Thursday, March 19, 2026

MAKAMU WA RAIS AONGOZA MAADHIMISHO YA SIKU YA MISITU DUNIANIA NA KAMPENI YA UPANDAJI MITI KITAIFA









Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi ameelekeza uongozi wa Mikoa yote nchini kuhakikisha jitihada za upandaji miti zinaendelezwa kwa kuwekewa mkakati mahsusi unaojumuisha makundi yote katika jamii na kuzingatia ikolojia ya maeneo husika, ikiwa ni pamoja na kuzuia uvamizi na uharibifu wa maeneo yote ya hifadhi ya misitu.

Makamu wa Rais, ametoa maelekezo hayo, wakati akifungua Maadhimisho ya Siku ya Misitu Duniani na Siku ya Upandaji Miti Kitaifa, iliyofanyika katika Uwanja wa Ilulu mkoani Lindi, leo tarehe 19 Machi 2026. 

Amesema ni muhimu kuhakikisha wananchi wanaoishi jirani na misitu ya asili na mashamba ya miti wanapatiwa elimu endelevu kuhusu matumizi bora ya ardhi, udhibiti wa uchomaji moto holela, na usimamizi shirikishi wa misitu ya vijiji.

Aidha, Makamu wa Rais amehimiza umuhimu wa Wizara ya Maliasili na Utalii kupitia Taasisi ya Utafiti wa Misitu Tanzania (TAFORI) kufanya tafiti zitakazojibu changamoto mbalimbali ambazo wakulima wa miti wanakabiliana nazo, hususan zile zinazojitokeza kwenye misitu ya asili. 

Amesema tafiti hizo zijumuishe zile zinazohusu miti inayofaa kwa maeneo ya Mkoa wa Lindi na mikoa mingine nchini, ikiwa ni pamoja na miti dawa.  

Makamu wa Rais amesema zoezi la upandaji miti linapaswa kuwa endelevu ambapo ameiagiza Wizara ya Maliasili na Utalii kupitia Mfuko wa Misitu (TaFF) kuwezesha miradi ya upandaji miti kwa kuanzisha mashamba ya miti ya vijiji na watu binafsi. 

Aidha, ameitaka Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) kuanzisha vitalu vya miche ya miti vya kutosha katika maeneo mbalimbali ya nchi, ikiwemo miti ya asili itakayopandwa katika maeneo mbalimbali. Sambamba na hilo, amesema ni vema elimu ya kutosha itolewe kwa wananchi ili kutunza na kukuza miti hiyo.

Halikdhalika, Makamu wa Rais amesema, pamoja na faida lukuki za rasilimali misitu, bado kuna changamoto nyingi zinazoikabili, zikiwemo, utegemezi mkubwa wa rasilimali za misitu kwa uchumi na kipato kwa jamii kwa njia ya kuni, mkaa na mbao, idadi kubwa ya mifugo inayoingizwa katika hifadhi za misitu kwa ajili ya kutafuta malisho, matukio ya uvamizi wa hifadhi za misitu kwa shughuli za kibinadamu hususan makazi, kilimo na uchimbaji wa madini, pamoja na uwepo wa matukio ya moto ndani ya hifadhi za misitu.

Amesema, Changamoto hizo na nyinginezo zimesababisha kiwango cha upotevu wa misitu nchini kuongezeka hadi kufikia hekta 469,400 kwa mwaka ambacho ni kiwango kikubwa sana kisichoweza kuendelea kuvumilika, na hivyo inahitaji kushirikiana kuhakikisha misitu inalindwa na kuhifadhiwa.  

Vilevile, Makamu wa Rais amesema Kampeni ya upandaji miti kitaifa iliyozinduliwa leo ni sehemu ya jitihada za makusudi zinazochukuliwa ili kulinda hifadhi za misitu na kuongeza uwajibikaji katika uhifadhi wa mazingira pamoja na kutambua na kuunga mkono jitihada za Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan za kutunza mazingira, ambapo amekuwa kinara wa uhifadhi, mathalan, aliposheherekea siku ya kumbukumbu ya kuzaliwa kwake mwaka huu alipanda miti na kuhimiza Watanzania kufanya hivyo.

Amesema ajenda ya upandaji miti, uhifadhi wa misitu na utunzaji wa mazingira kwa ujumla ni kipaumbele katika Taifa letu na utekelezaji wa Ilani ya Chama cha Mapinduzi (2025 – 2030) ambayo inalenga kulinda rasilimali za ardhi, misitu, maji na viumbe hai kwa lengo la kutetea ustawi wa wananchi na ukuaji wa uchumi endelevu.

