Thursday, April 23, 2026

TUME YA RAIS YAWEKA WAZI TAKWIMU ZA MATUKIO YA UVUNJIFU WA AMANI





Na Ikulu, Dar es Salaam

Mwenyekiti wa Tume ya Rais ya Kuchunguza Matukio ya Uvunjifu wa Amani wakati na baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2025, Jaji Mkuu Mstaafu Mhe. Mohamed Chande Othman, amewasilisha muhtasari wa ripoti ya tume hiyo, akibainisha kwa takwimu ukubwa wa matukio yaliyotokea katika kipindi hicho.

Akiwasilisha taarifa hiyo Aprili 23, 2026 Ikulu jijini Dar es Salaam, Jaji Othman amesema jumla ya vifo 518 vilitokana na vurugu zilizojitokeza kabla na baada ya uchaguzi huo. Aidha, watu 373 walifikishwa hospitalini wakiwa wamefariki, huku majeruhi 121 wakipatiwa matibabu katika vituo mbalimbali vya afya.

Amesema takwimu hizo zinatokana na uchunguzi wa kina uliofanywa na tume kwa kushirikisha ushahidi kutoka kwa wadau mbalimbali, ikiwa ni pamoja na taasisi za Serikali, vyombo vya ulinzi na usalama pamoja na wananchi.

“Ripoti hii inalenga kuweka wazi hali halisi ya matukio yaliyotokea, kubainisha chanzo chake na kutoa mapendekezo yatakayosaidia kuzuia matukio ya aina hii yasijirudie,” ameeleza Jaji Othman.

Aidha, tume imeainisha umuhimu wa kuimarisha mifumo ya usimamizi wa uchaguzi, kuongeza uwajibikaji kwa taasisi husika pamoja na kuendeleza ushirikiano kati ya wadau wote wa kisiasa na kijamii ili kulinda amani ya Taifa.

Uwasilishaji wa ripoti hiyo unatajwa kuwa hatua muhimu katika kujenga uelewa wa pamoja, kuimarisha imani ya wananchi katika mifumo ya kidemokrasia na kuweka msingi imara wa uchaguzi wenye amani katika siku zijazo.

SERIKALI YAPELEKA TABASAMU KWA WANANCHI KUPITIA MIRADI YA MAENDELEO










Na OWM – TAMISEMI, Arusha

Wananchi katika maeneo mbalimbali nchini wanaendelea kunufaika moja kwa moja na utekelezaji wa miradi ya maendeleo inayotekelezwa katika Mamlaka za Serikali za Mitaa, hatua inayobadilisha kwa kasi hali ya upatikanaji wa huduma muhimu za kijamii na kuboresha maisha yao kwa ujumla.

Akizungumza Aprili 22, 2026 jijini Arusha, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM-TAMISEMI), Mhe. Prof. Riziki Shemdoe, amesema hatua ya Serikali chini ya uongozi wa Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kupeleka fedha nyingi kwenye halmashauri imekuwa na matokeo chanya yanayoonekana moja kwa moja kwa wananchi.

Amesema kupitia uwekezaji huo, wananchi sasa wanashuhudia maboresho katika sekta za afya, elimu, miundombinu na huduma nyingine za kijamii, hali inayorahisisha upatikanaji wa huduma na kuongeza ustawi wa jamii.

“Mafanikio haya yanaonekana wazi kwa wananchi—kuanzia upatikanaji wa huduma bora za afya, mazingira mazuri ya kujifunzia kwa wanafunzi, hadi kuboreshwa kwa miundombinu inayorahisisha shughuli za kiuchumi,” ameeleza Prof. Shemdoe.

Katika hatua nyingine, amewataka viongozi wa Mamlaka za Serikali za Mitaa kuhakikisha wanaendeleza kasi hiyo kwa kusimamia miradi kwa ufanisi na kuhakikisha inakidhi mahitaji halisi ya wananchi.

Aidha, amesisitiza umuhimu wa uwajibikaji, weledi na ushirikiano kati ya viongozi na watendaji ili kuhakikisha manufaa ya miradi hiyo yanaendelea kuwafikia wananchi kwa kiwango kikubwa zaidi.

Kauli hiyo imetolewa kabla ya kumkaribisha Waziri Mkuu Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba kufungua Mkutano Mkuu Maalum wa Uchaguzi wa Viongozi wa Jumuiya ya Tawala za Mitaa Tanzania (ALAT), unaofanyika Aprili 22 hadi 23, 2026 jijini Arusha.

