Waziri wa Uchukuzi, Profesa Makame Mbarawa amesema Serikali ya Awamu ya Sita inaendelea kutekeleza uwekezaji mkubwa katika sekta ya uchukuzi unaolenga kuifanya Kigoma kuwa kitovu cha usafirishaji na biashara kinachounganisha Tanzania na nchi za Afrika Mashariki na Kati.
Profesa Mbarawa amesema hayo leo Jumatatu Julai 20, 2026 katika hafla iliyohudhuriwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, wakati wa uzinduzi wa meli nne za mizigo, uwekaji wa jiwe la msingi la ujenzi wa gati la abiria na mizigo Bandari ya Kigoma pamoja na uzinduzi wa ujenzi wa Reli ya Kisasa (SGR) kipande cha Tabora–Kigoma.
Amesema chini ya uongozi wa Rais Samia, Serikali imewekeza kwa kiwango kikubwa katika reli ya kisasa, bandari, viwanja vya ndege na usafiri wa majini kwa lengo la kuunganisha mikoa yote ya Tanzania pamoja na nchi jirani kupitia mfumo jumuishi wa uchukuzi.
Kwa mujibu wa Profesa Mbarawa, meli nne mpya za mizigo zitaongeza usalama wa usafirishaji katika Ziwa Tanganyika, kupunguza gharama za usafirishaji wa mizigo, kukuza biashara kati ya Tanzania, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo na Burundi, pamoja na kufungua fursa mpya za ajira na uwekezaji.
Aidha, amesema maboresho yanayoendelea Bandari ya Kigoma pamoja na ujenzi wa Reli ya Kisasa kutoka Tabora hadi Kigoma yataongeza ufanisi wa usafirishaji wa abiria na mizigo, huku yakiiunganisha Bandari ya Dar es Salaam na masoko ya ukanda wa Afrika Mashariki na Kati.
Profesa Mbarawa pia amesema Serikali inaendelea na maboresho ya uwanja wa ndege wa Kigoma kwa gharama ya Sh. bilioni 51.4, yanayojumuisha ujenzi wa jengo jipya la abiria, mnara wa kuongozea ndege, njia za ndege, taa za kuongozea ndege na miundombinu mingine muhimu.
Ameongeza kuwa miradi hiyo inaonesha dhamira ya Serikali ya kujenga mfumo wa uchukuzi unaounganisha reli, bandari na usafiri wa anga ili kuharakisha maendeleo ya uchumi wa Taifa.





.jpeg)

