Makamu wa Rais, ameutaka uongozi wa Mkoa wa Lindi kuhakikisha maeneo yote ya misitu yaliyohifadhiwa ndani ya Mkoa huo yanaendelea kulindwa na kutunzwa. Aidha, amewataka skusimamia ili kuhakikisha vijiji vinakuwa na mipango ya matumizi bora ya ardhi ambayo inasimamiwa vema.

Kaulimbiu ya maadhimisho hayo Kitaifa ambayo ni “Misitu ni Uchumi Endelevu, Tuihifadhi kwa Maendeleo ya Taifa.’’, na ile ya Kidunia “Misitu na Uchumi” (Forests and Economies) zote zinachagiza kutambua umuhimu wa misitu na mchango wake katika kukuza na kujenga uchumi wa nchi. 

Kaulimbiu ya kitaifa inaendana na mipango yetu ya Taifa, ikiwemo Dira 2050 pamoja na mikakati mingine yenye nia ya kuifanya Tanzania inufaike kupitia rasilimali za misitu, kwani misitu ina mchango mkubwa katika uhifadhi wa wanyamapori, ufugaji nyuki, utalii, kilimo, upatikanaji wa maji kwa matumizi nyumbani, viwandani na mashambani.

Tanzania inakadiriwa kuwa na eneo la misitu lenye ukubwa wa takriban hekta milioni 48.1 sawa na 55% ya eneo lote la nchi kavu. Katika eneo hili, hekta milioni 44.7 (93%) ni misitu ya uoto wa miombo na hekta milioni 3.4 (7%) ni Misitu ya Uwanda wa Chini, Milimani, Mikoko na Mashamba ya Miti. Sekta ya Misitu inayojumuisha ufugaji nyuki na wanyamapori, ilichangia takriban 3% katika Pato la Taifa mwaka 2024, hivyo kuifanya kuwa miongoni mwa vichocheo muhimu vya maendeleo ya Taifa.

TANZANIA YAWAVUTIA WAWEKEZAJI SEKTA YA UCHUKUZI AFRIKA KUSINI

 









Naibu Waziri wa Uchukuzi, David Kihenzile, ameipeperusha vyema bendera ya Tanzania katika Mkutano wa Kimataifa wa Uchukuzi (NCT) uliofanyika katika Ukumbi wa Gallagher Estate jijini Johannesburg, Afrika Kusini.

Mkutano huo uliofunguliwa na Rais wa Afrika Kusini, Cyril Ramaphosa, uliwakutanisha viongozi wa sekta ya uchukuzi kujadili mustakabali wa mifumo jumuishi, salama na endelevu ya uchukuzi barani Afrika.

Katika mjadala wa Mawaziri wa Uchukuzi, Kihenzile aliwasilisha mafanikio makubwa ya Tanzania, akibainisha uwekezaji unaoendelea katika miradi ya kimkakati ikiwemo reli ya kisasa ya SGR, maboresho ya bandari, viwanja vya ndege pamoja na miundombinu ya barabara.

Aidha, alisisitiza dhamira ya Serikali ya Tanzania katika kuimarisha mazingira rafiki kwa uwekezaji, akiwakaribisha wawekezaji wa ndani na nje kushiriki katika miradi ya uchukuzi yenye lengo la kukuza biashara, ajira na maendeleo ya kijamii katika ukanda wa Kusini mwa Afrika.

#Tanzania #Transport #SGR #Investment #Africa #Infrastructure #EconomicGrowth #Johannesburg #NCT #Development

Wednesday, March 18, 2026

RAIS SAMIA APOKEA RIPOTI YA MABORESHO YA MFUMO WA KODI, ASISITIZA UCHUMI JUMUISHI NA ENDELEVU 🇹🇿

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye hafla ya kupokea Ripoti ya Tume ya Rais ya Kutathmini Maboresho ya Mfumo wa Kodi nchini, Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 18, Machi, 2026.

Mwenyekiti wa Tume ya Rais ya Kutathmini Maboresho ya Mfumo wa Kodi nchini Katibu Mkuu Kiongozi Mstaafu Mhe. Balozi Ombeni Sefue akizungumza kabla ya kukabidhi Ripoti ya Tume hiyo kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 18, Machi, 2026.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, amepokea rasmi Ripoti ya Tume ya Rais ya Kutathmini Maboresho ya Mfumo wa Kodi nchini katika hafla iliyofanyika Ikulu, Dar es Salaam, tarehe 18 Machi 2026.

