Monday, July 27, 2026

WAZIRI NDEJEMBI AWASILI SHINYANGA KUSHUHUDIA MRADI MKUBWA WA UMEME WA JUA WA MEGAWATI 100





Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi (Mb.), leo Julai 27, 2026, amewasili mkoani Shinyanga kwa ziara ya kikazi, ambapo amepokelewa na Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Mhe. Mboni Mhita, tayari kwa shughuli muhimu ya uzinduzi wa hatua mpya ya maendeleo katika sekta ya nishati nchini.

Katika ziara hiyo, Waziri Ndejembi ataongoza viongozi na wananchi wa Mkoa wa Shinyanga kushuhudia utiaji saini wa utekelezaji wa Awamu ya Pili ya mradi wa ujenzi wa Kituo cha Kuzalisha Umeme wa Jua chenye uwezo wa Megawati 100, kitakachojengwa katika eneo la Ngunga, wilayani Kishapu.

Mradi huo unatarajiwa kuongeza upatikanaji wa umeme wa uhakika, kuimarisha matumizi ya nishati jadidifu na kuendelea kuiwezesha Tanzania kufikia malengo yake ya maendeleo kupitia uwekezaji katika vyanzo safi vya nishati.

Katika ziara hiyo, Waziri ameambatana na Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati anayeshughulikia Umeme na Nishati Jadidifu, Mhandisi Felchesmi Mramba, pamoja na Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, Mhe. Subira Mgalu (Mb.), na Makamu Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mhe. Simon Songe Lusengekile, wakionesha dhamira ya pamoja ya Serikali katika kusimamia utekelezaji wa miradi ya kimkakati ya nishati kwa maendeleo ya Taifa.

Thursday, July 23, 2026

DKT. ABBASI AKAGUA MIRADI YA UTALII PORI LA AKIBA LA PANDE, ATOA MAAGIZO YA KUKAMILIKA KABLA YA AFCON 2027







Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Dkt. Hassan Abbasi, leo Julai 23, 2026, ametembelea Pori la Akiba la Pande jijini Dar es Salaam na kukagua maendeleo ya miradi ya kuboresha miundombinu na huduma za utalii inayotekelezwa katika eneo hilo.

Miradi inayotekelezwa ni pamoja na ujenzi wa bwawa la kuogelea (swimming pool), bwawa la watoto (Kids Playing Grounds), uwanja mdogo wa mpira wa miguu na uwanja wa beach volleyball, ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya kupokea wageni na mashabiki wa AFCON 2027, ambayo Tanzania itaandaa kwa ushirikiano na Kenya na Uganda.

Dkt. Abbasi amesisitiza miradi hiyo ikamilike kwa wakati na kwa viwango vinavyotarajiwa ili kuhakikisha wageni watakaofika nchini wanapata fursa ya kutembelea na kufurahia vivutio vya utalii vilivyopo Pori la Akiba la Pande.

Pori la Akiba la Pande linapatikana takribani kilomita 45 kutoka katikati ya Jiji la Dar es Salaam na linaendelea kuimarishwa kuwa moja ya vivutio muhimu vya utalii wa asili nchini.

Wednesday, July 22, 2026

MIAKA 99 YA JESHI LA CHINA IWE CHACHU CHA KUIMARISHA USHIRIKIANO WA ULINZI NA TANZANIA- DKT RHIMO NYANSAHO






Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Dkt. Rhimo Nyansaho (Mb), amesisitiza umuhimu wa kuendeleza ushirikiano kati ya Tanzania na China katika diplomasia ya ulinzi ili kuimarisha usalama, maendeleo na uchumi endelevu wa mataifa hayo. Dkt. Nyansaho amesema hayo tarehe 21 Julai, 2026, wakati wa maadhimisho ya miaka 99 ya kuanzishwa kwa Jeshi la Ukombozi la Watu wa China (PLA), yaliyoandaliwa na Balozi wa China nchini, Mhe. Chen Mingjian.

