Wednesday, August 19, 2026

RC CHALAMILA ATOA SIKU SABA KWA MUAFAKA WA MGOGORO WA ARDHI TOANGOMA





Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Mhe. Albert Chalamila, ametoa muda wa siku saba kwa wadau wanaohusika na mgogoro wa muda mrefu wa ardhi katika eneo la Toangoma, Wilaya ya Temeke, kukutana na Shirika la Taifa la Hifadhi ya Jamii (NSSF) ili kutafuta muafaka kabla ya kurejea katika eneo hilo kwa ajili ya kuhitimisha mgogoro huo.

Mhe. Chalamila ametoa maelekezo hayo katika mkutano wa hadhara uliofanyika Toangoma, baada ya kusikiliza maelezo ya wananchi, NSSF pamoja na Ofisi ya Kamishna wa Ardhi. Amesema kwa mujibu wa nyaraka na maelezo yaliyowasilishwa, amejiridhisha kuwa eneo linalozungumziwa linamilikiwa na NSSF.

Hata hivyo, Mkuu huyo wa Mkoa amesema amepokea maombi ya wananchi wanaotaka masharti ya ununuzi wa maeneo wanayoishi yafanyiwe mapitio ili kuwawezesha kumudu gharama na kupata muda wa kutosha wa kufanya malipo.

Kwa mujibu wa maelezo yaliyotolewa katika mkutano huo, NSSF ilikuwa imeweka bei ya Sh. 15,000 kwa mita ya mraba katika eneo la Malela na Sh. 25,000 kwa mita ya mraba katika eneo la Mwapemba. Wananchi wameomba bei hiyo ipunguzwe hadi Sh. 5,000 kwa mita ya mraba, sambamba na kuongezewa muda wa kufanya malipo kutoka kipindi cha awali cha miezi mitatu hadi kati ya miaka minne na 10.

Mhe. Chalamila amesema katika kipindi cha siku saba alichotoa, atakutana na wadau husika kwa lengo la kutafuta suluhu inayozingatia maslahi ya pande zote. Aidha, ameelekeza wananchi kutosumbuliwa katika kipindi hicho huku muda wa awali uliokuwa umetolewa kwa ajili ya malipo ukisitishwa ili kutoa nafasi ya kufikiwa kwa mpango mpya.

Kamishna Msaidizi wa Ardhi Mkoa wa Dar es Salaam, Rehema Mwinuka, amethibitisha kuwa eneo hilo linamilikiwa na NSSF. Kwa upande wake, mwakilishi wa NSSF ameeleza kuwa baada ya kubaini kuwapo kwa wananchi katika eneo lake, Shirika liliamua kutoa fursa kwa wakazi hao kununua maeneo wanayoishi kwa bei zilizowekwa.

Awali, wananchi walieleza kuwa wengi wao wameishi katika maeneo hayo kwa zaidi ya miaka 16, wakidai kuwa walinunua viwanja kupitia taratibu zilizohusisha viongozi wa serikali za mitaa na hivyo kuamini kuwa ardhi hiyo haikuwa mali ya NSSF.

Kutokana na mazingira hayo, wananchi wamemuomba Mkuu wa Mkoa kusaidia kupatikana kwa suluhu itakayowawezesha kuendelea kumiliki maeneo hayo kwa gharama na masharti wanayoweza kumudu.

Mhe. Chalamila anatarajiwa kurejea Toangoma baada ya siku saba kwa ajili ya kutoa mrejesho wa majadiliano na kuweka hitimisho katika mgogoro huo wa muda mrefu.

Tuesday, August 18, 2026

RAIS TSHISEKEDI AFANYA ZIARA YA KIKAZI TANZANIA

 Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ampokea Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) Mhe. Félix Antoine Tshisekedi Tshilombo, Ikulu Ndogo ya Zanzibar.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiongoza Ujumbe wa Tanzania kwenye mazungumzo Rasmi na Ujumbe wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) ulioongozwa na Rais wa Nchi hiyo, Mhe. Félix Antoine Tshisekedi Tshilombo katika Ikulu Ndogo ya Zanzibar, tarehe 18 Agosti, 2026



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, amempokea Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), Mhe. Félix Antoine Tshisekedi Tshilombo, katika Ikulu Ndogo ya Zanzibar, akiwa nchini kwa ziara ya kikazi.

