Sunday, May 03, 2026

NHC YATOA ELIMU YA HATI PACHA, YASISITIZA UMOJA WA WAMILIKI SAMIA HOUSING SCHEME KAWE




 Samia Housing Scheme Kawe: nyumba 560, familia tofauti zikiunganishwa na mtindo mmoja wa maisha ya 
kisasa—ushirikiano, ustaarabu na “modern urban living” ya Tanzania ya leo.  

20260502_104409.jpg.jpeg
Menejimenti ya NHC ikifuatilia kwa kina lilichokuwa kikiendelea katika mkutano huo muhimu katika maendeleo ya sekta 
ya nyumba ikiwa ni estate ya 11 kutekeleza sheria ya hati pacha nchini.
20260502_105112.jpg.jpeg
Mhandisi Grace Msita ambaye ndiye Meneja wa Miradi ya NHC akiwahakikishai wamiliki hao ubora na uimara 
wa nyumba na weledi uliotumika.
20260502_105510.jpg.jpegMwakalukwa.jpeg
Mzee George Mwakalukwa ambaye ni mmoja wa wamiliki wa nyumba hizo akitia saini kitabu cha wageni 
kabla ya mkutano kuanza.
WhatsApp Image 2026-05-02 at 10.17.41.jpeg
Mmiliki Mwingine akitia saini kitabu cha wageni wakati akiwasili kwenye mkutano huo
 muhimu.
WhatsApp Image 2026-05-03 at 15.23.11(2).jpeg

Afisa Sheria Mwandamizi wa NHC, Scholastica Kilagane, alitoa elimu ya kina

 kuhusu dhana ya hati pacha (Unit title)

Uongozi wa Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) umefanya kikao pamoja na wateja 
wake wa nyumba za makazi za Samia Housing Scheme jana, tarehe 2/5/2026, 
katika eneo la Kawe jijini Dar es Salaam, kwa lengo la kuwajengea uelewa wa 
kina kuhusu umiliki wa nyumba za kisasa, hususan mfumo wa hati pacha pamoja 
na kuimarisha misingi ya usimamizi wa pamoja wa makazi hayo.

Akizungumza katika kikao hicho, kilichohudhuriwa na wamiliki wa nyumba hizo
 560 zilizopo Kawe Tanganyika Packers Dar es Salaam, Afisa Sheria Muandamizi 
wa NHC, Scholastica Kilagane, alitoa elimu ya kina kuhusu dhana ya hati pacha
 (Unit title), akieleza kuwa mfumo huo unampa mmiliki haki ya kumiliki sehemu
 yake binafsi ya nyumba huku akishiriki umiliki wa maeneo ya pamoja kama vile
 lifti, korido, ngazi, maeneo ya wazi na miundombinu mingine ya huduma.

Alisisitiza kuwa uelewa sahihi wa mfumo huo ni muhimu ili kuepusha migogoro ya 
kisheria na kuhakikisha matumizi bora ya mali hizo.

“Hati pacha inalenga kuweka uwazi katika umiliki wa mali na kugawanya wazi haki 
na wajibu wa kila mmiliki. Ni muhimu kwa kila mmiliki kuelewa kuwa pamoja na 
kumiliki nyumba yake, ana wajibu wa kushiriki kikamilifu katika kusimamia maeneo
 ya pamoja kwa mujibu wa sheria,” alieleza Kilagane.

Aidha, Kilagane alieleza umuhimu wa kuanzishwa kwa umoja wa wamiliki wa 
nyumba (Owners Association), akibainisha kuwa huo ndio chombo rasmi cha 
kisheria kitakachosimamia masuala yote ya pamoja ndani ya eneo hilo.

Alifafanua kuwa umoja huo utakuwa na viongozi watakaochaguliwa kwa mujibu 
wa taratibu za kisheria, ikiwemo Mwenyekiti, Katibu na Mweka Hazina, huku kila 
mmoja akiwa na majukumu mahsusi ya kuhakikisha uendeshaji 
mzuri na uwajibikaji.

