Friday, April 24, 2026

🏗️ MASASI COMMERCIAL COMPLEX YAKABIDHIWA RASMI









Mradi wa Masasi Commercial Complex umekabidhiwa rasmi, ukiwa ni alama ya mafanikio ya utekelezaji wa miradi ya kisasa yenye kuzingatia ubora na thamani kwa jamii.

Akizungumza katika hafla hiyo, Meneja wa NHC Mkoa wa Lindi, Omari Malalamangi, aliipongeza timu ya ujenzi kwa kazi kubwa waliyoifanya licha ya changamoto ya maji wakati wa uchimbaji wa msingi. 

Alisisitiza kuwa kujituma kwao kumezaa matokeo bora—jengo lenye hadhi linalovutia na kupongezwa na wengi.

Mradi huu umeacha alama chanya kwa jamii, ukitoa ajira kwa wakazi wa Masasi na kunufaisha sekta mbalimbali zikiwemo huduma za maji, umeme, mama lishe pamoja na wauzaji wa vifaa vya ujenzi.

Kwa upande wake, Meneja Usimamizi wa Miradi NHC, Grace Musita, alieleza kuwa ujenzi umefuata taratibu zote za kitaalamu, huku vipimo vya vifaa kama nondo, kokoto na tofali vikifanyika katika maabara ya Mtwara. 

Alibainisha kuwa kila hatua ya ujenzi ilisimamiwa kwa ukaribu na wataalamu ili kuhakikisha ubora unazingatiwa kabla ya kuendelea na hatua inayofuata.

Aidha, mradi umefungua fursa kwa wafanyabiashara wa ndani, ambapo baadhi ya kazi kama uwekaji wa milango ya mbao na tiles zilifanywa na mafundi wazawa wa Masasi.

Musita alimshukuru Mkurugenzi Mkuu pamoja na Menejimenti ya NHC kwa ushirikiano uliowezesha kukamilika kwa mradi huu kwa mafanikio.

Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa Madaraka, Kata ya Jida, alieleza furaha yake akisema ujio wa jengo hili umeubadilisha mtaa huo na kuongeza uhai wa shughuli za kijamii na kiuchumi, huku ajira ndogo ndogo zilizotolewa zikichochea vijana wengi kujikwamua kiuchumi.

Hafla ya makabidhiano ilihitimishwa kwa kukata keki, kuashiria rasmi kuwa Masasi Commercial Complex ipo tayari kutumika.

#NHC #MasasiComplex #UjenziBora #MaendeleoYaJamii #Tanzania

Thursday, April 23, 2026

UJUMBE WA MAAFISA KUTOKA CHUO CHA ULINZI CHA TAIFA MISRI WATEMBELEA MAKUMBUSHO YA TAIFA TANZANIA









Leo, tarehe 23/04/2026 Makumbusho ya Taifa la Tanzania imepokea ugeni maalum kutoka Chuo cha Kijeshi Misri (Egypt War College) walioko katika ziara ya mafunzo.

Ujumbe huo uliongozwa na Meja Jenerali Mohamed Yehia Zakaria Hassan akiambatana na Brigedia Jenerali Islam Sayed Bakry El-Sayed, huku kwa upande wa mwenyeji wao kutoka Tanzania wakiongozwa na Brigedia Jeneral Kamanda Makanya Erassy kutoka JWTZ Tanzania.

Wageni hao walipokelewa na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Makumbusho ya Taifa la Tanzania, Bi. Pendo Gondwe, ambaye aliwakaribisha na kuwapatia maelezo kuhusu dhima ya taasisi hiyo ya Kimkakati katika kuhifadhi, kulinda na kuendeleza urithi wa historia na utamaduni wa Taifa.

Ujumbe huo uliokuwa na lengo la kujifunza ulipata fursa ya kutembelea na kujifunza historia ya Tanzania kupitia vivutio mbalimbali vilivyopo katika Makumbusho, ikiwemo mabaki ya kihistoria, tamaduni za jamii mbalimbali pamoja na hatua za maendeleo ya taifa. Wageni hao walionesha kuvutiwa na ubora wa maonesho na namna historia ya Tanzania inavyoendelea kuhifadhiwa na kuwasilishwa kwa ufanisi.

