Friday, March 27, 2026

TBC Yawajengea Uwezo Washitiri Uzalishaji wa Vipindi

Kaimu Mkurugenzi wa Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC), Bw. Gwakisa Mlawa akizungumza wakati wa kufunga Mkutano wa 110 wa wadau wa elimu kwa umma (Washitiri), uliofanyika  katika ukumbi wa PAPU, Jijini Arusha, Machi 27, 2026

Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano LATRA, Bw. Salum Pazzy, akitoa salamu za shukrani kwa TBC kwa niaba ya washitiri wengine wakati wa kufunga Mkutano wa 110 wa wadau wa elimu kwa umma uliofanyika  katika ukumbi wa PAPU, Jijini Arusha, Machi 27, 2026.
Baadhi ya Washitiri walioshiriki Mkutano wa 110 wa wadau wa elimu kwa umma uliofanyika  katika ukumbi wa PAPU, Jijini Arusha, Machi 23 - 27, 2026.

Adelina Johnbosco na Timothy Mwakyenda – MAELEZO

Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC) limetoa mafunzo ya uandaaji bora wa vipindi kwa washitiri wa taasisi za umma nchini ili kuwajengea uwezo wa kutoa elimu kwa umma.

Washitiri hao kutoka vitengo vya mawasiliano vya wizara, taasisi, idara, mamlaka na mashirika ya umma wanahusika na utoaji wa taarifa za Serikali na utekelezaji wa shughuli na miradi mbalimbali ya maendeleo ya wananchi.

Akizungumza wakati wa kufunga mafunzo hayo, Kaimu Mkurugenzi wa TBC, Bw. Gwakisa Mlawa, amesema ana imani mafunzo hayo yataongeza ujuzi na ufanisi kwa washiriki katika majukumu yao ya kila siku ya mawasiliano.

Amesema mafunzo hayo pia yatakuwa chachu ya maboresho ya maudhui yanayozalishwa, kutokana na maarifa waliyopata kupitia wataalamu waliobobea katika nyanja tofauti.

Mafunzo hayo yamejumuisha mada mbalimbali zikiwemo uongozi bora, uandaaji wa vipindi, matumizi ya akili unde (AI) pamoja na mbinu za utatuzi wa migogoro kazini.

“Mawasiliano siyo suala la kutoa na kupokea taarifa tu, bali ni kujenga taswira nzuri ya taasisi na taifa kwa ujumla,” alisema Bw. Mlawa.

Aidha, amesema TBC inaendelea kuwekeza katika teknolojia za kisasa ili kuboresha utoaji wa huduma za habari na mawasiliano kwa wananchi akiwakaribisha wadau na wananchi kuendelea kuitumia TBC kama chombo muhimu cha utangazaji nchini.

Kwa upande wake Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano wa Mamlaka ya Udhibiti wa Usafiri Ardhini (LATRA), Bw. Salum Pazzy, akizungumza kwa niaba ya washiriki wenzake ameipongeza TBC kwa kuandaa mafunzo hayo, akieleza kuwa yamekuwa na manufaa makubwa kwa washitiri wote.

Amesema mafunzo hayo yamewajengea uwezo wa kuzalisha vipindi vya elimu kwa umma kwa weledi na uzalendo. 

TANZANIA NA ZAMBIA ZAIMARISHA USHIRIKIANO WA NISHATI KATIKA KUKUZA UCHUMI NA RASILIMALI ZA TAIFA









Katika kuendeleza ajenda ya kimkakati ya kukuza uchumi kupitia rasilimali za taifa, Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi, amekutana na kufanya mazungumzo na Waziri wa Nishati wa Zambia, Mhe. Makozo Chikote, tarehe 27 Machi 2026 jijini Lusaka, Zambia.

Mazungumzo hayo yamejikita katika kuimarisha ushirikiano wa sekta ya nishati, hususan mafuta na gesi, ambayo ni mhimili muhimu katika kuchochea maendeleo ya sekta nyingine za uzalishaji ikiwemo madini. Viongozi hao walisisitiza umuhimu wa kuunganisha nguvu za kikanda ili kuongeza thamani ya rasilimali, kuboresha miundombinu ya nishati na kuhakikisha upatikanaji wa nishati ya uhakika kwa shughuli za kiuchumi.