Naye Injinia Grace Msita, Meneja Miradi wa Shirika la Nyumba la Taifa (NHC), 
akizungumza na wamiliki hao aliwahakikishia kuwa miundombinu yote ya Samia 
Housing Scheme imekamilika kwa viwango vya juu vya ubora na usalama, huku 
akisisitiza kuwa usimamizi madhubuti wa miradi hiyo wakati wa utekelezaji ni 
sehemu ya dhamira ya NHC ya kutoa makazi endelevu na yenye thamani kwa 
wananchi.

Alieleza kuwa NHC itaendelea kushirikiana na umoja wa wamiliki katika hatua 
zote za wakati huu wa kipindi cha uangalizi yaani DLP wa mradi huo ili 
kuhakikisha changamoto zinazojitokeza zinapatiwa ufumbuzi wa haraka 
na kwa weledi, na hivyo kulinda uwekezaji wa kila mmiliki pamoja na kuhakikisha 
mazingira ya kuishi yanabaki kuwa bora na ya kisasa.

Kwa upande wake, Meneja wa Milki wa NHC, France Bahangarwa, alisisitiza 
wajibu wa wamiliki katika kuhakikisha uendelevu wa huduma ndani ya Samia 
Housing Scheme. Alieleza kuwa ulipaji wa service charge ni sharti la kisheria 
lisiloweza kuepukika kwani ndilo linalowezesha uendeshaji wa huduma muhimu 
za pamoja.

“Huduma kama lifti, usafi wa mazingira, ulinzi, taa za maeneo ya pamoja na 
matengenezo ya miundombinu haviwezi kuendelea bila michango ya wamiliki. 
Hivyo, kila mmiliki ana wajibu wa kulipa service charge kwa wakati ili 
kuhakikisha mazingira haya yanaendelea kuwa salama na yenye hadhi,” alisema 
Bahangarwa.

Aliongeza kuwa pamoja na hilo, wamiliki wanapaswa kutekeleza majukumu yao
 mengine ya kisheria ikiwemo kulipa kodi ya ardhi na kushiriki katika maamuzi 
ya pamoja kupitia umoja wao. Pia alisisitiza umuhimu wa kuajiri kampuni ya 
usimamizi wa milki au mtaalamu binafsi ili kuhakikisha shughuli za kila siku 
za uendeshaji zinafanyika kwa weledi na kwa kuzingatia viwango vya kitaalamu.

“Usimamizi wa kitaalamu ni nguzo muhimu katika mafanikio ya miradi ya makazi
 ya aina hii. Ni vyema wamiliki wakachagua njia bora ya usimamizi 
itakayolinda thamani ya mali zao na kuboresha maisha yao kwa ujumla,” 
aliongeza Bahangarwa.

Kwa upande wao, wamiliki wa nyumba katika Samia Housing Scheme 
walieleza kuridhishwa na kikao hicho, wakitoa shukurani kwa Shirika la Nyumba
 la Taifa kwa kuwapatia elimu hiyo muhimu.

Mmoja wa wamiliki alieleza kuwa, “Tunashukuru sana NHC kwa kutuletea elimu
 hii. Imetusaidia kuelewa kwa undani haki na wajibu wetu kama wamiliki wa 
nyumba za mfumo huu wa kisasa. Sasa tunaona umuhimu wa kushirikiana na 
kuunda umoja imara kwa ajili ya maendeleo ya makazi yetu.”

Kwa ujumla, kikao hiki kimekuwa jukwaa muhimu la kuwawezesha wamiliki 
kwa maarifa sahihi ya kisheria na kiutendaji, hatua inayotarajiwa kuimarisha 
usimamizi wa pamoja, kuongeza thamani ya mali na kuhakikisha Samia Housing
 Scheme inakuwa mfano bora wa makazi ya kisasa yanayosimamiwa kwa ufanisi 
nchini.

