Monday, July 06, 2026

RAIS SAMIA AMTEMBELEA PACOME, AMPATIA POLE NA KUMTAKIA AFYA NJEMA

 



Dar es Salaam – Mchezaji wa klabu ya Yanga, Pacome Zouzoua, amepata faraja ya kipekee baada ya kutembelewa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, alipokuwa akipatiwa matibabu katika Hospitali ya Aga Khan, jijini Dar es Salaam.

Rais Samia alikuwa hospitalini hapo kwa ajili ya kumjulia hali Sheikh Rashid Hamad Othman, lakini alipojulishwa kuwa Pacome amelazwa katika chumba jirani akipatiwa matibabu kufuatia majeraha aliyoyapata kwenye mchezo wa Ligi Kuu ya NBC dhidi ya JKT Tanzania, alitumia fursa hiyo kumtembelea na kumpa pole.

Hatua hiyo imeonesha moyo wa upendo na kujali kwa viongozi wakuu wa Taifa kwa wanamichezo, ikisisitiza nafasi muhimu ambayo michezo inaendelea kuwa nayo katika kuunganisha Watanzania.

Mashabiki wa soka nchini wanaendelea kumuombea Pacome apone haraka na kurejea uwanjani kuendelea kuonesha kipaji chake na kuiburudisha Yanga pamoja na wapenzi wa soka kwa ujumla.

Tunamtakia Pacome Zouzoua nafuu ya haraka na kurejea uwanjani akiwa imara zaidi. πŸ’š⚽

RAIS MWINYI ATOA SH. MILIONI 200 KWA KITUO CHA IRSHAAD LUSHOTO, ARIDHIA MAOMBI YA PROF. SHEMDOE

 










Na OWM – TAMISEMI, Lushoto

Rais wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, ametoa Shilingi Milioni 200 kwa ajili ya kuendeleza Kituo cha Elimu ya Kiislamu Irshaad (Irshaad Islamic Centre) kilichopo Lushoto, Mkoa wa Tanga, kufuatia ombi lililotolewa na Mbunge wa Jimbo la Lushoto na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, Mhe. Prof. Riziki Shemdoe.

Msaada huo utasaidia kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo katika kituo hicho, ikiwemo kuboresha Chuo cha Ufundi, kujenga madrasa ya kisasa, nyumba za walimu, hospitali, ukumbi wa mikutano, jengo la wageni pamoja na bustani ya kisasa, hatua inayotarajiwa kuongeza ubora wa elimu na huduma za kijamii kwa wananchi wa Lushoto na maeneo jirani.

Prof. Shemdoe aliwasilisha ombi hilo wakati wa Sherehe ya Maulidi ya Kumswalia Mtume Muhammad (S.A.W.) zilizofanyika Julai 5, 2026 katika Kituo cha Irshaad Islamic Centre, ambapo Mhe. Dkt. Hussein Mwinyi alikuwa Mgeni Rasmi.

Katika tukio hilo, Rais Mwinyi pia alikubali ombi la Sheikh Sharrif Hussein Ahmad Badawiyy la kuwa Mlezi wa Kituo cha Irshaad Islamic Centre, akiahidi kuendelea kushirikiana na viongozi na wadau mbalimbali katika kukiendeleza ili kiwe kitovu cha elimu bora, maadili mema na maendeleo ya jamii.

Aidha, Rais Mwinyi aliridhia ombi la kutambua mchango wa Hayati Alhaji Ali Hassan Mwinyi kwa kuruhusu bustani itakayojengwa ndani ya Chuo cha Ufundi cha kituo hicho kuitwa jina lake, ikiwa ni sehemu ya kuenzi mchango wake mkubwa katika maendeleo ya taasisi hiyo.

Wito wa Prof. Shemdoe uliungwa mkono na viongozi mbalimbali waliochangia kwa hiari yao, akiwemo yeye mwenyewe aliyetoa Shilingi Milioni 20, Mkuu wa Mkoa wa Tanga Dkt. Batilda Burian (Milioni 5), Mkuu wa Mkoa wa Morogoro Mhe. Adam Malima (Milioni 5), Mbunge wa Bumbuli Mhandisi Ramadhani Hamza (Milioni 5), Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Tanga Bw. Rajab Abdallah (Milioni 3) na Mbunge wa Afrika Mashariki Dkt. Abdullah Makame (Milioni 5), na kufanya jumla ya michango kufikia Shilingi Milioni 248.

