Saturday, June 20, 2026

RAIS SAMIA AMKARIBISHA RAIS WA NAMIBIA KATIKA ZIARA YA KITAIFA, WAIMARISHA USHIRIKIANO WA KIDIPLOMASIA NA MAENDELEO

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye picha na mgeni wake Rais wa Jamhuri ya Namibia Mhe. Dkt. Netumbo Nandi-Ndaitwah baada ya kuwasili Ikulu, Jijini Dar es Salaam kwa Ziara ya Kitaifa, tarehe 20 Juni, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akisalimiana na mgeni wake Rais wa Jamhuri ya Namibia Mhe. Dkt, Netumbo Nandi-Ndaitwah baada ya kuwasili katika viwanja vya Ikulu Jijini Dar es Salaam kwa Ziara ya Kitaifa, tarehe 20 Juni, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Namibia Mhe. Dkt. Netumbo Nandi-Ndaitwah akisaini kitabu cha wageni baada ya kuwasili Ikulu Jijini Dar es Salaam kwa Ziara ya Kitaifa, tarehe 20 Juni, 2026.


Rais wa Jamhuri ya Namibia Mhe. Dkt. Netumbo Nandi-Ndaitwah akiangalia vikundi vya ngoma za asili baada ya kuwasili katika Ukumbi wa Mikutano wa Kikwete, Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 20 Juni, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa na mgeni wake Rais wa Jamhuri ya Namibia Mhe. Dkt. Netumbo Nandi-Ndaitwah baada ya kuwasili katika viwanja vya Ikulu Jijini Dar es Salaam kwa Ziara ya Kitaifa, tarehe 20 Juni, 2026.



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, leo tarehe 20 Juni 2026 amempokea kwa heshima kubwa mgeni wake, Rais wa Jamhuri ya Namibia, Netumbo Nandi-Ndaitwah, katika Ikulu jijini Dar es Salaam kwa ziara rasmi ya kitaifa inayolenga kuimarisha uhusiano wa kihistoria na ushirikiano wa kimkakati kati ya mataifa hayo mawili.

Mara baada ya kuwasili Ikulu, Rais Netumbo Nandi-Ndaitwah alipokelewa na mwenyeji wake, Rais Samia, kabla ya kushiriki shughuli mbalimbali za mapokezi ikiwemo kusaini kitabu cha wageni wa heshima, hatua inayoashiria urafiki na ushirikiano wa kudumu kati ya Tanzania na Namibia.

Katika mwendelezo wa ziara hiyo, Rais wa Namibia alipata fursa ya kushuhudia na kufurahia maonesho ya vikundi vya ngoma za asili katika Ukumbi wa Mikutano wa Kikwete, yaliyobeba taswira ya utajiri wa utamaduni wa Tanzania na ukarimu wake kwa wageni wa kimataifa.

Viongozi hao wawili baadaye walifanya mazungumzo ya faragha na ya pamoja yaliyolenga kujadili namna ya kuendeleza ushirikiano katika sekta mbalimbali zikiwemo biashara, uwekezaji, uchumi, utalii, elimu, nishati na maendeleo ya kijamii. Mazungumzo hayo yanatarajiwa kufungua fursa mpya za ushirikiano zitakazonufaisha wananchi wa nchi zote mbili.

Ziara hiyo pia iliambatana na upigaji wa picha za pamoja katika Ikulu, ikiwa ni ishara ya uhusiano imara wa kidiplomasia na dhamira ya viongozi hao kuendeleza mshikamano, amani na maendeleo endelevu barani Afrika.

Ujio wa Rais Netumbo Nandi-Ndaitwah nchini Tanzania unaendelea kudhihirisha urafiki wa muda mrefu kati ya Tanzania na Namibia pamoja na azma ya pamoja ya kuimarisha ushirikiano wa kikanda na kimataifa kwa manufaa ya vizazi vya sasa na vijavyo.

