Makamu wa Rais wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi akihutubia wakati
Maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani, yaliyofanyika katika Kituo
cha Mikutano cha Jakaya Kikwete Mkoani Dodoma, tarehe 05 Juni 2026.Makamu wa Rais wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi akimkabidhi tuzo
Waziri wa Maliasili na Utalii Dkt. Ashatu Kijaji, iliyotolewa na Ofisi
ya Makamu wa Rais kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt.
Samia Suluhu Hassan kwa kutambua Uongozi wake Mahiri na dhamira ya dhati
ya kuimarisha Ajenda ya Uhifadhi wa Mazingira. Tuzo hiyo imetolewa
wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani yaliyofanyika katika
Kituo cha Mikutano cha Jakaya Kikwete mkoani Dodoma, leo tarehe 05 Juni
2026.
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi akimkabidhi tuzo
Mkurugenzi wa Mamlaka ya Udhibiti na Usimamizi wa Mazingira – Zanzibar
Bw. Sheha Mjaja Juma, iliyotolewa na Ofisi ya Makamu wa Rais wa Zanzibar
na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi kwa
kutambua Uongozi wake Mahiri na mchango wa kipekee katika kuimarisha
Ajenda ya Uhifadhi wa Mazingira. Tuzo hiyo imetolewa wakati wa
Maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani yaliyofanyika katika Kituo cha
Mikutano cha Jakaya Kikwete mkoani Dodoma, leo tarehe 05 Juni 2026.Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi akiwa katika picha ya pamoja na wanafunzi mbalimbali, ambao wanashiriki katika program ya utunzaji wa mazingira ya Eco School, mara baada ya kuhitimisha Maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani, yaliyofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Jakaya Kikwete mkoani Dodoma, leo tarehe 05 Juni 2026.
Na Alex Sonna,Mzalendo blog-DODOMA
Serikali imeweka mkazo mpya katika mapambano dhidi ya uharibifu wa mazingira na athari za mabadiliko ya tabianchi kwa kuzindua Programu ya Mageuzi ya Kimkakati ya Mazingira Endelevu Tanzania itakayotekelezwa kwa kipindi cha miaka mitano kuanzia mwaka 2026 hadi 2030.
Hayo yamesemwa na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi akimwakilisha Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika kilele cha Maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani mwaka 2026 ,leo Juni 5,2026 jijini Dodoma.
Dkt.Nchimbi amesema mazingira ni nguzo muhimu ya maendeleo ya taifa kwani yanachangia ukuaji wa uchumi, ustawi wa wananchi na upatikanaji wa rasilimali muhimu zinazohitajika kwa maendeleo ya sasa na ya baadaye.
Ameeleza kuwa Tanzania yenye zaidi ya wananchi milioni 67 kwa sasa inatarajiwa kuwa na zaidi ya watu milioni 118 ifikapo mwaka 2050, hali inayoongeza umuhimu wa kuhifadhi rasilimali za mazingira kama maji, ardhi yenye rutuba, misitu na vyanzo vya nishati ili kukidhi mahitaji ya idadi hiyo kubwa ya watu.
” Serikali imejumuisha masuala ya mazingira na ustahimilivu wa mabadiliko ya tabianchi katika Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, ikilenga kuhakikisha ukuaji wa uchumi unaenda sambamba na matumizi endelevu ya rasilimali za asili.”amesema Dkt.Nchimbi
Amesema maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani yanapaswa kuwa chachu ya kuimarisha ushirikiano kati ya Serikali, sekta binafsi, mashirika ya kiraia na wananchi katika kuhifadhi mazingira na kutumia rasilimali zilizopo kwa uangalifu mkubwa.
Katika hatua za kuimarisha usafi wa mazingira, Dkt.Nchimbi amesisitiza umuhimu wa kubadili mtazamo wa jamii kuhusu taka kwa kuziona kama fursa za kiuchumi badala ya mzigo. Amesema taka zinaweza kutumika kuzalisha mbolea, chakula cha mifugo na bidhaa nyingine zenye thamani ya kiuchumi huku zikichangia kupunguza uchafuzi wa mazingira.
Pia amepongeza mafanikio ya utekelezaji wa Mkakati wa Taifa wa Matumizi ya Nishati Safi ya Kupikia, akibainisha kuwa matumizi ya nishati hiyo yameongezeka kutoka asilimia 6.9 mwaka 2021 hadi asilimia 28.6 mwaka 2025.
