usafirishaji majini yenye thamani ya zaidi ya shilingi trilioni moja katika maziwa ya Victoria, Tanganyika na Nyasa pamoja na Bahari ya Hindi.

Amesema kuwa meli ya MV Mwanza ni moja ya mafanikio makubwa ambapo ina uwezo wa kubeba abiria 1,200 na mizigo tani 400, na ni miongoni mwa meli kubwa zaidi katika maji baridi barani Afrika.

Aidha, amebainisha kuwa ujenzi wa meli hiyo umegharimu shilingi bilioni 123 na ulikuwa umefikia asilimia 40 wakati Rais Samia Suluhu Hassan anaingia madarakani mwaka 2021, lakini sasa umekamilika kwa asilimia 100.

Pia ameongeza kuwa vijana takribani 200 wakiwemo mainjinia na mafundi walipata ujuzi kwa kushirikiana na wakandarasi kutoka Korea katika ujenzi wa meli hiyo.

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NJE WA AUSTRIA AWASILI NCHINI KWA ZIARA YA KIKAZI










Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Austria anayeshughulikia masuala ya kisiasa, Mheshimiwa Balozi Dkt. Hannah Liko, amewasili nchini Machi 22, 2026 kwa ziara ya kikazi ya siku tatu inayolenga kuimarisha uhusiano wa kidiplomasia, biashara na ushirikiano katika maeneo mbalimbali kati ya Tanzania na Austria.

Akiwasili katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere, Dkt. Liko amepokelewa na Balozi na Mwakilishi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania jijini Vienna, Mhe. Naimi S. Aziz, pamoja na Balozi wa Austria nchini, mwenye makazi yake jijini Nairobi nchini Kenya Mhe. Dkt. Christian Fellner.

Wakati wa ziara hiyo, Dkt. Liko anatarajiwa kufanya mazungumzo na viongozi mbalimbali akiwemo Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Ngwaru Maghembe (Mb.), pamoja na viongozi kutoka wizara mbalimbali zikiwemo Ofisi ya Rais (Mipango na Uwekezaji), Wizara ya Fedha, Wizara ya Mambo ya Ndani na Wizara ya Viwanda na Biashara.

Aidha, anatarajiwa kutembelea Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) kwa lengo la kuimarisha ushirikiano katika nyanja za kitaaluma na elimu ya juu. Ziara hiyo inatarajiwa kuhitimishwa Machi 25, 2026

MAKAMU WA PILI WA RAIS ZANZIBAR AWEKA JIWE LA MSINGI BANDARI JUMUISHI YA MANGAPWANI

Makamu wa PIli wa Rais wa Zanzibar Mhe. Hemed Suleiman Abdulla ameshiriki katika uwekaji wa Jiwe la Msingi la  Bandari Jumuishi ya Mangapwani, Wilaya ya Kaskazini "B", Mkoa wa Kaskazini Unguja.











Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Hemed Suleiman Abdulla, ameshiriki katika hafla ya uwekaji wa jiwe la msingi la mradi wa Bandari Jumuishi ya Mangapwani, iliyopo Wilaya ya Kaskazini “B”, Mkoa wa Kaskazini Unguja, leo tarehe 22 Machi 2026.

Akizungumza katika hafla hiyo, Mheshimiwa Hemed Suleiman Abdulla alieleza kuwa ujenzi wa bandari hiyo ni hatua muhimu katika kuimarisha miundombinu ya uchumi wa Zanzibar, hususan katika sekta za usafirishaji, biashara na uwekezaji. Alisisitiza kuwa Serikali inaendelea kuweka mazingira rafiki yatakayochochea ukuaji wa uchumi na kuongeza ajira kwa wananchi.

Aidha, alibainisha kuwa Bandari Jumuishi ya Mangapwani inatarajiwa kuwa kichocheo kikubwa cha maendeleo ya eneo hilo na visiwa vya Unguja kwa ujumla, kwa kurahisisha shughuli za upokeaji na usafirishaji wa bidhaa pamoja na huduma za baharini.

Mheshimiwa Hemed pia alitoa wito kwa wakandarasi na wadau wote wanaohusika na utekelezaji wa mradi huo kuhakikisha wanazingatia viwango vya ubora, muda uliopangwa pamoja na matumizi sahihi ya rasilimali ili kufanikisha kukamilika kwa mradi huo kwa ufanisi.

