Thursday, February 05, 2026

Serikali Yabainisha Maeneo ya Miradi ya Umeme wa Upepo na Jua, Kishapu kuzalisha MW 150







Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba amesema Serikali imekwishabainisha na kufanya utafiti wa maeneo mbalimbali yanayofaa kuendelezwa kwa ajili ya miradi ya kuzalisha umeme kwa kutumia upepo na jua, ikiwa ni pamoja na Zuzu-Dodoma, Same-Kilimanjaro na Manyoni-Singida.

Mhe. Salome ametoa kauli hiyo leo Februari 05, 2026 bungenini jijini Dodoma wakati akijibu swali la Mbunge wa Mwera, Mhe. Suleiman Mohamed Rashid aliyehoji juu ya mpango wa Serikali wa kutumia vyanzo vya umeme na upepo juu vilivyopo nchini.

" Kwa sasa Serikali inatekeleza mradi wa kuzalisha umeme wa megawati 150 katika Wilaya ya Kishapu, Shinyanga ambapo awamu ya kwanza ya mradi huo wenye megawati 50 imekamilika na hatua za kuingiza umeme huo katika Gridi ya Taifa zimeanza," Amesema Mhe. Salome.

Akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Kilimanjaro, Mhe Esther Malleko aliyehoji mkakati wa Serikali katika kumaliza usambazaji wa umeme kwenye vitongoji vilivyosalia mkoani humo, Mhe. Salome amesema Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) inaendelea na kazi za utekelezaji wa ujenzi wa miundombinu ya kusambaza umeme katika Mkoa wa Kilimanjaro ambapo hadi kufikia Januari 2026 jumla ya vitongoji 2,032 kati ya 2,258 sawa na asilimia 90 vilipatiwa umeme na kusalia vitongoji 226 ambavyo vitapelekewa umeme kupitia miradi mbalimbali.

Wednesday, February 04, 2026

RAIS SAMIA AENDELEZA DIPLOMASIA YA KIMATAIFA DUBAI, ALAKIWA NA MAZUNGUMZO NA MTAWALA WA DUBAI KANDO YA WGS 2026

 



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, ameendelea kuimarisha diplomasia ya kimataifa kwa kufanya mazungumzo ya ngazi ya juu na Makamu wa Rais wa Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) na Mtawala wa Dubai, Sheikh Mohammed bin Rashid Al Maktoum, kando ya Mkutas ya Dunia ya Serikali (World Governments Summit – WGS 2026), jijini Dubai, tarehe 04 Februari, 2026.

Mazungumzo hayo yalilenga kuendeleza ushirikiano kati ya Tanzania na UAE katika maeneo ya kimkakati ikiwemo biashara, uwekezaji, miundombinu, uvumbuzi na diplomasia ya kiuchumi, sambamba na kubadilishana uzoefu kuhusu uongozi na maendeleo ya kisasa.

Mara baada ya mazungumzo hayo, Mheshimiwa Rais Samia alipokea zawadi ya kitabu kutoka kwa Sheikh Mohammed bin Rashid Al Maktoum, ishara ya heshima, urafiki na uhusiano imara unaoendelea kuimarishwa kati ya Tanzania na UAE.

Ushiriki wa Rais Samia katika WGS 2026 unaendelea kuweka Tanzania katika ramani ya majadiliano ya kimataifa, huku ukitafsiri dira ya Serikali ya Awamu ya Sita ya kujenga ushirikiano wa kimataifa wenye tija, unaozingatia maslahi ya taifa na maendeleo endelevu.

#RaisSamia #WGS2026 #TanzaniaNaUAE #DiplomasiaYaKiuchumi #MahusianoYaKimataifa#KaziNaUtuTunasongaMbele

RAIS SAMIA AWEKA AFRIKA KATIKA RAMANI MPYA YA UWEKEZAJI WA KIMATAIFA KUPITIA GAIS DUBAI




Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, ameshiriki uzinduzi wa Global Africa Investment Summit (GAIS) jijini Dubai.

Tukio lililoashiria mwanzo wa sura mpya ya Afrika katika kuvutia mitaji ya kimataifa kupitia uwekezaji uliopangiliwa, wenye uthabiti wa kifedha na matokeo ya muda mrefu.