Viongozi hao wawili wanatarajiwa kufanya mazungumzo yatakayojikita katika kuimarisha zaidi ushirikiano baina ya Tanzania na DRC, sambamba na kujadili masuala mbalimbali yenye maslahi ya pamoja kwa mataifa hayo mawili.

Tanzania na DRC zina uhusiano wa muda mrefu wa kihistoria na kidugu, huku ushirikiano wao ukiendelea kuimarika katika nyanja mbalimbali za maendeleo.

Ziara hiyo ni mwendelezo wa jitihada za kuimarisha diplomasia, ujirani mwema na ushirikiano wa kikanda kwa manufaa ya wananchi wa Tanzania na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.

Wednesday, August 12, 2026

Msajili wa Hazina, Fitch Ratings watathmini mageuzi ya taasisi za umma





Na Mwandishi wa OTR

Dar es Salaam. Ofisi ya Msajili wa Hazina (OTR) Jumanne, Agosti 11, 2026, ilifanya mazungumzo na Fitch Ratings Ltd ambayo ni kampuni ya kimataifa inayofanya tathmini ya uwezo wa kifedha na hatari ya mikopo kwa nchi, kampuni, benki, taasisi za umma na hati za madeni ikiwa ni sehemu ya mapitio ya pili ya mwaka 2026 ya tathmini ya Fitch Ratings, katika mchakato unaohusisha taasisi mbalimbali za Serikali.

Mazungumzo hayo yanalenga  kuwapa wachambuzi wa Fitch Ratings fursa ya kupata taarifa za kina kuhusu mwenendo wa uchumi wa Tanzania, utekelezaji wa sera za kibajeti na fedha, pamoja na mikakati ya Serikali katika usimamizi wa deni la Taifa. 

Kwa upande wa OTR, mjadala ulijikita katika utendaji wa taasisi za umma, mageuzi yanayoendelea, vihatarishi vya kifedha, pamoja na mtiririko wa fedha kati ya Serikali na taasisi za Umma.

Mapema mwaka huu, Fitch Ratings iliendelea kuipa Tanzania daraja ‘B+’ kwa hadhi ya ulipaji wa madeni ya muda mrefu ya fedha za kigeni, ikitaja mwelekeo imara wa ukuaji wa uchumi na uwezo wa Serikali kukabiliana na changamoto za kifedha baada ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025.

Fitch inakadiria kuwa uchumi wa Tanzania utakua kwa asilimia 6 kwa mwaka 2026, kiwango ambacho ni kikubwa zaidi ya wastani wa asilimia 4.5 kwa nchi zenye daraja la ‘B’.

Fitch hutoa daraja kama AAA, AA, A, BBB, BB au B. Kwa kawaida, alama za juu zinaonesha uwezo mkubwa wa kulipa madeni na hatari ndogo; alama za chini zinaonesha hatari inayoongezeka.

Katika muktadha huo, Msajili wa Hazina, Bw. Nehemiah Mchechu, aliyeongoza timu ya OTR, aliieleza timu ya Fitch kuhusu mageuzi yanayolenga kuboresha utendaji na ufanisi wa taasisi za umma, kuimarisha utawala bora na uwajibikaji, pamoja na kupunguza utegemezi wa taasisi hizo kwa Serikali.

Alisema ajenda ya mageuzi ya OTR katika kipindi cha miaka miwili iliyopita imeweka mkazo zaidi katika uongozi, usimamizi wa utendaji na uwajibikaji, ikiwemo kuboresha ubora wa Bodi na timu za menejimenti na kuimarisha tathmini za Bodi ili kubaini mapungufu ya ujuzi.

Bw. Mchechu alisema matokeo ya mageuzi hayo yanaendelea kuonekana katika mchango wa kifedha wa taasisi za umma kwa Serikali.

Katika mwaka wa fedha ulioishia Juni 30, 2026, taasisi zilizo chini ya Msajili wa Hazina zilichangia takribani Sh1.881 trilioni kwa Serikali kupitia gawio na michango mingine, ikilinganishwa na Sh1.028 trilioni katika mwaka wa fedha uliotangulia.

“Tunachokiona ni utayari wa taasisi kuanza kuchangia, au kuongeza mchango wao kwa Serikali,” alisema Bw. Mchechu.

Aliongeza kuwa taasisi zinazoendelea kuhitaji msaada wa Serikali zinatarajiwa kuonesha namna zinavyopunguza utegemezi huo. 