Kwa upande wao, viongozi wa Mkoa na Wilaya walieleza kuwa mradi huo utaleta manufaa makubwa kwa wananchi wa Mangapwani na maeneo ya jirani, ikiwa ni pamoja na kuimarisha shughuli za uvuvi, utalii na biashara ndogo ndogo.

Hafla hiyo imehudhuriwa na viongozi mbalimbali wa Serikali, watendaji wa taasisi za umma, pamoja na wananchi wa eneo hilo waliokusanyika kushuhudia tukio hilo muhimu la maendeleo.

Saturday, March 21, 2026

RAIS SAMIA ASHIRIKI SWALA YA EID KINONDONI, AUNGANA NA WAUMINI KATIKA FURAHA YA SIKUKUU

 



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, akiagana na wananchi waliohudhuria swala ya Eid El-Fitri katika Msikiti Mkuu wa BAKWATA (Mfalme Mohamed VI), Kinondoni. jijini Dar es Salaam tarehe 21 Machi, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, akiagana na wananchi waliohudhuria swala ya Eid El-Fitri katika Msikiti Mkuu wa BAKWATA (Mfalme Mohamed VI), Kinondoni. jijini Dar es Salaam tarehe 21 Machi, 2026.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, ameungana na waumini wa Kiislamu kuswali Swala ya Eid al-Fitr katika Msikiti Mkuu wa BAKWATA (Mfalme Mohamed VI), uliopo Kinondoni jijini Dar es Salaam, leo tarehe 21 Machi 2026.

Ibada hiyo imehudhuriwa na mamia ya waumini waliokusanyika kwa pamoja kusherehekea siku kuu hiyo katika mazingira ya amani, furaha na mshikamano. 

Baada ya swala, Rais aliwasalimia wananchi na kubadilishana nao salamu za Eid, akisisitiza umuhimu wa kuendeleza maadili mema, upendo na umoja vilivyojengwa katika kipindi cha mwezi mtukufu wa Ramadhani.

#EidMubarak #SamiaSuluhuHassan #Kinondoni #DarEsSalaam #Eid2026 #AmaniNaUmoja #Mshikamano #Tanzania

Thursday, March 19, 2026

MAKAMU WA RAIS AONGOZA MAADHIMISHO YA SIKU YA MISITU DUNIANIA NA KAMPENI YA UPANDAJI MITI KITAIFA









Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi ameelekeza uongozi wa Mikoa yote nchini kuhakikisha jitihada za upandaji miti zinaendelezwa kwa kuwekewa mkakati mahsusi unaojumuisha makundi yote katika jamii na kuzingatia ikolojia ya maeneo husika, ikiwa ni pamoja na kuzuia uvamizi na uharibifu wa maeneo yote ya hifadhi ya misitu.

Makamu wa Rais, ametoa maelekezo hayo, wakati akifungua Maadhimisho ya Siku ya Misitu Duniani na Siku ya Upandaji Miti Kitaifa, iliyofanyika katika Uwanja wa Ilulu mkoani Lindi, leo tarehe 19 Machi 2026. 

Amesema ni muhimu kuhakikisha wananchi wanaoishi jirani na misitu ya asili na mashamba ya miti wanapatiwa elimu endelevu kuhusu matumizi bora ya ardhi, udhibiti wa uchomaji moto holela, na usimamizi shirikishi wa misitu ya vijiji.

Aidha, Makamu wa Rais amehimiza umuhimu wa Wizara ya Maliasili na Utalii kupitia Taasisi ya Utafiti wa Misitu Tanzania (TAFORI) kufanya tafiti zitakazojibu changamoto mbalimbali ambazo wakulima wa miti wanakabiliana nazo, hususan zile zinazojitokeza kwenye misitu ya asili. 

Amesema tafiti hizo zijumuishe zile zinazohusu miti inayofaa kwa maeneo ya Mkoa wa Lindi na mikoa mingine nchini, ikiwa ni pamoja na miti dawa.  

Makamu wa Rais amesema zoezi la upandaji miti linapaswa kuwa endelevu ambapo ameiagiza Wizara ya Maliasili na Utalii kupitia Mfuko wa Misitu (TaFF) kuwezesha miradi ya upandaji miti kwa kuanzisha mashamba ya miti ya vijiji na watu binafsi. 

Aidha, ameitaka Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) kuanzisha vitalu vya miche ya miti vya kutosha katika maeneo mbalimbali ya nchi, ikiwemo miti ya asili itakayopandwa katika maeneo mbalimbali. Sambamba na hilo, amesema ni vema elimu ya kutosha itolewe kwa wananchi ili kutunza na kukuza miti hiyo.

