Tuesday, February 24, 2026

TRENI YA MWENDOKASI KUFIKA MWANZA 2028

 



Waziri wa Uchukuzi, Profesa Makame Mbarawa (wa pili kutoka kulia),akizungumza baada ya kukagua daraja la kupitisha magari chn ya reli, leo.

Na Baltazar Mashaka, Mwanza

WAZIRI wa Uchukuzi, Makame Mbarawa, ameridhishwa na kasi ya ujenzi wa mradi wa reli ya kisasa (SGR) kipande cha Mwanza–Isaka chenye urefu wa kilomita 341, unaotarajiwa kukamilika mwaka 2028.

Akizungumza katika eneo la Fella, wilayani Misungwi, leo Februari 24, 2026, baada ya kukagua maendeleo ya mradi huo, Profesa Mbarawa alisema ujenzi wa mradi huo umefikia asilimia 68 na unaendelea vizuri.

Alisema mradi huo wa kimkakati unaogharimu dola za Marekani bilioni 1.326 (takribani shilingi trilioni 3.06), ni mkubwa na kielelezo cha kujivunia, huku akimshukuru Rais Dk.Samia Suluhu Hassan kwa kusimamia utekelezaji wake, akieleza kuwa wakati anaingia madarakani mradi ulikuwa hatua sifuri sasa umefikia hatua kubwa.

Kwa mujibu Profesa Mbarawa, jengo la stesheni kuu ya Mwanza lenye uwezo wa kuchukua abiria 900 pamoja na majengo mawili ya biashara ujenzi unaendelea vyema, miundombinu ikiwemo madaraja ikifikia takribani asilimia 90, huku ulazaji wa mataruma ukiwa asilimia 53.

Alisisitiza kuwa serikali itaendelea kutoa fedha ili kuhakikisha mradi huo unakamilika kwa viwango vya kimataifa na kwa kuzingatia thamani ya fedha, una uwezo wa kuhimili changamoto mbalimbali ikiwemo matetemeko ya ardhi.

Profesa Mbarawa aliwashukuru wananchi wa Mwanza kwa shughuli za maendeleo na kuunga mkono mradi huo, akibainisha kuwa eneo lililosalia na changamoto ni Mkuyuni ambako kuna makazi yanayochelewesha ulipuaji wa miamba.

Hata hivyo, alisema kuwa, mkandarasi ameahidi kukamilisha kazi hiyo ifikapo Agosti mwaka huu na kuanza uwekaji wa njia ya reli huku akionya waliopata kazi katika mrad huo wasifanye mambo ya ovyo ikiwemo wizi wa malighafi ya saruji, nondo na vyuma, wataakuwa wanawaiba Watanzania si mkandarasi.

Alisema kukamilika kwa mradi huo kutafungua fursa mbalimbali zikiwemo ujenzi wa Bandari Kavu ya kuhifadhi mizigo kutoka Bandari ya Dar es Salaam, kubadilisha vichwa vya treni na mabehewa, na kuchochea shughuli za kiuchumi katika eneo la Misungwi, aliwataka wananchi kutunza mali za mradi na kuepuka vitendo vya wizi wa vifaa vya ujenzi.

Mbunge wa Misungwi, Silvery Salvatory (CCM), alisema reli ya SGR itaongeza usafirishaji wa mizigo ya ndani na kutoka nchi jirani, hivyo kuchochea uchumi jumuishi kama ilivyoainishwa katika Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, alitoa wito kwa wananchi kujipanga kunufaika na fursa zitakazotokana na miradi hiyo.

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Misungwi, Johari Samizi, alisema miradi ya SGR, Bandari Kavu na Daraja la JPM itaimarisha uchumi wa wilaya hiyo na kuwataka wananchi kupanga matumizi bora ya ardhi ili kuepuka migogoro na madai ya fidia baadaye.

Naye Mkuu wa Wilaya ya Nyamagana, Amina Makilagi, kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Said Mtanda, alisema kukamilika kwa reli ya SGR kutaufungua mkoa wa Mwanza kiuchumi na kuongeza fursa za uwekezaji.

