Tuesday, September 01, 2026

SERIKALI, BARRICK ZAIMARISHA UBIA WA KIMKAKATI SEKTA YA MADINI

 

Serikali na Kampuni ya Barrick Corporation zimeendelea kuimarisha ushirikiano wao wa kibiashara na uwekezaji katika sekta ya madini, huku pande hizo mbili zikisisitiza umuhimu wa kujenga mazingira yatakayowezesha miradi inayotekelezwa kupitia Twiga Minerals Corporation Limited (TWIGA) kukua, kuongeza uzalishaji na kutoa manufaa endelevu kwa Taifa na wawekezaji.

Mwelekeo huo umejitokeza Jumanne, Septemba 1, 2026, wakati Msajili wa Hazina, Bw. Nehemiah Mchechu, alipokutana na kufanya mazungumzo na wawakilishi wa Barrick Corporation pamoja na uongozi wa TWIGA katika Ofisi ya Msajili wa Hazina (OTR), jijini Dar es Salaam.

Mazungumzo hayo yalijikita katika maendeleo ya biashara, uendeshaji wa miradi na masuala mbalimbali yanayohusu uwekezaji unaosimamiwa kupitia TWIGA, kampuni inayowakutanisha Serikali na Barrick kama wanahisa wenza katika shughuli za uchimbaji wa dhahabu nchini.

Miradi iliyojadiliwa ni pamoja na migodi ya North Mara na Bulyanhulu, pamoja na Buzwagi, ambao kwa sasa upo katika hatua za mwisho za kufungwa.

Ujumbe wa Barrick uliongozwa na Roelie Gey Von Pittius, Meneja wa Fedha wa Barrick kwa Afrika na Mashariki ya Kati, akiambatana na Candace Simpson, Meneja wa Kodi wa Afrika na Mashariki ya Kati; Melkiory Ngido, Meneja wa Barrick nchini Tanzania; na Judith Chambua, Meneja wa Kodi wa Barrick Tanzania.

Barrick Gold Corporation ni moja ya kampuni kubwa zaidi duniani za uchimbaji wa madini ya dhahabu na shaba, ikiwa na makao makuu yake mjini Toronto, Ontario, Canada.

SERIKALI YATAKA UBIA WENYE TIJA NA UENDELEVU

Akizungumza katika kikao hicho, Bw. Mchechu alisema Serikali, kupitia OTR, itaendelea kutoa ushirikiano unaohitajika katika kushughulikia changamoto zinazoweza kujitokeza katika utekelezaji wa miradi ya TWIGA, kwa lengo la kuhakikisha shughuli zake zinaendeshwa kwa ufanisi na kuendelea kuongeza mchango wake katika uchumi wa Tanzania.

Alisema sekta ya madini ina nafasi muhimu katika ukuaji wa uchumi na mapato ya Serikali, ikiwemo kupitia gawio linalotokana na uwekezaji wa Serikali katika kampuni zinazofanya shughuli za madini.

“Tunauthamini sana mchango wa aina ya ushirikiano tulionao na Barrick,” alisema Bw. Mchechu.

Kwa mujibu wa Msajili wa Hazina, uzoefu uliopatikana kupitia ushirikiano na Barrick umeendelea kuwa muhimu katika kuimarisha uwezo wa Serikali kusimamia uwekezaji mkubwa katika sekta ya madini na kujenga ubia wenye manufaa kwa pande zote.

Alisisitiza pia umuhimu wa taasisi za Serikali kuwa na uratibu na uelewa wa pamoja katika kushughulikia masuala yanayogusa uwekezaji mkubwa wa kimkakati.

“Katika masuala muhimu kama haya yanayomhusu mshirika muhimu katika biashara muhimu, ni lazima Serikali izungumze kwa sauti moja,” alisema.

UWEKEZAJI WA MUDA MREFU

Bw. Mchechu alisema dhamira ya Serikali ni kuona mazingira ya biashara na uwekezaji yanaendelea kuwa na uthabiti unaowezesha kampuni kufanya mipango ya muda mrefu na kuendeleza uwekezaji wenye manufaa kwa vizazi vijavyo.

“Tunataka kuwa na biashara ambayo inaweza kuendelea kwa utulivu kizazi hadi kizazi na kustahimili tawala mbalimbali za kisiasa,” alisema.

Kauli hiyo inaweka msisitizo katika kujenga uhusiano wa muda mrefu wa kibiashara, wenye msingi wa mazungumzo, uelewa wa pamoja na mazingira yanayowezesha uwekezaji kuendelea kukua.

