Saturday, July 04, 2026

UCHUMI WA TAIFA UNATEGEMEA UHIFADHI ASEMA MCHECHU AKIZINDUA GREAT RUAHA MARATHON 2026










RUAHA, IRINGA – Msajili wa Hazina na Mlezi wa Great Ruaha Marathon, Bw. Nehemiah Mchechu, ambaye alimwakilisha Mgeni Rasmi, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mwigulu Nchemba, amesema kuwa uhifadhi wa mazingira ni nguzo muhimu ya ukuaji wa uchumi wa Taifa na ustawi wa wananchi.

Akizindua rasmi Great Ruaha Marathon 2026 leo Julai 4, 2026 katika Hifadhi ya Taifa Ruaha, Bw. Mchechu alisema Mto Ruaha Mkuu ni moja ya vyanzo muhimu vya uhai nchini, ukiwezesha shughuli za kilimo, ufugaji, uzalishaji wa umeme pamoja na kuhifadhi mfumo wa ikolojia wa Hifadhi ya Taifa Ruaha.

Alisisitiza kuwa kulinda mazingira na vyanzo vya maji si jukumu la Serikali pekee, bali ni wajibu wa kila Mtanzania kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.

"Tunataka Watanzania wengi zaidi watembelee hifadhi zetu, wajivunie urithi tulionao na wawe mabalozi wa utalii wa nchi yao," amesema Mchechu.

Kwa upande wake, Kamishna wa Uhifadhi wa TANAPA, Massana Gibril Mwishawa, amesema utalii wa michezo umeendelea kuwa nyenzo muhimu ya kuitangaza Tanzania duniani, kuvutia watalii na wawekezaji, pamoja na kukuza biashara na uchumi wa Taifa.

Ameeleza kuwa TANAPA imejipanga kuendeleza utalii wa michezo kama zao jipya la kimkakati litakaloongeza mchango wa sekta ya utalii katika maendeleo ya nchi.

Naye Mratibu wa Great Ruaha Marathon, Hamim Kilahama, amesema mbio hizo si mashindano ya riadha pekee bali ni jukwaa la kuhamasisha jamii kulinda mazingira, kuhifadhi vyanzo vya maji vya Mto Ruaha Mkuu na kuitangaza Kanda ya Kusini kama kitovu cha utalii.

Amebainisha kuwa kwa mwaka wa tano mfululizo, Great Ruaha Marathon imeendelea kufungua fursa mpya za kuitangaza Hifadhi ya Taifa Ruaha kupitia utalii wa michezo, huku ikichochea maendeleo ya jamii na uchumi wa maeneo yanayozunguka hifadhi hiyo.

Hifadhi ya Taifa Ruaha, ambayo ni miongoni mwa hifadhi kubwa zaidi barani Afrika, inaendelea kuwa hazina ya kipekee ya utalii ikiwa na wanyamapori wengi wakiwemo tembo, simba, chui, mbwa mwitu wa porini, twiga, nyati na mamia ya aina za ndege wanaovutia wageni kutoka duniani kote.

Great Ruaha Marathon imeendelea kuthibitisha kuwa michezo, uhifadhi na utalii vinaweza kwenda sambamba katika kujenga uchumi imara, kulinda rasilimali za Taifa na kuitangaza Tanzania kimataifa.

 

MAKAMU WA RAIS DKT. NCHIMBI AMTEMBELEA JAJI MSTAAFU JOSEPH WARIOBA, AMJULIA HALI

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi amemtembelea na kumjulia hali, aliyewahi kuwa Waziri Mkuu na Makamu wa Kwanza wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Jaji. Joseph Sinde Warioba, katika makazi yake, Mbezi Juu Jijini Dar es Salaam.



Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi amemtembelea na kumjulia hali, aliyewahi kuwa Waziri Mkuu na Makamu wa Kwanza wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Jaji. Joseph Sinde Warioba, katika makazi yake, Mbezi Juu Jijini Dar es Salaam.

