Sunday, April 12, 2026

WABUNGE WAJENGEWA UWEZO WA HAKI MADINI NA HAKI ARDHI

 










Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini imepatiwa mafunzo maalum kuhusu Sheria, Kanuni na Miongozo ya Sekta ya Madini, kwa lengo la kuongeza uelewa hususan juu ya tofauti kati ya Haki ya Ardhi na Haki ya Madini.

Mafunzo hayo yamefanyika katika Ukumbi wa Tanzanite, Makao Makuu ya Tume ya Madini, jijini Dodoma.

Akizungumza katika semina hiyo, Waziri wa Madini, Mhe. Anthony Mavunde, amesema kuwa umiliki wa haki ya madini na haki ya ardhi ni mambo mawili tofauti kisheria, na kwamba mwenye leseni ya madini haruhusiwi kuanza shughuli za uchimbaji bila kufikia makubaliano na mmiliki wa ardhi husika.

Amefafanua kuwa, kwa mujibu wa Sheria, leseni ya madini inaweza kutolewa katika eneo lolote, lakini utekelezaji wake unahitaji ridhaa au makubaliano na mwenye haki ya ardhi. Hata hivyo, iwapo makubaliano hayatapatikana, Waziri ana mamlaka ya kuruhusu shughuli za uchimbaji kuendelea kwa kuzingatia sheria.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mhe. Subira Mgalu, ameipongeza Wizara ya Madini kwa kuandaa mafunzo hayo, akieleza kuwa yameongeza uelewa na kuwajengea wabunge uwezo wa kusimamia vyema sekta hiyo.

Wasilisho kuhusu haki ya madini na haki ya ardhi limetolewa na Mkurugenzi wa Huduma za Sheria kutoka Wizara ya Madini, Dkt. Arnold Gisase, ambaye ameeleza kuwa mtu anaweza kumiliki haki ya madini bila kuwa mmiliki wa ardhi, na kwamba umiliki wa ardhi pekee haumruhusu mtu kufanya shughuli za madini bila leseni husika.

Dkt. Gisase pia amebainisha changamoto zinazojitokeza, ikiwemo uelewa mdogo wa wananchi kuhusu haki na wajibu wao, kutokuelewa taratibu za uthamini na fidia, ucheleweshaji wa malipo ya fidia, pamoja na baadhi ya wamiliki wa ardhi kudai kuwa sehemu ya umiliki wa leseni za madini.

Naye, Mwanasheria kutoka Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Method Akilimali, amesisitiza kuwa fidia kwa mmiliki wa ardhi lazima ilipwe kabla ya kuanza kwa shughuli za utafiti au uchimbaji.

Ameongeza kuwa sheria inamtaka mmiliki wa leseni kurejesha eneo katika hali yake ya awali baada ya shughuli za madini kukamilika. Aidha, ameeleza kuwa ardhi yote nchini ni mali ya umma chini ya usimamizi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kama mdhamini.

Amesema pia fidia inapaswa kulipwa ndani ya miezi sita; kuchelewa hulazimu kulipwa riba, na endapo itazidi miaka miwili tangu uthamini kufanyika, tathmini hiyo hupoteza uhalali.

Akizungumzia muundo wa leseni, Mkurugenzi Mtendaji wa Tume ya Madini, Mhandisi Ramadhani Lwamo, amesema zipo aina kuu tatu za leseni ambazo ni leseni ya utafiti, uchimbaji mdogo na uchimbaji mkubwa ambapo kwa leseni ya uchimbaji mdogo Mtanzania pekee mwenye umri wa kuanzia miaka 18 ndiyo anaruhusiwa kuomba.

Mhandisi Lwamo amesema leseni kubwa na ya kati inaruhusiwa kuombwa na mtu yoyote na kwa sasa kuna mfumo wa kuomba leseni bila kufika ofisi za madini.

Mafunzo hayo yamelenga kuwawezesha wabunge kuelewa kwa kina masuala ya kisheria na kiutendaji katika sekta ya madini ili kuboresha usimamizi na maamuzi yenye tija kwa maendeleo ya taifa.

WAZIRI MKUU AKAGUA BARABARA YA NTYUKA - KIKOMBO








Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba amekagua ujenzi wa barabara ya kiwango cha lami ya Ntyuka–Mvumi–Kikombo yenye urefu wa kilomita 76 pamoja na kipande cha barabara ya Chololo–Mapinduzi (Makao Makuu ya TPDF) yenye urefu wa kilomita 5, katika Jimbo la Mvumi, Wilaya ya Chamwino, Mkoa wa Dodoma.

