Wednesday, August 26, 2026

NCHIMBI AFUKUZWA CCM, NDEJEMBI ARITHI MIKOBA


Halmashauri Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) imefanya maamuzi muhimu yanayofungua sura mpya katika uongozi wa chama na Serikali, kufuatia kujiuzulu kwa Dkt. Emmanuel Nchimbi katika nafasi ya Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Akizungumza na waandishi wa habari katika Ofisi Ndogo za CCM, Lumumba jijini Dar es Salaam, Jumatano, Agosti 26, 2026, Katibu Mkuu wa CCM, Dkt. Asha-Rose Migiro, amesema Halmashauri Kuu, baada ya kupitia taarifa zilizowasilishwa pamoja na Katiba ya CCM, imeamua kumvua uanachama Dkt. Nchimbi kutokana na kile kilichoelezwa kuwa ukiukwaji wa maadili.

Uamuzi huo unafuatia hatua ya Dkt. Nchimbi kuwasilisha kwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ombi la kujiuzulu nafasi ya Makamu wa Rais kuanzia Septemba 4, 2026, pamoja na kutangaza kustaafu shughuli za kisiasa.

Katika barua yake, Dkt. Nchimbi alimshukuru Rais Samia, CCM pamoja na Watanzania kwa imani na ushirikiano alioupata katika kipindi cha utumishi wake, huku akieleza dhamira yake ya kuendelea kuwa raia mwema na kulitumikia Taifa kwa namna nyingine.

NDEJEMBI APITISHWA

Katika kuhakikisha mwendelezo wa uongozi, Halmashauri Kuu ya CCM imepitisha jina la Deogratius Ndejembi, Waziri wa Nishati, kwa ajili ya hatua zinazofuata kuelekea kujaza nafasi ya Makamu wa Rais.

Kupitishwa kwa jina hilo kunafungua njia kwa taratibu zinazofuata za kikatiba, katika kuhakikisha nafasi hiyo inajazwa na shughuli za Serikali zinaendelea kwa utulivu.

Dkt. Nchimbi anaondoka akiwa na historia ndefu ya utumishi ndani ya CCM na Serikali, ikiwemo kuwa Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa, Mwenyekiti wa UVCCM, Katibu Mkuu wa CCM na baadaye Makamu wa Rais.

Maamuzi haya yanaashiria mabadiliko yenye mwendelezo wa uongozi, huku taasisi za chama na Serikali zikiendelea kutekeleza wajibu wake kwa mujibu wa taratibu zilizowekwa.

TANZANIA, CHINA ZAFUNGUA SURA MPYA YA USHIRIKIANO WA MASHIRIKA YA UMMA

Msajili wa Hazina, Nehemiah Mchechu, jijini Dar es Salaam, akifuatilia kwa makini wa akiwa katika mkutano na ujumbe wa wataalamu kutoka SASAC.


Tanzania na China zinatarajia kufungua sura mpya ya ushirikiano katika usimamizi na maendeleo ya mashirika ya umma, kupitia makubaliano yatakayoweka msingi wa kubadilishana uzoefu, utaalamu na kujenga uwezo wa taasisi za Serikali.

Hatua hiyo inakuja wakati Ofisi ya Msajili wa Hazina (OTR) ikiwa katika hatua za mwisho za kukamilisha hati mbili za makubaliano ya ushirikiano (MoU) na Tume ya Usimamizi wa Mali za Serikali za China (SASAC) pamoja na Jumuiya ya China ya Mageuzi na Maendeleo ya Mashirika (CERDS).

Akizungumza jijini Dar es Salaam, Jumatano Agosti 26, 2026, wakati wa mkutano na ujumbe wa wataalamu kutoka China, Msajili wa Hazina, Nehemiah Mchechu, alisema makubaliano hayo yanatarajiwa kukamilika ifikapo Ijumaa au Jumatatu ijayo.

Mchechu alisema ushirikiano huo utafungua fursa kwa taasisi za umma za Tanzania na China kubadilishana ujuzi na uzoefu katika maeneo ya utafiti, kujenga uwezo wa taasisi, sera, utawala bora, mageuzi ya mashirika ya umma na tathmini ya utendaji.

Aidha, Tanzania inatarajia kutumia ushirikiano huo kujifunza kutokana na uzoefu wa China katika usimamizi wa mali za Serikali, uendeshaji wa mashirika ya umma kwa kuzingatia misingi ya soko na namna ya kuongeza ufanisi na thamani ya mtaji wa Serikali.