Ripoti hiyo iliwasilishwa na Mwenyekiti wa Tume, Balozi Ombeni Sefue, ambaye alieleza kuwa mapendekezo yaliyomo yanalenga kuimarisha mfumo wa kodi ili uwe rafiki kwa wawekezaji, wenye tija kwa wananchi, na unaochochea ukuaji wa uchumi wa taifa.

Akizungumza katika hafla hiyo, Rais Samia alisisitiza umuhimu wa maboresho ya mfumo wa kodi yatakayojenga uchumi jumuishi, kuongeza uwazi na ufanisi, pamoja na kuimarisha mazingira ya biashara nchini.

Ripoti hiyo inatarajiwa kuwa chachu ya mageuzi ya sera za kodi, hatua itakayosaidia kuongeza mapato ya ndani, kuvutia uwekezaji zaidi, na kuharakisha maendeleo endelevu ya Taifa.

Serikali inaendelea kuonesha dhamira thabiti ya kuimarisha uchumi kupitia sera shirikishi zinazoweka mbele maslahi ya wananchi, huku ikiendeleza juhudi za diplomasia ya kiuchumi ili kufungua fursa mpya za maendeleo.


#KaziNaUtuTunasongaMbele #TabasamuLaUtu #MaendeleoEndelevu #DiplomasiaYaKiuchumi

Tuesday, March 17, 2026

SERIKALI YATOA MAELEKEZO NANE KUIMARISHA KAMPUNI AMBAZO INA UMILIKI HISA CHACHE KUELEKEA DIRA 2050






Arusha. Serikali imetoa maelekezo nane ya kimkakati yanayolenga kuimarisha utendaji wa kampuni ambazo ina umiliki wa hisa  chache, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuharakisha safari ya Tanzania kuelekea hadhi ya nchi ya kipato cha kati cha juu kama ilivyo ainishwa kwenye Dira 2050.

Dira hiyo inalenga kukuza uchumi wa Tanzania kutoka ukubwa wa sasa wa takribani dola za Marekani bilioni 85 hadi kufikia dola trilioni moja ifikapo mwaka 2050, lengo ambalo linahitaji kuimarika kwa uwekezaji wa umma, ikiwemo kampuni ambazo Serikali ina umiliki wa hisa za wachache.

Akifungua Mkutano wa Wakurugenzi wa Kampuni ambazo Serikali ina umiliki wa hisa chache (MIF 2026) unaofanyika kwa siku tatu jijini Arusha, Jumatatu, Machi 16, 2026, Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Dkt. Khamis Mussa Omar, alisema kuwa maelekezo hayo yanalenga kuhakikisha kampuni hizo zinaendeshwa kwa misingi ya mikakati thabiti, uwazi na ufanisi wa kibiashara, ili ziweze kutoa mchango mkubwa zaidi katika mageuzi ya uchumi wa taifa.

Wakati wa Mkutano huo ulioandaliwa na Ofisi ya Msajili wa Hazina, alisema bodi za wakurugenzi na menejimenti zinapaswa kuoanisha mikakati ya kampuni zao na vipaumbele vya maendeleo ya taifa pamoja na mwenendo wa uchumi wa dunia, ili uwekezaji uweze kukidhi mahitaji ya masoko yanayobadilika na wakati huo huo kuleta ukuaji shirikishi wa uchumi.

Aidha, Waziri huyo alizitaka kampuni hizo kutumia teknolojia kama nyenzo ya kuimarisha uwazi, kuongeza imani ya umma na kuboresha mifumo ya utawala bora katika taasisi zao.

Alieleza kuwa maelekezo hayo pia yanasisitiza umuhimu wa kuwa na uongozi unaotazama mbele, unaowawezesha wakurugenzi na watendaji wakuu kutambua mapema hatari zinazoweza kujitokeza na kutumia fursa mpya katika mazingira ya uchumi wa dunia yanayozidi kuwa na ushindani mkubwa.

Vilevile, Serikali inahamasisha kuimarishwa kwa ushirikiano na ubia kati ya kampuni mbalimbali ili ziweze kubadilishana uzoefu, kufungua fursa mpya za kiuchumi na kuongeza matokeo chanya kwa pamoja.

