Thursday, June 25, 2026

SERIKALI YAZITAKA TAASISI ZOTE KUJIANDAA KUKABILIANA NA ATHARI ZA EL NIÑO

 Naibu Katibu Mkuu wa Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu), Dkt. James Kilabuko.


Mkurugenzi wa Idara ya Menejimenti ya Maafa Ofisi ya Waziri Mkuu Brigedia Jenerali Hosea Ndagala





Naibu Katibu Mkuu wa Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu), Dkt. James Kilabuko,


Na, Mwandishi Wetu – Dodoma

SERIKALI imesema itaendelea kuimarisha mifumo ya usimamizi wa maafa nchini ili kupunguza madhara yanayosababishwa na majanga mbalimbali ambayo yamekuwa yakigharimu maisha ya watu, kuharibu mali na kurudisha nyuma maendeleo ya kijamii na kiuchumi.

Kauli hiyo imetolewa hii leo 25 Juni, 2026 na Naibu Katibu Mkuu wa Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu), Dkt. James Kilabuko, wakati akifunga Jukwaa la Wadau wa Usimamizi wa Maafa lililojadili Rasimu ya Mpango wa Taifa wa Dharura wa Kuzuia na Kukabiliana na Madhara ya El Niño Jijini Dodoma.

Amesema Tanzania imeendelea kukabiliwa na matukio ya maafa yanayosababisha athari kubwa kwa wananchi na uchumi wa Taifa, hali inayolazimu kuwepo kwa maandalizi madhubuti ya kukabiliana na changamoto hizo kabla hazijatokea.

“Nchi yetu imekuwa ikishuhudia matukio ya majanga ambayo yamekuwa yakisababisha maafa na kuathiri mfumo wa kawaida wa maisha ya jamii. Majanga hayo yamesababisha vifo, ulemavu wa kudumu, upotevu wa mali na uharibifu wa miundombinu,” amesema Dkt. Kilabuko.

Amesema kufuatia taarifa ya Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) ya Aprili 28, 2026 kuhusu uwezekano wa kujitokeza kwa hali ya El Niño, Ofisi ya Waziri Mkuu imeandaa Rasimu ya Mpango wa Taifa wa Dharura kwa ajili ya kuzuia na kukabiliana na madhara yanayoweza kutokea kuanzia Agosti 2026 hadi Juni 2027.

Kwa mujibu wa Dkt. Kilabuko, rasimu hiyo imejadiliwa na wadau mbalimbali ili kuiboresha kwa kuzingatia uzoefu uliopatikana wakati wa matukio ya El Niño yaliyowahi kutokea nchini, hususan ya mwaka 2023/2024.

Amesema ushirikishwaji wa wadau ni hatua muhimu itakayoiwezesha Serikali kuwa na mpango shirikishi na unaotekelezeka katika kuzuia, kujiandaa, kukabiliana na kurejesha hali endapo maafa yatatokea.

“Ni vema kushiriki kikamilifu na kutoa maoni yetu huku tukijielekeza kwenye athari tarajiwa na hatua za kuchukua ili kuwa na mpango thabiti utakaoiwezesha Serikali na wadau kuchukua hatua stahiki za kuzuia au kupunguza madhara,” amesema.

Aidha, ameeleza imani yake kuwa jukwaa hilo litatoa mchango mkubwa katika kuimarisha ufanisi wa usimamizi wa maafa nchini na kuongeza uwezo wa taasisi mbalimbali kukabiliana na changamoto za majanga.

Dkt. Kilabuko amesisitiza kuwa usimamizi wa maafa haupaswi kuonekana kama jukumu la taasisi chache pekee, bali unapaswa kujumuishwa katika mipango ya maendeleo na utekelezaji wa shughuli za kila siku za wizara, taasisi na mamlaka za serikali za mitaa.

