Monday, September 14, 2026

NAIBU WAZIRI SALOME ASHIRIKI UFUNGUZI WA GASTECH 2026 BANGKOK








Bangkok, Thailand 

Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba, leo ameshiriki katika ufunguzi rasmi wa Mkutano wa Kimataifa wa Nishati wa Gastech 2026, unaofanyika Bangkok, Thailand, ukiwakutanisha viongozi wa Serikali, wataalamu, wawekezaji na wadau mbalimbali wa sekta ya nishati kutoka zaidi ya nchi 150 duniani.

Gastech 2026 inafanyika katika kipindi ambacho mahitaji ya nishati duniani yanaendelea kuongezeka kutokana na ongezeko la watu na upanuzi wa viwanda, huku changamoto za kijiografia na kisiasa, kuvurugika kwa mifumo ya usambazaji na mabadiliko ya masoko zikiendelea kuathiri usalama wa nishati duniani.

Mkutano wa mwaka huu unafanyika kwa kaulimbiu “Advancing Global Energy Market Stability”, ukilenga kujadili hatua na suluhisho za kuimarisha usalama, uhimilivu na upatikanaji wa nishati ya uhakika kwa gharama nafuu.

Katika mkutano huo, gesi asilia, LNG, umeme, teknolojia za kupunguza hewa ukaa na Akili Bandia (AI) vinajadiliwa kama miongoni mwa nyenzo muhimu katika kuimarisha usalama wa nishati, unyumbufu wa mifumo ya nishati na ustahimilivu wa viwanda.

Ushiriki wa Naibu Waziri  Mhe. Salome katika Mkutano wa Gastech 2026 unaipa Tanzania fursa ya kuendelea kutangaza uwezo na fursa za uwekezaji katika rasilimali za gesi asilia, pamoja na kujenga na kuimarisha ushirikiano wa kimataifa katika sekta ya nishati.

Gastech 2026 inatarajiwa kuhudhuriwa na zaidi ya wataalamu 50,000 wa sekta ya nishati kutoka zaidi ya nchi 150 na kufunguliwa Rasmi na Waziri Mkuu wa Thailand Mhe. Anutin Charnvirakul.

Ushiriki wa Tanzania katika jukwaa hili unaendelea kuonesha dhamira ya Serikali ya kutumia rasilimali za nishati kuchochea uwekezaji, ukuaji wa uchumi na maendeleo endelevu, sambamba na kushirikiana na jumuiya ya kimataifa katika kujenga mifumo ya nishati yenye uhakika na ustahimilivu.

Prof. Silayo: TFS Itaendeleza Ushirikiano na Chuo cha Mipango ya Maendeleo Vijijini








DODOMA. Kamishna wa Uhifadhi wa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS), Profesa Dos Santos Silayo, ameahidi kuendeleza ushirikiano kati ya taasisi hiyo na Chuo cha Mipango ya Maendeleo Vijijini (IRDP-Mipango).

Profesa Silayo amesema hayo leo, Jumatatu, Septemba 14, 2026, jijini Dodoma, alipomtembelea Mkuu wa Chuo hicho, Profesa Hozen Mayaya, katika Main Campus ya IRDP-Mipango, kabla ya kushiriki katika ufunguzi wa programu ya mafunzo kwa watumishi wapya walioajiriwa na TFS katika kampasi ya Miyuji.

Amesema ushirikiano kati ya TFS na IRDP-Mipango ni muhimu katika kuimarisha mahusiano ya kitaasisi na kuwezesha taasisi hizo kushirikiana katika maeneo yenye manufaa kwa pande zote.

Kwa upande wake, Profesa Mayaya amemshukuru Profesa Silayo na TFS kwa ushirikiano uliopo, akisema chuo hicho kimekuwa kikifaidika na huduma na msaada mbalimbali kutoka TFS.

Ameutaja miongoni mwa ushirikiano huo ni upatikanaji wa miche ya miti kutoka TFS kila inapohitajika kwa ajili ya kupandwa katika maeneo mbalimbali ya chuo na katika jamii.

Profesa Mayaya amesema ushirikiano huo umeendelea kuchangia juhudi za utunzaji wa mazingira na kuongeza uoto wa miti katika maeneo ya chuo na jamii inayokizunguka.

Friday, September 04, 2026

MTUHUMIWA WA “KUFUTA MADENI” YA MIKOPO AKIRI KOSA, AHUKUMIWA KIGOMA





KIGOMA, Septemba 4, 2026 — Mahakama ya Hakimu Mkazi Mkoa wa Kigoma imemhukumu Nicholaus Komba Mahitana maarufu kama Abdallah Mahimbo baada ya kukiri makosa ya kughushi, kujifanya mtumishi wa Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB) na kuwalaghai wanufaika wa mikopo kwa madai kuwa angeweza kuwafutia madeni yao.