Mradi huu unaotekelezwa na Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) unafadhiliwa kwa asilimia 100 na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ukiwa na lengo la kuboresha miundombinu ya usafiri, kuimarisha muunganiko kati ya Wilaya ya Dodoma Mjini na Chamwino, pamoja na kurahisisha upatikanaji wa huduma muhimu za kijamii ikiwemo Hospitali ya Mvumi Mission.

Mradi huu unafanyika kwa awamu mbili ambapo awamu ya kwanza yenye urefu wa kilomita 25 (ikiwemo Ntyuka–Mvumi–Makulu na Kikombo–Chololo–Mapinduzi) imefikia utekelezaji wa asilimia 80.9, na inatekelezwa na Mkandarasi M/s China Henan International Corporation Company Ltd kwa gharama ya shilingi bilioni 38.199.

Awamu ya pili yenye urefu wa kilomita 53 (Ntyuka–Mvumi Hospitali–Kikombo) imeanza kutekelezwa na Mkandarasi China First Highway Engineering Co. Ltd, ikiwa imefikia asilimia 5.2 ya utekelezaji kwa sasa, kwa gharama ya shilingi bilioni 98.488.

Aidha, mradi huu umeendelea kutoa ajira kwa Watanzania ambapo zaidi ya wafanyakazi 500 wamehusishwa katika awamu zote mbili za ujenzi.

Taarifa ya utekelezaji wa mradi huo iliwasilishwa kwa Waziri Mkuu na Mhandisi Jefferson Nko, ambapo alieleza hatua zilizofikiwa pamoja na changamoto na mikakati ya kuhakikisha mradi unakamilika kwa wakati.

Akizungumza baada ya kupokea taarifa hiyo, Mheshimiwa Waziri Mkuu amesema: “Utekelezaji wa mradi huu ni dhamira ya Mhe. Rais Dkt. Samia kuwaachia alama ya kudumu wakazi wa eneo hili, hii ni barabara muhimu sana kwa kuwa nimepita nimeona hili ni eneo la uzalishaji.”

Mheshimiwa Waziri Mkuu alisisitiza umuhimu wa wakandarasi kuongeza kasi ya utekelezaji wa mradi huo ili ukamilike kwa wakati na ubora unaotakiwa kulingana na makubaliano ya mkataba.

Aidha, Waziri Mkuu alitoa maagizo kwa Meneja wa Mradi kuhakikisha malipo kwa wafanyakazi wote wanaoshiriki katika mradi huo, ikiwemo wakandarasi wa ndani, mafundi na vibarua, yanafanyika kwa wakati.

“Meneja wa Mradi simamia na hakikisha mafundi na vibarua wanalipwa kwa wakati fedha zinapotoka. Tunapokamilisha mradi wale wote waliohusika kufanya kazi walipwe malipo yao mara moja,” alisisitiza.

Saturday, April 11, 2026

MAKAMU WA RAIS AFUNGUA KONGAMANO LA VIJANA KATIKA KUMBUKIZI YA KUZALIWA BABA WA TAIFA HAYATI MWL. J.K NYERERE








Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi ametoa wito kwa vijana kusimama imara na kulinda umoja, kujenga uadilifu, kutumia elimu na ubunifu katika kukuza maendeleo ya nchi ili kuweza kumuenzi Baba wa Taifa Hayati Mwl. Julius Kambarage Nyerere kwa vitendo.

Makamu wa Rais ametoa wito huo wakati akifungua Kongamano la Vijana katika Kumbukizi ya Miaka 104 ya Kuzaliwaa Baba wa Taifa, Hayati Mwl. Julius Kambarage Nyerere, lililofanyika Ukumbi wa Chimwaga mkoani Dodoma, leo tarehe 11 Aprili 2026. Amesema ni muhimu kwa vijana kutambua wajibu wa msingi wa kizazi hiki, kwa kuhakakikisha wanafanya kila jitihada kuimarisha misingi ya kujitegemea kiuchumi, kiakili na kimaamuzi ili kuijenga nchi.

Makamu wa Rais amesema Hayati Baba wa Taifa alikuwa kiongozi aliyeunganisha Taifa na kutoa mchango mkubwa katika ukombozi wa Bara la Afrika. Amesema Taifa la Tanzania lilipata bahati ya pekee kuwa na Hayati Mwl. Nyerere kwa kuwa alichukia rushwa, ubadhirifu na matumizi mabaya ya madaraka. Aliamini katika utu na uhuru wa mwanadamu ikiwemo msisitizo wa kuhakikisha kila wananchi anapata elimu.