Amesema hatua hiyo itasaidia kujenga jamii yenye uwezo wa kuhimili majanga na kulinda maendeleo yaliyopatikana nchini dhidi ya athari zinazoweza kusababishwa na hali ya El Niño na majanga mengine.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Idara ya Menejimenti ya Maafa Ofisi ya Waziri Mkuu Brigedia Jenerali Hosea Ndagala amesema kuwa,Jukwaa hilo ni muhimu na lipo kisheria hivyo litumike kwa manufaa na kuzingatia umuhimu wake.

Aidha alitumia nafasi hiyo kuzikumbusha kamati za maafa ngazi zote kuendelea kujiandaa na kukabiliana na maafa pindi yanapotokea kwa kuendelea kuweka mipango madhubuti ili kupunguza madhara yanayoweza kujitokeza hasa yale ya uharibifu wa miundombinu na kuepuka madhara mengine kwa jamii na Taifa kwa Ujumla.

Wednesday, June 24, 2026

RAIS SAMIA AZINDUA HUDUMA YA SARATANI KCMC, AAHIDI USHIRIKIANO KUSOGEZA HUDUMA KARIBU NA WANANCHI

 
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akikata utepe kuashiria uzinduzi wa Jengo la Tiba Mionzi (Radiotherapy Unit) katika Hospitali ya Rufaa ya Kanda ya Kaskazini KCMC, Moshi mkoani Kilimanjaro tarehe 24 Juni, 2026. Uzinduzi huu unaashiria hatua kubwa ya kuimarisha huduma za matibabu ya saratani nchini kwa kuongeza upatikanaji wa huduma za kisasa katika mikoa ya Kaskazini na Afrika Mashariki.



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akivuta kitambaa pamoja na Mwenyekiti wa Bodi ya Usimamizi wa Hospitali ya Rufaa ya Kanda ya Kaskazini (KCMC) ambaye pia ni Mkuu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Askofu Dk. Alex Gehaz Malasusa, kuashiria uzinduzi wa Jengo la Tiba Mionzi (Radiotherapy Unit) katika Hospitali ya KCMC, Moshi mkoani Kilimanjaro tarehe 24 Juni, 2026. Uzinduzi huu unaashiria hatua kubwa ya kuimarisha huduma za matibabu ya saratani nchini kwa kuongeza upatikanaji wa huduma za kisasa katika mikoa ya Kaskazini na Afrika Mashariki.

Kilimanjaro, 24 Juni 2026

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan amesema Serikali, kwa kushirikiana na wadau wa maendeleo na taasisi za afya, itaendelea kupanua huduma za uchunguzi na matibabu ya saratani katika kanda mbalimbali za nchi ili kupunguza mzigo wa safari, gharama za matibabu na msongamano wa wagonjwa katika vituo vya matibabu nchini.

Rais Dkt. Samia ameyasema hayo leo wakati wa uzinduzi wa jengo la tiba mionzi katika Hospitali ya Rufaa ya Kanda ya KCMC, wilayani Moshi, mkoani Kilimanjaro.

Ameeleza kuwa kuanza kwa huduma za tiba mionzi katika Hospitali ya KCMC ni sehemu ya mkakati wa Serikali wa kusogeza huduma maalum na za kibingwa za afya karibu na wananchi, ili kuhakikisha matibabu bora yanapatikana kwa wakati na kwa watu wengi zaidi.

“Tulikuwa na kituo kimoja cha tiba ya saratani cha Ocean Road. Huduma hizo sasa zimefikishwa katika Hospitali za Bugando na KCMC; na tunaendelea kuzifikisha katika kanda nyingine ili wananchi wasilazimike kutegemea kituo kimoja pekee,” amesema Rais Dkt. Samia.

Aidha, amebainisha kuwa Serikali imechangia Shilingi bilioni 5.5 kufanikisha sehemu ya ujenzi na manunuzi ya vifaa vya mradi huo, na itaendelea kushirikiana na KCMC katika kuongeza ufanisi wa huduma hiyo kwa wananchi.

Halikadhalika, Rais Dkt. Samia ameitaka Wizara ya Afya, kwa kushirikiana na wadau wengine wa afya, kuongeza huduma za uchunguzi wa awali wa saratani, na kutoa wito kwa wananchi kuondoa hofu ya uchunguzi kwa kujitokeza kupima afya zao mara kwa mara, sambamba na kusisitiza umuhimu wa elimu ya afya kwa wananchi kuhusu ugonjwa wa saratani.