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi, amemtembelea na kumjulia hali aliyekuwa Waziri Mkuu na Makamu wa Kwanza wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Jaji Mstaafu Joseph Sinde Warioba, katika makazi yake yaliyopo Mbezi Juu, jijini Dar es Salaam.

Ziara hiyo imeonesha heshima na kuthamini mchango mkubwa wa viongozi wastaafu walioitumikia nchi kwa uadilifu na uzalendo. Katika mazungumzo yao, viongozi hao walipata fursa ya kubadilishana mawazo kuhusu masuala mbalimbali yanayohusu maendeleo ya Taifa na ustawi wa wananchi.

Hatua ya Makamu wa Rais kumtembelea Jaji Mstaafu Warioba imepokelewa kama ishara ya kuenzi utumishi wa viongozi walioweka msingi imara wa uongozi na utawala nchini, huku ikidhihirisha umuhimu wa kuendelea kuwajali na kuwathamini wazee wa Taifa kwa mchango wao katika kujenga Tanzania ya leo.


Wednesday, July 01, 2026

RAIS DKT. SAMIA AONGOZA MAADHIMISHO YA MIAKA 30 YA TRA

 
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye Maadhimisho ya miaka 30 ya kuanzishwa kwa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) katika ukumbi wa Mlimani City Jijini Dar es Salaam.



Viongozi, wafanyabiashara pamoja na wageni mbalimbali wakiwa kwenye Maadhimisho ya miaka 30 Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) katika ukumbi wa Mlimani City Jijini Dar es Salaam, tarehe 01 Julai, 2026



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akisikiliza historia ya miaka 30 ya Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) baada ya kuwasili katika ukumbi wa Mlimani City Jijini Dar es Salaam, tarehe 01 Julai, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, leo Julai 1, 2026, ameongoza Maadhimisho ya Miaka 30 ya kuanzishwa kwa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) yaliyofanyika katika Ukumbi wa Mlimani City, jijini Dar es Salaam.

Mara baada ya kuwasili katika ukumbi huo, Rais Samia alitembelea maonesho maalumu yaliyoandaliwa na TRA na kupata maelezo kuhusu historia ya mamlaka hiyo, mafanikio yaliyopatikana katika kipindi cha miaka 30 pamoja na mchango wake katika kuongeza mapato ya Serikali na kuchochea maendeleo ya kiuchumi nchini.

Maadhimisho hayo yamewakutanisha viongozi wa Serikali, taasisi za umma na binafsi, wadau wa kodi pamoja na washirika wa maendeleo kwa lengo la kuadhimisha mafanikio ya TRA tangu kuanzishwa kwake na kujadili mikakati ya kuendelea kuimarisha ukusanyaji wa mapato kwa maendeleo endelevu ya Taifa.

Kwa kipindi cha miaka 30, TRA imeendelea kuwa mhimili muhimu katika ukusanyaji wa mapato ya ndani, hatua iliyowezesha Serikali kugharamia utekelezaji wa miradi mikubwa ya maendeleo katika sekta mbalimbali zikiwemo elimu, afya, miundombinu, maji na huduma nyingine za kijamii.

Maadhimisho hayo pia yametoa fursa ya kutafakari mafanikio yaliyofikiwa, changamoto zilizopo na kuweka mikakati ya kuifanya TRA iendelee kuwa taasisi imara, bunifu na inayotoa huduma bora kwa walipakodi, sambamba na kuimarisha uchumi wa Taifa.