Awali, Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Reli Tanzania (TRC), Mhandisi Machibya Masanja, alisema eneo la Misungwi limepangwa kuwa kitovu cha shughuli za kilojistiki, na kuwataka wawekezaji kuchangamkia fursa za kuwekeza katika Bandari Kavu, ambayo serikali imeiachia sekta binafsi kuendesha.

Alisisitiza kuwa lengo ni kuhakikisha ifikapo mwaka 2028 treni ya SGR inasafiri kutoka Dar es Salaam hadi Mwanza ikiwa na mizigo na abiria, na hivyo kuimarisha uchumi wa taifa.







REA YAANZA USAMBAZAJI WA MAJIKO BANIFU 6,692 KATIKA MKOA WA SINGIDA

 Ilongero-Singida

Wakala wa Nishati Vijijini imeanza utekelezaji wa mpango mkakati wa kitaifa wa nishati safi ya kupikia ili kufikia lengo la zaidi ya asilimia themanini 80% ya watanzania ifikapo mwaka 2034 wawe wanatumia nishati safi ya kupikia nishati ambayo ni salama kwa mtumiaji na rafiki kwa mazingira.

Akizungumza wakati wa ugawaji wa majiko katika Kata na Tarafa ya Irongero katika Wilaya ya Singida leo tarehe 24 Februari 2026 Mhandisi wa miradi ya REA Mkoani Singida, Mha.Nathan Msanze amesema kuwa Wakala ya Nishati Vijijini-REA katika mkoa huo umeanza usambazaji wa majiko banifu 6,692.

Amesema kuwa majiko hayo yatagawiwa kwa wananchi kwa bei ya ruzuku katika wilaya zote na Halmashauri za mkoa huo ambazo ni Ikungi majiko 1,116, Iramba 1,116, Itigi 1,115, Manyoni 1,115, Mkalama 1,115 na Singida 1,115.

Mhandisi Nathan amesema kuwa mradi huo unahusisha usambazaji wa majiko banifu yanayotumia kuni na mkaa kidogo ili kupunguza matumizi ya vyanzo hivyo vya nishati pamoja na athari za moshi zitokanazo na matumizi katika majiko ya kawaida. Katika mkakati huo Wakala wa Nishati Vijijini umeandaa mpango wa uuzwaji wa majiko banifu 200,000 kwa bei ya ruzuku yenye ufanisi mkubwa katika utumiaji wake.

Amesema kuwa mikataba hiyo ilisainiwa tarehe 9 Mei , 2025 na itatekelezwa ndani ya miezi 15. Gharama ya mradi ni TZS 340,288,200 kwa mkoa wa Singida na ruzuku inayotolewa na Wakala wa Nishati Vijijini ni TZS 289,230,508.47 sawa na asilimia 85 ya gharama ya mradi. Wananchi wanachangia TZS 51,057,691.53 sawa na asilimia 15 ya gharama ya mradi.

Mtoa huduma ni Tango Energy Limited ambapo jumla ya majiko banifu 6,692 yatauzwa kwa wananchi kwa bei ya ruzuku. Gharama ya jiko moja ni TZS 50,847.46 lakini serikali imetoa ruzuku ya asilimia 85 hivyo mwananchi atanunua kwa gharama ya TZS 7,600

Kwa upande wao wananchi ambao wamenufaika na majiko hayo katika kata ya Ilongero wakiongozwa na Diwani wa Kata hiyo Mhe Issa Mwiru kwa kauli moja wamempongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe Dkt Samia Suluhu Hassan kwa kuamua kutoa majiko bunifu kwa bei ya ruzuku ambayo itawanufaisha wananchi wote.







PROF. SHEMDOE APIGA MARUFUKU UHAMISHO WA WATUMISHI WENYE CHANGAMOTO ZA KINIDHAMU

 


Na OWM – TAMISEMI, Muheza

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu -TAMISEMI Mhe. Prof. Riziki Shemdoe, amewaelekeza Makatibu Tawala wa Mikoa na Wakurugenzi wa Halmashauri kutowahamisha au kuwaombea uhamisho watumishi wanaobainika kuwa na changamoto za kinidhamu katika Mamlaka za Mikoa na Serikali za Mitaa, na badala yake kuchukua hatua kwa kuwafungulia mashauri ya kinidhamu.