Rais Dkt. Samia pia amesisitiza umuhimu wa uchunguzi wa awali wa saratani, hususan kwa aina ya saratani za mlango wa kizazi, matiti, tezi dume na koo, ambazo ni miongoni mwa saratani zinazoonekana zaidi nchini.

Katika hatua nyingine, Rais Dkt. Samia amepongeza hatua nzuri iliyofikiwa ya ujenzi wa Kituo cha Kisasa cha Magonjwa ya Moyo KCMC, na kuzitaka taasisi za utafiti wa afya nchini kufanya utafiti wa kina kuhusu ongezeko la saratani na magonjwa ya moyo kwa watoto ili kusaidia hatua za kinga, tiba na utoaji wa elimu kwa umma.

Akizungumza katika uzinduzi huo, Waziri wa Afya, Mhe. Mohamed Mchengerwa, amesema kuanza kwa huduma za tiba mionzi KCMC tangu mwezi Februari mwaka huu, kumeongeza uwezo wa nchi kutoa matibabu ya saratani nje ya jiji la Dar es Salaam na kusaidia kupunguza utegemezi wa Taasisi ya Saratani Ocean Road (ORCI).

Kwa upande wake, Rais wa Taasisi ya Foundation for Cancer Care in Tanzania (FCCT), Bi. Hazel Reinhardt, amesema mradi huo umeiwezesha KCMC kuwa sehemu ya mtandao wa vituo vinavyotoa huduma jumuishi za saratani, hatua inayopanua upatikanaji wa matibabu kwa wananchi wengi zaidi, akiitaja hatua hiyo muhimu kuwa ni matokeo ya ushirikiano kati ya Serikali ya Tanzania, KCMC, FCCT na wafadhili wake.

Naye, Mkuu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Askofu Dkt. Alex Malasusa, ameishukuru Serikali kwa kuendelea kushirikiana na Hospitali ya KCMC katika kuimarisha miundombinu, vifaa tiba na huduma za afya nchini.

Halikadhalika, ameiomba Serikali kuendelea kuunga mkono hatua zinazofuata za upanuzi wa huduma katika hospitali hiyo, ikiwemo upatikanaji wa vifaa vya awamu ya pili vya tiba mionzi na utekelezaji wa mradi wa Kituo cha Kisasa cha Magonjwa ya Moyo unaoendelea kujengwa hospitalini hapo.

Monday, June 22, 2026

RAIS NDAITWAH AONDOKA BAADA YA KUKAMILISHA ZIARA YA KITAIFA YA SIKU TATU NCHINI

 




Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiagana na mgeni wake Rais wa Jamhuri ya Namibia Mhe. Dkt, Netumbo Nandi-Ndaitwah katika viwanja vya Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 22 Juni, 2026.  Rais Mhe. Dkt. Ndaitwah amehitimisha Ziara yake ya Kitaifa ya siku 4 nchini Tanzania ambapo pamoja na kufanya mazungumzo na Rais Mhe. Dkt. Samia pia alitembelea Kambi ya Kihistoria ya Wapigania Uhuru wa nchi yake, Kongwa mkoani Dodoma.





Rais wa Jamhuri ya Namibia, Mhe. Dkt. Netumbo Nandi-Ndaitwah, ameondoka nchini baada ya kukamilisha Ziara ya Kitaifa ya siku tatu nchini  iliyofanyika kuanzia tarehe 19 hadi 21 Juni 2026.

Katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere jijini Dar es Salaam, Rais Ndaitwah alisindikizwa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo, pamoja na viongozi wengine wa Serikali, wanadiplomasia na maafisa mbalimbali. 

Wakati wa ziara yake nchini, Rais Nandi-Ndaitwah alifanya mazungumzo rasmi na Rais Samia yaliyolenga kuimarisha ushirikiano katika nyanja mbalimbali ikiwemo biashara, uwekezaji, elimu, kilimo, nishati na maendeleo ya kijamii.