Friday, June 19, 2026

RAIS SAMIA AMUAPISHA DKT. JOHN ANTHONY JINGU KUWA MTENDAJI MKUU WA MAHAKAMA YA TANZANIA


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, akimuapisha Dkt. John Anthony Jingu kuwa Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, kwenye hafla iliyofanyika Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 19 Juni, 2026.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Dkt. John Anthony Jingu akiapa Kiapo cha Maadili pamoja na Karani wa Baraza la Mawaziri Bw. Francis Petro Mossongo,  Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 19 Juni, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, akizungumza na viongozi mbalimbali baada ya kumuapisha Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Dkt. John Anthony Jingu, Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 19 Juni, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa na kwenye picha na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Dkt. John Anthony Jingu pamoja na Mtendaji Mkuu Mstaafu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elistante Ole Gabriel mara baada ya hafla ya Uapisho,  Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 19 Juni, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa na viongozi mbalimbali kwenye picha na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Dkt. John Anthony Jingu, Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 19 Juni, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, leo tarehe 19 Juni 2026 amemuapisha John Anthony Jingu kuwa Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania katika hafla iliyofanyika Ikulu, jijini Dar es Salaam.

Katika hafla hiyo, Dkt. Jingu aliapishwa rasmi kushika nafasi hiyo na baadaye akaapa Kiapo cha Maadili mbele ya Karani wa Baraza la Mawaziri, Francis Petro Mossongo, ikiwa ni hatua muhimu ya kuthibitisha dhamira yake ya kutekeleza majukumu kwa uadilifu, uwajibikaji na kwa kuzingatia sheria za nchi.

Baada ya uapisho huo, Rais Samia alizungumza na viongozi mbalimbali waliohudhuria hafla hiyo, akisisitiza umuhimu wa kuendelea kuimarisha utoaji wa haki, utawala wa sheria na ufanisi wa utendaji ndani ya Mahakama ya Tanzania kwa manufaa ya wananchi na maendeleo ya taifa.

Aidha, hafla hiyo ilihitimishwa kwa upigaji wa picha za pamoja ambapo Rais Samia alipiga picha na Mtendaji Mkuu mpya wa Mahakama ya Tanzania, Dkt. John Anthony Jingu, pamoja na Mtendaji Mkuu Mstaafu wa Mahakama ya Tanzania, Elistante Ole Gabriel. Vilevile, Rais alijumuika katika picha za pamoja na viongozi mbalimbali waliohudhuria tukio hilo, kuashiria mshikamano na kuendelea kwa jukumu la kuimarisha taasisi za utoaji haki nchini.

Uteuzi na uapisho wa Dkt. Jingu unatarajiwa kuongeza nguvu katika juhudi za kuendeleza maboresho ya kiutendaji ndani ya Mahakama ya Tanzania na kuimarisha utoaji wa huduma za haki kwa ufanisi, uwazi na weledi.

Tuesday, June 16, 2026

MAMA NEEMA MWIGULU AHIMIZA TAASISI KUUNGA MKONO JUHUDI ZA SERIKALI KUPITIA UWAJIBIKAJI KWA JAMII







Mwenza wa Waziri Mkuu, Mama Neema Mwigulu Nchemba, amehimiza taasisi za umma na binafsi kuendelea kuunga mkono juhudi za Serikali katika kuboresha huduma za kijamii kupitia utekelezaji wa programu za uwajibikaji kwa jamii (CSR).

Mama Neema amesema hayo leo Jumanne, Juni 16, 2026 katika hafla ya kukabidhi vifaa vya hospitali vilivyotolewa na Shirika la Viwango Tanzania (TBS) katika Hospitali ya Wilaya ya Chamwino, Mkoa wa Dodoma, ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya miaka 50 ya shirika hilo.

Mama Neema ambae alikuwa mgeni rasmi katika hafla hiyo, amesema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imefanya uwekezaji mkubwa katika sekta ya afya kupitia ujenzi wa miundombinu ya kutolea huduma za afya, ajira kwa wataalamu wa afya, upatikanaji wa dawa na vifaa tiba pamoja na kuimarisha huduma za kibingwa na ubingwa bobezi.

“Tunashuhudia maboresho makubwa katika sekta ya afya kutokana na uwekezaji unaoendelea kufanywa na Serikali. Leo tunajivunia huduma nyingi ambazo hapo awali zilikuwa zinapatikana nje ya nchi kupatikana hapa nchini,” amesema.

