Friday, August 28, 2026

BUNGE LAMTHIBITISHA NDEJEMBI KWA ASILIMIA 100 UMAKAMU WA RAIS.










Waziri Mkuu asema anatosha, kiti kimempata mtu sahihi wa kumsaidia Mheshimiwa Rais.

BUNGE la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania leo (Ijumaa, Agosti 28, 2026) limemthibitisha Mheshimiwa Deogratius Ndejembi kuwa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mheshimiwa Ndejembi amepitishwa kwa asilimia 100 ya kura zote 324 zilizopigwa na waheshimiwa wabunge, ambapo amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa imani aliyoionesha kwake kwa kumteua kuwa Makamu wa Rais na katika nafasi nyingine mbalimbali za uongozi.

Pia Mheshimiwa Ndejembi amelishukuru Bunge kwa imani kubwa waliyompa kiasi cha kumpigia kura kwa asilimia mia moja.

Mapema akiwasilisha hoja ya kuthibitisha uteuzi wa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba amesema Mheshimiwa Deogratius Ndejembi anatosha na ni mtu sahihi wa kumsaidia Mheshimiwa Rais katika nafasi ya Makamu wa Rais, 

akiitaja kuwa ni nafasi yenye dhamana na majukumu makubwa katika uongozi wa nchi.

"Majukumu hayo yanahitaji mtu mwenye uzoefu wa uongozi, uelewa mpana wa shughuli za Serikali, uwezo wa kufanya kazi kwa karibu na Rais, busara katika kushughulikia masuala ya kitaifa, pamoja na uwezo wa kuratibu na kufuatilia utekelezaji wa majukumu mbalimbali ya Serikali," amesema Dkt. Mwigulu.

"Mheshimiwa Rais amemteua Mheshimiwa Deogratius John Pancras Ndejembi kwa kuzingatia, pamoja na mambo mengine, uzoefu alioujenga katika uongozi wa kisiasa na katika nafasi mbalimbali za Serikali," ameongeza Waziri Mkuu.

Dkt. Mwigulu amesisitiza kuwa uzoefu wa uongozi alionao Mheshimiwa Deogratius Ndejembi unadhihirisha kuwa ni mtu sahihi kutumikia wadhifa wa Makamu wa Rais.

"Mheshimiwa Deogratius John Pancras Ndejembi si mgeni katika uongozi wa Umma na katika siasa za nchi yetu. Kabla ya kuwa Mbunge, Mheshimiwa Ndejembi alihudumu kama Mkuu wa Wilaya katika Wilaya ya Kongwa. Mheshimiwa Spika, baada ya kuchaguliwa kuwa Mbunge, Mheshimiwa Ndejembi ameendelea kuaminiwa na Mheshimiwa Rais na kupewa majukumu mbalimbali ndani ya Serikali."

"Amehudumu katika nafasi ya Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora; Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa; Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu; Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, kabla ya kuhudumu kama Waziri wa Nishati," ameongeza Waziri Mkuu.

Dkt. Mwigulu amesema katika kipindi ambacho amehudumu ndani ya Serikali, Mheshimiwa Ndejembi ameonesha uwezo wa kubeba majukumu mbalimbali na kufanya kazi katika sekta zenye mahitaji na changamoto zinazotofautiana, akisisitiza kuwa uzoefu huo ni muhimu kwa Makamu wa Rais ambaye, kwa nafasi yake, anatakiwa kuwa tayari kumsaidia Rais katika masuala mbalimbali ya Jamhuri ya Muungano na kutekeleza majukumu yoyote atakayokabidhiwa kwa mujibu wa Katiba.

"Kwa kuzingatia majukumu ya Kikatiba ya Makamu wa Rais niliyoyaeleza, pamoja na uzoefu wa kisiasa, kiutawala na kiutendaji wa Mheshimiwa Deogratius John Pancras Ndejembi, Serikali inaamini kuwa ana uwezo wa kutekeleza kwa uaminifu na ufanisi majukumu ya nafasi ya Makamu wa Rais na kumsaidia Mheshimiwa Rais katika kuendeleza shughuli za Serikali na maendeleo ya Taifa letu," amefafanua Dkt. Mwigulu.

