Sunday, August 02, 2026

TAWIRI YASHIRIKI MKUTANO WA KIMKAKATI WA WIZARA YA MALIASILI NA UTALII





Mkurugenzi Mkuu TAWIRI Dkt. Eblate Mjingo ni miongoni mwa Wakuu wa taasisi zilizo chini ya Wizara ya Maliasili na Utalii wanaoshiriki  mkutano wa  kimkakati unaowajumuisha  watendaji wote wa Wizara hiyo kujadili  namna bora ya kuboresha utendaji ili kufikia malengo tarajiwa hususani ya Dira ya Taifa ya Maendeleo ya 2050.

Akifungua mkutano huo, Waziri wa Maliasili na Utalii Dkt. Ashatu Kijaji (Mb) ameitaka Menejimenti ya Wizara na Wakuu wa Taasisi za Wizara hiyo  kuongeza ubunifu sambamba na  kuzigeuza  changamoto za kiutendaji kuwa fursa za matokeo chanya kwa wananchi.

Amefafanua kuwa sekta ya Maliasili na Utalii ni moja ya sekta za mageuzi hapa nchini kutokana na mchango wake katika kuchochea ukuaji wa uchumi, kuongeza ajira, mapato ya fedha za kigeni na maendeleo ya jamii kwa ujumla.

“ Utendaji katika sekta hii  ni lazima uwe wa kimkakati na unaozingatia utu kwa kuwa unagusa sehemu kubwa ya maisha ya wananchi,” amehimiza Dkt. Kijaji

Mkutano huo unaoendelea kwa siku nne katika Hifadhi ya Taifa ya Nyerere ni fursa kwa Menejimenti na viongozi wakuu wa Taasisi zilizo chini ya Wizara ya Maliasili na Utalii kubadilishana uzoefu na kujifunza mbinu bora za kuendeleza uhifadhi na utalii.

TAWIRI ni injini katika sekta ya Uhifadhi na Utalii

Friday, July 31, 2026

Waziri Mkuu azindua boti mbili za doria na uokozi










Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba ametoa siku 14 kwa wizara na taasisi zinazohusika na Kituo cha Kitaifa cha pamoja cha Oparesheni zipeleke wawakilishi ili kianze kufanya kazi mara moja.

"Wizara na taasisi zote zinazohusika na utekelezaji wa majukumu katika Kituo cha Kitaifa cha pamoja cha Oparesheni zipeleke wawakilishi wote wanaohitajika ndani ya siku 14 kuanzia leo. Kituo hiki kianze kazi mara moja ili kuleta tija inayokusudiwa," amesema Waziri Mkuu. 

Dkt. Mwigulu ametoa wito huo leo Julai 31, 2026 wakati akizungumza na washiriki wa hafla ya makabidhiano na uzinduzi wa boti mbili za doria aina ya PB Sailfish 02 na PB Sailfish 03 iliyofanyika bandarini, jijini Dar es Salaam. Boti hizo zimenunuliwa kwa thamani ya dola za Marekani milioni 1.6. 

Amezitaka Wizara za Muungano zinazohusika na suala hilo zishirikiane ili kuziba chochoro zote ambazo zingetumiwa na wahalifu katika eneo hili tunalolilenga na hasa katika mipaka ya mwambao wa bahari.

Ili kuhakikisha boti hizo zinafanya kazi kama inavyotarajiwa, Waziri Mkuu ameziagiza wizara na taasisi zote za umma zinazohusika katika matumizi ya boti hizi za doria zitenge fedha kwa ajili ya kazi za boti hizi.

"Ninasisitiza suala la kutenga bajeti ili kazi za doria zisikwamishwe na ukosefu wa bajeti. Nimekuwa nikikutana na kesi kama hizo mikoani ambapo Mheshimiwa Rais Dkt Samia Suluhu Hassan alinunua ambulance za kisasa na nyingine zina ICU lakini zinashindwa kuhudumia wagonjwa kwa wakati kwa kukosa mafuta. Hili linakinzana na dhamira njema ya Mheshimiwa Rais ya kutaka kuokoa maisha ya Watanzania pindi wanahitaji huduma hizo," amefafanua.

Akielezea umuhimu wa boti hizo za doria, Waziri Mkuu amesema makabidhiano ya boti hizo ni tukio muhimu kiuchumi kwa sababu zinaenda kulinda mazao yatokanayo na uchumi wa bluu. Amesema uhitaji wa boti hizo umekuwa ni kilio cha muda mrefu tangu yeye akiwa Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi.