Naye Meneja Mauzo na Masoko wa NHC, Deogratius Batakanwa alieleza kuwa 
Samia Housing Scheme ni zaidi ya makazi; ni uwekezaji wenye thamani unaohitaji
 uelewa sahihi wa kisheria na usimamizi wa pamoja ili kulinda na kukuza thamani 
yake kwa muda mrefu.

“Kupitia mfumo wa hati pacha, kila mmiliki anapata umiliki halali wa sehemu 
yake binafsi huku akishiriki umiliki wa maeneo ya pamoja. Huu ni mfumo wa 
kisasa unaolenga kuongeza uwazi, kulinda uwekezaji na kuhakikisha mazingira 
bora ya kuishi kwa wakazi wote,” alisema Batakanwa.

Alisisitiza kuwa uelewa wa mfumo huo unawawezesha wamiliki kufanya maamuzi 
sahihi kuhusu mali zao na kushiriki kikamilifu katika uendeshaji wa makazi yao kwa
 tija.

Katika kuimarisha usimamizi wa pamoja, Batakanwa alibainisha umuhimu wa 
kuunda umoja wa wamiliki wa nyumba (Owners Association) utakaosimamia 
masuala ya pamoja kwa weledi na uwazi. Alieleza kuwa uongozi wa umoja huo 
utachaguliwa kwa kufuata taratibu rasmi na utakuwa na jukumu la kuhakikisha 
huduma zote zinaendeshwa kwa ufanisi.

Katika hatua ya kuimarisha usimamizi wa pamoja, wamiliki wa Samia Housing 
Scheme wamechagua uongozi wa umoja wao ukiongozwa na Mwenyekiti Catherine
 Mrosso akisaidiwa na Makamu Mwenyekiti Eng. Juma Kiboko, huku nafasi ya 
Katibu ikishikiliwa na Grace Lemunge akisaidiwa na Katibu Msaidizi George 
Laurian, na Mweka Hazina akiwa Veronica Rukeha.

Wajumbe wa kamati hiyo ni Rehema Chonda, Ramadhani Mshana, Dkt. Petronila
 Ngiloi, Bi. Hadija Mwema, Isack Ngovi, Faith Kayombo, Robert Matapu, Jesca 
Macharia, Salma Juma, Dkt. Oreste Munishi na Grace Mwaihojo.

Kwa upande wao, wamiliki wa nyumba walitoa shukurani kwa NHC kwa 
kuandaa kikao hicho, wakieleza kuwa elimu waliyoipata imewasaidia kuelewa 
thamani halisi ya uwekezaji wao na namna bora ya kuilinda.

“Tunathamini jitihada za NHC kutuelimisha. Sasa tunaelewa kuwa mafanikio ya
 makazi haya yanategemea ushirikiano wetu na utekelezaji wa majukumu yetu 
ipasavyo,” walieleza baadhi ya wamiliki.

Kwa ujumla, kikao hiki kimeweka msingi thabiti wa kuifanya Samia Housing Scheme 
kuwa mfano wa makazi ya kisasa yanayosimamiwa kwa ufanisi, huku yakitoa 
thamani ya juu kwa wamiliki wake—ikiwa ni sehemu ya dhamira ya NHC ya 
kuendeleza makazi bora na uwekezaji salama kwa Watanzania.

RAIS DKT. SAMIA AFANYA MAZUNGUMZO NA RAIS KAGAME IKULU DAR ES SALAAM

 
 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza na Waandishi wa Habari kuhusu Ziara ya Kikazi ya Rais wa Jamhuri ya Rwanda Mhe. Paul Kagame, Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 03 Mei, 2026.





