Wednesday, February 18, 2026

RAIS DKT. MWINYI: MUUNGANO UENDELEE KUWA CHACHU YA UKUAJI WA UCHUMI








Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amesema kuwa ushirikiano uliopo kati ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Wizara ya Fedha ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania unatoa fursa muhimu ya kupatiwa ufumbuzi wa haraka changamoto zinazojitokeza katika masuala ya pamoja ya Muungano.

Rais Dkt. Mwinyi ameyasema hayo alipokutana na Waziri wa Fedha wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar, aliyeambatana na watendaji wakuu wa Wizara hiyo, waliofika Ikulu, Zanzibar, leo tarehe 18 Februari 2026 kwa ajili ya kujitambulisha.

Katika mazungumzo hayo, Rais Dkt. Mwinyi amesema Zanzibar inaridhishwa na mwendelezo wa vikao vya pamoja vinavyolenga kutatua changamoto za masuala ya Muungano, na kusisitiza umuhimu wa kuwepo kwa utaratibu bora zaidi utakaoinufaisha Zanzibar, hususan katika suala la upatikanaji wa mikopo kutoka taasisi za fedha za kimataifa.

Aidha, Dkt. Mwinyi ameishauri Wizara ya Fedha kuendelea kushirikiana kwa karibu na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuimarisha ushirikiano wa kifedha na kiuchumi, ili kuhakikisha masuala ya Muungano yanashughulikiwa kwa ufanisi, uwazi na kwa manufaa ya pande zote mbili za Muungano.

Kwa upande wake, Waziri wa Fedha wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar, amemuhakikishia Rais Dkt. Mwinyi kuwa Wizara yake itaendelea kutoa ushirikiano wa kiwango cha juu na kufanya kazi kwa pamoja katika kuzitumia kikamilifu fursa za kifedha na kiuchumi, kwa lengo la kuchochea ukuaji wa uchumi na maendeleo ya Zanzibar na Tanzania Bara

RAIS MWINYI APONGEZA WAZO LA BUNGE KUJENGA CHUO ZANZIBAR








Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amesema kuwa Zanzibar inahitaji kuwa na vyuo vikuu zaidi vitakavyosaidia kuiweka Zanzibar katika ramani ya kimataifa kama kituo muhimu cha utoaji wa mafunzo na elimu ya viwango vya juu katika fani mbalimbali.

Rais Dkt. Mwinyi ameyasema hayo leo, tarehe 18 Februari 2026, alipokutana na wajumbe wa Tume ya Utumishi ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, wakiongozwa na Spika wa Bunge hilo, Mhe. Mussa Azan Zungu, waliofika Ikulu, Zanzibar.

Katika mazungumzo hayo, Rais Dkt. Mwinyi ameridhishwa na wazo la Bunge la ujenzi wa Chuo cha Mafunzo ya Diplomasia na Huduma za Bunge kinachotarajiwa kujengwa Zanzibar, akieleza kuwa mradi huo ni fursa adhimu kwa taifa. Amesema kuwa uwepo wa chuo hicho utachochea ujio wa wanafunzi na wataalamu kutoka mataifa mbalimbali kuja kujifunza Zanzibar, hali itakayochangia kukuza uchumi na kuongeza mapato ya nchi kupitia sekta ya elimu na huduma zinazohusiana nayo.

Aidha, Rais Dkt. Mwinyi amewahakikishia wajumbe hao kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ipo tayari kushirikiana kikamilifu katika utekelezaji wa mradi huo, na kuwataka wajumbe wa Tume hiyo kulifanikisha wazo hilo kwa haraka ili Zanzibar iweze kunufaika na fursa hiyo mapema.

Kwa upande wake, Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Mussa Azan Zungu, amempongeza Rais Dkt. Mwinyi kwa uongozi wake thabiti ulioleta mabadiliko makubwa ya maendeleo Zanzibar, hususan katika ujenzi wa miundombinu ya barabara na kasi ya ukuaji wa uchumi inayoendana na mabadiliko ya dunia.

Wajumbe wa Tume ya Utumishi ya Bunge wako Zanzibar kwa ajili ya mafunzo ya siku tatu ya uongozi kwa Kamati ya Uongozi na Tume ya Utumishi ya Bunge, yaliyofanyika Tunguu, Mkoa wa Kusini, Unguja.