Ameongeza kwamba Baba wa Taifa alitengeneza misingi ya amani, utulivu na mshikamano katika Taifa pamoja na kufundisha vitu vyote vinavyoweza kuleta mpasuko kama vile ukabila, dini, rangi, kupuuza maendeleo na usawa katika jamii.

Makamu wa Rais amesema ni dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kuendeleza mshikamano na umoja ambao Baba wa Taifa aliujenga.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Bodi wa Taasisi ya Kumbukumbu ya Mwal. Nyerere ambaye ni Waziri Mkuu Mstaafu Mhe. Mizengo Pinda ametoa rai kwa vijana kuhakikisha wanafanya jitihada za kujifunza historia ya Taifa ili kufahamu waliotoa mchango mkubwa katika historia hiyo.

Amewahimiza kusoma vitabu vilivyoandikwa kuhusu Hayati Mwal.Julius Kambarage Nyerere ili kufahamu mchango mkubwa aliyoutoa katika ukombozi wa Bara la Afrika na msisitizo alioutoa wa katika kuhakikisha umoja wa Afrika. Ameongeza Taasisi hiyo imejikita katika kutoa mchango kwa kuwasaidia viongozi vijana kuwa wazalendo na wanaowajibika.

Kongamano hilo limejadili mada mbalimbali zenye lengo la kuwajengea vijana uzalendo, uwajibikaji, matumizi sahihi ya mitandao na matumizi bora ya fursa zilizopo nchini.

Watumishi Tume ya Uchaguzi watakiwa kuepuka uchochezi, wajipanga uchaguzi Isimani

 








Na Mwandishi Wetu, Morogoro

Watumishi wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi wametakiwa kutekeleza majukumu yao kwa kuzingatia katiba, sheria, kanuni  na taratibu na kuepuka lugha zozote za uchochezi zinazoweza kuleta uvunjifu wa amani na kuhatarisha maisha ya Watanzania.

Hayo yamesemwa leo Aprili 11, 2026 na Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na wenye Ulemavu), Dkt. James Henry Kilabuko kwa niaba ya Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Dkt Jimmy Yonaz wakati akifungua kikao cha Baraza la Wafanyakazi la Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, katika kikao kilichoketi Mkoani Morogoro. 

“Napenda kuwaasa, kuzingatia katiba, sheria, kanuni  na taratibu mnapotekeleza majukumu ya Tume na kuepuka lugha zozote za uchochezi zinazoweza kuleta uvunjifu wa amani na kuhatarisha maisha ya Watanzania,”alisema Dkt Kilabuko.

Dkt. Kilabuko amesema, taasisi ina malengo yake, upo uwezakano wa kuepusha migogoro ya ndani na nje ya taasisi inayoweza kuathiri utekelezaji wa majukumu ya Tume kwa ufanisi.

Mapema akimkaribisha Mgeni Rasmi, Mwenyekiti wa Baraza la Wafanyakazi INEC ambaye pia ni Mkurugenzi wa Uchaguzi wa Tume, Ndg. Ramadhani Kailima alisema kwa sasa Tume inaendelea na zoezi la uandishi wa Taarifa ya Uchaguzi Mkuu wa Rais, Wabunge na Madiwani ya Mwaka 2025.

“Tume imekamilisha Uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2025 ambao ulifanyika tarehe 29 Oktoba, 2025.  Kwa sasa Tume inaendelea na zoezi la uandishi wa Taarifa ya Uchaguzi Mkuu wa Rais, Wabunge na Madiwani ya Mwaka 2025. Taarifa hiyo baada ya kukamilika, itawasilishwa kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,”alisema Kailima.

Aidha, amesema Tume ipo katika maandalizi ya uchaguzi mdogo wa Ubunge katika Jimbo la Isimani mkoani Iringa kufuatia kifo cha aliyekuwa Mbunge wa Jimbo hilo, Mhe. William Lukuvi pamoja na uchaguzi wa udiwani katika Kata mbalimbali nchini ambazo madiwani wake walifariki.

Katika Kikao hicho cha siku moja pia kilitumika kwa kufanya uchaguzi wa Katibu wa Baraza hilo ambapo wajumbe walimchagua Ndg. Mwitaru Keboya kuwa Katibu mpya wa Baraza akichukua nafasi ya Ndg. Livini Avith ambaye amemaliza muda wake. 