 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiongoza Ujumbe wa Tanzania kwenye mazungumzo na Ujumbe wa Rwanda uliongozwa na Rais wa Nchi hiyo Mhe. Paul Kagame, tarehe 03 Mei, 2026.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, ameongoza mazungumzo ya ngazi ya juu kati ya Tanzania na Rwanda yaliyofanyika Ikulu jijini Dar es Salaam tarehe 03 Mei 2026, akiwa mwenyeji wa Rais wa Jamhuri ya Rwanda, Mhe. Paul Kagame, katika ziara ya kikazi yenye lengo la kuimarisha zaidi uhusiano wa kidiplomasia na ushirikiano wa kiuchumi kati ya mataifa hayo mawili.

Mazungumzo hayo yalijikita katika maeneo muhimu ya ushirikiano ikiwemo biashara, uwekezaji, miundombinu ya kikanda, pamoja na kuimarisha amani na usalama katika ukanda wa Afrika Mashariki. Viongozi hao wawili walisisitiza umuhimu wa kuendeleza mshikamano wa kihistoria uliopo kati ya Tanzania na Rwanda kwa manufaa ya wananchi wa pande zote.

Baada ya mazungumzo hayo, Rais Samia pia alizungumza na waandishi wa habari ambapo alieleza kuwa ziara hiyo ni ishara ya kuimarika kwa mahusiano ya kidiplomasia na nia ya pamoja ya kuharakisha maendeleo ya kikanda kupitia ushirikiano wa karibu zaidi.

Kwa ujumla, ziara ya Rais Paul Kagame nchini Tanzania imeacha alama ya diplomasia yenye nguvu, ikithibitisha dhamira ya viongozi hao wawili kuendeleza ushirikiano wa kimkakati unaolenga ustawi wa wananchi wa Afrika Mashariki.

ZIARA YA RAIS PAUL KAGAME IKULU DAR ES SALAAM YAASHIRIA KUIMARIKA KWA USHIRIKIANO WA TANZANIA NA RWANDA

Rais wa Jamhuri ya Rwanda Mhe. Paul Kagame akisaini Kitabu cha Wageni mara baada ya kuwasili Ikulu Jijini Dar es Salaam kwa Ziara ya Kikazi, tarehe 03 Mei, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa na mgeni wake Rais wa Jamhuri ya Rwanda Mhe. Paul Kagame mara baada ya kuwasili Ikulu Jijini Dar es Salaam kwa Ziara ya Kikazi, tarehe 03 Mei, 2026.


Rais wa Jamhuri ya Rwanda, Mhe. Paul Kagame, amewasili Ikulu Jijini Dar es Salaam kwa ziara ya kikazi tarehe 03 Mei, 2026, na kupokelewa rasmi na mwenyeji wake, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan—hatua inayoashiria kuendelea kuimarika kwa uhusiano wa kidiplomasia na kiuchumi kati ya mataifa haya mawili ya Afrika Mashariki.

Mara baada ya kuwasili, Mhe. Kagame alisaini Kitabu cha Wageni Ikulu, ishara ya heshima na uthibitisho wa ziara yake rasmi nchini Tanzania. 

Tukio hilo linaakisi umuhimu wa ziara hii katika kukuza ushirikiano wa kimkakati kati ya Rwanda na Tanzania, hususan katika maeneo ya biashara, uwekezaji, miundombinu na maendeleo ya kikanda.

Katika picha nyingine, Rais Samia Suluhu Hassan anaonekana akiwa pamoja na mgeni wake Mhe. Paul Kagame mara baada ya kuwasili Ikulu—taswira inayoonyesha ukaribu wa kidiplomasia na dhamira ya pamoja ya viongozi hawa katika kusukuma mbele ajenda za maendeleo na ustawi wa wananchi wao.

Ziara hii ya kikazi inatarajiwa kufungua ukurasa mpya wa ushirikiano wa pande mbili, huku ikiimarisha nafasi ya nchi hizi katika kuchochea ukuaji wa uchumi na mshikamano wa kikanda ndani ya Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Tuesday, April 28, 2026

WAZIRI WA MAMBO YA NJE WA BELARUS AWASILI NCHINI KWA ZIARA YA KIKAZI

 








Waziri wa Mambo ya Nje wa Jamhuri ya Belarus, Mheshimiwa Maxim Ryzhenkov, amewasili nchini kwa ziara ya kikazi ya siku tatu kuanzia Aprili 28 hadi 30, 2026, kufuatia mwaliko wa Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo.