Akizungumza baada ya hafla hiyo, Prof. Shemdoe alimshukuru Rais Mwinyi kwa kukubali ombi hilo, akieleza kuwa msaada huo utakuwa chachu ya kuimarisha elimu, kukuza ustawi wa jamii na kuboresha huduma zinazotolewa na Kituo cha Irshaad.

Wananchi na viongozi waliohudhuria hafla hiyo walimpongeza Rais Mwinyi kwa uamuzi huo, wakieleza kuwa utaacha alama ya kudumu katika maendeleo ya elimu, ujuzi na huduma za kijamii kwa vizazi vya sasa na vijavyo katika Wilaya ya Lushoto.

Saturday, July 04, 2026

UCHUMI WA TAIFA UNATEGEMEA UHIFADHI ASEMA MCHECHU AKIZINDUA GREAT RUAHA MARATHON 2026










RUAHA, IRINGA – Msajili wa Hazina na Mlezi wa Great Ruaha Marathon, Bw. Nehemiah Mchechu, ambaye alimwakilisha Mgeni Rasmi, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mwigulu Nchemba, amesema kuwa uhifadhi wa mazingira ni nguzo muhimu ya ukuaji wa uchumi wa Taifa na ustawi wa wananchi.

Akizindua rasmi Great Ruaha Marathon 2026 leo Julai 4, 2026 katika Hifadhi ya Taifa Ruaha, Bw. Mchechu alisema Mto Ruaha Mkuu ni moja ya vyanzo muhimu vya uhai nchini, ukiwezesha shughuli za kilimo, ufugaji, uzalishaji wa umeme pamoja na kuhifadhi mfumo wa ikolojia wa Hifadhi ya Taifa Ruaha.

Alisisitiza kuwa kulinda mazingira na vyanzo vya maji si jukumu la Serikali pekee, bali ni wajibu wa kila Mtanzania kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.

"Tunataka Watanzania wengi zaidi watembelee hifadhi zetu, wajivunie urithi tulionao na wawe mabalozi wa utalii wa nchi yao," amesema Mchechu.

Kwa upande wake, Kamishna wa Uhifadhi wa TANAPA, Massana Gibril Mwishawa, amesema utalii wa michezo umeendelea kuwa nyenzo muhimu ya kuitangaza Tanzania duniani, kuvutia watalii na wawekezaji, pamoja na kukuza biashara na uchumi wa Taifa.

Ameeleza kuwa TANAPA imejipanga kuendeleza utalii wa michezo kama zao jipya la kimkakati litakaloongeza mchango wa sekta ya utalii katika maendeleo ya nchi.

Naye Mratibu wa Great Ruaha Marathon, Hamim Kilahama, amesema mbio hizo si mashindano ya riadha pekee bali ni jukwaa la kuhamasisha jamii kulinda mazingira, kuhifadhi vyanzo vya maji vya Mto Ruaha Mkuu na kuitangaza Kanda ya Kusini kama kitovu cha utalii.

Amebainisha kuwa kwa mwaka wa tano mfululizo, Great Ruaha Marathon imeendelea kufungua fursa mpya za kuitangaza Hifadhi ya Taifa Ruaha kupitia utalii wa michezo, huku ikichochea maendeleo ya jamii na uchumi wa maeneo yanayozunguka hifadhi hiyo.

Hifadhi ya Taifa Ruaha, ambayo ni miongoni mwa hifadhi kubwa zaidi barani Afrika, inaendelea kuwa hazina ya kipekee ya utalii ikiwa na wanyamapori wengi wakiwemo tembo, simba, chui, mbwa mwitu wa porini, twiga, nyati na mamia ya aina za ndege wanaovutia wageni kutoka duniani kote.

