Tuesday, April 28, 2026

WAZIRI WA MAMBO YA NJE WA BELARUS AWASILI NCHINI KWA ZIARA YA KIKAZI

 








Waziri wa Mambo ya Nje wa Jamhuri ya Belarus, Mheshimiwa Maxim Ryzhenkov, amewasili nchini kwa ziara ya kikazi ya siku tatu kuanzia Aprili 28 hadi 30, 2026, kufuatia mwaliko wa Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo.

Mheshimiwa Ryzhenkov amewasili kupitia Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere jijini Dar es Salaam, ambapo alipokewa na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Ngwaru Maghembe, pamoja na Balozi wa Jamhuri ya Belarus nchini Mhe.Dzmitry Krasouski.

Katika ziara hiyo, Mheshimiwa Ryzhenkov anatarajiwa kufanya mazungumzo ya pande mbili na mwenyeji wake, Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo, Aprili 28, 2026, jijini Dar es Salaam. Aidha, atakutana na viongozi wengine wa Serikali kwa lengo la kuendeleza na kupanua ushirikiano kati ya nchi hizo mbili.

Ziara hiyo inalenga kuimarisha uhusiano wa kidiplomasia kati ya Tanzania na Belarus pamoja na kukuza ushirikiano wa kiuchumi katika maeneo yenye maslahi ya pamoja.

Monday, April 27, 2026

SEKTA YA MADINI YACHOCHEA UCHUMI: MAPATO YAVUKA MALENGO NA MAUZO

 

Na. Meleka Kulwa- Fullshangwe Blog, Dodoma 

Waziri wa Madini, Mhe. Anthony Mavunde, amesema kuwa Serikali inaendelea kuonesha dhamira ya dhati ya kuifanya sekta ya madini kuwa injini muhimu ya kukuza uchumi wa Taifa kwa kuwekeza zaidi katika mnyororo wa thamani wa madini mkakati na kuhamasisha uwekezaji katika uongezaji thamani.

Ameyabainisha hayo Aprili 27, 2026 Jijini Dodoma, wakati akiwasilisha  bajeti ya Wizara kwa mwaka wa fedha 2026/2027, amesema kuwa madini mkakati yakiwemo lithium, graphite, nickel, cobalt na rare earth elements yana nafasi kubwa katika maendeleo ya teknolojia za kisasa hususan nishati safi. Aidha amebainisha kuwa mwelekeo wa dunia kutumia teknolojia rafiki kwa mazingira unaongeza mahitaji na thamani ya madini hayo katika soko la kimataifa.

Pia ameongeza kuwa Serikali imejipanga kuimarisha uwekezaji katika utafutaji na uchimbaji wa madini hayo ili kuongeza uzalishaji pamoja na mapato ya Taifa. Amesema kuwa tafiti za masoko mapya zitafanyika ili kupanua wigo wa biashara huku taratibu za utoaji leseni zikirahisishwa kwa wawekezaji.

Amesema kuwa lengo kuu ni kuhakikisha Watanzania wananufaika moja kwa moja kupitia ajira, mapato na maendeleo ya viwanda vinavyotokana na rasilimali hizo.

Aidha amebainisha kuwa Serikali imeweka mkakati wa kuhamasisha ujenzi wa viwanda vya uchenjuaji, uyeyushaji na usafishaji wa madini ili kuongeza thamani kabla ya kusafirishwa nje ya nchi. Amesema hatua hiyo inalenga kupunguza usafirishaji wa madini ghafi na kuongeza mapato kupitia bidhaa zilizoboreshwa.

Pia ameongeza kuwa eneo la Buzwagi wilayani Kahama limetengwa kwa ajili ya uwekezaji wa viwanda vya kuongeza thamani madini, hatua inayotarajiwa kuvutia wawekezaji na kuongeza ajira kwa wananchi.

Aidha amebainisha kuwa Serikali inaendelea kushirikiana na wadau kuhakikisha viwanda vya usafishaji wa dhahabu vinapata ithibati ya kimataifa ili kuongeza ushindani wa bidhaa za Tanzania katika soko la dunia.

Amesema kuwa Tanzania inatarajia kuandaa mkutano wa saba wa kimataifa wa uwekezaji katika sekta ya madini utakaofanyika Dar es Salaam mwezi Novemba 2026, ambapo wadau mbalimbali watakutana kujadili fursa na changamoto za sekta hiyo.

Kwa upande wa utekelezaji wa bajeti ya mwaka 2025/2026, amesema kuwa Wizara imepiga hatua kubwa ikiwemo kuvuka malengo ya ukusanyaji wa mapato na kuimarisha usimamizi wa rasilimali madini.

