Wednesday, April 15, 2026

RAIS SAMIA AKUTANA NA MJUMBE MAALUM WA JUMUIYA YA MADOLA IKULU DAR ES SALAAM






Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, leo tarehe 15 Aprili 2026, amekutana na kufanya mazungumzo na Mjumbe Maalum wa Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Madola (Commonwealth), ambaye pia ni Rais wa zamani wa Jamhuri ya Malawi, Mhe. Dkt. Lazarus McCarthy Chakwera, Ikulu Jijini Dar es Salaam.

Mazungumzo yao yamejikita katika kuimarisha ushirikiano wa kimataifa, kukuza maendeleo ya kijamii na kiuchumi, pamoja na kuendeleza ajenda za pamoja ndani ya Jumuiya ya Madola.

Mkutano huo unaakisi dhamira ya Tanzania kuendelea kujenga mahusiano imara ya kidiplomasia na washirika wa kimataifa, sambamba na kuimarisha nafasi yake katika jukwaa la kimataifa.

#SamiaSuluhuHassan #Tanzania #Commonwealth #Diplomasia #Maendeleo

TRC YASAFIRISHA ABIRIA 5,512,995

 

Shirika la Reli Tanzania (TRC) lilianza kutoa huduma ya usafirishaji abiria kutumia reli ya kiwango cha kimataifa (SGR) mnamo mwezi Juni 2024, toka kipindi hicho mpaka Machi 2026, abiria 5,512,995, wamesafiri kwa kutumia treni za SGR.  

Takwimu hiyo ina ujumbe mkubwa sana kimkakati kuhusu ubora na mafanikio ya huduma ya SGR, na ina maana zifuatazo:

Kwanza ni Kukubalika kwa Huduma (High public acceptance)

Abiria zaidi ya milioni 5.5 ndani ya muda mfupi inaonyesha kuwa, Wananchi wameikubali kwa kiwango cha juu kabisa, huduma ya SGR kwani mejenga imani kubwa kwa watumiaji. Ukiachana na hilo, SGR imekuwa chaguo kuu la usafiri ukilinganisha na njia nyingine na usafiri na usafirishaji, lakini kubwq zaidi hii ni ishara ya market penetration yenye mafanikio makubwa.

Pili inadhihirisha Ufanisi wa Utoaji Huduma (Service Efficiency), na kwa muktadha huo, idadi hii inaashiria kuwa, huduma inapatikana kwa uhakika na ratiba zinazingatiwa , katika kipindi chote hicho uendeshaji umekuwa ni wa kuaminika (reliable), hili la pili lina maanisha kwamba ,TRC imefanikiwa kusimamia miundombinu na uendeshaji kwa ufanisi.

Tatu, ni kudhihirika kwa Ubora wa Huduma (Customer Experience), abiria kuendelea kutumia huduma hiyo kunamaanisha, wanaridhika na usalama, mwendo na faraja aidha kuna uzoefu mzuri wa safari (customer satisfaction), la tatu lina maanisha kwamba huduma hii mpya katika sekta ndogo ya reli nchini, imeleta thamani halisi kwa mtumiaji.

Nne, Mchango wa Kiuchumi na Kijamii, huduma hii ya treni za SGR, inachochea ukuaji wa uchumi (biashara, ajira na utalii) pia inarahisisha muunganiko wa mikoa (kati ya Dar es Salaam, Morogoro na Dodoma) hili la nne linajipambanua kuwa kusafiri na treni za SGR, kunapunguza gharama na muda wa usafiri kwa wananchi.