Kwa upande wake, Von Pittius alisema Barrick inathamini ushirikiano wake na Serikali ya Tanzania na itaendelea kufanya kazi kwa karibu na mamlaka husika katika masuala yanayohusu shughuli na uwekezaji wake nchini.

Alieleza utayari wa kampuni hiyo kuendelea kushirikiana na Serikali katika maeneo yenye maslahi ya pamoja kwa maendeleo ya sekta ya madini.

Mazungumzo hayo yanaendeleza ushirikiano kati ya Serikali na Barrick katika kuimarisha TWIGA kama jukwaa la ubia wa kibiashara, huku msisitizo ukiwekwa katika kuongeza ufanisi, uzalishaji na thamani inayotokana na rasilimali za madini kwa manufaa ya Taifa na wadau wa uwekezaji.

TANZANIA, UINGEREZA ZATAZAMA FURSA MPYA ZA UWEKEZAJI SEKTA YA MADINI










 Tanzania na Uingereza zimeendelea kuimarisha diplomasia ya kiuchumi, safari hii zikiweka mkazo katika uwekezaji, uongezaji thamani wa madini na namna sekta hiyo inavyoweza kuleta manufaa mapana zaidi kwa wananchi na uchumi wa Taifa.

Hatua hiyo imejidhihirisha leo jijini Dodoma, wakati Waziri wa Madini, Mhe. Anthony Mavunde, alipokutana na Balozi wa Uingereza nchini Tanzania, Mhe. Marianne Young, kwa mazungumzo yaliyolenga kuchambua fursa zilizopo katika sekta ya madini na maeneo mapya ya ushirikiano kati ya mataifa hayo mawili.

Mazungumzo hayo yana umuhimu mkubwa katika kipindi ambacho Tanzania inaendelea kuweka msisitizo katika kuhakikisha rasilimali zake za madini haziondoki nchini zikiwa malighafi pekee, bali zinaongezewa thamani ili kuchochea uwekezaji wa viwanda, kuongeza ajira, kukuza biashara na kupanua mchango wa sekta hiyo katika uchumi.

Kwa mantiki hiyo, kuvutia uwekezaji katika sekta ya madini hakulengi tu kuongeza mitaji, bali pia kujenga minyororo ya thamani inayoweza kutoa nafasi kwa Watanzania kushiriki katika hatua mbalimbali—kuanzia uchimbaji na uchakataji hadi biashara na huduma zinazohusiana na sekta hiyo.

Katika mazungumzo hayo, pande hizo mbili pia zimeweka mkazo katika umuhimu wa ukuaji wa sekta ya madini unaoshirikisha wote, ili manufaa yatokanayo na rasilimali hizo yaweze kugusa maisha ya wananchi na kuchangia maendeleo endelevu.

Mkutano wa Mhe. Mavunde na Balozi Young unaendeleza uhusiano wa muda mrefu kati ya Tanzania na Uingereza, huku diplomasia ya kiuchumi ikizidi kuwa daraja muhimu la kufungua fursa mpya za biashara, uwekezaji na ushirikiano wa maendeleo.

Tanzania na Uingereza zimeahidi kuendelea kufanya kazi pamoja katika maeneo yenye maslahi ya pande zote, kwa lengo la kuimarisha ustawi wa mataifa hayo mawili na kuhakikisha ushirikiano wao unazalisha matokeo yanayoonekana katika uchumi na maisha ya wananchi.

NDEJEMBI: NITAMSAIDIA RAIS SAMIA KWA HEKIMA, UADILIFU NA UAMINIFU




Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Deogratius Ndejembi, amewahakikishia Watanzania kuwa atatekeleza majukumu yake kwa uadilifu, umakini na kujituma, huku akiahidi kutumia nafasi yake kumsaidia Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kuwatumikia wananchi na kusukuma mbele maendeleo ya Taifa.

Makamu wa Rais ametoa kauli hiyo leo, Septemba 1, 2026, alipowasalimu wananchi wa Mbuyuni, Wilaya ya Moshi mkoani Kilimanjaro, waliojitokeza kwa wingi kumlaki akiwa katika ziara binafsi mkoani humo.

Akizungumza na wananchi hao, Mhe. Ndejembi aliwashukuru kwa mapokezi yao na kuwaomba waendelee kumuombea Rais Samia pamoja na yeye, akisisitiza kuwa maombi na imani ni nyenzo muhimu katika kuwawezesha viongozi kutekeleza dhamana waliyopewa kwa hekima na ufanisi.

