Thursday, February 12, 2026

Rais Dkt. Samia Awasili Addis Ababa Kushiriki Mkutano wa 39 wa Wakuu wa Nchi wa AU




Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, amewasili katika Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Bole, Jijini Addis Ababa, Ethiopia, tarehe 12 Februari 2026, kwa ajili ya kushiriki Mkutano wa 39 wa Kawaida wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Umoja wa Afrika (AU).

Ushiriki wa Rais Dkt. Samia katika mkutano huo wa ngazi ya juu unadhihirisha dhamira thabiti ya Tanzania kuendelea kuchangia kikamilifu katika ajenda za maendeleo, amani na usalama barani Afrika. Mkutano huo unawakutanisha viongozi wakuu wa nchi wanachama wa AU kujadili masuala ya kimkakati yanayohusu ustawi wa bara, ikiwemo maendeleo ya kiuchumi, ushirikiano wa kikanda, mabadiliko ya tabianchi, pamoja na mageuzi ya taasisi za Umoja wa Afrika.

Mara baada ya kuwasili, Rais Dkt. Samia alipokelewa rasmi na Waziri wa Kazi na Ukuzaji wa Ujuzi wa Ethiopia, Mheshimiwa Muferihat Kamil Ahmed, pamoja na viongozi wengine waandamizi wa Serikali ya Ethiopia na maafisa wa Ubalozi wa Tanzania nchini humo.

Katika mkutano huo, viongozi wanatarajiwa kupokea na kujadili taarifa mbalimbali za utekelezaji wa maazimio ya awali ya AU, pamoja na kuweka mikakati mipya ya kuimarisha ajenda ya Afrika ya maendeleo jumuishi na endelevu. Aidha, mkutano huo utatoa fursa kwa Rais Dkt. Samia kufanya mazungumzo ya kando na viongozi wengine wa Afrika kwa lengo la kuimarisha ushirikiano wa kidiplomasia na kiuchumi.

Ushiriki wa Tanzania katika jukwaa hilo muhimu unaendelea kuiweka nchi katika nafasi ya kimkakati ndani ya bara, sambamba na kuendeleza sera ya diplomasia ya uchumi inayolenga kuvutia uwekezaji, kupanua masoko na kuimarisha mahusiano ya kimataifa.

Mkutano wa 39 wa Kawaida wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Umoja wa Afrika unatarajiwa kuhitimishwa kwa kupitisha maazimio yatakayochochea kasi ya utekelezaji wa Ajenda 2063 – dira ya muda mrefu ya maendeleo ya bara la Afrika.

SERIKALI YAPUNGUZA ADA ZA USAJILI WA VYOMBO VYA HABARI MTANDAONI; MWANA FA AAGIZA MALIPO YA WAFANYAKAZI YASHUGHULIKIWE NDANI YA WIKI MOJA

 Naibu Waziri wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Hamis Mwinjuma maarufu kama Mwana FA, akizungumza wakati akifungua rasmi Mkutano Mkuu wa Mwaka wa Vyombo vya Utangazaji unaoandaliwa na Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA)

Naibu Waziri wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Hamis Mwinjuma maarufu kama Mwana FA, akizungumza wakati akifungua rasmi Mkutano Mkuu wa Mwaka wa Vyombo vya Utangazaji unaoandaliwa na Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) katika Ukumbi wa New Generation jijini Dodoma.








Naibu Waziri wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Hamis Mwinjuma maarufu kama Mwana FA, akizungumza wakati akifungua rasmi Mkutano Mkuu wa Mwaka wa Vyombo vya Utangazaji unaoandaliwa na Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) katika Ukumbi wa New Generation jijini Dodoma.