Tano, haya ni Mafanikio ya Uwekezaji wa Serikali, na kwamba takwimu hizo za abiria katika kipindi cha muda mfupi wa huduma ya treni za SGR, inaonyesha kuwa, Uwekezaji wa Serikali kwenye SGR umeanza kuzaa matunda, kwa kuongeza huu ni mradi wenye tija (value for money) na unatekeleza dira ya maendeleo ya Taifa 2050 sambamba na Ilani ya Chama cha Mapinduzi ya mwaka 2025/30, ambayo moja ya malengo yake ni kuimarisha miundombinu ya kisasa ya usafiri na usafirishaji

Hitimisho, idadi ya abiria zaidi ya milioni 5.5 waliotumia SGR ndani ya kipindi kifupi tangu kuanza kwa huduma inaonyesha kiwango kikubwa cha kukubalika kwa huduma hiyo, ufanisi wa uendeshaji, na mchango wake muhimu katika kurahisisha usafiri, kukuza uchumi na kuboresha maisha ya wananchi. 



RAIS SAMIA AKUTANA NA RAIS WA KAMPUNI YA GRUPA ZENITH YA POLAND








Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan amekutana na kufanya mazungumzo na Rais wa Kampuni ya Grupa Zenith kutoka nchini Poland, Dkt. Aleksander Joseph Widuchi, tarehe 14 Aprili, 2026 Ikulu Dar es Salaam.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan amekutana na kufanya mazungumzo na Rais wa Kampuni ya Grupa Zenith kutoka nchini Poland, Dkt. Aleksander Joseph Widuchi, tarehe 14 Aprili, 2026 Ikulu Dar es Salaam. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiangalia kitabu kinachoelezea masuala ya Mazingira, Nishati na masuala mbalimbali ya Poland wengine pichani ni Rais wa Kampuni ya Grupa Zenith kutoka nchini Poland, Dkt. Aleksander Joseph Widuchi pamoja na Mkurugenzi Mtendaji Bi. Aleksandra Stephania Widuchi, tarehe 14 Aprili, 2026 Ikulu Dar es laam.


Tuesday, April 14, 2026

RAIS DKT.MWINYI AKAGUA MRADI WA MJI WA AFCON FUMBA, AANGALIA MAENDELEO YA UWANJA










Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Hussein Ali Mwinyi, leo Aprili 14, 2026, ameandika historia mpya baada ya kukagua maendeleo ya mradi mkubwa wa kimkakati wa Mji wa AFCON Fumba, uliopo Mkoa wa Mjini Magharibi.

Akiwa ameambatana na Waziri wa Habari, Sanaa, Utamaduni na Michezo, Riziki Pembe Juma, pamoja na wadau wa mradi huo, Rais Mwinyi alipata fursa ya kujionea kwa karibu kasi ya ujenzi wa uwanja wa kisasa wa AFCON unaojengwa na kampuni ya kimataifa ya ORKUN GROUP kutoka Uturuki.

Uwanja huo, unaotarajiwa kuwa miongoni mwa alama kuu za michezo Afrika Mashariki, unajengwa kwa viwango vya juu vinavyotambuliwa na CAF, ukiwa na uwezo wa kuchukua mashabiki zaidi ya 35,000. Mradi huu ni sehemu ya maandalizi ya michuano ya AFCON 2027, ambayo kwa mara ya kwanza itafanyika kwa ushirikiano wa Tanzania, Kenya na Uganda.

Lakini zaidi ya uwanja, mradi wa Mji wa AFCON Fumba unaibua sura mpya ya maendeleo ya kisasa Zanzibar. Rais Mwinyi alikagua pia mipango ya miundombinu itakayouzunguka uwanja huo — ikiwemo hospitali za kisasa, barabara za kiwango cha juu, migahawa, maduka makubwa (malls), na huduma nyingine muhimu zitakazobadilisha kabisa mandhari ya eneo hilo.

Ziara hiyo imeonyesha dhamira ya dhati ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuifanya Fumba kuwa kitovu cha michezo, uwekezaji na maisha ya kisasa — hatua inayotarajiwa kuongeza ajira, kukuza uchumi na kuiweka Zanzibar kwenye ramani ya kimataifa.

Kwa kasi hii ya utekelezaji, Mji wa AFCON Fumba si tu mradi wa uwanja—ni alama ya Zanzibar mpya inayokuja kwa nguvu.

