Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Kazi Maalum), Palamagamba Kabudi, amefanya mazungumzo na Katibu Mkuu wa Commonwealth of Nations, Shirley Botchwey, yaliyojikita katika kuimarisha ushirikiano wa kimataifa hususan katika maeneo ya utawala bora, demokrasia na maendeleo ya pamoja.
Mazungumzo hayo yamefanyika jijini London, ambako Prof. Kabudi yuko kwa ziara ya kikazi kushiriki mikutano mbalimbali ya Jumuiya ya Madola inayowakutanisha nchi wanachama 56 kutoka sehemu mbalimbali duniani.
Katika mazungumzo hayo, Prof. Kabudi alisisitiza kuwa Tanzania inaendelea kuthamini nafasi na mchango wa Jumuiya ya Madola katika kukuza ushirikiano wa kimataifa, kujenga taasisi imara za kidemokrasia na kuimarisha utawala bora miongoni mwa nchi wanachama.
Alieleza kuwa ushiriki wa Tanzania katika majukwaa ya Jumuiya hiyo unaendelea kuwa fursa muhimu ya kubadilishana uzoefu na kuimarisha mahusiano ya kidiplomasia na kiuchumi.
Kwa upande wake, Katibu Mkuu Shirley Botchwey aliipongeza Tanzania kwa mchango wake thabiti ndani ya Jumuiya ya Madola, akieleza kuwa ushiriki wa nchi hiyo katika shughuli na mijadala ya jumuiya hiyo umeendelea kusaidia kuimarisha ajenda za maendeleo, demokrasia na ushirikiano wa kimataifa.
Aidha, aliahidi kuwa Ofisi ya Katibu Mkuu itaendelea kushirikiana kwa karibu na Tanzania pamoja na nchi nyingine wanachama ili kuhakikisha malengo ya Jumuiya ya Madola yanafikiwa kwa manufaa ya wananchi wa nchi zote wanachama.
Prof. Kabudi yuko London kushiriki mikutano muhimu ya Jumuiya hiyo ikiwemo Commonwealth Ministerial Action Group 72nd Meeting (CMAG) inayotarajiwa kufanyika Machi 7, 2026, pamoja na 26th Commonwealth Foreign Affairs Ministers Meeting utakaofanyika Machi 8, 2026. Mikutano hiyo inalenga kujadili masuala ya utawala bora, demokrasia, haki za binadamu na ushirikiano wa maendeleo miongoni mwa nchi wanachama.










































%20-%20Copy.jpeg)