Great Ruaha Marathon imeendelea kuthibitisha kuwa michezo, uhifadhi na utalii vinaweza kwenda sambamba katika kujenga uchumi imara, kulinda rasilimali za Taifa na kuitangaza Tanzania kimataifa.

 

MAKAMU WA RAIS DKT. NCHIMBI AMTEMBELEA JAJI MSTAAFU JOSEPH WARIOBA, AMJULIA HALI

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi amemtembelea na kumjulia hali, aliyewahi kuwa Waziri Mkuu na Makamu wa Kwanza wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Jaji. Joseph Sinde Warioba, katika makazi yake, Mbezi Juu Jijini Dar es Salaam.



Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi amemtembelea na kumjulia hali, aliyewahi kuwa Waziri Mkuu na Makamu wa Kwanza wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Jaji. Joseph Sinde Warioba, katika makazi yake, Mbezi Juu Jijini Dar es Salaam.

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi, amemtembelea na kumjulia hali aliyekuwa Waziri Mkuu na Makamu wa Kwanza wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Jaji Mstaafu Joseph Sinde Warioba, katika makazi yake yaliyopo Mbezi Juu, jijini Dar es Salaam.

Ziara hiyo imeonesha heshima na kuthamini mchango mkubwa wa viongozi wastaafu walioitumikia nchi kwa uadilifu na uzalendo. Katika mazungumzo yao, viongozi hao walipata fursa ya kubadilishana mawazo kuhusu masuala mbalimbali yanayohusu maendeleo ya Taifa na ustawi wa wananchi.

Hatua ya Makamu wa Rais kumtembelea Jaji Mstaafu Warioba imepokelewa kama ishara ya kuenzi utumishi wa viongozi walioweka msingi imara wa uongozi na utawala nchini, huku ikidhihirisha umuhimu wa kuendelea kuwajali na kuwathamini wazee wa Taifa kwa mchango wao katika kujenga Tanzania ya leo.


Wednesday, July 01, 2026

RAIS DKT. SAMIA AONGOZA MAADHIMISHO YA MIAKA 30 YA TRA

 
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye Maadhimisho ya miaka 30 ya kuanzishwa kwa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) katika ukumbi wa Mlimani City Jijini Dar es Salaam.



Viongozi, wafanyabiashara pamoja na wageni mbalimbali wakiwa kwenye Maadhimisho ya miaka 30 Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) katika ukumbi wa Mlimani City Jijini Dar es Salaam, tarehe 01 Julai, 2026



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akisikiliza historia ya miaka 30 ya Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) baada ya kuwasili katika ukumbi wa Mlimani City Jijini Dar es Salaam, tarehe 01 Julai, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, leo Julai 1, 2026, ameongoza Maadhimisho ya Miaka 30 ya kuanzishwa kwa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) yaliyofanyika katika Ukumbi wa Mlimani City, jijini Dar es Salaam.

Mara baada ya kuwasili katika ukumbi huo, Rais Samia alitembelea maonesho maalumu yaliyoandaliwa na TRA na kupata maelezo kuhusu historia ya mamlaka hiyo, mafanikio yaliyopatikana katika kipindi cha miaka 30 pamoja na mchango wake katika kuongeza mapato ya Serikali na kuchochea maendeleo ya kiuchumi nchini.

Maadhimisho hayo yamewakutanisha viongozi wa Serikali, taasisi za umma na binafsi, wadau wa kodi pamoja na washirika wa maendeleo kwa lengo la kuadhimisha mafanikio ya TRA tangu kuanzishwa kwake na kujadili mikakati ya kuendelea kuimarisha ukusanyaji wa mapato kwa maendeleo endelevu ya Taifa.

Kwa kipindi cha miaka 30, TRA imeendelea kuwa mhimili muhimu katika ukusanyaji wa mapato ya ndani, hatua iliyowezesha Serikali kugharamia utekelezaji wa miradi mikubwa ya maendeleo katika sekta mbalimbali zikiwemo elimu, afya, miundombinu, maji na huduma nyingine za kijamii.

Maadhimisho hayo pia yametoa fursa ya kutafakari mafanikio yaliyofikiwa, changamoto zilizopo na kuweka mikakati ya kuifanya TRA iendelee kuwa taasisi imara, bunifu na inayotoa huduma bora kwa walipakodi, sambamba na kuimarisha uchumi wa Taifa.

