Wednesday, March 25, 2026

WILLIAM LUKUVI: SAFARI YA MWALIMU ALIYEGUSA TAIFA, SAUTI ILIYOJENGA SIASA ZA HUDUMA

Marehemu William Vangimembe Lukuvi alizaliwa Agosti 15, 1955 katika kijiji cha Mapogoro, mkoani Iringa—mahali palipomlea katika misingi ya nidhamu, uwajibikaji na uzalendo, ambavyo vilikuja kuwa alama ya maisha yake ya uongozi.

Alianza safari yake ya elimu katika Shule ya Msingi Kitanewa mwaka 1962 hadi 1970, kabla ya kujiunga na Chuo cha Ualimu Tabora (Tabora TTC) mwaka 1974 hadi 1975, alipohitimu na kuwa mwalimu. 

Akiwa darasani, hakufundisha tu masomo—alijenga misingi ya maadili na kuwasha taa za matumaini kwa kizazi cha vijana. Hata hivyo, ndani yake kulikuwa na wito mpana zaidi: wito wa kulitumikia taifa.

Mwaka 1995, alipochaguliwa kuwa Mbunge wa Jimbo la Ismani, ndipo safari yake ya kisiasa ilipoanza rasmi. Hakuwa tu mwakilishi wa wananchi; alikuwa sauti yao. Kwa zaidi ya miaka 30 mfululizo, alibaki kuwa chaguo la wananchi wake—uthibitisho wa imani, ukaribu na uaminifu alioujenga kwa vitendo.

Katika utumishi wake serikalini, Lukuvi alionyesha uthabiti na uelewa mpana wa masuala ya umma. Kuanzia mwaka 2010 hadi 2015, alihudumu kama Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera na Bunge), akisimamia uratibu wa shughuli za serikali bungeni kwa umahiri mkubwa. 

Baadaye, kati ya mwaka 2015 hadi 2022, aliongoza Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi—sekta nyeti inayogusa maisha ya kila Mtanzania—akiwa mstari wa mbele katika kusimamia rasilimali ardhi na mageuzi ya makazi.

Mwaka 2023, aliaminiwa zaidi na kuteuliwa kuwa mshauri wa Rais katika masuala ya kisiasa na kijamii, jukumu lililodhihirisha hekima yake ya muda mrefu. Alirejea tena serikalini kushika wadhifa wa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu), nafasi aliyoiendeleza kwa uadilifu na uzito hadi siku za mwisho za maisha yake.

Mnamo Machi 25, 2026, taifa lilipokea kwa masikitiko taarifa ya kifo chake, iliyotangazwa rasmi na Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan. Alifariki dunia katika Hospitali ya Benjamin Mkapa, Dodoma, alipokuwa akipatiwa matibabu ya matatizo ya moyo.

Kifo chake si tu mwisho wa maisha ya mtu—ni hitimisho la sura muhimu ya uongozi wa kizazi chake. Lukuvi alikuwa daraja kati ya wananchi na serikali, kiongozi aliyesikiliza, aliyetenda, na aliyesimama imara hata katika nyakati ngumu. 

Alibeba uzito wa dhamana ya umma kwa ujasiri na kuacha alama isiyofutika katika historia ya siasa za Tanzania.

Urithi wake unabaki kuwa funzo: kwamba uongozi si cheo, bali ni huduma; si mamlaka, bali ni uwajibikaji; na si maneno, bali ni vitendo vinavyoacha alama mioyoni mwa watu.

PIC YAAHIRISHA ZIARA BAADA YA KIFO CHA WAZIRI LUKUVI

Mkurugenzi Mkuu wa NHC Hamad Abdallah akimpokea Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma - PIC na wajumbe wake Mhe. Massanja Kadogosa walipowasili katika mradi wa Samia Housing Scheme Kawe.



Mkurugenzi Mkuu wa NHC Hamad Abdallah akiionesha Kamati ya PIC eneo ambalo zitajengwa nyumba nyingine za makazi pembeni ya mradi wa Samia Housing Scheme Kawe.


Mhandisi Grace Musita akiielezea Kamati ya PIC kwa undani kuhusu mradi wa Samia Housing Scheme Kawe.


Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma - PIC wakiingia katika moja ya nyumba.

Afisa sheria wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Elizabeth Malogo akisoma kanuni ya kuahirisha ziara hiyo

Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma - PIC Mhe. Massanja Kadogosa akihairisha ziara hiyo

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma (PIC) imeahirisha ziara yake katika miradi ya Samia Housing na 711 Kawe inayotekelezwa na Shirika la Nyumba la Taifa (NHC).