Aidha amebainisha kuwa Bunge liliidhinisha shilingi bilioni 224.98 kwa ajili ya Wizara, ambapo kati ya hizo shilingi bilioni 100.38 zilitengwa kwa matumizi ya kawaida na shilingi bilioni 124.60 kwa miradi ya maendeleo. Amesema kuwa hadi Machi 2026, Wizara ilikuwa imepokea shilingi bilioni 82.90.

Pia ameongeza kuwa katika ukusanyaji wa maduhuli, Wizara ilipangiwa kukusanya shilingi trilioni 1.41 lakini hadi Machi 2026 tayari ilikuwa imekusanya shilingi trilioni 1.03, sawa na asilimia 114.94 ya lengo la kipindi husika.

Amesema kuwa mafanikio hayo yametokana na kuimarishwa kwa ukaguzi katika maeneo ya uchimbaji, masoko ya madini, vituo vya ununuzi pamoja na mipaka ya nchi ili kudhibiti upotevu wa mapato.

Aidha amebainisha kuwa thamani ya biashara ya madini imeongezeka na kufikia shilingi trilioni 4.90 katika kipindi cha Julai 2025 hadi Machi 2026 ikilinganishwa na shilingi trilioni 2.82 kwa kipindi kama hicho mwaka uliopita.

Pia ameongeza kuwa Serikali imeendelea kudhibiti utoroshaji wa madini ambapo madini yenye thamani ya shilingi bilioni 3.31 yalikamatwa katika matukio 55 na wahusika kuchukuliwa hatua za kisheria.

Amesema kuwa mapato ya fedha za kigeni yameongezeka ambapo mauzo ya madini nje ya nchi yalifikia dola milioni 5,401.9 mwaka 2025 kutoka dola milioni 4,119.9 mwaka 2024.

Aidha amebainisha kuwa mchango wa sekta ya madini katika Pato la Taifa umeongezeka kutoka asilimia 9.1 mwaka 2023 hadi asilimia 10.1 mwaka 2024 na kufikia wastani wa asilimia 11.9 katika robo tatu za mwaka 2025

Friday, April 24, 2026

🏗️ MASASI COMMERCIAL COMPLEX YAKABIDHIWA RASMI









Mradi wa Masasi Commercial Complex umekabidhiwa rasmi, ukiwa ni alama ya mafanikio ya utekelezaji wa miradi ya kisasa yenye kuzingatia ubora na thamani kwa jamii.

Akizungumza katika hafla hiyo, Meneja wa NHC Mkoa wa Lindi, Omari Malalamangi, aliipongeza timu ya ujenzi kwa kazi kubwa waliyoifanya licha ya changamoto ya maji wakati wa uchimbaji wa msingi. 

Alisisitiza kuwa kujituma kwao kumezaa matokeo bora—jengo lenye hadhi linalovutia na kupongezwa na wengi.

Mradi huu umeacha alama chanya kwa jamii, ukitoa ajira kwa wakazi wa Masasi na kunufaisha sekta mbalimbali zikiwemo huduma za maji, umeme, mama lishe pamoja na wauzaji wa vifaa vya ujenzi.

Kwa upande wake, Meneja Usimamizi wa Miradi NHC, Grace Musita, alieleza kuwa ujenzi umefuata taratibu zote za kitaalamu, huku vipimo vya vifaa kama nondo, kokoto na tofali vikifanyika katika maabara ya Mtwara. 

Alibainisha kuwa kila hatua ya ujenzi ilisimamiwa kwa ukaribu na wataalamu ili kuhakikisha ubora unazingatiwa kabla ya kuendelea na hatua inayofuata.

Aidha, mradi umefungua fursa kwa wafanyabiashara wa ndani, ambapo baadhi ya kazi kama uwekaji wa milango ya mbao na tiles zilifanywa na mafundi wazawa wa Masasi.

Musita alimshukuru Mkurugenzi Mkuu pamoja na Menejimenti ya NHC kwa ushirikiano uliowezesha kukamilika kwa mradi huu kwa mafanikio.

Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa Madaraka, Kata ya Jida, alieleza furaha yake akisema ujio wa jengo hili umeubadilisha mtaa huo na kuongeza uhai wa shughuli za kijamii na kiuchumi, huku ajira ndogo ndogo zilizotolewa zikichochea vijana wengi kujikwamua kiuchumi.

Hafla ya makabidhiano ilihitimishwa kwa kukata keki, kuashiria rasmi kuwa Masasi Commercial Complex ipo tayari kutumika.

#NHC #MasasiComplex #UjenziBora #MaendeleoYaJamii #Tanzania

Thursday, April 23, 2026

UJUMBE WA MAAFISA KUTOKA CHUO CHA ULINZI CHA TAIFA MISRI WATEMBELEA MAKUMBUSHO YA TAIFA TANZANIA









Leo, tarehe 23/04/2026 Makumbusho ya Taifa la Tanzania imepokea ugeni maalum kutoka Chuo cha Kijeshi Misri (Egypt War College) walioko katika ziara ya mafunzo.