Monday, April 13, 2026

SAMIA APEPERUSHA BENDERA YA USHIRIKIANO EAC, AKUTANA NA KATIBU MKUU IKULU CHAMWINO

 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan amekutana na kufanya mazungumzo na Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) Mhe. Balozi Stephen Mbundi, Ikulu ya Chamwino mkoani Dodoma tarehe 13 Aprili, 2026.



Rais wa Samia Suluhu Hassan ameendeleza diplomasia ya kimkakati baada ya kukutana na kufanya mazungumzo na Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), Stephen Mbundi, katika Ikulu ya Chamwino mkoani Dodoma leo Aprili 13, 2026.

Mazungumzo hayo yamejikita katika kuimarisha ushirikiano wa kikanda, kukuza biashara huria na kuharakisha utekelezaji wa miradi ya maendeleo inayogusa maisha ya wananchi ndani ya ukanda wa Afrika Mashariki. Viongozi hao wawili walisisitiza umuhimu wa mshikamano wa nchi wanachama wa EAC katika kukabiliana na changamoto za kiuchumi na kijamii, huku wakitazama fursa mpya za uwekezaji na miundombinu.

Katika kikao hicho, Rais Samia alisisitiza dhamira ya Tanzania kuendelea kuwa nguzo ya utulivu, amani na maendeleo ndani ya EAC, akibainisha kuwa ushirikiano madhubuti ni msingi wa mafanikio ya pamoja. Kwa upande wake, Balozi Mbundi alieleza kuridhishwa na mchango wa Tanzania katika kuendeleza ajenda za jumuiya hiyo, akiahidi kuimarisha uratibu wa sera na miradi ya kikanda.

Mkutano huo unakuja wakati ambapo nchi wanachama wa EAC zinaongeza kasi ya utekelezaji wa mikakati ya kiuchumi, ikiwa ni pamoja na kuimarisha miundombinu ya usafirishaji, biashara na uwekezaji—hatua zinazolenga kuifanya Afrika Mashariki kuwa kitovu cha ushindani wa kiuchumi barani Afrika.

Kwa ujumla, kikao hicho kinaashiria hatua nyingine muhimu katika safari ya kuijenga EAC imara, yenye mshikamano na inayowanufaisha wananchi wake kwa vitendo.



RAIS DKT. MWINYI AWAAPISHA WAKUU WA WILAYA WAPYA IKULU ZANZIBAR

 

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amewaapisha Wakuu wa Wilaya aliowateua hivi karibuni.

Hafla hiyo ya uapisho imefanyika leo tarehe 13 Aprili 2026, Ikulu Zanzibar, na kuhudhuriwa na viongozi mbalimbali wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Wakuu wa Vikosi vya Ulinzi na Usalama pamoja na wanafamilia wa Wakuu wa Wilaya walioapishwa.

Walioapishwa ni:

* Mkuu wa Wilaya ya Magharibi A, Mhe. Lailah Burhani Ngozi

* Mkuu wa Wilaya ya Mjini, Mhe. Dkt. Said Haji Mrisho

* Mkuu wa Wilaya ya Magharibi B, Mhe. Ali Abdalla Said Natepe

* Mkuu wa Wilaya ya Kaskazini A, Mhe. Riziki Daniel Yussuf

* Mkuu wa Wilaya ya Chake Chake, Mhe. Zuhura Mgeni Othman

Hafla hiyo imehudhuriwa na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Mhe. Hemed Suleiman Abdulla; Jaji Mkuu wa Zanzibar, Khamis Ramadhan Abdalla; Mwanasheria Mkuu wa Zanzibar, Dkt. Mwinyi Talib Haji; Mufti Mkuu wa Zanzibar, Sheikh Saleh Omar Kaabi; Wakuu wa Mikoa pamoja na baadhi ya Mawaziri wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.



Sunday, April 12, 2026

WABUNGE WAJENGEWA UWEZO WA HAKI MADINI NA HAKI ARDHI

 










Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini imepatiwa mafunzo maalum kuhusu Sheria, Kanuni na Miongozo ya Sekta ya Madini, kwa lengo la kuongeza uelewa hususan juu ya tofauti kati ya Haki ya Ardhi na Haki ya Madini.