Akizungumza baada ya ziara hiyo, kiongozi wa ujumbe, Meja Jenerali Mohamed Yehia Zakaria Hassan, alieleza kufurahishwa kwake na kiwango cha maonesho hayo akisema, “ Maonesho ni bora sana na nimefurahishwa kuona mwendelezo wa historia ukiendelea kukua na kuendelezwa"* 

Ziara hiyo ni sehemu ya programu ya mafunzo kwa wanafunzi wa Egypt War College, yenye lengo la kuwajengea uelewa mpana kuhusu historia, utamaduni na mifumo ya kijamii ya mataifa rafiki, pamoja na kuimarisha ushirikiano wa kijeshi na kidiplomasia kati ya Tanzania na Misri.

MHANDISI SEFF AKAGUA UJENZI WA BARABARA ZA UWANJA WA AFCON ARUSHA






#Ataka kazi zikamilike ifikapo Mei 2027

Arusha

Mtendaji Mkuu wa Wakala ya Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) Mhandisi Victor Seff amefanya ziara ya kukagua maendeleo ya ujenzi wa barabara zinazoingia katika uwanja utakaotumika kwa mashindano ya AFCON jijini Arusha.

Mhandisi Seff amesema kwamba ziara hiyo imelenga kujionea hatua za utekelezaji wa mradi wa barabara zenye urefu wa kilomita 21.4 ambapo kazi tayari zimeanza katika sehemu ya barabara ya Essuri.

Amesema serikali imejipanga kuhakikisha miundombinu hiyo inakamilika kwa wakati na kuongeza kuwa maeneo ambayo bado hayajaanza yanasubiri kukamilisha taratibu za fidia kwa wananchi watakaoathiriwa na mradi huo huku mkakati ukiwa ni kuendelea kuzungumza nao ili kutoa ushirikiano na kuruhusu kazi ziendelee bila vikwazo.

“Lengo la Serikali ni kuhakikisha barabara hizi zinakamilika ifikapo Mei mwaka 2027 ili ziwe tayari kabla ya mashindano ya AFCON,” amesema Mhandisi Seff.

Aidha, amesema mradi huo unatekelezwa kwa utaratibu wa Sanifu na Jenga (Design and Build) unaotumika pale ambapo muda ni mchache huku hatua zote za ununuzi tayari zikikamilika.

Ameeleza kuwa TARURA itaendelea kufanya ufuatiliaji wa karibu kuhakikisha mkandarasi anakamilisha kazi kwa wakati na kwa viwango vinavyotakiwa sanjari na ratiba ya mashindano hayo makubwa ya Mataifa ya  Afrika.

Ameongeza kuwa kwa sasa Mkandarasi M/s China Railway Construction Engineering Group tayari ameanza kazi ambapo ameanza na barabara ya Essuri yenye urefu wa kilomita 2.45 pia kutajengwa daraja lenye urefu wa mita 100.

Kwa upande wa barabara ya Lendita yenye kilomita 2.75, Mhandisi Seff amesema barabara hiyo itajengwa pamoja na daraja katika awamu ya pili ya mradi huku barabara hiyo ikitarajiwa kuwa ya njia nne.

Ameongeza kusema pia barabara ya Mateves yenye kilomita 6.5 itajengwa kwa sehemu mbili ambapo kilomita 5.5 zitakuwa njia mbili na kilomita 1 itakuwa njia nne.

Mtendaji Mkuu huyo amesema kukamilika kwa mradi huo kutaleta mafanikio makubwa kwa Taasisi hiyo kwa kupata uzoefu wa kusimamia miradi ya  Sanifu na Jenga, huku wananchi wakinufaika kwa kuondokana na changamoto ya miundombinu  katika maeneo hayo.

Vilevile, amesema wakazi wa maeneo yanayozunguka mradi huo watapewa kipaumbele cha ajira na amewataka vijana kujitokeza  kupata ajira na kutumia fursa hiyo kujiongezea kipato pamoja na  uzoefu wa kazi.

