Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, amewasili katika Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Bole, Jijini Addis Ababa, Ethiopia, tarehe 12 Februari 2026, kwa ajili ya kushiriki Mkutano wa 39 wa Kawaida wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Umoja wa Afrika (AU).
Ushiriki wa Rais Dkt. Samia katika mkutano huo wa ngazi ya juu unadhihirisha dhamira thabiti ya Tanzania kuendelea kuchangia kikamilifu katika ajenda za maendeleo, amani na usalama barani Afrika. Mkutano huo unawakutanisha viongozi wakuu wa nchi wanachama wa AU kujadili masuala ya kimkakati yanayohusu ustawi wa bara, ikiwemo maendeleo ya kiuchumi, ushirikiano wa kikanda, mabadiliko ya tabianchi, pamoja na mageuzi ya taasisi za Umoja wa Afrika.
Mara baada ya kuwasili, Rais Dkt. Samia alipokelewa rasmi na Waziri wa Kazi na Ukuzaji wa Ujuzi wa Ethiopia, Mheshimiwa Muferihat Kamil Ahmed, pamoja na viongozi wengine waandamizi wa Serikali ya Ethiopia na maafisa wa Ubalozi wa Tanzania nchini humo.
Katika mkutano huo, viongozi wanatarajiwa kupokea na kujadili taarifa mbalimbali za utekelezaji wa maazimio ya awali ya AU, pamoja na kuweka mikakati mipya ya kuimarisha ajenda ya Afrika ya maendeleo jumuishi na endelevu. Aidha, mkutano huo utatoa fursa kwa Rais Dkt. Samia kufanya mazungumzo ya kando na viongozi wengine wa Afrika kwa lengo la kuimarisha ushirikiano wa kidiplomasia na kiuchumi.
Ushiriki wa Tanzania katika jukwaa hilo muhimu unaendelea kuiweka nchi katika nafasi ya kimkakati ndani ya bara, sambamba na kuendeleza sera ya diplomasia ya uchumi inayolenga kuvutia uwekezaji, kupanua masoko na kuimarisha mahusiano ya kimataifa.
Mkutano wa 39 wa Kawaida wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Umoja wa Afrika unatarajiwa kuhitimishwa kwa kupitisha maazimio yatakayochochea kasi ya utekelezaji wa Ajenda 2063 – dira ya muda mrefu ya maendeleo ya bara la Afrika.

























.jpeg)