Viongozi hao pia walijadiliana kuhusu masuala ya kikanda na kimataifa, huku wakisisitiza umuhimu wa kuendeleza mshikamano wa Afrika katika kukabiliana na changamoto za maendeleo na uchumi wa dunia.

Aidha, Rais Nandi-Ndaitwah alishiriki katika ufunguzi wa Jukwaa la Biashara la Tanzania na Namibia lililowakutanisha wafanyabiashara na wawekezaji kutoka nchi hizo mbili kwa lengo la kuibua fursa mpya za biashara na uwekezaji. 

Pia alitembelea maeneo yenye umuhimu wa kihistoria ikiwemo Magomeni, Mikumi na Kongwa mkoani Dodoma, ambayo yana kumbukumbu muhimu zinazohusiana na historia ya Namibia na harakati za ukombozi wa Kusini mwa Afrika.

Ziara hiyo imeacha alama muhimu katika kuimarisha mahusiano ya kidiplomasia, kiuchumi na kijamii kati ya Tanzania na Namibia. 

Viongozi wa nchi hizo mbili wameeleza dhamira yao ya kuhakikisha makubaliano na maelekezo yaliyotolewa wakati wa ziara hiyo yanatekelezwa kwa vitendo ili kuwanufaisha wananchi wa mataifa yote mawili na kuendeleza urithi wa urafiki uliojengwa kwa miongo mingi.

Saturday, June 20, 2026

RAIS SAMIA AMKARIBISHA RAIS WA NAMIBIA KATIKA ZIARA YA KITAIFA, WAIMARISHA USHIRIKIANO WA KIDIPLOMASIA NA MAENDELEO

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye picha na mgeni wake Rais wa Jamhuri ya Namibia Mhe. Dkt. Netumbo Nandi-Ndaitwah baada ya kuwasili Ikulu, Jijini Dar es Salaam kwa Ziara ya Kitaifa, tarehe 20 Juni, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akisalimiana na mgeni wake Rais wa Jamhuri ya Namibia Mhe. Dkt, Netumbo Nandi-Ndaitwah baada ya kuwasili katika viwanja vya Ikulu Jijini Dar es Salaam kwa Ziara ya Kitaifa, tarehe 20 Juni, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Namibia Mhe. Dkt. Netumbo Nandi-Ndaitwah akisaini kitabu cha wageni baada ya kuwasili Ikulu Jijini Dar es Salaam kwa Ziara ya Kitaifa, tarehe 20 Juni, 2026.


Rais wa Jamhuri ya Namibia Mhe. Dkt. Netumbo Nandi-Ndaitwah akiangalia vikundi vya ngoma za asili baada ya kuwasili katika Ukumbi wa Mikutano wa Kikwete, Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 20 Juni, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa na mgeni wake Rais wa Jamhuri ya Namibia Mhe. Dkt. Netumbo Nandi-Ndaitwah baada ya kuwasili katika viwanja vya Ikulu Jijini Dar es Salaam kwa Ziara ya Kitaifa, tarehe 20 Juni, 2026.



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, leo tarehe 20 Juni 2026 amempokea kwa heshima kubwa mgeni wake, Rais wa Jamhuri ya Namibia, Netumbo Nandi-Ndaitwah, katika Ikulu jijini Dar es Salaam kwa ziara rasmi ya kitaifa inayolenga kuimarisha uhusiano wa kihistoria na ushirikiano wa kimkakati kati ya mataifa hayo mawili.

Mara baada ya kuwasili Ikulu, Rais Netumbo Nandi-Ndaitwah alipokelewa na mwenyeji wake, Rais Samia, kabla ya kushiriki shughuli mbalimbali za mapokezi ikiwemo kusaini kitabu cha wageni wa heshima, hatua inayoashiria urafiki na ushirikiano wa kudumu kati ya Tanzania na Namibia.