RAIS SAMIA AWAAGA WANAFUNZI WA SAMIA SCHOLARSHIP EXTENDED WANAOKWENDA MASOMONI IRELAND NA URUSI

 

Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania akiwa kwenye mazungumzo na wanafunzi walionufaika na Ufadhili wa Samia Scholarship Extended katika Sayansi ya Data, Akili Unde na Sayansi Shirikishi, Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 28 Agosti, 2026. Mhe. Rais Dkt. Samia alizungumza na kuagana na wanafunzi hao ambao wanaoenda masomoni nchini Ireland na Urusi












Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, amefanya mazungumzo na kuwaaga wanafunzi walionufaika na Samia Scholarship Extended wanaokwenda kuendelea na masomo nchini Ireland na Urusi, katika hafla iliyofanyika Ikulu jijini Dar es Salaam, Agosti 28, 2026.

Wanafunzi hao watapata fursa ya kujiendeleza katika maeneo ya kimkakati ya Sayansi ya Data, Akili Unde (Artificial Intelligence) na Sayansi Shirikishi, ikiwa ni sehemu ya jitihada za Serikali ya Awamu ya Sita za kuwekeza katika maarifa, teknolojia na rasilimali watu yenye ujuzi unaoendana na mahitaji ya dunia ya sasa na yajayo.

Mazungumzo ya Mhe. Rais na wanafunzi hao yamebeba ujumbe wa matumaini na dhamira ya Tanzania ya kuwajengea vijana uwezo wa kushindana katika medani za kimataifa, huku wakitarajiwa kurejesha maarifa na ujuzi watakaoupata kwa manufaa ya Taifa.

Kupitia Samia Scholarship Extended, Serikali inaendelea kufungua milango ya elimu ya kiwango cha juu kwa vijana wa Kitanzania na kuandaa kizazi cha wataalamu kitakachochangia katika mageuzi ya kidijitali, ubunifu na maendeleo endelevu ya Taifa.

Safari yao kwenda Ireland na Urusi si safari ya elimu pekee, bali ni uwekezaji katika mustakabali wa Tanzania.

Thursday, August 27, 2026

WAZIRI MKUU DKT. MWIGULU AMPONGEZA NDEJEMBI, AMSIFIA KWA UADILIFU NA UCHAPAKAZI







Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba, amempongeza Mhe. Deogratius John Ndejembi kwa kuaminiwa na Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, pamoja na vyombo vya maamuzi vya Chama Cha Mapinduzi (CCM), kuelekea kushika dhamana ya Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Akizungumza Bungeni jijini Dodoma leo, Alhamisi, Agosti 27, 2026, wakati wa kipindi cha Maswali na Majibu kwa Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu amesema Ndejembi amejijengea rekodi ya kuwa kiongozi mahiri, makini na mchapakazi, anayetekeleza majukumu yake kwa bidii kwa lengo la kuleta manufaa kwa Watanzania.

“Deogratius Ndejembi kama kiongozi ni kiongozi mahiri sana, ni kiongozi makini, kiongozi mchapakazi anayefanya kazi bila kuchoka ili Watanzania waweze kupata manufaa.” amesema Dkt. Mwigulu.

Waziri Mkuu pia amempongeza Rais Samia kwa kutambua uwezo na sifa za kiuongozi za Ndejembi, akieleza kuwa pamoja na uchapakazi wake, ana sifa za unyenyekevu, upole na utu, ambazo ni muhimu katika kubeba dhamana kubwa ya kitaifa.

Aidha, Dkt. Mwigulu amemhakikishia Ndejembi ushirikiano kutoka kwake na Mawaziri wenzake katika utekelezaji wa majukumu yake, hususan katika kusimamia na kutekeleza maelekezo ya Rais Samia yanayolenga kuendeleza ujenzi wa Tanzania.

Kauli hiyo inaonesha imani katika uwezo, uzoefu na sifa za kiuongozi za Ndejembi, huku ikisisitiza umuhimu wa mshikamano na ushirikiano wa viongozi katika kuendeleza utekelezaji wa mipango ya maendeleo ya Taifa.