Katika hotuba yake kwenye maadhimisho hayo, Waziri wa Ulinzi na JKT ametoa pongezi kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu, Dkt. Samia Suluhu Hassan na Rais wa China, Xi Jinping, kwa kuendeleza urafiki wa kihistoria ulioasisiwa na Mwalimu Julius Kambarage Nyerere na Mao Zedong, hususan katika sekta ya ulinzi. 

Kwa upande wake, Balozi Chen Mingjian aliahidi kuwa China itaendelea kuimarisha ushirikiano wake wa kihistoria na Tanzania katika masuala ya ulinzi, ikiwemo mafunzo ya kijeshi.

Tuesday, July 21, 2026

WACHIMBAJI WADOGO WAISHUKURU SERIKALI KWA USAMBAZAJI WA UMEME MIGODINI







*Nyang’hwale, Geita*

Wachimbaji wadogo wa madini wilayani Nyang'hwale, mkoani Geita, wameishukuru Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kuendelea kuwekeza katika upatikanaji wa nishati ya umeme kwenye maeneo ya migodi, hatua inayopunguza gharama za uzalishaji na kuongeza tija katika shughuli za uchimbaji.

Shukrani hizo zimetolewa wakati Waziri wa Madini, Mhe. Anthony Mavunde, alipozindua mradi wa kuzalisha nishati ya umeme wenye uwezo wa KVA 500 kwenye Mgodi wa wachimbaji wadogo katika eneo la Igalula, wilayani Nyang'hwale. Mradi huo umetekelezwa kwa gharama ya zaidi ya Shilingi milioni 426 na ni sehemu ya juhudi za Serikali za kuboresha miundombinu ya nishati katika maeneo ya uchimbaji wa madini.

Akizungumza katika uzinduzi huo, Mhe. Mavunde amesema Serikali imeendelea kutekeleza kwa vitendo dhamira ya kuboresha mazingira ya uwekezaji na uzalishaji katika sekta ya madini kwa kusambaza umeme kwenye migodi ya wachimbaji wadogo na wa kati.

Amesema Serikali tayari imetumia zaidi ya Shilingi bilioni 7 kusambaza umeme katika maeneo mbalimbali ya migodi nchini, hatua iliyowezesha wachimbaji kupunguza utegemezi wa mitambo inayotumia mafuta na hivyo kushusha gharama za uzalishaji huku ikiongeza ufanisi wa shughuli za uchimbaji.

Katika kuendelea na ziara yake, Waziri Mavunde amekagua mradi wa maji safi na salama unaotekelezwa katika Kijiji cha Kakola, ambao unatarajiwa kuwanufaisha zaidi ya wananchi 24,801

Amesema mradi huo unatekeleza maelekezo ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuhakikisha wananchi, hususan wanawake, wanaondokana na adha ya kutembea umbali mrefu kutafuta maji.

"Ahadi ya Mheshimiwa Rais ya kumtua mama ndoo kichwani inaendelea kutekelezwa kwa vitendo kupitia miradi ya maji kama huu wa Kakola ambao utaboresha afya, ustawi na shughuli za kiuchumi za wananchi,"  amesema.

Katika sekta ya elimu, Waziri Mavunde amezindua Shule ya Msingi Imara Baruti iliyojengwa ili kuondoa changamoto ya wanafunzi kutembea umbali wa takribani kilomita nne kwenda kusoma katika Shule ya Msingi Shabaka.

Amesema ujenzi wa shule hiyo unatekeleza Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), inayosisitiza ujenzi wa shule karibu na makazi ya wananchi ili watoto wapate elimu katika mazingira bora.

"Serikali ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan inaendelea kuthibitisha kuwa ahadi zinazotolewa kwa wananchi si maneno ya kampeni pekee, bali ni mipango inayotekelezwa kwa vitendo kwa manufaa ya Watanzania," amesema.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Geita, Martin Shigella, amempongeza Waziri Mavunde kwa kufanya ziara ya kukagua na kuzindua miradi ya maendeleo mkoani humo, akisema hatua hiyo imeongeza kasi ya utekelezaji wa miradi na kuimarisha ufuatiliaji wa huduma zinazowagusa wananchi moja kwa moja.

