Na Ikulu, Dar es Salaam
Mwenyekiti wa Tume ya Rais ya Kuchunguza Matukio ya Uvunjifu wa Amani wakati na baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2025, Jaji Mkuu Mstaafu Mhe. Mohamed Chande Othman, amewasilisha muhtasari wa ripoti ya tume hiyo, akibainisha kwa takwimu ukubwa wa matukio yaliyotokea katika kipindi hicho.
Akiwasilisha taarifa hiyo Aprili 23, 2026 Ikulu jijini Dar es Salaam, Jaji Othman amesema jumla ya vifo 518 vilitokana na vurugu zilizojitokeza kabla na baada ya uchaguzi huo. Aidha, watu 373 walifikishwa hospitalini wakiwa wamefariki, huku majeruhi 121 wakipatiwa matibabu katika vituo mbalimbali vya afya.
Amesema takwimu hizo zinatokana na uchunguzi wa kina uliofanywa na tume kwa kushirikisha ushahidi kutoka kwa wadau mbalimbali, ikiwa ni pamoja na taasisi za Serikali, vyombo vya ulinzi na usalama pamoja na wananchi.
“Ripoti hii inalenga kuweka wazi hali halisi ya matukio yaliyotokea, kubainisha chanzo chake na kutoa mapendekezo yatakayosaidia kuzuia matukio ya aina hii yasijirudie,” ameeleza Jaji Othman.
Aidha, tume imeainisha umuhimu wa kuimarisha mifumo ya usimamizi wa uchaguzi, kuongeza uwajibikaji kwa taasisi husika pamoja na kuendeleza ushirikiano kati ya wadau wote wa kisiasa na kijamii ili kulinda amani ya Taifa.
Uwasilishaji wa ripoti hiyo unatajwa kuwa hatua muhimu katika kujenga uelewa wa pamoja, kuimarisha imani ya wananchi katika mifumo ya kidemokrasia na kuweka msingi imara wa uchaguzi wenye amani katika siku zijazo.






.jpeg)


.jpeg)



.jpeg)
















.jpeg)











.jpeg)