MTAMBO WA OKSIJENI WAOKOA MAISHA YA WANANCHI LUSHOTO





Na OWM - TAMISEMI, Lushoto

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu -TAMISEMI Mhe. Prof. Riziki Shemdoe ameshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuokoa maisha yake na wananchi wa Lushoto kwa kutoa fedha zilizowezesha kupatikana kwa mtambo wa kuzalisha hewa tiba ya oksijeni katika Hospitali ya Wilaya ya Lushoto.

Prof. Shemdoe ametoa shukrani hizo leo kwa Mhe. Rais wakati alipopewa fursa na Mhe. Waziri Mkuu ya kuwasalimia wananchi wa Lushoto, mara baada ya Mhe. Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba kuzindua rasmi mtambo wa kuzalisha hewa tiba ya oksijeni katika Hospitali ya Wilaya ya Lushoto uliowekwa na Serikali ili kuboresha utoaji wa huduma za tiba kwa wananchi.

“Mhe. Waziri Mkuu namshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kutuletea Shilingi Bilioni 5 zilizotuwezesha kupata vituo vya afya, zahanati pamoja na ununuzi wa mtambo huu wa kuzalisha hewa tiba ya oksijeni uliotuzindulia leo,” ameeleza Prof. Shemdoe.

Prof. Shemdoe amemueleza Mhe. Waziri Mkuu kuwa, anatambua na kuthamini umuhimu wa mtambo wa kuzalisha hewa tiba ya oksijeni kwani mwaka 2020 hewa ya Oksijeni iliokoa maisha yake alipolazwa Hospitali ya Benjamini Mkapa, na Septemba 11, 2025 alisafirishwa kwa ajili ya matibabu akiwa ametundikiwa oksijeni kutoka Hospitali ya Wilaya ya Lushoto kwenda Hospitali ya Muhimbili.

Mhandisi Vifaa Tiba wa Halmashauri ya Wilaya ya Lushoto Bw. Paschal Protace amemshukuru Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuwezesha kupatikana na mtambo unaozalisha hewa tiba ya oksijeni, ambayo inatumika kuwahudumia watoto njiti na akina mama wajawazito ambao wanauhitaji mkubwa wa hewa tiba hiyo ya oksijeni.

Kwa upande wake, mkazi wa Lushoto Bi. Khadija Rashidi ameshukuru Mungu kwa kujifungua salama na amemshukuru pia Mhe. Rais kwa kuwezesha uwepo wa vifaa tiba  ambavyo ni mtambo wa kuzalisha hewa tiba ya oksijeni na kifaa cha kuhifadhia watoto njiti (incubator) vilivyomsaidia mtoto wake kuhifadhiwa ili kupata joto na hewa safi ya oksijeni mpaka alipoimarika kiafya.

Naye Muuguzi wa Hospitali ya Wilaya ya Lushoto Bi. Theodora Tesha amesema, watoto wengi walikuwa wakipoteza maisha kabla ya kuwekwa kwa mtambo wa kuzalisha hewa tiba ya oksijeni, lakini hivi sasa idadi ya vifo imepungua kwa kiasi kikubwa na ameongeza kuwa hawajawahi kupungukiwa oksijeni kwa ajili ya kuwahudumia watoto na akina mama wajawazito.

Monday, February 16, 2026

DKT. POSSI: VIONGOZI NI TASWIRA YA TAASISI NA SERIKALI KWA JAMII


Bi. Alice Mtulo, Naibu Wakili Mkuu wa Serikali akizungumza na Menejimenti ya Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali wakati wa kikao cha faragha kilichofanyika jijini Dodoma.
Ndugu Kadari Singo, Mtendaji Mkuu wa Taasisi ya Uongozi akitoa mada kuhusu Ugawaji wa Majukumu na Usimamizi wa Muda kwa wajumbe wa Menejimenti ya Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali wakati wa kikao cha faragha kilichofanyika jijini 

Ndugu Camilius Ruhinda, Mkurugenzi wa Idara ya Usimamizi wa Mashauri na Udhibiti Ubora wa Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali akizungumza wakati wa kikao cha faragha kwa wajumbe wa menejimenti ya Ofisi hiyo kilichofanyika jijini Dodoma
Ndugu Godwin Gonde, Mhadhiri wa Chuo cha Diplomasia akitoa mada kuhusu Kanuni za Msingi za Itifaki na Maadili kwa Viongozi wakati wa kikao cha faragha kwa wajumbe wa Menejimenti ya Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali kilichofanyika jijini Dodoma.