Kwa upande mwingine amewataka wasimamizi wa mradi huo kusimamia kwa karibu utekelezaji wake kwani mashindano hayo yanatarajiwa kuanza Julai mwakani.

Naye, Mhandisi Mshauri kutoka  kampuni ya M/s Afrisa Construction Engineering Group Bw. Idephonce Karol amesema mradi huo ulianza rasmi  tarehe 1 Aprili, 2026 na kwa sasa hatua za awali zinaendelea vizuri.

Amesema tayari wamehamasisha timu ya wataalamu, kufanya upimaji wa maeneo yote matatu ya barabara, uchunguzi wa udongo, tathmini ya vifaa vya ujenzi pamoja na kusafisha sehemu ya barabara ya Essuri urefu wa kilomita 1.8.

“Tumejipanga kikamilifu na tunafahamu umuhimu wa mradi huu hivyo tutafanya kazi usiku na mchana ili kuhakikisha unakamilika kwa wakati,” amesema Karol.

KIWANDA CHA KUCHAKATA MADINI CHUMVI MBIONI KUKAMILIKA MKOANI LINDI

 





●Wadau wa chumvi kuanza kuuza chumvi iliyochakatwa

●Zaidi ya tani 60 hadi 100 kuchakatwa kwa mwezi

●Wazalishaji wa chumvi waipongeza serikali kwa utatuzi wa changamoto

Dodoma

Katika juhudi za kuendeleza na kuboresha uzalishaji wa madini chumvi nchini Serikali kupitia Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) ipo mbioni kukamilisha kiwanda cha kuchakata madini chumvi kilwa mkoani Lindi pamoja kusaidia ujenzi wa viwanda mkoani Tanga na Mtwara.

Hayo yameelezwa leo Aprili 23, 2026 na Waziri wa Madini Mhe. Anthony Mavunde wakati wa kikao baina ya Chama cha Wazalishaji Chumvi Tanzania (TASPA) na Wizara ya Madini na taasisi zake  kilichofanyika jijini Dodoma.

Waziri  Mavunde , amesema kuwa, Serikali ilipokea maombi ya TASPA na kufanikiwa kushusha mrabaha katika madini chumvi kutoka asilimia 4 mpaka asilimia 1 ya bei elekezi.

Waziri Mavunde ameongeza kuwa, Serikali inaendelea kushughulikia uanzishwaji wa leseni moja katika shamba moja lengo ni kutofautisha na madini mengine ikiwa pamoja kuongeza uzalishaji wa chumvi bora nchini.

Naye, Mkurugenzi Mtendaji  wa Shirika ya Madini la Taifa (STAMICO) Dkt.Venance Mwase amesema kuwa miundombinu ndani ya kiwanda yamekamilika kwa asilimia kubwa.

Dkt. Mwase ameongeza kuwa , kiwanda kitakuwa na uwezo wa kupokea  chumvi ghafi kutoka kwa wazalisha kuanzia 50 hadi 60 kwa siku.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa TASPA Bi. Hawa Ghasia ameishukuru Serikali kwa kuwezesha mazingira bora ya uvunaji wa chumvi ikiwa pamoja na kupanda kwa bei ya chumvi baada ya kuwepo kwa zuio la uingizwaji wa chumvi ghafi kiholela kutoka nje ya nchi.

Kiwanda cha kuchakata chumvi mkoani Lindi pindi kitakapoanza kazi  kinatarajia kuchakataji tani 60 hadi 100 kwa siku.

Zaidi ya Watu 500 Wapoteza Maisha Kwenye Ghasia za Uchaguzi Mkuu








 

TUME YA RAIS YAWEKA WAZI TAKWIMU ZA MATUKIO YA UVUNJIFU WA AMANI





Na Ikulu, Dar es Salaam

Mwenyekiti wa Tume ya Rais ya Kuchunguza Matukio ya Uvunjifu wa Amani wakati na baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2025, Jaji Mkuu Mstaafu Mhe. Mohamed Chande Othman, amewasilisha muhtasari wa ripoti ya tume hiyo, akibainisha kwa takwimu ukubwa wa matukio yaliyotokea katika kipindi hicho.