Alisema hatua za urekebishaji na uwekezaji wa mtaji zilizochukuliwa katika taasisi kama Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) na Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) zimesaidia kupunguza majukumu hayo na kuimarisha hali ya kifedha ya taasisi hizo.

Timu ya Fitch pia iliomba taarifa kuhusu mipango ya kuorodhesha baadhi ya taasisi za umma katika soko la mitaji.

Bw. Mchechu alisema Benki ya Biashara Tanzania (TCB) ni miongoni mwa taasisi zinazotayarishwa kuorodheshwa katika soko la mitaji kupitia uuzaji wa hisa kwa umma kwa mara ya kwanza (IPO), huku Shirika la Taifa la Bima (NIC) likifanyiwa tathmini kwa ajili ya uwezekano wa kuorodheshwa katika soko hilo.

Lengo la muda mrefu ni kurekebisha, kuimarisha na kuorodhesha katika soko la mitaji taasisi kadhaa za umma zinazofaa kabla ya mwaka 2030.

Bw. Mchechu alisema pia OTR imezipa taasisi 58 za umma uhuru zaidi wa kiutendaji, unaoziruhusu kutekeleza majukumu yao kwa mujibu wa mamlaka walizopewa bila kuingiliwa katika utekelezaji wa majukumu yao.

Alisema mageuzi hayo yameimarisha pia uwezo wa ndani wa OTR, hususan katika uchambuzi wa biashara, na hivyo kuiwezesha Ofisi kufanya uchambuzi wa kina zaidi wa bajeti, uwekezaji na mipango ya kimkakati ya taasisi za umma.

Msajili wa Hazina alisema ushirikiano kati ya OTR na Wizara zinazosimamia sekta mbalimbali umeimarika, huku uhusiano huo ukielekezwa zaidi katika kuhakikisha taasisi za umma zinatekeleza vipaumbele vya Serikali.

“Si suala tena la kusema ‘unapaswa kufanya hili na si lile’, bali ‘unafanyaje ili taasisi hii itekeleze kile ambacho Mhe. Rais anataka?’” alisema Bw. Mchechu.

Ujumbe wa Fitch uliongozwa na Bw. José Mantero, Mkurugenzi Mshirika  na mchambuzi mkuu anayeshughulikia Tanzania, akifuatana na Bi. Gaimin Nonyane, Mkurugenzi wa Kitengo cha Sovereign and Supranational Group cha Fitch Ratings, na Bw. Gerard Arabian, Makamu wa Rais na Mshauri wa Masuala ya Serikali ‘Sovereign Advisor’ katika Kitengo cha Public Sector Group Corporate Banking.

Bw. Mantero alisema Fitch ililenga kupata uelewa mpana zaidi kuhusu ajenda ya mageuzi ya OTR katika mashirika ya umma, hususan juhudi za kuboresha utendaji wa taasisi na kusimamia madeni na mtiririko wa fedha kati ya Serikali na taasisi za umma.

Alisema mapitio hayo pia yanatathmini athari za maendeleo yanayoendelea katika Mashariki ya Kati kwa Tanzania, ikiwemo athari zinazoweza kujitokeza katika fedha za Serikali, urari wa malipo na mfumuko wa bei kutokana na mabadiliko ya bei za mafuta na mbolea.

Akizungumzia hali chanya ya kifedha ya Serikali inayotokana na uhusiano wake wa kifedha na taasisi za umma, Bw. Mantero alisema: “Hii ni habari njema sana kwa hali ya fedha za Serikali.”

Kwa upande wake, Bi. Nonyane alionekana kuvutiwa na kuongezeka kwa mchango wa mashirika ya umma, akibainisha kuwa mchango huo wa hivi karibuni ulikuwa sawa na takribani asilimia 0.8 ya Pato la Taifa. 

Alitaka pia kufahamu namna hali hiyo ilivyobadilika kutoka kipindi ambacho baadhi ya mashirika ya umma nchini yalikuwa yakikabiliwa na changamoto za kifedha. 

Mwelekeo huo unaongeza matumaini kwamba mageuzi yanayoendelea yataimarisha zaidi utendaji na uendelevu wa kifedha wa taasisi za umma, kuongeza mchango wao katika uchumi na mapato ya Serikali, pamoja na kuunga mkono juhudi pana za Tanzania za kudumisha uimara wa kifedha na kuboresha hadhi yake ya mikopo.

