Sunday, February 08, 2026

RAIS SAMIA AFUNGUA SOKO LA KISASA KARIAKOO LILILOGHARIMU BILIONI 28, SASA BIASHARA SAA 24

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akisalimiana na viongozi mbalimbali mara baada ya kuwasili katika Soko Kuu jipya la Kariakoo, Ilala Jijini Dar es Salaam tarehe 08 Februari, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akivuta kitambaa kuashiria uzinduzi wa Soko Kuu jipya la Kariakoo, Ilala Jijini Dar es Salaam tarehe 08 Februari, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa katika picha ya pamoja na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba, katika eneo la jiwe la ufunguzi wa Soko Kuu jipya la Kariakoo, Ilala Jijini Dar es Salaam tarehe 08 Februari, 2026
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akikata utepe kuashiria uzinduzi wa Soko Kuu jipya la Kariakoo, Ilala Jijini Dar es Salaam tarehe 08 Februari, 2026

Wageni na viongozi mbalimbali wakiwa kwenye hafla ya ufunguzi wa Soko Kuu jipya la Kariakoo, Ilala Jijini Dar es Salaam tarehe 08 Februari, 2026.

Jiji la Dar es Salaam limeshuhudia tukio la kihistoria na lenye sura mpya ya maendeleo ya mijini leo [tarehe 08 Februari, 2026], kufuatia uzinduzi rasmi wa Soko Kuu Jipya la Kariakoo uliofanywa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan. 

Uzinduzi huo umeashiria hatua kubwa katika mageuzi ya biashara, miundombinu na ustawi wa wafanyabiashara wadogo na wakubwa jijini Dar es Salaam. Mara baada ya kuwasili katika eneo la soko hilo lililopo Ilala, Rais Dkt. Samia alisalimiana na viongozi mbalimbali wa Serikali, wafanyabiashara na wananchi, akionesha ukaribu na mshikamano wake na Watanzania katika safari ya maendeleo.

Tukio hilo lilipambwa na hali ya shangwe na matumaini, likidhihirisha furaha ya wananchi kuona ndoto yao ya soko la kisasa ikitimia. Akivuta kitambaa kuashiria uzinduzi rasmi wa Soko Kuu Jipya la Kariakoo, Rais Samia alifungua ukurasa mpya wa biashara ya kisasa inayozingatia usalama, mazingira bora ya kazi na miundombinu inayokidhi mahitaji ya karne ya 21. 

Soko hilo limejengwa kwa kuzingatia viwango vya kisasa, likiwa na nafasi za kutosha za wafanyabiashara, mifumo ya kisasa ya umeme, maji, usafi wa mazingira pamoja na tahadhari za usalama dhidi ya majanga. 

Katika hatua nyingine ya uzinduzi huo, Rais Samia alikata utepe kuashiria rasmi kuanza kwa matumizi ya soko hilo, tendo lililopokelewa kwa shangwe na nderemo kutoka kwa wageni na wananchi waliohudhuria hafla hiyo. Kitendo hicho kimekuwa ishara ya dhamira thabiti ya Serikali ya Awamu ya Sita katika kuboresha mazingira ya biashara na kuinua uchumi wa wananchi. 

Rais Samia pia alipiga picha ya pamoja na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba, pamoja na viongozi wengine wakuu wa Serikali katika eneo la jiwe la ufunguzi wa soko hilo, picha ambayo itabaki kuwa kumbukumbu ya mafanikio makubwa ya Serikali katika kuimarisha miundombinu ya biashara nchini. 

Hafla hiyo ilihudhuriwa na wageni na viongozi mbalimbali kutoka Serikalini na sekta binafsi, ambao kwa pamoja walionesha kuridhishwa na ubora wa mradi huo na kupongeza juhudi za Serikali katika kuijenga Kariakoo mpya yenye hadhi, usalama na tija zaidi. 

Uzinduzi wa Soko Kuu Jipya la Kariakoo unatajwa kuwa kichocheo kikubwa cha ukuaji wa uchumi wa jiji la Dar es Salaam na Taifa kwa ujumla, huku ukitarajiwa kuongeza fursa za ajira, mapato ya wafanyabiashara na mapato ya Serikali. 

 Kwa ujumla, uzinduzi huu umeonesha wazi dira ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kujenga Tanzania yenye uchumi imara, miji ya kisasa na mazingira bora ya maisha kwa wananchi wake, ambapo maendeleo yanagusa moja kwa moja maisha ya watu wa kawaida. 

