Monday, May 11, 2026

WIZARA YA AFYA YAOMBA SH. TRILIONI 1.8 BAJETI YA 2026/2027

 


Wizara ya Afya imeomba kuidhinishiwa jumla ya Shilingi trilioni 1.8 kwa mwaka wa fedha 2026/2027 kwa ajili ya kuendelea kuboresha huduma za afya nchini, kuimarisha hospitali na taasisi zake pamoja na kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo katika sekta hiyo.

Akiwasilisha bungeni jijini Dodoma hotuba ya makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara ya Afya kwa mwaka wa fedha 2026/2027, Waziri wa Afya, Mohamed Omary Mchengerwa amesema wizara hiyo inaomba kuidhinishiwa jumla ya Shilingi 1,800,262,058,000.00.

Waziri Mchengerwa amesema kati ya fedha hizo, Shilingi 652,236,871,000.00 sawa na asilimia 36 ya bajeti yote zimetengwa kwa matumizi ya kawaida, huku Shilingi 1,148,025,187,000.00 sawa na asilimia 64 zikielekezwa kwenye utekelezaji wa miradi ya maendeleo.

Ameeleza kuwa katika fedha za matumizi ya kawaida, kiasi cha Shilingi 516,323,356,000.00 kimetengwa kwa ajili ya mishahara ya watumishi wa Wizara, hospitali pamoja na taasisi zilizo chini yake, huku Shilingi 135,913,515,000.00 zikitengewa matumizi mengineyo.

Kwa upande wa fedha za maendeleo, Waziri huyo amesema Shilingi 789,458,609,000.00 ni fedha za ndani, wakati Shilingi 358,566,578,000.00 ni fedha kutoka vyanzo vya nje kwa ajili ya kuendeleza miradi mbalimbali ya afya nchini.

Aidha, Wizara ya Afya imekadiria kukusanya maduhuli ya Shilingi 747,200,091,299.81 katika mwaka wa fedha 2026/2027 kupitia Wizara, taasisi pamoja na hospitali zake.

Kwa mujibu wa Waziri Mchengerwa, kati ya fedha hizo, Shilingi 76,195,850,735.53 zinatarajiwa kukusanywa kutoka vyanzo vya ndani vya Makao Makuu ya Wizara, Shilingi 165,804,149,264.47 kutoka Hospitali za Rufaa za Mikoa, huku zaidi ya Shilingi bilioni 505 zikitarajiwa kukusanywa kutoka taasisi, Hospitali ya Taifa, hospitali maalum pamoja na hospitali za kanda.

Waziri huyo amesema fedha zinazoombwa zitawezesha Wizara ya Afya kuendelea kuboresha huduma za afya nchini, kuimarisha miundombinu ya matibabu, kuongeza upatikanaji wa vifaa tiba pamoja na kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma kwa wananchi.

SERIKALI YATOA BILIONI 48.8 BIMA YA AFYA KWA WOTE

 


Na Mwandishi Wetu , Dodoma

Serikali imeanza rasmi utekelezaji wa Mpango wa Bima ya Afya kwa Wote kwa kaya zisizo na uwezo kwa kutoa Shilingi bilioni 48.8 kwa ajili ya kuwawezesha wananchi wa makundi maalum kupata huduma za afya kwa uhakika.

Kupitia utekelezaji huo, jumla ya kaya 172,297 tayari zimefikiwa na kuingizwa kwenye mpango huo, huku wanufaika 463,228 wakianza kupata huduma mbalimbali za matibabu katika vituo vilivyosajiliwa nchini.

Akiwasilisha Hotuba ya Bajeti ya Wizara ya Afya Fungu 52 kwa mwaka 2026/27 Waziri wa Afya Mhe. Omary Mchengerwa amesema kuwa, utekelezaji huu unaonesha dhamira ya Serikali ya kuhakikisha kila Mtanzania anapata huduma bora za afya bila kujali hali yake ya kiuchumi, ikiwa ni sehemu ya safari ya kuelekea huduma jumuishi za afya kwa wananchi wote.

