Monday, July 20, 2026

MIRADI YA UCHUKUZI KUIFANYA KIGOMA KUWA KITOVU CHA BIASHARA AFRIKA MASHARIKI NA KATI - PROF. MBARAWA








Waziri wa Uchukuzi, Profesa Makame Mbarawa amesema Serikali ya Awamu ya Sita inaendelea kutekeleza uwekezaji mkubwa katika sekta ya uchukuzi unaolenga kuifanya Kigoma kuwa kitovu cha usafirishaji na biashara kinachounganisha Tanzania na nchi za Afrika Mashariki na Kati.

Profesa Mbarawa amesema hayo leo Jumatatu Julai 20, 2026 katika hafla iliyohudhuriwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, wakati wa uzinduzi wa meli nne za mizigo, uwekaji wa jiwe la msingi la ujenzi wa gati la abiria na mizigo Bandari ya Kigoma pamoja na uzinduzi wa ujenzi wa Reli ya Kisasa (SGR) kipande cha Tabora–Kigoma.

Amesema chini ya uongozi wa Rais Samia, Serikali imewekeza kwa kiwango kikubwa katika reli ya kisasa, bandari, viwanja vya ndege na usafiri wa majini kwa lengo la kuunganisha mikoa yote ya Tanzania pamoja na nchi jirani kupitia mfumo jumuishi wa uchukuzi.

Kwa mujibu wa Profesa Mbarawa, meli nne mpya za mizigo zitaongeza usalama wa usafirishaji katika Ziwa Tanganyika, kupunguza gharama za usafirishaji wa mizigo, kukuza biashara kati ya Tanzania, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo na Burundi, pamoja na kufungua fursa mpya za ajira na uwekezaji.

Aidha, amesema maboresho yanayoendelea Bandari ya Kigoma pamoja na ujenzi wa Reli ya Kisasa kutoka Tabora hadi Kigoma yataongeza ufanisi wa usafirishaji wa abiria na mizigo, huku yakiiunganisha Bandari ya Dar es Salaam na masoko ya ukanda wa Afrika Mashariki na Kati.

Profesa Mbarawa pia amesema Serikali inaendelea na maboresho ya uwanja wa ndege wa Kigoma kwa gharama ya Sh. bilioni 51.4, yanayojumuisha ujenzi wa jengo jipya la abiria, mnara wa kuongozea ndege, njia za ndege, taa za kuongozea ndege na miundombinu mingine muhimu. 

Ameongeza kuwa miradi hiyo inaonesha dhamira ya Serikali ya kujenga mfumo wa uchukuzi unaounganisha reli, bandari na usafiri wa anga ili kuharakisha maendeleo ya uchumi wa Taifa.

Tuesday, July 14, 2026

MMUYA: WANANCHI WANUFAIKE NA UWEKEZAJI WA NHC KUPITIA NYUMBA ZA GHARAMA NAFUU










Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Mhe. Kaspar Mmuya, amekagua maendeleo ya ujenzi wa mradi wa maghala unaotekelezwa na Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) katika Mtaa wa Viwandani, Kata ya Railway, Halmashauri ya Manispaa ya Mtwara-Mikindani.

Mhe. Mmuya amefanya ukaguzi huo Julai 13, 2026, ikiwa ni sehemu ya ziara yake ya kikazi ya siku mbili mkoani Mtwara yenye lengo la kukagua utekelezaji wa miradi iliyo chini ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi.

Akipokea taarifa ya mradi huo, Mhe. Mmuya ameelezwa kuwa ujenzi wa maghala hayo unagharimu shilingi bilioni 4.1, ambapo hadi sasa shilingi bilioni 2.6 zimetumika. Mradi huo unatarajiwa kukamilika Septemba 2026.

Katika ukaguzi huo, Mhe. Mmuya amelishauri Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) kuendelea kubuni na kuwekeza katika miradi inayogusa maisha ya wananchi moja kwa moja, hususan ujenzi wa nyumba za gharama nafuu, ili kusaidia kukabiliana na changamoto ya upungufu wa makazi nchini.

Aidha, amepongeza Shirika hilo kwa kuwekeza katika ujenzi wa maghala katika eneo lenye shughuli kubwa za kiuchumi, akibainisha kuwa uwepo wa Bandari ya Mtwara pamoja na uzalishaji wa mazao ya biashara, hususan korosho, unafanya mradi huo kuwa na umuhimu mkubwa katika kuchochea biashara na maendeleo ya uchumi wa mkoa huo.