Wednesday, August 26, 2026

NCHIMBI AFUKUZWA CCM, NDEJEMBI ARITHI MIKOBA


Halmashauri Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) imefanya maamuzi muhimu yanayofungua sura mpya katika uongozi wa chama na Serikali, kufuatia kujiuzulu kwa Dkt. Emmanuel Nchimbi katika nafasi ya Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Akizungumza na waandishi wa habari katika Ofisi Ndogo za CCM, Lumumba jijini Dar es Salaam, Jumatano, Agosti 26, 2026, Katibu Mkuu wa CCM, Dkt. Asha-Rose Migiro, amesema Halmashauri Kuu, baada ya kupitia taarifa zilizowasilishwa pamoja na Katiba ya CCM, imeamua kumvua uanachama Dkt. Nchimbi kutokana na kile kilichoelezwa kuwa ukiukwaji wa maadili.

Uamuzi huo unafuatia hatua ya Dkt. Nchimbi kuwasilisha kwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ombi la kujiuzulu nafasi ya Makamu wa Rais kuanzia Septemba 4, 2026, pamoja na kutangaza kustaafu shughuli za kisiasa.

Katika barua yake, Dkt. Nchimbi alimshukuru Rais Samia, CCM pamoja na Watanzania kwa imani na ushirikiano alioupata katika kipindi cha utumishi wake, huku akieleza dhamira yake ya kuendelea kuwa raia mwema na kulitumikia Taifa kwa namna nyingine.

NDEJEMBI APITISHWA

Katika kuhakikisha mwendelezo wa uongozi, Halmashauri Kuu ya CCM imepitisha jina la Deogratius Ndejembi, Waziri wa Nishati, kwa ajili ya hatua zinazofuata kuelekea kujaza nafasi ya Makamu wa Rais.

Kupitishwa kwa jina hilo kunafungua njia kwa taratibu zinazofuata za kikatiba, katika kuhakikisha nafasi hiyo inajazwa na shughuli za Serikali zinaendelea kwa utulivu.

Dkt. Nchimbi anaondoka akiwa na historia ndefu ya utumishi ndani ya CCM na Serikali, ikiwemo kuwa Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa, Mwenyekiti wa UVCCM, Katibu Mkuu wa CCM na baadaye Makamu wa Rais.

Maamuzi haya yanaashiria mabadiliko yenye mwendelezo wa uongozi, huku taasisi za chama na Serikali zikiendelea kutekeleza wajibu wake kwa mujibu wa taratibu zilizowekwa.

TANZANIA, CHINA ZAFUNGUA SURA MPYA YA USHIRIKIANO WA MASHIRIKA YA UMMA

Msajili wa Hazina, Nehemiah Mchechu, jijini Dar es Salaam, akifuatilia kwa makini wa akiwa katika mkutano na ujumbe wa wataalamu kutoka SASAC.


Tanzania na China zinatarajia kufungua sura mpya ya ushirikiano katika usimamizi na maendeleo ya mashirika ya umma, kupitia makubaliano yatakayoweka msingi wa kubadilishana uzoefu, utaalamu na kujenga uwezo wa taasisi za Serikali.

Hatua hiyo inakuja wakati Ofisi ya Msajili wa Hazina (OTR) ikiwa katika hatua za mwisho za kukamilisha hati mbili za makubaliano ya ushirikiano (MoU) na Tume ya Usimamizi wa Mali za Serikali za China (SASAC) pamoja na Jumuiya ya China ya Mageuzi na Maendeleo ya Mashirika (CERDS).

Akizungumza jijini Dar es Salaam, Jumatano Agosti 26, 2026, wakati wa mkutano na ujumbe wa wataalamu kutoka China, Msajili wa Hazina, Nehemiah Mchechu, alisema makubaliano hayo yanatarajiwa kukamilika ifikapo Ijumaa au Jumatatu ijayo.

Mchechu alisema ushirikiano huo utafungua fursa kwa taasisi za umma za Tanzania na China kubadilishana ujuzi na uzoefu katika maeneo ya utafiti, kujenga uwezo wa taasisi, sera, utawala bora, mageuzi ya mashirika ya umma na tathmini ya utendaji.

Aidha, Tanzania inatarajia kutumia ushirikiano huo kujifunza kutokana na uzoefu wa China katika usimamizi wa mali za Serikali, uendeshaji wa mashirika ya umma kwa kuzingatia misingi ya soko na namna ya kuongeza ufanisi na thamani ya mtaji wa Serikali.