Wednesday, April 22, 2026

MAKAMU WA RAIS ASHIRIKI IBADA YA KUMUAGA MAREHEMU ASKOFU MFUMBUSA


Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi akiwasili Katika Kanisa Kuu la Mtakatifu Paulo wa Msalaba , Jimbo Kuu Katoliki Dodoma, kushiriki Ibada ya kumuaga na kumuombea Askofu wa Jimbo Katoliki Kondoa, marehemu Askofu Bernadin Francis Mfumbusa, jana tarehe 21 Aprili 2026

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi akitoa heshima za mwisho kwa mwili wa Askofu wa Jimbo Katoliki Kondoa, marehemu Askofu Bernadin Francis Mfumbusa, mara baada ya Ibada ya kumuaga na kumuombea iliyofanyika Katika Kanisa Kuu la Mtakatifu Paulo wa Msalaba , Jimbo Kuu Katoliki Dodoma, jana tarehe 21 Aprili 2026.



Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi akishiriki Ibada ya kumuaga na kumuombea Askofu wa Jimbo Katoliki Kondoa, marehemu Askofu Bernadin Francis Mfumbusa, iliyofanyika Katika Kanisa Kuu la Mtakatifu Paulo wa Msalaba , Jimbo Kuu Katoliki Dodoma, jana tarehe 21 Aprili 2026.
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi amesema Taifa litaukumbuka mchango mkubwa aliyoutoa marehemu Askofu Bernadin Mfumbusa, enzi za uhai wake ikiwemo kuwa kiungo muhimu wa kuunganisha Kanisa Katoliki na Madhehebu mbalimbali pamoja na Dini zingine.

Makamu wa Rais amesema hayo mara baada ya kushiriki Ibada ya kumuaga na kumuombea Askofu wa Jimbo Katoliki Kondoa, marehemu Askofu Bernadin Francis Mfumbusa, iliyofanyika Katika Kanisa Kuu la Mtakatifu Paulo wa Msalaba, Jimbo Kuu Katoliki Dodoma.

Amesema Marehemu Askofu Mfumbusa alijitolea katika kuunganisha dini na madhehebu ili zifanye kazi kwa kuheshimiana, kushirikiana na kupendana. Ameongeza kwamba Taifa litakumbuka mchango wake katika kuhamasisha elimu pamoja na kufanya kazi kubwa ya kuhamasisha na kusimamia ujenzi na uendelezaji wa huduma za Afya katika Wilaya ya Kondoa na Taifa kwa ujumla.

Makamu wa Rais amesema Marehemu Askofu Mfumbusa ametoa mchango katika sekta ya Mawasiliano na Habari akiwa mbobezi na mwalimu katika fani hiyo. Amesema Marehemu Mfumbusa atakumbukwa kwa kutimiza wajibu wake kwa binadamu kwa kutambua Maisha tunayoishi leo, na kutimiza wajibu wake kwa Mungu kwa kutuongoza katika njia ya uzima wa milele.

Aidha Makamu wa Rais amewasilisha salamu za pole za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, alizotoa kwa Kanisa, Waumini na Familia na kuiombea familia nguvu na uvumilivu katika kipindi hiki kigumu.

Makamu wa Rais amewashukuru Viongozi wa Kanisa Katoliki kwa malezi ya marehemu Askofu Mfumbusa ambayo yalimfanya kuwa mtume wa Taifa zima.

Ibada hiyo, imeongozwa na Askofu Msaidizi wa Jimbo Kuu Katoliki Dodoma Mhashamu Wilbroad Kibozi na kuhudhuriwa na Maaskofu mbalimbali, Mapadre, Watawa, Viongozi mbalimbali wa Serikali na Wananchi.

Imetolewa na
Ofisi ya Makamu wa Rais
21 Aprili 2026
Dodoma.

NHC NA SKAUTI TANZANIA WAIMARISHA USHIRIKIANO KUPITIA UBIA







Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) limeendelea kupanua wigo wa ushirikiano wake kwa taasisi mbalimbali baada ya kufanya kikao maalum na viongozi wa Skauti Tanzania, kikilenga kujadili fursa za ubia katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo.

Kikao hicho kiliwakutanisha viongozi wa ngazi ya juu kutoka Skauti Tanzania akiwemo Mwenyekiti wa Bodi, Bethi Mkwasa, pamoja na wajumbe wa bodi Juma Dossa na Marry. 

