Thursday, May 28, 2026

SEKTA YA NYUMBA YAPATA MSUKUMO MPYA, NHC YATEKELEZA MIRADI YA MABILIONI NCHINI

Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Mhe. Dkt. Leonard Akwilapo akiwasilisha  Bungeni Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara kwa mwaka 2026/27
Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Nyumba la Taifa, Hamad Abdallah akisalimiana na Katibu Mkuu wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Injinia Anthony Sanga Bungeni Dodoma.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Injinia Anthony Sanga Bungeni Dodoma. akisalimiana na Mweyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Shirika la Nyumba la Taifa, Dk. Sophia Kongela
Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Nyumba la Taifa, Hamad Abdallah akiwa katika gallery ya Spika kufuatilia hotuba ya Bunge.

Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Nyumba la Taifa, Hamad Abdallah akiwa katika gallery ya Spika kufuatilia hotuba ya Bunge.

Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Nyumba la Taifa, Hamad Abdallah akijadiliana jambo na Bw. Deodatus Philip Mwanyika, Mbunge wa Jimbo la Njombe Mjini (CCM) na mmoja wa Wenyeviti wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Injinia Anthony Sanga Bungeni Dodoma. akisalimiana na Waziri wa Mstaafu  wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Dk. Angelina Lubala Mabula

DODOMA — Serikali kupitia Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi imeendelea kuonesha dhamira ya kuimarisha sekta ya makazi na biashara nchini kupitia utekelezaji wa miradi mikubwa ya Shirika la Nyumba la Taifa (NHC), huku miradi kadhaa ya kimkakati ikitarajiwa kukamilika ndani ya mwaka 2026 na mingine kuanza rasmi mwaka wa fedha 2026/27.

Akiwasilisha Bungeni Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara kwa mwaka 2026/27, Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Mhe. Dkt. Leonard Akwilapo amesema Serikali kupitia NHC imeendelea kusimamia utekelezaji wa miradi ya nyumba, biashara na uwekezaji inayolenga kuongeza upatikanaji wa makazi bora pamoja na kuchochea ukuaji wa uchumi wa miji mbalimbali nchini.

Katika hotuba hiyo, Mhe. Dkt. Akwilapo amesema ujenzi wa nyumba 422 katika mradi wa Kawe 711 jijini Dar es Salaam wenye thamani ya shilingi bilioni 169 umefikia asilimia 85 ya utekelezaji na unatarajiwa kukamilika ifikapo Juni 30, 2026. Aidha, mradi wa nyumba 196 wa Golden Premier Residence (GPR) wenye thamani ya shilingi bilioni 127 umefikia asilimia 50 huku ukitarajiwa kukamilika mwaka 2027.

Waziri huyo amesema Serikali pia inaendelea na maandalizi ya utekelezaji wa miradi mipya ya makazi kupitia mpango wa nyumba 5,000 wa Samia Housing Scheme katika maeneo ya Mtoni Kijichi na Kawe jijini Dar es Salaam pamoja na Medeli na Iyumbu jijini Dodoma.

“Katika mwaka 2026/27, Shirika litaendelea na ujenzi wa nyumba katika miradi ya Samia Housing Scheme sambamba na kuanza utekelezaji wa miradi mipya katika maeneo ya Njedengwa Dodoma, Urafiki Dar es Salaam, Makongoro Mwanza na Sokoine Complex Arusha,” amesema Mhe. Dkt. Akwilapo.

Kwa upande wa nyumba za gharama nafuu, Waziri Akwilapo amesema NHC limekamilisha maandalizi ya awamu ya kwanza ya ujenzi wa nyumba 800 katika maeneo ya Salama Creek Kigamboni, Sabasaba Morogoro, Iyumbu Dodoma na Buswelu Mwanza, ambapo utekelezaji rasmi utaanza mwaka 2026/27.

Mbali na sekta ya makazi, Waziri huyo amesema NHC linaendelea na utekelezaji wa miradi mbalimbali ya majengo ya biashara nchini, hatua inayochochea shughuli za kiuchumi pamoja na kuongeza thamani ya maeneo ya mijini.