“Kupitia uhusiano wetu wa pande mbili na SASAC, tunalenga kujifunza namna China ilivyofanikiwa kufanya mageuzi na kuelekeza mtaji wa Serikali katika sekta muhimu za kimkakati ili kuchochea ukuaji wa uchumi wa taifa,” alisema Mchechu.

Kwa sasa, OTR inasimamia taasisi za umma 308, zikiwamo 252 ambazo Serikali inamiliki hisa nyingi na 56 ambazo Serikali ina hisa chache.

Kwa upande wake, Rais wa CERDS, Peng Huagang, alisema uzoefu wa China umeonesha kuwa mashirika ya umma yanaweza kuendeshwa kwa misingi ya soko na ushindani huku yakiendelea kutekeleza majukumu yake ya kimkakati kwa taifa.

Alisema mageuzi hayo yanalenga kujenga mashirika yaliyo imara zaidi, yenye ufanisi na uwezo wa kushindana, sambamba na kuhakikisha mali na mitaji ya Serikali inalindwa na kuongezeka thamani.

“Mageuzi yanayozingatia misingi ya soko ndiyo njia ya msingi ya kuongeza ushindani wa mashirika ya umma, na kuyawezesha kufanya kazi kwa ufanisi sambamba na aina nyingine za umiliki,” alisema Peng.

Alisema ushirikiano huo pia unaendeleza uhusiano wa muda mrefu kati ya Tanzania na China na unaendana na utekelezaji wa ahadi zilizowekwa kupitia Jukwaa la Ushirikiano kati ya China na Afrika (FOCAC).

FURSA ZA USHIRIKIANO

Sura hiyo mpya ya ushirikiano pia inatarajiwa kufungua fursa katika sekta za kimkakati, ikiwamo miundombinu, reli, bandari, usafiri wa anga, uhandisi, teknolojia, viwanda na usafirishaji wa mizigo.

Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA), Dkt. Boniphace Nobeji, alisema uboreshaji wa utendaji na ufanisi wa bandari una nafasi kubwa katika kukuza biashara na maendeleo ya kiuchumi ya Tanzania pamoja na ukanda wa Afrika Mashariki na Kati.

“Tunaamini ustawi wa taifa lolote unatokana na biashara, na sehemu kubwa ya biashara inawezeshwa na bandari zenye ufanisi. Hakuna shaka kwamba maboresho katika utendaji na ufanisi wa TPA yataharakisha maendeleo ya kiuchumi ya Afrika Mashariki na Kati,” alisema Dkt. Nobeji.

Alitaja maeneo yanayoweza kunufaika na ushirikiano huo kuwa ni pamoja na uendelezaji wa bandari kavu, uhamishaji wa teknolojia, ujenzi wa uwezo na kujifunza kutokana na uzoefu wa China katika usimamizi wa bandari.

Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Reli Tanzania (TRC), Mhandisi Machibya Shiwa, alitaja fursa katika vituo vya usafirishaji wa mizigo, huduma za usafirishaji wa mizigo, kongani za viwanda zinazounganishwa na reli pamoja na vituo shirikishi vya usafirishaji.

Pia alibainisha uwezekano wa kutumia mfumo wa ubia kati ya Serikali na sekta binafsi (PPP) katika ujenzi wa njia za kusafirisha umeme kando ya korido za reli.

Kaimu Mkurugenzi Mtendaji na Afisa Mkuu Mtendaji wa Shirika la Ndege Tanzania (ATCL), John Nzunda, alitaja usafirishaji wa mizigo kwa njia ya anga, matengenezo na uhandisi, teknolojia za kidijitali, usimamizi wa mafuta na mafunzo maalumu kwa wataalamu wa sekta ya anga kuwa miongoni mwa maeneo yenye nafasi ya kuimarishwa kupitia ushirikiano huo.

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa CCECC East Africa Ltd, Lu Haiqiang, alisema kampuni hiyo iko tayari kuimarisha ushirikiano na mashirika ya umma ya Tanzania katika maeneo ya miundombinu, uhandisi, ujenzi na uendeshaji.