Mradi huo unatarajiwa kuongeza uwezo wa kuhifadhi bidhaa mbalimbali, ikiwemo mazao ya kimkakati kama korosho, hatua itakayochangia kuongeza thamani ya mazao, kuboresha huduma za uhifadhi na kuimarisha shughuli za biashara kwa wakazi wa Mkoa wa Mtwara na maeneo ya jirani.

NGORONGORO NA SIMBA WAUNGANA KUITANGAZA TANZANIA KUPITIA UTALII NA MICHEZO


Arusha: Mamlaka ya Hifadhi ya Eneo la Ngorongoro (NCAA) na Klabu ya Simba Sports Club zimeanzisha ushirikiano wa kimkakati unaolenga kuitangaza Tanzania kupitia utalii na michezo, hatua inayotarajiwa kuongeza hamasa ya kutembelea vivutio vya utalii nchini huku ikiimarisha taswira ya Tanzania kimataifa.

Akizungumza katika uzinduzi wa ushirikiano huo, Makamu Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya NCAA, Dkt. Harrieth Mtae, alisema ushirikiano huo ni mwanzo wa enzi mpya unaoonyesha namna sekta ya umma na taasisi za michezo zinavyoweza kushirikiana kuleta thamani kwa taifa.

"Ninawashukuru viongozi wa Simba Sports Club kwa kukubali kuwa washirika wetu katika safari hii muhimu ya kuitangaza Tanzania kupitia michezo na utalii. Leo tunashuhudia mwanzo mpya wa ushirikiano unaounganisha chapa mbili kubwa za Afrika kwa lengo la kuitangaza Tanzania duniani," alisema Dkt. Mtae.

Alieleza kuwa Bodi ya Wakurugenzi ya NCAA inaunga mkono kikamilifu ushirikiano huo kwa kuwa unaendana na maono ya kuifanya Ngorongoro kuwa kivutio cha utalii cha kiwango cha kimataifa, sambamba na kuchangia utekelezaji wa vipaumbele vya taifa katika kukuza utalii, uchumi na diplomasia ya kimkakati.

Kwa mujibu wa Dkt. Mtae, kupitia kampeni ya "The Pride Returns Home", mamilioni ya Watanzania pamoja na mashabiki wa mpira wa miguu ndani na nje ya nchi watapata sababu mpya ya kutembelea Ngorongoro na kujivunia urithi wa kipekee wa Tanzania.

Alibainisha kuwa wakati Tanzania ikijiandaa kuwa mwenyeji wa fainali za AFCON 2027, ushirikiano huo unathibitisha kuwa michezo inaweza kuwa jukwaa muhimu la kutangaza utalii, kuhamasisha uhifadhi wa maliasili na kuijenga Tanzania kama moja ya maeneo bora ya utalii barani Afrika.

Dkt. Mtae alihitimisha kwa kueleza matarajio ya NCAA kuona ushirikiano huo ukidumu kwa muda mrefu na kuleta manufaa kwa pande zote mbili pamoja na taifa kwa ujumla.

"Karibuni Nyumbani, Karibuni Ngorongoro," alisisitiza.

Wednesday, July 08, 2026

MBUNGE WA BUNGE LA NORWAY AVUTIWA NA VIVUTIO VYA SERENGETI, AIKARIBISHA DUNIA KUTEMBELEA TANZANIA


Mbunge wa Bunge la Norway, Mhe. Himanshu Gulati, akiongozana na mwenyeji wake, Mbunge wa Jimbo la Buchosa, Mhe. Eric Shigongo, ametembelea Hifadhi ya Taifa Serengeti na kujionea vivutio vya kipekee vya utalii, wanyamapori mbalimbali pamoja na mandhari ya kuvutia inayoifanya Tanzania kuwa miongoni mwa nchi zinazoongoza kwa utalii duniani.

Akizungumza baada ya ziara hiyo, Mhe. Gulati alisema amefurahishwa na ubora wa vivutio vya utalii nchini pamoja na juhudi kubwa zinazofanywa na Serikali ya Tanzania katika kuhifadhi rasilimali za asili na wanyamapori kwa manufaa ya vizazi vya sasa na vijavyo.