Katika muktadha wa sera ya madini ya Tanzania, nishati imeendelea kuwa nyenzo muhimu katika kuongeza ufanisi wa uchimbaji na uchakataji wa madini, hivyo ushirikiano huu unatarajiwa kuongeza kasi ya uwekezaji na tija katika sekta hiyo. Uimarishaji wa miundombinu ya mafuta na gesi unatoa msingi imara wa kukuza viwanda vinavyotegemea rasilimali za madini, na hivyo kuongeza mchango wa sekta hiyo katika pato la taifa.

Kikao hicho kilihudhuriwa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati anayeshughulikia Mafuta na Gesi, Dkt. James Mataragio, Balozi wa Tanzania nchini Zambia, Luteni Jenerali Mathew Edward Mkingule pamoja na wataalam kutoka Wizara ya Nishati na taasisi zake, wakionesha dhamira ya dhati ya pande zote mbili katika kuendeleza ushirikiano huo.

Historia ya ushirikiano kati ya Tanzania na Zambia inaendelea kudhihirishwa kupitia mradi wa kimkakati wa Bomba la Mafuta la TAZAMA, ambalo limekuwa mhimili wa usafirishaji wa mafuta kutoka Bandari ya Dar es Salaam kwenda Zambia. Mradi huo sio tu umeimarisha usalama wa nishati bali pia umefungua fursa za kiuchumi na uwekezaji katika ukanda wa Kusini mwa Afrika.

Kwa ujumla, hatua hii inaashiria mwelekeo mpya wa ushirikiano unaolenga kuunganisha sekta ya nishati na maendeleo ya madini, sambamba na utekelezaji wa sera za kitaifa zinazolenga kuongeza thamani ya rasilimali za ndani na kukuza uchumi shindani.

#Nishati #Madini #Ushirikiano #Tanzania #Zambia #TAZAMA #Uwekezaji #Maendeleo #Rasilimali #EnergySector #MiningPolicy

WANAWAKE WAJENGEWA UWEZO KATIKA UTATUZI WA MIGOGORO KWA NJIA MBADALA (ADR)

Mkurugenzi wa Idara ya Usuluhishi wa Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali, ndugu Saddy Sevingi akizungumza wakati akifunga mafunzo kuhusu ushirikishwaji wa wanawake kwenye utatuzi wa migogoro kwa njia mbadala yaliyofanyika Jijini Dar es Salaam.
Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Usuluhishi Tanzania, Bi. Madeline Kimei akitoa mada kuhusu fursa mbalimbali zilizopo kwenye utatuzi wa migogoro kwa njia mbadala wakati wa mafunzo kuhusu ushirikishwaji wa wanawake kwenye utatuzi wa migogoro kwa njia mbadala yaliyofanyika Jijini Dar es Salaam.
Wakili wa Serikali wa Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali, Bi. Lydia Thomas akitoa mada kuhusu mbinu za utatuzi wa migogoro ya kibiashara kwa njia mbadala (ADR) wakati wa mafunzo kuhusu ushirikishwaji wa wanawake kwenye utatuzi wa migogoro kwa njia mbadala yaliyofanyika Jijini Dar es Salaam.
Wakili wa Serikali Mwandamizi wa Wizara ya Katiba na Sheria, Bi. Aveline Ombock akitoa maelezo kuhusu namna ya kujisajili kupia mfumo wakati wa mafunzo kuhusu ushirikishwaji wa wanawake kwenye utatuzi wa migogoro kwa njia mbadala yaliyofanyika Jijini Dar es Salaam.

Baadhi ya washiriki wa mafunzo kuhusu ushirikishwaji wa wanawake kwenye utatuzi wa migogoro kwa njia mbadala wakimsikiliza Mkurugenzi wa Usuluhishi wa Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali, ndugu Saddy Sevingi wakati akifunga mafunzo kuhusu ushirikishwaji wa wanawake kwenye utatuzi wa migogoro kwa njia mbadala yaliyofanyika Jijini Dar es Salaam.

&&&&&&&&&&&&&&&&&&&

Jijini Dar es Salaam kumeshuhudiwa hatua muhimu katika kuimarisha ushiriki wa wanawake kwenye sekta ya sheria, kufuatia kufanyika kwa mafunzo maalum kuhusu ushirikishwaji wa wanawake katika utatuzi wa migogoro kwa njia mbadala (ADR).