Serikali imewekeza shilingi bilioni 28 katika ujenzi wa Soko Kuu Jipya la Kariakoo lililopo Wilaya ya Ilala, Jijini Dar es Salaam, ikiwa ni hatua madhubuti ya kuimarisha mazingira ya biashara, kuongeza ushindani wa kiuchumi na kupunguza msongamano wa shughuli za kibiashara katika eneo la Kariakoo.

Soko hilo jipya, lenye ghorofa sita, limejengwa kwa kuzingatia viwango vya kisasa vya ujenzi na upangaji wa miundombinu ya biashara. Linatarajiwa kuendesha shughuli zake masaa 24 kwa siku, hatua itakayoongeza tija, urahisi wa biashara na upatikanaji wa huduma kwa wafanyabiashara na wateja. Miongoni mwa huduma muhimu zilizopo katika soko hilo ni usalama wa kudumu, huduma zote za kibenki, zaidi ya maeneo 400 ya maegesho ya magari pamoja na maeneo maalum ya migahawa ili kukidhi mahitaji mbalimbali ya watumiaji wa soko.

Mradi huo mkubwa wa kimkakati unatarajiwa kutoa ajira zaidi ya 6,000, zikiwemo ajira 4,000 za moja kwa moja zitakazotokana na shughuli za kila siku ndani ya soko. Aidha, wafanyabiashara zaidi ya 1,520 wanatarajiwa kunufaika moja kwa moja na uwepo wa soko hilo jipya, ambalo limejengwa kufuatia tukio la kuteketea kwa soko la zamani, tukio lililoathiri kwa kiasi kikubwa shughuli za biashara katika eneo la Kariakoo.

Kwa historia, Soko la Kariakoo lilianzishwa mwaka 1914 wakati wa ukoloni wa Kijerumani, likiwa ni miongoni mwa masoko ya zamani na muhimu zaidi nchini. Kufikia mwaka 2026, soko hilo linatimiza miaka 112 tangu kuanzishwa kwake. Ujenzi wa Soko Kuu Jipya la Kariakoo unaashiria mwanzo mpya wa maendeleo ya biashara na uchumi wa Jiji la Dar es Salaam, sambamba na kuhifadhi urithi wa kihistoria wa eneo hilo la biashara.

Soko hilo jipya limezinduliwa rasmi leo, tarehe 08 Februari, 2026, ikiwa ni sehemu ya jitihada za Serikali ya Awamu ya Sita kuboresha mazingira ya biashara, kuwawezesha wafanyabiashara wadogo na wa kati, pamoja na kuchochea ukuaji wa uchumi wa jiji na Taifa kwa ujumla. Uzinduzi wa soko hili unathibitisha dhamira ya Serikali ya kuwekeza katika miradi ya kimkakati inayogusa moja kwa moja maisha ya wananchi na kuimarisha ustawi wa kiuchumi wa Taifa.

HESLB YATUZWA TAASISI KINARA MATUMIZI YA MIFUMO KIDIGITALI










Dar es salaam, Februari 08, 2026

Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari Mhe. Angela Kairuki ameipongeza Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB) kwa kuwa taasisi kinara na ya kidigitali katika utoaji wa huduma na utendaji wa kila siku na kuikabidhi tuzo ya kutambua mchango wake katika matumizi ya anwani za makazi.

Waziri Kairuki ambaye amemwakilisha Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba, ameyasema hayo leo (Jumapili, Februari 08, 2026) alipotembelea banda la HESLB kwenye Maonesho yaliyoenda sambamba na Mkutano wa Kimataifa wa Mwaka wa Anwani za Makazi na Teknolojia ya Huduma za Posta (TACPA) yaliyofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Julius Nyerere, jijini Dar es Salaam.

Aidha, Mhe. Waziri Kairuki ameiagiza HESLB kuongeza kasi ya makusanyo ya mikopo ya wanafunzi ili kuongeza mchango wake katika utoaji wa mikopo ya wanafunzi ambao wanaendelea kuongezeka mwaka hadi mwaka.

“Ningependa kuona kiasi cha makusanyo kinaongezeka … hii itasaidia kupunguza mzigo kwa Serikali na kuwezesha wanafunzi wengi zaidi kujiunga na elimu ya juu”, amesema Mhe. Kairuki.

Licha ya maonesho, HESLB pia ilishiriki katika kongamano kuhusu Nafasi ya Anwani za Makazi katika ukuaji wa Sekta mbalimbali na kisha kuendelea kwenye majadiliano kuhusu jinsi ambayo HESLB imetumia anwani za makazi na changamoto zilizojitokeza wakati wa maombi ya mikopo kwa mwaka 2025/2026 kuanzia Julai 15, hadi Septemba 15, 2025.

