Thursday, July 30, 2026

SERIKALI NA WAWEKEZAJI & WATOA HUDUMA MIGODINI WAJADILI CHANGAMOTO NA MAFANIKIO KWENYE SEKTA YA MADINI





▪️Rais Samia apongezwa kwa mazingira rafiki ya uwekezaji

▪️ Wadau wapongeza hatua za serikali za kutatua changamoto

▪️Waziri Mavunde awataka Watanzania kuanza ujenzi wa viwanda vya bidhaa za migodini

▪️ Kampuni ya MANTRA yanuia

kuiweka Tanzania kwenye kumi bora ya wazalishaji wa Uranium Duniani

Dar es salaam

Waziri wa Madini, Mhe. Anthony Mavunde, amesema Serikali itaendelea kushirikiana na wadau wa sekta ya madini kupitia majukwaa ya majadiliano kwa lengo la kujenga sekta yenye ushindani, inayovutia uwekezaji na kutoa mchango mkubwa katika ukuaji wa uchumi wa Taifa.

Mhe. Mavunde ameyasema hayo katika kikao cha Mining Breakfast Briefing (MBB), kilichoandaliwa kwa ushirikiano wa Chemba ya Migodi Tanzania (TCM) na Wizara ya Madini, ambapo ametoa wito kwa wadau kuendelea kutumia majukwaa hayo kujadili fursa na changamoto zinazohusu sekta ya madini.

Amewashukuru viongozi na wanachama wa Chemba ya Migodi Tanzania kwa kuendelea kutoa nafasi ya Serikali na wadau kukutana na kujadiliana kuhusu masuala mbalimbali ya sekta hiyo, huku akilipongeza Mantra Tanzania Limited kwa kudhamini kikao hicho.

Amesema ushiriki wa wadau katika majukwaa hayo unaonesha dhamira ya pamoja ya kujenga sekta ya madini yenye ushindani, inayovutia mitaji na teknolojia, pamoja na kuhakikisha rasilimali za madini zinatumika kikamilifu kuchochea maendeleo ya kiuchumi na kijamii.

“Serikali inathamini utaratibu huu wa kukutana na wadau wa sekta ya madini kupitia Mining Breakfast Briefing, kwa kuwa unatoa fursa ya kufanya mazungumzo yenye tija, kujenga uelewa wa pamoja, kupokea changamoto zinazojitokeza na kutafuta suluhisho kwa pamoja,” amesema.

Amesema Serikali itaendelea kushirikiana na wadau wa sekta hiyo katika kutatua changamoto zinazojitokeza na kuboresha mazingira ya uwekezaji ili kuongeza uzalishaji, ajira, mapato ya Serikali na kutumia fursa hiyo kuwataka watoa huduma migodini kuchangamkia fursa ya ujenzi wa viwanda vya kuzalisha bidhaa za migodini.

“Ni vyema kuendelea kukutana mara kwa mara kupitia jukwaa hili muhimu, kwa sababu linatupa nafasi ya kusikilizana, kujadiliana na kutafuta suluhisho la changamoto zinazotukabili kwa pamoja,” amesema.

Naye, Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini, Eng. Yahya Samamba, amewashukuru wadau wa sekta ya madini kwa kushiriki katika kikao hicho, akiwataka kuongeza ushirikiano na mshikamano katika kukuza sekta hiyo.

Amesema ushirikiano kati ya Serikali na sekta binafsi ni muhimu katika kutatua changamoto, kuchochea uwekezaji na kuhakikisha fursa zinazotokana na rasilimali za madini zinatumika kwa manufaa mapana ya Taifa.

Amesisitiza kuwa mawasiliano ya mara kwa mara kati ya Serikali na wadau yataendelea kuwa nyenzo muhimu katika kubaini changamoto mapema na kuzitafutia ufumbuzi wa pamoja.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Chemba ya Migodi Tanzania, Mhandisi Philbert Rweyemamu, amemshukuru Waziri Mavunde kwa kuendelea kudumisha mahusiano mazuri na wadau wa sekta ya madini.

Amepongeza utaratibu wa Serikali kukutana mara kwa mara na wadau kupitia Mining Breakfast Briefing, akisema majukwaa hayo ni muhimu katika kujenga mawasiliano ya karibu, kubadilishana uzoefu na kujadili changamoto pamoja na fursa zilizopo katika sekta hiyo.

Amesema Chemba ya Migodi Tanzania itaendelea kushirikiana na Serikali chini ya uongozi imara wa Mh. Rais Dkt. Samia S. Hassan katika kuhakikisha sekta ya madini inaendelea kuimarika, kuvutia uwekezaji na kuongeza mchango wake katika maendeleo ya uchumi wa Tanzania.

Akizungumzia maendeleo ya mradi wa Uranium, Meneja wa Uendelevu wa Mantra Tanzania Limited, Majani Wambura, amesema mradi huo umebaini uwepo wa hifadhi ya takribani tani 58,500 za Uranium, huku uzalishaji ukitarajiwa kufikia tani 3,000 kwa mwaka.

Amesema mradi huo unatarajiwa kutoa ajira kwa zaidi ya wafanyakazi 4,000 baada ya kuanza uzalishaji, hatua itakayochochea shughuli za kiuchumi na kuongeza fursa kwa Watanzania.

Kwa mujibu wa Wambura, mradi huo unatarajiwa kuanza uzalishaji mwaka 2029  na kuwa na maisha ya zaidi ya miaka 20, huku utafiti ukiendelea ili kubaini uwepo wa rasilimali zaidi katika maeneo yanayohusishwa na mradi huo ambapo hatua zote hizo zitaifanya Tanzania kuwa miongoni mwa wazalishaji wakubwa 10 wa Uraniaum Duniani.

Ameeleza kuwa Uranium ni rasilimali yenye matumizi mbalimbali, ikiwemo katika uzalishaji wa nishati ya umeme na sekta ya afya, hususan matumizi ya mionzi katika uchunguzi na matibabu.

Akifunga jukwaa hilo, Naibu Waziri wa Madini, Dkt. Steven Kiruswa, amesema Serikali na wadau wa sekta ya madini wanapaswa kuendelea kukutana mara kwa mara kupitia Mining Breakfast Briefing (MBB) ili kujadili na kutatua changamoto zinazojitokeza katika sekta hiyo.

Amesema mikutano ya mara kwa mara itasaidia kujenga mawasiliano na uelewa wa pamoja kati ya Serikali na wadau, kujadili changamoto na fursa zilizopo, pamoja na kuweka mazingira bora zaidi ya uwekezaji katika sekta ya madini.

Wednesday, July 29, 2026

WANANCHI WALIPONGEZA JESHI LA POLISI KATAVI KWA KUFANYA USAFI MAENEO MBALIMBALI.

Wananchi wa eneo la soko kuu la Manispaa ya Mpanda mjini, Mkoani Katavi wamelipongeza Jeshi la Polisi kwa kuendesha zoezi la usafi lililofanyika sokoni hapo, ambapo wamesema hatua hiyo imechangia kuboresha mazingira ya biashara na afya ya jamii kwa ujumla.

Zoezi hilo limefanyika Julai 29, 2026 likiongozwa na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Katavi Kamishna msaidizi Mwandamizi (SACP) Kaster Ngonyani ambapo, amesema kuwa zoezi hilo ni endelevu lenye lengo la kuhamasisha wananchi kutunza mazingira huku akiwataka wafanyabiashara na wananchi kuendelea kushirikiana katika kudumisha usafi wa soko na maeneo mengine yanayowazunguka.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa mtaa wa Kashaulili Ndugu Johari Korongo amelipongeza Jeshi la Polisi Mkoa wa Katavi kwa kuonyesha ushirikiano mzuri na wananchi kwa kujitolea na ametoa wito kwa taasisi nyingine kuiga mfano huo kwa kushiriki shughuli mbalimbali za maendeleo na huduma kwa jamii.