“Tunakwenda katika mwelekeo sahihi wa kufikia lengo la zaidi ya asilimia 80 ya Watanzania kutumia nishati safi ya kupikia ifikapo mwaka 2034,” amesema.
Katika kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi, Serikali imeendelea kuimarisha utekelezaji wa mikakati mbalimbali ya kisekta inayolenga kujenga uchumi wenye uzalishaji mdogo wa gesi joto pamoja na kuimarisha uwezo wa jamii kustahimili athari za mabadiliko hayo.
Aidha, Serikali imeeleza kuwa biashara ya kaboni ni miongoni mwa fursa muhimu zinazoweza kuongeza mapato ya ndani huku zikichochea juhudi za uhifadhi wa mazingira. Hivyo, wizara na taasisi mbalimbali zimeagizwa kujumuisha fursa hizo katika mipango, miradi na programu zao za maendeleo.
Katika maelekezo mahsusi kwa taasisi za Serikali, Dkt.Nchimbi ameagiza majiji na manispaa nchini kuanzisha na kutunza bustani za kijani, huku mamlaka zinazotoa vibali vya ujenzi zikihakikisha kila kibali kinaambatana na sharti la kupanda miti isiyopungua mitano.
Pia ameitaka Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania kuhakikisha upatikanaji wa miche ya miti ya kutosha kwa ajili ya kuendeleza kampeni za upandaji miti nchini, sambamba na kuimarisha ulinzi wa maeneo yote yanayopandwa miti.
Kwa upande wa usimamizi wa taka, Serikali imezielekeza mamlaka za serikali za mitaa kuanzisha vituo vya kuchakata taka ili kupunguza mzigo wa taka katika madampo na kuongeza shughuli za urejelezaji ambazo zitasaidia kulinda mazingira na kufungua fursa mpya za ajira.
Kadhalika, Ofisi ya Waziri Mkuu (TAMISEMI), Wizara ya Maliasili na Utalii pamoja na Wizara ya Maji zimeagizwa kuimarisha usimamizi wa maeneo ya ardhi oevu ambayo ni muhimu kwa uzalishaji wa chakula, maji na nishati.
Dkt.Nchimbi pia amezitaka taasisi za utafiti nchini kufanya tafiti za kina kuhusu mimea na viumbe vamizi vinavyoendelea kuathiri mifugo, mazao na mifumo ya ikolojia katika maeneo mbalimbali ya Tanzania.
Hata hivyo amesisitiza kuwa suala la uhifadhi wa mazingira halina mbadala kwa kuwa mazingira ndiyo msingi wa maisha na uchumi wa taifa.
“Mazingira yetu ndiyo uhai wetu na uchumi wetu. Kila mmoja wetu anapaswa kuwajibika katika kulinda, kutunza na kuhakikisha usafi wa mazingira ili kupunguza athari za mabadiliko ya tabianchi na kuacha urithi bora kwa vizazi vijavyo,” amesema.
Kwa upande wake Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira, Mhandisi Hamad Yusuf Masauni, amesema katika maadhimisho hayo mwaka huu shughuli nyingi zimefanyika za utoaji elimu ya utunzaji wa mazingira.
Amesema shughuli nyingine zilizofanyika ni pamoja na upandaji miti katika maeneo korofi na kuratibiwa kwa kongamano la wadau wa mazingira.
“Vilevile Mheshimiwa Makamu wa Rais, katika hafla hii tutakuomba utuzindulie Programu ya Mageuzi ya Usimamizi wa Mazingira Kuelekea Dira 2050 itakayotekelezwa kwa kipindi cha miaka mitano (2026–2030),” amesema
Mhandisi Masauni amesema programu hiyo inalenga kuchochea matokeo makubwa na ya haraka katika kurejesha uoto wa asili, kuimarisha ustawi wa mifumo ikolojia pamoja na huduma za kiikolojia ambazo ni msingi muhimu wa uzalishaji katika sekta mbalimbali za uchumi.
Amesema hatua hizo zitachangia kwa kiasi kikubwa katika kufanikisha malengo ya Dira ya 2050, ambayo inalenga kuifanya Tanzania kuwa miongoni mwa nchi kumi barani Afrika zenye ustawi wa mazingira na ustahimilivu mkubwa dhidi ya mabadiliko ya tabianchi.