HESLB ni miongoni mwa taasisi zinazotumia anwani ya makazi hususan katika huduma ya maombi ya mikopo kwa wanafunzi kikiwa ni kipengele muhimu kuanzia mwaka wa masomo 2025/2026 ambacho kimewekwa kuwa ni moja ya taarifa ya msingi inayohitajika kutoka kwa mwombaji na wazazi wake kabla ya kumpangia mkopo stahiki.  

Washiriki kutoka ndani na nje ya nchi wametumia jukwaa hilo la siku nne kuanzia Februari 5 hadi 8, 2026 ili kujadili kwa pamoja mafanikio, changamoto na kubadilishana uzoefu miongoni mwa wadau kwa lengo la kuboresha eneo la anwani za makazi na teknolojia ya huduma za Posta likiwa na kauli mbiu isemayo, “Anwani Mahiri na Ubunifu wa Huduma za Posta kwa Ukuaji Jumuishi.

Mkutano na Kongamano hilo lmefanyika kwa mara ya pili na kujumuisha washiriki 1, 000 kutoka nchi mwenyeji Tanzania na wageni kutoka Guinea, Burkina Faso, Korea ya Kusini, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), Rwanda na Malawi.

PROF. SHEMDOE AKUTANA NA MKURUGENZI WA BENKI YA AZANIA KUJADILI MAENEO YA USHIRIKIANO







Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM-TAMISEMI) Mhe. Prof. Riziki Shemdoe amekutana na Mkurugenzi mtendaji Benki ya Azania Bi. Esther Mangenya na kufanya mazungumzo ya namna bora ya kushirikiana katika kuboresha utoaji wa huduma za afya msingi, elimu msingi na ujenzi wa miundombinu ya barabara pamoja miundombinu ya huduma nyinginezo za kijamii.

Prof. Shemdoe alifanya mazungumzo hayo na Mkurugenzi Mtendaji huyo wa Benki ya Azania tarehe 05 Februari 2026 ofisini kwake Jijini Dodoma, alipomtembelea kwa lengo la kujitambulisha ili kujenga mahusiano mazuri ya kiutendaji yatakayowanufaisha wananchi waliopo kwenye Mamlaka za Serikali za Mitaa.

Katika kikao kazi hicho, Prof. Shemdoe na Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Azania Bi. Esther Mangenya wamekubaliana kujenga mahusiano mazuri ili wananchi wanufaike na mchango wa Serikali na benki hiyo katika kuboresha miundombinu ya utoaji wa huduma za kijamii.

Kwa kutambua mchango wa taasisi za kifedha kwa jamii, Prof. Shemdoe amesema ofisi yake ipo tayari kushirikiana na benki hiyo na kuitambulisha katika Mamlaka za Serikali za Mitaa ili waifikie jamii na kuihudumia.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Azania Bi. Esther Mangenya amemueleza Prof. Shemdoe kuwa benki yake imedhamiria kuwajibika kwa jamii kwa kutoa mchango utakaoboresha huduma mbalimbali za kijamii ikiwepo na za kifedha.

Prof. Shemdoe tangu apewe dhamana na Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kusimamia Mamlaka za Serikali za Mitaa, amekuwa mstari wa mbele katika kukutana na Wadau wa Maendeleo kwa lengo la kuboresha ushirikiano na ofisi ili kupeleka tabasamu kwa wananchi na ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa maelekezo ya Mheshimiwa Rais.

Saturday, February 07, 2026

Rais Museveni Afanya Ziara ya Kikazi Tanzania, Aimarisha Ushirikiano wa Kidiplomasia na Kiuchumi na Rais Samia












Rais wa Jamhuri ya Uganda, Mheshimiwa Yoweri Kaguta Museveni, amewasili jijini Dar es Salaam kwa ziara ya kikazi ya siku moja, ziara inayodhihirisha undugu wa kihistoria na mshikamano wa kidiplomasia uliodumu kwa muda mrefu kati ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Jamhuri ya Uganda.

Mara baada ya kuwasili, Mheshimiwa Rais Museveni anatarajiwa kufanya mazungumzo rasmi ya pande mbili na mwenyeji wake, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan.

 Mazungumzo hayo yatafanyika kwa kuzingatia taratibu na itifaki za kimataifa, yakiwa na lengo la kuimarisha zaidi uhusiano wa kidiplomasia, kisiasa na kiuchumi kati ya mataifa hayo mawili jirani na rafiki.