Tuesday, June 30, 2026

DKT MWIGULU: SERIKALI INAENDELEA KUIMARISHA MAZINGIRA YA BIASHARA NA UWEKEZAJI







Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba amesema Serikali itaendelea kuimarisha mazingira ya biashara, uwekezaji na viwanda kwa kufanya mageuzi ya sera, sheria, kanuni na mifumo ya utoaji huduma ili kuiwezesha sekta binafsi kuwa mhimili wa ukuaji wa uchumi na utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Amesema hayo leo, Jumanne Juni 30, 2026, alipokuwa Mgeni Rasmi katika Kongamano la Biashara na Uwekezaji la Mwaka 2026 lililoandaliwa na Chemba ya Taifa ya Biashara Tanzania (TNCC) katika Hoteli ya Johari Rotana, jijini Dar es Salaam.

Waziri Mkuu amesema Serikali imejipanga kuhama kutoka katika mfumo wa kudhibiti biashara kwenda katika mfumo wa kuwezesha biashara kwa kuendelea kuboresha mazingira ya uwekezaji, kupunguza urasimu, kuimarisha matumizi ya teknolojia na kuongeza ufanisi wa taasisi zinazotoa huduma kwa wafanyabiashara na wawekezaji.

"Ajenda ya sekta binafsi ni ajenda ya Taifa. Hatuwezi kufikia malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 bila sekta binafsi yenye nguvu, inayowezeshwa na inayoshirikiana kwa karibu na Serikali," amesema.

Aidha, amesema Serikali itaendelea kupokea na kufanyia kazi mapendekezo ya sekta binafsi yanayolenga kuboresha mazingira ya biashara, kuondoa vikwazo vinavyokwamisha uwekezaji na kuongeza ushindani wa bidhaa na huduma za Tanzania katika masoko ya kikanda na kimataifa.

Waziri Mkuu amesema amani, utulivu na mshikamano wa Taifa ni msingi muhimu wa maendeleo ya uchumi, hivyo kila Mtanzania ana wajibu wa kuendelea kuvilinda ili kuwezesha biashara, uwekezaji na uzalishaji kustawi.

Awali, Waziri wa Viwanda na Biashara, Judith Kapinga alisema Serikali inaendelea kujenga mazingira rafiki ya biashara kwa kuimarisha ushirikiano na sekta binafsi, kukuza matumizi ya teknolojia na kuhakikisha taasisi za umma zinafanya kazi kwa mtazamo wa kuwezesha biashara badala ya kuzikwamisha.

Kwa upande wake, Rais wa Chemba ya Taifa ya Biashara Tanzania (TNCC), Bw. Vincent Minja alisema chemba hiyo imeendelea kufanya mageuzi ya kiutawala na kidijitali yanayolenga kuboresha huduma kwa wanachama, kuimarisha uwakilishi wa sekta binafsi na kuongeza ushindani wa biashara za Tanzania.

Katika kongamano hilo, Waziri Mkuu alizindua rasmi Mfumo wa Kidijitali wa Chemba ya Taifa ya Biashara Tanzania, utakaorahisisha utoaji wa huduma mbalimbali za chemba hiyo, ikiwemo usajili wa wanachama, utoaji wa vyeti vya asili ya bidhaa na huduma nyingine za biashara kwa njia ya mtandao.

Aidha, alishuhudia utiaji saini wa hati mbalimbali za makubaliano ya ushirikiano kati ya Chemba ya Taifa ya Biashara Tanzania na taasisi za umma pamoja na sekta binafsi, hatua inayolenga kuimarisha biashara, uwekezaji, utafiti, ubunifu na maendeleo ya sekta binafsi nchini.

Kongamano hilo lilihudhuriwa na viongozi wa Serikali, taasisi za umma, sekta binafsi, washirika wa maendeleo, mabalozi, wawekezaji na wafanyabiashara kutoka ndani na nje ya nchi.