Mama Neema amewapongeza viongozi wa Shirika la Viwango Tanzania kwa kuendelea kutekeleza kwa vitendo sera ya uwajibikaji kwa jamii na kuchangia ustawi wa wananchi kupitia sekta ya afya pamoja na makundi mbalimbali yenye mahitaji maalum.

Amesema vifaa vilivyotolewa vitasaidia kuboresha utoaji wa huduma katika Hospitali ya Wilaya ya Chamwino na kuongeza ustawi wa mama na mtoto.

Vifaa hivyo vinajumuisha vitimwendo 20, vitanda vya kujifungulia vitano, vitanda vya kufanyia uchunguzi vitano, vitanda vitano vya kulaza wagonjwa, machela moja ya kisasa, makabati matatu ya kuhifadhia vifaa tiba pamoja na mabeseni yenye vifaa mbalimbali kwa ajili ya akinamama 30 waliojifungua.

Awali, akimkaribisha mgeni rasmi kuzungumza katika hafla hiyo, Waziri wa Viwanda na Biashara, Judith Kapinga amesema Serikali itaendelea kuhimiza taasisi zake kutekeleza kwa vitendo sera ya uwajibikaji kwa jamii ili kuchangia kuboresha huduma za kijamii na maisha ya wananchi.

Amesema msaada uliotolewa na Shirika la Viwango Tanzania (TBS) katika Hospitali ya Wilaya ya Chamwino ni sehemu ya mchango wa taasisi za umma katika kuunga mkono jitihada za Serikali za kuimarisha huduma za afya nchini pamoja na kuendelea kuyaishi maono ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuboresha ustawi wa wananchi.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Viwango Tanzania (TBS), Dkt. Ashura Katunzi amesema shirika hilo limeendelea kutekeleza miradi mbalimbali ya kijamii katika sekta ya afya, elimu na makundi maalum ikiwa ni sehemu ya mchango wake kwa maendeleo ya jamii.

Amesema TBS itaendelea kushirikiana na Serikali na wadau mbalimbali katika kuboresha maisha ya wananchi kupitia programu zake za uwajibikaji kwa jamii.

TANESCO YAKAMILISHA MIRADI YA KUIMARISHA UPATIKANAJI WA UMEME DODOMA







📌 Itanufaisha wilaya za Kongwa,Gairo, Mpwapwa, na Chamwino 

📌 Waziri Ndejembi azindua Kituo cha Kubadilishia Njia za Usambazaji Umeme na Transfoma ya Kudhibiti Umeme

📌 Serikali yawekeza zaidi ya Shilingi Bilioni 10.5 kuimarisha huduma ya umeme

Na Mwandishi Wetu, Kongwa

Wananchi wa Wilaya za Gairo, Mpwapwa, Kongwa, Chamwino na Kiteto wanatarajiwa kunufaika na huduma ya umeme wa uhakika zaidi kufuatia kukamilika kwa miradi ya kuimarisha mfumo wa usambazaji wa umeme iliyotekelezwa na Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) kwa gharama ya zaidi ya Shilingi bilioni 10.5.

Miradi hiyo inahusisha Kituo cha Kubadilishia Njia za Usambazaji Umeme (Switching Station), Transfoma ya Kudhibiti Umeme (Automatic Voltage Regulator – AVR) yenye uwezo wa MVA 20 pamoja na njia ya kusafirisha umeme ya msongo wa kilovoti 33 kutoka Kituo cha Kupokea na Kupoza Umeme cha Zuzu hadi Mbande yenye urefu wa kilomita 92.

Akizindua miradi hiyo Juni 16, 2026 katika eneo la Mbande, Wilaya ya Kongwa, Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi, alisema uwekezaji huo ni sehemu ya juhudi za Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, za kuhakikisha wananchi wanapata huduma ya umeme wa uhakika kwa ajili ya shughuli za kijamii na kiuchumi.

Alisema miradi hiyo imeleta maboresho makubwa katika mfumo wa usambazaji wa umeme katika ukanda huo, ambapo hapo awali hitilafu zilizokuwa zikitokea katika eneo moja zilisababisha wananchi wa maeneo mengine kukosa huduma ya umeme kwa muda.