Miradi hiyo ni pamoja na Meru View Shops Arusha iliyofikia asilimia 52, Tabora Commercial Complex asilimia 46, Singida 2F Plaza asilimia 85, Mkwakwani Commercial Complex Tanga asilimia 40, Kashozi Commercial Complex Kagera asilimia 65, Uluguru Plaza Morogoro asilimia 42 na Iringa Commercial Complex asilimia 40.

Aidha, Serikali imeeleza kuwa miradi ya biashara na ofisi katika maeneo ya Masasi, Mtanda Lindi na Zongomela Kahama imekamilika huku maandalizi ya mwisho ya miradi ya Usa River na Ngarenaro yakiendelea.

Katika eneo la ubia, Mhe. Dkt. Akwilapo amesema NHC linaendelea kusimamia miradi 21 ya ubia yenye thamani ya shilingi bilioni 351 ambapo miradi mitatu imekamilika na mingine ipo katika hatua mbalimbali za utekelezaji kwa wastani wa asilimia 56.

Amesema pia Shirika linaendelea kutwaa na kufufua miradi iliyokuwa imesimama kwa muda mrefu ili kuhakikisha uwekezaji huo unaleta tija kwa wananchi na Taifa kwa ujumla. Kati ya miradi 24 iliyokuwa imesimama, miradi 13 imekamilika huku mingine ikiendelea kushughulikiwa.

Katika hatua nyingine, Waziri huyo amesema NHC limeendelea kuimarisha utendaji wake wa kifedha ambapo hadi Mei 15, 2026 limefanikiwa kupunguza madeni kutoka shilingi bilioni 27.98 mwaka 2024/25 hadi shilingi bilioni 19 mwaka 2025/26.

Pia, Shirika limeendelea na mpango wa ukarabati wa nyumba zake ambapo nyumba 1,283 kati ya nyumba 1,600 zilizopangwa kukarabatiwa tayari zimekamilika sawa na asilimia 80 ya lengo.

Kwa upande wa miradi ya ukandarasi na ushauri elekezi, Waziri Akwilapo amesema NHC limekamilisha ujenzi wa majengo nane ya Ofisi za Serikali katika Mji wa Serikali Mtumba Dodoma pamoja na jengo la Soko la Madini la Tanzanite Mirerani Manyara.

Kadhalika, ujenzi wa majengo ya TCRA Dodoma umefikia asilimia 73 huku mradi wa Zanzibar ukiwa umefikia asilimia 50.

Hotuba hiyo imeendelea kuonesha nafasi ya NHC kama chombo muhimu cha Serikali katika utekelezaji wa miradi ya kimkakati ya makazi, biashara na huduma za ushauri elekezi nchini, huku Serikali ikiendelea kuweka mazingira bora ya uwekezaji na upatikanaji wa nyumba kwa Watanzania wa makundi mbalimbali.

Friday, May 22, 2026

MAKAMU WA PILI WA RAIS ZANZIBAR AMTEMBELEA MHE. FARIDA AMOUR MOH'D HOSPITALINI, AMTAKIA AFYA NJEMA






Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Mhe. Hemed Suleiman Abdulla, leo tarehe 21 Mei 2026 amemtembelea na kumjulia hali Mwakilishi wa Viti Maalum kupitia Chama cha ACT Wazalendo, Mhe. Farida Amour Moh’d, ambaye amelazwa katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Mjini Magharibi Lumumba kwa ajili ya matibabu.

Katika ziara hiyo, Mhe. Hemed alipata fursa ya kuzungumza na Mhe. Farida pamoja na madaktari wanaomuhudumia, ambapo alielezwa maendeleo ya afya yake na hatua zinazoendelea kuchukuliwa katika kumpatia huduma stahiki za matibabu.

Makamu wa Pili wa Rais alimtakia Mhe. Farida nafuu ya haraka na kurejea katika majukumu yake ya kuwahudumia wananchi, huku akisisitiza umuhimu wa kuendelea kumpatia huduma bora za afya hadi atakapopona kikamilifu.

Ziara hiyo imeonesha mshikamano, upendo na utamaduni wa viongozi kujali ustawi wa wenzao wakati wa changamoto za kiafya.

Imetolewa na Kitengo cha Habari (OMPR)
Tarehe 21 Mei 2026.

