Tuesday, July 21, 2026

WACHIMBAJI WADOGO WAISHUKURU SERIKALI KWA USAMBAZAJI WA UMEME MIGODINI







*Nyang’hwale, Geita*

Wachimbaji wadogo wa madini wilayani Nyang'hwale, mkoani Geita, wameishukuru Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kuendelea kuwekeza katika upatikanaji wa nishati ya umeme kwenye maeneo ya migodi, hatua inayopunguza gharama za uzalishaji na kuongeza tija katika shughuli za uchimbaji.

Shukrani hizo zimetolewa wakati Waziri wa Madini, Mhe. Anthony Mavunde, alipozindua mradi wa kuzalisha nishati ya umeme wenye uwezo wa KVA 500 kwenye Mgodi wa wachimbaji wadogo katika eneo la Igalula, wilayani Nyang'hwale. Mradi huo umetekelezwa kwa gharama ya zaidi ya Shilingi milioni 426 na ni sehemu ya juhudi za Serikali za kuboresha miundombinu ya nishati katika maeneo ya uchimbaji wa madini.

Akizungumza katika uzinduzi huo, Mhe. Mavunde amesema Serikali imeendelea kutekeleza kwa vitendo dhamira ya kuboresha mazingira ya uwekezaji na uzalishaji katika sekta ya madini kwa kusambaza umeme kwenye migodi ya wachimbaji wadogo na wa kati.

Amesema Serikali tayari imetumia zaidi ya Shilingi bilioni 7 kusambaza umeme katika maeneo mbalimbali ya migodi nchini, hatua iliyowezesha wachimbaji kupunguza utegemezi wa mitambo inayotumia mafuta na hivyo kushusha gharama za uzalishaji huku ikiongeza ufanisi wa shughuli za uchimbaji.

Katika kuendelea na ziara yake, Waziri Mavunde amekagua mradi wa maji safi na salama unaotekelezwa katika Kijiji cha Kakola, ambao unatarajiwa kuwanufaisha zaidi ya wananchi 24,801

Amesema mradi huo unatekeleza maelekezo ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuhakikisha wananchi, hususan wanawake, wanaondokana na adha ya kutembea umbali mrefu kutafuta maji.

"Ahadi ya Mheshimiwa Rais ya kumtua mama ndoo kichwani inaendelea kutekelezwa kwa vitendo kupitia miradi ya maji kama huu wa Kakola ambao utaboresha afya, ustawi na shughuli za kiuchumi za wananchi,"  amesema.

Katika sekta ya elimu, Waziri Mavunde amezindua Shule ya Msingi Imara Baruti iliyojengwa ili kuondoa changamoto ya wanafunzi kutembea umbali wa takribani kilomita nne kwenda kusoma katika Shule ya Msingi Shabaka.

Amesema ujenzi wa shule hiyo unatekeleza Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), inayosisitiza ujenzi wa shule karibu na makazi ya wananchi ili watoto wapate elimu katika mazingira bora.

"Serikali ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan inaendelea kuthibitisha kuwa ahadi zinazotolewa kwa wananchi si maneno ya kampeni pekee, bali ni mipango inayotekelezwa kwa vitendo kwa manufaa ya Watanzania," amesema.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Geita, Martin Shigella, amempongeza Waziri Mavunde kwa kufanya ziara ya kukagua na kuzindua miradi ya maendeleo mkoani humo, akisema hatua hiyo imeongeza kasi ya utekelezaji wa miradi na kuimarisha ufuatiliaji wa huduma zinazowagusa wananchi moja kwa moja.

Shigella amebainisha kuwa uwekezaji unaoendelea katika sekta za madini, elimu, maji na nishati unaendelea kuifanya Geita kuwa kitovu muhimu cha uzalishaji wa madini na maendeleo ya kijamii nchini.

WAZIRI NDEJEMBI AMTEMBELEA NA KUMJULIA HALI KAPTENI MSTAAFU GEORGE MKUCHIKA

 

Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi amemtembelea na kumjulia hali Kapteni Mstaafu George Huruma Mkuchika, aliyewahi kushika nafasi mbalimbali za uongozi Serikalini, ikiwemo Uwaziri katika wizara tofauti na Ubunge wa Jimbo la Newala Mjini, leo tarehe 21 Julai 2026 nyumbani kwake wilayani kijiji cha Nambunga Newala, mkoani Mtwara.



Newala, Mtwara | 21 Julai 2026

Waziri wa Nishati, Mheshimiwa Deogratius Ndejembi, leo tarehe 21 Julai 2026 amemtembelea na kumjulia hali Kapteni Mstaafu George Huruma Mkuchika nyumbani kwake katika Kijiji cha Nambunga, Wilaya ya Newala, mkoani Mtwara.