Taarifa zilizotolewa katika mazungumzo ya OTR na Fitch Ratings yatachangia katika tathmini pana ya kampuni hiyo kuhusu uwezo wa Tanzania wa kutimiza majukumu yake ya kifedha, ikiwa ni sehemu ya mapitio ya pili ya mwaka 2026 ya tathmini ya hadhi ya Tanzania ya ulipaji wa madeni ya Serikali

RAIS DKT. MWINYI: TAMASHA LA KIZIMKAZI NI JUKWAA LA UTAMADUNI, UTALII NA FURSA ZA UWEKEZAJI








Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amesema Tamasha la Kizimkazi limeendelea kuwa jukwaa muhimu la kutangaza utamaduni, utalii, biashara na fursa za uwekezaji zilizopo Zanzibar, sambamba na kuchochea maendeleo ya wananchi.

Rais Dkt. Mwinyi ameyasema hayo leo, tarehe 12 Agosti 2026, alipokuwa akizindua rasmi Tamasha la Kizimkazi 2026 lenye kaulimbiu “KIZIMKAZI Kumenoga!” katika Mkoa wa Kusini Unguja.

Amepongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa maono ya kuasisi Tamasha hilo, ambalo limekuwa likichangia kuhifadhi mila na utamaduni, kukuza utalii na kufungua fursa za kiuchumi kwa wananchi.

Aidha, Rais Dkt. Mwinyi amesisitiza umuhimu wa kutumia Tamasha hilo kutangaza fursa za uwekezaji katika utalii, uvuvi, mwani na Uchumi wa Buluu, huku Serikali ikiendelea kuimarisha mazingira ya uwekezaji na miundombinu ya uzalishaji.

Amesema Tamasha la Kizimkazi linaunga mkono dhamira ya Serikali ya kuongeza idadi ya watalii wanaotembelea Zanzibar kutoka 800,000 hadi milioni 1.5, kupitia matukio maalum ya utalii na utangazaji wa vivutio, utamaduni, vyakula na ukarimu wa Wazanzibari.

Rais Dkt. Mwinyi amewapongeza waandaaji, wadhamini, taasisi za Serikali, Sekta Binafsi, wajasiriamali, wasanii, wanamichezo na wananchi kwa kufanikisha Tamasha la Kizimkazi 2026, akihimiza kuendelea kulitumia kama jukwaa la kufungua fursa mpya za maendeleo.

Tamasha hilo linaendelea hadi tarehe 14 Agosti 2026, ambapo kilele chake kitafanyika katika Uwanja wa Mwehe, Kizimkazi, Mkoa wa Kusini Unguja.

Monday, August 10, 2026

DKT. NCHIMBI: SAFARI YA HESHIMA KWA WAZEE WA TAIFA

 
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi amemtembelea na kumjulia hali, Rais Mstaafu wa Awamu ya Nne wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, katika makazi yake, Kawe Jijini Dar es Salaam, leo tarehe 10 Agosti 2026.




Uongozi bora hauanzi na madaraka pekee, bali hujengwa juu ya heshima kwa historia, kuthamini waliotangulia na kusikiliza sauti ya uzoefu.

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi, ameendelea kuonesha falsafa hiyo kwa vitendo kupitia ziara zake kwa viongozi mbalimbali wastaafu.

Leo, tarehe 10 Agosti 2026, Mhe. Dkt. Nchimbi amemtembelea na kumjulia hali Rais Mstaafu wa Awamu ya Nne, Mhe. Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, katika makazi yake Kawe, jijini Dar es Salaam.

Ziara hiyo si tukio la pekee. Ni sehemu ya mwendelezo wa safari ya heshima ambayo imemfikisha kwa Marais wastaafu wa Zanzibar, Mhe. Amani Abeid Karume na Mhe. Dkt. Ali Mohamed Shein; Mawaziri Wakuu wastaafu, Mhe. John Samwel Malecela na Mhe. Jaji Joseph Sinde Warioba; pamoja na Mzee Yusuph Makamba.

Katika kila mlango anaoubisha, kuna historia ya Taifa. Katika kila mkono anaoushika, kuna uzoefu wa miaka mingi. Na katika kila mazungumzo, kuna fursa ya kuunganisha busara za jana na wajibu wa leo kwa manufaa ya kesho.