Thursday, May 21, 2026

Tanzania kudhibiti ujenzi holela pembezoni mwa miji kuepuka gharama za miundombinu










Na Mwandishi Wetu

WAKATI mataifa mengi ya Afrika yaliyo Kusini mwa Jangwa la Sahara yakishuhudia kasi kubwa ya ukuaji wa miji, Tanzania imechukua msimamo thabiti wa kudhibiti uendelezaji holela wa makazi pembezoni mwa miji ili kuepuka gharama kubwa za kurekebisha miundombinu baadaye.

Akizungumza katika Jukwaa la 13 la Miji Duniani (WUF13) jijini Cairo, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Prof. Riziki Shemdoe, ameeleza kuwa Tanzania imeweka mkakati madhubuti wa kitaifa wa kusuka upya mustakabali wa miji kabla ya ujenzi holela kushamiri.

Prof. Shemdoe amesema kuwa serikali imeamua kuelekeza nguvu zake katika maeneo ya pembezoni mwa miji, akibainisha kuwa Dar es Salaam, Dodoma, Mwanza, Mbeya na Arusha zinapanuka kwa kasi ya mlalo. 

Ameonya kuwa ukuaji wa miji bila mpango wa mapema unasababisha makazi yasiyo rasmi, ukosefu wa ajira na changamoto za huduma muhimu kama maji safi, umeme na usafi wa mazingira.

“Ukuaji wa miji unapotokea bila mipango ya mapema unatengeneza makazi yaliyotawanyika na ukosefu wa ajira. Kuweka miundombinu katika maeneo haya baada ya kuwa tayari yamejengwa ni gharama kubwa zaidi kuliko kuyapanga mapema kabla hayajajengwa,” amesema Prof. Shemdoe.

Serikali imezindua miongozo mipya ya mipango ya miji na udhibiti wa uendelezaji, pamoja na miongozo ya kuhifadhi mazingira ya kijani. 

Kupitia mifumo ya kidijitali na taarifa za kijiografia (GIS), serikali inarasimisha makazi ya pembezoni na kugawa viwanja vilivyopimwa ili kuhakikisha matumizi bora ya ardhi.

Prof. Shemdoe ametaja Programu ya Tanzania ya Kupandisha Kiwango cha Miundombinu na Ushindani wa Miji (TACTIC) inayotekelezwa katika miji 45, ikilenga barabara, masoko na udhibiti wa mafuriko. 

Aidha, ameeleza kuwa Mradi wa Maendeleo ya Jiji la Dar es Salaam (DMDP) Awamu ya Kwanza na ya Pili unalenga kuongeza miundombinu inayohimili mabadiliko ya tabianchi.

Serikali pia inawekeza katika miji ya kati na pembezoni kwa kujenga masoko ya kisasa 28, vituo vya usindikaji wa mazao ya kilimo na kuanzisha Ukanda wa Kiuchumi wa Kwala.

Hatua hizi zinahakikisha fursa za ajira zinapatikana karibu na wananchi na kupunguza shinikizo la ukuaji holela katika Dar es Salaam.

Prof. Shemdoe amesisitiza kuwa ujenzi wa masoko makubwa zaidi ya 15 na uboreshaji wa sekta isio rasmi, hususan kwa vijana na wafanyabiashara wadogo ni sehemu ya ajenda kuu ya kitaifa ya kupunguza tatizo la ajira na kuimarisha uchumi wa miji.

Kwa mkakati huu, Tanzania inalenga kujenga miji yenye usawa, yenye miundombinu imara na inayoweza kukabiliana na changamoto za tabianchi, huku ikiepuka gharama kubwa za kurekebisha makosa ya uendelezaji holela.

Wednesday, May 13, 2026

KASI YA UJENZI WA RELI YA SGR IMEONGEZEKA – PROF. MBARAWA

 

Wahudumu wa ndani (Train crew) wa shirika la reli Tanzania (TRC) upande wa Standard Gauge Railway (SGR) wamehudhuria Bungeni Jijini Dodoma kwa mwaliko maalum wa Waziri wa Uchukuzi Mhe. Prof. Makame Mnyaa Mbarawa ili kuweza kushuhudia uwasilishwaji wa hotuba ya bajeti ya Uchukuzi ya makadirio ya mapato na matumizi kwa mwaka wa fedha 2026/2027.