Akiwasilisha taarifa hiyo Aprili 23, 2026 Ikulu jijini Dar es Salaam, Jaji Othman amesema jumla ya vifo 518 vilitokana na vurugu zilizojitokeza kabla na baada ya uchaguzi huo. Aidha, watu 373 walifikishwa hospitalini wakiwa wamefariki, huku majeruhi 121 wakipatiwa matibabu katika vituo mbalimbali vya afya.

Amesema takwimu hizo zinatokana na uchunguzi wa kina uliofanywa na tume kwa kushirikisha ushahidi kutoka kwa wadau mbalimbali, ikiwa ni pamoja na taasisi za Serikali, vyombo vya ulinzi na usalama pamoja na wananchi.

“Ripoti hii inalenga kuweka wazi hali halisi ya matukio yaliyotokea, kubainisha chanzo chake na kutoa mapendekezo yatakayosaidia kuzuia matukio ya aina hii yasijirudie,” ameeleza Jaji Othman.

Aidha, tume imeainisha umuhimu wa kuimarisha mifumo ya usimamizi wa uchaguzi, kuongeza uwajibikaji kwa taasisi husika pamoja na kuendeleza ushirikiano kati ya wadau wote wa kisiasa na kijamii ili kulinda amani ya Taifa.

Uwasilishaji wa ripoti hiyo unatajwa kuwa hatua muhimu katika kujenga uelewa wa pamoja, kuimarisha imani ya wananchi katika mifumo ya kidemokrasia na kuweka msingi imara wa uchaguzi wenye amani katika siku zijazo.

SERIKALI YAPELEKA TABASAMU KWA WANANCHI KUPITIA MIRADI YA MAENDELEO










Na OWM – TAMISEMI, Arusha

Wananchi katika maeneo mbalimbali nchini wanaendelea kunufaika moja kwa moja na utekelezaji wa miradi ya maendeleo inayotekelezwa katika Mamlaka za Serikali za Mitaa, hatua inayobadilisha kwa kasi hali ya upatikanaji wa huduma muhimu za kijamii na kuboresha maisha yao kwa ujumla.

Akizungumza Aprili 22, 2026 jijini Arusha, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM-TAMISEMI), Mhe. Prof. Riziki Shemdoe, amesema hatua ya Serikali chini ya uongozi wa Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kupeleka fedha nyingi kwenye halmashauri imekuwa na matokeo chanya yanayoonekana moja kwa moja kwa wananchi.

Amesema kupitia uwekezaji huo, wananchi sasa wanashuhudia maboresho katika sekta za afya, elimu, miundombinu na huduma nyingine za kijamii, hali inayorahisisha upatikanaji wa huduma na kuongeza ustawi wa jamii.

“Mafanikio haya yanaonekana wazi kwa wananchi—kuanzia upatikanaji wa huduma bora za afya, mazingira mazuri ya kujifunzia kwa wanafunzi, hadi kuboreshwa kwa miundombinu inayorahisisha shughuli za kiuchumi,” ameeleza Prof. Shemdoe.

Katika hatua nyingine, amewataka viongozi wa Mamlaka za Serikali za Mitaa kuhakikisha wanaendeleza kasi hiyo kwa kusimamia miradi kwa ufanisi na kuhakikisha inakidhi mahitaji halisi ya wananchi.

Aidha, amesisitiza umuhimu wa uwajibikaji, weledi na ushirikiano kati ya viongozi na watendaji ili kuhakikisha manufaa ya miradi hiyo yanaendelea kuwafikia wananchi kwa kiwango kikubwa zaidi.

Kauli hiyo imetolewa kabla ya kumkaribisha Waziri Mkuu Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba kufungua Mkutano Mkuu Maalum wa Uchaguzi wa Viongozi wa Jumuiya ya Tawala za Mitaa Tanzania (ALAT), unaofanyika Aprili 22 hadi 23, 2026 jijini Arusha.

🏗️ MASASI COMMERCIAL COMPLEX YAKABIDHIWA RASMI

Mradi wa Masasi Commercial Complex umekabidhiwa rasmi, ukiwa ni alama ya mafanikio ya utekelezaji wa miradi ya kisasa yenye kuzingatia ubor...