Mwenyekiti wa PIC, Masanja Kadogosa amewatangazia wajumbe wa kamati hiyo kuwa uamuzi huo umefikiwa kufuatia kifo cha Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Wenye Ulemavu), Mhe. William Lukuvi, kilichotokea leo Machi 25, 2026 katika Hospitali ya Benjamin Mkapa jijini Dodoma alipokuwa akipatiwa matibabu.

Kabla ya kuahirishwa kwa ziara hiyo, Kamati hiyo ilikuwa imetembelea mradi wa Samia Housing Scheme uliopo Kawe na kujionea uwekezaji mkubwa uliofanywa na NHC katika eneo hilo. Akiwa na wajumbe wa kamati hiyo, Mwenyekiti Kadogosa alipata fursa ya kusikiliza maelezo ya utekelezaji wa mradi huo kutoka kwa Mkurugenzi Mkuu wa NHC, Hamad Abdallah.

Katika maelezo yake, Mkurugenzi Mkuu alibainisha kuwa mradi huo wa majengo ya ghorofa kumi, unaojumuisha jumla ya nyumba 560, ulitekelezwa kikamilifu na wahandisi wa Shirika la Nyumba la Taifa, hatua inayodhihirisha uwezo wa ndani wa taasisi hiyo katika kusimamia na kutekeleza miradi mikubwa ya kimkakati.

Akitoa ufafanuzi wa kina kuhusu mradi huo, Msimamizi wa Utekelezaji, Mhandisi Grace Musita, alisema kuwa majengo hayo yanajumuisha nyumba za vyumba vitatu zenye ukubwa wa mita za mraba 89, ambazo zimeuzwa kwa shilingi milioni 192.7. 

Aidha, kuna nyumba 160 za vyumba viwili zenye ukubwa wa mita za mraba 68, zilizouzwa kwa shilingi milioni 147, pamoja na nyumba ndogo zenye ukubwa wa mita za mraba 21.2 zilizouzwa kwa shilingi milioni 38.8.

Aliongeza kuwa mradi huo ulianza Novemba 2022 na kukamilika Juni 2025, ambapo kwa sasa wakazi tayari wameanza kuishi, huku Shirika likiendelea kushughulikia dosari ndogo ndogo zinazojitokeza ili kuboresha zaidi huduma kwa wateja.

Mhandisi Musita alibainisha kuwa mradi huo umeleta manufaa makubwa kijamii na kiuchumi, ikiwemo kuzalisha ajira 11,800 kwa mafundi na wataalamu mbalimbali. Pia wanafunzi 630 kutoka taasisi mbalimbali ikiwemo Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na Taasisi ya Teknolojia Dar es Salaam (DIT) walipata mafunzo ya vitendo, ambapo kati yao wanafunzi 47 walipata ajira za kudumu na muda mfupi. Vilevile, vibarua 100 wasio na elimu rasmi lakini wenye nidhamu walipata ajira kupitia mradi huo.

Alisisitiza kuwa NHC ilitekeleza mradi huo kwa viwango vya juu kwa kuwa mkandarasi na mbunifu, huku malighafi zote zilizotumika zikifanyiwa vipimo na taasisi mbalimbali ikiwemo Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na Shirika la Viwango Tanzania (TBS), pamoja na kukaguliwa na mamlaka husika za Kinondoni na wataalamu wa ndani wa NHC.

Aidha, alieleza kuwa matumizi ya mitambo ya kisasa inayomilikiwa na Shirika, ikiwemo mtambo mkubwa wa kuzalisha zege, magari ya kusafirisha zege na pampu, yalichangia kukamilika kwa mradi huo kwa wakati na kwa ufanisi mkubwa.

Mradi wa Samia Housing Scheme Kawe umegharimu jumla ya shilingi bilioni 49, ambapo hadi sasa takribani shilingi bilioni 45 tayari zimetumika.

Hata hivyo, ziara ya Kamati hiyo haikuweza kuendelea katika mradi wa Kawe 711 kufuatia tukio hilo la msiba. Akisoma kanuni za kudumu za Bunge, Afisa Sheria wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Elizabeth Malogo, alinukuu kanuni namba 176 inayotaka shughuli za Bunge kuahirishwa endapo Mbunge atafariki dunia wakati wa shughuli za Bunge, ili kutoa nafasi kwa maombolezo.

Tuesday, March 24, 2026

SERIKALI YAIMARISHA UPATIKANAJI WA MAFUTA YA PETROLI NCHINI MALAWI







Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

Serikali kupitia Bandari ya Dar es Salaam imeendelea kuwa nguzo muhimu ya upatikanaji wa mafuta kwa nchi jirani ya Malawi, hatua inayochochea shughuli za kiuchumi na kuboresha maisha ya wananchi wa nchi hizo mbili.