Mafunzo hayo yamefanyika katika Ukumbi wa Tanzanite, Makao Makuu ya Tume ya Madini, jijini Dodoma.

Akizungumza katika semina hiyo, Waziri wa Madini, Mhe. Anthony Mavunde, amesema kuwa umiliki wa haki ya madini na haki ya ardhi ni mambo mawili tofauti kisheria, na kwamba mwenye leseni ya madini haruhusiwi kuanza shughuli za uchimbaji bila kufikia makubaliano na mmiliki wa ardhi husika.

Amefafanua kuwa, kwa mujibu wa Sheria, leseni ya madini inaweza kutolewa katika eneo lolote, lakini utekelezaji wake unahitaji ridhaa au makubaliano na mwenye haki ya ardhi. Hata hivyo, iwapo makubaliano hayatapatikana, Waziri ana mamlaka ya kuruhusu shughuli za uchimbaji kuendelea kwa kuzingatia sheria.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mhe. Subira Mgalu, ameipongeza Wizara ya Madini kwa kuandaa mafunzo hayo, akieleza kuwa yameongeza uelewa na kuwajengea wabunge uwezo wa kusimamia vyema sekta hiyo.

Wasilisho kuhusu haki ya madini na haki ya ardhi limetolewa na Mkurugenzi wa Huduma za Sheria kutoka Wizara ya Madini, Dkt. Arnold Gisase, ambaye ameeleza kuwa mtu anaweza kumiliki haki ya madini bila kuwa mmiliki wa ardhi, na kwamba umiliki wa ardhi pekee haumruhusu mtu kufanya shughuli za madini bila leseni husika.

Dkt. Gisase pia amebainisha changamoto zinazojitokeza, ikiwemo uelewa mdogo wa wananchi kuhusu haki na wajibu wao, kutokuelewa taratibu za uthamini na fidia, ucheleweshaji wa malipo ya fidia, pamoja na baadhi ya wamiliki wa ardhi kudai kuwa sehemu ya umiliki wa leseni za madini.

Naye, Mwanasheria kutoka Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Method Akilimali, amesisitiza kuwa fidia kwa mmiliki wa ardhi lazima ilipwe kabla ya kuanza kwa shughuli za utafiti au uchimbaji.

Ameongeza kuwa sheria inamtaka mmiliki wa leseni kurejesha eneo katika hali yake ya awali baada ya shughuli za madini kukamilika. Aidha, ameeleza kuwa ardhi yote nchini ni mali ya umma chini ya usimamizi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kama mdhamini.

Amesema pia fidia inapaswa kulipwa ndani ya miezi sita; kuchelewa hulazimu kulipwa riba, na endapo itazidi miaka miwili tangu uthamini kufanyika, tathmini hiyo hupoteza uhalali.

Akizungumzia muundo wa leseni, Mkurugenzi Mtendaji wa Tume ya Madini, Mhandisi Ramadhani Lwamo, amesema zipo aina kuu tatu za leseni ambazo ni leseni ya utafiti, uchimbaji mdogo na uchimbaji mkubwa ambapo kwa leseni ya uchimbaji mdogo Mtanzania pekee mwenye umri wa kuanzia miaka 18 ndiyo anaruhusiwa kuomba.

Mhandisi Lwamo amesema leseni kubwa na ya kati inaruhusiwa kuombwa na mtu yoyote na kwa sasa kuna mfumo wa kuomba leseni bila kufika ofisi za madini.

Mafunzo hayo yamelenga kuwawezesha wabunge kuelewa kwa kina masuala ya kisheria na kiutendaji katika sekta ya madini ili kuboresha usimamizi na maamuzi yenye tija kwa maendeleo ya taifa.

RAIS SAMIA AKUTANA NA MJUMBE MAALUM WA JUMUIYA YA MADOLA IKULU DAR ES SALAAM

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, leo tarehe 15 Aprili 2026, amekutana na kufanya mazungumzo na Mjumbe...