Katika kuimarisha sekta ya afya sambamba na utekelezaji wa mpango huo, mabaraza na bodi za kitaaluma yameendelea kusimamia ubora wa huduma kwa kusajili wataalam wa afya 14,310, hatua inayoongeza nguvu kazi muhimu kwa utoaji wa huduma nchini.

Amesema kuwa kuhusu upatikanaji wa huduma za matibabu, jumla ya maduka ya dawa 330 yamesajiliwa pamoja na watarajali 3,004, huku vituo vya kutolea huduma za afya 3,643 vikisajiliwa ili kuongeza upatikanaji wa huduma karibu na wananchi.

Katika kuhakikisha taaluma na maadili yanaendelea kuzingatiwa hususan wakati huu wa kuhudumia wananchi wengi zaidi kupitia mfumo wa Bima ya Afya, vituo binafsi vya afya 654 vimekaguliwa ili kuhakikisha vinakidhi viwango na kutoa huduma salama kwa wananchi.

Mafanikio hayo yanaakisi hatua kubwa ya Serikali katika kujenga mfumo imara wa afya unaojali usawa, ubora na upatikanaji wa huduma kwa wote, huku Bima ya Afya kwa Wote ikiendelea kuwa nguzo muhimu ya maendeleo ya kijamii na kiuchumi. 

WAZIRI KOMBO ASHIRIKI MKUTANO WA DHARURA WA KAMATI YA MAWAZIRI SADC

 

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo (Mb.), ameshiriki Mkutano wa Dharura wa Kamati ya Mawaziri wa Asasi ya Siasa, Ulinzi, na Usalama ya Jumuiya ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika (SADC-MCO), uliofanyika tarehe 10 Mei, 2026, Jijini Nairobi, Kenya.

Mkutano huo uliolenga kuimarisha misingi ya amani, umeongozwa na Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mhe. Dkt. George Chaponda, ambaye ni Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa wa Jamhuri ya Malawi.

Katika mazungumzo hayo, Mawaziri wamejadili changamoto mbalimbali za kiusalama zinazoikabili kanda hiyo ikiwemo Vurugu zinazoendelea nchini Afrika Kusini dhidi ya raia wa nchi nyingine za Afrika.

Kwa Upande wake Mwenyekiti Dkt. Chaponda amewahakikishia wajumbe wa mkutano huo kuwa mapendekezo yote yaliyofikiwa yatafanyiwa kazi kwa haraka na kwa ufanisi.

Hatua hii ni sehemu ya mikakati ya SADC kuhakikisha kuwa Kanda ya Kusini mwa Afrika inasalia kuwa kisiwa cha amani, utulivu, na ushirikiano wa kiuchumi.






WAKAZI WA NUNGWI KUNUFAIKA NA HUDUMA ZA KIDIJITALI BAADA YA YAS KUFUNGUA DUKA JIPYA


 Zanzibar…08 Mei 2026.

Kampuni ya mawasiliano ya Yas imefungua rasmi duka jipya la huduma katika eneo la Nungwi, Mkoa wa Kaskazini Unguja, hatua inayolenga kurahisisha upatikanaji wa huduma za mawasiliano na kifedha kwa wakazi wa Zanzibar.

Uzinduzi huo umefanyika hivi karibuni eneo la Nungwi – Zanzibar na kuongozwa na Mstahiki Meya wa Baraza la Manispaa ya Wilaya ya Kaskazini A’ Unguja, Mhe. Nyange Kher Ali, aliyemwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Kaskazini Unguja.

Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Mhe. Nyange Kher Ali aliipongeza Yas kwa kuendelea kuwekeza Zanzibar na kusaidia jitihada za Serikali katika kuboresha huduma za mawasiliano pamoja na kuongeza fursa za ajira kwa vijana.

“Uwekezaji huu una mchango mkubwa katika kukuza uchumi wa wananchi wetu pamoja na kuongeza upatikanaji wa huduma muhimu za kidijitali,” alisema Mhe. Nyange Kher Ali.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Huduma kwa Wateja na Uendeshaji wa Yas, Bi. Mwangaza Matotola, alisema kufunguliwa kwa duka hilo ni sehemu ya mkakati wa kampuni wa kusogeza huduma karibu zaidi na wananchi na kuendelea kuimarisha uchumi wa kidijitali nchini.