Kwa mujibu wa Waziri huyo, kuimarishwa kwa mifumo madhubuti ya utawala inayozingatia uwajibikaji, uwazi na uongozi wenye maadili ni jambo la msingi katika kuhakikisha uwekezaji wa umma unaleta tija endelevu.

Alisisitiza kuwa kampuni zinapaswa kuendesha shughuli zake kwa kuzingatia matokeo, kwa lengo la kuongeza ufanisi wa kiutendaji, kukuza faida na hatimaye kuongeza thamani kwa wanahisa pamoja na Serikali.

Mhe. Omar pia alisisitiza umuhimu wa kuimarisha uchambuzi wa taarifa za kiuchumi na ushindani ili maamuzi ya kibiashara yafanywe kwa kuzingatia takwimu sahihi na taarifa za soko, hatua itakayosaidia kuongeza tija na ushindani katika masoko ya kikanda na kimataifa.

Aidha, alisisitiza umuhimu wa kuimarisha ushirikiano kati ya Serikali na sekta binafsi, akibainisha kuwa ubia imara kati ya pande hizo ni nyenzo muhimu katika kufungua fursa za uwekezaji na kuharakisha maendeleo ya taifa.

Serikali kupitia Dira 2050 imejipanga kuongeza mchango wa mapato yasiyotokana na kodi katika bajeti ya taifa kutoka asilimia tatu ya sasa hadi kufikia asilimia kumi ndani ya miaka mitano ijayo, sawa na lengo la kukusanya takribani shilingi trilioni tano kila mwaka.

Mhe. Waziri alisema kuwa kufikiwa kwa lengo hilo kunahitaji mabadiliko ya makusudi katika fikra na mifumo ya uendeshaji wa taasisi.

“Hii inahitaji kuondoka katika mtazamo wa uangalizi wa kawaida na badala yake kujenga uongozi unaotazama mbele, unaozingatia ubunifu, wepesi wa kufanya maamuzi na uwezo wa kutabiri mwelekeo wa maendeleo,” alisema Mhe. Omar.

Alisisitiza kuwa mabadiliko hayo yanapaswa kwenda sambamba na matumizi bora ya kila uwekezaji katika kampuni husika ili uweze kuleta matokeo makubwa zaidi ya kiuchumi na kifedha.

Bila mabadiliko hayo, alisema, itakuwa vigumu kufikia malengo yaliyowekwa katika Dira 2050.

Waziri huyo aliwataka wakurugenzi na watendaji wakuu wa kampuni hizo kuwa viongozi wanaotazama mbele na kushughulikia kikamilifu changamoto zinazoathiri utendaji wa taasisi wanazosimamia.

“Ni lazima tukubali mabadiliko na tuwe viongozi wanaotafakari kwa kina, kuchukua hatua mapema, na kutambua changamoto zinazoathiri utendaji wa kampuni zetu, huku tukitafuta suluhisho endelevu,” alisema.

Aidha, aliwataka viongozi wa kampuni hizo kuchukua jukumu la moja kwa moja katika kuimarisha utendaji na uendelevu wa taasisi wanazoongoza.

“Kupitia mkutano huu, nawapa changamoto kila mmoja wenu kutekeleza kikamilifu wajibu wenu kama viongozi wa kampuni zenye umiliki wa hisa chache,” alisema.

“Ni lazima tuje na mikakati madhubuti itakayoboresha kwa kiasi kikubwa utendaji wa kampuni hizi huku tukihakikisha zinadumu na kuendelea kustawi.”

Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa Ofisi ya Rais – Uwekezaji, Dk. Fred Msemwa, alieleza dhamira ya Serikali ya kuendelea kuboresha mazingira ya biashara na uwekezaji nchini ili kuimarisha sekta binafsi. 

“Tutafanya kila linalowezekana, ikiwemo kupitia upya sheria na sera mbalimbali kwa lengo la kuboresha zaidi mazingira ya biashara, kwani tunatambua kuwa sekta binafsi ni chachu ya kufanikisha malengo ya Dira 2050,” alisisitiza.

Awali akizungumza katika mkutano huo, Msajili wa Hazina, Bw. Nehemiah Mchechu, alisema jukwaa hilo ambalo linafanyika kwa mara ya tatu tangu kuanzishwa kwake mwaka 2024, limekuwa sehemu muhimu ya viongozi wa kampuni hizo kujadili masuala ya utawala bora, utendaji na mchango wao katika mageuzi ya uchumi wa Tanzania.