Wengine waliohudhuria ni Kamishna wa SkautiTanzania, Hellen Mkami, pamoja na wajumbe wa kamati ya ubia, akiwemo Nassoro Abubakari.

Katika kikao hicho, viongozi hao walipata ufafanuzi wa kina kuhusu namna ambavyo NHC inatekeleza miradi kupitia mfumo wa ubia (PPP), ikiwemo aina mbalimbali za ubia zinazotekelezwa, taratibu za kuingia ubia, pamoja na vigezo vinavyotumika kuchagua washirika.

Aidha, faida za kuingia ubia na NHC zilielezwa kwa kina, zikiwemo uendelezaji wa ardhi kwa tija, uhakika wa uwekezaji wenye tija, pamoja na mchango wake katika kukuza uchumi na huduma za kijamii.

Kikao hicho kimeelezwa kuwa ni hatua muhimu katika kujenga msingi wa ushirikiano madhubuti kati ya NHC na Skauti Tanzania, unaotarajiwa kufungua fursa mpya za uwekezaji na maendeleo yenye manufaa kwa pande zote pamoja na jamii kwa ujumla.

SERIKALI YAHAKIKISHA UPATIKANAJI WA MAFUTA LICHA YA CHANGAMOTO ZA KIMATAIFA






Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius J. Ndejembi (Mb.), akiwasilisha Hotuba ya Bajeti ya Wizara ya Nishati na Taasisi zake kwa Mwaka wa Fedha 2026/27, leo, tarehe 22 Aprili 2026, Bunge jijini Dodoma.

Na Mwandishi Wetu, Dodoma

Serikali imesema itaendelea kuhakikisha upatikanaji wa uhakika wa mafuta nchini licha ya changamoto za kimataifa zinazoathiri mnyororo wa usambazaji wa nishati hiyo , ikiwemo vita inayoendelea katika Ukanda wa Mashariki ya Kati.

Akizungumza bungeni jijini Dodoma wakati wa uwasilishaji wa Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati kwa Mwaka wa Fedha 2026/27 ,Waziri wa Nishati, Mhe. Dkt. Deogratius Ndejembi, alisema kuwa Serikali imeweka mikakati madhubuti ya kuhakikisha wananchi wanapata bidhaa za mafuta ya petroli kwa uhakika.

“Sambamba na kuimarika kwa upatikanaji wa umeme, nchi yetu pia imeendelea kuwa na uhakika wa upatikanaji wa bidhaa za mafuta ya petroli licha ya changamoto za kimataifa zilizotokana na vita baina ya Marekani, Israel na Iran,” alisema Mhe. Ndejembi.

Alifafanua kuwa vita hiyo imesababisha athari kubwa katika usambazaji wa mafuta duniani, ikiwemo kufungwa kwa Mlango Bahari wa Hormuz ambao hupitisha zaidi ya asilimia 20 ya mafuta yote duniani, pamoja na kuathiri miundombinu ya uzalishaji na uhifadhi wa mafuta.

“Hali hii imeathiri kwa kiasi kikubwa nchi za Mashariki ya Kati ambako Tanzania inaagiza takribani asilimia 59 ya mafuta yake, huku asilimia 41 ikitoka India ambayo nayo hutegemea mafuta ghafi kutoka ukanda huo huo,” aliongeza.

Kutokana na hali hiyo, Waziri Ndejembi alisema Serikali imechukua hatua za haraka na za kimkakati ili kulinda usalama wa nishati nchini. Moja ya hatua hizo ni kuliwezesha Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) kuagiza mafuta ya kutosha kwa kipindi cha miezi mitatu ijayo.

Aidha, alisema Serikali inaendelea kufuatilia kwa karibu mwenendo wa soko la mafuta duniani na iko tayari kuchukua hatua zaidi kulingana na mabadiliko yatakayotokea

Tuesday, April 21, 2026

RAIS SAMIA AGAWA MITUNGI YA GESI NA KUVAA VAZI LA MAMA NA BABA LISHE KUHAMASISHA NISHATI SAFI






Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, ameendeleza dhamira ya Serikali ya kusukuma mbele ajenda ya nishati safi na lishe bora kwa vitendo, baada ya kushiriki kikamilifu katika shughuli za Mama na Baba Lishe zilizofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC), jijini Dar es Salaam, tarehe 21 Aprili, 2026.