Mheshimiwa Ryzhenkov amewasili kupitia Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere jijini Dar es Salaam, ambapo alipokewa na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Ngwaru Maghembe, pamoja na Balozi wa Jamhuri ya Belarus nchini Mhe.Dzmitry Krasouski.

Katika ziara hiyo, Mheshimiwa Ryzhenkov anatarajiwa kufanya mazungumzo ya pande mbili na mwenyeji wake, Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo, Aprili 28, 2026, jijini Dar es Salaam. Aidha, atakutana na viongozi wengine wa Serikali kwa lengo la kuendeleza na kupanua ushirikiano kati ya nchi hizo mbili.

Ziara hiyo inalenga kuimarisha uhusiano wa kidiplomasia kati ya Tanzania na Belarus pamoja na kukuza ushirikiano wa kiuchumi katika maeneo yenye maslahi ya pamoja.

Monday, April 27, 2026

SEKTA YA MADINI YACHOCHEA UCHUMI: MAPATO YAVUKA MALENGO NA MAUZO

 

Na. Meleka Kulwa- Fullshangwe Blog, Dodoma 

Waziri wa Madini, Mhe. Anthony Mavunde, amesema kuwa Serikali inaendelea kuonesha dhamira ya dhati ya kuifanya sekta ya madini kuwa injini muhimu ya kukuza uchumi wa Taifa kwa kuwekeza zaidi katika mnyororo wa thamani wa madini mkakati na kuhamasisha uwekezaji katika uongezaji thamani.

Ameyabainisha hayo Aprili 27, 2026 Jijini Dodoma, wakati akiwasilisha  bajeti ya Wizara kwa mwaka wa fedha 2026/2027, amesema kuwa madini mkakati yakiwemo lithium, graphite, nickel, cobalt na rare earth elements yana nafasi kubwa katika maendeleo ya teknolojia za kisasa hususan nishati safi. Aidha amebainisha kuwa mwelekeo wa dunia kutumia teknolojia rafiki kwa mazingira unaongeza mahitaji na thamani ya madini hayo katika soko la kimataifa.

Pia ameongeza kuwa Serikali imejipanga kuimarisha uwekezaji katika utafutaji na uchimbaji wa madini hayo ili kuongeza uzalishaji pamoja na mapato ya Taifa. Amesema kuwa tafiti za masoko mapya zitafanyika ili kupanua wigo wa biashara huku taratibu za utoaji leseni zikirahisishwa kwa wawekezaji.

Amesema kuwa lengo kuu ni kuhakikisha Watanzania wananufaika moja kwa moja kupitia ajira, mapato na maendeleo ya viwanda vinavyotokana na rasilimali hizo.

Aidha amebainisha kuwa Serikali imeweka mkakati wa kuhamasisha ujenzi wa viwanda vya uchenjuaji, uyeyushaji na usafishaji wa madini ili kuongeza thamani kabla ya kusafirishwa nje ya nchi. Amesema hatua hiyo inalenga kupunguza usafirishaji wa madini ghafi na kuongeza mapato kupitia bidhaa zilizoboreshwa.

Pia ameongeza kuwa eneo la Buzwagi wilayani Kahama limetengwa kwa ajili ya uwekezaji wa viwanda vya kuongeza thamani madini, hatua inayotarajiwa kuvutia wawekezaji na kuongeza ajira kwa wananchi.

Aidha amebainisha kuwa Serikali inaendelea kushirikiana na wadau kuhakikisha viwanda vya usafishaji wa dhahabu vinapata ithibati ya kimataifa ili kuongeza ushindani wa bidhaa za Tanzania katika soko la dunia.