Tuesday, June 30, 2026

DKT MWIGULU: SERIKALI INAENDELEA KUIMARISHA MAZINGIRA YA BIASHARA NA UWEKEZAJI







Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba amesema Serikali itaendelea kuimarisha mazingira ya biashara, uwekezaji na viwanda kwa kufanya mageuzi ya sera, sheria, kanuni na mifumo ya utoaji huduma ili kuiwezesha sekta binafsi kuwa mhimili wa ukuaji wa uchumi na utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Amesema hayo leo, Jumanne Juni 30, 2026, alipokuwa Mgeni Rasmi katika Kongamano la Biashara na Uwekezaji la Mwaka 2026 lililoandaliwa na Chemba ya Taifa ya Biashara Tanzania (TNCC) katika Hoteli ya Johari Rotana, jijini Dar es Salaam.

Waziri Mkuu amesema Serikali imejipanga kuhama kutoka katika mfumo wa kudhibiti biashara kwenda katika mfumo wa kuwezesha biashara kwa kuendelea kuboresha mazingira ya uwekezaji, kupunguza urasimu, kuimarisha matumizi ya teknolojia na kuongeza ufanisi wa taasisi zinazotoa huduma kwa wafanyabiashara na wawekezaji.

"Ajenda ya sekta binafsi ni ajenda ya Taifa. Hatuwezi kufikia malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 bila sekta binafsi yenye nguvu, inayowezeshwa na inayoshirikiana kwa karibu na Serikali," amesema.

Aidha, amesema Serikali itaendelea kupokea na kufanyia kazi mapendekezo ya sekta binafsi yanayolenga kuboresha mazingira ya biashara, kuondoa vikwazo vinavyokwamisha uwekezaji na kuongeza ushindani wa bidhaa na huduma za Tanzania katika masoko ya kikanda na kimataifa.

Waziri Mkuu amesema amani, utulivu na mshikamano wa Taifa ni msingi muhimu wa maendeleo ya uchumi, hivyo kila Mtanzania ana wajibu wa kuendelea kuvilinda ili kuwezesha biashara, uwekezaji na uzalishaji kustawi.

Awali, Waziri wa Viwanda na Biashara, Judith Kapinga alisema Serikali inaendelea kujenga mazingira rafiki ya biashara kwa kuimarisha ushirikiano na sekta binafsi, kukuza matumizi ya teknolojia na kuhakikisha taasisi za umma zinafanya kazi kwa mtazamo wa kuwezesha biashara badala ya kuzikwamisha.

Kwa upande wake, Rais wa Chemba ya Taifa ya Biashara Tanzania (TNCC), Bw. Vincent Minja alisema chemba hiyo imeendelea kufanya mageuzi ya kiutawala na kidijitali yanayolenga kuboresha huduma kwa wanachama, kuimarisha uwakilishi wa sekta binafsi na kuongeza ushindani wa biashara za Tanzania.

Katika kongamano hilo, Waziri Mkuu alizindua rasmi Mfumo wa Kidijitali wa Chemba ya Taifa ya Biashara Tanzania, utakaorahisisha utoaji wa huduma mbalimbali za chemba hiyo, ikiwemo usajili wa wanachama, utoaji wa vyeti vya asili ya bidhaa na huduma nyingine za biashara kwa njia ya mtandao.

Aidha, alishuhudia utiaji saini wa hati mbalimbali za makubaliano ya ushirikiano kati ya Chemba ya Taifa ya Biashara Tanzania na taasisi za umma pamoja na sekta binafsi, hatua inayolenga kuimarisha biashara, uwekezaji, utafiti, ubunifu na maendeleo ya sekta binafsi nchini.

Kongamano hilo lilihudhuriwa na viongozi wa Serikali, taasisi za umma, sekta binafsi, washirika wa maendeleo, mabalozi, wawekezaji na wafanyabiashara kutoka ndani na nje ya nchi.