Alitaja pia ufufuaji wa Reli ya Tanzania-Zambia (TAZARA) kuwa fursa muhimu ya kuimarisha ushirikiano wa kiuchumi kwa kuunganisha korido za biashara na shughuli za madini, kilimo, usafirishaji na viwanda.

Mkutano huo uliwakutanisha viongozi na wataalamu kutoka OTR, SASAC na CERDS, Balozi wa China nchini Tanzania, Mhe. Chen Mingjian, pamoja na viongozi waandamizi kutoka TPA, TRC na ATCL, ukiweka msingi wa hatua mpya ya ushirikiano kati ya mashirika ya umma ya Tanzania na China.

Tuesday, August 25, 2026

TANZANIA YAUNGA MKONO MABADILIKO YA MFUMO WA AFYA DUNIANI








Na Hassan Kimweri, WAF - Addis Ababa

Tanzania imeunga mkono juhudi za kuimarisha Shirika la Afya Duniani (WHO) kupitia maboresho ya Muundo wa Mfumo wa Afya Duniani (Global Health Architecture), huku ikisisitiza umuhimu wa WHO kuendelea kutekeleza jukumu lake la msingi kama mamlaka ya kiufundi ya afya duniani. 

Naibu Waziri wa Afya Mhe. Dkt. Florence Samizi, amesema hayo leo Agosti 25, 2026 kwenye Mkutano wa 76 wa Kamati ya Kanda ya Afrika ya Shirika la Afya Duniani (WHO-AFRO), unaofanyika jijini Addis Ababa, Ethiopia.

"Tanzania inapongeza uongozi wa WHO katika kuratibu ushiriki wa Kanda ya Afrika kwenye utekelezaji wa marekebisho ya Kanuni za Kimataifa za Afya (International Health Regulations – IHR 2024) pamoja na kukamilishwa kwa viambatisho vyake katika Mkataba wa WHO," amesema Dkt. Samizi 

Aidha, Dkt. Samizi amesema Tanzania inatambua mchango wa WHO katika kutoa msaada wa kiufundi ili kuimarisha mifumo ya afya, kuboresha ufuatiliaji wa magonjwa, kukabiliana na milipuko, kuendeleza huduma jumuishi za afya kwa wote pamoja na kuboresha afya ya mama na mtoto pamoja na vijana.

Tanzania imeeleza dhamira yake ya kuendelea kushirikiana kwa karibu na WHO, taasisi za kikanda, washirika wa maendeleo na nchi wanachama katika kujenga mifumo ya afya imara, yenye usawa na inayomlenga mwananchi. 

Pai, Dkt. Samizi amesema Tanzania imedhamiria kukabiliana na changamoto za magonjwa yanayojitokeza na kuibuka upya, mabadiliko ya tabianchi, usugu wa vimelea dhidi ya dawa pamoja na upungufu wa rasilimali.

Monday, August 24, 2026

TRC KUONGEZA SAFARI ZA SGR DAR ES SALAAM–DODOMA 🚆🇹🇿

 


Habari njema kwa wasafiri! Shirika la Reli Tanzania (TRC) limetangaza kuongeza safari za treni ya SGR kati ya Dar es Salaam na Dodoma kuanzia Septemba 1, 2026.

Kuongezeka kwa safari kunatarajiwa kutoa nafasi zaidi kwa abiria, kuongeza urahisi wa usafiri na kuimarisha zaidi muunganiko kati ya Dar es Salaam na Dodoma.

Hatua hii ni mwendelezo wa matumizi ya miundombinu ya kisasa ya reli katika kurahisisha usafiri wa wananchi na kuchochea shughuli za kiuchumi.

🚆 Safari zaidi. Urahisi zaidi. Muunganiko zaidi.

#TRC #SGR #DarEsSalaam #Dodoma #Usafiri #Miundombinu #Maendeleo #Tanzania

BUNGE LAMTHIBITISHA NDEJEMBI KWA ASILIMIA 100 UMAKAMU WA RAIS.

Waziri Mkuu asema anatosha, kiti kimempata mtu sahihi wa kumsaidia Mheshimiwa Rais. BUNGE la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania leo (Ijumaa, Ag...