Katika ziara hiyo ya heshima na faraja, Waziri Ndejembi alipata fursa ya kuzungumza na Kapteni Mstaafu Mkuchika kuhusu hali yake ya afya, huku akimtakia afya njema, nguvu na maisha marefu.

Kapteni Mstaafu George Huruma Mkuchika ni mmoja wa viongozi waliotoa mchango mkubwa katika utumishi wa umma na maendeleo ya Taifa. Katika kipindi chake cha utumishi, aliwahi kushika nafasi mbalimbali za juu Serikalini ikiwemo Uwaziri katika wizara tofauti, pamoja na kulitumikia Jimbo la Newala Mjini kama Mbunge kwa vipindi kadhaa.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Waziri Ndejembi alieleza kuwa Serikali inaendelea kuthamini mchango wa viongozi wastaafu walioweka msingi imara wa maendeleo ya nchi kupitia utumishi wao wa kujituma na uzalendo. Alisisitiza kuwa kuwatembelea na kuwajulia hali viongozi hao ni sehemu ya kutambua na kuheshimu mchango wao kwa Taifa.

Kwa upande wake, Kapteni Mstaafu Mkuchika alimshukuru Waziri Ndejembi kwa kutenga muda wa kumtembelea na kumjulia hali, akieleza kuwa hatua hiyo inaonesha mshikamano, utu na kuthamini viongozi waliolitumikia Taifa kwa uaminifu.

Ziara hiyo imeakisi utamaduni wa viongozi kuendeleza mshikamano, upendo na kuthaminiana, huku ikitoa ujumbe kwamba mchango wa viongozi wastaafu katika ujenzi wa Taifa unaendelea kutambuliwa na kuheshimiwa.

Monday, July 20, 2026

MIRADI YA UCHUKUZI KUIFANYA KIGOMA KUWA KITOVU CHA BIASHARA AFRIKA MASHARIKI NA KATI - PROF. MBARAWA








Waziri wa Uchukuzi, Profesa Makame Mbarawa amesema Serikali ya Awamu ya Sita inaendelea kutekeleza uwekezaji mkubwa katika sekta ya uchukuzi unaolenga kuifanya Kigoma kuwa kitovu cha usafirishaji na biashara kinachounganisha Tanzania na nchi za Afrika Mashariki na Kati.

Profesa Mbarawa amesema hayo leo Jumatatu Julai 20, 2026 katika hafla iliyohudhuriwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, wakati wa uzinduzi wa meli nne za mizigo, uwekaji wa jiwe la msingi la ujenzi wa gati la abiria na mizigo Bandari ya Kigoma pamoja na uzinduzi wa ujenzi wa Reli ya Kisasa (SGR) kipande cha Tabora–Kigoma.

Amesema chini ya uongozi wa Rais Samia, Serikali imewekeza kwa kiwango kikubwa katika reli ya kisasa, bandari, viwanja vya ndege na usafiri wa majini kwa lengo la kuunganisha mikoa yote ya Tanzania pamoja na nchi jirani kupitia mfumo jumuishi wa uchukuzi.

Kwa mujibu wa Profesa Mbarawa, meli nne mpya za mizigo zitaongeza usalama wa usafirishaji katika Ziwa Tanganyika, kupunguza gharama za usafirishaji wa mizigo, kukuza biashara kati ya Tanzania, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo na Burundi, pamoja na kufungua fursa mpya za ajira na uwekezaji.

Aidha, amesema maboresho yanayoendelea Bandari ya Kigoma pamoja na ujenzi wa Reli ya Kisasa kutoka Tabora hadi Kigoma yataongeza ufanisi wa usafirishaji wa abiria na mizigo, huku yakiiunganisha Bandari ya Dar es Salaam na masoko ya ukanda wa Afrika Mashariki na Kati.

Profesa Mbarawa pia amesema Serikali inaendelea na maboresho ya uwanja wa ndege wa Kigoma kwa gharama ya Sh. bilioni 51.4, yanayojumuisha ujenzi wa jengo jipya la abiria, mnara wa kuongozea ndege, njia za ndege, taa za kuongozea ndege na miundombinu mingine muhimu. 

Ameongeza kuwa miradi hiyo inaonesha dhamira ya Serikali ya kujenga mfumo wa uchukuzi unaounganisha reli, bandari na usafiri wa anga ili kuharakisha maendeleo ya uchumi wa Taifa.