Alisema kaulimbiu ya mkutano wa mwaka huu inayosema “Kutoka Ufuatiliaji wa kawaida hadi Uongozi wa Kimkakati unaotazama mbele:” inaakisi umuhimu wa bodi za wakurugenzi na viongozi wakuu kuacha mtazamo wa usimamizi wa kawaida na badala yake kuwa na uongozi unaoweza kutambua mapema changamoto na fursa za baadaye.

“Katika dunia ya leo inayobadilika kwa kasi kiuchumi na kiteknolojia, uongozi hauwezi tena kujikita tu katika kusimamia hali ya sasa, bali pia unapaswa kutazama mbele na kujiandaa kwa siku za usoni,” alisema.

Aliongeza kuwa taasisi zinazojenga utamaduni wa kufikiri mbele, ubunifu na wepesi wa kufanya maamuzi ndizo zitakazoweza kukabiliana na shinikizo la mabadiliko na pia kuongoza mwelekeo wa maendeleo.

Bw. Mchechu alisema mkutano huo pia unaendana na malengo ya Dira 2050, inayolenga kujenga uchumi imara, shindani na unaochochewa na ubunifu, unaoungwa mkono na taasisi zenye ufanisi, uwajibikaji na uongozi unaotazama mbele.

Alifafanua kuwa mkutano huo unatoa fursa kwa wakurugenzi na watendaji wakuu kubadilishana uzoefu, kuimarisha mifumo ya utawala bora na kujenga uwezo katika maeneo muhimu kwa ushindani na uendelevu wa taasisi zao.

Bw. Mchechu pia alieleza kuwa uwekezaji wa Serikali katika kampuni ambazo Serikali ina hisa chache umeongezeka kwa kiasi kikubwa katika kipindi cha miaka mitano iliyopita, kutoka Sh821 bilioni hadi kufikia  Sh3.6 trilioni, jambo linaloonesha kuendelea kuimarika kwa ushirikiano kati ya Serikali na sekta binafsi.

Aidha, michango ya gawio kutoka katika kampuni hizo imeongezeka kwa kiwango kikubwa, kutoka Sh58 bilioni hadi kufikia Sh266 bilioni, sawa na ongezeko la asilimia 357 katika kipindi hicho.

Mkutano wa MIF 2026 umewakutanisha zaidi ya wakurugenzi 200, Maafisa Watendaji Wakuu, watunga sera na wataalamu kutoka ndani na nje ya Tanzania kwa lengo la kujadili mikakati ya kuimarisha utendaji na utawala wa kampuni ambazo Serikali ina umiliki wa hisa chache, ili ziweze kuchangia kwa ufanisi zaidi katika maendeleo ya uchumi wa taifa kwa muda mrefu.

Saturday, March 14, 2026

RAIS SAMIA AJUMUIKA NA WANANCHI WETE KWENYE FUTARI YA RAMADHANI PEMBA

 



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akijumuika na makundi mbalimbali ya Wananchi wa Wete kwenye Futari aliyowaandalia katika ukumbi wa Shule ya Sekondari Utaani, Mkoa wa Kaskazini Pemba, tarehe 14 Machi, 2026.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, ameendelea kudhihirisha ukaribu wake na wananchi baada ya kujumuika na makundi mbalimbali ya wananchi wa Wete katika futari maalum aliyowaandalia, iliyofanyika katika ukumbi wa Shule ya Sekondari Utaani, Mkoa wa Kaskazini Pemba, tarehe 14 Machi 2026.

Katika tukio hilo lililojaa hali ya upendo, mshikamano na ibada, wananchi kutoka makundi mbalimbali walipata fursa ya kufutari pamoja na Rais huku wakibadilishana mawazo na salamu za Ramadhani. Futari hiyo imeakisi utamaduni wa mshikamano na kuimarisha mahusiano kati ya viongozi na wananchi, hususan katika kipindi hiki kitukufu cha Mwezi Mtukufu wa Ramadhani.

Wananchi waliohudhuria walieleza kufurahishwa na kitendo cha Rais kujumuika nao, wakisema hatua hiyo inaonesha kujali na kuthamini mchango wa jamii katika kujenga Taifa lenye umoja na mshikamano. Tukio hilo pia lilikuwa fursa ya kuimarisha maadili ya kijamii, upendo na ushirikiano miongoni mwa Watanzania.