“Kituo hiki kimeimarisha upatikanaji wa umeme wa uhakika. Tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa uwekezaji mkubwa uliofanyika. Hapo awali changamoto zilikuwa kubwa, hususan wakati wa mvua ambapo hitilafu katika wilaya moja ziliathiri huduma katika wilaya nyingine. Leo tunashuhudia matokeo ya uwekezaji huu kwa manufaa ya wananchi wetu,” alisema Mhe. Ndejembi.

Waziri huyo alibainisha kuwa Serikali itaendelea kuwekeza katika sekta ya nishati kupitia miradi mbalimbali ya kimkakati inayolenga kuimarisha uzalishaji, usafirishaji na usambazaji wa umeme nchini ili kuendana na kasi ya maendeleo ya Taifa na mahitaji ya wananchi.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, Mhe. Subira Mgalu, alisema utekelezaji wa miradi ya umeme unaendelea kuleta matokeo chanya kwa wananchi na kuchangia kufanikisha agenda ya maendeleo ya Serikali.

“Tunafarijika kuona kazi kubwa inayofanywa na TANESCO kuhakikisha Watanzania wanapata umeme wa uhakika. Hapo nyuma kulikuwa na changamoto za kukatika kwa umeme mara kwa mara katika maeneo haya, lakini Serikali ya Awamu ya Sita imefanya uwekezaji mkubwa kupitia TANESCO na matokeo yake yanaonekana wazi,” alisema Mhe. Mgalu.

Naye Mkuu wa Wilaya ya Kongwa, Mhe. Mayeka Simon Mayeka, aliwataka wananchi na wawekezaji kutumia fursa ya upatikanaji wa umeme wa uhakika kuanzisha shughuli mbalimbali za uzalishaji mali ikiwemo viwanda vya usindikaji, biashara na shughuli nyingine za kiuchumi zitakazochochea maendeleo ya eneo hilo.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO, Bw. Lazaro Twange, alisema kwa muda mrefu wananchi wa Kongwa na maeneo jirani walitegemea njia moja ya umeme ya msongo wa kilovoti 33 kutoka Dodoma Mjini, hali iliyokuwa ikisababisha changamoto za upatikanaji wa umeme wa uhakika kutokana na ongezeko la mahitaji ya huduma hiyo.

Alisema kukamilika kwa miradi hiyo kumeimarisha mfumo wa usambazaji wa umeme katika ukanda huo na kupunguza kwa kiasi kikubwa changamoto zilizokuwa zikiathiri upatikanaji wa huduma.

“Awali kulikuwa na njia moja ya kusambaza umeme inayopita katika wilaya tano tofauti. Kuongezeka kwa mahitaji ya umeme pamoja na fursa za uwekezaji kulianza kuleta changamoto katika utoaji wa huduma. Tangu miradi hii ilipoanza kufanya kazi, tumeshuhudia maboresho makubwa na changamoto zilizokuwa zikiathiri huduma zimepungua kwa zaidi ya asilimia 90,” alisema Bw. Twange.

Kukamilika kwa miradi hiyo kunatarajiwa kuimarisha zaidi upatikanaji wa huduma ya umeme, kuongeza fursa za uwekezaji, kukuza shughuli za kiuchumi na kuboresha utoaji wa huduma za kijamii katika Wilaya za Gairo, Mpwapwa, Kongwa, Chamwino na Kiteto.

Friday, June 12, 2026

CGP. KATUNGU AWATAKA MAAFISA USTAWI KUELIMISHA WAFUNGWA HAKI NA WAJIBU WAO


 Na. Ssgt Mawazo Mtondo – Dodoma.

Mkuu wa Jeshi la Magereza, CGP Jeremiah Yoram Katungu, amewataka Maafisa Ustawi wa Jamii wa Jeshi la Magereza kuhakikisha wanawaelimisha wafungwa na mahabusu kuhusu haki na wajibu wao mara wanapopokelewa magerezani pamoja na taratibu zinazopaswa kufuatwa katika kipindi chote wanaposhikiliwa gerezani.