Prof. Shemdoe ametoa maelekezo hayo hivi karibuni akiwa katika kikao kazi na watumishi wa Muheza kilicholenga kuhimiza uwajibikaji katika usimamizi na matumizi ya fedha za miradi ya maendeleo, ikiwa ni utekelezaji wa maelekezo ya Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba, ambaye wakati wa ziara yake wilayani Muheza alibaini ubadhirifu wa fedha katika Mradi wa Jengo la Utawala na kumuelekeza Prof. Shemdoe na Waziri wa Ofisi ya Rais UTUMISHI na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete kuchukua hatua.

Aidha, Prof. Shemdoe amewaeleleza viongozi hao, kutotumia fedha au vifungu vya bajeti ya maendeleo kufanya malipo ya stahiki za watumishi, na kwamba fedha za mapato ya ndani zinazotengwa na Halmashauri kwa ajili ya miradi ya maendeleo zitumike kwenye shughuli zilizopangwa na si vinginevyo.

Sanjali na hayo, Prof. Shemdoe amewataka Wakurugenzi wa Halmashauri kuendelea kusimamia kikamilifu upatikanaji wa rasilimali fedha na matumizi sahihi ya rasilimali hizo ili kuwaletea wananchi maendeleo endelevu na tabasamu la kudumu.

Vivile, amewataka Makatibu Tawala wa Mikoa kufanya uchambuzi wa matumizi wa fedha za miradi ya maendeleo, pamoja na zinazotoka Serikali kuu na za mapato ya ndani katika kipindi cha kuanzia mwaka wa fedha 2024/25 hadi sasa, “Kama ikibainika kuna Halmashauri yoyote ina ubadhilifu na kuna watuhumiwa wa ubadhirifu huo mimi na Mhe. Ridhiwani Kikwete tutachukua hatua,” amesisitiza Prof. Shemdoe.

Hatua hiyo ya Prof. Shemdoe ni sehemu ya jitihada za kuunga mkono kwa vitendo azma ya Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kutaka fedha za miradi ya maendeleo kutumika katika kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi kupitia ujenzi wa miundombinu bora afya, elimu na barabara.


JENERALI VENANCE MABEYO AONGOZA KIKAO CHA BODI YA WAKURUGENZI NCAA

 Bodi ya Wakurugenzi wa Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro (NCAA) inayoongozwa na Mwenyekiti wake, Mkuu wa Majeshi mstaafu Jenerali Venance Salvatory Mabeyo imeanza Vikao vya Bodi hiyo ngazi ya Kamati za Kisekta kujadili utekelezaji wa Majukumu mbalimbali ya shirika kwa kipindi cha miezi 6 iliyopita (Julai- Desemba 2025) mwaka wa Fedha 2025/2026






NeST KUONDOA UCHELEWESHAJI WA MALIPO KWA WAZABUNI – PPRA YAIHAKIKISHIA KAMATI YA BUNGE

 


Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma (PPRA) imefanya wasilisho kuhusu maendeleo ya usimamizi wa sekta ya ununuzi wa umma nchini kwa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) katika Ukumbi wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dodoma.

Mkurugenzi Mkuu wa PPRA, Bw. Dennis Simba, aliieleza Kamati hiyo kuwa Mfumo wa NeST unatarajiwa kupunguza kwa kiasi kikubwa changamoto ya ucheleweshaji wa malipo kwa wazabuni, kufuatia kuunganishwa kwake na mifumo ya malipo na mifumo ya bajeti ya Serikali.

Bw. Simba alieleza kuwa hadi sasa Mfumo wa NeST una moduli sita kuu, ambazo ni Moduli ya Usajili, Moduli ya Uchakataji wa Zabuni, Moduli ya Usimamizi wa Mikataba, Moduli ya Upokeaji wa Malalamiko, Moduli ya Mnada wa Kielektroniki, pamoja na Moduli ya Malipo ya Kielektroniki (e-payment).