Rais Samia Atunukiwa Shahada ya Uzamivu ya Heshima kwa Uongozi na Mchango wa Kijamii Afrika

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akitunukiwa Shahada ya Uzamivu ya Heshima kutoka Chuo Kikuu cha Jimbo la Nasarawa, Keffi nchini Nigeria kwa njia ya mtandao, tarehe 11 Aprili, 2026 Ikulu, Dodoma.

Mhe. Rais ametunukiwa Shahada hiyo ya Uzamivu ya Heshima kwa kutambua mchango wake kama Kinara wa Nishati Safi ya Kupikia, Afya ya Mama na Mtoto, Taswira nzuri katika masuala ya Uongozi kwa Wanawake Afrika na Kusimamia Masuala ya Biashara hususani kwa Vijana Afrika.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akizungumza kwa njia ya mtandao na Chuo Kikuu cha Jimbo la Nasarawa, Keffi nchini Nigeria ambacho kimemtunuku Shahada ya Uzamivu ya Heshima , tarehe 11 Aprili, 2026 Ikulu, Dodoma.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan, ametunukiwa Shahada ya Uzamivu ya Heshima na Nasarawa State University kwa njia ya mtandao, katika hafla iliyofanyika tarehe 11 Aprili 2026, Ikulu jijini Dodoma.

Tuzo hiyo imetolewa kwa kutambua mchango wake mkubwa katika kuendeleza ajenda za kijamii na kiuchumi barani Afrika, hususan katika maeneo ya nishati safi ya kupikia, afya ya mama na mtoto, pamoja na kukuza taswira chanya ya uongozi wa wanawake.

Aidha, Mhe. Rais ametambuliwa kwa juhudi zake za kusimamia na kuhamasisha maendeleo ya biashara, hasa kwa vijana, ambapo amekuwa kinara wa kuweka mazingira rafiki ya uwekezaji na ujasiriamali.

Kutunukiwa kwa heshima hiyo kunadhihirisha nafasi ya Tanzania katika ramani ya uongozi bora barani Afrika, pamoja na mchango wa Mhe. Rais katika kuleta mageuzi yenye tija kwa jamii na vizazi vijavyo.

MFUMO MPYA WA MAFUTA WAONGEZA MAPATO, WAFANYABIASHARA WAFURAHIA

 


KAMPUNI ya Uingizaji na Usambazaji wa mafuta Jamii ya Petrol nchini ya ‘MOIL Energies’ imesema imefurahishwa kwa kuanzishwa kwa mfumo mpya wa ulipaji kodi ya nishati hiyo kabla ya kuyatoa vituoni na kwenda sokoni (BIL)kwa kiasi kikubwa umesaidia kudhibiti ‘ujanja ujanja’ uliokuwepo hapo awali

Akizungumza Dar es Salaam Meneja Mkuu wa Kampuni hiyo nchini, Dkt Sajad Habib Rai amesema wao kama Kampuni ya kwanza nchini kutoa mapendekezo ya kuanzishwa kwa mfumo huo kwa EWURA na Wakala wa Uagizaji wa Mafuta kwa Pamoja (PBPA) na baadae kuanzishwa rasmi na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), wanajivunia kuona umetekelezwa kwa kuwa dhamira yao ilikuwa kuona huduma ya usambazaji wa mafuta nchini na nje ya nchi unaleta tija kwa Taifa.

“Tumefurahi kuona TRA wameusimamia kikamilifu mfumo huu kwa kuwa unazuia ukwepaji kodi ambao hapo awali ulikuwa ukifanywa na wafanyabiashara, hivi sasa TRA inapata kodi yake mapema kabla ya kuyaingiza mafuta sokoni” amesema Dk Sajad ambaye pia ni Meneja MKAZI wa ‘Mansoor Industry Limited’

Hivi karibuni Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) ilitangaza rasmi kuanza kutumika kwa mfumo huo ambao kwa kiasi kikubwa unalezwa kuleta tija kwa Serikali kwa kuwa umesaidia kudhibiti upotevu wa mapato unaotakana na Kodi za uingizaji wa mafuta hayo nchini.

Kupitia mfumo huo mpya na wa kisasa, kila mwagizaji au muingizaji wa mafuta atalazimika kutaja kiasi cha mafuta alichokiingiza nchini ambapo kupitia Shirika la Viwango Tanzania (TBS) watayataweka vinasaba kama alama ya kila mwagizaji kwa lengo la kuwatambua wahusika wote na kiasi alichoagiza ili kuwakadiria viwango vya Kodi wanavyopaswa kulipa.