CGP Katungu ametoa maelekezo hayo leo Juni 12, 2026 wakati akifunga rasmi Mafunzo ya Maafisa Ustawi wa Jamii kuhusu Mwongozo wa Utekelezaji wa Programu za Urekebishaji yaliyofanyika kwa siku tatu katika Ukumbi wa Rugimbana, Msalato jijini Dodoma.

Amesema mafunzo hayo ni sehemu ya jitihada za Jeshi la Magereza za kuendelea kuboresha huduma za urekebishaji kwa wafungwa sambamba na kutekeleza maelekezo ya Serikali na mapendekezo ya Tume ya Kuboresha Vyombo vya Haki Jinai.

Akizungumza na washiriki wa mafunzo hayo, CGP Katungu alisema mwongozo huo umebainisha maeneo muhimu yanayopaswa kuzingatiwa katika utekelezaji wa jukumu la urekebishaji, ikiwemo maadili ya kazi, dhana ya urekebishaji wa wafungwa, haki za binadamu katika utekelezaji wa programu za urekebishaji pamoja na matumizi sahihi ya nyaraka na fomu mbalimbali za kazi.

Aliwataka washiriki kutumia maarifa waliyojifunza kwa weledi na ufanisi ili kuleta mageuzi chanya katika utekelezaji wa jukumu la msingi la Jeshi la Magereza la kuwarekebisha wafungwa. Aidha, aliwahimiza kushirikiana na Wakuu wa Magereza kuanzisha na kuimarisha shughuli zinazolenga kuwapatia wafungwa elimu, maarifa na ujuzi wa kujitegemea.

Vilevile, aliwataka maafisa na askari wote wa Jeshi la Magereza kutekeleza majukumu yao kwa kuzingatia haki za wafungwa na mahabusu bila kuathiri usalama wao na wa magereza kwa ujumla. Alisisitiza umuhimu wa kudumisha upendo, mshikamano na umoja miongoni mwa watumishi wa Jeshi la Magereza ili kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa majukumu na kuendelea kulitumikia Taifa kwa ufanisi.

Awali akimkaribisha Mkuu wa Jeshi la Magereza, Kamishna wa Sheria na Uendeshaji wa Magereza, CP Nicodemus Tenga, alimshukuru kwa kuridhia kufanyika kwa mafunzo hayo yaliyolenga kuwajengea uwezo, maarifa na stadi za kiutendaji Maafisa Ustawi wa Jamii.

CP Tenga alisema mafunzo hayo pia yalitoa fursa kwa washiriki kubadilishana uzoefu na kujifunza mbinu mbalimbali za kuboresha utendaji wao katika maeneo ya kazi kwa lengo la kuimarisha huduma za urekebishaji ndani ya Jeshi la Magereza.











RAIS SAMIA AIPONGEZA BOT KWA KUKUSANYA DHAHABU YA THAMANI YA TSH TRILIONI 10, ATOA MAELEKEZO MAPYA KUHUSU MIKOPO KWA WANANCHI

 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye picha na Waziri wa Fedha Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar pamoja na Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania Bw. Emmanuel Tutuba kwenye Maadhimisho ya cha miaka 60 ya Benki Kuu ya Tanzania yaliyofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC), Jijini Dar es Salaam tarehe 12 Juni, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akipokea zawadi ya Kitabu cha picha za matoleo ya noti kuanzia mwaka 1966-2026, pamoja na Sarafu ya kumbukumbu ya miaka 60 ya Benki Kuu ya Tanzania kutoka kwa Gavana wa Benki hiyo Bw. Emmanuel Tutuba katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC), Jijini Dar es Salaam tarehe 12 Juni, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akipokea zawadi ya Kitabu cha picha za matoleo ya noti kuanzia mwaka 1966-2026, pamoja na Sarafu ya kumbukumbu ya miaka 60 ya Benki Kuu ya Tanzania kutoka kwa Gavana wa Benki hiyo Bw. Emmanuel Tutuba katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC), Jijini Dar es Salaam tarehe 12 Juni, 2026.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akipokea Tuzo Maalum kutoka Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania Bw. Emmanuel Tutuba kwenye Maadhimisho ya cha miaka 60 ya Benki hiyo yaliyofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC), Jijini Dar es Salaam tarehe 12 Juni, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, ameipongeza Benki Kuu ya Tanzania (BoT) kwa mafanikio makubwa ya kukusanya tani 27.05 za dhahabu zenye thamani ya zaidi ya Shilingi trilioni 10, hatua aliyoitaja kuwa ya kimkakati katika kuimarisha uchumi wa Taifa na kulinda thamani ya Shilingi ya Tanzania.

Rais Samia ametoa pongezi hizo leo Juni 12, 2026, wakati akihutubia kilele cha Maadhimisho ya Miaka 60 ya Benki Kuu ya Tanzania yaliyofanyika katika Ukumbi wa Kimataifa wa Mikutano wa Julius Nyerere (JNICC), jijini Dar es Salaam.

"Nipongeze Benki Kuu kwa mpango wa ununuzi wa dhahabu ya ndani. Hadi mwezi Mei mwaka huu tumefanikiwa kukusanya tani 27.05 za dhahabu zenye thamani ya shilingi trilioni 10. Hapa tulipofika si haba," amesema Rais Samia huku akisisitiza umuhimu wa kuendelea kuimarisha akiba ya Taifa.

Ameeleza kuwa mkakati wa kununua dhahabu kutoka ndani ya nchi umeiwezesha Tanzania kuongeza uwezo wa kukabiliana na misukosuko ya uchumi wa dunia huku ukiimarisha akiba ya fedha za kigeni na kuongeza uthabiti wa mfumo wa kifedha.

Katika hotuba yake, Rais Samia ameitaka Benki Kuu kuendelea kusimamia kwa karibu sekta ya fedha ili kuhakikisha mfumuko wa bei unaendelea kudhibitiwa na uchumi wa nchi unaendelea kukua kwa manufaa ya wananchi wote.

Aidha, amesisitiza umuhimu wa matumizi ya teknolojia na ubunifu wa kidijitali katika sekta ya fedha ili huduma za kifedha ziweze kuwafikia Watanzania wengi zaidi, hususan waliopo maeneo ya vijijini na pembezoni.

Katika hatua nyingine, Rais Samia ametoa maelekezo muhimu kwa Benki Kuu na taasisi za fedha nchini kutafuta njia mbadala za kuwawezesha wananchi kupata mikopo hata kama hawana dhamana za kawaida kama nyumba, viwanja au magari.

Amesema wananchi wenye biashara zinazoonekana, historia nzuri ya mauzo pamoja na rekodi za miamala wanapaswa kupewa nafasi ya kupata mikopo kwa kuzingatia kiwango chao cha uaminifu na uwezo wa kurejesha fedha.

"Tusimnyime mtu mkopo kwa sababu hana mali tulizozizoea wakati ana historia inayoonesha wazi kuwa anaaminika. Uaminifu ni mali kubwa kuliko hata mali inayoonekana," amesisitiza Rais Samia.

Kauli hiyo imepokelewa kwa matumaini makubwa na wadau wa uchumi na biashara, ikitarajiwa kufungua fursa zaidi kwa wajasiriamali wadogo na wa kati ambao mara nyingi hukosa mikopo kutokana na kutokuwa na dhamana za jadi zinazotakiwa na taasisi za fedha.

Maadhimisho ya miaka 60 ya Benki Kuu ya Tanzania yamekuwa fursa ya kutafakari mchango wa taasisi hiyo katika maendeleo ya uchumi wa Taifa huku yakifungua ukurasa mpya wa mageuzi yanayolenga kujenga mfumo wa kifedha unaojumuisha wananchi wengi zaidi na kuchochea ukuaji wa uchumi unaogusa maisha ya kila Mtanzania.

RAIS SAMIA AMKARIBISHA RAIS WA NAMIBIA KATIKA ZIARA YA KITAIFA, WAIMARISHA USHIRIKIANO WA KIDIPLOMASIA NA MAENDELEO

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye picha na mgeni wake Rais wa Jamhuri ya Namibia Mhe. Dkt....