Monday, June 29, 2026

PROF. SHEMDOE AWAASA WANAFUNZI KUENDELEZA VIPAJI VYAO VYA MICHEZO, SANAA








Awataka kuwa na nidhamu na kusoma kwa bidii

Na OWM - TAMISEMI, Iringa

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM-TAMISEMI) Mhe. Prof. Riziki Shemdoe amewaasa wanafunzi walioshiriki mashindano ya UMISSETA mwaka 2026 kuendeleza vipaji vya michezo na Sanaa walivyonavyo kwani vitawasaidia katika maisha yao ya baadaye, huku akiwataka kuzingatia nidhamu na kusoma kwa bidii ili  kufikia ndoto zao na kutoa mchango katika maendeleo ya taifa.

Prof. Shemdoe ametoa wito huo kwa wanafunzi leo Juni 28, 2026 mjini Iringa katika Viwanja vya Shule ya Sekondari Lugalo, wakati akifunga mashindano ya UMISSETA kwa mwaka wa 2026.

“Nina wasihi muendelee kuwa na nidhamu, kujituma katika masomo yenu na kuendeleza vipaji vyenu vya michezo na sanaa, msiviache vipaji vyenu kwani hata mimi juzi tulipokuwa tunapokea Mwenge wa Uhuru Lushoto nilijikuta nikikumbushia kipaji changu cha kupiga ngoma za utamaduni na kuimba kwa umahiri,” amesisitiza Prof. Shemdoe.

Prof. Shemdoe amewahakikishia wanafunzi hao kuwa, Serikali itaendelea kuweka mazingira bora ya kuhakikisha vipaji vya wanafunzi vinaibuliwa, vinatambuliwa, vinakuzwa ili kuwanufaisha na kulinufaisha taifa kupitia ushiriki wao katika kuliwakilisha taifa kwenye mashindano ya michezo na Sanaa ndani na nje ya nchi.

Aidha, Prof. Shemdoe ametumia fursa hiyo kumpongeza Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuipa kipaumbele sekta ya elimu, michezo, sanaa na maendeleo ya vijana kwenye ajenda kuu ya taifa na kuongeza kuwa, uwekezaji huo unaendelea kuweka msingi imara wa kuibua na kuendeleza vipaji vya watoto na vijana wa Tanzania.

 Kwa upande wake Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu - TAMISEMI anayeshughulikia Elimu Bw. Atupele Mwambene amesema kuwa, ushiriki wa wanafunzi katika michezo mbalimbali ya UMITASHUMTA na UMISSETA umeendelea kuwa jukwaa muhimu la kitaifa la kuibua vipaji, kuimarisha afya, kujenga urafiki na kuendeleza umoja wa kitaifa miongoni mwa wanafunzi. 

Naye Mwakilishi wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Bi. Leah Kihimbi amemuhakikishia Prof. Shemdoe kuwa wizara yake itatekeleza ipasavyo jukumu la kuibua kuendeleza vipaji na vipawa vinavyotokana na mashindano hayo ya sanaa na michezo shuleni. 

Mwakilishi wa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar ambaye ni Afisa Mdhamini Bw. Mohamed Nassoro Salimu amesema Zanzibar inakwenda kujipanga ili kuleta ushindani mkubwa katika mashindano ya mwakani, ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa maelekezo ya Rais wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi ya kufanya mageuzi katika sekta ya michezo.

Akitoa neno la shukrani, Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu - TAMISEMI Bw. Adolf Ndunguru amewashukuru maafisa elimu, wakuu wa shule, walimu, waratibu wa michezo na walezi wa wanafunzi, kwa kazi kubwa walioifanya ya kuwaandaa na kuwaleta wanafunzi katika mashindano ambayo yamewawezesha kujifunza thamani ya nidhamu, ushindani wa haki, uvumilivu, uzalendo na mshikamano wa kitaifa.

RAIS SAMIA AMTEMBELEA PACOME, AMPATIA POLE NA KUMTAKIA AFYA NJEMA

  Dar es Salaam – Mchezaji wa klabu ya Yanga, Pacome Zouzoua , amepata faraja ya kipekee baada ya kutembelewa na Rais wa Jamhuri ya Muungan...