“Nawapongeza TRA kwa kuona tija na umuhimu wa kuutumia mfumo huu, sisi kama wafanyabiashara tunaozingatia taratibu halali za uingizaji na Usambazaji wa mafuta tunaiona kuwa hatua hii ni kubwa na inayostahili kupongezwa kwa kuwa italeletea manufaa Taifa” ameongeza Dkt Sajad.

Utaratibu huo wa kikodi unawataka wamiliki wa mafuta hayo kuyalipia kodi kabla ya kuyaingiza sokoni ili yanapoingizwa sokoni yanaendelea na taratibu za uuzwaji hali ambayo inarahisisha usambazaji na kuwafikishia wateja huduma ya mafuta kwa wakati sambamba na kudhibiti kubaki nchini mafuta ambayo kimsingi yanapaswa kusafirishwa kwenda nje ya nchi.

Aidha akizungumza wakati wa ziara yake aliyoifanya hivi karibuni katika bohari za kuhifadhia mafuta zilizopo Jijini Dar es Salaam, Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Yusuph Juma Mwenda pamoja na mambo mengine alisema lengo la TRA kuweka utaratibu huo ni kuwezesha biashara kufanyika kwa urahisi na kuondoa changamoto zilizokuwepo hapo awali huku akitoa wito kwa wafanyabiashara watakaokutana na changamoto zozote kuwasiliana na TRA.

Pamoja na mambo mengine pia Kamishina Mwenda alisema Mamlaka hiyo pia umeweka utaratibu wa kufanya kazi kwa Saa 24 ili kuharakisha utolewaji wa huduma kwa walipakodi ambao ni waingizaji, wasambazaji na wauzaji wa mafuta hayo.



DKT. AKWILAPO AKUTANA NA MTENDAJI MKUU WA SHELTER AFRIQUE

 


Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo (Kushoto) na Mtendaji Mkuu wa Shelter Afrique Bw.Thierno-Habib Hann wakiwa katika picha ya pamoja mara baada ya kikao chao jijini Nairobi, Kenya, walipokutana pembezoni mwa Kongamano la pili la Miji Afrika lilofanyika nchini humo.

Na Munir Shemweta, WANMM Nairobi

Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Dkt Leonard Akwilapo, amekutana na kufanya mazungumzo na Afisa Mtendaji Mkuu wa Shelter Afrique Bw. Thierno-Habib Hann jijini Nairobi, nchini Kenya.

Viongozi hao wawili wamekutana pembezoni mwa Kongamano la Miji Afrika (2nd Africa Urban Forum) lililofanyika kuanzia Aprili 8 hadi 10, 2026 nchini Kenya, na kukutanisha mataifa mbalimbali Barani Afrika kwa lengo la kubadilishana uzoefu na suluhisho bunifu katika kukabiliana na changamoto za maendeleo ya miji na makazi.

Dkt Akwilapo na Bw.Thierno-Habib Hann katika kikao chao walijadili masuala mbambali yanayohusu uimarishaji wa upatikanaji wa makazi nafuu kwa wananchi pamoja na ushirikiano kati ya serikali na taasisi za kifedha katika kufanikisha azma hiyo. 

Shelter Afrique ni taasisi ya kifedha ya kimataifa inayolenga kusaidia maendeleo ya makazi Barani Afrika, huku makao makuu yake makuu yakiwa jijini Nairobi nchini Kenya.

Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo (Kulia) akizungumza na Mtendaji Mkuu wa Shelter Afrique Bw.Thierno-Habib Hann jijini Nairobi, Kenya walipokutana pembezoni mwa Kongamano la pili la Miji Afrika (2ND Africa Urban Forum) lilofanyika nchini humo.
Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo (Kulia) akitambulishwa baadhi ya maafisa wa taasisi ya Shelter Afrique alipokutana na Mtendaji Mkuu wa taasisi hiyo Bw.Thierno-Habib Hann pembezoni mwa Kongamano la pili la Miji Afrika (2nd Africa Urban Forum) lilofanyika jijini Nairobi nchini Kenya. (PICHA ZOTE NA WIZARA YA ARDHI)

WABUNGE WAJENGEWA UWEZO WA HAKI MADINI NA HAKI ARDHI

  Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini imepatiwa mafunzo maalum kuhusu Sheria, Kanuni na Miongozo ya Sekta ya Madini, kwa lengo la...