Akifunga mafunzo hayo, Mkurugenzi wa Idara ya Usuluhishi wa Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali, ndugu Saddy Sevingi, alisisitiza umuhimu wa kuwajengea wanawake uwezo na ujasiri wa kushiriki kikamilifu katika mifumo ya utatuzi wa migogoro, akieleza kuwa ADR ni nyenzo muhimu inayochochea upatikanaji wa haki kwa haraka, nafuu na kwa ufanisi zaidi.

Katika mafunzo hayo, wataalamu mbalimbali walitoa mada zenye kujenga uelewa mpana kwa washiriki. Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Usuluhishi Tanzania, Bi. Madeline Kimei, aliwasilisha mada kuhusu fursa zilizopo katika sekta ya ADR na namna wanawake wanavyoweza kuzitumia kujenga taaluma na kuchangia maendeleo ya jamii.

Kwa upande wake, Wakili wa Serikali, Bi. Lydia Thomas, alielezea mbinu za kisasa za utatuzi wa migogoro ya kibiashara kwa njia mbadala, akisisitiza umuhimu wa weledi na uadilifu katika kushughulikia migogoro hiyo. Naye Wakili wa Serikali Mwandamizi kutoka Wizara ya Katiba na Sheria, Bi. Aveline Ombock, alitoa mwongozo wa kina kuhusu namna ya kujisajili kupitia mfumo husika, hatua inayolenga kurahisisha ushiriki wa wadau wengi zaidi katika huduma za usuluhishi.

Washiriki wa mafunzo hayo walionesha hamasa kubwa kwa kufuatilia kwa makini mada mbalimbali zilizowasilishwa, hatua inayoashiria mwitikio chanya na utayari wa wanawake kushiriki kikamilifu katika kuimarisha mifumo ya haki mbadala nchini.

Mafunzo haya yanaendelea kuwa chachu ya mabadiliko, yakifungua milango ya fursa kwa wanawake katika sekta ya sheria na kuchangia ujenzi wa jamii yenye usawa, haki na maendeleo endelevu.

#ADR #Wanawake #Uwezeshaji #Usuluhishi #Sheria #Migogoro #Maendeleo #DarEsSalaam #LegalEmpowerment #GenderEquality

SAMIA AENDELEA KUIPEPERUSHA VYEMA TANZANIA KATIKA MAJUKWAA YA KIMATAIFA

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, ambaye pia ni Makamu wa Pili wa Mwenyekiti wa Umoja wa Afrika (AU), akishiriki Kikao cha Baraza la Uongozi la Umoja wa Afrika (African Union Bureau of Assembly) kilichofanyika kwa njia ya mtandao, tarehe 26 Machi, 2026, Ikulu Ndogo ya Tunguu, Zanzibar. 

Kikao hicho kiliongozwa na Mwenyekiti wa Umoja wa Afrika (AU) Rais wa Jamhuri ya Burundi Mhe. Évariste Ndayishimiye.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, ameendelea kuimarisha nafasi ya Tanzania katika majukwaa ya kimataifa kwa kushiriki kikao muhimu cha Baraza la Uongozi la Umoja wa Afrika (African Union Bureau of Assembly), kilichofanyika kwa njia ya mtandao tarehe 26 Machi 2026.

Kikao hicho kilichofanyika kutoka Ikulu Ndogo ya Tunguu, Zanzibar, kiliwakutanisha viongozi wakuu wa Bara la Afrika kujadili masuala ya kimkakati yanayolenga kuimarisha mshikamano, kukuza uchumi na kuleta maendeleo endelevu kwa wananchi wa Afrika. 

Mheshimiwa Dkt. Samia, ambaye pia ni Makamu wa Pili wa Mwenyekiti wa Umoja wa Afrika (AU), alishiriki kikamilifu katika majadiliano hayo, akisisitiza umuhimu wa ushirikiano wa kikanda na maendeleo jumuishi.

