Friday, April 03, 2026

TANZANIA NA URUSI ZAIMARISHA USHIRIKIANO WA KIMKAKATI KATIKA SEKTA YA UCHUKUZI

Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Shirikisho la Urusi zimeingia hatua mpya ya ushirikiano wa maendeleo baada ya kusaini hati ya makubaliano katika sekta ya uchukuzi, ikiwa ni sehemu ya jitihada za kukuza miundombinu ya kisasa na kuongeza ufanisi wa usafirishaji nchini.

Makubaliano hayo yalisainiwa tarehe 03 Aprili 2026 jijini St. Petersburg, Urusi, pembezoni mwa Mkutano wa Kimataifa wa Uchukuzi na Usafirishaji, yakihusisha Wizara ya Uchukuzi ya Tanzania na Wizara ya Uchukuzi ya Shirikisho la Urusi.

Kwa upande wa Urusi, Waziri wa Uchukuzi, Mhe. Andrey Nikitin, alieleza kuwa nchi yake ipo tayari kuendeleza ushirikiano wa karibu na Tanzania, akisisitiza kuwa hatua hiyo ni utekelezaji wa maazimio ya Mkutano wa Russia–Africa 2023. Alibainisha kuwa ushirikiano huo utahusisha uwekezaji katika miundombinu ya kisasa, msaada wa kiufundi, pamoja na ushiriki katika miradi ya kimkakati yenye tija kwa pande zote mbili.

Naye Waziri wa Uchukuzi wa Tanzania, Mhe. Prof. Makame Mbarawa, alisema makubaliano hayo yanaendana kikamilifu na mkakati wa Serikali wa kuimarisha sekta ya uchukuzi kwa kushirikiana na mataifa yenye uzoefu mkubwa na teknolojia ya hali ya juu.

Alifafanua kuwa kupitia ushirikiano huo, Tanzania itanufaika na ubadilishanaji wa utaalamu, mafunzo kwa wataalamu, pamoja na uhamishaji wa teknolojia utakaosaidia kuongeza ufanisi, ubora na ushindani wa miundombinu ya uchukuzi. Aidha, alisisitiza kuwa hatua hiyo itaiwezesha Tanzania kujijengea nafasi imara kama kitovu cha usafirishaji na biashara katika ukanda wa Afrika Mashariki na kati.

Kwa mtazamo mpana, makubaliano haya yanafungua ukurasa mpya wa fursa za uwekezaji, utafiti na ubunifu, huku yakichochea maendeleo ya rasilimali watu na kuimarisha zaidi uhusiano wa kidiplomasia na kiuchumi kati ya Tanzania na Urusi.

#Tanzania #Urusi #Uchukuzi #Maendeleo #Uwekezaji #Diplomasia #Miundombinu #HabariZaLeo








UPATIKANAJI WA DAWA WAIMARIKA NCHINI

 OWM-TAMISEMI

Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa  (OWM– TAMISEMI) anayeshughulikia masuala ya Afya, Mhe. Dkt. Jafari Seif, amesema kuwa hali ya upatikanaji wa bidhaa za afya katika ngazi ya huduma za afya ya msingi nchini imeendelea kuimarika na kufikia kiwango cha kuridhisha ikilinganishwa na miaka iliyopita.

Akizungumza Aprili 2, 2026 jijini Dar es Salaam, katika kikao kazi kilichoongozwa na Waziri wa Afya, Mhe.Mohamed Mchengerwa, pamoja na wadau wa sekta ya afya, katika ofisi za Bohari ya Dawa (MSD), Mhe. Dkt. Seif amesema kuwa tathmini ya mwaka 2026 inaonesha hali ya upatikanaji wa dawa imefikia asilimia 89 katika hospitali, asilimia 88 katika vituo vya afya, na asilimia 88 katika zahanati.

Ameongeza kuwa katika mwaka wa fedha 2024/25, vituo vya kutolea huduma za afya ngazi ya msingi vilikusanya takribani Shilingi Bilioni 108, huku makusanyo hayo yakitarajiwa kuongezeka hadi kufikia Shilingi Bilioni 192 katika mwaka 2025/26.   

Kwa upande wake, Waziri wa Afya, Mhe. Mohamed Mchengerwa, amemuelekeza Katibu Mkuu wa wizara hiyo kushirikiana kwa karibu na Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI kuandaa na kusimamia miongozo, taratibu na miundo ya usimamizi wa vituo vya kutolea huduma za afya. Lengo la hatua hiyo ni kuhakikisha kuwa wafamasia kote nchini wanakuwa sehemu muhimu ya timu za menejimenti katika vituo hivyo, ili kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma za afya.