“Kupitia uhusiano wetu wa pande mbili na SASAC, tunalenga kujifunza namna China ilivyofanikiwa kufanya mageuzi na kuelekeza mtaji wa Serikali katika sekta muhimu za kimkakati ili kuchochea ukuaji wa uchumi wa taifa,” alisema Mchechu.

Kwa sasa, OTR inasimamia taasisi za umma 308, zikiwamo 252 ambazo Serikali inamiliki hisa nyingi na 56 ambazo Serikali ina hisa chache.

Kwa upande wake, Rais wa CERDS, Peng Huagang, alisema uzoefu wa China umeonesha kuwa mashirika ya umma yanaweza kuendeshwa kwa misingi ya soko na ushindani huku yakiendelea kutekeleza majukumu yake ya kimkakati kwa taifa.

Alisema mageuzi hayo yanalenga kujenga mashirika yaliyo imara zaidi, yenye ufanisi na uwezo wa kushindana, sambamba na kuhakikisha mali na mitaji ya Serikali inalindwa na kuongezeka thamani.

“Mageuzi yanayozingatia misingi ya soko ndiyo njia ya msingi ya kuongeza ushindani wa mashirika ya umma, na kuyawezesha kufanya kazi kwa ufanisi sambamba na aina nyingine za umiliki,” alisema Peng.

Alisema ushirikiano huo pia unaendeleza uhusiano wa muda mrefu kati ya Tanzania na China na unaendana na utekelezaji wa ahadi zilizowekwa kupitia Jukwaa la Ushirikiano kati ya China na Afrika (FOCAC).

FURSA ZA USHIRIKIANO

Sura hiyo mpya ya ushirikiano pia inatarajiwa kufungua fursa katika sekta za kimkakati, ikiwamo miundombinu, reli, bandari, usafiri wa anga, uhandisi, teknolojia, viwanda na usafirishaji wa mizigo.

Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA), Dkt. Boniphace Nobeji, alisema uboreshaji wa utendaji na ufanisi wa bandari una nafasi kubwa katika kukuza biashara na maendeleo ya kiuchumi ya Tanzania pamoja na ukanda wa Afrika Mashariki na Kati.

“Tunaamini ustawi wa taifa lolote unatokana na biashara, na sehemu kubwa ya biashara inawezeshwa na bandari zenye ufanisi. Hakuna shaka kwamba maboresho katika utendaji na ufanisi wa TPA yataharakisha maendeleo ya kiuchumi ya Afrika Mashariki na Kati,” alisema Dkt. Nobeji.

Alitaja maeneo yanayoweza kunufaika na ushirikiano huo kuwa ni pamoja na uendelezaji wa bandari kavu, uhamishaji wa teknolojia, ujenzi wa uwezo na kujifunza kutokana na uzoefu wa China katika usimamizi wa bandari.

Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Reli Tanzania (TRC), Mhandisi Machibya Shiwa, alitaja fursa katika vituo vya usafirishaji wa mizigo, huduma za usafirishaji wa mizigo, kongani za viwanda zinazounganishwa na reli pamoja na vituo shirikishi vya usafirishaji.

Pia alibainisha uwezekano wa kutumia mfumo wa ubia kati ya Serikali na sekta binafsi (PPP) katika ujenzi wa njia za kusafirisha umeme kando ya korido za reli.

Kaimu Mkurugenzi Mtendaji na Afisa Mkuu Mtendaji wa Shirika la Ndege Tanzania (ATCL), John Nzunda, alitaja usafirishaji wa mizigo kwa njia ya anga, matengenezo na uhandisi, teknolojia za kidijitali, usimamizi wa mafuta na mafunzo maalumu kwa wataalamu wa sekta ya anga kuwa miongoni mwa maeneo yenye nafasi ya kuimarishwa kupitia ushirikiano huo.

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa CCECC East Africa Ltd, Lu Haiqiang, alisema kampuni hiyo iko tayari kuimarisha ushirikiano na mashirika ya umma ya Tanzania katika maeneo ya miundombinu, uhandisi, ujenzi na uendeshaji.

Alitaja pia ufufuaji wa Reli ya Tanzania-Zambia (TAZARA) kuwa fursa muhimu ya kuimarisha ushirikiano wa kiuchumi kwa kuunganisha korido za biashara na shughuli za madini, kilimo, usafirishaji na viwanda.