Amesema kuwa Tanzania inatarajia kuandaa mkutano wa saba wa kimataifa wa uwekezaji katika sekta ya madini utakaofanyika Dar es Salaam mwezi Novemba 2026, ambapo wadau mbalimbali watakutana kujadili fursa na changamoto za sekta hiyo.

Kwa upande wa utekelezaji wa bajeti ya mwaka 2025/2026, amesema kuwa Wizara imepiga hatua kubwa ikiwemo kuvuka malengo ya ukusanyaji wa mapato na kuimarisha usimamizi wa rasilimali madini.

Aidha amebainisha kuwa Bunge liliidhinisha shilingi bilioni 224.98 kwa ajili ya Wizara, ambapo kati ya hizo shilingi bilioni 100.38 zilitengwa kwa matumizi ya kawaida na shilingi bilioni 124.60 kwa miradi ya maendeleo. Amesema kuwa hadi Machi 2026, Wizara ilikuwa imepokea shilingi bilioni 82.90.

Pia ameongeza kuwa katika ukusanyaji wa maduhuli, Wizara ilipangiwa kukusanya shilingi trilioni 1.41 lakini hadi Machi 2026 tayari ilikuwa imekusanya shilingi trilioni 1.03, sawa na asilimia 114.94 ya lengo la kipindi husika.

Amesema kuwa mafanikio hayo yametokana na kuimarishwa kwa ukaguzi katika maeneo ya uchimbaji, masoko ya madini, vituo vya ununuzi pamoja na mipaka ya nchi ili kudhibiti upotevu wa mapato.

Aidha amebainisha kuwa thamani ya biashara ya madini imeongezeka na kufikia shilingi trilioni 4.90 katika kipindi cha Julai 2025 hadi Machi 2026 ikilinganishwa na shilingi trilioni 2.82 kwa kipindi kama hicho mwaka uliopita.

Pia ameongeza kuwa Serikali imeendelea kudhibiti utoroshaji wa madini ambapo madini yenye thamani ya shilingi bilioni 3.31 yalikamatwa katika matukio 55 na wahusika kuchukuliwa hatua za kisheria.

Amesema kuwa mapato ya fedha za kigeni yameongezeka ambapo mauzo ya madini nje ya nchi yalifikia dola milioni 5,401.9 mwaka 2025 kutoka dola milioni 4,119.9 mwaka 2024.

Aidha amebainisha kuwa mchango wa sekta ya madini katika Pato la Taifa umeongezeka kutoka asilimia 9.1 mwaka 2023 hadi asilimia 10.1 mwaka 2024 na kufikia wastani wa asilimia 11.9 katika robo tatu za mwaka 2025

Friday, April 24, 2026

🏗️ MASASI COMMERCIAL COMPLEX YAKABIDHIWA RASMI









Mradi wa Masasi Commercial Complex umekabidhiwa rasmi, ukiwa ni alama ya mafanikio ya utekelezaji wa miradi ya kisasa yenye kuzingatia ubora na thamani kwa jamii.

Akizungumza katika hafla hiyo, Meneja wa NHC Mkoa wa Lindi, Omari Malalamangi, aliipongeza timu ya ujenzi kwa kazi kubwa waliyoifanya licha ya changamoto ya maji wakati wa uchimbaji wa msingi. 

Alisisitiza kuwa kujituma kwao kumezaa matokeo bora—jengo lenye hadhi linalovutia na kupongezwa na wengi.

Mradi huu umeacha alama chanya kwa jamii, ukitoa ajira kwa wakazi wa Masasi na kunufaisha sekta mbalimbali zikiwemo huduma za maji, umeme, mama lishe pamoja na wauzaji wa vifaa vya ujenzi.

Kwa upande wake, Meneja Usimamizi wa Miradi NHC, Grace Musita, alieleza kuwa ujenzi umefuata taratibu zote za kitaalamu, huku vipimo vya vifaa kama nondo, kokoto na tofali vikifanyika katika maabara ya Mtwara. 