Katika mwendelezo wa ziara hiyo, Rais wa Namibia alipata fursa ya kushuhudia na kufurahia maonesho ya vikundi vya ngoma za asili katika Ukumbi wa Mikutano wa Kikwete, yaliyobeba taswira ya utajiri wa utamaduni wa Tanzania na ukarimu wake kwa wageni wa kimataifa.

Viongozi hao wawili baadaye walifanya mazungumzo ya faragha na ya pamoja yaliyolenga kujadili namna ya kuendeleza ushirikiano katika sekta mbalimbali zikiwemo biashara, uwekezaji, uchumi, utalii, elimu, nishati na maendeleo ya kijamii. Mazungumzo hayo yanatarajiwa kufungua fursa mpya za ushirikiano zitakazonufaisha wananchi wa nchi zote mbili.

Ziara hiyo pia iliambatana na upigaji wa picha za pamoja katika Ikulu, ikiwa ni ishara ya uhusiano imara wa kidiplomasia na dhamira ya viongozi hao kuendeleza mshikamano, amani na maendeleo endelevu barani Afrika.

Ujio wa Rais Netumbo Nandi-Ndaitwah nchini Tanzania unaendelea kudhihirisha urafiki wa muda mrefu kati ya Tanzania na Namibia pamoja na azma ya pamoja ya kuimarisha ushirikiano wa kikanda na kimataifa kwa manufaa ya vizazi vya sasa na vijavyo.

Friday, June 19, 2026

RAIS SAMIA AMUAPISHA DKT. JOHN ANTHONY JINGU KUWA MTENDAJI MKUU WA MAHAKAMA YA TANZANIA


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, akimuapisha Dkt. John Anthony Jingu kuwa Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, kwenye hafla iliyofanyika Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 19 Juni, 2026.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Dkt. John Anthony Jingu akiapa Kiapo cha Maadili pamoja na Karani wa Baraza la Mawaziri Bw. Francis Petro Mossongo,  Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 19 Juni, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, akizungumza na viongozi mbalimbali baada ya kumuapisha Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Dkt. John Anthony Jingu, Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 19 Juni, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa na kwenye picha na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Dkt. John Anthony Jingu pamoja na Mtendaji Mkuu Mstaafu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elistante Ole Gabriel mara baada ya hafla ya Uapisho,  Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 19 Juni, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa na viongozi mbalimbali kwenye picha na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Dkt. John Anthony Jingu, Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 19 Juni, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, leo tarehe 19 Juni 2026 amemuapisha John Anthony Jingu kuwa Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania katika hafla iliyofanyika Ikulu, jijini Dar es Salaam.

Katika hafla hiyo, Dkt. Jingu aliapishwa rasmi kushika nafasi hiyo na baadaye akaapa Kiapo cha Maadili mbele ya Karani wa Baraza la Mawaziri, Francis Petro Mossongo, ikiwa ni hatua muhimu ya kuthibitisha dhamira yake ya kutekeleza majukumu kwa uadilifu, uwajibikaji na kwa kuzingatia sheria za nchi.

Baada ya uapisho huo, Rais Samia alizungumza na viongozi mbalimbali waliohudhuria hafla hiyo, akisisitiza umuhimu wa kuendelea kuimarisha utoaji wa haki, utawala wa sheria na ufanisi wa utendaji ndani ya Mahakama ya Tanzania kwa manufaa ya wananchi na maendeleo ya taifa.

Aidha, hafla hiyo ilihitimishwa kwa upigaji wa picha za pamoja ambapo Rais Samia alipiga picha na Mtendaji Mkuu mpya wa Mahakama ya Tanzania, Dkt. John Anthony Jingu, pamoja na Mtendaji Mkuu Mstaafu wa Mahakama ya Tanzania, Elistante Ole Gabriel. Vilevile, Rais alijumuika katika picha za pamoja na viongozi mbalimbali waliohudhuria tukio hilo, kuashiria mshikamano na kuendelea kwa jukumu la kuimarisha taasisi za utoaji haki nchini.

Uteuzi na uapisho wa Dkt. Jingu unatarajiwa kuongeza nguvu katika juhudi za kuendeleza maboresho ya kiutendaji ndani ya Mahakama ya Tanzania na kuimarisha utoaji wa huduma za haki kwa ufanisi, uwazi na weledi.