“Kupitia moduli ya malipo ya kielektroniki, taasisi nunuzi zinaweza kutekeleza michakato yote ya zabuni kupitia Mfumo wa NeST hadi hatua ya malipo. Mfumo huu umeunganishwa na mifumo ya malipo ya Serikali (MUSE na EMRS).

 Aidha, tunakamilisha taratibu za kuunganisha na mifumo ya bajeti. Baada ya kupata kibali cha Serikali, taasisi haitaruhusiwa kuanzisha mchakato wa ununuzi bila kuwa na kifungu cha bajeti husika na kukizuia kwenye Mfumo wa NeST mara tu mchakato unapoanza,” alisema Bw. Simba.

Alifafanua kuwa ucheleweshaji wa malipo kwa wazabuni mara nyingi husababishwa na baadhi ya watumishi wa umma kuanzisha michakato ya ununuzi bila kuhakikisha upatikanaji na ulinzi wa vifungu vya bajeti husika. 

Ameongeza kuwa baadhi ya taasisi nunuzi hubadili matumizi ya vifungu hivyo wakati mchakato ukiendelea, hali inayosababisha changamoto wakati wa kulipa wazabuni.

Hata hivyo, alibainisha kuwa kutakuwepo dirisha maalum la ununuzi wa dharura kwa zabuni zitakazothibitishwa kuhitaji kuanza mara moja, hata kama hazikupangwa awali katika bajeti ya ununuzi.

“Pamoja na kwamba ucheleweshwaji wa malipo unawaumiza wazabuni, pia unaongeza mzigo wa gharama zisizo za lazima kwa Serikali kwani wazabuni huweka ongezeko kwenye madai (interest rate),” alisema. 

Katika hatua nyingine, Bw. Simba aliieleza Kamati kuwa PPRA imeendelea kuimarisha udhibiti wa matumizi ya fedha za umma kwenye michakato ya zabuni kwa kuongeza ufanisi wa usimamizi kupitia Mfumo wa NeST. 

Alisema kuwa kuanzia mwezi Machi, mfumo huo utaanza kutuma taarifa za tahadhari (red flag notifications) kwa zabuni zitakazobainika kuwa na viashiria vya ukiukwaji wa taratibu.

 Hatua hiyo itawezesha PPRA kuingilia kati michakato ya zabuni mapema na kuchukua hatua stahiki, badala ya kusubiri ukaguzi baada ya mchakato kukamilika.

Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya PAC, Mhe. Khalfan Aeshi, aliipongeza PPRA kwa kuimarisha usimamizi wa ununuzi wa umma kupitia Mfumo wa NeST, na kuisisitiza Mamlaka kuendelea kuongeza juhudi katika utoaji wa elimu kwa umma ili Watanzania wengi zaidi waweze kufahamu na kunufaika na fursa zilizopo.

Alitolea mfano wa asilimia 30 ya bajeti ya ununuzi wa umma iliyotengwa kwa ajili ya makundi maalu (vijana, wanawake, wazee na watu wenye ulemavu), kuwa utekelezaji madhubuti wa mpango huo unaweza kusaidia kupunguza changamoto ya ukosefu wa ajira na kazi nchini.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Bodi ya PPRA, Prof. Leonada Mwagike, aliishukuru Kamati kwa maelekezo na ushauri wake, na kuahidi kuyafanyia kazi kwa haraka ili kuendelea kuimarisha usimamizi wa sekta ya ununuzi wa umma nchini.







MIF 2026: Tanzania Yaanza Safari ya Trilioni 1 — Viongozi Wakuu Wakutana Kuweka Ramani ya Uchumi wa Kati wa Juu 2050 🚀

 




Dar es Salaam. Serikali imetangaza kuwa Mkutano wa Jukwaa la Wakurugenzi wa Bodi na Watendaji Wakuu wa Kampuni ambazo Serikali ina hisa chache (Minority Interests Forum – MIF 2026) utakuwa chachu muhimu ya kuharakisha safari ya Tanzania kuelekea uchumi wa kati wa juu ifikapo mwaka 2050.