Mkutano huo uliongozwa na Mwenyekiti wa Umoja wa Afrika, Rais wa Jamhuri ya Burundi Mheshimiwa Évariste Ndayishimiye, ambapo ajenda kuu zilihusu kuharakisha utekelezaji wa miradi ya maendeleo, kuimarisha amani na usalama, pamoja na kukuza uchumi wa bara kwa manufaa ya wote.

Ushiriki wa Mheshimiwa Dkt. Samia unaendelea kudhihirisha dhamira ya Tanzania ya kuwa sehemu muhimu ya ujenzi wa Afrika yenye umoja, nguvu na ustawi wa pamoja.

#SamiaSuluhuHassan #Tanzania #AfricanUnion #AU #Diplomasia #Uongozi #Maendeleo #Afrika #Ushirikiano #GlobalLeadership

Wednesday, March 25, 2026

KIKWETE ATEULIWA KUWA MWAKILISHI WA NGAZI YA JUU WA MWENYEKITI WA KAMISHENI YA AU


Mwenyekiti wa Kamisheni ya Umoja wa Afrika (AUC), Mhe. Mahmoud Ali Youssouf, amemteua Rais Mstaafu wa Tanzania, Mhe. Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, kuwa Mwakilishi wa Ngazi ya Juu wa Mwenyekiti wa AUC katika eneo la Pembe ya Afrika na Bahari ya Shamu.

Uteuzi huo uliotangazwa rasmi leo, Machi 25, 2026, unalenga kuimarisha juhudi za Umoja wa Afrika katika kushughulikia changamoto za kisiasa, amani, na masuala ya kiusalama yanayoikabili kanda hiyo.

Kufuatia uteuzi huo, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan amempongeza Dkt. Kikwete na kueleza kuwa ni heshima kubwa kwake na kwa Tanzania. Aidha, amemtakia majukumu mema katika kuimarisha Umoja wa Afrika na kupata suluhu ya amani ya kudumu kwa manufaa ya Afrika na ulimwengu wote. 

Katika nafasi hiyo, Dkt. Kikwete atakuwa na jukumu la kuunga mkono jitihada za AU kupitia: kuendeleza diplomasia ya kuzuia migogoro na kuratibu mazungumzo jumuishi ya kisiasa. Aidha, kujenga uaminifu miongoni mwa wadau mbalimbali wa kikanda na kuimarisha ushirikiano wa kikanda unaolenga kukuza amani na utulivu wa kudumu.

Mhe. Dkt. Kikwete, kama Mwakilishi wa Ngazi ya Juu, atafanya kazi kwa uratibu wa karibu na AU na washirika muhimu wa kikanda na kimataifa, ikiwa ni pamoja na Mamlaka ya Kiserikali ya Maendeleo (IGAD), Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), Umoja wa Nchi za Kiarabu, na Umoja wa Mataifa (UN) ili kujenga amani na utulivu wa kudumu.

Ushirikiano huo ni muhimu kutokana na nafasi ya kimkakati ya Pembe ya Afrika na Bahari ya Shamu kwa biashara ya kimataifa na utulivu wa Bara la Afrika kwa ujumla.

Mhe. Youssouf ameeleza kuwa na imani kubwa na uzoefu, uongozi, na hekima za Dkt. Kikwete, na kwamba atatoa mchango mkubwa katika kuzisaidia nchi za kanda hiyo kukabiliana na changamoto zilizopo, kukuza ustawi pamoja na amani ya kudumu.

Uteuzi huu unakuja wakati ambapo eneo la Pembe ya Afrika na Bahari ya Shamu linaendelea kuhitaji ushirikiano wa karibu wa kidiplomasia ili kuhakikisha usalama wa kanda na ulinzi wa njia kuu za biashara duniani.




WILLIAM LUKUVI: SAFARI YA MWALIMU ALIYEGUSA TAIFA, SAUTI ILIYOJENGA SIASA ZA HUDUMA

Marehemu William Vangimembe Lukuvi alizaliwa Agosti 15, 1955 katika kijiji cha Mapogoro, mkoani Iringa—mahali palipomlea katika misingi ya nidhamu, uwajibikaji na uzalendo, ambavyo vilikuja kuwa alama ya maisha yake ya uongozi.

Alianza safari yake ya elimu katika Shule ya Msingi Kitanewa mwaka 1962 hadi 1970, kabla ya kujiunga na Chuo cha Ualimu Tabora (Tabora TTC) mwaka 1974 hadi 1975, alipohitimu na kuwa mwalimu. 