Dkt. Ally Possi, Wakili Mkuu wa Serikali (aliyesimama katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na wakufunzi baada ya kufungua kikao cha faragha kwa wajumbe wa Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali kilichofanyika jijini Dodoma.
Bi. Alice Mtulo, Naibu Wakili Mkuu wa Serikali (aliyesimama katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na wakufunzi baada ya ufunguzi wa kikao cha faragha kwa wajumbe wa Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali kilichofanyika jijini Dodoma.

Baadhi ya wajumbe wa Menejimenti ya Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali wakichangia mada kuhusu Ugawaji wa Majukumu na Usimamizi wa Muda wakati wa kikao cha faragha kwa viongozi hao kilichofanyika jijini Dodoma.

Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali imeendesha mafunzo kwa viongozi wa taasisi hiyo na menejimenti yake ambayo yamefanyika jijini Dodoma mwishoni mwa wiki ambapo pamoja na mafunzo hayo viongozi hao wamejitathmini utendaji kazi wao wa kila siku, wamepatiwa mafunzo ya uongozi ikiwemo usimamizi na mgawanyo wa majukumu, usimamizi wa muda, itifaki na ustaarabu.

Wakili Mkuu wa Serikali, Dkt. Ally Possi alifungua mafunzo hayo na kuwaeleza wajumbe wa menejimenti ya Ofisi hiyo kuwa viongozi ni taswira ya taasisi na Serikali kwa ujumla ambapo amewaeleza kuwa kiongozi yeyote awe Mkuu wa Idara au Mkuu wa Kitengo atambue kuwa anabeba taswira ya taasisi anayofanyia kazi na Serikali kwa ujumla popote alipo, iwe kazi au unapoishi, hivyo ni muhimu kuzingatia sheria, taratibu, kanuni, maadili ya uongozi, mila na desturi za uongozi.

“Kila mmoja ajitambue wadhifa alionao na bendera anayopeperusha kwa niaba ya Serikali na kwa wale tunaowaongoza. Tuwe walezi kwa kuzingatia kuwa muda mwingi tupo mahali pa kazi kuliko familia zetu, watu tunaofanya nao kazi wafurahie kufanya kazi na wewe badala ya kukasirika, tujitathmini na kutafakari utendaji kazi wetu ili kuwa na matokeo mazuri mahali pa kazi na kujipa muda wa kujisahihisha huku tukifanya kazi kwa kuzingatia sheria, taratibu na kanuni, tuwe wabunifu na tufanye ufuatiliaji wa majukumu,” amesisitiza Dkt. Possi.

Naye Naibu Wakili Mkuu wa Serikali, Bi. Alice Mtulo amesema kuwa kikao hicho cha faragha na mafunzo hayo ni muhimu kwa wajumbe wa menejimenti wa Ofisi hiyo ili kupata muda wa kutathmini utendaji kazi na ana amini kuwa mafunzo hayo yataleta mabadiliko katika taasisi, kuwawezesha kuwafahamu na kuwasimamia vizuri wasaidizi wao, kumiliki kazi zao, kufanya maamuzi kwa wakati na kuzingatia muda katika utekelezaji wa majukumu.

Akitoa mada kuhusu uongozi na mgawanyo wa majukumu kwa wajumbe hao, Afisa Mtendaji Mkuu wa Taasisi ya Uongozi, ndugu Kadari Singo, amewapongeza viongozi wa Ofisi hiyo kwa kuandaa na kushiriki mafunzo hayo na ametoa rai kwao kujenga utaratibu wa kuwajenga wasaidizi wao ili wanapoondoka kwenye nafasi zao wawe na watu wa kuhakikisha mifumo inafanya kazi.

Aidha, Mhadhiri wa Chuo cha Diplomasia, ndugu Godwin Gonde Amani, aliwafundisha wajumbe wa menejimenti hiyo mada kuhusu itifaki na ustaarabu ambayo ilijikita kwenye masuala ya muonekano wa mtu, mavazi, mawasiliano, tabia, mienendo, matumizi ya akili ya kuzaliwa, kuheshimu mamlaka na madaraka ya kiongozi, kutambua, kujali na kuthamini uwepo wa kiongozi.