Alibainisha kuwa kila hatua ya ujenzi ilisimamiwa kwa ukaribu na wataalamu ili kuhakikisha ubora unazingatiwa kabla ya kuendelea na hatua inayofuata.

Aidha, mradi umefungua fursa kwa wafanyabiashara wa ndani, ambapo baadhi ya kazi kama uwekaji wa milango ya mbao na tiles zilifanywa na mafundi wazawa wa Masasi.

Musita alimshukuru Mkurugenzi Mkuu pamoja na Menejimenti ya NHC kwa ushirikiano uliowezesha kukamilika kwa mradi huu kwa mafanikio.

Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa Madaraka, Kata ya Jida, alieleza furaha yake akisema ujio wa jengo hili umeubadilisha mtaa huo na kuongeza uhai wa shughuli za kijamii na kiuchumi, huku ajira ndogo ndogo zilizotolewa zikichochea vijana wengi kujikwamua kiuchumi.

Hafla ya makabidhiano ilihitimishwa kwa kukata keki, kuashiria rasmi kuwa Masasi Commercial Complex ipo tayari kutumika.

#NHC #MasasiComplex #UjenziBora #MaendeleoYaJamii #Tanzania

Thursday, April 23, 2026

UJUMBE WA MAAFISA KUTOKA CHUO CHA ULINZI CHA TAIFA MISRI WATEMBELEA MAKUMBUSHO YA TAIFA TANZANIA









Leo, tarehe 23/04/2026 Makumbusho ya Taifa la Tanzania imepokea ugeni maalum kutoka Chuo cha Kijeshi Misri (Egypt War College) walioko katika ziara ya mafunzo.

Ujumbe huo uliongozwa na Meja Jenerali Mohamed Yehia Zakaria Hassan akiambatana na Brigedia Jenerali Islam Sayed Bakry El-Sayed, huku kwa upande wa mwenyeji wao kutoka Tanzania wakiongozwa na Brigedia Jeneral Kamanda Makanya Erassy kutoka JWTZ Tanzania.

Wageni hao walipokelewa na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Makumbusho ya Taifa la Tanzania, Bi. Pendo Gondwe, ambaye aliwakaribisha na kuwapatia maelezo kuhusu dhima ya taasisi hiyo ya Kimkakati katika kuhifadhi, kulinda na kuendeleza urithi wa historia na utamaduni wa Taifa.

Ujumbe huo uliokuwa na lengo la kujifunza ulipata fursa ya kutembelea na kujifunza historia ya Tanzania kupitia vivutio mbalimbali vilivyopo katika Makumbusho, ikiwemo mabaki ya kihistoria, tamaduni za jamii mbalimbali pamoja na hatua za maendeleo ya taifa. Wageni hao walionesha kuvutiwa na ubora wa maonesho na namna historia ya Tanzania inavyoendelea kuhifadhiwa na kuwasilishwa kwa ufanisi.

Akizungumza baada ya ziara hiyo, kiongozi wa ujumbe, Meja Jenerali Mohamed Yehia Zakaria Hassan, alieleza kufurahishwa kwake na kiwango cha maonesho hayo akisema, “ Maonesho ni bora sana na nimefurahishwa kuona mwendelezo wa historia ukiendelea kukua na kuendelezwa"* 

Ziara hiyo ni sehemu ya programu ya mafunzo kwa wanafunzi wa Egypt War College, yenye lengo la kuwajengea uelewa mpana kuhusu historia, utamaduni na mifumo ya kijamii ya mataifa rafiki, pamoja na kuimarisha ushirikiano wa kijeshi na kidiplomasia kati ya Tanzania na Misri.

NHC YATOA ELIMU YA HATI PACHA, YASISITIZA UMOJA WA WAMILIKI SAMIA HOUSING SCHEME KAWE

 Samia Housing Scheme Kawe: nyumba 560, familia tofauti zikiunganishwa na mtindo mmoja wa maisha ya  kisasa—ushirikiano, ustaarabu na “moder...