Akizungumza wakati wa ziara ya kukagua miundombinu ya mafuta katika Kituo cha Kurasini Oil Jet (KOJ-1), kilichopo katika Bandari ya Dar es Salaam, Waziri wa Nishati na Madini wa Malawi, Mhe. Dkt. Jean Mathanga, aliishukuru Serikali ya Tanzania kwa mchango wake mkubwa katika kuwezesha mtiririko wa mafuta kwenda nchini Malawi.

Alisema kuwa kutokana na Malawi kutokuwa na bandari, nchi hiyo inategemea kwa kiasi kikubwa miundombinu ya nchi jirani, hususan Tanzania, katika kuhakikisha upatikanaji wa mafuta unaendelea kuwa wa uhakika.

Alibainisha kuwa ziara hiyo imelenga kujionea kwa vitendo namna mafuta yanavyopokelewa na kusimamiwa bandarini ili kuboresha mipango ya ununuzi na usambazaji wa mafuta nchini Malawi. 

Kwa upande wake, Mwakilishi wa Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Uagizaji Mafuta kwa Pamoja (PBPA), ambaye ni Mkurugenzi wa Uendeshaji wa Petroli PBPA, Mhandisi Bruno Tarimo, alifafanua kuwa sehemu kubwa ya mafuta yanayoingia Malawi hupitia Tanzania kupitia Mfumo wa Uagizaji Mafuta kwa Pamoja (BPS), huku wakati mwingine nchi hiyo ikiagiza moja kwa moja kutoka kwa wazabuni wake.

Sunday, March 22, 2026

UWEKEZAJI USAFIRI KANDA YA ZIWA KUCHOCHEA UCHUMI, WAWEKEZAJI WAHIMIZWA KUTUMIA FURSA


 Na Baltazar Mashaka, Mwanza

Serikali imesema uwekezaji mkubwa unaoendelea kufanywa katika sekta ya usafiri na usafirishaji Kanda ya Ziwa utachochea ukuaji wa uchumi wa Tanzania na nchi jirani za Ukanda wa Maziwa Makuu, huku ikiwahimiza wawekezaji wa sekta binafsi kutumia fursa zinazojitokeza katika eneo hilo.

 Kauli hiyo ilitolewa leo, jijini Mwanza na Msemaji Mkuu wa Serikali na Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Gerson Msigwa, alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari kuhusu maendeleo ya miradi mbalimbali ya serikali.

Msigwa alisema ujenzi wa meli kubwa ya kisasa ya New MV Mwanza ni sehemu ya juhudi za serikali kuboresha miundombinu ya usafiri katika Ziwa Victoria, hatua itakayofungua fursa mpya za kiuchumi hususan katika sekta ya utalii na biashara.

Alisisitiza kuwa serikali imeweka mazingira wezeshi kwa wawekezaji, hivyo wadau wa utalii wanapaswa kujitokeza kuwekeza ili kunufaika na ongezeko la shughuli za kiuchumi katika Kanda ya Ziwa.

Msemaji Mkuu huyo wa Serikali alisema, meli hiyo yenye uwezo wa kubeba abiria 1,200 na tani 400 za mizigo itakuza biashara na uchumi, itaimarisha usafiri wa majini kati ya Mwanza na miji ya Jinja na Port Bell nchini Uganda pamoja na Kisumu nchini Kenya.

Kwa mujibu wa Msigwa, hatua hiyo itaongeza mzunguko wa biashara na kukuza uchumi wa bidhaa mbalimbali zikiwemo pamba, madini, samaki, nyama na maziwa, huku akionya kuwa serikali haitaridhika kuona uwekezaji huo mkubwa unakosa tija.

Akizungumzia mradi wa reli ya kisasa ya kiwango cha kimataifa (SGR), Msigwa alisema ni uwekezaji mkubwa wenye thamani ya dola za Marekani bilioni 12 unaolenga kuimarisha uchumi wa taifa na nchi jirani.

Alieleza kuwa ujenzi unaendelea katika vipande mbalimbali, huku lengo likiwa ni kufikisha reli hiyo Mwanza ifikapo mwaka 2028 ili kurahisisha usafirishaji wa mizigo na kuongeza ufanisi wa biashara za kikanda.

Aidha, alisema serikali inaendelea na mipango ya kujenga reli ya kisasa inayotumia umeme yenye uwezo wa kusafirisha tani 10,000 za mizigo kutoka Bandari ya Dar es Salaam pamoja na meli nyingine ya mizigo katika Ziwa Victoria na Ziwa Tanganyika.