“Iitifaki ni jambo muhimu Serikalini na katika uongozi kwa kuwa ni jambo nyeti lina athari chanya na hasi baina yako binafsi na mtu mwingine katika muonekano wa mavazi, salamu, mazungumzo na mawasiliano,” amesisitiza Mhadhiri Amani.

Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali imekuwa na utaratibu wa kuendesha mafunzo kwa viongozi wa Ofisi hiyo, kufanya kikao cha faragha kwa ajili ya kutathmini utendaji kazi na utekelezaji wa majukumu mara moja kwa mwaka.

Sunday, February 15, 2026

SERIKALI KUONGEZA NGUVU KUPAMBANA NA WANYAMAPORI WAKALI TANGA








Na Sixmund Begashe, Tanga

Wizara ya Maliasili na Utalii inaendelea kutumia mbinu na teknolojia mbalimbali za kupambana na Wanyamapori wakali na waharibifu sambamba na kufungua fursa za uhifadhi na Utalii kupitia sekta za Maliasili na Utalii, kwa Watanzania ikiwemo Wilaya ya Mkinga iliyoko Mkoa wa Tanga. 

Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji (Mb), ameyasema hayo kwenye Mkutano wa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Mwigulu Lameki Nchemba (Mb) na Wananchi wa Mkinga katika hafla ya uwekaji jiwe la msingi chuo Kikuu Mzumbe tawi la Tanga.

Dkt. Kijaji amesema kuwa, ni dhamira ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe.Dkt. Samia Suluhu Hassan ambaye ndiye Mhifadhi namba moja nchini,  kuhakikisha wananchi wananufaika na uhifadhi wakiwa salama na wenye furaha. 

"Vituo vya Askari wa kuzuia Wanyamapori wakali na waharibifu (PAC) vitajengwa  katika eneo la vijiji vya Mwanyumba na Mavovo Wilayani Mkinga kwa sababu ndio eneo lenye changamoto kubwa ya tembo kwani ni mapito ya tembo kuelekea misitu ya mtoni bombo". Alisema Dkt. Kijaji.

Akizungumza kwa niaba ya wanamkinga, Mbunge wa Jimbo la Mkinga Mhe.Twaha Mwakihoja (Mb) ameipongeza Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kazi kubwa ya uhifadhi na mapambano dhidi ya Wanyamapori wakali na waharibifu, nakuomba juhudi hizo ziongezeke zaidi sambamba na kufungua fursa zaidi ya kiuchumi kwa wananchi kupitia swkta ya Utalii.

Dkt. Kijaji yupo Mkoani Tanga, kwenye ziara ya kikazi ya  Waziri Mkuu Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba, pamoja naye ameambatana na baadhi ya wajumbe wa  Menejimenti ya Wizara hiyo, pamoja na wataalam mbalimbali.

JAB YAJIPANGA KUENDELEA KUTOA MAFUNZO KWA WAANDISHI, WAMILIKI WA VYOMBO VYA HABARI




Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) imejipanga kuendelea kutoa mafunzo kwa waandishi wa habari pamoja na wamiliki wa vyombo vya habari ili kuongeza uelewa wa sheria, maadili ya taaluma na umuhimu wa ithibati katika utendaji kazi wa kila siku.

Sambamba na hilo, Bodi imebainisha haja ya kufanya mapitio ya haraka ya Sera na Sheria ya Huduma za Habari nchini ili kuendana na kasi kubwa ya mabadiliko ya teknolojia ya kidijitali.

Hatua hiyo inalenga kuhakikisha kuwa sheria hiyo, iliyotungwa mwaka 2016 kabla ya ukuaji wa sasa wa mitandao ya kijamii, inatoa tafsiri pana itakayowawezesha bloga na watengeneza maudhui ya mtandaoni kutambulika na kusimamiwa kisheria.

Kutokana na mazingira ya sasa, JAB inaona kuna umuhimu wa kufanya mapitio hayo ili kuyaingiza katika mfumo makundi hayo mapya yanayochipukia kwa kasi katika tasnia ya habari.