Akiwa darasani, hakufundisha tu masomo—alijenga misingi ya maadili na kuwasha taa za matumaini kwa kizazi cha vijana. Hata hivyo, ndani yake kulikuwa na wito mpana zaidi: wito wa kulitumikia taifa.

Mwaka 1995, alipochaguliwa kuwa Mbunge wa Jimbo la Ismani, ndipo safari yake ya kisiasa ilipoanza rasmi. Hakuwa tu mwakilishi wa wananchi; alikuwa sauti yao. Kwa zaidi ya miaka 30 mfululizo, alibaki kuwa chaguo la wananchi wake—uthibitisho wa imani, ukaribu na uaminifu alioujenga kwa vitendo.

Katika utumishi wake serikalini, Lukuvi alionyesha uthabiti na uelewa mpana wa masuala ya umma. Kuanzia mwaka 2010 hadi 2015, alihudumu kama Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera na Bunge), akisimamia uratibu wa shughuli za serikali bungeni kwa umahiri mkubwa. 

Baadaye, kati ya mwaka 2015 hadi 2022, aliongoza Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi—sekta nyeti inayogusa maisha ya kila Mtanzania—akiwa mstari wa mbele katika kusimamia rasilimali ardhi na mageuzi ya makazi.

Mwaka 2023, aliaminiwa zaidi na kuteuliwa kuwa mshauri wa Rais katika masuala ya kisiasa na kijamii, jukumu lililodhihirisha hekima yake ya muda mrefu. Alirejea tena serikalini kushika wadhifa wa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu), nafasi aliyoiendeleza kwa uadilifu na uzito hadi siku za mwisho za maisha yake.

Mnamo Machi 25, 2026, taifa lilipokea kwa masikitiko taarifa ya kifo chake, iliyotangazwa rasmi na Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan. Alifariki dunia katika Hospitali ya Benjamin Mkapa, Dodoma, alipokuwa akipatiwa matibabu ya matatizo ya moyo.

Kifo chake si tu mwisho wa maisha ya mtu—ni hitimisho la sura muhimu ya uongozi wa kizazi chake. Lukuvi alikuwa daraja kati ya wananchi na serikali, kiongozi aliyesikiliza, aliyetenda, na aliyesimama imara hata katika nyakati ngumu. 

Alibeba uzito wa dhamana ya umma kwa ujasiri na kuacha alama isiyofutika katika historia ya siasa za Tanzania.

Urithi wake unabaki kuwa funzo: kwamba uongozi si cheo, bali ni huduma; si mamlaka, bali ni uwajibikaji; na si maneno, bali ni vitendo vinavyoacha alama mioyoni mwa watu.

PIC YAAHIRISHA ZIARA BAADA YA KIFO CHA WAZIRI LUKUVI

Mkurugenzi Mkuu wa NHC Hamad Abdallah akimpokea Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma - PIC na wajumbe wake Mhe. Massanja Kadogosa walipowasili katika mradi wa Samia Housing Scheme Kawe.



Mkurugenzi Mkuu wa NHC Hamad Abdallah akiionesha Kamati ya PIC eneo ambalo zitajengwa nyumba nyingine za makazi pembeni ya mradi wa Samia Housing Scheme Kawe.


Mhandisi Grace Musita akiielezea Kamati ya PIC kwa undani kuhusu mradi wa Samia Housing Scheme Kawe.


Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma - PIC wakiingia katika moja ya nyumba.

Afisa sheria wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Elizabeth Malogo akisoma kanuni ya kuahirisha ziara hiyo

Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma - PIC Mhe. Massanja Kadogosa akihairisha ziara hiyo

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma (PIC) imeahirisha ziara yake katika miradi ya Samia Housing na 711 Kawe inayotekelezwa na Shirika la Nyumba la Taifa (NHC).

Mwenyekiti wa PIC, Masanja Kadogosa amewatangazia wajumbe wa kamati hiyo kuwa uamuzi huo umefikiwa kufuatia kifo cha Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Wenye Ulemavu), Mhe. William Lukuvi, kilichotokea leo Machi 25, 2026 katika Hospitali ya Benjamin Mkapa jijini Dodoma alipokuwa akipatiwa matibabu.