Amesema upatikanaji wa boti hizo mbili, utaimarisha ulinzi hasa ikizingatiwa kwamba Tanzania ni lango la nchi nyingi zikiwemo za Afrika Mashariki na za SADC lakini usalama utakaokuwepo unahusu Tanzania na wananchi wa hizo nchi jirani.

RAIS SAMIA AANZA ZIARA YA KIDIPLOMASIA ANGOLA, ATAONGOZA UZINDUZI WA HOSPITALI YA MWALIMU NYERERE

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiagana na viongozi mbalimbali kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA) Jijini Dar es Salaam kabla ya kuondoka nchini, kuelekea Luanda, Angola ambapo anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika hafla ya Uzinduzi wa Hospitali iliyopewa jina la Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, tarehe 31 Julai, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano
wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiagana na viongozi mbalimbali kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA) Jijini Dar es Salaam kabla ya kuondoka nchini, kuelekea Luanda, Angola ambapo anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika hafla ya Uzinduzi wa Hospitali iliyopewa jina la Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, tarehe 31 Julai,
2026.



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, ameondoka nchini kuelekea Luanda, Angola, ambako anatarajiwa kuwa Mgeni Rasmi katika hafla ya uzinduzi wa Hospitali iliyopewa jina la Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, tarehe 31 Julai, 2026.

Kabla ya kuanza safari hiyo, Rais Samia alipata fursa ya kuzungumza na Mama Maria Nyerere, mazungumzo yanayoakisi heshima na dhamira ya kuendeleza urithi wa Mwalimu Nyerere, ambaye mchango wake katika harakati za ukombozi wa Bara la Afrika na kuimarisha mshikamano wa mataifa unaendelea kutambuliwa kimataifa.

Aidha, katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA) jijini Dar es Salaam, Rais Samia aliagana na viongozi mbalimbali kabla ya kuondoka nchini kwa ajili ya ziara hiyo yenye umuhimu wa kidiplomasia.

Ushiriki wa Tanzania katika hafla hiyo unaendelea kuimarisha uhusiano wa kihistoria na kindugu kati ya Tanzania na Angola, huku ukidhihirisha heshima ya kudumu inayotolewa kwa maono, uongozi na mchango wa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere katika maendeleo ya Afrika na ustawi wa ushirikiano wa mataifa ya bara hili.

Thursday, July 30, 2026

SERIKALI NA WAWEKEZAJI & WATOA HUDUMA MIGODINI WAJADILI CHANGAMOTO NA MAFANIKIO KWENYE SEKTA YA MADINI





▪️Rais Samia apongezwa kwa mazingira rafiki ya uwekezaji

▪️ Wadau wapongeza hatua za serikali za kutatua changamoto

▪️Waziri Mavunde awataka Watanzania kuanza ujenzi wa viwanda vya bidhaa za migodini

▪️ Kampuni ya MANTRA yanuia

kuiweka Tanzania kwenye kumi bora ya wazalishaji wa Uranium Duniani

Dar es salaam

Waziri wa Madini, Mhe. Anthony Mavunde, amesema Serikali itaendelea kushirikiana na wadau wa sekta ya madini kupitia majukwaa ya majadiliano kwa lengo la kujenga sekta yenye ushindani, inayovutia uwekezaji na kutoa mchango mkubwa katika ukuaji wa uchumi wa Taifa.

Mhe. Mavunde ameyasema hayo katika kikao cha Mining Breakfast Briefing (MBB), kilichoandaliwa kwa ushirikiano wa Chemba ya Migodi Tanzania (TCM) na Wizara ya Madini, ambapo ametoa wito kwa wadau kuendelea kutumia majukwaa hayo kujadili fursa na changamoto zinazohusu sekta ya madini.

Amewashukuru viongozi na wanachama wa Chemba ya Migodi Tanzania kwa kuendelea kutoa nafasi ya Serikali na wadau kukutana na kujadiliana kuhusu masuala mbalimbali ya sekta hiyo, huku akilipongeza Mantra Tanzania Limited kwa kudhamini kikao hicho.

Amesema ushiriki wa wadau katika majukwaa hayo unaonesha dhamira ya pamoja ya kujenga sekta ya madini yenye ushindani, inayovutia mitaji na teknolojia, pamoja na kuhakikisha rasilimali za madini zinatumika kikamilifu kuchochea maendeleo ya kiuchumi na kijamii.