Ziara hizi zina ujumbe mkubwa: Taifa linalowaheshimu viongozi wake wastaafu linaiheshimu historia yake; na uongozi unaosikiliza waliotangulia hujenga msingi imara wa umoja, mshikamano na mwendelezo wa kitaifa.

Hii ni zaidi ya kuwajulia hali. Ni daraja kati ya vizazi vya uongozi, ni utamaduni wa shukrani na ni ishara kwamba, ingawa madaraka yana ukomo, mchango wa kuitumikia Tanzania unaendelea kuthaminiwa.

Saturday, August 08, 2026

NANENANE 2026: RAIS SAMIA ASISITIZA KILIMO CHA TIJA, MASOKO NA TEKNOLOJIA KUELEKEA DIRA 2050

 









Dodoma, Agosti 8, 2026

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, ameongoza kilele cha Maadhimisho ya Nanenane 2026 jijini Dodoma, huku ujumbe mkubwa ukiwa ni kuifanya sekta ya kilimo kuwa injini imara zaidi ya uchumi kwa kuunganisha uzalishaji, masoko, teknolojia na ongezeko la tija.

Maadhimisho hayo yaliyofanyika katika Viwanja vya Dkt. John Samuel Malecela yamebeba kaulimbiu ya “Tambua Soko; Ongeza Tija Kutekeleza Dira 2050”, inayosisitiza umuhimu wa wakulima kuzalisha kwa kuzingatia mahitaji ya soko, ubora na kuongeza thamani ya mazao.

Katika kuonesha kwa vitendo mwelekeo huo wa mageuzi ya kilimo, Rais Samia amezindua magari kwa ajili ya Wakala wa Taifa wa Huduma za Ugani (NAESA) pamoja na matrekta kwa ajili ya vyama vya ushirika, hatua inayolenga kusogeza huduma na teknolojia karibu zaidi na wakulima.

Moja ya matukio yaliyoongeza shamrashamra katika kilele hicho ni Rais Samia kupanda moja ya matrekta baada ya uzinduzi, tukio lililobeba taswira pana ya dhamira ya Serikali ya kuhamisha kilimo kutoka mbinu za kawaida kuelekea uzalishaji wa kisasa wenye tija na ushindani.

Nanenane 2026 hivyo haikuwa tu sherehe ya mafanikio ya wakulima, bali imekuwa jukwaa la kuonesha mwelekeo mpya wa kilimo cha Tanzania—kilimo kinachotambua soko, kinachotumia teknolojia, kinachoongeza thamani na kinachochangia utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Friday, August 07, 2026

RAIS SAMIA AZINDUA TUME YA UCHUNGUZI KWA AJILI YA KUIMARISHA AMANI, HAKI NA UWAJIBIKAJI

 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye picha na Wajumbe wa Tume ya Rais ya Uchunguzi wa Wahusika wa Ghasia na Ukiukwaji wa Sheria katika Matukio ya Ghasia wakati na baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba, 2025 mara baada ya uzinduzi wa Tume hiyo, Ikulu, Jijini Dar es Salaam, tarehe 07 Agosti, 2026.








Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, tarehe 07 Agosti, 2026 amezindua rasmi Tume ya Rais ya Uchunguzi wa matukio ya ghasia na ukiukwaji wa sheria yaliyojitokeza wakati na baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba, 2025.

Uzinduzi huo umefanyika Ikulu jijini Dar es Salaam na kuhudhuriwa na Wajumbe wa Tume hiyo, ambao baada ya hafla walipata picha ya pamoja na Rais Samia.

Tume imepewa jukumu la kuchunguza kwa kina mazingira, matukio na wahusika wanaohusishwa na ghasia pamoja na ukiukwaji wa sheria katika kipindi hicho.

Uchunguzi huo unatarajiwa kusaidia kuweka uelewa mpana wa matukio yaliyotokea na kutoa msingi wa hatua na maamuzi yatakayochukuliwa kwa mujibu wa sheria, ikiwa ni sehemu ya kuimarisha amani, haki na uwajibikaji nchini.

RC CHALAMILA ATOA SIKU SABA KWA MUAFAKA WA MGOGORO WA ARDHI TOANGOMA

Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Mhe. Albert Chalamila, ametoa muda wa siku saba kwa wadau wanaohusika na mgogoro wa muda mrefu wa ardhi katik...