
Afisa Sheria Mwandamizi wa NHC, Scholastica Kilagane, alitoa elimu ya kina
kuhusu dhana ya hati pacha (Unit title)
Uongozi wa Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) umefanya kikao pamoja na wateja
wake wa nyumba za makazi za Samia Housing Scheme jana, tarehe 2/5/2026,
katika eneo la Kawe jijini Dar es Salaam, kwa lengo la kuwajengea uelewa wa
kina kuhusu umiliki wa nyumba za kisasa, hususan mfumo wa hati pacha pamoja
na kuimarisha misingi ya usimamizi wa pamoja wa makazi hayo.
Akizungumza katika kikao hicho, kilichohudhuriwa na wamiliki wa nyumba hizo
560 zilizopo Kawe Tanganyika Packers Dar es Salaam, Afisa Sheria Muandamizi
wa NHC, Scholastica Kilagane, alitoa elimu ya kina kuhusu dhana ya hati pacha
(Unit title), akieleza kuwa mfumo huo unampa mmiliki haki ya kumiliki sehemu
yake binafsi ya nyumba huku akishiriki umiliki wa maeneo ya pamoja kama vile
lifti, korido, ngazi, maeneo ya wazi na miundombinu mingine ya huduma.
Alisisitiza kuwa uelewa sahihi wa mfumo huo ni muhimu ili kuepusha migogoro ya
kisheria na kuhakikisha matumizi bora ya mali hizo.
“Hati pacha inalenga kuweka uwazi katika umiliki wa mali na kugawanya wazi haki
na wajibu wa kila mmiliki. Ni muhimu kwa kila mmiliki kuelewa kuwa pamoja na
kumiliki nyumba yake, ana wajibu wa kushiriki kikamilifu katika kusimamia maeneo
ya pamoja kwa mujibu wa sheria,” alieleza Kilagane.
Aidha, Kilagane alieleza umuhimu wa kuanzishwa kwa umoja wa wamiliki wa
nyumba (Owners Association), akibainisha kuwa huo ndio chombo rasmi cha
kisheria kitakachosimamia masuala yote ya pamoja ndani ya eneo hilo.
Alifafanua kuwa umoja huo utakuwa na viongozi watakaochaguliwa kwa mujibu
wa taratibu za kisheria, ikiwemo Mwenyekiti, Katibu na Mweka Hazina, huku kila
mmoja akiwa na majukumu mahsusi ya kuhakikisha uendeshaji
mzuri na uwajibikaji.
Naye Injinia Grace Msita, Meneja Miradi wa Shirika la Nyumba la Taifa (NHC),
akizungumza na wamiliki hao aliwahakikishia kuwa miundombinu yote ya Samia
Housing Scheme imekamilika kwa viwango vya juu vya ubora na usalama, huku
akisisitiza kuwa usimamizi madhubuti wa miradi hiyo wakati wa utekelezaji ni
sehemu ya dhamira ya NHC ya kutoa makazi endelevu na yenye thamani kwa
wananchi.
Alieleza kuwa NHC itaendelea kushirikiana na umoja wa wamiliki katika hatua
zote za wakati huu wa kipindi cha uangalizi yaani DLP wa mradi huo ili
kuhakikisha changamoto zinazojitokeza zinapatiwa ufumbuzi wa haraka
na kwa weledi, na hivyo kulinda uwekezaji wa kila mmiliki pamoja na kuhakikisha
mazingira ya kuishi yanabaki kuwa bora na ya kisasa.
Kwa upande wake, Meneja wa Milki wa NHC, France Bahangarwa, alisisitiza
wajibu wa wamiliki katika kuhakikisha uendelevu wa huduma ndani ya Samia
Housing Scheme. Alieleza kuwa ulipaji wa service charge ni sharti la kisheria
lisiloweza kuepukika kwani ndilo linalowezesha uendeshaji wa huduma muhimu
za pamoja.
“Huduma kama lifti, usafi wa mazingira, ulinzi, taa za maeneo ya pamoja na
matengenezo ya miundombinu haviwezi kuendelea bila michango ya wamiliki.
Hivyo, kila mmiliki ana wajibu wa kulipa service charge kwa wakati ili
kuhakikisha mazingira haya yanaendelea kuwa salama na yenye hadhi,” alisema
Bahangarwa.
Aliongeza kuwa pamoja na hilo, wamiliki wanapaswa kutekeleza majukumu yao
mengine ya kisheria ikiwemo kulipa kodi ya ardhi na kushiriki katika maamuzi
ya pamoja kupitia umoja wao. Pia alisisitiza umuhimu wa kuajiri kampuni ya
usimamizi wa milki au mtaalamu binafsi ili kuhakikisha shughuli za kila siku
za uendeshaji zinafanyika kwa weledi na kwa kuzingatia viwango vya kitaalamu.