Ujumbe huo uliongozwa na Meja Jenerali Mohamed Yehia Zakaria Hassan akiambatana na Brigedia Jenerali Islam Sayed Bakry El-Sayed, huku kwa upande wa mwenyeji wao kutoka Tanzania wakiongozwa na Brigedia Jeneral Kamanda Makanya Erassy kutoka JWTZ Tanzania.

Wageni hao walipokelewa na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Makumbusho ya Taifa la Tanzania, Bi. Pendo Gondwe, ambaye aliwakaribisha na kuwapatia maelezo kuhusu dhima ya taasisi hiyo ya Kimkakati katika kuhifadhi, kulinda na kuendeleza urithi wa historia na utamaduni wa Taifa.

Ujumbe huo uliokuwa na lengo la kujifunza ulipata fursa ya kutembelea na kujifunza historia ya Tanzania kupitia vivutio mbalimbali vilivyopo katika Makumbusho, ikiwemo mabaki ya kihistoria, tamaduni za jamii mbalimbali pamoja na hatua za maendeleo ya taifa. Wageni hao walionesha kuvutiwa na ubora wa maonesho na namna historia ya Tanzania inavyoendelea kuhifadhiwa na kuwasilishwa kwa ufanisi.

Akizungumza baada ya ziara hiyo, kiongozi wa ujumbe, Meja Jenerali Mohamed Yehia Zakaria Hassan, alieleza kufurahishwa kwake na kiwango cha maonesho hayo akisema, “ Maonesho ni bora sana na nimefurahishwa kuona mwendelezo wa historia ukiendelea kukua na kuendelezwa"* 

Ziara hiyo ni sehemu ya programu ya mafunzo kwa wanafunzi wa Egypt War College, yenye lengo la kuwajengea uelewa mpana kuhusu historia, utamaduni na mifumo ya kijamii ya mataifa rafiki, pamoja na kuimarisha ushirikiano wa kijeshi na kidiplomasia kati ya Tanzania na Misri.

MHANDISI SEFF AKAGUA UJENZI WA BARABARA ZA UWANJA WA AFCON ARUSHA






#Ataka kazi zikamilike ifikapo Mei 2027

Arusha

Mtendaji Mkuu wa Wakala ya Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) Mhandisi Victor Seff amefanya ziara ya kukagua maendeleo ya ujenzi wa barabara zinazoingia katika uwanja utakaotumika kwa mashindano ya AFCON jijini Arusha.

Mhandisi Seff amesema kwamba ziara hiyo imelenga kujionea hatua za utekelezaji wa mradi wa barabara zenye urefu wa kilomita 21.4 ambapo kazi tayari zimeanza katika sehemu ya barabara ya Essuri.

Amesema serikali imejipanga kuhakikisha miundombinu hiyo inakamilika kwa wakati na kuongeza kuwa maeneo ambayo bado hayajaanza yanasubiri kukamilisha taratibu za fidia kwa wananchi watakaoathiriwa na mradi huo huku mkakati ukiwa ni kuendelea kuzungumza nao ili kutoa ushirikiano na kuruhusu kazi ziendelee bila vikwazo.

“Lengo la Serikali ni kuhakikisha barabara hizi zinakamilika ifikapo Mei mwaka 2027 ili ziwe tayari kabla ya mashindano ya AFCON,” amesema Mhandisi Seff.

Aidha, amesema mradi huo unatekelezwa kwa utaratibu wa Sanifu na Jenga (Design and Build) unaotumika pale ambapo muda ni mchache huku hatua zote za ununuzi tayari zikikamilika.

Ameeleza kuwa TARURA itaendelea kufanya ufuatiliaji wa karibu kuhakikisha mkandarasi anakamilisha kazi kwa wakati na kwa viwango vinavyotakiwa sanjari na ratiba ya mashindano hayo makubwa ya Mataifa ya  Afrika.

Ameongeza kuwa kwa sasa Mkandarasi M/s China Railway Construction Engineering Group tayari ameanza kazi ambapo ameanza na barabara ya Essuri yenye urefu wa kilomita 2.45 pia kutajengwa daraja lenye urefu wa mita 100.

Kwa upande wa barabara ya Lendita yenye kilomita 2.75, Mhandisi Seff amesema barabara hiyo itajengwa pamoja na daraja katika awamu ya pili ya mradi huku barabara hiyo ikitarajiwa kuwa ya njia nne.