Shigella amebainisha kuwa uwekezaji unaoendelea katika sekta za madini, elimu, maji na nishati unaendelea kuifanya Geita kuwa kitovu muhimu cha uzalishaji wa madini na maendeleo ya kijamii nchini.

WAZIRI NDEJEMBI AMTEMBELEA NA KUMJULIA HALI KAPTENI MSTAAFU GEORGE MKUCHIKA

 

Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi amemtembelea na kumjulia hali Kapteni Mstaafu George Huruma Mkuchika, aliyewahi kushika nafasi mbalimbali za uongozi Serikalini, ikiwemo Uwaziri katika wizara tofauti na Ubunge wa Jimbo la Newala Mjini, leo tarehe 21 Julai 2026 nyumbani kwake wilayani kijiji cha Nambunga Newala, mkoani Mtwara.



Newala, Mtwara | 21 Julai 2026

Waziri wa Nishati, Mheshimiwa Deogratius Ndejembi, leo tarehe 21 Julai 2026 amemtembelea na kumjulia hali Kapteni Mstaafu George Huruma Mkuchika nyumbani kwake katika Kijiji cha Nambunga, Wilaya ya Newala, mkoani Mtwara.

Katika ziara hiyo ya heshima na faraja, Waziri Ndejembi alipata fursa ya kuzungumza na Kapteni Mstaafu Mkuchika kuhusu hali yake ya afya, huku akimtakia afya njema, nguvu na maisha marefu.

Kapteni Mstaafu George Huruma Mkuchika ni mmoja wa viongozi waliotoa mchango mkubwa katika utumishi wa umma na maendeleo ya Taifa. Katika kipindi chake cha utumishi, aliwahi kushika nafasi mbalimbali za juu Serikalini ikiwemo Uwaziri katika wizara tofauti, pamoja na kulitumikia Jimbo la Newala Mjini kama Mbunge kwa vipindi kadhaa.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Waziri Ndejembi alieleza kuwa Serikali inaendelea kuthamini mchango wa viongozi wastaafu walioweka msingi imara wa maendeleo ya nchi kupitia utumishi wao wa kujituma na uzalendo. Alisisitiza kuwa kuwatembelea na kuwajulia hali viongozi hao ni sehemu ya kutambua na kuheshimu mchango wao kwa Taifa.

Kwa upande wake, Kapteni Mstaafu Mkuchika alimshukuru Waziri Ndejembi kwa kutenga muda wa kumtembelea na kumjulia hali, akieleza kuwa hatua hiyo inaonesha mshikamano, utu na kuthamini viongozi waliolitumikia Taifa kwa uaminifu.

Ziara hiyo imeakisi utamaduni wa viongozi kuendeleza mshikamano, upendo na kuthaminiana, huku ikitoa ujumbe kwamba mchango wa viongozi wastaafu katika ujenzi wa Taifa unaendelea kutambuliwa na kuheshimiwa.

Monday, July 20, 2026

MIRADI YA UCHUKUZI KUIFANYA KIGOMA KUWA KITOVU CHA BIASHARA AFRIKA MASHARIKI NA KATI - PROF. MBARAWA








Waziri wa Uchukuzi, Profesa Makame Mbarawa amesema Serikali ya Awamu ya Sita inaendelea kutekeleza uwekezaji mkubwa katika sekta ya uchukuzi unaolenga kuifanya Kigoma kuwa kitovu cha usafirishaji na biashara kinachounganisha Tanzania na nchi za Afrika Mashariki na Kati.

Profesa Mbarawa amesema hayo leo Jumatatu Julai 20, 2026 katika hafla iliyohudhuriwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, wakati wa uzinduzi wa meli nne za mizigo, uwekaji wa jiwe la msingi la ujenzi wa gati la abiria na mizigo Bandari ya Kigoma pamoja na uzinduzi wa ujenzi wa Reli ya Kisasa (SGR) kipande cha Tabora–Kigoma.