Mkutano huo uliwakutanisha viongozi na wataalamu kutoka OTR, SASAC na CERDS, Balozi wa China nchini Tanzania, Mhe. Chen Mingjian, pamoja na viongozi waandamizi kutoka TPA, TRC na ATCL, ukiweka msingi wa hatua mpya ya ushirikiano kati ya mashirika ya umma ya Tanzania na China.

Tuesday, August 25, 2026

TANZANIA YAUNGA MKONO MABADILIKO YA MFUMO WA AFYA DUNIANI








Na Hassan Kimweri, WAF - Addis Ababa

Tanzania imeunga mkono juhudi za kuimarisha Shirika la Afya Duniani (WHO) kupitia maboresho ya Muundo wa Mfumo wa Afya Duniani (Global Health Architecture), huku ikisisitiza umuhimu wa WHO kuendelea kutekeleza jukumu lake la msingi kama mamlaka ya kiufundi ya afya duniani. 

Naibu Waziri wa Afya Mhe. Dkt. Florence Samizi, amesema hayo leo Agosti 25, 2026 kwenye Mkutano wa 76 wa Kamati ya Kanda ya Afrika ya Shirika la Afya Duniani (WHO-AFRO), unaofanyika jijini Addis Ababa, Ethiopia.

"Tanzania inapongeza uongozi wa WHO katika kuratibu ushiriki wa Kanda ya Afrika kwenye utekelezaji wa marekebisho ya Kanuni za Kimataifa za Afya (International Health Regulations – IHR 2024) pamoja na kukamilishwa kwa viambatisho vyake katika Mkataba wa WHO," amesema Dkt. Samizi 

Aidha, Dkt. Samizi amesema Tanzania inatambua mchango wa WHO katika kutoa msaada wa kiufundi ili kuimarisha mifumo ya afya, kuboresha ufuatiliaji wa magonjwa, kukabiliana na milipuko, kuendeleza huduma jumuishi za afya kwa wote pamoja na kuboresha afya ya mama na mtoto pamoja na vijana.

Tanzania imeeleza dhamira yake ya kuendelea kushirikiana kwa karibu na WHO, taasisi za kikanda, washirika wa maendeleo na nchi wanachama katika kujenga mifumo ya afya imara, yenye usawa na inayomlenga mwananchi. 

Pai, Dkt. Samizi amesema Tanzania imedhamiria kukabiliana na changamoto za magonjwa yanayojitokeza na kuibuka upya, mabadiliko ya tabianchi, usugu wa vimelea dhidi ya dawa pamoja na upungufu wa rasilimali.

Monday, August 24, 2026

TRC KUONGEZA SAFARI ZA SGR DAR ES SALAAM–DODOMA 🚆🇹🇿

 


Habari njema kwa wasafiri! Shirika la Reli Tanzania (TRC) limetangaza kuongeza safari za treni ya SGR kati ya Dar es Salaam na Dodoma kuanzia Septemba 1, 2026.

Kuongezeka kwa safari kunatarajiwa kutoa nafasi zaidi kwa abiria, kuongeza urahisi wa usafiri na kuimarisha zaidi muunganiko kati ya Dar es Salaam na Dodoma.

Hatua hii ni mwendelezo wa matumizi ya miundombinu ya kisasa ya reli katika kurahisisha usafiri wa wananchi na kuchochea shughuli za kiuchumi.

🚆 Safari zaidi. Urahisi zaidi. Muunganiko zaidi.

#TRC #SGR #DarEsSalaam #Dodoma #Usafiri #Miundombinu #Maendeleo #Tanzania

Saturday, August 22, 2026

RAIS SAMIA AZINDUA KITUO CHA KUZALISHA UMEME CHA JULIUS NYERERE, AAGIZA UKAMILISHAJI WA MIUNDOMBINU YA KUSAFIRISHA UMEME NCHINI


 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akihutubia viongozi, wageni mbalimbali pamoja na wananchi waliohudhuria hafla ya Uzinduzi wa Kituo cha Kuzalisha Umeme cha Julius Nyerere (JNHPP), chenye uwezo wa kuzalisha Megawati 2115 katika eneo la Rufiji mkoani Pwani tarehe 22 Agosti, 2026.









Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, ameitaka Wizara ya Nishati kusimamia ukamilishaji wa haraka wa miundombinu ya usafirishaji na usambazaji wa umeme kote nchini, ili umeme unaozalishwa katika Kituo cha Kuzalisha Umeme cha Julius Nyerere uweze kufika katika maeneo yenye mahitaji ya uzalishaji na uwekezaji.

Rais Dkt. Samia ametoa agizo hilo leo, tarehe 22 Agosti, 2026, wakati wa uzinduzi wa Kituo cha Kuzalisha Umeme cha Julius Nyerere, Rufiji, mkoani Pwani.

Amesema kukamilika kwa kituo hicho kunapaswa kuleta matokeo yanayoonekana katika uzalishaji, viwanda, biashara, madini, kilimo cha kisasa, huduma za kijamii, uwekezaji na ajira.

Kituo hicho chenye uwezo wa kuzalisha Megawati 2,115, kinachangia takribani nusu ya umeme unaoingizwa katika Gridi ya Taifa, hatua inayoongeza kwa kiasi kikubwa upatikanaji na uhakika wa nishati nchini.

Rais Dkt. Samia amesema kukamilika kwa mradi huo ni matokeo ya fikra na maono ya Baba wa Taifa, Hayati Mwalimu Julius Nyerere, yaliyoendelezwa katika awamu mbalimbali za uongozi hadi sasa.

Katika hilo, ametambua mchango wa Marais waliomtangulia, hususan Hayati Dkt. John Pombe Magufuli, ambaye katika awamu yake ya uongozi alichukua hatua thabiti za kuanza utekelezaji wa ujenzi wa mradi huo muhimu mwaka 2019.

Aidha, Rais Dkt. Samia amewataka Watanzania kulinda amani na utulivu wa nchi, sambamba na kuimarishwa kwa ulinzi wa miundombinu, mazingira na vyanzo vya maji vinavyotegemewa na kituo hicho ili kiendelee kufanya kazi kwa ufanisi.

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Kiarabu ya Misri, Mhe. Dkt. Mostafa Madbouly, ameipongeza Tanzania kwa kukamilisha kituo hicho, akisema mafanikio hayo yamedhihirisha uwezo wa ushirikiano wa Afrika katika kutekeleza miradi mikubwa ya maendeleo.

Ameongeza kuwa kukamilika kwake kunafungua nafasi ya kukuza zaidi ushirikiano kati ya Tanzania na Misri katika biashara, uwekezaji, ujenzi, barabara, bandari, kilimo, umeme na nishati.

Naye, Waziri wa Nishati, Mhe. Deo Ndejembi, amesema Serikali inaendelea kujenga njia ya kusafirisha umeme ya Kilovolti 400 ya Iringa–Mbeya–Songea–Rukwa, pamoja na njia za Songea–Tunduru–Masasi–Maumbika na Tanzania–Uganda ili kuunganisha vituo vya uzalishaji, maeneo ya shughuli za kiuchumi na masoko ya kikanda.

Akizungumza katika hafla hiyo, Rais Mstaafu wa Benki ya Maendeleo ya Afrika, Dkt. Akinwumi Adesina, amesema kituo hicho kinaiweka Tanzania katika nafasi nzuri ya kuwa kitovu cha uzalishaji wa nishati na shughuli za kiuchumi katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kati.

Ujenzi wa Kituo cha Kuzalisha Umeme cha Julius Nyerere ulianza mwaka 2019 kwa gharama ya shilingi trilioni 7.452. Kituo kina mitambo tisa yenye uwezo wa kuzalisha jumla ya Megawati 2,115, jengo la mitambo, transfoma 27 na kituo cha kupokea na kusafirisha umeme kwa msongo wa Kilovolti 400.

Wednesday, August 19, 2026

RC CHALAMILA ATOA SIKU SABA KWA MUAFAKA WA MGOGORO WA ARDHI TOANGOMA





Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Mhe. Albert Chalamila, ametoa muda wa siku saba kwa wadau wanaohusika na mgogoro wa muda mrefu wa ardhi katika eneo la Toangoma, Wilaya ya Temeke, kukutana na Shirika la Taifa la Hifadhi ya Jamii (NSSF) ili kutafuta muafaka kabla ya kurejea katika eneo hilo kwa ajili ya kuhitimisha mgogoro huo.

Mhe. Chalamila ametoa maelekezo hayo katika mkutano wa hadhara uliofanyika Toangoma, baada ya kusikiliza maelezo ya wananchi, NSSF pamoja na Ofisi ya Kamishna wa Ardhi. Amesema kwa mujibu wa nyaraka na maelezo yaliyowasilishwa, amejiridhisha kuwa eneo linalozungumziwa linamilikiwa na NSSF.