Amesema anatambua ukubwa wa jukumu alilopewa na kwamba ataendelea kumsaidia Rais Samia kwa hekima, utii na uaminifu, huku akishirikiana kwa karibu na viongozi wa Serikali pamoja na wananchi katika kutekeleza majukumu yake.

“Endeleeni kumuombea Mheshimiwa Rais na kuniombea mimi pia, ili niweze kumsaidia kwa hekima na utii katika jukumu kubwa la kuwatumikia Watanzania,” amesisitiza Makamu wa Rais.

Katika ujumbe uliopokelewa kwa shangwe na wananchi, Mhe. Ndejembi alirejea kauli aliyowahi kuitoa kwa wananchi wa Chamwino mkoani Dodoma mara baada ya kuapishwa, akisema: “Sitawazingua wana wala sitamzingua Mama.”

Kauli hiyo imebeba ujumbe wa dhamira yake ya kuwa mshirika mwaminifu katika uongozi, anayelenga kuimarisha mshikamano, ushirikiano na utendaji wenye tija kwa maslahi ya Taifa.

Awali, Makamu wa Rais aliwasili katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro (KIA) ambako alipokelewa na viongozi mbalimbali wa Serikali, viongozi wa dini pamoja na wajumbe wa Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa wa Kilimanjaro.

Ziara hiyo ni miongoni mwa safari za mwanzo za Mhe. Ndejembi mkoani Kilimanjaro tangu kuapishwa kwake kuwa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

RAIS SAMIA ASHUHUDIA UAPISHO WA HICHILEMA, TANZANIA NA ZAMBIA ZAZIDI KUIMARISHA UNDUGU







LUSAKA, Zambia

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, amehudhuria sherehe za kuapishwa kwa Rais wa Zambia, Mhe. Hakainde Hichilema, jijini Lusaka, ikiwa ni ishara ya kuendelea kuimarika kwa uhusiano wa kihistoria, kidiplomasia na kiuchumi kati ya Tanzania na Zambia.

Rais Hichilema ameapishwa kuongoza Zambia kwa muhula wa pili, baada ya kushinda uchaguzi mkuu uliofanyika Agosti 13, 2026.

Ushiriki wa Rais Samia katika sherehe hizo unaakisi undugu wa muda mrefu baina ya mataifa hayo mawili, uliojengwa tangu enzi za waasisi wa mataifa hayo, Hayati Mwalimu Julius Nyerere na Hayati Dkt. Kenneth Kaunda.

Uhusiano huo umeendelea kupanuka kutoka katika undugu wa kihistoria na kisiasa na sasa kujikita zaidi katika biashara, uwekezaji, nishati, miundombinu na usafirishaji, maeneo ambayo yana umuhimu mkubwa kwa maendeleo ya uchumi wa nchi hizo mbili.

Miongoni mwa miradi ya kimkakati inayozidi kuunganisha Tanzania na Zambia ni ufufuaji wa Reli ya Tanzania na Zambia (TAZARA), ujenzi wa bomba jipya la mafuta la TAZAMA, pamoja na juhudi za kuimarisha muunganisho wa gridi za umeme kati ya Zambia, Tanzania na Kenya.

BIASHARA YAPAA, UWEKEZAJI WAONGEZEKA

Uhusiano huo pia umeendelea kutoa matokeo yanayoonekana katika biashara. Katika muhula wa kwanza wa Rais Hichilema, thamani ya biashara kati ya Tanzania na Zambia iliongezeka kutoka Sh bilioni 320.978 mwaka 2021 hadi Sh bilioni 820.359 mwaka 2024, ikiwa ni zaidi ya mara mbili ndani ya kipindi hicho.

Zambia pia ni mtumiaji wa pili kwa ukubwa wa Bandari ya Dar es Salaam, jambo linaloifanya Tanzania kuwa lango muhimu la kibiashara kwa Zambia na nchi nyingine zisizo na bahari katika ukanda wa Kusini na Kati mwa Afrika.

Kwa upande wa uwekezaji, Zambia imewekeza katika miradi 29 nchini Tanzania yenye thamani ya Dola za Marekani milioni 86.34, ambayo imezalisha ajira 1,204. Wakati huohuo, Watanzania wanamiliki hisa katika kampuni kubwa na za kati takribani 965 nchini Zambia.