Mahakama imemuamuru Mahitana kulipa faini ya Shilingi milioni 1.6 na kurejesha Shilingi milioni 3, pamoja na kuripoti katika Kituo Kikuu cha Polisi Mkoa wa Mbeya mara moja kila mwezi kwa kipindi cha miaka mitatu.

Kesi hiyo imehitimishwa leo, Ijumaa, baada ya mtuhumiwa kumuandikia Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP) akiomba kuingia katika makubaliano ya kukiri kosa (Plea Bargaining).

Hukumu hiyo imeshuhudiwa na Mkurugenzi Mtendaji wa HESLB, Dkt. Bill Kiwia, ambaye amewataka wanufaika wa mikopo kufuata taratibu rasmi za urejeshaji wa mikopo na kuepuka kutumia vishoka wanaodai kuwa na uwezo wa kufuta madeni.

Dkt. Kiwia ameonya kuwa vitendo vya kutumia njia zisizo rasmi vinaweza kuwaingiza wanufaika katika matatizo makubwa, ikiwemo kupoteza fedha na kuhatarisha ajira zao.

HESLB imeendelea kusisitiza kuwa wanufaika wanapaswa kutumia njia na taratibu rasmi katika masuala yote yanayohusu urejeshaji wa mikopo na kuepuka watu wanaojitambulisha kama mawakala wenye uwezo wa kufuta madeni.

PUMAGAS YAPAZA SAUTI NISHATI SAFI, YAANZA ZIARA YA MIKOA MITANO

Wafanyakazi wa Puma Energy Tanzania wakiwa katika picha ya pamoja huku wakipeperusha bendera, ikiwa ni ishara ya uzinduzi wa ziara ya PumaGas katika mikoa mitano nchini. Ziara hiyo imezinduliwa katika kituo cha Puma kilichopo Bunju, Dar es Salaam, tarehe 3 Septemba 2026, na itaendelea kwa wiki nane ikianzia Dar es Salaam, Pwani, Morogoro na Dodoma, kabla ya kuhitimishwa rasmi jijini Mwanza. 



Katika kuunga mkono jitihada za kuhamasisha matumizi ya nishati safi na salama ya kupikia, Puma Energy Tanzania imezindua ziara ya PumaGas itakayopita katika mikoa mitano nchini, ikiwa na lengo la kusogeza elimu na uelewa kuhusu matumizi ya nishati safi karibu zaidi na wananchi.

Uzinduzi wa ziara hiyo umefanyika katika kituo cha Puma kilichopo Bunju, Dar es Salaam, Septemba 3, 2026, ambapo wafanyakazi wa Puma Energy Tanzania waliashiria kuanza kwa safari hiyo kwa kupeperusha bendera.

Ziara hiyo ya wiki nane itaanzia Dar es Salaam, kisha kuelekea Pwani, Morogoro na Dodoma, kabla ya kuhitimishwa jijini Mwanza.

Hatua hiyo inaongeza nguvu katika juhudi za kuhamasisha jamii kuhamia katika nishati safi ya kupikia, ambayo ni muhimu katika kuboresha mazingira ya nyumbani na kuendeleza matumizi ya vyanzo vya nishati vinavyosaidia kupunguza athari kwa mazingira.

Kupitia ziara hiyo, PumaGas inalenga kuwa sehemu ya mabadiliko ya kuelekea matumizi endelevu ya nishati safi, huku ikisisitiza umuhimu wa wananchi kupata uelewa na fursa ya kutumia nishati bora ya kupikia.

Nishati safi, mazingira bora, maisha bora.

#PumaGas #NishatiSafi #CleanCooking #MazingiraBora #NishatiKwaMaendeleo #Tanzania

Thursday, September 03, 2026

SERIKALI YAIMARISHA MIUNDOMBINU YA UMEME IGUNGA” MHE. SALOME






Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba, amesema Serikali kupitia Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) imeendelea kuimarisha miundombinu ya umeme katika Wilaya ya Igunga kwa kutekeleza miradi mbalimbali yenye lengo la kuongeza upatikanaji na uhakika wa umeme katika maeneo ya Wilaya hiyo.

Mhe. Makamba amesema hayo leo, Septemba 3, 2026, katika Bunge la 13, Mkutano wa Nne, Kikao cha Saba, jijini Dodoma, wakati akijibu swali la Mbunge wa Jimbo la Manonga, Mhe. Abubakar Alli Omari, aliyeuliza ni lini Serikali itaanza ujenzi wa Kituo cha Kupoza Umeme cha Ziba, kama alivyoahidi Mheshimiwa Rais wakati wa kampeni za Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025.