Monday, June 29, 2026

PROF. SHEMDOE AWAASA WANAFUNZI KUENDELEZA VIPAJI VYAO VYA MICHEZO, SANAA








Awataka kuwa na nidhamu na kusoma kwa bidii

Na OWM - TAMISEMI, Iringa

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM-TAMISEMI) Mhe. Prof. Riziki Shemdoe amewaasa wanafunzi walioshiriki mashindano ya UMISSETA mwaka 2026 kuendeleza vipaji vya michezo na Sanaa walivyonavyo kwani vitawasaidia katika maisha yao ya baadaye, huku akiwataka kuzingatia nidhamu na kusoma kwa bidii ili  kufikia ndoto zao na kutoa mchango katika maendeleo ya taifa.

Prof. Shemdoe ametoa wito huo kwa wanafunzi leo Juni 28, 2026 mjini Iringa katika Viwanja vya Shule ya Sekondari Lugalo, wakati akifunga mashindano ya UMISSETA kwa mwaka wa 2026.

“Nina wasihi muendelee kuwa na nidhamu, kujituma katika masomo yenu na kuendeleza vipaji vyenu vya michezo na sanaa, msiviache vipaji vyenu kwani hata mimi juzi tulipokuwa tunapokea Mwenge wa Uhuru Lushoto nilijikuta nikikumbushia kipaji changu cha kupiga ngoma za utamaduni na kuimba kwa umahiri,” amesisitiza Prof. Shemdoe.

Prof. Shemdoe amewahakikishia wanafunzi hao kuwa, Serikali itaendelea kuweka mazingira bora ya kuhakikisha vipaji vya wanafunzi vinaibuliwa, vinatambuliwa, vinakuzwa ili kuwanufaisha na kulinufaisha taifa kupitia ushiriki wao katika kuliwakilisha taifa kwenye mashindano ya michezo na Sanaa ndani na nje ya nchi.

Aidha, Prof. Shemdoe ametumia fursa hiyo kumpongeza Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuipa kipaumbele sekta ya elimu, michezo, sanaa na maendeleo ya vijana kwenye ajenda kuu ya taifa na kuongeza kuwa, uwekezaji huo unaendelea kuweka msingi imara wa kuibua na kuendeleza vipaji vya watoto na vijana wa Tanzania.

 Kwa upande wake Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu - TAMISEMI anayeshughulikia Elimu Bw. Atupele Mwambene amesema kuwa, ushiriki wa wanafunzi katika michezo mbalimbali ya UMITASHUMTA na UMISSETA umeendelea kuwa jukwaa muhimu la kitaifa la kuibua vipaji, kuimarisha afya, kujenga urafiki na kuendeleza umoja wa kitaifa miongoni mwa wanafunzi. 

Naye Mwakilishi wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Bi. Leah Kihimbi amemuhakikishia Prof. Shemdoe kuwa wizara yake itatekeleza ipasavyo jukumu la kuibua kuendeleza vipaji na vipawa vinavyotokana na mashindano hayo ya sanaa na michezo shuleni. 

Mwakilishi wa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar ambaye ni Afisa Mdhamini Bw. Mohamed Nassoro Salimu amesema Zanzibar inakwenda kujipanga ili kuleta ushindani mkubwa katika mashindano ya mwakani, ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa maelekezo ya Rais wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi ya kufanya mageuzi katika sekta ya michezo.

Akitoa neno la shukrani, Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu - TAMISEMI Bw. Adolf Ndunguru amewashukuru maafisa elimu, wakuu wa shule, walimu, waratibu wa michezo na walezi wa wanafunzi, kwa kazi kubwa walioifanya ya kuwaandaa na kuwaleta wanafunzi katika mashindano ambayo yamewawezesha kujifunza thamani ya nidhamu, ushindani wa haki, uvumilivu, uzalendo na mshikamano wa kitaifa.

Sunday, June 28, 2026

RAIS SAMIA AKUTANA NA ALIKO DANGOTE; AENDELEA KUFUNGUA MILANGO YA FURSA ZA UWEKEZAJI TANZANIA

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye picha na Mfanyabiashara kutoka nchini Nigeria ambaye pia ni Mwanzilishi na Mmiliki wa Dangote Group, Alhaji Aliko Dangote, Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 28 Juni, 2026.









Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, leo Juni 28, 2026, amekutana na kufanya mazungumzo na mfanyabiashara mashuhuri kutoka Nigeria na Mwanzilishi wa Dangote Group, Alhaji Aliko Dangote, pamoja na ujumbe wake katika Ikulu, Dar es Salaam.

Mkutano huo unaakisi juhudi za Rais Samia za kuendelea kuimarisha diplomasia ya uchumi kwa kuvutia wawekezaji wakubwa duniani, kuongeza ushirikiano wa kibiashara na kufungua fursa mpya za maendeleo kwa Watanzania.

Kwa miaka ya hivi karibuni, Tanzania imeendelea kujijengea sifa ya kuwa moja ya maeneo yenye mazingira rafiki ya uwekezaji barani Afrika. Kukutana kwa Rais Samia na Aliko Dangote kunatazamwa kama ishara ya kuongezeka kwa imani ya wawekezaji wa kimataifa katika uchumi wa Tanzania.

Uwekezaji wa sekta binafsi una mchango mkubwa katika kukuza viwanda, kuongeza ajira, kuimarisha uzalishaji na kuongeza mapato ya Taifa. Hivyo, mazungumzo ya viongozi hawa yanatoa matumaini ya ushirikiano mpana zaidi wenye manufaa kwa pande zote mbili.

Hatua hizi zinaendelea kuiweka Tanzania katika nafasi nzuri ya kuvutia mitaji, teknolojia na ubunifu unaochochea ukuaji wa uchumi jumuishi na maendeleo endelevu.

Friday, June 26, 2026

RAIS SAMIA APONGEZA MPANGO WA HEIDELBERG MATERIALS KUPANUA UWEKEZAJI NCHINI




Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, amepokea ujumbe wa Kampuni ya Heidelberg Materials, wazalishaji wa saruji za Simba Cement na Twiga Cement, ulioongozwa na Mjumbe wa Bodi ya Uongozi na Mtendaji Mkuu wa Afrika, Mediterranean na Asia Magharibi, Bw. Hakan Gurdal, katika mazungumzo yaliyofanyika Ikulu, Dar es Salaam, tarehe 26 Juni 2026.

Katika kikao hicho, Heidelberg Materials imewasilisha mpango wake wa kupanua uwekezaji nchini Tanzania, ukiwa na lengo la kuongeza uzalishaji wa saruji ili kukidhi mahitaji yanayoongezeka ya sekta ya ujenzi na miundombinu.

Mbali na kuongeza uwezo wa uzalishaji, kampuni hiyo imeeleza dhamira ya kuwekeza zaidi katika matumizi ya nishati safi pamoja na kutekeleza mradi wa usindikaji wa taka za majiji kwa ajili ya uzalishaji, hatua inayolenga kuimarisha ulinzi wa mazingira na kuchochea maendeleo ya uchumi wa kijani.

Mpango huo unatarajiwa kuimarisha sekta ya ujenzi, kuongeza ajira, kukuza shughuli za viwanda na kuendelea kuiweka Tanzania kuwa kitovu muhimu cha uwekezaji katika ukanda wa Afrika Mashariki.

Hatua hiyo inaendana na juhudi za Serikali ya Awamu ya Sita za kuvutia uwekezaji wenye tija, kuongeza thamani ya rasilimali za nchi na kuharakisha maendeleo ya uchumi kupitia sekta ya viwanda.


UCHUMI WA TAIFA UNATEGEMEA UHIFADHI ASEMA MCHECHU AKIZINDUA GREAT RUAHA MARATHON 2026

RUAHA, IRINGA – Msajili wa Hazina na Mlezi wa Great Ruaha Marathon , Bw. Nehemiah Mchechu , ambaye alimwakilisha Mgeni Rasmi, Waziri Mkuu w...