Akihutubia viongozi wa kisiasa, wawekezaji na wadau wa kimataifa jana usiku, Rais alisisitiza kuwa katika mazingira ya sasa ya uchumi wa dunia, wawekezaji hawatafuti fursa pekee, bali uaminifu—uthabiti wa sera, taasisi imara na serikali zinazotekeleza ahadi zake kwa vitendo. 

Alieleza kuwa Tanzania imejikita katika kujenga misingi imara ya uwekezaji kupitia mageuzi ya sera na uwekezaji mkubwa katika nishati, reli ya kisasa, bandari na miundombinu ya uchukuzi, sambamba na uanzishwaji wa Maeneo Maalum ya Uwekezaji na Dirisha Moja la Uwekezaji, ili kurahisisha na kuharakisha huduma kwa wawekezaji.

Ushiriki wa Tanzania katika GAIS unaakisi dhamira ya nchi ya kuingia kwenye ushirikiano wa kimkakati unaopangiliwa vizuri, unaozingatia vipaumbele vya maendeleo ya taifa na matarajio ya wawekezaji wa kimataifa, kwa lengo la kujenga uchumi shindani na jumuishi.

GAIS inalenga kuoanisha uongozi wa kisiasa, rasilimali za kitaifa na mitaji ya kimataifa, na kuifanya Afrika—na hususan Tanzania—kuwa kitovu cha uwekezaji unaozalisha matokeo halisi, fursa za ajira na maendeleo endelevu kwa kizazi cha sasa na kijacho.

#GAIS2026 #EconomicDiplomacy #TanzaniaNaUwekezaji #RaisSamia #GlobalAfricaInvestmentSummit #KaziNaUtuTunasongaMbele

Tuesday, February 03, 2026

WMA YAFUNGA MTAMBO WA KISASA UNAOHAKIKI DIRA ZA MAJI DODOMA

Mtambo wa kisasa unaotumika kuhakiki dira za maji. Mtambo huu wa kidijitali umefungwa katika Jengo la Makao Makuu ya Wakala wa Vipimo (WMA), Dodoma.

Sehemu ya Mtambo wa kisasa unaotumika kuhakiki dira za maji. Mtambo huu wa kidijitali umefungwa katika Jengo la Makao Makuu ya Wakala wa Vipimo (WMA), Dodoma.

Jengo lenye mitambo ya kuhakiki dira za maji, lililopo katika Kituo cha Uhakiki Vipimo Misugusugu, Mkoa wa Pwani.

Afisa Vipimo kutoka Wakala wa Vipimo (WMA), akihakiki dira za maji.

 Veronica Simba - WMA 

Wakala wa Vipimo (WMA) umesimika mtambo wa kisasa wa kidijitali wa kuhakiki dira za maji katika jengo la makao yake makuu lililopo jijini Dodoma.

Meneja Uhakiki wa Vipimo na Viwango wa WMA Makao Makuu, Magesa Biyani amesema usimikaji mtambo huo uliogharimu takribani shilingi milioni 400, utawezesha uidhinishaji na uhakiki wa dira za maji kwa muda mfupi na kwa usahihi zaidi kupitia miradi mingi ya maji inayoendelea kutekelezwa nchini ikiwemo Mkoa wa Dodoma na mikoa mingine jirani.

Akizungumza na wanahabari wa WMA Februari 3, 2026, Biyani amesema kuwa “Mtambo huu umekuja kwa wakati mwafaka kuwezesha wafanyabiashara pamoja na Mamlaka za Maji kuzingatia kwamba dira za maji zote ambazo wanawafungia wateja katika maeneo yao ziwe zimehakikiwa na WMA ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma kulingana na thamani ya fedha wanazolipa.”

Akifafanua zaidi, amesema kuwa mtambo huo una uwezo wa kuhakiki dira za maji nyingi zaidi kwa wakati mmoja kwa kutumia muda mfupi zaidi tofauti na mitambo ya awali ambayo ni ya ki-makenikali (Mechanical Test Bench) yenye uwezo wa kuhakiki dira za maji 10 kwa wakati mmoja ikitumia dakika 20 hadi 30.