“Uzinduzi wa duka hili hapa Nungwi ni sehemu ya mkakati wetu wa kuhakikisha kila Mtanzania anapata huduma za mawasiliano na kifedha kwa urahisi, haraka na kwa viwango vya hali ya juu,” alisema Bi. Matotola.

Alisema Yas imeendelea kuwekeza katika upanuzi wa miundombinu yake nchini kupitia teknolojia za 4G na 5G, huku kampuni hiyo ikiwa na zaidi ya minara 4,800 inayohudumia zaidi ya wateja milioni 31 Tanzania Bara na Zanzibar.

Bi. Matotola alisema Nungwi ni eneo muhimu kiuchumi kutokana na shughuli za utalii, uvuvi na biashara, hivyo uwepo wa duka hilo utasaidia wananchi na wafanyabiashara kupata huduma kwa ukaribu zaidi.

Aidha, aliwahamasisha wananchi kutumia applikesheni mpya ya Yas inayowezesha upatikanaji rahisi wa huduma mbalimbali kidijitali.

Duka la Nungwi linaungana na mtandao wa zaidi ya maduka 556 ya Yas yaliyopo nchini kote, yakilenga kuboresha huduma kwa wateja na kuongeza upatikanaji wa huduma za kidijitali kwa Watanzania.




Thursday, May 07, 2026

WAZIRI MKUU: SERIKALI YAENDELEA KUHAKIKISHA MAFUTA HAYAADIMIKI NCHINI



Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba amesema Serikali imeendelea kuchukua hatua mbalimbali kuhakikisha upatikanaji wa mafuta nchini unaendelea kuwa wa uhakika na bidhaa hiyo haiadimiki.

Akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum, Janeth Mahawanga Bungeni jijini Dodoma, aliyetaka kujua hatua zilizochukuliwa na Serikali katika kukabiliana na athari za migogoro ya kimataifa na kidunia zilizopelekea changamoto ya mafuta nchini.

“Hatua ya kwanza ambayo Serikali imechukua ni kuhakikisha bidhaa hii haiadimiki. Zipo nchi ambazo tayari matatizo yameshajitokeza ya bidhaa hiyo kuadimika, hata kama una fedha hupati mafuta,” amesema Dkt. Nchemba.

Waziri Mkuu amesema Serikali imeanza taratibu za kuweka ruzuku ili kupunguza makali ya athari zinazotokana na hali inayoendelea Mashariki ya Kati.

Aidha, amesema Serikali imekaa na kuwasikiliza wadau mbalimbali, wakiwemo wadau wa usafirishaji, kwa lengo la kujadiliana namna ya kudhibiti ongezeko la gharama za usafirishaji.

“Tulikubaliana na wasafirishaji kupunguza baadhi ya gharama zinazotokana na hatua zinazochukuliwa na Serikali ambazo kimsingi si za lazima. Mfano, ulikuwepo uratibu wa mabasi yote ya mikoani kupita kila stendi, tumesema hakuna ulazima wa basi kupita kila stendi,” amesema Waziri Mkuu.

Sunday, May 03, 2026

NHC YATOA ELIMU YA HATI PACHA, YASISITIZA UMOJA WA WAMILIKI SAMIA HOUSING SCHEME KAWE




 Samia Housing Scheme Kawe: nyumba 560, familia tofauti zikiunganishwa na mtindo mmoja wa maisha ya 
kisasa—ushirikiano, ustaarabu na “modern urban living” ya Tanzania ya leo.  

20260502_104409.jpg.jpeg
Menejimenti ya NHC ikifuatilia kwa kina lilichokuwa kikiendelea katika mkutano huo muhimu katika maendeleo ya sekta 
ya nyumba ikiwa ni estate ya 11 kutekeleza sheria ya hati pacha nchini.
20260502_105112.jpg.jpeg
Mhandisi Grace Msita ambaye ndiye Meneja wa Miradi ya NHC akiwahakikishai wamiliki hao ubora na uimara 
wa nyumba na weledi uliotumika.
20260502_105510.jpg.jpegMwakalukwa.jpeg
Mzee George Mwakalukwa ambaye ni mmoja wa wamiliki wa nyumba hizo akitia saini kitabu cha wageni 
kabla ya mkutano kuanza.
WhatsApp Image 2026-05-02 at 10.17.41.jpeg
Mmiliki Mwingine akitia saini kitabu cha wageni wakati akiwasili kwenye mkutano huo
 muhimu.
WhatsApp Image 2026-05-03 at 15.23.11(2).jpeg