Naibu Waziri wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Hamis Mwinjuma maarufu kama Mwana FA, akizungumza wakati akifungua rasmi Mkutano Mkuu wa Mwaka wa Vyombo vya Utangazaji unaoandaliwa na Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA)


Na Mwandishi Wetu

Serikali imepunguza kwa kiasi kikubwa ada za maombi ya leseni kwa vyombo vya habari mtandaoni, kutoka shilingi laki tano hadi 50,000= huku ada ya maombi ikiwa shilingi 10,000/= tu kutoka shilingi 50,000/= hatua inayotajwa kuwa mkombozi kwa wanahabari na wamiliki wa blogu na Online Tv nchini.

Hatua hiyo imetangazwa na Naibu Waziri wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Hamis Mwinjuma maarufu kama Mwana FA, wakati akifungua rasmi Mkutano Mkuu wa Mwaka wa Vyombo vya Utangazaji unaoandaliwa na Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) katika Ukumbi wa New Generation jijini Dodoma.

Mbali na kupunguza ada hizo, Mwinjuma ameielekeza TCRA kushirikiana na Bodi ya Ithibati kuhakikisha wafanyakazi wa vyombo vya habari wanalipwa stahiki zao kwa wakati, wakiwemo wale wanaodai mishahara ya zaidi ya miezi sita.

Amesisitiza kuwa ndani ya wiki moja anatarajia kupokea mrejesho wa hatua zilizochukuliwa kuhusu suala hilo.

Amesema Serikali inayoongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan itaendelea kuboresha mazingira ya ufanyaji kazi kwa vyombo vya habari, huku akisisitiza umuhimu wa ubora wa maudhui, kuzingatia maadili ya taaluma na kulinda haki miliki.

“Haki ya kupata taarifa ni ya kila Mtanzania, hivyo vyombo vya habari vinapaswa kuwafikia wananchi wote bila upendeleo,” amesisitiza.

Aidha, amesema Wizara itaendelea kuimarisha mazingira ya sekta hiyo ili wananchi wa vijijini wanufaike na huduma za utangazaji kwa urahisi, sambamba na kuhimiza matumizi ya teknolojia za kisasa ikiwemo Akili Unde (AI) kwa tija.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Chama cha Watangazaji Huru Tanzania (NIBA), Amos Ngosha, ameomba Serikali kupunguza wingi wa tozo zinazoikabili sekta hiyo, akieleza kuwa vyombo vya habari hulipa zaidi ya tozo 19 kila mwaka chini ya sheria tofauti, hali inayodhoofisha uwezo wao kifedha na kusababisha baadhi kushindwa kuendelea na huduma au kufungiwa.


Naye Mkurugenzi Mkuu wa TCRA, Dkt. Jabir Bakari, amesema mwaka 2025 jumla ya wanahabari 2,054 wamepatiwa mafunzo ya kuwajengea uwezo, huku usikivu wa redio ukifikia asilimia 85 na usambazaji wa televisheni kupitia satelaiti kufikia asilimia 100.

Hadi Desemba 2025, jumla ya leseni 770 za utangazaji zilikuwa zimetolewa, huku TCRA ikiwa na mpango wa kuanzisha mfumo wa redio kidijitali ili kuendana na maendeleo ya teknolojia na mahitaji ya soko la mawasiliano.

Mkutano huo wa siku mbili, unaofanyika Februari 12 na 13, 2026, umewakutanisha viongozi na wadau wa sekta ya utangazaji kujadili namna ya kuimarisha na kupanua huduma za utangazaji nchini.

AKWILAPO ATEMBELEA ENEO UNAPOJENGWA UWANJA WA AFCON ARUSHA

Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Leonard Akwilapo akipata maelezo ya maendeleo ya ujenzi wa uwanja wa mpira unaotarajiwa kutumika katika mashindano ya mataifa ya afrika (AFCON 2027) jijini Arusha jana.
Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Leonard Akwilapo (Kushoto) na Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Ardhi Bi. Lucy Kabyemera wakipata maelezo ya mradi wa viwanja vinavyozunguka uwanja wa AFCON Arusha jana alipofanya ziara katika eneo hilo.

Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Leonard Akwilapo (wa tatu kulia) na Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Ardhi Bi. Lucy Kabyemera (kushoto) wakielekea katika uwanja wa AFCON wakati wa ziara ya siku moja katika maeneo ya uwanja huo jana. (PICHA NA WIZARA YA ARDHI)

 Na Munir Shemweta, WANMM, ARUSHA.

Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Akwilapo tarehe 11 Februari 2026 ametembeleo eneo unapojengwa uwanja wa kisasa wa mpira kwa ajili Mashindano ya Fainali za Mataifa ya Afrika (AFCON 2027) mkoani Arusha.

Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi imetekeleza Mradi wa Kupanga, Kupima na Kumilikisha Ardhi katika eneo lililopo pembezoni unapojengwa Uwanja wa mpira wa Afcon katika kata ya Olmoti Jiji la Arusha, mkoani Arusha.

Hata hivyo, pamoja na viwanja kuuzwa kwa ajili ya matumizi mbalimbali lakini kuna baadhi ya waliochukua viwanja kushindwa kukamilisha malipo ndani ya muda huku baadhi waliomilikishwa wakishindwa kuendeleza maeneo yao.

Akiwa katika eneo la uwanja huo, Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo alijionea maendeleo ya ujenzi wa uwanja huo ambapo alipongeza jitihada zinazofanyika za kuhakikisha uwanja huo unakamilika kwa wakati na hatimaye kutumika katika mashindano hayo makubwa ya Afrika.

Akigeukia wananchi waliochukua viwanja na kushindwa kukamilisha malipo kwa wakati, Mhe Akwilapo amewataka kuhakikisha wanafanya malipo ndani ya siku kumi na tano kuanzia tarehe 12 Februari 2026.

“Kuna wananchi walioomba viwanja katika maeneo yanayozunguka uwanja wa AFCON 2027 na kushindwa kukamilisha malipo ya viwanja hivyo, wanatakiwa kulipa ndani ya siku kumi na tano na baada ya hapo tutawanyang’anya na kuwapatia wengine”. Amesema Akwilapo

Aidha, amesisitiza wananchi wenye hati milki za ardhi katika eneo linalozunguka uwanja huo kuhakikisha wanafanya maendelezo kwenye maeneo yao huku akiweka bayana kuwa, kama kuna mtu anayedhani hawawezi kufanya maendelezo katika muda wa kuelekea Mashindano ya AFCON 2027 basi airejeshe hati ili kupatiwa wale wanaoweza kufanya maendelezo.

Ujenzi wa mradi wa uwanja wa AFCON Arusha kwa sasa umefikia asilimia 74 na unatarajiwa kukamilika Julai, 2026.

DKT. MATARAGIO APOKELEWA RASMI WIZARA YA NISHATI




Katibu Mkuu Wizara ya Nishati anayeshughulikia Mafuta na Gesi Asilia, Dkt. James Mataragio ameripoti  na kupokelewa rasmi katika Ofisi Ndogo za Wizara jijini Dar es Salaam mara baada ya kuapishwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, mwanzoni mwa wiki hii.

Katika maboresho ya muundo wa Wizara ya Nishati yaliyofanywa na Mhe. Rais, Wizara imepata Makatibu Wakuu wawili. Mhandisi Felchesmi Mramba ameendelea na wadhifa wake kama Katibu Mkuu anayeshughulikia Umeme na Nishati Jadidifu, huku Dkt. James Mataragio akiteuliwa kuwa Katibu Mkuu anayeshughulikia Mafuta na Gesi Asilia.

Mapokezi ya Dkt. Mataragio yameongozwa na Katibu Mkuu anayeshughulikia Umeme na Nishati Jadidifu, Mhandisi Felichesmi Mramba, yakihudhuriwa na baadhi ya wajumbe wa Menejimenti pamoja na Wakuu wa Taasisi zilizo chini ya Wizara, mapema leo tarehe 12 Februari, 2026.