Katika wasilisho lililotolewa na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa JAB, Wakili Patrick Kipangula, katika mkutano wa mwaka wa utangazaji 2026 jijini Dodoma, imeelezwa kuwa mfumo rasmi wa ithibati umewekwa kwa mujibu wa Sheria ya Huduma za Habari, Sura ya 229, kwa lengo la kulinda maslahi ya umma na kuimarisha maadili ya kitaaluma.

Kwa sasa, JAB inasimamia utambuzi wa wataalamu wa habari kupitia mfumo wa kidijitali wa TAI-HABARI, ambapo waandishi waliokidhi vigezo hupatiwa vitambulisho (Press Cards) vyenye uhalali wa miaka miwili. Hadi kufikia Januari 2026, takwimu zinaonyesha kuwa zaidi ya maombi 3,200 yameidhinishwa, huku maombi mengine yakiendelea kufanyiwa kazi.

Licha ya mafanikio hayo, Bodi imetaja kuwepo kwa changamoto ya mtazamo hasi miongoni mwa baadhi ya wadau ambao wanaiona ithibati kama chombo cha kudhibiti badala ya nyenzo ya kuimarisha ubora wa uandishi.

Aidha, uelewa mdogo wa sheria umekuwa ukisababisha baadhi ya waandishi kuwasilisha maombi yasiyokidhi vigezo vya kitaaluma, ikiwemo hitaji la kuwa na angalau Stashahada au Shahada ya Uandishi wa Habari. JAB imesisitiza kuwa mwandishi asiye na ithibati hukosa uhalali wa kisheria na anaweza kuchukuliwa hatua kali, huku ikionya kuwa hali hiyo inadhoofisha uaminifu wa habari nchini.

Wakili Kipangula amesema kuwa Bodi itaendelea kushirikiana na mamlaka nyingine ikiwemo Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) pamoja na taasisi za elimu, kuhakikisha ithibati inatumika kama nyenzo ya kumlinda mwandishi katika utekelezaji wa majukumu yake, kumpatia ulinzi wa kitaaluma dhidi ya vitisho, na kuhakikisha jamii inapata habari sahihi na za kweli.

RAIS DKT. SAMIA REJEA TANZANIA BAADA YA KUSHIRIKI MKUTANO WA AU ETHIOPIA

 









Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, leo tarehe 15 Februari 2026 ameondoka katika Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Bole, jijini Addis Ababa, kurejea nchini baada ya kukamilisha ziara ya kikazi ya siku nne nchini Ethiopia. 

Katika ziara hiyo, Rais Dkt. Samia alishiriki Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Umoja wa Afrika (AU) uliofanyika tarehe 14 na 15 Februari 2026, mkutano uliowakutanisha viongozi wa bara la Afrika kujadili masuala ya amani, usalama, maendeleo ya uchumi na ushirikiano wa kikanda. 

Ushiriki wa Tanzania katika mkutano huo umeendelea kudhihirisha nafasi ya nchi katika diplomasia ya kimataifa na mchango wake katika ajenda za pamoja za bara la Afrika, hususan katika kuimarisha mshikamano, biashara baina ya nchi za Afrika na utekelezaji wa miradi ya kimkakati ya maendeleo. 

Baada ya kuondoka Addis Ababa, Rais Dkt. Samia aliwasili katika Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Abeid Amani Karume, Zanzibar, ambako alipokelewa na viongozi mbalimbali wa Serikali na Chama. Mapokezi hayo yaliashiria hitimisho la ziara yenye umuhimu wa kidiplomasia na kiuchumi kwa Taifa.

 Ziara hiyo ya siku nne imeimarisha mahusiano ya Tanzania na Ethiopia pamoja na nchi nyingine wanachama wa AU, huku ikiendeleza msimamo wa Tanzania katika kushiriki kikamilifu mijadala na maamuzi yanayolenga ustawi wa bara la Afrika. 

Kwa ujumla, ushiriki wa Rais Dkt. Samia katika Mkutano wa AU na ziara yake nchini Ethiopia umeendelea kuweka Tanzania katika nafasi thabiti ya uongozi na ushirikiano wa kikanda na kimataifa.      #RaisSamia #Tanzania #AU2026 #DiplomasiaYaAfrika #MahusianoYaKikanda #MaendeleoYaAfrika

RAIS DKT. MWINYI: MUUNGANO UENDELEE KUWA CHACHU YA UKUAJI WA UCHUMI

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amesema kuwa ushirikiano uliopo kati ya Serikali ya Map...