Amesema chini ya uongozi wa Rais Samia, Serikali imewekeza kwa kiwango kikubwa katika reli ya kisasa, bandari, viwanja vya ndege na usafiri wa majini kwa lengo la kuunganisha mikoa yote ya Tanzania pamoja na nchi jirani kupitia mfumo jumuishi wa uchukuzi.

Kwa mujibu wa Profesa Mbarawa, meli nne mpya za mizigo zitaongeza usalama wa usafirishaji katika Ziwa Tanganyika, kupunguza gharama za usafirishaji wa mizigo, kukuza biashara kati ya Tanzania, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo na Burundi, pamoja na kufungua fursa mpya za ajira na uwekezaji.

Aidha, amesema maboresho yanayoendelea Bandari ya Kigoma pamoja na ujenzi wa Reli ya Kisasa kutoka Tabora hadi Kigoma yataongeza ufanisi wa usafirishaji wa abiria na mizigo, huku yakiiunganisha Bandari ya Dar es Salaam na masoko ya ukanda wa Afrika Mashariki na Kati.

Profesa Mbarawa pia amesema Serikali inaendelea na maboresho ya uwanja wa ndege wa Kigoma kwa gharama ya Sh. bilioni 51.4, yanayojumuisha ujenzi wa jengo jipya la abiria, mnara wa kuongozea ndege, njia za ndege, taa za kuongozea ndege na miundombinu mingine muhimu. 

Ameongeza kuwa miradi hiyo inaonesha dhamira ya Serikali ya kujenga mfumo wa uchukuzi unaounganisha reli, bandari na usafiri wa anga ili kuharakisha maendeleo ya uchumi wa Taifa.

Tuesday, July 14, 2026

MMUYA: WANANCHI WANUFAIKE NA UWEKEZAJI WA NHC KUPITIA NYUMBA ZA GHARAMA NAFUU










Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Mhe. Kaspar Mmuya, amekagua maendeleo ya ujenzi wa mradi wa maghala unaotekelezwa na Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) katika Mtaa wa Viwandani, Kata ya Railway, Halmashauri ya Manispaa ya Mtwara-Mikindani.

Mhe. Mmuya amefanya ukaguzi huo Julai 13, 2026, ikiwa ni sehemu ya ziara yake ya kikazi ya siku mbili mkoani Mtwara yenye lengo la kukagua utekelezaji wa miradi iliyo chini ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi.

Akipokea taarifa ya mradi huo, Mhe. Mmuya ameelezwa kuwa ujenzi wa maghala hayo unagharimu shilingi bilioni 4.1, ambapo hadi sasa shilingi bilioni 2.6 zimetumika. Mradi huo unatarajiwa kukamilika Septemba 2026.

Katika ukaguzi huo, Mhe. Mmuya amelishauri Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) kuendelea kubuni na kuwekeza katika miradi inayogusa maisha ya wananchi moja kwa moja, hususan ujenzi wa nyumba za gharama nafuu, ili kusaidia kukabiliana na changamoto ya upungufu wa makazi nchini.

Aidha, amepongeza Shirika hilo kwa kuwekeza katika ujenzi wa maghala katika eneo lenye shughuli kubwa za kiuchumi, akibainisha kuwa uwepo wa Bandari ya Mtwara pamoja na uzalishaji wa mazao ya biashara, hususan korosho, unafanya mradi huo kuwa na umuhimu mkubwa katika kuchochea biashara na maendeleo ya uchumi wa mkoa huo.

Mradi huo unatarajiwa kuongeza uwezo wa kuhifadhi bidhaa mbalimbali, ikiwemo mazao ya kimkakati kama korosho, hatua itakayochangia kuongeza thamani ya mazao, kuboresha huduma za uhifadhi na kuimarisha shughuli za biashara kwa wakazi wa Mkoa wa Mtwara na maeneo ya jirani.

WAZIRI NDEJEMBI AWASILI SHINYANGA KUSHUHUDIA MRADI MKUBWA WA UMEME WA JUA WA MEGAWATI 100

Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi (Mb.) , leo Julai 27, 2026 , amewasili mkoani Shinyanga kwa ziara ya kikazi, ambapo amepokelewa ...