“Serikali inathamini utaratibu huu wa kukutana na wadau wa sekta ya madini kupitia Mining Breakfast Briefing, kwa kuwa unatoa fursa ya kufanya mazungumzo yenye tija, kujenga uelewa wa pamoja, kupokea changamoto zinazojitokeza na kutafuta suluhisho kwa pamoja,” amesema.

Amesema Serikali itaendelea kushirikiana na wadau wa sekta hiyo katika kutatua changamoto zinazojitokeza na kuboresha mazingira ya uwekezaji ili kuongeza uzalishaji, ajira, mapato ya Serikali na kutumia fursa hiyo kuwataka watoa huduma migodini kuchangamkia fursa ya ujenzi wa viwanda vya kuzalisha bidhaa za migodini.

“Ni vyema kuendelea kukutana mara kwa mara kupitia jukwaa hili muhimu, kwa sababu linatupa nafasi ya kusikilizana, kujadiliana na kutafuta suluhisho la changamoto zinazotukabili kwa pamoja,” amesema.

Naye, Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini, Eng. Yahya Samamba, amewashukuru wadau wa sekta ya madini kwa kushiriki katika kikao hicho, akiwataka kuongeza ushirikiano na mshikamano katika kukuza sekta hiyo.

Amesema ushirikiano kati ya Serikali na sekta binafsi ni muhimu katika kutatua changamoto, kuchochea uwekezaji na kuhakikisha fursa zinazotokana na rasilimali za madini zinatumika kwa manufaa mapana ya Taifa.

Amesisitiza kuwa mawasiliano ya mara kwa mara kati ya Serikali na wadau yataendelea kuwa nyenzo muhimu katika kubaini changamoto mapema na kuzitafutia ufumbuzi wa pamoja.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Chemba ya Migodi Tanzania, Mhandisi Philbert Rweyemamu, amemshukuru Waziri Mavunde kwa kuendelea kudumisha mahusiano mazuri na wadau wa sekta ya madini.

Amepongeza utaratibu wa Serikali kukutana mara kwa mara na wadau kupitia Mining Breakfast Briefing, akisema majukwaa hayo ni muhimu katika kujenga mawasiliano ya karibu, kubadilishana uzoefu na kujadili changamoto pamoja na fursa zilizopo katika sekta hiyo.

Amesema Chemba ya Migodi Tanzania itaendelea kushirikiana na Serikali chini ya uongozi imara wa Mh. Rais Dkt. Samia S. Hassan katika kuhakikisha sekta ya madini inaendelea kuimarika, kuvutia uwekezaji na kuongeza mchango wake katika maendeleo ya uchumi wa Tanzania.

Akizungumzia maendeleo ya mradi wa Uranium, Meneja wa Uendelevu wa Mantra Tanzania Limited, Majani Wambura, amesema mradi huo umebaini uwepo wa hifadhi ya takribani tani 58,500 za Uranium, huku uzalishaji ukitarajiwa kufikia tani 3,000 kwa mwaka.

Amesema mradi huo unatarajiwa kutoa ajira kwa zaidi ya wafanyakazi 4,000 baada ya kuanza uzalishaji, hatua itakayochochea shughuli za kiuchumi na kuongeza fursa kwa Watanzania.

Kwa mujibu wa Wambura, mradi huo unatarajiwa kuanza uzalishaji mwaka 2029  na kuwa na maisha ya zaidi ya miaka 20, huku utafiti ukiendelea ili kubaini uwepo wa rasilimali zaidi katika maeneo yanayohusishwa na mradi huo ambapo hatua zote hizo zitaifanya Tanzania kuwa miongoni mwa wazalishaji wakubwa 10 wa Uraniaum Duniani.

Ameeleza kuwa Uranium ni rasilimali yenye matumizi mbalimbali, ikiwemo katika uzalishaji wa nishati ya umeme na sekta ya afya, hususan matumizi ya mionzi katika uchunguzi na matibabu.

Akifunga jukwaa hilo, Naibu Waziri wa Madini, Dkt. Steven Kiruswa, amesema Serikali na wadau wa sekta ya madini wanapaswa kuendelea kukutana mara kwa mara kupitia Mining Breakfast Briefing (MBB) ili kujadili na kutatua changamoto zinazojitokeza katika sekta hiyo.

Amesema mikutano ya mara kwa mara itasaidia kujenga mawasiliano na uelewa wa pamoja kati ya Serikali na wadau, kujadili changamoto na fursa zilizopo, pamoja na kuweka mazingira bora zaidi ya uwekezaji katika sekta ya madini.