Ameongeza kusema pia barabara ya Mateves yenye kilomita 6.5 itajengwa kwa sehemu mbili ambapo kilomita 5.5 zitakuwa njia mbili na kilomita 1 itakuwa njia nne.

Mtendaji Mkuu huyo amesema kukamilika kwa mradi huo kutaleta mafanikio makubwa kwa Taasisi hiyo kwa kupata uzoefu wa kusimamia miradi ya  Sanifu na Jenga, huku wananchi wakinufaika kwa kuondokana na changamoto ya miundombinu  katika maeneo hayo.

Vilevile, amesema wakazi wa maeneo yanayozunguka mradi huo watapewa kipaumbele cha ajira na amewataka vijana kujitokeza  kupata ajira na kutumia fursa hiyo kujiongezea kipato pamoja na  uzoefu wa kazi.

Kwa upande mwingine amewataka wasimamizi wa mradi huo kusimamia kwa karibu utekelezaji wake kwani mashindano hayo yanatarajiwa kuanza Julai mwakani.

Naye, Mhandisi Mshauri kutoka  kampuni ya M/s Afrisa Construction Engineering Group Bw. Idephonce Karol amesema mradi huo ulianza rasmi  tarehe 1 Aprili, 2026 na kwa sasa hatua za awali zinaendelea vizuri.

Amesema tayari wamehamasisha timu ya wataalamu, kufanya upimaji wa maeneo yote matatu ya barabara, uchunguzi wa udongo, tathmini ya vifaa vya ujenzi pamoja na kusafisha sehemu ya barabara ya Essuri urefu wa kilomita 1.8.

“Tumejipanga kikamilifu na tunafahamu umuhimu wa mradi huu hivyo tutafanya kazi usiku na mchana ili kuhakikisha unakamilika kwa wakati,” amesema Karol.

KIWANDA CHA KUCHAKATA MADINI CHUMVI MBIONI KUKAMILIKA MKOANI LINDI

 





●Wadau wa chumvi kuanza kuuza chumvi iliyochakatwa

●Zaidi ya tani 60 hadi 100 kuchakatwa kwa mwezi

●Wazalishaji wa chumvi waipongeza serikali kwa utatuzi wa changamoto

Dodoma

Katika juhudi za kuendeleza na kuboresha uzalishaji wa madini chumvi nchini Serikali kupitia Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) ipo mbioni kukamilisha kiwanda cha kuchakata madini chumvi kilwa mkoani Lindi pamoja kusaidia ujenzi wa viwanda mkoani Tanga na Mtwara.

Hayo yameelezwa leo Aprili 23, 2026 na Waziri wa Madini Mhe. Anthony Mavunde wakati wa kikao baina ya Chama cha Wazalishaji Chumvi Tanzania (TASPA) na Wizara ya Madini na taasisi zake  kilichofanyika jijini Dodoma.

Waziri  Mavunde , amesema kuwa, Serikali ilipokea maombi ya TASPA na kufanikiwa kushusha mrabaha katika madini chumvi kutoka asilimia 4 mpaka asilimia 1 ya bei elekezi.

Waziri Mavunde ameongeza kuwa, Serikali inaendelea kushughulikia uanzishwaji wa leseni moja katika shamba moja lengo ni kutofautisha na madini mengine ikiwa pamoja kuongeza uzalishaji wa chumvi bora nchini.

Naye, Mkurugenzi Mtendaji  wa Shirika ya Madini la Taifa (STAMICO) Dkt.Venance Mwase amesema kuwa miundombinu ndani ya kiwanda yamekamilika kwa asilimia kubwa.

Dkt. Mwase ameongeza kuwa , kiwanda kitakuwa na uwezo wa kupokea  chumvi ghafi kutoka kwa wazalisha kuanzia 50 hadi 60 kwa siku.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa TASPA Bi. Hawa Ghasia ameishukuru Serikali kwa kuwezesha mazingira bora ya uvunaji wa chumvi ikiwa pamoja na kupanda kwa bei ya chumvi baada ya kuwepo kwa zuio la uingizwaji wa chumvi ghafi kiholela kutoka nje ya nchi.

Kiwanda cha kuchakata chumvi mkoani Lindi pindi kitakapoanza kazi  kinatarajia kuchakataji tani 60 hadi 100 kwa siku.

Zaidi ya Watu 500 Wapoteza Maisha Kwenye Ghasia za Uchaguzi Mkuu








 

WAZIRI WA MAMBO YA NJE WA BELARUS AWASILI NCHINI KWA ZIARA YA KIKAZI

  Waziri wa Mambo ya Nje wa Jamhuri ya Belarus, Mheshimiwa Maxim Ryzhenkov, amewasili nchini kwa ziara ya kikazi ya siku tatu kuanzia Aprili...