Kwa mujibu wa ratiba ya ziara hiyo, viongozi hao wawili watajadiliana kwa kina masuala ya ushirikiano wa kiuchumi, hususan katika sekta muhimu za kimkakati ikiwemo nishati, biashara na miundombinu.

Kipaumbele kikubwa kinatarajiwa kuwa Mradi wa Bomba la Mafuta Ghafi la Afrika Mashariki (EACOP), mradi wa kihistoria unaotekelezwa kwa ushirikiano wa kikanda na unaotajwa kuwa kichocheo kikubwa cha maendeleo ya kiuchumi, ajira na mapato kwa Tanzania, Uganda na ukanda wa Afrika Mashariki kwa ujumla.

Viongozi hao pia wanatarajiwa kubadilishana mawazo kuhusu masuala ya kikanda na kimataifa yenye maslahi ya pamoja, ikiwemo amani na usalama wa ukanda, mshikamano wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), pamoja na mchango wa nchi zao katika kuimarisha diplomasia ya kiuchumi na maendeleo endelevu barani Afrika.

Ziara hii ya kikazi inaakisi dhamira ya dhati ya Tanzania na Uganda ya kuendeleza diplomasia ya majirani wema, kuheshimiana na kushirikiana kwa manufaa ya wananchi wao. Aidha, inathibitisha uongozi wa busara wa Marais Dkt. Samia Suluhu Hassan na Yoweri Kaguta Museveni katika kusukuma mbele ajenda ya ushirikiano wa kikanda unaolenga ustawi wa pamoja, maendeleo ya kiuchumi na mshikamano wa Afrika Mashariki.

Kwa ujumla, ujio wa Rais Museveni nchini Tanzania ni ishara chanya ya kuendelea kuimarika kwa mahusiano ya kihistoria kati ya mataifa haya mawili, huku ukitarajiwa kuzaa matokeo yenye manufaa ya muda mrefu kwa pande zote mbili na kwa ukanda mzima wa Afrika Mashariki.

Friday, February 06, 2026

WAZIRI MKUU ACHUKIZWA NA MIGOGORO YA ARDHI





Awasisitiza watendaji kuwafuata wananchi na kutatua kero zinazowakabili

WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba amewasisitiza Mawaziri, Wakuu wa Mikoa, Wakuu wa Wilaya pamoja na watumishi wa umma wahakikishe wanatenga muda wa kusikiliza na kutatua kero za wananchi katika maeneo yao hususani kwenye migogoro ya ardhi katika ngazi zao za kiutawala. 

Ameyasema hayo leo Ijumaa, Februari 6, 2026 wakati wa kuahirisha Mkutano wa Pili wa Bunge la 13 jijini Dodoma, akisisitiza kuwa viongozi hao wanapaswa kuwafuata wananchi, kuwasikiliza na kuchukua hatua za haraka za kutatua changamoto mbalimbali zinazowakabili wakiwa katika maeneo yao.

“Wafuateni, wasikilizeni na tatueni kero zao ili wasilazimike kwenda ngazi za juu au kusubiri ziara za viongozi wa kitaifa kwa masuala ambayo mngeweza kuyafanyia kazi.” Waziri Mkuu ameongeza kuwa Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan anataka kuona wananchi wakihudumiwa ipasavyo.

Katika hatua nyingine, Mheshimiwa Waziri Mkuu amesema Serikali imeendelea kuhakikisha kuwa upatikanaji wa elimu bora katika ngazi mbalimbali, lengo likiwa ni kuwawezesha wanafunzi wa Kitanzania kupata ujuzi utakaomudu ushindani Kitaifa na Kimataifa.

Waziri Mkuu amesema kuwa mbali na upatikanaji wa elimu bora Serikali imepata mafanikio makubwa katika sekta hiyo ikiwa ni pamoja na kuzindua Mpango Mkakati wa Kisayansi wa Kujenga Umahiri wa Kusoma, Kuandika na Kuhesabu (KKK) unaolenga kuhakikisha mtoto wa darasa la tatu anasoma, anaandika na anahesabu bila shida.

Pia, Waziri Mkuu amesema Serikali imeajiri na kuwapangia vituo vya kazi jumla ya walimu 7,000 wa masomo ya Sayansi na Hisabati na kukamilisha mpango wa pamoja kati ya Waajiri, Vyuo vya Ufundi Stadi na Vyuo Vikuu kwa lengo la kulinganisha mafunzo na mahitaji ya sekta za kipaumbele.