Aidha, amewahamasisha wananchi wa Norway na mataifa mengine duniani kuitembelea Tanzania ili kujionea uzuri wa Hifadhi za Taifa, urithi wa asili na uzoefu wa kipekee unaopatikana katika vivutio vya utalii vya nchi hii.

"Tanzania ni nchi yenye vivutio vya kipekee na mazingira ya kuvutia. Kila mtu anapaswa kupata nafasi ya kuitembelea na kujionea uzuri wake," alisema Mhe. Gulati.

WAZIRI MKUU AKUTANA NA MAKAMU WA RAIS WA KAMPUNI YA ALSTOM




▪️Yaonesha nia ya kushirikiana na Serikali katika usafiri ya Mijini.

▪️Dkt. Mwigulu awahakikishia mazingira bora ya uwekezaji

WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba, amekutana na Makamu wa Rais wa Kampuni ya ALSTOM ya nchini Ufaransa, Philippe Deller ambapo wamejadiliana kuhusu fursa za uwekezaji katika sekta ya miundombinu ya usafiri nchini Tanzania.

Katika mazungumzo hayo, Dkt. Mwigulu Nchemba aliikaribisha ALSTOM kuwekeza nchini, akieleza kuwa Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan inaendelea kuweka mazingira wezeshi kwa wawekezaji na kutekeleza mageuzi yanayolenga kuifanya Tanzania kuwa kitovu cha biashara, usafiri na uwekezaji katika ukanda wa Afrika Mashariki.

Kwa Upande wake Bw. Phillepe alieleza nia ya kampuni hiyo kushirikiana na Serikali ya Tanzania katika utekelezaji wa miradi ya kimkakati ya usafiri wa mijini.

Kampuni hiyo imeonesha utayari wa kuwekeza katika ujenzi wa mifumo ya usafiri wa haraka na miundombinu ya kisasa yenye lengo la kupunguza msongamano wa magari katika Jiji la Dar es Salaam, huku ikitazama pia fursa za utekelezaji wa miradi kama hiyo katika majiji ya Mwanza, Mbeya na Arusha.

Miradi hiyo inatarajiwa kuongeza ufanisi wa usafiri wa mijini, kupunguza muda wa safari, kuimarisha shughuli za biashara na uwekezaji, pamoja na kuchochea ukuaji wa uchumi na kuboresha maisha ya wananchi kupitia matumizi ya teknolojia za kisasa.

Mazungumzo hayo ni sehemu ya jitihada za Serikali za kuimarisha ushirikiano na kampuni kubwa za kimataifa ili kuleta teknolojia, utaalamu na mitaji inayochochea maendeleo ya miundombinu na uchumi wa Taifa.

Kampuni ya ALSTOM, ina uzoefu mkubwa katika kubuni, kujenga na kuendesha mifumo ya kisasa ya usafiri wa umma ikiwemo reli za kisasa, treni za mwendo kasi, metro, tram na teknolojia za usimamizi wa usafiri.

Monday, July 06, 2026

RAIS SAMIA AMTEMBELEA PACOME, AMPATIA POLE NA KUMTAKIA AFYA NJEMA

 



Dar es Salaam – Mchezaji wa klabu ya Yanga, Pacome Zouzoua, amepata faraja ya kipekee baada ya kutembelewa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, alipokuwa akipatiwa matibabu katika Hospitali ya Aga Khan, jijini Dar es Salaam.

Rais Samia alikuwa hospitalini hapo kwa ajili ya kumjulia hali Sheikh Rashid Hamad Othman, lakini alipojulishwa kuwa Pacome amelazwa katika chumba jirani akipatiwa matibabu kufuatia majeraha aliyoyapata kwenye mchezo wa Ligi Kuu ya NBC dhidi ya JKT Tanzania, alitumia fursa hiyo kumtembelea na kumpa pole.

Hatua hiyo imeonesha moyo wa upendo na kujali kwa viongozi wakuu wa Taifa kwa wanamichezo, ikisisitiza nafasi muhimu ambayo michezo inaendelea kuwa nayo katika kuunganisha Watanzania.