Alibainisha kuwa uwekezaji huo wa kimkakati utaongeza matumizi ya reli, kukuza biashara na kuchochea mageuzi ya kiuchumi kwa wananchi, huku Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 ikilenga kufikia pato la mtu mmoja mmoja la dola 7,000 kwa mchango mkubwa wa sekta binafsi.

MAKAMU WA RAIS AONGOZA KILELE CHA WIKI YA MAJI 2026, ATOA WITO KUIMARISHA ULINZI WA VYANZO VYA MAJI NCHINI











Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Emmanuel Nchimbi, ametoa wito kwa mamlaka husika pamoja na wananchi wote kuweka kipaumbele katika utunzaji na ulinzi wa vyanzo vya maji, akisisitiza kuwa rasilimali hiyo ni msingi wa maendeleo endelevu na urithi muhimu kwa vizazi vijavyo.

Makamu wa Rais aliyasema hayo alipomwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, katika Maadhimisho ya Kilele cha Wiki ya Maji 2026 sambamba na Siku ya Maji Duniani, yaliyofanyika katika Viwanja vya Mkwawa mkoani Morogoro tarehe 22 Machi 2026.

Amesisitiza umuhimu wa kufanya uwekezaji wa kimkakati unaolenga kulinda na kuongeza vyanzo vya maji ili kuhakikisha upatikanaji endelevu wa huduma hiyo muhimu kwa wananchi wote. Aidha, ametoa rai kwa wizara na taasisi za umma kujenga ushirikiano thabiti utakaowezesha kukabiliana kwa pamoja na changamoto zinazoikabili sekta ya maji nchini.

Katika hatua ya kuimarisha sekta hiyo, Makamu wa Rais amezitaka mamlaka za maji kubuni vyanzo mbadala vya mapato ili kuongeza ufanisi wa utekelezaji wa miradi. Ameipongeza Mamlaka ya Maji Tanga kwa kutumia mfumo wa hati fungani (bonds) kugharamia miradi ya maji, akieleza kuwa ubunifu huo ni mfano wa kuigwa kitaifa.

Vilevile, amesisitiza umuhimu wa sekta binafsi kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya miradi ya maji, akieleza kuwa ushirikiano kati ya serikali na wadau binafsi ni nguzo muhimu ya kufanikisha upatikanaji wa huduma bora na endelevu.

Makamu wa Rais pia ameelekeza juhudi zaidi katika utekelezaji wa Mpango wa Gridi ya Taifa ya Maji, akibainisha kuwa kukamilika kwake kutakuwa suluhisho la kudumu la changamoto ya maji nchini. Aidha, ameitaka Wizara ya Maji kuhakikisha ufungaji wa mita za maji unaimarishwa ili kudhibiti upotevu na kuongeza uwajibikaji kwa watumiaji.

Akizungumzia dira ya maendeleo ya taifa, amesema kuwa Dira ya Maendeleo 2050 inalenga kuifanya Tanzania kuwa nchi ya kipato cha kati ngazi ya juu, huku ikikabiliwa na ongezeko la idadi ya watu litakalofikia takriban milioni 118. Alisisitiza kuwa hali hiyo inahitaji mipango madhubuti ya kuhakikisha upatikanaji wa huduma muhimu za kijamii ikiwemo maji safi na salama.

Kwa mujibu wa takwimu za Sera ya Taifa ya Maji ya Mwaka 2002 (Toleo la 2025), upatikanaji wa maji umeendelea kuimarika ambapo huduma hiyo imefikia wastani wa asilimia 85.2 vijijini na asilimia 92.5 mijini. Jumla ya vijiji 10,758 tayari vimefikiwa na huduma hiyo, huku jitihada maalum zikiendelea kuhakikisha vijiji vilivyosalia vinaunganishwa na huduma ya maji.

Kwa upande wake, Waziri wa Maji, Jumaa Aweso, alimshukuru Rais kwa kuwezesha utekelezaji wa miradi ya maji kwa ufanisi, akiahidi kuwa wizara hiyo itaendelea kuhakikisha wananchi wanapata huduma ya maji safi na salama bila vikwazo.

Katika kuimarisha matumizi ya teknolojia, Makamu wa Rais alizindua Mfumo wa Utabiri wa Kiasi cha Maji katika mito nchini, katika eneo la Bwawa la Mindu mjini Morogoro. Mfumo huo unatarajiwa kuboresha upatikanaji wa taarifa sahihi za kiwango cha maji na kusaidia kupanga matumizi na uhifadhi wake kwa ufanisi zaidi.