Amesema kuwa mtambo huo pamoja na mingine miwili ya aina hiyo iliyoko katika Kituo cha Uhakiki Vipimo, Misugusugu mkoani Pwani, kwa pamoja imeleta faida kubwa ikiwemo kupima dira za maji nyingi zaidi, kwa usahihi zaidi na kwa muda mfupi tofauti na awali kabla ya uwepo wake.

Akitoa mfano, Biyani amesema mathalani kwa Kituo cha Misugusugu ambako mitambo ya aina hiyo ilitangulia kusimikwa kabla ya Dodoma, dira za maji kati ya laki mbili hadi laki tatu zimekuwa zikipimwa kwa mwaka kutegemea na uhitaji kutokana na kuongezeka kwa miradi ya kimkakati.

“Kwahiyo imeleta faida kubwa sana na kusaidia thamani ya fedha iweze kuonekana kwa wateja/wananchi, Mamlaka za Maji na wafanyabiashara na hata kwa uchumi wa nchi,” ameeleza Biyani.

 Akidadavua zaidi namna WMA inavyohusika katika uidhinishaji na uhakiki wa dira za maji, ameeleza kuwa hilo ni mojawapo ya majukumu yake ya uhakiki wa vipimo vya aina mbalimbali nchini kwa lengo la kumlinda mlaji.

Amesema kuwa, WMA huidhinisha na kuhakiki vipimo kwa niaba ya Serikali ambapo kwa upande wa dira za maji, mfanyabiashara yeyote binafsi au kampuni kabla ya kuagiza au kuzalisha bidhaa hizo anatakiwa awasilishe sampuli yake WMA ili kuhakiki muundo wake na baada ya kuidhinishwa anatakiwa kuziwasilisha bidhaa zote alizoagiza au kuzalisha ili zihakikiwe kwa kila moja kujiridhisha kuhusu usahihi wake.

Biyani amefafanua zaidi kuwa zoezi hilo hulenga kuzilinda pande zote mbili yaani mteja na muuzaji ili yeyote kati yao asipunjwe. Dira za maji zilizohakikiwa humuwezesha mteja kulipia kiwango stahiki kulingana na matumizi yake ilhali kwa upande wa muuzaji humwezesha kupata malipo stahiki kulingana na huduma anayotoa.

Akijibu swali la mwandishi kuhusu mipango ya WMA kufikisha huduma hiyo nchi nzima, Biyani ameeleza kuwa Mpango Mkakati wa Wakala wa miaka mitano ijayo kuanzia mwaka huu wa 2026 ni kusimika mitambo ya aina hiyo katika Kanda zote zilizosalia nchini ambazo amezitaja kuwa ni Kanda ya Kaskazini, Kanda ya Ziwa, Kanda ya Magharibi pamoja na Kanda ya Kusini.

Hata hivyo, ameweka bayana kuwa kutokuwepo kwa mitambo ya kisasa katika Kanda tajwa haimaanishi kuwa kazi hiyo haifanyiki katika maeneo hayo, la hasha, inafanyika kwa kutumia mitambo ya ki-makenikali pamoja na ile midogo inayobebeka (Portable Test Kit) ambayo amesema Maafisa Vipimo kote nchini huibeba mikononi na kwenda nayo katika maeneo mbalimbali kuhakiki dira za maji.

Katika hatua nyingine, Biyani ametoa hamasa kwa wadau wa vipimo mkoani Dodoma na mikoa ya jirani hususani katika sekta ya maji kutumia fursa ya uwepo wa mtambo huo wa kisasa kupeleka dira za maji WMA zikahakikiwe na kuidhinishwa.

Biyani ameonya kwamba ni kosa kisheria kwa mtu yeyote kufunga na/au kutumia dira ya maji ambayo haijahakikiwa na Wakala wa Vipimo huku akibainisha kuwa adhabu yake huanzia kutozwa faini ya shilingi laki moja hadi milioni 20 kwa kosa la kwanza na shilingi milioni 20 hadi milioni 50 kwa kosa la pili kutegemea na aina ya kosa.

Ametaja gharama za kuhakiki dira za maji kwa mujibu wa sheria kuwa ni shilingi elfu kumi tu kwa kila moja na kwa uidhinishaji wa muundo ni shilingi elfu hamsini.

Sheria ya Vipimo, Sura Namba 340 kupitia kanuni zake mbalimbali inaielekeza WMA kuhakiki dira za maji walau mara moja kila mwaka lakini pia Wakala hufanya kaguzi mbalimbali za kushtukiza ili kubaini endapo kuna udanganyifu na kuchukua hatua.