WATER AID WAJA NA MPANGO WA BILIONI 94.62 KUIMARISHA HUDUMA ZA MAJI HANANG

 




Na John Walter-Manyara

Wizara ya Maji imezindua mpango maalum wa uwekezaji katika maji safi, usafi wa mazingira na usafi binafsi wenye thamani ya shilingi bilioni 94.62, utakaotekelezwa wilayani Hanang’, mkoani Manyara.

Mpango huo wa miaka mitano unaotekelezwa kwa ushirikiano na Shirika la WaterAid Tanzania, umezinduliwa Februari 11, 2026 na Naibu Waziri wa Maji, Mhandisi Kundo Mathew, katika hafla iliyofanyika wilayani humo.

Lengo kuu la mpango huo ni kutatua changamoto ya ukosefu wa maji katika vijiji vya wilaya ya Hanang’ na kuboresha huduma za usafi wa mazingira na usafi binafsi kwa wananchi.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Mhandisi Mathew amesema kuwa rasilimali zinazotarajiwa kupatikana kupitia vyanzo vya kawaida hadi mwaka 2030 ni shilingi bilioni 41.75, hali inayoacha pengo kubwa la kifedha.

Kutokana na hali hiyo, amesisitiza umuhimu wa mchango kutoka sekta binafsi na wadau wa maendeleo katika kufanikisha utekelezaji wa mpango huo.

Naibu Waziri ametoa wito kwa wadau mbalimbali kuendelea kushirikiana na Serikali katika kuziba pengo hilo kwa maslahi ya wananchi, na kuhakikisha mpango huo unaingizwa kikamilifu katika mipango na bajeti za kila mwaka.

Pia amewahimiza wadau wa maendeleo na sekta binafsi kuuona mpango huo kama ramani na mwaliko rasmi wa kuwekeza katika Wilaya ya Hanang’.

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Hanang’, Almish Hazal, amemshukuru Naibu Waziri kwa jitihada zinazofanywa na Serikali pamoja na wadau katika kuimarisha miradi ya maji.

Hata hivyo, ameeleza kuwa changamoto kubwa inayokabili miradi ya visima ni upatikanaji wa nishati, hususan majenereta, akibainisha kuwa matumizi ya sola bado ni tatizo kutokana na hali ya baridi katika wilaya hiyo.

Ameomba kuwepo kwa ushirikiano kati ya Tanesco na RUWASA ili kuhakikisha upatikanaji wa umeme wa uhakika katika miradi ya maji, hatua itakayosaidia “kumtua mama ndoo kichwani kwa asilimia 100.”

Naye Mkurugenzi wa WaterAid Tanzania, Anna Mzinga, ameipongeza Serikali kwa kuendelea kushirikiana na wadau wa maendeleo, huku akiiomba kutoa kipaumbele katika rasilimali zitakazohitajika wakati wa utekelezaji wa mpango huo.

“Leo hii tunapouweka mpango huu mezani, tunatoa mwaliko wa wazi kwa kila mmoja kushiriki. Tunaishukuru Serikali kwa ushirikiano wake, lakini tunaomba iendelee kuongoza kwa kutoa kipaumbele katika uwekezaji wa mpango huu, Washirika wa maendeleo na sekta binafsi waweke nguvu zao pale ambapo mpango wa Serikali unaelekeza,” amesema Mzinga.

Uzinduzi wa mpango huo unatarajiwa kuwa chachu ya maboresho makubwa ya huduma za maji na usafi wa mazingira katika Wilaya ya Hanang’, na kuchangia ustawi wa afya na maendeleo ya wananchi wake.

Viongozi wa Taasisi Zanzibar Wasisitizwa Mafunzo Endelevu





Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe. Hemed Suleiman Abdulla amesema ni jambo muhimu kwa viongozi wa Taasisi za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar zinazojitegemea kupatiwa mafunzo yatakayowajengea uwelewa mpana katika utekelezaji wa majukumu yao.

Ameyasema hayo katika hafla ya ufunguzi wa mafunzo ya wakuu wa Taasisi zinazojitegemea za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar yaliyofanyika katika Ukumbi wa Ofisi za Tume ya Uchaguzi Maisara Zanzibar.