Rais Samia atoa Bilioni 15 Maboresho Shule ya Polisi Kilimanjaro








Na Mwandishi Wetu,Kilimanjaro

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,Dkt.Samia Suluhu Hassan ametoa  Shilingi Bilioni 25 ikiwa ni utekelezaji wa ahadi aliyoitoa wakati wa Kikao cha Maafisa Wakuu Waandamizi wa Jeshi la Polisi kilichofanyika mwaka 2024 lengo ikiwa kuifanyia maboresho Shule cha Polisi Kilimanjaro ambacho kinakabiliwa na uchakavu wa Majengo ambayo yalijengwa tangu  mwaka 1933 ambapo yanajumuisha Mabweni ya Wanafunzi,Madarasa na Nyumba za Askari.

Kauli hiyo imetolewa na Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi,Patrobas Katambi wakati wa ziara ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje Ulinzi na Usalama(NUU) iliyotembelea shule hiyo kukagua matumizi ya fedha hiyo iliyotolewa na Mheshimiwa Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan ikiwa ni utaratibu wa Kamati za Bunge kufuatilia matumizi ya fedha zinazotolewa na serikali kwa miradi mbalimbali ya maendeleo.

“Leo tunazungumza Wizara ya Mambo ya Ndani ambapo Rais ameweza kuyafanya haya ambayo wajumbe mmeyashuhudia leo kwa kiasi cha Shilingi Bilioni 25 ambazo mmeona kwa kiwango kikubwa na uweledi mkubwa wa jeshi katika utekelezaji na uwezo wa kusimamia kazi.Kwa kweli hatuna namna ya kuweza kumshukuru Mheshimiwa Rais Zaidi ya kumuombea afya njema,umri na rizki ili Mwenyenzi Mungu aendelee kumpa hekima na busara ili sisi wizara tuendelee kuwa wanufaika wa uongozi wake” amesema Waziri Katambi

“Lakini tuna miradi ya ujenzi wa nyumba sehemu mbalimbali ambapo Mheshimiwa Rais pia anatoa kiasi kikubwa cha fedha na pale Dodoma tayari mradi ushaanza na tunatumia wataalamu wetu wa ndani na wanajenga kwa viwango vile vile kama mlivyoona hapa Shule ya Polisi,tunaenda kufanya maboresho ya maslahi kwa askari,mabadiliko ya sera na sheria  na teknolojia za kisasa pia zinaendelea kuingizwa jeshini ili vifaa vya kisasa vitumike katika kulinda usalama wetu.” aliongeza Waziri Katambi

Akizungumza katika ziara hiyo,Mwenyekiti wa Kamati hiyo ya NUU, Najma Murtaza Giga, ametoa pongezi kwa Jeshi la Polisi kwa kujenga mradi huo kwa ufanisi na uweledi mkubwa huku akikiri kuona thamani ya kiasi cha fedha kilichotolewa na Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan huku akiweka wazi Kamati kuendelea  kuwa na imani na Jeshi la Polisi katika masuala mbalimbali na hivyo haina budi kuendelea kulisemea Jeshi la Polisi kuhakikisha linawezeshwa ili liweze kutekeleza majukumu yake ya kulinda usalama wa raia na mali zao kwa weledi na ufanisi wa hali ya juu.

Nae Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini IGP Camillus Wambura, ameishukuru Kamati hiyo ya Kudumu ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama (NUU) kwa kutenga muda na kuona umuhimu wa kutembelea Shule ya Polisi Tanzania-Moshi mkoani Kilimanjaro na kuona thamani ya fedha iliyotolewa na Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, inavyotumika kwa kuhakikisha ubora na ufanisi unaonekana kwenye miradi hiyo ya ujenzi.

Aidha, IGP Wambura, ameiambia kamati hiyo kuwa, serikali ya awamu ya sita imeendelea kuliwezesha Jeshi la Polisi kwenye miundombinu mbalimbali kote nchini ili kuhakikisha askari Polisi wanafanya kazi kwenye mazingira mazuri na wezeshi katika kuwahudumia wananchi, kutatua kero mbalimbali ili waendelee kufanya kazi zao bila uwepo wa matishio ya kihalifu nchini.

MAKAMU WA RAIS AONGOZA MAADHIMISHO YA SIKU YA MISITU DUNIANIA NA KAMPENI YA UPANDAJI MITI KITAIFA

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi ameelekeza uongozi wa Mikoa yote nchini kuhakikisha jitih...