Halikdhalika, Makamu wa Rais amesema, pamoja na faida lukuki za rasilimali misitu, bado kuna changamoto nyingi zinazoikabili, zikiwemo, utegemezi mkubwa wa rasilimali za misitu kwa uchumi na kipato kwa jamii kwa njia ya kuni, mkaa na mbao, idadi kubwa ya mifugo inayoingizwa katika hifadhi za misitu kwa ajili ya kutafuta malisho, matukio ya uvamizi wa hifadhi za misitu kwa shughuli za kibinadamu hususan makazi, kilimo na uchimbaji wa madini, pamoja na uwepo wa matukio ya moto ndani ya hifadhi za misitu.

Amesema, Changamoto hizo na nyinginezo zimesababisha kiwango cha upotevu wa misitu nchini kuongezeka hadi kufikia hekta 469,400 kwa mwaka ambacho ni kiwango kikubwa sana kisichoweza kuendelea kuvumilika, na hivyo inahitaji kushirikiana kuhakikisha misitu inalindwa na kuhifadhiwa.  

Vilevile, Makamu wa Rais amesema Kampeni ya upandaji miti kitaifa iliyozinduliwa leo ni sehemu ya jitihada za makusudi zinazochukuliwa ili kulinda hifadhi za misitu na kuongeza uwajibikaji katika uhifadhi wa mazingira pamoja na kutambua na kuunga mkono jitihada za Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan za kutunza mazingira, ambapo amekuwa kinara wa uhifadhi, mathalan, aliposheherekea siku ya kumbukumbu ya kuzaliwa kwake mwaka huu alipanda miti na kuhimiza Watanzania kufanya hivyo.

Amesema ajenda ya upandaji miti, uhifadhi wa misitu na utunzaji wa mazingira kwa ujumla ni kipaumbele katika Taifa letu na utekelezaji wa Ilani ya Chama cha Mapinduzi (2025 – 2030) ambayo inalenga kulinda rasilimali za ardhi, misitu, maji na viumbe hai kwa lengo la kutetea ustawi wa wananchi na ukuaji wa uchumi endelevu.

Makamu wa Rais, ameutaka uongozi wa Mkoa wa Lindi kuhakikisha maeneo yote ya misitu yaliyohifadhiwa ndani ya Mkoa huo yanaendelea kulindwa na kutunzwa. Aidha, amewataka skusimamia ili kuhakikisha vijiji vinakuwa na mipango ya matumizi bora ya ardhi ambayo inasimamiwa vema.

Kaulimbiu ya maadhimisho hayo Kitaifa ambayo ni “Misitu ni Uchumi Endelevu, Tuihifadhi kwa Maendeleo ya Taifa.’’, na ile ya Kidunia “Misitu na Uchumi” (Forests and Economies) zote zinachagiza kutambua umuhimu wa misitu na mchango wake katika kukuza na kujenga uchumi wa nchi. 

Kaulimbiu ya kitaifa inaendana na mipango yetu ya Taifa, ikiwemo Dira 2050 pamoja na mikakati mingine yenye nia ya kuifanya Tanzania inufaike kupitia rasilimali za misitu, kwani misitu ina mchango mkubwa katika uhifadhi wa wanyamapori, ufugaji nyuki, utalii, kilimo, upatikanaji wa maji kwa matumizi nyumbani, viwandani na mashambani.

Tanzania inakadiriwa kuwa na eneo la misitu lenye ukubwa wa takriban hekta milioni 48.1 sawa na 55% ya eneo lote la nchi kavu. Katika eneo hili, hekta milioni 44.7 (93%) ni misitu ya uoto wa miombo na hekta milioni 3.4 (7%) ni Misitu ya Uwanda wa Chini, Milimani, Mikoko na Mashamba ya Miti. Sekta ya Misitu inayojumuisha ufugaji nyuki na wanyamapori, ilichangia takriban 3% katika Pato la Taifa mwaka 2024, hivyo kuifanya kuwa miongoni mwa vichocheo muhimu vya maendeleo ya Taifa.

UWEKEZAJI USAFIRI KANDA YA ZIWA KUCHOCHEA UCHUMI, WAWEKEZAJI WAHIMIZWA KUTUMIA FURSA

  Na Baltazar Mashaka, Mwanza Serikali imesema uwekezaji mkubwa unaoendelea kufanywa katika sekta ya usafiri na usafirishaji Kanda ya Ziwa...