Amesema kuwa Serikali imeimarisha matumizi ya TEHAMA shuleni kwa kusambaza vifaa katika shule za msingi na sekondari na kuendeleza tafiti na bunifu kupitia mfuko maalum wa Samia Commercialization Fund ili kubidhaisha bunifu na teknolojia.

Vilevile, Waziri Mkuu amesema Serikali imeongeza fursa za upatikanaji wa elimu kwa kuendelea kutoa mikopo ya elimu ya juu kupitia mikopo ya wanafunzi pamoja na ufadhili na kutekeleza mpango wa elimu bila ya ada kwa shule za msingi na sekondari.

Thursday, February 05, 2026

Serikali Yabainisha Maeneo ya Miradi ya Umeme wa Upepo na Jua, Kishapu kuzalisha MW 150







Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba amesema Serikali imekwishabainisha na kufanya utafiti wa maeneo mbalimbali yanayofaa kuendelezwa kwa ajili ya miradi ya kuzalisha umeme kwa kutumia upepo na jua, ikiwa ni pamoja na Zuzu-Dodoma, Same-Kilimanjaro na Manyoni-Singida.

Mhe. Salome ametoa kauli hiyo leo Februari 05, 2026 bungenini jijini Dodoma wakati akijibu swali la Mbunge wa Mwera, Mhe. Suleiman Mohamed Rashid aliyehoji juu ya mpango wa Serikali wa kutumia vyanzo vya umeme na upepo juu vilivyopo nchini.

" Kwa sasa Serikali inatekeleza mradi wa kuzalisha umeme wa megawati 150 katika Wilaya ya Kishapu, Shinyanga ambapo awamu ya kwanza ya mradi huo wenye megawati 50 imekamilika na hatua za kuingiza umeme huo katika Gridi ya Taifa zimeanza," Amesema Mhe. Salome.

Akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Kilimanjaro, Mhe Esther Malleko aliyehoji mkakati wa Serikali katika kumaliza usambazaji wa umeme kwenye vitongoji vilivyosalia mkoani humo, Mhe. Salome amesema Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) inaendelea na kazi za utekelezaji wa ujenzi wa miundombinu ya kusambaza umeme katika Mkoa wa Kilimanjaro ambapo hadi kufikia Januari 2026 jumla ya vitongoji 2,032 kati ya 2,258 sawa na asilimia 90 vilipatiwa umeme na kusalia vitongoji 226 ambavyo vitapelekewa umeme kupitia miradi mbalimbali.

Wednesday, February 04, 2026

RAIS SAMIA AENDELEZA DIPLOMASIA YA KIMATAIFA DUBAI, ALAKIWA NA MAZUNGUMZO NA MTAWALA WA DUBAI KANDO YA WGS 2026

 



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, ameendelea kuimarisha diplomasia ya kimataifa kwa kufanya mazungumzo ya ngazi ya juu na Makamu wa Rais wa Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) na Mtawala wa Dubai, Sheikh Mohammed bin Rashid Al Maktoum, kando ya Mkutas ya Dunia ya Serikali (World Governments Summit – WGS 2026), jijini Dubai, tarehe 04 Februari, 2026.

Mazungumzo hayo yalilenga kuendeleza ushirikiano kati ya Tanzania na UAE katika maeneo ya kimkakati ikiwemo biashara, uwekezaji, miundombinu, uvumbuzi na diplomasia ya kiuchumi, sambamba na kubadilishana uzoefu kuhusu uongozi na maendeleo ya kisasa.

Mara baada ya mazungumzo hayo, Mheshimiwa Rais Samia alipokea zawadi ya kitabu kutoka kwa Sheikh Mohammed bin Rashid Al Maktoum, ishara ya heshima, urafiki na uhusiano imara unaoendelea kuimarishwa kati ya Tanzania na UAE.

Ushiriki wa Rais Samia katika WGS 2026 unaendelea kuweka Tanzania katika ramani ya majadiliano ya kimataifa, huku ukitafsiri dira ya Serikali ya Awamu ya Sita ya kujenga ushirikiano wa kimataifa wenye tija, unaozingatia maslahi ya taifa na maendeleo endelevu.

#RaisSamia #WGS2026 #TanzaniaNaUAE #DiplomasiaYaKiuchumi #MahusianoYaKimataifa#KaziNaUtuTunasongaMbele

RAIS SAMIA AFUNGUA SOKO LA KISASA KARIAKOO LILILOGHARIMU BILIONI 28, SASA BIASHARA SAA 24

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akisalimiana na viongozi mbalimbali mara baada ya kuwasili katika Sok...