Kama sehemu ya maadhimisho hayo, Makamu wa Rais pia alipanda miti rafiki wa maji katika eneo la chanzo hicho, akihamasisha utunzaji wa mazingira kama nguzo muhimu ya kulinda rasilimali za maji.

Maadhimisho ya mwaka huu yalibebwa na kaulimbiu “Maji na Usawa wa Kijinsia,” ikilenga kuangazia uhusiano kati ya upatikanaji wa maji safi na usawa wa kijinsia katika jamii. Ripoti mbalimbali zinaonesha kuwa ukosefu wa maji safi na huduma bora za usafi wa mazingira unaathiri kwa kiasi kikubwa uchumi wa nchi nyingi barani Afrika, hususan Kusini mwa Jangwa la Sahara.

Kwa ujumla, maadhimisho hayo yamekuwa jukwaa muhimu la kuimarisha uelewa, kuongeza ushirikiano na kuhamasisha hatua za pamoja katika kuhakikisha Tanzania inafikia malengo ya kuwa na upatikanaji wa maji safi, salama na endelevu kwa wananchi wote.

MSIGWA: SERIKALI IMEWEKEZA ZAIDI YA TRILIONI 1 USAFIRI WA MAJINI


Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo na Msemaji Mkuu wa Serikali, Ndg, Gerson Msigwa, akizungumza na waandishi wa habari kuhusu miradi ya maendeleo inayotekelezwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika Mkoa wa Mwanza, leo Machi 22, 2026, katika Bandari ya Mwanza South, jijini Mwanza

Na. Fullshangwe Blog, Mwanza

Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo ambaye pia ni Msemaji Mkuu wa Serikali, Bw. Gerson Msigwa, amesema kuwa Serikali ya Awamu ya Sita inaendelea kutekeleza miradi ya usafiri na usafirishaji majini yenye thamani ya zaidi ya shilingi trilioni moja katika maziwa ya Victoria, Tanganyika na Nyasa pamoja na Bahari ya Hindi.

Amesema kuwa meli ya MV Mwanza ni moja ya mafanikio makubwa ambapo ina uwezo wa kubeba abiria 1,200 na mizigo tani 400, na ni miongoni mwa meli kubwa zaidi katika maji baridi barani Afrika.

Aidha, amebainisha kuwa ujenzi wa meli hiyo umegharimu shilingi bilioni 123 na ulikuwa umefikia asilimia 40 wakati Rais Samia Suluhu Hassan anaingia madarakani mwaka 2021, lakini sasa umekamilika kwa asilimia 100.

Pia ameongeza kuwa vijana takribani 200 wakiwemo mainjinia na mafundi walipata ujuzi kwa kushirikiana na wakandarasi kutoka Korea katika ujenzi wa meli hiyo.

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NJE WA AUSTRIA AWASILI NCHINI KWA ZIARA YA KIKAZI










Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Austria anayeshughulikia masuala ya kisiasa, Mheshimiwa Balozi Dkt. Hannah Liko, amewasili nchini Machi 22, 2026 kwa ziara ya kikazi ya siku tatu inayolenga kuimarisha uhusiano wa kidiplomasia, biashara na ushirikiano katika maeneo mbalimbali kati ya Tanzania na Austria.

Akiwasili katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere, Dkt. Liko amepokelewa na Balozi na Mwakilishi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania jijini Vienna, Mhe. Naimi S. Aziz, pamoja na Balozi wa Austria nchini, mwenye makazi yake jijini Nairobi nchini Kenya Mhe. Dkt. Christian Fellner.

Wakati wa ziara hiyo, Dkt. Liko anatarajiwa kufanya mazungumzo na viongozi mbalimbali akiwemo Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Ngwaru Maghembe (Mb.), pamoja na viongozi kutoka wizara mbalimbali zikiwemo Ofisi ya Rais (Mipango na Uwekezaji), Wizara ya Fedha, Wizara ya Mambo ya Ndani na Wizara ya Viwanda na Biashara.

Aidha, anatarajiwa kutembelea Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) kwa lengo la kuimarisha ushirikiano katika nyanja za kitaaluma na elimu ya juu. Ziara hiyo inatarajiwa kuhitimishwa Machi 25, 2026

WILLIAM LUKUVI: SAFARI YA MWALIMU ALIYEGUSA TAIFA, SAUTI ILIYOJENGA SIASA ZA HUDUMA

Marehemu William Vangimembe Lukuvi alizaliwa Agosti 15, 1955 katika kijiji cha Mapogoro, mkoani Iringa—mahali palipomlea katika misingi ya n...