“Usimamizi wa kitaalamu ni nguzo muhimu katika mafanikio ya miradi ya makazi
ya aina hii. Ni vyema wamiliki wakachagua njia bora ya usimamizi
itakayolinda thamani ya mali zao na kuboresha maisha yao kwa ujumla,”
aliongeza Bahangarwa.
Kwa upande wao, wamiliki wa nyumba katika Samia Housing Scheme
walieleza kuridhishwa na kikao hicho, wakitoa shukurani kwa Shirika la Nyumba
la Taifa kwa kuwapatia elimu hiyo muhimu.
Mmoja wa wamiliki alieleza kuwa, “Tunashukuru sana NHC kwa kutuletea elimu
hii. Imetusaidia kuelewa kwa undani haki na wajibu wetu kama wamiliki wa
nyumba za mfumo huu wa kisasa. Sasa tunaona umuhimu wa kushirikiana na
kuunda umoja imara kwa ajili ya maendeleo ya makazi yetu.”
Kwa ujumla, kikao hiki kimekuwa jukwaa muhimu la kuwawezesha wamiliki
kwa maarifa sahihi ya kisheria na kiutendaji, hatua inayotarajiwa kuimarisha
usimamizi wa pamoja, kuongeza thamani ya mali na kuhakikisha Samia Housing
Scheme inakuwa mfano bora wa makazi ya kisasa yanayosimamiwa kwa ufanisi
nchini.
Naye Meneja Mauzo na Masoko wa NHC, Deogratius Batakanwa alieleza kuwa
Samia Housing Scheme ni zaidi ya makazi; ni uwekezaji wenye thamani unaohitaji
uelewa sahihi wa kisheria na usimamizi wa pamoja ili kulinda na kukuza thamani
yake kwa muda mrefu.
“Kupitia mfumo wa hati pacha, kila mmiliki anapata umiliki halali wa sehemu
yake binafsi huku akishiriki umiliki wa maeneo ya pamoja. Huu ni mfumo wa
kisasa unaolenga kuongeza uwazi, kulinda uwekezaji na kuhakikisha mazingira
bora ya kuishi kwa wakazi wote,” alisema Batakanwa.
Alisisitiza kuwa uelewa wa mfumo huo unawawezesha wamiliki kufanya maamuzi
sahihi kuhusu mali zao na kushiriki kikamilifu katika uendeshaji wa makazi yao kwa
tija.
Katika kuimarisha usimamizi wa pamoja, Batakanwa alibainisha umuhimu wa
kuunda umoja wa wamiliki wa nyumba (Owners Association) utakaosimamia
masuala ya pamoja kwa weledi na uwazi. Alieleza kuwa uongozi wa umoja huo
utachaguliwa kwa kufuata taratibu rasmi na utakuwa na jukumu la kuhakikisha
huduma zote zinaendeshwa kwa ufanisi.
Katika hatua ya kuimarisha usimamizi wa pamoja, wamiliki wa Samia Housing
Scheme wamechagua uongozi wa umoja wao ukiongozwa na Mwenyekiti Catherine
Mrosso akisaidiwa na Makamu Mwenyekiti Eng. Juma Kiboko, huku nafasi ya
Katibu ikishikiliwa na Grace Lemunge akisaidiwa na Katibu Msaidizi George
Laurian, na Mweka Hazina akiwa Veronica Rukeha.
Wajumbe wa kamati hiyo ni Rehema Chonda, Ramadhani Mshana, Dkt. Petronila
Ngiloi, Bi. Hadija Mwema, Isack Ngovi, Faith Kayombo, Robert Matapu, Jesca
Macharia, Salma Juma, Dkt. Oreste Munishi na Grace Mwaihojo.
Kwa upande wao, wamiliki wa nyumba walitoa shukurani kwa NHC kwa
kuandaa kikao hicho, wakieleza kuwa elimu waliyoipata imewasaidia kuelewa
thamani halisi ya uwekezaji wao na namna bora ya kuilinda.
“Tunathamini jitihada za NHC kutuelimisha. Sasa tunaelewa kuwa mafanikio ya
makazi haya yanategemea ushirikiano wetu na utekelezaji wa majukumu yetu
ipasavyo,” walieleza baadhi ya wamiliki.
Kwa ujumla, kikao hiki kimeweka msingi thabiti wa kuifanya Samia Housing Scheme
kuwa mfano wa makazi ya kisasa yanayosimamiwa kwa ufanisi, huku yakitoa
thamani ya juu kwa wamiliki wake—ikiwa ni sehemu ya dhamira ya NHC ya
kuendeleza makazi bora na uwekezaji salama kwa Watanzania.