Wakala imeendelea kutoa elimu kwa wadau wa vipimo na umma kwa ujumla katika maeneo mbalimbali ikiwemo namna ya kutambua kipimo ambacho kimehakikiwa ambapo kwa upande wa dira za maji, utambuzi kuwa dira husika imehakikiwa ni kwa kuona lakiri iliyofungwa pamoja na muhuri wa WMA ukionesha tarehe, mwezi na muda ambao kifaa hicho kimehakikiwa. Dira yoyote ambayo haina lakiri na muhuri wa WMA inamaanisha kuwa haijahakikiwa.

DKT. MWIGULU AKUTANA NA NAIBU MKURUGENZI WA FAO






WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba amefanya mazungumzo na Naibu Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa (FAO), Bi. Beth Bechdol jijini Dar es salaam leo tarehe 3 Februari, 2026.

Pamoja na mambo mengine, Viongozi hao wameahidi kuendeleza ushirikiano uliopo baina ya Tanzania na FAO ili kukuza na kuimarisha sekta ya Kilimo nchini.

 

RAIS SAMIA AANZA ZIARA YA KIKAZI DUBAI, AONGEZA KASI YA DIPLOMASIA YA KIUCHUMI NA UWEKEZAJI


Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ameanza rasmi ziara ya kikazi nchini Dubai, Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE), akilenga kuimarisha diplomasia ya kiuchumi, kupanua wigo wa ushirikiano wa kimataifa na kuvutia uwekezaji wa moja kwa moja nchini Tanzania.

Katika ratiba ya leo, Rais Samia anafanya mazungumzo ya ngazi ya juu na Mheshimiwa Gaston Browne, Waziri Mkuu wa Antigua and Barbuda, ikiwa ni sehemu ya kuimarisha uhusiano wa kidiplomasia na kiuchumi kati ya Tanzania na nchi rafiki. 

Aidha, Rais Samia anakutana na Bi. Shaikha Al Nuwais, Katibu Mkuu wa Shirika la Utalii la Umoja wa Mataifa (UN Tourism), kwa mazungumzo ya pande mbili yanayolenga kuendeleza sekta ya utalii kama nguzo muhimu ya uchumi na kichocheo cha uwekezaji.

Jioni ya leo, Rais Samia anatarajiwa kushiriki uzinduzi wa Global Africa Investment Summit (GAIS), jukwaa mahsusi la uwekezaji linalolenga kuoanisha miradi iliyo tayari kuwekezeka barani Afrika na wawekezaji wa kimataifa. Ushiriki wa Tanzania katika GAIS unaakisi dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita ya kugeuza fursa kuwa matokeo halisi ya kiuchumi.

GAIS ni mpango wa kimkakati unaoendeshwa sambamba na majadiliano ya sera ya World Governments Summit (WGS), ukiwa na lengo la kubadili mijadala ya sera kuwa uwekezaji wenye tija, unaochochea ukuaji wa uchumi, ajira na maendeleo endelevu barani Afrika.

Wananchi wanaendelea kushauriwa kufuatilia taarifa zaidi kupitia akaunti rasmi za Ikulu Mawasiliano, kwa maendeleo ya ziara hii muhimu kwa mustakabali wa uchumi wa Taifa.

KATAMBI AKUTANA NA BALOZI WA UINGEREZA



Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi,Patrobas Katambi amekutana na Balozi wa Uingereza nchini,Marianne Young ambae aliambatana na Mkuu wa Usalama na Sheria,Alex Beck pamoja na Mkuu wa Ofisi ya Dodoma,Godfrida Magubo.

Katika kikao hicho mambo mbalimbali yalijadiliwa chini ya mwamvuli wa kusimamia na kuhakikisha Amani,Utii wa Sheria,Usalama wa Raia na Mali.

Kikao hicho kimefanyika Makao Makuu ya wizara,Mtumba jijini Dodoma.

Serikali Yabainisha Maeneo ya Miradi ya Umeme wa Upepo na Jua, Kishapu kuzalisha MW 150

Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba amesema Serikali imekwishabainisha na kufanya utafiti wa maeneo mbalimbali yanayofaa kuendelezw...