Mkutano huo unaoratibiwa na Ofisi ya Msajili wa Hazina (OMH), utafanyika kuanzia Machi 16 hadi 18, 2026 katika Ukumbi wa PAPU, jijini Arusha. Unatarajiwa kuwakutanisha viongozi kati ya 150 hadi 200 kutoka kampuni 56 ambazo Serikali inamiliki hisa chache (chini ya asilimia 51), ikiwa ni sehemu ya mkakati wa kuimarisha usimamizi, ufanisi na tija ya uwekezaji wa umma.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam Februari 24, 2026, Mkurugenzi wa Usimamizi wa Utendaji, Ufuatiliaji na Tathmini – Mashirika ya Kibiashara, Bi. Lightness Mauki, amesema MIF 2026 si mkutano wa kawaida, bali ni jukwaa la kimkakati litakaloweka dira ya pamoja ya namna ya kukabiliana na mabadiliko ya kiuchumi na kiteknolojia katika safari ya kufikia malengo ya Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050.

Alisisitiza kuwa safari ya kuelekea uchumi wa kati wa juu ni matokeo ya maamuzi sahihi, uongozi thabiti na usimamizi unaotazama mbele.“Tunakwenda kujadili namna bora ya kuharakisha safari hii kwa kuoanisha mikakati ya taasisi zetu na Dira 2050, huku tukijenga uongozi bunifu unaotambua vihatarishi mapema na kutumia fursa za kimkakati,” alisema Bi. Mauki.

Kaulimbiu Inayochochea Mageuzi ya Uongozi

Kaulimbiu ya mwaka huu — “Kutoka ufuatiliaji na usimamizi wa kawaida kwenda katika uongozi na usimamizi unaoangalia mbele” — inalenga kuhamasisha mageuzi ya fikra na mbinu za uendeshaji. Lengo ni kuondoka katika usimamizi wa kimazoea na kuelekea katika uongozi wa kimkakati unaochochea ubunifu, uwazi na uwajibikaji.

Kupitia jukwaa hilo, viongozi watajadili:

  • Uoanifu wa mikakati ya taasisi na Dira 2050

  • Matumizi ya teknolojia kuimarisha uwazi na utendaji

  • Uchambuzi wa taarifa za kiuchumi na kiushindani kwa maamuzi bora ya uwekezaji

  • Ushirikiano imara kati ya sekta ya umma na sekta binafsi

Takwimu Zinaonyesha Mafanikio Makubwa

Katika kipindi cha miaka minne iliyopita (2020–2024), kampuni ambazo Serikali ina hisa chache zimeonesha mafanikio makubwa yanayothibitisha kuwa mwelekeo uliopo ni sahihi na wenye matokeo chanya kwa Taifa.

  • Thamani ya uwekezaji wa Serikali imeongezeka kutoka Sh bilioni 821.51 mwaka 2020 hadi Sh trilioni 1.94 mwaka 2024 (ongezeko la asilimia 136).

  • Mapato ghafi yameongezeka kutoka Sh trilioni 6.81 hadi Sh trilioni 10.74 (ongezeko la asilimia 58).

  • Faida imeongezeka kutoka Sh trilioni 1.79 hadi Sh trilioni 1.95.

  • Serikali imekusanya takribani Sh trilioni 3.67 kama kodi ya mapato ya kampuni.

  • Gawio limeongezeka kwa asilimia 357 — kutoka Sh bilioni 58.26 hadi Sh bilioni 266.52.

Mafanikio haya yanaashiria mchango mkubwa wa kampuni hizo katika kukuza mapato ya Serikali, kuongeza ajira na kuimarisha sekta za kimkakati za uchumi.

Kulinda Rasilimali, Kuongeza Thamani

Bi. Mauki alisisitiza pia umuhimu wa kulinda rasilimali na mipaka ya nchi kwa weledi na uzalendo, ili kuhakikisha uwekezaji unaingiza thamani halisi kwa Taifa na kuimarisha ustawi wa wananchi.

Kwa ujumla, MIF 2026 inaonekana kuwa hatua madhubuti na ya kimkakati katika kuijenga Tanzania yenye uchumi imara, shindani na jumuishi. Ni jukwaa linaloonesha dhamira ya dhati ya Serikali kuhakikisha uwekezaji wa umma unaleta tija, unakuwa na matokeo yanayopimika na unaichangia Tanzania kufikia lengo la uchumi wa kati wa juu ifikapo mwaka 2050.