Tuesday, June 16, 2026

MAMA NEEMA MWIGULU AHIMIZA TAASISI KUUNGA MKONO JUHUDI ZA SERIKALI KUPITIA UWAJIBIKAJI KWA JAMII







Mwenza wa Waziri Mkuu, Mama Neema Mwigulu Nchemba, amehimiza taasisi za umma na binafsi kuendelea kuunga mkono juhudi za Serikali katika kuboresha huduma za kijamii kupitia utekelezaji wa programu za uwajibikaji kwa jamii (CSR).

Mama Neema amesema hayo leo Jumanne, Juni 16, 2026 katika hafla ya kukabidhi vifaa vya hospitali vilivyotolewa na Shirika la Viwango Tanzania (TBS) katika Hospitali ya Wilaya ya Chamwino, Mkoa wa Dodoma, ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya miaka 50 ya shirika hilo.

Mama Neema ambae alikuwa mgeni rasmi katika hafla hiyo, amesema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imefanya uwekezaji mkubwa katika sekta ya afya kupitia ujenzi wa miundombinu ya kutolea huduma za afya, ajira kwa wataalamu wa afya, upatikanaji wa dawa na vifaa tiba pamoja na kuimarisha huduma za kibingwa na ubingwa bobezi.

“Tunashuhudia maboresho makubwa katika sekta ya afya kutokana na uwekezaji unaoendelea kufanywa na Serikali. Leo tunajivunia huduma nyingi ambazo hapo awali zilikuwa zinapatikana nje ya nchi kupatikana hapa nchini,” amesema.

Mama Neema amewapongeza viongozi wa Shirika la Viwango Tanzania kwa kuendelea kutekeleza kwa vitendo sera ya uwajibikaji kwa jamii na kuchangia ustawi wa wananchi kupitia sekta ya afya pamoja na makundi mbalimbali yenye mahitaji maalum.

Amesema vifaa vilivyotolewa vitasaidia kuboresha utoaji wa huduma katika Hospitali ya Wilaya ya Chamwino na kuongeza ustawi wa mama na mtoto.

Vifaa hivyo vinajumuisha vitimwendo 20, vitanda vya kujifungulia vitano, vitanda vya kufanyia uchunguzi vitano, vitanda vitano vya kulaza wagonjwa, machela moja ya kisasa, makabati matatu ya kuhifadhia vifaa tiba pamoja na mabeseni yenye vifaa mbalimbali kwa ajili ya akinamama 30 waliojifungua.

Awali, akimkaribisha mgeni rasmi kuzungumza katika hafla hiyo, Waziri wa Viwanda na Biashara, Judith Kapinga amesema Serikali itaendelea kuhimiza taasisi zake kutekeleza kwa vitendo sera ya uwajibikaji kwa jamii ili kuchangia kuboresha huduma za kijamii na maisha ya wananchi.

Amesema msaada uliotolewa na Shirika la Viwango Tanzania (TBS) katika Hospitali ya Wilaya ya Chamwino ni sehemu ya mchango wa taasisi za umma katika kuunga mkono jitihada za Serikali za kuimarisha huduma za afya nchini pamoja na kuendelea kuyaishi maono ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuboresha ustawi wa wananchi.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Viwango Tanzania (TBS), Dkt. Ashura Katunzi amesema shirika hilo limeendelea kutekeleza miradi mbalimbali ya kijamii katika sekta ya afya, elimu na makundi maalum ikiwa ni sehemu ya mchango wake kwa maendeleo ya jamii.

Amesema TBS itaendelea kushirikiana na Serikali na wadau mbalimbali katika kuboresha maisha ya wananchi kupitia programu zake za uwajibikaji kwa jamii.

SERIKALI YAZITAKA TAASISI ZOTE KUJIANDAA KUKABILIANA NA ATHARI ZA EL NIÑO

  Naibu Katibu Mkuu wa Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu), Dkt. James Kilabuko. Mkurugenzi wa Idara ya Menejimenti...