Afisa Sheria Mwandamizi wa NHC, Scholastica Kilagane, alitoa elimu ya kina

 kuhusu dhana ya hati pacha (Unit title)

Uongozi wa Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) umefanya kikao pamoja na wateja 
wake wa nyumba za makazi za Samia Housing Scheme jana, tarehe 2/5/2026, 
katika eneo la Kawe jijini Dar es Salaam, kwa lengo la kuwajengea uelewa wa 
kina kuhusu umiliki wa nyumba za kisasa, hususan mfumo wa hati pacha pamoja 
na kuimarisha misingi ya usimamizi wa pamoja wa makazi hayo.

Akizungumza katika kikao hicho, kilichohudhuriwa na wamiliki wa nyumba hizo
 560 zilizopo Kawe Tanganyika Packers Dar es Salaam, Afisa Sheria Muandamizi 
wa NHC, Scholastica Kilagane, alitoa elimu ya kina kuhusu dhana ya hati pacha
 (Unit title), akieleza kuwa mfumo huo unampa mmiliki haki ya kumiliki sehemu
 yake binafsi ya nyumba huku akishiriki umiliki wa maeneo ya pamoja kama vile
 lifti, korido, ngazi, maeneo ya wazi na miundombinu mingine ya huduma.

Alisisitiza kuwa uelewa sahihi wa mfumo huo ni muhimu ili kuepusha migogoro ya 
kisheria na kuhakikisha matumizi bora ya mali hizo.

“Hati pacha inalenga kuweka uwazi katika umiliki wa mali na kugawanya wazi haki 
na wajibu wa kila mmiliki. Ni muhimu kwa kila mmiliki kuelewa kuwa pamoja na 
kumiliki nyumba yake, ana wajibu wa kushiriki kikamilifu katika kusimamia maeneo
 ya pamoja kwa mujibu wa sheria,” alieleza Kilagane.

Aidha, Kilagane alieleza umuhimu wa kuanzishwa kwa umoja wa wamiliki wa 
nyumba (Owners Association), akibainisha kuwa huo ndio chombo rasmi cha 
kisheria kitakachosimamia masuala yote ya pamoja ndani ya eneo hilo.

Alifafanua kuwa umoja huo utakuwa na viongozi watakaochaguliwa kwa mujibu 
wa taratibu za kisheria, ikiwemo Mwenyekiti, Katibu na Mweka Hazina, huku kila 
mmoja akiwa na majukumu mahsusi ya kuhakikisha uendeshaji 
mzuri na uwajibikaji.

Naye Injinia Grace Msita, Meneja Miradi wa Shirika la Nyumba la Taifa (NHC), 
akizungumza na wamiliki hao aliwahakikishia kuwa miundombinu yote ya Samia 
Housing Scheme imekamilika kwa viwango vya juu vya ubora na usalama, huku 
akisisitiza kuwa usimamizi madhubuti wa miradi hiyo wakati wa utekelezaji ni 
sehemu ya dhamira ya NHC ya kutoa makazi endelevu na yenye thamani kwa 
wananchi.

Alieleza kuwa NHC itaendelea kushirikiana na umoja wa wamiliki katika hatua 
zote za wakati huu wa kipindi cha uangalizi yaani DLP wa mradi huo ili 
kuhakikisha changamoto zinazojitokeza zinapatiwa ufumbuzi wa haraka 
na kwa weledi, na hivyo kulinda uwekezaji wa kila mmiliki pamoja na kuhakikisha 
mazingira ya kuishi yanabaki kuwa bora na ya kisasa.

Kwa upande wake, Meneja wa Milki wa NHC, France Bahangarwa, alisisitiza 
wajibu wa wamiliki katika kuhakikisha uendelevu wa huduma ndani ya Samia 
Housing Scheme. Alieleza kuwa ulipaji wa service charge ni sharti la kisheria 
lisiloweza kuepukika kwani ndilo linalowezesha uendeshaji wa huduma muhimu 
za pamoja.

