Thursday, April 02, 2026

UTEKELEZAJI WA DIRA 2050 UANZE - DKT. MWIGULU





WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba ameagiza kuanza utekelezaji wa Dira 2050 kupitia Mpango na Bajeti iliyoandaliwa na kuendelea kuishirikisha sekta binafsi na wadau wa maendeleo katika kuharakisha utekelezaji wake ili kujenga uchumi jumuishi, shindani na unaotegemea uzalishaji wenye tija.

Aidha, Waziri Mkuu ameilekeza Tume ya Mipango kuendelea kutoa elimu kwa umma kuhusu Dira 2050 ili kuwezesha kushiriki kikamilifu katika utekelezaji wake kwa sababu suala hilo litawezekana ikiwa wadau wote watakuwa na ufahamu wa kutosha kuhusu vipaumbele vilivyoainishwa katika Dira 2050.

Waziri Mkuu ametoa maagizo hayo leo (Jumatano, Aprili 1, 2026) wakati akiwasilisha hotuba yake kuhusu Mapitio na Mwelekeo wa Kazi za Serikali na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na Ofisi ya Bunge kwa Mwaka 2026/2027 Bungeni jijini Dodoma.

Amesema Dira 2050 iliyozinduliwa na Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan mnamo tarehe 17 Julai, 2025, itaongoza mipango ya maendeleo katika miaka 25 ijayo inalenga kujenga Taifa jumuishi, lenye ustawi kwa wote, lenye haki na linalojitegemea.

 “Nitoe rai kwa viongozi wa Serikali, Dini, Sekta Binafsi, Asasi za Kiraia na Wadau wa Maendeleo kuhakikisha kwamba mipango yao inawiana na vipaumbele vya Dira 2050 na kuiunga mkono katika utekelezaji wake”.

Amesema utekelezaji wa Dira hiyo, utawezesha Taifa kuwa na uchumi wenye thamani ya dola za Marekani trilioni moja na wastani wa pato la mtu mmoja mmoja kuwa dola za Marekani 7,000 kwa mwaka ifikapo 2050. “Nguzo muhimu za kutuwezesha kufikia malengo hayo ni pamoja na utawala bora, amani, usalama na utulivu.”

Vilevile, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu amewaagiza viongozi wa kila sekta wahakikishe rasilimali zote za Taifa zinaelekezwa katika maeneo yenye tija na matokeo makubwa ili kupunguza utegemezi kutoka nje.

Amesema kuwa Dira 2050 imejengwa na nguzo kuu tatu ambazo ni uchumi imara jumuishi na shindani; uwezo wa watu na maendeleo ya jamii; na uhifadhi wa mazingira na ustahimilivu wa mabadiliko ya tabianchi.

Amesema katika hatua za kutekeleza Dira hiyo kwa vitendo, Serikali kwa kushirikiana na wadau imeweka mikakati mbalimbali ya utekelezaji, ambayo ni pamoja na kuchagiza ubia kati ya sekta ya umma na binafsi.

Waziri Mkuu ameongeza kuwa mikakati mingine ni pamoja na matumizi yenye tija ya rasilimali za Taifa kupitia utekelezaji wa programu za kimkakati na kukuza utamaduni wa kuweka akiba kwa ajili ya uwekezaji.

Amesema Mpango na Bajeti itakayopitishwa na Bunge hilo ni hatua ya kwanza ya utekelezaji wa Mpango wa Nne wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano 2026/2027 - 2030/2031 na Dira 2050,huku dhima ya mpango huo ni “Mageuzi katika Kukuza Uchumi na Kuzalisha Ajira.”

Amesema mipango hiyo inawezesha Taifa kuelekeza rasilimali katika vipaumbele vya kimkakati vyenye matokeo makubwa kwa ajili ya ukuaji wa uchumi na ustawi wa wananchi.