Tuesday, July 28, 2026

Rais Samia Akutana na Balozi wa China Nchini Tanzania



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, amekutana na kufanya mazungumzo na Balozi wa Jamhuri ya Watu wa China nchini Tanzania, Mhe. Chen Mingjian, katika Ikulu ya Tunguu, Zanzibar, tarehe 28 Julai 2026.

Mazungumzo hayo yamejikita katika kuendelea kuimarisha uhusiano wa muda mrefu wa kidiplomasia na ushirikiano wa kimkakati kati ya Tanzania na China, hususan katika maeneo ya biashara, uwekezaji, maendeleo ya miundombinu na sekta nyingine za maendeleo ya kijamii na kiuchumi.

Tanzania na China zimeendelea kushirikiana kwa karibu kwa miongo kadhaa, ambapo ushirikiano huo umechangia utekelezaji wa miradi mbalimbali yenye manufaa kwa wananchi na kukuza mahusiano ya kirafiki kati ya mataifa hayo mawili.

Mkutano huo unaakisi dhamira ya pande zote mbili ya kuendeleza ushirikiano unaojengwa juu ya kuheshimiana, maslahi ya pamoja na maendeleo endelevu kwa manufaa ya wananchi wa Tanzania na China.

VIONGOZI WATEULE WAAPA KIAPO CHA UADILIFU MBELE YA RAIS SAMIA







Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, amewaapisha viongozi mbalimbali walioteuliwa kula Kiapo cha Uadilifu kwa Viongozi wa Umma katika hafla iliyofanyika Ikulu ya Tunguu, Zanzibar, tarehe 27 Julai, 2026.

Rais Samia Suluhu Hassan, aliwaapisha Dkt. Latifa Mohammed Khamis kuwa Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Makamu wa Rais – Muungano na Ndugu Prisca Burton Lwangili kuwa Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora.

Hafla hiyo ya uapisho imefanyika Ikulu ya Tunguu, Zanzibar, tarehe 27 Julai, 2026, ambapo viongozi hao wameapishwa rasmi kuanza kutekeleza majukumu yao katika nafasi walizoteuliwa.

Kiapo hicho ni sehemu ya utekelezaji wa matakwa ya sheria na utaratibu wa utumishi wa umma, kikilenga kuimarisha uwajibikaji, uadilifu, uzalendo na uzingatiaji wa maadili katika utekelezaji wa majukumu ya viongozi wa umma.

Hafla hiyo imeashiria mwanzo rasmi wa viongozi hao kuanza kutekeleza majukumu yao kwa kuzingatia misingi ya uongozi bora na kutoa huduma zenye tija kwa wananchi.

Monday, July 27, 2026

WAZIRI NDEJEMBI AWASILI SHINYANGA KUSHUHUDIA MRADI MKUBWA WA UMEME WA JUA WA MEGAWATI 100





Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi (Mb.), leo Julai 27, 2026, amewasili mkoani Shinyanga kwa ziara ya kikazi, ambapo amepokelewa na Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Mhe. Mboni Mhita, tayari kwa shughuli muhimu ya uzinduzi wa hatua mpya ya maendeleo katika sekta ya nishati nchini.

Katika ziara hiyo, Waziri Ndejembi ataongoza viongozi na wananchi wa Mkoa wa Shinyanga kushuhudia utiaji saini wa utekelezaji wa Awamu ya Pili ya mradi wa ujenzi wa Kituo cha Kuzalisha Umeme wa Jua chenye uwezo wa Megawati 100, kitakachojengwa katika eneo la Ngunga, wilayani Kishapu.