Amesema Serikali kupitia TANESCO tayari imekamilisha ujenzi wa njia ya kusambaza umeme ya msongo wa Kilovoti 33 yenye urefu wa kilomita 41 kutoka Kituo cha Kupoza Umeme cha Lusu, pamoja na ujenzi wa Kituo cha Kudhibiti Mifumo ya Umeme (Switching Station) katika eneo la Ziba.

“Ujenzi wa Kituo cha Kudhibiti Mifumo ya Umeme (Switching Station) katika eneo la Ziba umekamilika na umeendelea kusaidia kuimarisha upatikanaji na usambazaji wa umeme katika maeneo mbalimbali ya Wilaya ya Igunga,” amesema Mhe. Makamba.

Aidha, amesema Serikali inaendelea na hatua za kuimarisha zaidi miundombinu ya umeme katika Wilaya ya Igunga, ambapo TANESCO inatarajia kuanza kufanya Upembuzi Yakinifu wa Awali (Pre-Feasibility Study) kwa ajili ya maandalizi ya utekelezaji wa mradi wa ujenzi wa Kituo cha Kupoza Umeme cha Igunga.

Tuesday, September 01, 2026

SERIKALI, BARRICK ZAIMARISHA UBIA WA KIMKAKATI SEKTA YA MADINI

 

Serikali na Kampuni ya Barrick Corporation zimeendelea kuimarisha ushirikiano wao wa kibiashara na uwekezaji katika sekta ya madini, huku pande hizo mbili zikisisitiza umuhimu wa kujenga mazingira yatakayowezesha miradi inayotekelezwa kupitia Twiga Minerals Corporation Limited (TWIGA) kukua, kuongeza uzalishaji na kutoa manufaa endelevu kwa Taifa na wawekezaji.

Mwelekeo huo umejitokeza Jumanne, Septemba 1, 2026, wakati Msajili wa Hazina, Bw. Nehemiah Mchechu, alipokutana na kufanya mazungumzo na wawakilishi wa Barrick Corporation pamoja na uongozi wa TWIGA katika Ofisi ya Msajili wa Hazina (OTR), jijini Dar es Salaam.

Mazungumzo hayo yalijikita katika maendeleo ya biashara, uendeshaji wa miradi na masuala mbalimbali yanayohusu uwekezaji unaosimamiwa kupitia TWIGA, kampuni inayowakutanisha Serikali na Barrick kama wanahisa wenza katika shughuli za uchimbaji wa dhahabu nchini.

Miradi iliyojadiliwa ni pamoja na migodi ya North Mara na Bulyanhulu, pamoja na Buzwagi, ambao kwa sasa upo katika hatua za mwisho za kufungwa.

Ujumbe wa Barrick uliongozwa na Roelie Gey Von Pittius, Meneja wa Fedha wa Barrick kwa Afrika na Mashariki ya Kati, akiambatana na Candace Simpson, Meneja wa Kodi wa Afrika na Mashariki ya Kati; Melkiory Ngido, Meneja wa Barrick nchini Tanzania; na Judith Chambua, Meneja wa Kodi wa Barrick Tanzania.

Barrick Gold Corporation ni moja ya kampuni kubwa zaidi duniani za uchimbaji wa madini ya dhahabu na shaba, ikiwa na makao makuu yake mjini Toronto, Ontario, Canada.

SERIKALI YATAKA UBIA WENYE TIJA NA UENDELEVU

Akizungumza katika kikao hicho, Bw. Mchechu alisema Serikali, kupitia OTR, itaendelea kutoa ushirikiano unaohitajika katika kushughulikia changamoto zinazoweza kujitokeza katika utekelezaji wa miradi ya TWIGA, kwa lengo la kuhakikisha shughuli zake zinaendeshwa kwa ufanisi na kuendelea kuongeza mchango wake katika uchumi wa Tanzania.

Alisema sekta ya madini ina nafasi muhimu katika ukuaji wa uchumi na mapato ya Serikali, ikiwemo kupitia gawio linalotokana na uwekezaji wa Serikali katika kampuni zinazofanya shughuli za madini.

“Tunauthamini sana mchango wa aina ya ushirikiano tulionao na Barrick,” alisema Bw. Mchechu.

Kwa mujibu wa Msajili wa Hazina, uzoefu uliopatikana kupitia ushirikiano na Barrick umeendelea kuwa muhimu katika kuimarisha uwezo wa Serikali kusimamia uwekezaji mkubwa katika sekta ya madini na kujenga ubia wenye manufaa kwa pande zote.

Alisisitiza pia umuhimu wa taasisi za Serikali kuwa na uratibu na uelewa wa pamoja katika kushughulikia masuala yanayogusa uwekezaji mkubwa wa kimkakati.