Hata hivyo, Mkuu huyo wa Mkoa amesema amepokea maombi ya wananchi wanaotaka masharti ya ununuzi wa maeneo wanayoishi yafanyiwe mapitio ili kuwawezesha kumudu gharama na kupata muda wa kutosha wa kufanya malipo.

Kwa mujibu wa maelezo yaliyotolewa katika mkutano huo, NSSF ilikuwa imeweka bei ya Sh. 15,000 kwa mita ya mraba katika eneo la Malela na Sh. 25,000 kwa mita ya mraba katika eneo la Mwapemba. Wananchi wameomba bei hiyo ipunguzwe hadi Sh. 5,000 kwa mita ya mraba, sambamba na kuongezewa muda wa kufanya malipo kutoka kipindi cha awali cha miezi mitatu hadi kati ya miaka minne na 10.

Mhe. Chalamila amesema katika kipindi cha siku saba alichotoa, atakutana na wadau husika kwa lengo la kutafuta suluhu inayozingatia maslahi ya pande zote. Aidha, ameelekeza wananchi kutosumbuliwa katika kipindi hicho huku muda wa awali uliokuwa umetolewa kwa ajili ya malipo ukisitishwa ili kutoa nafasi ya kufikiwa kwa mpango mpya.

Kamishna Msaidizi wa Ardhi Mkoa wa Dar es Salaam, Rehema Mwinuka, amethibitisha kuwa eneo hilo linamilikiwa na NSSF. Kwa upande wake, mwakilishi wa NSSF ameeleza kuwa baada ya kubaini kuwapo kwa wananchi katika eneo lake, Shirika liliamua kutoa fursa kwa wakazi hao kununua maeneo wanayoishi kwa bei zilizowekwa.

Awali, wananchi walieleza kuwa wengi wao wameishi katika maeneo hayo kwa zaidi ya miaka 16, wakidai kuwa walinunua viwanja kupitia taratibu zilizohusisha viongozi wa serikali za mitaa na hivyo kuamini kuwa ardhi hiyo haikuwa mali ya NSSF.

Kutokana na mazingira hayo, wananchi wamemuomba Mkuu wa Mkoa kusaidia kupatikana kwa suluhu itakayowawezesha kuendelea kumiliki maeneo hayo kwa gharama na masharti wanayoweza kumudu.

Mhe. Chalamila anatarajiwa kurejea Toangoma baada ya siku saba kwa ajili ya kutoa mrejesho wa majadiliano na kuweka hitimisho katika mgogoro huo wa muda mrefu.

Tuesday, August 18, 2026

RAIS TSHISEKEDI AFANYA ZIARA YA KIKAZI TANZANIA

 Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ampokea Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) Mhe. Félix Antoine Tshisekedi Tshilombo, Ikulu Ndogo ya Zanzibar.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiongoza Ujumbe wa Tanzania kwenye mazungumzo Rasmi na Ujumbe wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) ulioongozwa na Rais wa Nchi hiyo, Mhe. Félix Antoine Tshisekedi Tshilombo katika Ikulu Ndogo ya Zanzibar, tarehe 18 Agosti, 2026



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, amempokea Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), Mhe. Félix Antoine Tshisekedi Tshilombo, katika Ikulu Ndogo ya Zanzibar, akiwa nchini kwa ziara ya kikazi.

Viongozi hao wawili wanatarajiwa kufanya mazungumzo yatakayojikita katika kuimarisha zaidi ushirikiano baina ya Tanzania na DRC, sambamba na kujadili masuala mbalimbali yenye maslahi ya pamoja kwa mataifa hayo mawili.

Tanzania na DRC zina uhusiano wa muda mrefu wa kihistoria na kidugu, huku ushirikiano wao ukiendelea kuimarika katika nyanja mbalimbali za maendeleo.

Ziara hiyo ni mwendelezo wa jitihada za kuimarisha diplomasia, ujirani mwema na ushirikiano wa kikanda kwa manufaa ya wananchi wa Tanzania na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.

NCHIMBI AFUKUZWA CCM, NDEJEMBI ARITHI MIKOBA

Halmashauri Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) imefanya maamuzi muhimu yanayofungua sura mpya katika uongozi wa chama na Serikali , kufuatia k...