Waziri wa Uchukuzi, Profesa
Makame Mbarawa (wa pili kutoka kulia),akizungumza baada ya kukagua
daraja la kupitisha magari chn ya reli, leo.Na Baltazar Mashaka, Mwanza
WAZIRI
wa Uchukuzi, Makame Mbarawa, ameridhishwa na kasi ya ujenzi wa mradi wa
reli ya kisasa (SGR) kipande cha Mwanza–Isaka chenye urefu wa kilomita
341, unaotarajiwa kukamilika mwaka 2028.
Akizungumza
katika eneo la Fella, wilayani Misungwi, leo Februari 24, 2026, baada
ya kukagua maendeleo ya mradi huo, Profesa Mbarawa alisema ujenzi wa
mradi huo umefikia asilimia 68 na unaendelea vizuri.
Alisema
mradi huo wa kimkakati unaogharimu dola za Marekani bilioni 1.326
(takribani shilingi trilioni 3.06), ni mkubwa na kielelezo cha
kujivunia, huku akimshukuru Rais Dk.Samia Suluhu Hassan kwa kusimamia
utekelezaji wake, akieleza kuwa wakati anaingia madarakani mradi ulikuwa
hatua sifuri sasa umefikia hatua kubwa.
Kwa
mujibu Profesa Mbarawa, jengo la stesheni kuu ya Mwanza lenye uwezo wa
kuchukua abiria 900 pamoja na majengo mawili ya biashara ujenzi
unaendelea vyema, miundombinu ikiwemo madaraja ikifikia takribani
asilimia 90, huku ulazaji wa mataruma ukiwa asilimia 53.
Alisisitiza
kuwa serikali itaendelea kutoa fedha ili kuhakikisha mradi huo
unakamilika kwa viwango vya kimataifa na kwa kuzingatia thamani ya
fedha, una uwezo wa kuhimili changamoto mbalimbali ikiwemo matetemeko ya
ardhi.
Profesa
Mbarawa aliwashukuru wananchi wa Mwanza kwa shughuli za maendeleo na
kuunga mkono mradi huo, akibainisha kuwa eneo lililosalia na changamoto
ni Mkuyuni ambako kuna makazi yanayochelewesha ulipuaji wa miamba.
Hata
hivyo, alisema kuwa, mkandarasi ameahidi kukamilisha kazi hiyo ifikapo
Agosti mwaka huu na kuanza uwekaji wa njia ya reli huku akionya
waliopata kazi katika mrad huo wasifanye mambo ya ovyo ikiwemo wizi wa
malighafi ya saruji, nondo na vyuma, wataakuwa wanawaiba Watanzania si
mkandarasi.
Alisema
kukamilika kwa mradi huo kutafungua fursa mbalimbali zikiwemo ujenzi wa
Bandari Kavu ya kuhifadhi mizigo kutoka Bandari ya Dar es Salaam,
kubadilisha vichwa vya treni na mabehewa, na kuchochea shughuli za
kiuchumi katika eneo la Misungwi, aliwataka wananchi kutunza mali za
mradi na kuepuka vitendo vya wizi wa vifaa vya ujenzi.
Mbunge
wa Misungwi, Silvery Salvatory (CCM), alisema reli ya SGR itaongeza
usafirishaji wa mizigo ya ndani na kutoka nchi jirani, hivyo kuchochea
uchumi jumuishi kama ilivyoainishwa katika Dira ya Taifa ya Maendeleo
2050, alitoa wito kwa wananchi kujipanga kunufaika na fursa
zitakazotokana na miradi hiyo.
Kwa
upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Misungwi, Johari Samizi, alisema miradi
ya SGR, Bandari Kavu na Daraja la JPM itaimarisha uchumi wa wilaya hiyo
na kuwataka wananchi kupanga matumizi bora ya ardhi ili kuepuka migogoro
na madai ya fidia baadaye.
Naye
Mkuu wa Wilaya ya Nyamagana, Amina Makilagi, kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa
wa Mwanza, Said Mtanda, alisema kukamilika kwa reli ya SGR kutaufungua
mkoa wa Mwanza kiuchumi na kuongeza fursa za uwekezaji.
Awali,
Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Reli Tanzania (TRC), Mhandisi Machibya
Masanja, alisema eneo la Misungwi limepangwa kuwa kitovu cha shughuli za
kilojistiki, na kuwataka wawekezaji kuchangamkia fursa za kuwekeza
katika Bandari Kavu, ambayo serikali imeiachia sekta binafsi kuendesha.
Alisisitiza
kuwa lengo ni kuhakikisha ifikapo mwaka 2028 treni ya SGR inasafiri
kutoka Dar es Salaam hadi Mwanza ikiwa na mizigo na abiria, na hivyo
kuimarisha uchumi wa taifa.