Mara baada ya kuwasili katika ukumbi huo, Rais Samia alipata fursa ya kukagua mabanda ya maonesho ya mapishi yaliyoandaliwa na Mama na Baba Lishe kutoka maeneo mbalimbali ya nchi. Katika ziara hiyo, alijionea ubunifu wa wahudumu hao katika kuandaa vyakula salama na vyenye kuzingatia viwango vya lishe, huku akisisitiza umuhimu wa kuboresha ubora wa huduma za chakula kama sehemu ya kulinda afya za Watanzania.

Akizungumza na washiriki wa maonesho hayo, Rais Samia alibainisha kuwa sekta ya Mama na Baba Lishe ina mchango mkubwa katika ajira na uchumi wa watu wa kipato cha chini, hivyo inahitaji kuendelezwa kwa kuzingatia usalama wa chakula, usafi na matumizi ya teknolojia rafiki kwa mazingira.

Katika hatua nyingine yenye uzito wa kipekee, Rais Samia aligawa mitungi ya gesi kwa Mama na Baba Lishe ikiwa ni sehemu ya juhudi za Serikali kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia. Hatua hiyo inalenga kupunguza utegemezi wa nishati chafu kama kuni na mkaa, ambayo imekuwa na athari hasi kwa afya na mazingira.

Ugawaji huo wa mitungi ya gesi umechukuliwa kama chachu ya mabadiliko kwa wahudumu hao, wengi wao wakiwa wanawake, kwa kuwa utawawezesha kupunguza gharama za uendeshaji, kuongeza ufanisi wa kazi, na kulinda afya zao dhidi ya madhara ya moshi.

Tukio hilo limeonesha kwa vitendo mwelekeo wa Serikali katika kuunganisha ajenda ya lishe bora, afya ya jamii na matumizi ya nishati safi, huku likitoa ujumbe mpana wa kuwahamasisha Watanzania kubadili mtindo wa maisha kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.

RAIS SAMIA ATUNUKIWA TUZO YA “MALKIA WA NISHATI SAFI”








Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, ametunukiwa Tuzo ya Heshima ya “Malkia wa Nishati Safi” ikiwa ni ishara ya kutambua mchango wake mkubwa katika kuhamasisha matumizi ya nishati safi na kulinda afya za jamii pamoja na mazingira.

Tuzo hiyo imetolewa na Umoja wa Mama na Baba Lishe Tanzania (UMALITA), kupitia Mwenyekiti wake Bi. Havijawa Omary, katika hafla iliyofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC), jijini Dar es Salaam, tarehe 21 Aprili, 2026.

Akizungumza wakati wa tukio hilo, Bi. Havijawa alisema kuwa Dkt. Samia amekuwa kinara wa mageuzi katika sekta ya nishati safi nchini, hususan katika kuhimiza matumizi ya nishati mbadala kwa ajili ya kupikia, hatua inayolenga kupunguza athari za kiafya na kimazingira zitokanazo na matumizi ya kuni na mkaa. 

Alieleza kuwa juhudi hizo zimechangia kuboresha ustawi wa familia nyingi, hasa wanawake na watoto ambao ndio waathirika wakuu wa moshi unaotokana na nishati chafu.

Kwa upande wake, Rais Samia alipokea tuzo hiyo kwa shukrani, akisisitiza dhamira ya Serikali ya kuendelea kuweka mazingira wezeshi yatakayoharakisha upatikanaji na matumizi ya nishati safi kwa Watanzania wote.

Alibainisha kuwa ajenda ya nishati safi siyo tu ya mazingira, bali pia ni suala la afya ya umma na maendeleo endelevu ya taifa.

Hafla hiyo ilihudhuriwa na wadau mbalimbali wa sekta ya lishe, afya, mazingira na nishati, ambapo ilitumika pia kama jukwaa la kuhimiza ushirikiano wa taasisi na jamii katika kuendeleza matumizi ya nishati safi nchini.

Tuzo ya “Malkia wa Nishati Safi” inaendelea kuwa alama ya kutambua viongozi na wadau wanaochochea mabadiliko chanya katika matumizi ya nishati rafiki kwa mazingira, hatua inayochangia kwa kiasi kikubwa utekelezaji wa ajenda ya maendeleo endelevu nchini.

TUME YA RAIS YAWEKA WAZI TAKWIMU ZA MATUKIO YA UVUNJIFU WA AMANI

Na Ikulu, Dar es Salaam Mwenyekiti wa Tume ya Rais ya Kuchunguza Matukio ya Uvunjifu wa Amani wakati na baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 20...