“Huduma kama lifti, usafi wa mazingira, ulinzi, taa za maeneo ya pamoja na 
matengenezo ya miundombinu haviwezi kuendelea bila michango ya wamiliki. 
Hivyo, kila mmiliki ana wajibu wa kulipa service charge kwa wakati ili 
kuhakikisha mazingira haya yanaendelea kuwa salama na yenye hadhi,” alisema 
Bahangarwa.

Aliongeza kuwa pamoja na hilo, wamiliki wanapaswa kutekeleza majukumu yao
 mengine ya kisheria ikiwemo kulipa kodi ya ardhi na kushiriki katika maamuzi 
ya pamoja kupitia umoja wao. Pia alisisitiza umuhimu wa kuajiri kampuni ya 
usimamizi wa milki au mtaalamu binafsi ili kuhakikisha shughuli za kila siku 
za uendeshaji zinafanyika kwa weledi na kwa kuzingatia viwango vya kitaalamu.

“Usimamizi wa kitaalamu ni nguzo muhimu katika mafanikio ya miradi ya makazi
 ya aina hii. Ni vyema wamiliki wakachagua njia bora ya usimamizi 
itakayolinda thamani ya mali zao na kuboresha maisha yao kwa ujumla,” 
aliongeza Bahangarwa.

Kwa upande wao, wamiliki wa nyumba katika Samia Housing Scheme 
walieleza kuridhishwa na kikao hicho, wakitoa shukurani kwa Shirika la Nyumba
 la Taifa kwa kuwapatia elimu hiyo muhimu.

Mmoja wa wamiliki alieleza kuwa, “Tunashukuru sana NHC kwa kutuletea elimu
 hii. Imetusaidia kuelewa kwa undani haki na wajibu wetu kama wamiliki wa 
nyumba za mfumo huu wa kisasa. Sasa tunaona umuhimu wa kushirikiana na 
kuunda umoja imara kwa ajili ya maendeleo ya makazi yetu.”

Kwa ujumla, kikao hiki kimekuwa jukwaa muhimu la kuwawezesha wamiliki 
kwa maarifa sahihi ya kisheria na kiutendaji, hatua inayotarajiwa kuimarisha 
usimamizi wa pamoja, kuongeza thamani ya mali na kuhakikisha Samia Housing
 Scheme inakuwa mfano bora wa makazi ya kisasa yanayosimamiwa kwa ufanisi 
nchini.

Naye Meneja Mauzo na Masoko wa NHC, Deogratius Batakanwa alieleza kuwa 
Samia Housing Scheme ni zaidi ya makazi; ni uwekezaji wenye thamani unaohitaji
 uelewa sahihi wa kisheria na usimamizi wa pamoja ili kulinda na kukuza thamani 
yake kwa muda mrefu.

“Kupitia mfumo wa hati pacha, kila mmiliki anapata umiliki halali wa sehemu 
yake binafsi huku akishiriki umiliki wa maeneo ya pamoja. Huu ni mfumo wa 
kisasa unaolenga kuongeza uwazi, kulinda uwekezaji na kuhakikisha mazingira 
bora ya kuishi kwa wakazi wote,” alisema Batakanwa.

Alisisitiza kuwa uelewa wa mfumo huo unawawezesha wamiliki kufanya maamuzi 
sahihi kuhusu mali zao na kushiriki kikamilifu katika uendeshaji wa makazi yao kwa
 tija.

Katika kuimarisha usimamizi wa pamoja, Batakanwa alibainisha umuhimu wa 
kuunda umoja wa wamiliki wa nyumba (Owners Association) utakaosimamia 
masuala ya pamoja kwa weledi na uwazi. Alieleza kuwa uongozi wa umoja huo 
utachaguliwa kwa kufuata taratibu rasmi na utakuwa na jukumu la kuhakikisha 
huduma zote zinaendeshwa kwa ufanisi.