Mahudhurio ya Rais Samia katika sherehe hizo, hivyo, hayabebi tu ujumbe wa kidiplomasia, bali yanaendelea kusisitiza dhamira ya Tanzania ya kutumia uhusiano wake wa kihistoria na Zambia kufungua fursa zaidi za biashara, uwekezaji, ajira na maendeleo ya wananchi wa mataifa yote mawili.

Kwa Tanzania na Zambia, urafiki uliojengwa na waasisi wa mataifa hayo unaendelea kuingia katika sura mpya—kutoka undugu wa kihistoria kuelekea ushirikiano wa kimkakati wa kiuchumi na maendeleo ya pamoja.

Friday, August 28, 2026

BUNGE LAMTHIBITISHA NDEJEMBI KWA ASILIMIA 100 UMAKAMU WA RAIS.










Waziri Mkuu asema anatosha, kiti kimempata mtu sahihi wa kumsaidia Mheshimiwa Rais.

BUNGE la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania leo (Ijumaa, Agosti 28, 2026) limemthibitisha Mheshimiwa Deogratius Ndejembi kuwa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mheshimiwa Ndejembi amepitishwa kwa asilimia 100 ya kura zote 324 zilizopigwa na waheshimiwa wabunge, ambapo amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa imani aliyoionesha kwake kwa kumteua kuwa Makamu wa Rais na katika nafasi nyingine mbalimbali za uongozi.

Pia Mheshimiwa Ndejembi amelishukuru Bunge kwa imani kubwa waliyompa kiasi cha kumpigia kura kwa asilimia mia moja.

Mapema akiwasilisha hoja ya kuthibitisha uteuzi wa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba amesema Mheshimiwa Deogratius Ndejembi anatosha na ni mtu sahihi wa kumsaidia Mheshimiwa Rais katika nafasi ya Makamu wa Rais, 

akiitaja kuwa ni nafasi yenye dhamana na majukumu makubwa katika uongozi wa nchi.

"Majukumu hayo yanahitaji mtu mwenye uzoefu wa uongozi, uelewa mpana wa shughuli za Serikali, uwezo wa kufanya kazi kwa karibu na Rais, busara katika kushughulikia masuala ya kitaifa, pamoja na uwezo wa kuratibu na kufuatilia utekelezaji wa majukumu mbalimbali ya Serikali," amesema Dkt. Mwigulu.

"Mheshimiwa Rais amemteua Mheshimiwa Deogratius John Pancras Ndejembi kwa kuzingatia, pamoja na mambo mengine, uzoefu alioujenga katika uongozi wa kisiasa na katika nafasi mbalimbali za Serikali," ameongeza Waziri Mkuu.

Dkt. Mwigulu amesisitiza kuwa uzoefu wa uongozi alionao Mheshimiwa Deogratius Ndejembi unadhihirisha kuwa ni mtu sahihi kutumikia wadhifa wa Makamu wa Rais.

"Mheshimiwa Deogratius John Pancras Ndejembi si mgeni katika uongozi wa Umma na katika siasa za nchi yetu. Kabla ya kuwa Mbunge, Mheshimiwa Ndejembi alihudumu kama Mkuu wa Wilaya katika Wilaya ya Kongwa. Mheshimiwa Spika, baada ya kuchaguliwa kuwa Mbunge, Mheshimiwa Ndejembi ameendelea kuaminiwa na Mheshimiwa Rais na kupewa majukumu mbalimbali ndani ya Serikali."

"Amehudumu katika nafasi ya Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora; Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa; Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu; Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, kabla ya kuhudumu kama Waziri wa Nishati," ameongeza Waziri Mkuu.

Dkt. Mwigulu amesema katika kipindi ambacho amehudumu ndani ya Serikali, Mheshimiwa Ndejembi ameonesha uwezo wa kubeba majukumu mbalimbali na kufanya kazi katika sekta zenye mahitaji na changamoto zinazotofautiana, akisisitiza kuwa uzoefu huo ni muhimu kwa Makamu wa Rais ambaye, kwa nafasi yake, anatakiwa kuwa tayari kumsaidia Rais katika masuala mbalimbali ya Jamhuri ya Muungano na kutekeleza majukumu yoyote atakayokabidhiwa kwa mujibu wa Katiba.

"Kwa kuzingatia majukumu ya Kikatiba ya Makamu wa Rais niliyoyaeleza, pamoja na uzoefu wa kisiasa, kiutawala na kiutendaji wa Mheshimiwa Deogratius John Pancras Ndejembi, Serikali inaamini kuwa ana uwezo wa kutekeleza kwa uaminifu na ufanisi majukumu ya nafasi ya Makamu wa Rais na kumsaidia Mheshimiwa Rais katika kuendeleza shughuli za Serikali na maendeleo ya Taifa letu," amefafanua Dkt. Mwigulu.