Mashabiki wa soka nchini wanaendelea kumuombea Pacome apone haraka na kurejea uwanjani kuendelea kuonesha kipaji chake na kuiburudisha Yanga pamoja na wapenzi wa soka kwa ujumla.

Tunamtakia Pacome Zouzoua nafuu ya haraka na kurejea uwanjani akiwa imara zaidi. 💚⚽

RAIS MWINYI ATOA SH. MILIONI 200 KWA KITUO CHA IRSHAAD LUSHOTO, ARIDHIA MAOMBI YA PROF. SHEMDOE

 










Na OWM – TAMISEMI, Lushoto

Rais wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, ametoa Shilingi Milioni 200 kwa ajili ya kuendeleza Kituo cha Elimu ya Kiislamu Irshaad (Irshaad Islamic Centre) kilichopo Lushoto, Mkoa wa Tanga, kufuatia ombi lililotolewa na Mbunge wa Jimbo la Lushoto na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, Mhe. Prof. Riziki Shemdoe.

Msaada huo utasaidia kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo katika kituo hicho, ikiwemo kuboresha Chuo cha Ufundi, kujenga madrasa ya kisasa, nyumba za walimu, hospitali, ukumbi wa mikutano, jengo la wageni pamoja na bustani ya kisasa, hatua inayotarajiwa kuongeza ubora wa elimu na huduma za kijamii kwa wananchi wa Lushoto na maeneo jirani.

Prof. Shemdoe aliwasilisha ombi hilo wakati wa Sherehe ya Maulidi ya Kumswalia Mtume Muhammad (S.A.W.) zilizofanyika Julai 5, 2026 katika Kituo cha Irshaad Islamic Centre, ambapo Mhe. Dkt. Hussein Mwinyi alikuwa Mgeni Rasmi.

Katika tukio hilo, Rais Mwinyi pia alikubali ombi la Sheikh Sharrif Hussein Ahmad Badawiyy la kuwa Mlezi wa Kituo cha Irshaad Islamic Centre, akiahidi kuendelea kushirikiana na viongozi na wadau mbalimbali katika kukiendeleza ili kiwe kitovu cha elimu bora, maadili mema na maendeleo ya jamii.

Aidha, Rais Mwinyi aliridhia ombi la kutambua mchango wa Hayati Alhaji Ali Hassan Mwinyi kwa kuruhusu bustani itakayojengwa ndani ya Chuo cha Ufundi cha kituo hicho kuitwa jina lake, ikiwa ni sehemu ya kuenzi mchango wake mkubwa katika maendeleo ya taasisi hiyo.

Wito wa Prof. Shemdoe uliungwa mkono na viongozi mbalimbali waliochangia kwa hiari yao, akiwemo yeye mwenyewe aliyetoa Shilingi Milioni 20, Mkuu wa Mkoa wa Tanga Dkt. Batilda Burian (Milioni 5), Mkuu wa Mkoa wa Morogoro Mhe. Adam Malima (Milioni 5), Mbunge wa Bumbuli Mhandisi Ramadhani Hamza (Milioni 5), Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Tanga Bw. Rajab Abdallah (Milioni 3) na Mbunge wa Afrika Mashariki Dkt. Abdullah Makame (Milioni 5), na kufanya jumla ya michango kufikia Shilingi Milioni 248.

Akizungumza baada ya hafla hiyo, Prof. Shemdoe alimshukuru Rais Mwinyi kwa kukubali ombi hilo, akieleza kuwa msaada huo utakuwa chachu ya kuimarisha elimu, kukuza ustawi wa jamii na kuboresha huduma zinazotolewa na Kituo cha Irshaad.

Wananchi na viongozi waliohudhuria hafla hiyo walimpongeza Rais Mwinyi kwa uamuzi huo, wakieleza kuwa utaacha alama ya kudumu katika maendeleo ya elimu, ujuzi na huduma za kijamii kwa vizazi vya sasa na vijavyo katika Wilaya ya Lushoto.

MIRADI YA UCHUKUZI KUIFANYA KIGOMA KUWA KITOVU CHA BIASHARA AFRIKA MASHARIKI NA KATI - PROF. MBARAWA

Waziri wa Uchukuzi, Profesa Makame Mbarawa amesema Serikali ya Awamu ya Sita inaendelea kutekeleza uwekezaji mkubwa katika sekta ya uchukuzi...