Tuesday, July 14, 2026

MMUYA: WANANCHI WANUFAIKE NA UWEKEZAJI WA NHC KUPITIA NYUMBA ZA GHARAMA NAFUU










Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Mhe. Kaspar Mmuya, amekagua maendeleo ya ujenzi wa mradi wa maghala unaotekelezwa na Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) katika Mtaa wa Viwandani, Kata ya Railway, Halmashauri ya Manispaa ya Mtwara-Mikindani.

Mhe. Mmuya amefanya ukaguzi huo Julai 13, 2026, ikiwa ni sehemu ya ziara yake ya kikazi ya siku mbili mkoani Mtwara yenye lengo la kukagua utekelezaji wa miradi iliyo chini ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi.

Akipokea taarifa ya mradi huo, Mhe. Mmuya ameelezwa kuwa ujenzi wa maghala hayo unagharimu shilingi bilioni 4.1, ambapo hadi sasa shilingi bilioni 2.6 zimetumika. Mradi huo unatarajiwa kukamilika Septemba 2026.

Katika ukaguzi huo, Mhe. Mmuya amelishauri Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) kuendelea kubuni na kuwekeza katika miradi inayogusa maisha ya wananchi moja kwa moja, hususan ujenzi wa nyumba za gharama nafuu, ili kusaidia kukabiliana na changamoto ya upungufu wa makazi nchini.

Aidha, amepongeza Shirika hilo kwa kuwekeza katika ujenzi wa maghala katika eneo lenye shughuli kubwa za kiuchumi, akibainisha kuwa uwepo wa Bandari ya Mtwara pamoja na uzalishaji wa mazao ya biashara, hususan korosho, unafanya mradi huo kuwa na umuhimu mkubwa katika kuchochea biashara na maendeleo ya uchumi wa mkoa huo.

Mradi huo unatarajiwa kuongeza uwezo wa kuhifadhi bidhaa mbalimbali, ikiwemo mazao ya kimkakati kama korosho, hatua itakayochangia kuongeza thamani ya mazao, kuboresha huduma za uhifadhi na kuimarisha shughuli za biashara kwa wakazi wa Mkoa wa Mtwara na maeneo ya jirani.

NGORONGORO NA SIMBA WAUNGANA KUITANGAZA TANZANIA KUPITIA UTALII NA MICHEZO


Arusha: Mamlaka ya Hifadhi ya Eneo la Ngorongoro (NCAA) na Klabu ya Simba Sports Club zimeanzisha ushirikiano wa kimkakati unaolenga kuitangaza Tanzania kupitia utalii na michezo, hatua inayotarajiwa kuongeza hamasa ya kutembelea vivutio vya utalii nchini huku ikiimarisha taswira ya Tanzania kimataifa.

Akizungumza katika uzinduzi wa ushirikiano huo, Makamu Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya NCAA, Dkt. Harrieth Mtae, alisema ushirikiano huo ni mwanzo wa enzi mpya unaoonyesha namna sekta ya umma na taasisi za michezo zinavyoweza kushirikiana kuleta thamani kwa taifa.

"Ninawashukuru viongozi wa Simba Sports Club kwa kukubali kuwa washirika wetu katika safari hii muhimu ya kuitangaza Tanzania kupitia michezo na utalii. Leo tunashuhudia mwanzo mpya wa ushirikiano unaounganisha chapa mbili kubwa za Afrika kwa lengo la kuitangaza Tanzania duniani," alisema Dkt. Mtae.

Alieleza kuwa Bodi ya Wakurugenzi ya NCAA inaunga mkono kikamilifu ushirikiano huo kwa kuwa unaendana na maono ya kuifanya Ngorongoro kuwa kivutio cha utalii cha kiwango cha kimataifa, sambamba na kuchangia utekelezaji wa vipaumbele vya taifa katika kukuza utalii, uchumi na diplomasia ya kimkakati.

Kwa mujibu wa Dkt. Mtae, kupitia kampeni ya "The Pride Returns Home", mamilioni ya Watanzania pamoja na mashabiki wa mpira wa miguu ndani na nje ya nchi watapata sababu mpya ya kutembelea Ngorongoro na kujivunia urithi wa kipekee wa Tanzania.

Alibainisha kuwa wakati Tanzania ikijiandaa kuwa mwenyeji wa fainali za AFCON 2027, ushirikiano huo unathibitisha kuwa michezo inaweza kuwa jukwaa muhimu la kutangaza utalii, kuhamasisha uhifadhi wa maliasili na kuijenga Tanzania kama moja ya maeneo bora ya utalii barani Afrika.