Kabla ya kuahirishwa kwa ziara hiyo, Kamati hiyo ilikuwa imetembelea mradi wa Samia Housing Scheme uliopo Kawe na kujionea uwekezaji mkubwa uliofanywa na NHC katika eneo hilo. Akiwa na wajumbe wa kamati hiyo, Mwenyekiti Kadogosa alipata fursa ya kusikiliza maelezo ya utekelezaji wa mradi huo kutoka kwa Mkurugenzi Mkuu wa NHC, Hamad Abdallah.

Katika maelezo yake, Mkurugenzi Mkuu alibainisha kuwa mradi huo wa majengo ya ghorofa kumi, unaojumuisha jumla ya nyumba 560, ulitekelezwa kikamilifu na wahandisi wa Shirika la Nyumba la Taifa, hatua inayodhihirisha uwezo wa ndani wa taasisi hiyo katika kusimamia na kutekeleza miradi mikubwa ya kimkakati.

Akitoa ufafanuzi wa kina kuhusu mradi huo, Msimamizi wa Utekelezaji, Mhandisi Grace Musita, alisema kuwa majengo hayo yanajumuisha nyumba za vyumba vitatu zenye ukubwa wa mita za mraba 89, ambazo zimeuzwa kwa shilingi milioni 192.7. 

Aidha, kuna nyumba 160 za vyumba viwili zenye ukubwa wa mita za mraba 68, zilizouzwa kwa shilingi milioni 147, pamoja na nyumba ndogo zenye ukubwa wa mita za mraba 21.2 zilizouzwa kwa shilingi milioni 38.8.

Aliongeza kuwa mradi huo ulianza Novemba 2022 na kukamilika Juni 2025, ambapo kwa sasa wakazi tayari wameanza kuishi, huku Shirika likiendelea kushughulikia dosari ndogo ndogo zinazojitokeza ili kuboresha zaidi huduma kwa wateja.

Mhandisi Musita alibainisha kuwa mradi huo umeleta manufaa makubwa kijamii na kiuchumi, ikiwemo kuzalisha ajira 11,800 kwa mafundi na wataalamu mbalimbali. Pia wanafunzi 630 kutoka taasisi mbalimbali ikiwemo Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na Taasisi ya Teknolojia Dar es Salaam (DIT) walipata mafunzo ya vitendo, ambapo kati yao wanafunzi 47 walipata ajira za kudumu na muda mfupi. Vilevile, vibarua 100 wasio na elimu rasmi lakini wenye nidhamu walipata ajira kupitia mradi huo.

Alisisitiza kuwa NHC ilitekeleza mradi huo kwa viwango vya juu kwa kuwa mkandarasi na mbunifu, huku malighafi zote zilizotumika zikifanyiwa vipimo na taasisi mbalimbali ikiwemo Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na Shirika la Viwango Tanzania (TBS), pamoja na kukaguliwa na mamlaka husika za Kinondoni na wataalamu wa ndani wa NHC.

Aidha, alieleza kuwa matumizi ya mitambo ya kisasa inayomilikiwa na Shirika, ikiwemo mtambo mkubwa wa kuzalisha zege, magari ya kusafirisha zege na pampu, yalichangia kukamilika kwa mradi huo kwa wakati na kwa ufanisi mkubwa.

Mradi wa Samia Housing Scheme Kawe umegharimu jumla ya shilingi bilioni 49, ambapo hadi sasa takribani shilingi bilioni 45 tayari zimetumika.

Hata hivyo, ziara ya Kamati hiyo haikuweza kuendelea katika mradi wa Kawe 711 kufuatia tukio hilo la msiba. Akisoma kanuni za kudumu za Bunge, Afisa Sheria wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Elizabeth Malogo, alinukuu kanuni namba 176 inayotaka shughuli za Bunge kuahirishwa endapo Mbunge atafariki dunia wakati wa shughuli za Bunge, ili kutoa nafasi kwa maombolezo.

TBC Yawajengea Uwezo Washitiri Uzalishaji wa Vipindi

Kaimu Mkurugenzi wa Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC), Bw. Gwakisa Mlawa akizungumza wakati wa kufunga Mkutano wa 110 wa wadau wa elimu k...