Mradi huo unatarajiwa kuongeza upatikanaji wa umeme wa uhakika, kuimarisha matumizi ya nishati jadidifu na kuendelea kuiwezesha Tanzania kufikia malengo yake ya maendeleo kupitia uwekezaji katika vyanzo safi vya nishati.

Katika ziara hiyo, Waziri ameambatana na Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati anayeshughulikia Umeme na Nishati Jadidifu, Mhandisi Felchesmi Mramba, pamoja na Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, Mhe. Subira Mgalu (Mb.), na Makamu Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mhe. Simon Songe Lusengekile, wakionesha dhamira ya pamoja ya Serikali katika kusimamia utekelezaji wa miradi ya kimkakati ya nishati kwa maendeleo ya Taifa.

Thursday, July 23, 2026

DKT. ABBASI AKAGUA MIRADI YA UTALII PORI LA AKIBA LA PANDE, ATOA MAAGIZO YA KUKAMILIKA KABLA YA AFCON 2027







Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Dkt. Hassan Abbasi, leo Julai 23, 2026, ametembelea Pori la Akiba la Pande jijini Dar es Salaam na kukagua maendeleo ya miradi ya kuboresha miundombinu na huduma za utalii inayotekelezwa katika eneo hilo.

Miradi inayotekelezwa ni pamoja na ujenzi wa bwawa la kuogelea (swimming pool), bwawa la watoto (Kids Playing Grounds), uwanja mdogo wa mpira wa miguu na uwanja wa beach volleyball, ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya kupokea wageni na mashabiki wa AFCON 2027, ambayo Tanzania itaandaa kwa ushirikiano na Kenya na Uganda.

Dkt. Abbasi amesisitiza miradi hiyo ikamilike kwa wakati na kwa viwango vinavyotarajiwa ili kuhakikisha wageni watakaofika nchini wanapata fursa ya kutembelea na kufurahia vivutio vya utalii vilivyopo Pori la Akiba la Pande.

Pori la Akiba la Pande linapatikana takribani kilomita 45 kutoka katikati ya Jiji la Dar es Salaam na linaendelea kuimarishwa kuwa moja ya vivutio muhimu vya utalii wa asili nchini.

Wednesday, July 22, 2026

MIAKA 99 YA JESHI LA CHINA IWE CHACHU CHA KUIMARISHA USHIRIKIANO WA ULINZI NA TANZANIA- DKT RHIMO NYANSAHO






Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Dkt. Rhimo Nyansaho (Mb), amesisitiza umuhimu wa kuendeleza ushirikiano kati ya Tanzania na China katika diplomasia ya ulinzi ili kuimarisha usalama, maendeleo na uchumi endelevu wa mataifa hayo. Dkt. Nyansaho amesema hayo tarehe 21 Julai, 2026, wakati wa maadhimisho ya miaka 99 ya kuanzishwa kwa Jeshi la Ukombozi la Watu wa China (PLA), yaliyoandaliwa na Balozi wa China nchini, Mhe. Chen Mingjian.

Katika hotuba yake kwenye maadhimisho hayo, Waziri wa Ulinzi na JKT ametoa pongezi kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu, Dkt. Samia Suluhu Hassan na Rais wa China, Xi Jinping, kwa kuendeleza urafiki wa kihistoria ulioasisiwa na Mwalimu Julius Kambarage Nyerere na Mao Zedong, hususan katika sekta ya ulinzi. 

Kwa upande wake, Balozi Chen Mingjian aliahidi kuwa China itaendelea kuimarisha ushirikiano wake wa kihistoria na Tanzania katika masuala ya ulinzi, ikiwemo mafunzo ya kijeshi.

SERIKALI NA WAWEKEZAJI & WATOA HUDUMA MIGODINI WAJADILI CHANGAMOTO NA MAFANIKIO KWENYE SEKTA YA MADINI

▪️Rais Samia apongezwa kwa mazingira rafiki ya uwekezaji ▪️ Wadau wapongeza hatua za serikali za kutatua changamoto ▪️Waziri Mavunde awataka...