MAKAMU WA PILI WA RAIS ZANZIBAR AUNGANA NA WAUMINI IJUMAA PEMBA, ASISITIZA UMOJA NA MAADILI






Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Alhajj Hemed Suleiman Abdulla, leo ameungana na Waumini wa Dini ya Kiislamu katika ibada ya Sala ya Ijumaa iliyofanyika katika Msikiti wa Al-Tawfiiq, uliopo Jundamiti Kiwani, Wilaya ya Mkoani, Mkoa wa Kusini Pemba.

Mara baada ya ibada hiyo, Alhajj Hemed alipata fursa ya kuwasalimia waumini na kubadilishana nao salamu za amani, upendo na mshikamano, akionesha ukaribu wa dhati kati ya uongozi na wananchi. Tukio hilo liligubikwa na hali ya furaha na heshima, huku waumini wakionesha kuthamini uwepo wa kiongozi huyo miongoni mwao.

Katika mazungumzo yake, alisisitiza umuhimu wa kudumisha maadili mema, kuheshimiana na kuendeleza umoja kama nguzo muhimu ya ustawi wa jamii na maendeleo endelevu. Amesema mshikamano wa kijamii na kiroho ni msingi imara unaoweza kuijenga jamii yenye amani na utulivu.

Tukio hilo limeendelea kudhihirisha dhamira ya viongozi kuwa karibu na wananchi pamoja na kuimarisha uhusiano unaojenga mshikamano na maelewano katika jamii.

Imetolewa na Kitengo cha Habari (OMPR)
Leo, tarehe 03 Aprili 2026.

#Zanzibar #Pemba #Ijumaa #Uongozi #Mshikamano #Amani #Maendeleo #OMPR #HabariZaLeo

TAIFA GAS IMETANGAZA KUWA HAITAPANDISHA BEI YA GESI YA MAJUMBANI (LPG) LICHA YA ONGEZEKO LA BEI KATIKA SOKO LA KIMATAIFA

 

Picha ni ya AI

Taifa Gesi haitapandisha bei ya gesi ya majumbani (LPG) licha ya ongezeko la takribani asilimia 43 ya bei ya gesi hiyo duniani. Hatua hii ni sehemu ya juhudi za kampuni hiyo kuendeleza upatikanaji nafuu wa nishati hiyo pamoja na kupunguza za athari za mabadiliko ya soko la kimataifa kwa wateja wake.

Katika taarifa yake kwa vyombo vya habari, Taifa Gas imeeleza kuwa soko la kimataifa la gesi ya kupikia limekumbwa na ongezeko kubwa la bei katika wiki za hivi karibuni na hivyo kusababisha kuongezeka kwa gharama za ununuzi katika minyororo ya ugavi na usambazaji duniani.

Alieleza kuwa katika wiki za hivi karibuni, soko la kimataifa la gesi ya kupikia limekumbwa na ongezeko kubwa la bei, hali iliyosababisha kupanda kwa gharama katika minyororo ya ugavi na usambazaji duniani.

“Katika mazingira haya ya sasa, tunayo dhamira ya dhati ya kuwasaidia wateja wetu kwa kubeba athari za ongezeko la gharama ya nishati ya kupikia kwa kutokuongeza bei huku tukihakikisha upatikanaji endelevu wa gesi safi na ya kuaminika,” alisema Deogratius.

Aliongeza kuwa kipaumbele cha kampuni hiyo kwa sasa ni kuhakikisha utulivu wa bei unaendelea ili kusaidia shughuli za kiuchumi, akibainisha kuwa gesi ya kupikia ni nishati muhimu kwa kaya nyingi pamoja na biashara ndogo ndogo nchini.

“Tunatambua kuwa gesi ya kupikia ni nishati muhimu kwa Watanzania wengi na lengo letu ni kuhakikisha kwamba inapatikana kwa bei nafuu huku tukidumisha usambazaji wa uhakika kote nchini,” alisisitiza.

Kwa upande wa usambazaji, kampuni hiyo imeeleza kuwa itaendelea kuhakikisha upatikanaji wa gesi kupitia mtandao wake wa maghala 25 yaliyosambaa nchini, hatua inayolenga kufikisha huduma hiyo katika maeneo ya mijini na vijijini.

Deogratius alibainisha kuwa Tanzania ni nchi kubwa yenye mahitaji tofauti ya nishati, hivyo uwekezaji katika miundombinu ya usambazaji umezingatiwa ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma hiyo kwa urahisi zaidi.