“Katika masuala muhimu kama haya yanayomhusu mshirika muhimu katika biashara muhimu, ni lazima Serikali izungumze kwa sauti moja,” alisema.

UWEKEZAJI WA MUDA MREFU

Bw. Mchechu alisema dhamira ya Serikali ni kuona mazingira ya biashara na uwekezaji yanaendelea kuwa na uthabiti unaowezesha kampuni kufanya mipango ya muda mrefu na kuendeleza uwekezaji wenye manufaa kwa vizazi vijavyo.

“Tunataka kuwa na biashara ambayo inaweza kuendelea kwa utulivu kizazi hadi kizazi na kustahimili tawala mbalimbali za kisiasa,” alisema.

Kauli hiyo inaweka msisitizo katika kujenga uhusiano wa muda mrefu wa kibiashara, wenye msingi wa mazungumzo, uelewa wa pamoja na mazingira yanayowezesha uwekezaji kuendelea kukua.

Kwa upande wake, Von Pittius alisema Barrick inathamini ushirikiano wake na Serikali ya Tanzania na itaendelea kufanya kazi kwa karibu na mamlaka husika katika masuala yanayohusu shughuli na uwekezaji wake nchini.

Alieleza utayari wa kampuni hiyo kuendelea kushirikiana na Serikali katika maeneo yenye maslahi ya pamoja kwa maendeleo ya sekta ya madini.

Mazungumzo hayo yanaendeleza ushirikiano kati ya Serikali na Barrick katika kuimarisha TWIGA kama jukwaa la ubia wa kibiashara, huku msisitizo ukiwekwa katika kuongeza ufanisi, uzalishaji na thamani inayotokana na rasilimali za madini kwa manufaa ya Taifa na wadau wa uwekezaji.

TANZANIA, UINGEREZA ZATAZAMA FURSA MPYA ZA UWEKEZAJI SEKTA YA MADINI










 Tanzania na Uingereza zimeendelea kuimarisha diplomasia ya kiuchumi, safari hii zikiweka mkazo katika uwekezaji, uongezaji thamani wa madini na namna sekta hiyo inavyoweza kuleta manufaa mapana zaidi kwa wananchi na uchumi wa Taifa.

Hatua hiyo imejidhihirisha leo jijini Dodoma, wakati Waziri wa Madini, Mhe. Anthony Mavunde, alipokutana na Balozi wa Uingereza nchini Tanzania, Mhe. Marianne Young, kwa mazungumzo yaliyolenga kuchambua fursa zilizopo katika sekta ya madini na maeneo mapya ya ushirikiano kati ya mataifa hayo mawili.

Mazungumzo hayo yana umuhimu mkubwa katika kipindi ambacho Tanzania inaendelea kuweka msisitizo katika kuhakikisha rasilimali zake za madini haziondoki nchini zikiwa malighafi pekee, bali zinaongezewa thamani ili kuchochea uwekezaji wa viwanda, kuongeza ajira, kukuza biashara na kupanua mchango wa sekta hiyo katika uchumi.

Kwa mantiki hiyo, kuvutia uwekezaji katika sekta ya madini hakulengi tu kuongeza mitaji, bali pia kujenga minyororo ya thamani inayoweza kutoa nafasi kwa Watanzania kushiriki katika hatua mbalimbali—kuanzia uchimbaji na uchakataji hadi biashara na huduma zinazohusiana na sekta hiyo.

Katika mazungumzo hayo, pande hizo mbili pia zimeweka mkazo katika umuhimu wa ukuaji wa sekta ya madini unaoshirikisha wote, ili manufaa yatokanayo na rasilimali hizo yaweze kugusa maisha ya wananchi na kuchangia maendeleo endelevu.

Mkutano wa Mhe. Mavunde na Balozi Young unaendeleza uhusiano wa muda mrefu kati ya Tanzania na Uingereza, huku diplomasia ya kiuchumi ikizidi kuwa daraja muhimu la kufungua fursa mpya za biashara, uwekezaji na ushirikiano wa maendeleo.

Tanzania na Uingereza zimeahidi kuendelea kufanya kazi pamoja katika maeneo yenye maslahi ya pande zote, kwa lengo la kuimarisha ustawi wa mataifa hayo mawili na kuhakikisha ushirikiano wao unazalisha matokeo yanayoonekana katika uchumi na maisha ya wananchi.

NAIBU WAZIRI SALOME ASHIRIKI UFUNGUZI WA GASTECH 2026 BANGKOK

Bangkok, Thailand  Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba, leo ameshiriki katika ufunguzi rasmi wa Mkutano wa Kimataifa wa Nishati wa ...