Amesema mafunzo hayo kwa kiasi kikubwa yatawasaidia katika kutekeleza majukumu yao, kutambua muelekeo sahihi wa Serikali sambamba na kujengewa uwezo wa kuziongoza Taasisi na Idara zao kwa weledi, ufanisi na tija.

Mhe. Hemed amefahamisha kuwa kufanyika  kwa mafunzo hayo ni hatua nzuri katika kufikia malengo ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar yanayoendelea kusisistiza umuhimu wa kujenga rasilimali watu wenye ujuzi, madili, weledi na uwezo wa kuendana na mabadiliko ya kiutawala, kiuchumi na kiteknolojia.

Aidha, amesema katika kukabiliana na mabadiliko ya mifumo ya kazi, matumizi ya Teknoloji na uwajibikaji wa Umma ni dhahiri kwamba mafunzo endelevu kwa watumishi wa umma na viongozi wa ngazi za juu si hiari bali ni hitaji la msingi katika kujenga utwala bora na utoaji wa huduma bora kwa wananchi.

Sambamba na hayo Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar ameeleza kuwa mafuzo hayo yanawapa viongozi fursa ya kujitathmini, kubadilishana uzoefu, kujifunza mbinu bora za uongozi na kuimarisha maamuzi yenye tija kwa Taasisi na Taifa kwa ujumla.

Hata hivyo Mhe. Hemed ametoa wito kwa washiriki wa mafunzo hayo kushiriki kikamilifu na kujifunza kwa umakini ili kuweza kuwa mabolozi wazuri wa mabadiliko chanya katika Taasisi zao.

Kwa upande  wake Mwenyekiti wa Baraza la Chuo cha Utawala wa Umma Zanzibar (IPA ) Dkt. Abduhamid Yahya Mzee amesema Chuo cha IPA kitaendelea na mpango wake wa kutoa mafunzo kwa watumishi na viongozi wa Taasisi mbali mbali ili kuweza kukumbushana, kujadili na kubadilishana uzowefu katika utendaji wa kazi za kila siku.

Dkt. Abdulhamid amefahamisha kuwa Mafuzo hayo yanalenga kuwapatia taaluma viongozi  juu ya namna bora ya kuongoza kwa weledi, ufanisi na kufanya kazi kwa kushirikiana na watendaji wao wanaowaongoza ili kufikia adhma ya kuwa viongozi wabunifu, wenye busara na hekima kwenye Taasisi zau wanazoziongoza.

Katibu Mkuu Kiongozi na Katibu wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Balozi, Mhandisi Zena Ahmed Said amesema mafunzo hayo yatakuwa endelevu ambayo yanalenga kuwakumbusha viongozi wa Umma kuwajibika ipasavyo kwa uadilifu na nidhamu katika majukumu yao.

Balozi Muhandisi Zena amesema katika mafunzo hayo mada mbali mbali zitawasilishwa ikiwemo  Uongozi Bora, Itifaki na Uongozi, Uongozi wa Kimkakati  na jukumu la usalama, Maadili na Usiri katika sehemu za kazi.

KAMISHNA WA UHIFADHI NCAA APOKELEWA NA WAFANYAKAZI

Kamishna wa Uhifadhi wa Mamlaka ya Hifadhi ya eneo la Ngorongoro Bw. Abdul-Razaq Badru amepokelewa Rasmi kwa kukagua gwaride la heshma katika ofisi za Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro eneo la Njia Panda Karatu baada ya Kivishwa Cheo na kuapishwa na Waziri wa Maliasili na Utalii Dkt. Ashatu Kijaji (Mb) kuwa kamishna wa Uhifadhi hivi Karibuni.






Rais Dkt. Samia Awasili Addis Ababa Kushiriki Mkutano wa 39 wa Wakuu wa Nchi wa AU

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, amewasili katika Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Bole, Jij...