Aidha, kampuni hiyo imeeleza kuwa inaendelea kuunga mkono vipaumbele vya kitaifa vya nishati pamoja na Malengo ya Maendeleo Endelevu (SDGs), kwa kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia.

Ilieleza kuwa matumizi ya gesi ya kupikia yanachangia kuboresha afya za wananchi kwa kupunguza athari za moshi wa kuni na mkaa, sambamba na kulinda mazingira na kuchochea ushiriki wa wananchi katika shughuli za kiuchumi.

Thursday, April 02, 2026

UTEKELEZAJI WA DIRA 2050 UANZE - DKT. MWIGULU





WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba ameagiza kuanza utekelezaji wa Dira 2050 kupitia Mpango na Bajeti iliyoandaliwa na kuendelea kuishirikisha sekta binafsi na wadau wa maendeleo katika kuharakisha utekelezaji wake ili kujenga uchumi jumuishi, shindani na unaotegemea uzalishaji wenye tija.

Aidha, Waziri Mkuu ameilekeza Tume ya Mipango kuendelea kutoa elimu kwa umma kuhusu Dira 2050 ili kuwezesha kushiriki kikamilifu katika utekelezaji wake kwa sababu suala hilo litawezekana ikiwa wadau wote watakuwa na ufahamu wa kutosha kuhusu vipaumbele vilivyoainishwa katika Dira 2050.

Waziri Mkuu ametoa maagizo hayo leo (Jumatano, Aprili 1, 2026) wakati akiwasilisha hotuba yake kuhusu Mapitio na Mwelekeo wa Kazi za Serikali na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na Ofisi ya Bunge kwa Mwaka 2026/2027 Bungeni jijini Dodoma.

Amesema Dira 2050 iliyozinduliwa na Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan mnamo tarehe 17 Julai, 2025, itaongoza mipango ya maendeleo katika miaka 25 ijayo inalenga kujenga Taifa jumuishi, lenye ustawi kwa wote, lenye haki na linalojitegemea.

 “Nitoe rai kwa viongozi wa Serikali, Dini, Sekta Binafsi, Asasi za Kiraia na Wadau wa Maendeleo kuhakikisha kwamba mipango yao inawiana na vipaumbele vya Dira 2050 na kuiunga mkono katika utekelezaji wake”.

Amesema utekelezaji wa Dira hiyo, utawezesha Taifa kuwa na uchumi wenye thamani ya dola za Marekani trilioni moja na wastani wa pato la mtu mmoja mmoja kuwa dola za Marekani 7,000 kwa mwaka ifikapo 2050. “Nguzo muhimu za kutuwezesha kufikia malengo hayo ni pamoja na utawala bora, amani, usalama na utulivu.”

Vilevile, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu amewaagiza viongozi wa kila sekta wahakikishe rasilimali zote za Taifa zinaelekezwa katika maeneo yenye tija na matokeo makubwa ili kupunguza utegemezi kutoka nje.

Amesema kuwa Dira 2050 imejengwa na nguzo kuu tatu ambazo ni uchumi imara jumuishi na shindani; uwezo wa watu na maendeleo ya jamii; na uhifadhi wa mazingira na ustahimilivu wa mabadiliko ya tabianchi.

Amesema katika hatua za kutekeleza Dira hiyo kwa vitendo, Serikali kwa kushirikiana na wadau imeweka mikakati mbalimbali ya utekelezaji, ambayo ni pamoja na kuchagiza ubia kati ya sekta ya umma na binafsi.

Waziri Mkuu ameongeza kuwa mikakati mingine ni pamoja na matumizi yenye tija ya rasilimali za Taifa kupitia utekelezaji wa programu za kimkakati na kukuza utamaduni wa kuweka akiba kwa ajili ya uwekezaji.

Amesema Mpango na Bajeti itakayopitishwa na Bunge hilo ni hatua ya kwanza ya utekelezaji wa Mpango wa Nne wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano 2026/2027 - 2030/2031 na Dira 2050,huku dhima ya mpango huo ni “Mageuzi katika Kukuza Uchumi na Kuzalisha Ajira.”

Amesema mipango hiyo inawezesha Taifa kuelekeza rasilimali katika vipaumbele vya kimkakati vyenye matokeo makubwa kwa ajili ya ukuaji wa uchumi na ustawi wa wananchi.