Katika hatua ya kuimarisha usimamizi wa pamoja, wamiliki wa Samia Housing 
Scheme wamechagua uongozi wa umoja wao ukiongozwa na Mwenyekiti Catherine
 Mrosso akisaidiwa na Makamu Mwenyekiti Eng. Juma Kiboko, huku nafasi ya 
Katibu ikishikiliwa na Grace Lemunge akisaidiwa na Katibu Msaidizi George 
Laurian, na Mweka Hazina akiwa Veronica Rukeha.

Wajumbe wa kamati hiyo ni Rehema Chonda, Ramadhani Mshana, Dkt. Petronila
 Ngiloi, Bi. Hadija Mwema, Isack Ngovi, Faith Kayombo, Robert Matapu, Jesca 
Macharia, Salma Juma, Dkt. Oreste Munishi na Grace Mwaihojo.

Kwa upande wao, wamiliki wa nyumba walitoa shukurani kwa NHC kwa 
kuandaa kikao hicho, wakieleza kuwa elimu waliyoipata imewasaidia kuelewa 
thamani halisi ya uwekezaji wao na namna bora ya kuilinda.

“Tunathamini jitihada za NHC kutuelimisha. Sasa tunaelewa kuwa mafanikio ya
 makazi haya yanategemea ushirikiano wetu na utekelezaji wa majukumu yetu 
ipasavyo,” walieleza baadhi ya wamiliki.

Kwa ujumla, kikao hiki kimeweka msingi thabiti wa kuifanya Samia Housing Scheme 
kuwa mfano wa makazi ya kisasa yanayosimamiwa kwa ufanisi, huku yakitoa 
thamani ya juu kwa wamiliki wake—ikiwa ni sehemu ya dhamira ya NHC ya 
kuendeleza makazi bora na uwekezaji salama kwa Watanzania.

RAIS DKT. SAMIA AFANYA MAZUNGUMZO NA RAIS KAGAME IKULU DAR ES SALAAM

 
 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza na Waandishi wa Habari kuhusu Ziara ya Kikazi ya Rais wa Jamhuri ya Rwanda Mhe. Paul Kagame, Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 03 Mei, 2026.





 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiongoza Ujumbe wa Tanzania kwenye mazungumzo na Ujumbe wa Rwanda uliongozwa na Rais wa Nchi hiyo Mhe. Paul Kagame, tarehe 03 Mei, 2026.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, ameongoza mazungumzo ya ngazi ya juu kati ya Tanzania na Rwanda yaliyofanyika Ikulu jijini Dar es Salaam tarehe 03 Mei 2026, akiwa mwenyeji wa Rais wa Jamhuri ya Rwanda, Mhe. Paul Kagame, katika ziara ya kikazi yenye lengo la kuimarisha zaidi uhusiano wa kidiplomasia na ushirikiano wa kiuchumi kati ya mataifa hayo mawili.

Mazungumzo hayo yalijikita katika maeneo muhimu ya ushirikiano ikiwemo biashara, uwekezaji, miundombinu ya kikanda, pamoja na kuimarisha amani na usalama katika ukanda wa Afrika Mashariki. Viongozi hao wawili walisisitiza umuhimu wa kuendeleza mshikamano wa kihistoria uliopo kati ya Tanzania na Rwanda kwa manufaa ya wananchi wa pande zote.

Baada ya mazungumzo hayo, Rais Samia pia alizungumza na waandishi wa habari ambapo alieleza kuwa ziara hiyo ni ishara ya kuimarika kwa mahusiano ya kidiplomasia na nia ya pamoja ya kuharakisha maendeleo ya kikanda kupitia ushirikiano wa karibu zaidi.

Kwa ujumla, ziara ya Rais Paul Kagame nchini Tanzania imeacha alama ya diplomasia yenye nguvu, ikithibitisha dhamira ya viongozi hao wawili kuendeleza ushirikiano wa kimkakati unaolenga ustawi wa wananchi wa Afrika Mashariki.

WIZARA YA AFYA YAOMBA SH. TRILIONI 1.8 BAJETI YA 2026/2027

  Wizara ya Afya imeomba kuidhinishiwa jumla ya Shilingi trilioni 1.8 kwa mwaka wa fedha 2026/2027 kwa ajili ya kuendelea kuboresha huduma z...