RAIS SAMIA AWAAGA WANAFUNZI WA SAMIA SCHOLARSHIP EXTENDED WANAOKWENDA MASOMONI IRELAND NA URUSI

 

Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania akiwa kwenye mazungumzo na wanafunzi walionufaika na Ufadhili wa Samia Scholarship Extended katika Sayansi ya Data, Akili Unde na Sayansi Shirikishi, Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 28 Agosti, 2026. Mhe. Rais Dkt. Samia alizungumza na kuagana na wanafunzi hao ambao wanaoenda masomoni nchini Ireland na Urusi












Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, amefanya mazungumzo na kuwaaga wanafunzi walionufaika na Samia Scholarship Extended wanaokwenda kuendelea na masomo nchini Ireland na Urusi, katika hafla iliyofanyika Ikulu jijini Dar es Salaam, Agosti 28, 2026.

Wanafunzi hao watapata fursa ya kujiendeleza katika maeneo ya kimkakati ya Sayansi ya Data, Akili Unde (Artificial Intelligence) na Sayansi Shirikishi, ikiwa ni sehemu ya jitihada za Serikali ya Awamu ya Sita za kuwekeza katika maarifa, teknolojia na rasilimali watu yenye ujuzi unaoendana na mahitaji ya dunia ya sasa na yajayo.

Mazungumzo ya Mhe. Rais na wanafunzi hao yamebeba ujumbe wa matumaini na dhamira ya Tanzania ya kuwajengea vijana uwezo wa kushindana katika medani za kimataifa, huku wakitarajiwa kurejesha maarifa na ujuzi watakaoupata kwa manufaa ya Taifa.

Kupitia Samia Scholarship Extended, Serikali inaendelea kufungua milango ya elimu ya kiwango cha juu kwa vijana wa Kitanzania na kuandaa kizazi cha wataalamu kitakachochangia katika mageuzi ya kidijitali, ubunifu na maendeleo endelevu ya Taifa.

Safari yao kwenda Ireland na Urusi si safari ya elimu pekee, bali ni uwekezaji katika mustakabali wa Tanzania.

Thursday, August 27, 2026

WAZIRI MKUU DKT. MWIGULU AMPONGEZA NDEJEMBI, AMSIFIA KWA UADILIFU NA UCHAPAKAZI







Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba, amempongeza Mhe. Deogratius John Ndejembi kwa kuaminiwa na Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, pamoja na vyombo vya maamuzi vya Chama Cha Mapinduzi (CCM), kuelekea kushika dhamana ya Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Akizungumza Bungeni jijini Dodoma leo, Alhamisi, Agosti 27, 2026, wakati wa kipindi cha Maswali na Majibu kwa Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu amesema Ndejembi amejijengea rekodi ya kuwa kiongozi mahiri, makini na mchapakazi, anayetekeleza majukumu yake kwa bidii kwa lengo la kuleta manufaa kwa Watanzania.

“Deogratius Ndejembi kama kiongozi ni kiongozi mahiri sana, ni kiongozi makini, kiongozi mchapakazi anayefanya kazi bila kuchoka ili Watanzania waweze kupata manufaa.” amesema Dkt. Mwigulu.

Waziri Mkuu pia amempongeza Rais Samia kwa kutambua uwezo na sifa za kiuongozi za Ndejembi, akieleza kuwa pamoja na uchapakazi wake, ana sifa za unyenyekevu, upole na utu, ambazo ni muhimu katika kubeba dhamana kubwa ya kitaifa.

Aidha, Dkt. Mwigulu amemhakikishia Ndejembi ushirikiano kutoka kwake na Mawaziri wenzake katika utekelezaji wa majukumu yake, hususan katika kusimamia na kutekeleza maelekezo ya Rais Samia yanayolenga kuendeleza ujenzi wa Tanzania.

Kauli hiyo inaonesha imani katika uwezo, uzoefu na sifa za kiuongozi za Ndejembi, huku ikisisitiza umuhimu wa mshikamano na ushirikiano wa viongozi katika kuendeleza utekelezaji wa mipango ya maendeleo ya Taifa.

SERIKALI, BARRICK ZAIMARISHA UBIA WA KIMKAKATI SEKTA YA MADINI

  Serikali na Kampuni ya Barrick Corporation zimeendelea kuimarisha ushirikiano wao wa kibiashara na uwekezaji katika sekta ya madini, huku...