“Tunapoelekea 2050, huu si wakati wa kusubiri matokeo — ni wakati wa kuyatengeneza,” alihitimisha Bi. Mauki.

Kwa mwelekeo huu, MIF 2026 si tu mkutano, bali ni alama ya matumaini mapya na uthibitisho kuwa Tanzania iko kwenye njia sahihi ya kujenga uchumi imara wa kizazi cha sasa na kijacho

🔰RAIS DKT. SAMIA AZINDUA MAKAO MAKUU YA ULINZI KIKOMBO DODOMA

 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akipiga light pistol juu kuashiria uzinduzi wa jengo la Makao Makuu ya Ulinzi wa Taifa (MMUT), Kikombo Mkoani Dodoma tarehe 24 Februari, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa na viongozi mbalimbali kwenye picha ya pamoja na baadhi ya Maafisa na Askari wa Kikosi Kazi kutoka Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) walioshiriki Ujenzi wa Makao Makuu ya Ulinzi wa Taifa (MMUT), Kikombo Mkoani Dodoma tarehe 24 Februari, 2026


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwasili katika Makao Makuu ya Ulinzi wa Taifa (MMUT), Kikombo Mkoani Dodoma tarehe 24 Februari, 2026.RAIS SAMIA AZINDUA RASMI MAKAO MAKUU YA ULINZI WA TAIFA (MMUT) KIKOMBO

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akimkabidhi Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa Mhe. Dkt. Rhimo Simeon Nyansaho, funguo mara baada ya kuzindua jengo la Makao Makuu ya Ulinzi wa Taifa (MMUT), Kikombo Mkoani Dodoma tarehe 24 Februari, 2026. 

Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu, tarehe 24 Februari 2026 amefanya uzinduzi rasmi wa Makao Makuu ya Ulinzi wa Taifa (MMUT), Kikombo mkoani Dodoma — hatua muhimu inayodhihirisha kuimarika kwa miundombinu ya kimkakati ya ulinzi nchini.

Katika hafla hiyo ya kihistoria, Rais alipokelewa na viongozi waandamizi wa Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) pamoja na maafisa wa vyombo vya ulinzi na usalama. Uzinduzi wa MMUT ni sehemu ya juhudi za Serikali za kuimarisha uwezo wa kiutendaji, uratibu na usimamizi wa masuala ya ulinzi na usalama wa Taifa kwa viwango vya kisasa zaidi.

Akizungumza wakati wa uzinduzi, Mheshimiwa Rais alisisitiza kuwa uwekezaji katika miundombinu ya ulinzi ni msingi wa kulinda mipaka ya nchi, rasilimali za Taifa na kuhakikisha amani na utulivu vinaendelea kudumishwa.

Alieleza kuwa Serikali itaendelea kuimarisha maslahi na vitendea kazi vya wanajeshi ili kuongeza weledi, nidhamu na utayari wa kukabiliana na changamoto za kiusalama katika dunia ya sasa.

Aidha, Rais alipiga picha ya pamoja na Maafisa na Askari wa Kikosi Kazi cha JWTZ walioshiriki katika ujenzi wa makao hayo makuu, akitambua mchango wao mkubwa katika kufanikisha mradi huo wa kimkakati kwa Taifa.

Uzinduzi wa MMUT Kikombo unaashiria hatua mpya ya kuimarisha ulinzi wa Taifa, kujenga taasisi imara na kuhakikisha Tanzania inaendelea kuwa kisiwa cha amani, uthabiti na maendeleo katika ukanda wa Afrika Mashariki na Bara la Afrika kwa ujumla.

#RaisSamia
#AmiriJeshiMkuu
#UzinduziMMUT
#UlinziWaTaifa
#Dodoma
#Tanzania 🇹🇿







TRENI YA MWENDOKASI KUFIKA MWANZA 2028

  Waziri wa Uchukuzi, Profesa Makame Mbarawa (wa pili kutoka kulia),akizungumza baada ya kukagua daraja la kupitisha magari chn ya reli, l...