Aidha, Waziri Mkuu amesema kwa kutambua umuhimu wa Dira hiyo, Serikali itaendelea kuimarisha mfumo wa ufuatiliaji na tathmini pamoja na kuhimiza uwajibikaji, ili kuhakikisha tunafikia malengo tuliyojiwekea.

Waziri Mkuu ameliomba Bunge liidhinishe jumla ya shilingi trilioni 12.50 kati ya fedha hizo, shilingi trilioni 8.73 ni kwa ajili ya matumizi ya kawaida na shilingi trilioni 3.76 ni kwa ajili ya matumizi ya maendeleo. Fedha hizo ni kwa ajili ya Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake kwa mwaka 2026/2027.

Vilevile, Waziri Mkuu ameliomba Bunge liidhinishe jumla ya shilingi 225,021,780,000 kwa ajili ya Mfuko wa Bunge. Kati ya fedha hizo, shilingi 207,992,798,000 ni kwa ajili ya matumizi ya kawaida na shilingi 17,028,982,000 ni kwa ajili ya matumizi ya maendeleo.

Wednesday, April 01, 2026

WATENGENEZA MAUDHUI MTANDAONI WATAKIWA KUTENGENEZA MAUDHUI YANAYOLINDA TASWIRA YA NCHI

 

Mkuu wa Wilaya ya Nyamagana iliyopo mkoani Mwanza, Mhe. Amina Makilagi {pichani juu] amewataka Watengeneza Maudhui Mtandaoni kuzingatia maadili, uzalendo pamoja na kulinda taswira ya Tanzania kwenye maudhui wanayoyatengeneza.

Mhe. Amina ametoa rai hiyo Aprili 1, 2026 mkoani hapo wakati akizungumza kwenye Mafunzo kwa Watengenza Maudhui Mtandaoni (Content Creators) awamu ya kwanza yaliyoandaliwa na Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo. 

“Msisitizo kwenu watengeneza maudhui, mafunzo mliyoyapata hapa yasiishie hapa bali yatumieni katika kuboresha kazi zenu ili muweze kuongeza kipato cha familia na Taifa kwa ujumla” alisistiza Mhe. Amina.

Aidha, amewataka washiriki hao kuongeza ujuzi kupitia njia mbalimbali ili kuendana na mabadiliko ya teknolojia.

Kwa upande wake Afisa Mtendaji Mkuu wa Mfuko wa Utamaduni na Sanaa Tanzania, CPA (T) Nyakaho Mahemba amesema kuwa, lengo la mafunzo hayo ni kuwasaidia wazalisha maudhui mtandaoni kupata elimu ya mkopo, uandishi wa mradi pamoja na namna ya kuzalisha kazi bora zaidi zitakazokidhi soko la ndani na nje pamoja na kuweza kuweka ushindani.

Naye Bw. Andrew Ngonyani (Brother K) aliyeshiriki mafunzo hayo aliishukuru Serikali kwa kutoa mafunzo hayo ambayo yamewasaidia vijana wengi kuweza kutumia maudhui yao kupata pesa, akiishauri Serikali kuendelea kuweka mazingira bora kwa wasanii kufanya sanaa na kunufaika nayo.

Mafunzo hayo yamekuwa na mada mbalimbali ikiwemo Elimu ya Mtaji, Kubiasharisha Maudhui Mtandaoni, Uaminifu uwajibikaji kwa wafuasi wako pamoja na hatua kwa hatua namna ya kutengeneza akaunti ya biashara na kuingiza kipato.










NCHIMBI AKISALIMIANA NA BABA MTAKATIFU BAADA YA IBADA YA HIJA VATICAN

 
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi, akisalimiana na Kiongozi Mkuu wa Kanisa Katoliki Duniani, Baba Mtakatifu Leo XIV, mara baada ya Ibada ya Hija iliyofanyika katika Uwanja wa Kanisa Kuu la Mtakatifu Petro – Vatican, leo tarehe 01 April 2026.




Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi akifurahi jambo na Kiongozi Mkuu wa Kanisa Katoliki Duniani, Baba Mtakatifu Leo XIV, wakati wakiagana mara baada ya Ibada ya Hija iliyofanyika katika Uwanja wa Kanisa Kuu la Mtakatifu Petro – Vatican leo tarehe 01 Aprili 2026.

TANZANIA NA URUSI ZAIMARISHA USHIRIKIANO WA KIMKAKATI KATIKA SEKTA YA UCHUKUZI

Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Shirikisho la Urusi zimeingia hatua mpya ya ushirikiano wa maendeleo baada ya kus...