Aidha, Waziri Mkuu amesema kwa kutambua umuhimu wa Dira hiyo, Serikali itaendelea kuimarisha mfumo wa ufuatiliaji na tathmini pamoja na kuhimiza uwajibikaji, ili kuhakikisha tunafikia malengo tuliyojiwekea.

Waziri Mkuu ameliomba Bunge liidhinishe jumla ya shilingi trilioni 12.50 kati ya fedha hizo, shilingi trilioni 8.73 ni kwa ajili ya matumizi ya kawaida na shilingi trilioni 3.76 ni kwa ajili ya matumizi ya maendeleo. Fedha hizo ni kwa ajili ya Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake kwa mwaka 2026/2027.

Vilevile, Waziri Mkuu ameliomba Bunge liidhinishe jumla ya shilingi 225,021,780,000 kwa ajili ya Mfuko wa Bunge. Kati ya fedha hizo, shilingi 207,992,798,000 ni kwa ajili ya matumizi ya kawaida na shilingi 17,028,982,000 ni kwa ajili ya matumizi ya maendeleo.

Wednesday, April 01, 2026

WATENGENEZA MAUDHUI MTANDAONI WATAKIWA KUTENGENEZA MAUDHUI YANAYOLINDA TASWIRA YA NCHI

 

Mkuu wa Wilaya ya Nyamagana iliyopo mkoani Mwanza, Mhe. Amina Makilagi {pichani juu] amewataka Watengeneza Maudhui Mtandaoni kuzingatia maadili, uzalendo pamoja na kulinda taswira ya Tanzania kwenye maudhui wanayoyatengeneza.

Mhe. Amina ametoa rai hiyo Aprili 1, 2026 mkoani hapo wakati akizungumza kwenye Mafunzo kwa Watengenza Maudhui Mtandaoni (Content Creators) awamu ya kwanza yaliyoandaliwa na Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo. 

“Msisitizo kwenu watengeneza maudhui, mafunzo mliyoyapata hapa yasiishie hapa bali yatumieni katika kuboresha kazi zenu ili muweze kuongeza kipato cha familia na Taifa kwa ujumla” alisistiza Mhe. Amina.

Aidha, amewataka washiriki hao kuongeza ujuzi kupitia njia mbalimbali ili kuendana na mabadiliko ya teknolojia.

Kwa upande wake Afisa Mtendaji Mkuu wa Mfuko wa Utamaduni na Sanaa Tanzania, CPA (T) Nyakaho Mahemba amesema kuwa, lengo la mafunzo hayo ni kuwasaidia wazalisha maudhui mtandaoni kupata elimu ya mkopo, uandishi wa mradi pamoja na namna ya kuzalisha kazi bora zaidi zitakazokidhi soko la ndani na nje pamoja na kuweza kuweka ushindani.

Naye Bw. Andrew Ngonyani (Brother K) aliyeshiriki mafunzo hayo aliishukuru Serikali kwa kutoa mafunzo hayo ambayo yamewasaidia vijana wengi kuweza kutumia maudhui yao kupata pesa, akiishauri Serikali kuendelea kuweka mazingira bora kwa wasanii kufanya sanaa na kunufaika nayo.

Mafunzo hayo yamekuwa na mada mbalimbali ikiwemo Elimu ya Mtaji, Kubiasharisha Maudhui Mtandaoni, Uaminifu uwajibikaji kwa wafuasi wako pamoja na hatua kwa hatua namna ya kutengeneza akaunti ya biashara na kuingiza kipato.










NCHIMBI AKISALIMIANA NA BABA MTAKATIFU BAADA YA IBADA YA HIJA VATICAN

 
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi, akisalimiana na Kiongozi Mkuu wa Kanisa Katoliki Duniani, Baba Mtakatifu Leo XIV, mara baada ya Ibada ya Hija iliyofanyika katika Uwanja wa Kanisa Kuu la Mtakatifu Petro – Vatican, leo tarehe 01 April 2026.




Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi akifurahi jambo na Kiongozi Mkuu wa Kanisa Katoliki Duniani, Baba Mtakatifu Leo XIV, wakati wakiagana mara baada ya Ibada ya Hija iliyofanyika katika Uwanja wa Kanisa Kuu la Mtakatifu Petro – Vatican leo tarehe 01 Aprili 2026.

RAIS SAMIA AKUTANA NA WAGOMBEA URAIS: ASISITIZA UMOJA, DEMOKRASIA NA MAENDELEO ENDELEVU

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye mazungumzo na Wagombea wa Nafasi ya Urais na Wagombea Wenza kutoka vyama vya Siasa 16 vilivyoshiriki Uchaguzi Mkuu uliofanyika mwezi Oktoba, 2025. Mazungumzo hayo yalifanyika Ikulu jijini Dar es Salaam tarehe 31 Machi, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye picha na Wagombea wa nafasi ya Urais pamoja na Wagombea Wenza wa Vyama vya Siasa 16 vilivyoshiriki Uchaguzi Mkuu uliofanyika mwezi Oktoba, 2025 mara baada ya Mazungumzo yao, Ikulu jijini Dar es Salaam tarehe 31 Machi, 2026.



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye picha na Wagombea wa nafasi ya Urais Wanawake ambao ni Saum Hussein Rashid kutoka chama cha UDP na Mwajuma Noty Mirambo kutoka chama cha UMD walioshiriki Uchaguzi Mkuu uliofanyika mwezi Oktoba, 2025 mara baada ya mazungumzo yao, Ikulu jijini Dar es Salaam tarehe 31 Machi, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, amekutana na Wagombea wa nafasi ya Urais pamoja na Wagombea Wenza kutoka vyama vya siasa 16 vilivyoshiriki katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2025, katika mazungumzo yaliyofanyika Ikulu jijini Dar es Salaam tarehe 31 Machi, 2026.

Mkutano huo umebeba uzito wa kipekee katika kuendeleza misingi ya demokrasia jumuishi, maridhiano ya kisiasa, na mshikamano wa kitaifa. Kupitia majadiliano hayo, viongozi hao walipata fursa ya kubadilishana mawazo, kujenga uelewano wa pamoja, na kuweka msingi imara wa ushirikiano kwa maslahi mapana ya Taifa.

Rais Samia alisisitiza umuhimu wa siasa za ustaarabu, kuheshimu tofauti za kiitikadi, na kuweka mbele maslahi ya wananchi. Alieleza kuwa maendeleo endelevu hayawezi kupatikana bila kuwepo kwa mazingira ya amani, utulivu na mshikamano wa kisiasa.

Kwa upande wao, wagombea walionesha utayari wa kushirikiana na Serikali katika kujenga Taifa lenye umoja na lenye kulenga maendeleo ya kiuchumi na kijamii, wakitambua nafasi yao katika kuimarisha demokrasia na uwajibikaji.

Hatua hii inaakisi dhamira ya dhati ya uongozi wa juu wa nchi katika kukuza diplomasia ya ndani (internal political diplomacy) na kuimarisha misingi ya utawala bora. Ni ishara kwamba Tanzania inaendelea kusonga mbele kwa umoja, kwa misingi ya kazi, utu, na mshikamano wa kitaifa.

#KaziNaUtuTunasongaMbele #TabasamuLaUtu #MaendeleoEndelevu #DiplomasiaYaKiuchumi

Tuesday, March 31, 2026

VIONGOZI WAUNGANA KUAGA MWILI WA MAREHEMU MHE. WILLIAM LUKUVI IRINGA

 










Iringa, Machi 31, 2026 — Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba, amewasili nyumbani kwa aliyekuwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu) na Mbunge wa Jimbo la Isimani, Marehemu Mhe. William Lukuvi, kilichopo Kijiji cha Idodi mkoani Iringa, kuongoza mamia ya waombolezaji katika shughuli za maziko zilizofanyika leo.

Ujio wa kiongozi huyo umeambatana na viongozi mbalimbali wa Serikali, wabunge, viongozi wa vyama vya siasa pamoja na wananchi kutoka maeneo tofauti ya nchi waliojitokeza kutoa heshima zao za mwisho kwa kiongozi huyo aliyekuwa na mchango mkubwa katika utumishi wa umma.

Akizungumza katika shughuli hiyo, Mhe. Dkt. Nchemba alieleza kuwa taifa limepoteza kiongozi mwenye uzoefu, aliyekuwa mstari wa mbele kusimamia sera, uratibu wa shughuli za Serikali na utetezi wa masuala ya watu wenye ulemavu. Alisisitiza kuwa mchango wa Marehemu Lukuvi utaendelea kukumbukwa na kuthaminiwa na vizazi vya sasa na vijavyo.

Marehemu Mhe. William Lukuvi alifariki dunia tarehe 25 Machi, 2026 katika Hospitali ya Benjamin Mkapa jijini Dodoma alipokuwa akipatiwa matibabu. Enzi za uhai wake, alitumikia nafasi mbalimbali za uongozi serikalini kwa weledi na uzalendo mkubwa, akijijengea heshima ndani na nje ya Bunge.

Maziko hayo yamefanyika katika kijiji chake cha nyumbani cha Idodi, huku yakihudhuriwa na umati mkubwa wa wananchi waliokusanyika kumlaki na kumuaga kiongozi wao kwa heshima na majonzi makubwa.

Taifa linaendelea kuungana na familia, ndugu, jamaa na wananchi wa Jimbo la Isimani katika kipindi hiki kigumu cha maombolezo. Mwenyezi Mungu ailaze roho ya Marehemu mahali pema peponi.

TARURA YATEKELEZA UJENZI WA KM 56 ZA BARABARA ZA LAMI ILALA KUPITIA DMDP II






‎Serikali kupitia Wakala ya Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) imeanza kutekeleza ujenzi wa barabara zaidi ya Kilomita 56 kwa kiwango cha lami na zege kupitia mradi wa Uendelezaji Jiji la Dar es Salaam Awamu ya Pili (DMDP II) katika Halmashauri ya Manispaa ya Ilala mkoani humo.

‎Akiwa katika ziara ya ukaguzi wa miradi hiyo Kaimu Meneja wa TARURA wilaya ya Ilala, Mhandisi Grayson Nzunda amesema kuwa miradi inayojengwa ni barabara za lami na zege, mifereji ya maji ya mvua, makalavati, njia za waenda kwa miguu, uwekaji wa taa za barabarani pamoja na kuweka alama za barabarani ambapo mradi unagharimu shilingi Bilioni 138.

‎“Hapa tulipo ni maeneo ya Kivule tupo kukagua ujenzi wa barabara zenye urefu wa Kilomita 12, barabara ya Kivule-Majohe Junction Km 2.79 inajengwa kwa kiwango cha zege na barabara ya Kitunda-Kivule-Msongola Km 9.95 inajengwa kwa kiwango cha lami, mradi umegharimu shilingi Bilioni 30 kati ya Bilioni 138 za wilaya nzima ya Ilala”, alisema.

‎Ameeleza kuwa barabara hizo zilikuwa na changamoto kubwa hivyo kukamilika kwake zitasaidia wananchi kufikia huduma mbalimbali kwa urahisi na kupunguza gharama za usafiri na usafirishaji, pia barabara hizo zinatumika kama ‘bypass’ kwa wanaokwenda Chanika au Majohe kama barabara kubwa ikiwa na foleni.

‎Naye, Bi. Vicky Shayo mkazi wa Kitunda amesema kuwa wamekuwa wakikosa wateja katika biashara zao kutokana na changamoto ya barabara hasa kipindi cha mvua kutokana na maji mengi na matope ambapo inapelekea watu kuanguka kwasababu ya udongo kuteleza, lakini barabara ikikamilika itawasaidia kufanya biashara zao na kipato kitaongezeka.

‎Bi. Maria Petro mkazi wa Kivule ameishukuru serikali kwa uboreshaji wa miundombinu ya barabara kwani walikuwa wanapata changamoto kwenda hospitalini lakini sasa hivi usafiri umekuwa rahisi kufika mpaka Banana.

‎Aidha, Mwenyekiti wa mtaa wa Karume Bw. Hajibu China amemshukuru Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwani anaiona Ilala inakwenda kubadilika kutokana na maboresho ya barabara kwani wananchi wanajenga nyumba zao, pia kutakuwa na taa za barabarani zitakazopendezesha mji na kuongeza ulinzi na usalama.

Friday, March 27, 2026

TBC Yawajengea Uwezo Washitiri Uzalishaji wa Vipindi

Kaimu Mkurugenzi wa Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC), Bw. Gwakisa Mlawa akizungumza wakati wa kufunga Mkutano wa 110 wa wadau wa elimu kwa umma (Washitiri), uliofanyika  katika ukumbi wa PAPU, Jijini Arusha, Machi 27, 2026

Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano LATRA, Bw. Salum Pazzy, akitoa salamu za shukrani kwa TBC kwa niaba ya washitiri wengine wakati wa kufunga Mkutano wa 110 wa wadau wa elimu kwa umma uliofanyika  katika ukumbi wa PAPU, Jijini Arusha, Machi 27, 2026.
Baadhi ya Washitiri walioshiriki Mkutano wa 110 wa wadau wa elimu kwa umma uliofanyika  katika ukumbi wa PAPU, Jijini Arusha, Machi 23 - 27, 2026.

Adelina Johnbosco na Timothy Mwakyenda – MAELEZO

Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC) limetoa mafunzo ya uandaaji bora wa vipindi kwa washitiri wa taasisi za umma nchini ili kuwajengea uwezo wa kutoa elimu kwa umma.

Washitiri hao kutoka vitengo vya mawasiliano vya wizara, taasisi, idara, mamlaka na mashirika ya umma wanahusika na utoaji wa taarifa za Serikali na utekelezaji wa shughuli na miradi mbalimbali ya maendeleo ya wananchi.

Akizungumza wakati wa kufunga mafunzo hayo, Kaimu Mkurugenzi wa TBC, Bw. Gwakisa Mlawa, amesema ana imani mafunzo hayo yataongeza ujuzi na ufanisi kwa washiriki katika majukumu yao ya kila siku ya mawasiliano.

Amesema mafunzo hayo pia yatakuwa chachu ya maboresho ya maudhui yanayozalishwa, kutokana na maarifa waliyopata kupitia wataalamu waliobobea katika nyanja tofauti.

Mafunzo hayo yamejumuisha mada mbalimbali zikiwemo uongozi bora, uandaaji wa vipindi, matumizi ya akili unde (AI) pamoja na mbinu za utatuzi wa migogoro kazini.

“Mawasiliano siyo suala la kutoa na kupokea taarifa tu, bali ni kujenga taswira nzuri ya taasisi na taifa kwa ujumla,” alisema Bw. Mlawa.

Aidha, amesema TBC inaendelea kuwekeza katika teknolojia za kisasa ili kuboresha utoaji wa huduma za habari na mawasiliano kwa wananchi akiwakaribisha wadau na wananchi kuendelea kuitumia TBC kama chombo muhimu cha utangazaji nchini.

Kwa upande wake Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano wa Mamlaka ya Udhibiti wa Usafiri Ardhini (LATRA), Bw. Salum Pazzy, akizungumza kwa niaba ya washiriki wenzake ameipongeza TBC kwa kuandaa mafunzo hayo, akieleza kuwa yamekuwa na manufaa makubwa kwa washitiri wote.

Amesema mafunzo hayo yamewajengea uwezo wa kuzalisha vipindi vya elimu kwa umma kwa weledi na uzalendo. 

UTEKELEZAJI WA DIRA 2050 UANZE - DKT. MWIGULU

WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba ameagiza kuanza utekelezaji wa Dira 2050 kupitia Mpango na Bajeti iliyoandaliwa na kuendelea kuishirikisha ...