Wednesday, July 29, 2026

WANANCHI WALIPONGEZA JESHI LA POLISI KATAVI KWA KUFANYA USAFI MAENEO MBALIMBALI.

Wananchi wa eneo la soko kuu la Manispaa ya Mpanda mjini, Mkoani Katavi wamelipongeza Jeshi la Polisi kwa kuendesha zoezi la usafi lililofanyika sokoni hapo, ambapo wamesema hatua hiyo imechangia kuboresha mazingira ya biashara na afya ya jamii kwa ujumla.

Zoezi hilo limefanyika Julai 29, 2026 likiongozwa na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Katavi Kamishna msaidizi Mwandamizi (SACP) Kaster Ngonyani ambapo, amesema kuwa zoezi hilo ni endelevu lenye lengo la kuhamasisha wananchi kutunza mazingira huku akiwataka wafanyabiashara na wananchi kuendelea kushirikiana katika kudumisha usafi wa soko na maeneo mengine yanayowazunguka.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa mtaa wa Kashaulili Ndugu Johari Korongo amelipongeza Jeshi la Polisi Mkoa wa Katavi kwa kuonyesha ushirikiano mzuri na wananchi kwa kujitolea na ametoa wito kwa taasisi nyingine kuiga mfano huo kwa kushiriki shughuli mbalimbali za maendeleo na huduma kwa jamii.



Tuesday, July 28, 2026

Rais Samia Akutana na Balozi wa China Nchini Tanzania



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, amekutana na kufanya mazungumzo na Balozi wa Jamhuri ya Watu wa China nchini Tanzania, Mhe. Chen Mingjian, katika Ikulu ya Tunguu, Zanzibar, tarehe 28 Julai 2026.

Mazungumzo hayo yamejikita katika kuendelea kuimarisha uhusiano wa muda mrefu wa kidiplomasia na ushirikiano wa kimkakati kati ya Tanzania na China, hususan katika maeneo ya biashara, uwekezaji, maendeleo ya miundombinu na sekta nyingine za maendeleo ya kijamii na kiuchumi.

Tanzania na China zimeendelea kushirikiana kwa karibu kwa miongo kadhaa, ambapo ushirikiano huo umechangia utekelezaji wa miradi mbalimbali yenye manufaa kwa wananchi na kukuza mahusiano ya kirafiki kati ya mataifa hayo mawili.

Mkutano huo unaakisi dhamira ya pande zote mbili ya kuendeleza ushirikiano unaojengwa juu ya kuheshimiana, maslahi ya pamoja na maendeleo endelevu kwa manufaa ya wananchi wa Tanzania na China.

VIONGOZI WATEULE WAAPA KIAPO CHA UADILIFU MBELE YA RAIS SAMIA







Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, amewaapisha viongozi mbalimbali walioteuliwa kula Kiapo cha Uadilifu kwa Viongozi wa Umma katika hafla iliyofanyika Ikulu ya Tunguu, Zanzibar, tarehe 27 Julai, 2026.

Rais Samia Suluhu Hassan, aliwaapisha Dkt. Latifa Mohammed Khamis kuwa Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Makamu wa Rais – Muungano na Ndugu Prisca Burton Lwangili kuwa Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora.

Hafla hiyo ya uapisho imefanyika Ikulu ya Tunguu, Zanzibar, tarehe 27 Julai, 2026, ambapo viongozi hao wameapishwa rasmi kuanza kutekeleza majukumu yao katika nafasi walizoteuliwa.

Kiapo hicho ni sehemu ya utekelezaji wa matakwa ya sheria na utaratibu wa utumishi wa umma, kikilenga kuimarisha uwajibikaji, uadilifu, uzalendo na uzingatiaji wa maadili katika utekelezaji wa majukumu ya viongozi wa umma.

Hafla hiyo imeashiria mwanzo rasmi wa viongozi hao kuanza kutekeleza majukumu yao kwa kuzingatia misingi ya uongozi bora na kutoa huduma zenye tija kwa wananchi.

TAWIRI YASHIRIKI MKUTANO WA KIMKAKATI WA WIZARA YA MALIASILI NA UTALII

Mkurugenzi Mkuu TAWIRI Dkt. Eblate Mjingo ni miongoni mwa Wakuu wa taasisi zilizo chini ya Wizara ya Maliasili na Utalii wanaoshiriki  mkuta...