Dkt. Mtae alihitimisha kwa kueleza matarajio ya NCAA kuona ushirikiano huo ukidumu kwa muda mrefu na kuleta manufaa kwa pande zote mbili pamoja na taifa kwa ujumla.

"Karibuni Nyumbani, Karibuni Ngorongoro," alisisitiza.

Wednesday, July 08, 2026

MBUNGE WA BUNGE LA NORWAY AVUTIWA NA VIVUTIO VYA SERENGETI, AIKARIBISHA DUNIA KUTEMBELEA TANZANIA


Mbunge wa Bunge la Norway, Mhe. Himanshu Gulati, akiongozana na mwenyeji wake, Mbunge wa Jimbo la Buchosa, Mhe. Eric Shigongo, ametembelea Hifadhi ya Taifa Serengeti na kujionea vivutio vya kipekee vya utalii, wanyamapori mbalimbali pamoja na mandhari ya kuvutia inayoifanya Tanzania kuwa miongoni mwa nchi zinazoongoza kwa utalii duniani.

Akizungumza baada ya ziara hiyo, Mhe. Gulati alisema amefurahishwa na ubora wa vivutio vya utalii nchini pamoja na juhudi kubwa zinazofanywa na Serikali ya Tanzania katika kuhifadhi rasilimali za asili na wanyamapori kwa manufaa ya vizazi vya sasa na vijavyo.

Aidha, amewahamasisha wananchi wa Norway na mataifa mengine duniani kuitembelea Tanzania ili kujionea uzuri wa Hifadhi za Taifa, urithi wa asili na uzoefu wa kipekee unaopatikana katika vivutio vya utalii vya nchi hii.

"Tanzania ni nchi yenye vivutio vya kipekee na mazingira ya kuvutia. Kila mtu anapaswa kupata nafasi ya kuitembelea na kujionea uzuri wake," alisema Mhe. Gulati.

WAZIRI MKUU AKUTANA NA MAKAMU WA RAIS WA KAMPUNI YA ALSTOM




▪️Yaonesha nia ya kushirikiana na Serikali katika usafiri ya Mijini.

▪️Dkt. Mwigulu awahakikishia mazingira bora ya uwekezaji

WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba, amekutana na Makamu wa Rais wa Kampuni ya ALSTOM ya nchini Ufaransa, Philippe Deller ambapo wamejadiliana kuhusu fursa za uwekezaji katika sekta ya miundombinu ya usafiri nchini Tanzania.

Katika mazungumzo hayo, Dkt. Mwigulu Nchemba aliikaribisha ALSTOM kuwekeza nchini, akieleza kuwa Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan inaendelea kuweka mazingira wezeshi kwa wawekezaji na kutekeleza mageuzi yanayolenga kuifanya Tanzania kuwa kitovu cha biashara, usafiri na uwekezaji katika ukanda wa Afrika Mashariki.

Kwa Upande wake Bw. Phillepe alieleza nia ya kampuni hiyo kushirikiana na Serikali ya Tanzania katika utekelezaji wa miradi ya kimkakati ya usafiri wa mijini.

Kampuni hiyo imeonesha utayari wa kuwekeza katika ujenzi wa mifumo ya usafiri wa haraka na miundombinu ya kisasa yenye lengo la kupunguza msongamano wa magari katika Jiji la Dar es Salaam, huku ikitazama pia fursa za utekelezaji wa miradi kama hiyo katika majiji ya Mwanza, Mbeya na Arusha.

Miradi hiyo inatarajiwa kuongeza ufanisi wa usafiri wa mijini, kupunguza muda wa safari, kuimarisha shughuli za biashara na uwekezaji, pamoja na kuchochea ukuaji wa uchumi na kuboresha maisha ya wananchi kupitia matumizi ya teknolojia za kisasa.

Mazungumzo hayo ni sehemu ya jitihada za Serikali za kuimarisha ushirikiano na kampuni kubwa za kimataifa ili kuleta teknolojia, utaalamu na mitaji inayochochea maendeleo ya miundombinu na uchumi wa Taifa.

Kampuni ya ALSTOM, ina uzoefu mkubwa katika kubuni, kujenga na kuendesha mifumo ya kisasa ya usafiri wa umma ikiwemo reli za kisasa, treni za mwendo kasi, metro, tram na teknolojia za usimamizi wa usafiri.

WACHIMBAJI WADOGO WAISHUKURU SERIKALI KWA USAMBAZAJI WA UMEME MIGODINI

*Nyang’hwale, Geita* Wachimbaji wadogo wa madini wilayani Nyang'hwale, mkoani Geita, wameishukuru Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa...