Thursday, March 05, 2026

Mhe. Ndejembi Akutana na Chama cha Waagizaji na Wasambazaji wa Mafuta (TAOMAC)

 













Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi, amekutana na kufanya mazungumzo na Chama cha Waagizaji na Wasambazaji wa Mafuta Tanzania (TAOMAC) kwa lengo la kuboresha na kukuza sekta ya mafuta nchini pamoja na kuimarisha ushirikiano kati ya Serikali na wadau wa sekta hiyo.

Kikao hicho kimefanyika leo, Machi 5, katika Ofisi Ndogo za Wizara ya Nishati zilizopo jijini Dar es Salaam.

Katika Kikao hicho wamejadili masuala mbalimbali yanayolenga kuimarisha usimamizi, ufanisi na maendeleo ya sekta ya mafuta nchini kwa manufaa ya uchumi na wananchi kwa ujumla.

Kikao hicho kimehudhuriwa na Kamishna wa Mafuta kutoka Wizara ya Nishati, Bw. Goodluck Shirima; Mtendaji Mkuu wa PBPA, Bw. Erasto Simon; Mkurugenzi Mkuu wa EWURA, Dkt. James Mwainyekule; pamoja na viongozi na wanachama wa TAOMAC.

Tuesday, March 03, 2026

RAIS SAMIA AWEKA JIWE LA MSINGI UJENZI WA MATANKI YA KUPOKELEA MAFUTA KIGAMBONI

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akivuta kitambaa kuashiria uwekaji wa jiwe la msingi Mradi wa ujenzi wa Matanki ya kupokea mafuta katika Bandari ya Dar es Salaam katika eneo la Kigamboni Jijini Dar es Salaam, tarehe 03 Machi, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akivuta kitambaa kuashiria uwekaji wa jiwe la msingi Mradi wa ujenzi wa Matanki ya kupokea mafuta katika Bandari ya Dar es Salaam katika eneo la Kigamboni Jijini Dar es Salaam, tarehe 03 Machi, 2026.



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan mara baada ya kuweka jiwe la msingi Mradi wa Ujenzi wa Matanki ya kupokea Mafuta katika Bandari ya Dar es Salaam, Kigamboni, Jijini Dar es Salaam, tarehe 03 Machi, 2026.




Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akisikiliza maelezo ya Mradi wa ujenzi wa Matanki ya kupokea Mafuta katika Bandari ya Dar es Salaam, Kigamboni Jijini Dar es Salaam, tarehe 03 Machi, 2026. Ujenzi wa Matanki hayo utasaidia kupunguza uhaba wa mafuta nchini, kupunguza muda wa meli kusubiri nangani kutoka wastani wa siku 22 hadi siku 7, kupunguza muda wa kushusha shehena ya mafuta kutoka siku 7 hadi siku 1, kuongeza mapato ya Taifa pamoja na kutoa ajira kwa Watanzania.

Monday, March 02, 2026

TANZANIA NA GHANA KUIMARISHA USHIRIKIANO WA KIUCHUMI NA AJIRA KWA VIJANA

Arusha, 02 Machi 2026

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, amefanya mazungumzo ya pande mbili na Rais wa Jamhuri ya Ghana, Mheshimiwa John Dramani Mahama, Ikulu ya Arusha, yakilenga kuimarisha ushirikiano wa kimkakati katika sekta za uchumi, ajira kwa vijana na maendeleo ya uchumi wa kidijitali.

Taarifa iliyotolewa na Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais, Ikulu mazungumzo hayo yamejikita katika kuongeza thamani ya rasilimali za ndani badala ya kuendelea kuuza malighafi, sambamba na kukuza mageuzi ya viwanda na biashara kati ya nchi hizo mbili. 

Viongozi hao wameonesha dhamira ya pamoja ya kuimarisha usimamizi wa sekta za madini na mazao ya kimkakati kama kakao na pamba, kwa lengo la kuongeza mapato ya ndani na kuchochea uchakataji wa ndani.

Kwa upande wake, Rais Dkt. Samia amesisitiza kuwa Tanzania inaendelea kuharakisha mkakati wa uchumi wa viwanda, ikiwa ni pamoja na kuongeza thamani ya mazao ya kimkakati na kuimarisha uchakataji wa madini. 

Ameeleza kuwa uzoefu wa Ghana katika usimamizi wa rasilimali na sera za uchumi wa ndani ni fursa muhimu ya kujifunza na kushirikiana kwa maslahi mapana ya mataifa hayo mawili.

Kuhusu ajira kwa vijana, Marais hao wamekubaliana kuongeza ushirikiano katika nyanja za ujuzi, ubunifu na ujasiriamali, pamoja na kuweka mazingira bora ya uwekezaji yatakayochochea ajira endelevu. Msisitizo umewekwa katika kukuza sekta za teknolojia, ubunifu wa kidijitali na huduma za kifedha ili kuongeza ushindani wa kiuchumi.

Katika eneo la TEHAMA, Rais Dkt. Samia ameeleza kuwa Serikali inaendelea kuwekeza katika miundombinu ya kidijitali na kuimarisha usalama wa mitandao. Amebainisha kuwa uzoefu wa Ghana katika teknolojia ya fedha na ulinzi wa miundombinu ya kimtandao ni eneo la kimkakati la ushirikiano, likiwa na lengo la kuongeza ujumuishwaji wa kifedha na ufanisi wa huduma za kifedha.

Viongozi hao pia wamepongeza hatua ya kuimarisha usafiri wa anga kati ya nchi hizo mbili kupitia Shirika la Ndege la Air Tanzania (ATCL), wakieleza kuwa safari za moja kwa moja zitarahisisha biashara, utalii na mwingiliano wa wananchi, si tu kati ya Tanzania na Ghana bali pia katika ukanda wa Bara la Afrika.

Rais wa Ghana yupo nchini kwa ziara ya kikazi ya siku moja. Leo, tarehe 02 Machi 2026, anatarajiwa kuwa Mgeni Rasmi katika Ufunguzi wa Mwaka wa Mahakama, pamoja na Maadhimisho ya Miaka 20 ya Mahakama ya Afrika ya Haki za Binadamu na Watu, yenye makao makuu jijini Arusha.







Thursday, February 26, 2026

MHE. NDEJEMBI AITAKA PURA KUWAJENGEA UWEZO WATANZANIA KUSHIRIKI MRADI WA LNG

Na Mwandishi Wetu, Morogoro

Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratous Ndejembi, ameitaka Mamlaka ya Udhibiti Mkondo wa Juu wa Petroli (PURA) kuimarisha mipango yake katika ukusanyaji wa data sahihi, tathmini ya vitalu vya utafiti, na maandalizi ya Watanzania kushiriki kikamilifu katika miradi mikubwa ya kimkakati, ikiwemo mradi wa kuchakata gesi asilia kuwa kimiminika (LNG).

Mhe. Ndejembi ameyasema hayo wakati wa Kikao cha Tano cha Mkutano wa Pili wa Baraza la Wafanyakazi la PURA kilichofanyika mkoani Morogoro leo Februari 26, 2026.

 Amesisitiza kwamba sekta ya nishati ina nafasi ya kipekee katika kufanikisha malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, hivyo PURA inatakiwa kuhakikisha mipango yake inaendana na maono hayo.

“Sekta ya Nishati imetambuliwa kama moja ya vichocheo muhimu vya uchumi wa taifa. Taasisi zilizo chini ya Wizara ya Nishati zina wajibu mkubwa kuhakikisha upatikanaji endelevu, salama na wa uhakika wa rasilimali za mafuta na gesi asilia,” amesema Mhe. Ndejembi.

Aidha, Mhe. Ndejembi amewataka PURA kuongeza juhudi katika ukusanyaji na usimamizi wa data za kijiolojia na kufanya tafiti za awali, hasa ikizingatiwa kwamba maeneo makubwa ya nchi bado hayajafanyiwa utafiti wa kina.

“Takwimu sahihi ni msingi wa kuvutia uwekezaji na kuongeza ugunduzi wa rasilimali. Hatuwezi kuendeleza sekta bila taarifa za kutosha na tafiti madhubuti,” amesisitiza.

Waziri huyo pia ameagiza PURA kufanya tathmini ya kina katika vitalu vilivyopo, hususan katika ukanda wa Tanga, Ruvu, na maeneo mengine, ili kubaini iwapo wamiliki wa vitalu wanafanya shughuli za utafutaji kama inavyotakiwa.

 Ameongeza kuwa si vyema kwa vitalu kukaa mikononi mwa wawekezaji wasioendeleza shughuli za utafutaji, na mamlaka za udhibiti zinapaswa kuchukua hatua pale inapobainika hakuna maendeleo yanayofanyika kwa manufaa ya Taifa.

Akizungumzia mradi wa LNG, Mhe. Ndejembi amewataka PURA kuanza mapema kuandaa mkakati wa kujenga uwezo wa kitaasisi katika kusimamia mradi huo. 

Sambamba na hilo, amewahimiza kuandaa Watanzania kushiriki kikamilifu katika mnyororo wa thamani wa LNG, badala ya kusubiri utekelezaji wa mradi kuanza.

Awali katika kikao hicho, Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati anayeshughulikia Mafuta na Gesi Asilia, Dkt. James Mataragio, amewataka PURA kusimamia majukumu yake ya msingi kama yanavyoainishwa katika malengo ya kuanzishwa kwa taasisi hiyo.











MGODI WA ITRACOM WACHANGIA SHILINGI BILIONI 1.29 MAPATO YA SERIKALI MANYARA









📍Manyara

MGODI wa Itracom Fertilizer Limited unaojihusisha na uchimbaji na uchakataji wa madini ya phosphate uliopo  katika eneo la Vilima Vitatu, Wilayani Babati mkoani Manyara, umechangia Shilingi Bilioni 1.29 katika mapato ya Serikali tangu kuanza kwa shughuli zake mwaka 2023.

Hayo yamebainishwa na Mjiolojia, Waziri Mkupe, akizungumza kwa niaba ya Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Manyara, Godfrey Nyanda, ambapo amesema mapato hayo yametokana na mrabaha na ada ya ukaguzi wa madini.

Amesema tangu kuanza kwa uzalishaji, mgodi huo umezalisha jumla ya tani 69,929 za madini ya phosphate zenye thamani ya Shilingi Bilioni 36.99, ambazo zimeuzwa katika soko la ndani na nje ya nchi, hususan Nala mkoani Dodoma na nchini Burundi.

Kwa mujibu wa Mkupe, mchango huo umeimarisha ukusanyaji wa maduhuli ya Serikali na kuchochea maendeleo ya jamii inayozunguka mgodi kupitia utekelezaji wa miradi ya Uwajibikaji kwa Jamii (CSR).

Ameeleza kuwa tangu kuanza kwa shughuli zake, mgodi huo umechangia utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo ikiwemo ujenzi wa Shule ya Msingi Vilima Vitatu, nyumba za walimu, na upo katika hatua za awali za ujenzi wa bweni la shule ya sekondari ya wasichana.

Akifafanua kuhusu mauzo ya ndani, amesema kuanzia Desemba 16, 2023 hadi Februari 24, 2026, jumla ya tani 22,686 zenye thamani ya Shilingi bilioni 9.07 ziliuzwa kwenda Nala, Dodoma. Katika mauzo hayo, Serikali ilikusanya Shilingi milioni 90.74 kama mrabaha na kiasi kama hicho kama ada ya ukaguzi.

Kuhusu mauzo ya nje, amesema vibali 13 vilitolewa kwa ajili ya kusafirisha tani 47,243 za madini ya phosphate kwenda Burundi zenye thamani ya Shilingi Bilioni 27.92. Katika kipindi cha Septemba 4, 2024 hadi Februari 24, 2026, Serikali ilikusanya Shilingi milioni 837.64 kama mrabaha na Shilingi milioni 279.21 kama ada ya ukaguzi.

“Mgodi wa Itracom Fertilizer Limited umeendelea kudhihirisha kuwa sekta ya madini ya phosphate ni kichocheo muhimu cha ukuaji wa uchumi wa Mkoa wa Manyara kwa kuongeza mapato ya Serikali, kutoa ajira na kuimarisha maendeleo ya jamii,” amesema Mkupe.

Aidha, amewahimiza Watanzania kuchangamkia fursa za uwekezaji zilizopo mkoani humo, akibainisha kuwa pamoja na madini ya phosphate, Mkoa wa Manyara una rasilimali nyingine zikiwemo dhahabu, moonstone, green tourmaline, amethyst, green aventurine, limestone, azurite, chumvi, muscovite mica, feldspar na quartz crystal.

BARABARA YA MLIMA KITONGA KUWA NJIA NNE

 
📌Lengo ni kupunguza foleni, usalama

📌Ni Maelekezo ya Rais Samia

📌Waziri Ulega aagiza manunuzi yaanze mara moja

SERIKALI iko katika hatua za mwisho za kuanza upanuzi wa barabara ya Kitonga mkoani Iringa ambayo sasa itakuwa ya njia nne na yenye taa za barabarani. 

Waziri wa Ujenzi, Abdallah Ulega, amesema kuwa hatua hiyo ni uamuzi wa Rais Samia Suluhu Hassan ili kupunguza foleni na kuboresha usalama wa watumiaji barabara katika njia hiyo inayotumiwa na magari mengi. 

Waziri Ulega aliyekuwa katika ziara ya ukaguzi wa eneo la zaidi ya kilomita saba linalopaswa kupanuliwa, alisema barabara hiyo ni ya kimkakati kwa uchumi wa nchi kwa sababu inatumiwa pia na magari yanayokwenda katika nchi zinazotumia bandari ya Dar wa Salaam kubeba mizigo yao. 

“Barabara hii sasa itakuwa ya njia nne – mbili za kwenda na mbili za kurudi ambapo sasa ni njia mbili tu zinatumika. Na tutafunga taa kote ili kuhakikisha muda wote barabara inapitika muda wote, “ alisema Ulega. 

Akitoa picha ya ongezeko la uhitaji wa upanuzi wa barabara hiyo, Mbunge huyo wa Jimbo la Mkuranga alisema idadi ya magari yanayopita katika Barabara Kuu ya TANZAM imeongezeka kutoka magari 1,700 hadi 3,400 kwa siku, hali inayopelekea barabara hiyo kuzidiwa na wingi wa magari.

“Nimepokea mapendekezo kutoka kwa Meneja wa TANROADS Iringa ya kuhakikisha tunaondoa msongamano wa magari katika mlima Kitonga, na nimeelekeza kwa wataalamu wetu kupanua hii barabara kwa kilometa 7. Kwa sasa hivi barabara ina njia mbili kwa hiyo tutatanua na kuwa njia nne”, amesema Ulega.

Waziri Ulega ameongeza kuwa ni maelekezo ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwamba kila mradi wa barabara uende sambamba na uwekaji wa taa za barabarani ili kuhakikisha usalama wa watumiaji ikiwemo wananchi, wafanyabiashara na madereva pamoja na kuweka kingo pembezoni mwa barabara ili kuzuia magari yasianguke kwenye makorongo.

“Ninaagiza manunuzi yaanze mara moja ili kuhakikisha kwamba barabara hii inatanuliwa kwani ina umuhimu mkubwa katika uchumi wa nchi hivyo hatuwezi kuiacha katika hali hii na kutimiza pia maelekezo ya Mheshimiwa Rais kutatua changamoto zote”, ameongeza Waziri Ulega. 

Naye Mbunge wa Jimbo la Kilolo, Ritha Kabati, amesema barabara hiyo ni ya uchumi wa kimataifa hivyo ikitengenezwa itainua zaidi uchumi wa mkoa wa Iringa na Taifa kwa ujumla pamoja na kuwasaidia wananchi ambao hupata changamoto ya kufuata huduma za kijamii ikiwemo matibabu Iringa mjini. 

Kwa upande wake Meneja wa TANROADS mkoa wa Iringa Eng. Yudas Msangi amesema gharama ya upanuzi wa kilometa 7 wa njia mbili katika barabara hiyo ni bilioni 59.2 na ukarabati wa njia mbili zilizopo ni bilioni 16.2.







Mhe. Ndejembi Akutana na Chama cha Waagizaji na Wasambazaji wa Mafuta (TAOMAC)

  Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi, amekutana na kufanya mazungumzo na Chama cha Waagizaji na Wasambazaji wa Mafuta Tanzania (TAO...