Waziri wa Uchukuzi, Makame Mbarawa amesema Serikali kupitia Shirika la Reli Tanzania inaendelea kuandika historia mpya katika sekta ya usafiri wa reli nchini kupitia utekelezaji wa mradi mkubwa wa reli ya kisasa ya Standard Gauge Railway (SGR), ambao umeendelea kuonesha mafanikio makubwa katika vipande mbalimbali vya ujenzi.

Akiwasilisha makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara ya Uchukuzi kwa mwaka wa fedha 2026/2027 bungeni jijini Dodoma leo Jumatano Mei 13, 2026, Profesa Mbarawa amesema Serikali imeongeza kasi ya utekelezaji wa mradi huo wa kimkakati ambao unatajwa kuwa miongoni mwa miradi mikubwa zaidi ya miundombinu barani Afrika.

Amesema hadi kufikia mwezi Machi mwaka huu, vipande vya kwanza vya reli kutoka Dar es Salaam hadi Morogoro pamoja na kutoka Morogoro hadi Makutupora vimekamilika kwa kiwango kikubwa na tayari huduma za usafiri zimeanza kutolewa kwa wananchi kupitia vipande hivyo.

Hatua hiyo imeendelea kutoa matumaini makubwa kwa wananchi na wadau wa maendeleo kutokana na mchango wa reli hiyo katika kurahisisha usafirishaji wa abiria na mizigo, kupunguza gharama za usafiri pamoja na kuchochea ukuaji wa uchumi wa Taifa.

Kwa upande wa kipande cha Mwanza hadi Isaka, Profesa Mbarawa amesema ujenzi umefikia asilimia 68.77 huku kazi zikiendelea vizuri na kwa kasi kubwa ili kuhakikisha mradi huo unakamilika kwa wakati.

Aidha, amesema Serikali inaendelea na utekelezaji wa kipande cha tatu kutoka Makutupora hadi Tabora pamoja na kipande cha nne kutoka Tabora hadi Isaka, ambapo shughuli mbalimbali za ujenzi zinaendelea katika maeneo hayo.

Profesa Mbarawa amesema pamoja na changamoto zilizojitokeza katika baadhi ya vipande vya mradi huo na kusababisha kuchelewa kwa utekelezaji katika hatua za awali, Serikali imefanikiwa kupata suluhisho la kudumu baada ya kupata mkopo wa masharti nafuu wenye thamani ya dola za Marekani bilioni 1.277, sawa na takribani Shilingi trilioni 3.32.

Amesema hatua hiyo inaonesha dhamira thabiti ya Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Samia Suluhu Hassan katika kuimarisha miundombinu ya reli nchini kwa lengo la kuongeza ufanisi wa usafiri, kukuza biashara na kuharakisha maendeleo ya uchumi wa Taifa.

Katika tukio hilo, wahudumu wa ndani wa treni (Train Crew) wa Shirika la Reli Tanzania upande wa SGR walihudhuria kikao hicho cha Bunge kwa mwaliko maalum wa Waziri wa Uchukuzi ili kushuhudia uwasilishwaji wa hotuba ya bajeti ya Wizara ya Uchukuzi kwa mwaka wa fedha 2026/2027, jambo lililoonesha heshima na kutambua mchango wao katika mafanikio ya sekta ya reli nchini.

Mradi wa SGR unaendelea kuwa alama ya mapinduzi makubwa ya miundombinu nchini Tanzania, huku ukitajwa kuwa chachu muhimu ya maendeleo ya uchumi, biashara na usafiri wa kisasa kwa kizazi cha sasa na kijacho.

Monday, May 11, 2026

WIZARA YA AFYA YAOMBA SH. TRILIONI 1.8 BAJETI YA 2026/2027

 


Wizara ya Afya imeomba kuidhinishiwa jumla ya Shilingi trilioni 1.8 kwa mwaka wa fedha 2026/2027 kwa ajili ya kuendelea kuboresha huduma za afya nchini, kuimarisha hospitali na taasisi zake pamoja na kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo katika sekta hiyo.

Akiwasilisha bungeni jijini Dodoma hotuba ya makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara ya Afya kwa mwaka wa fedha 2026/2027, Waziri wa Afya, Mohamed Omary Mchengerwa amesema wizara hiyo inaomba kuidhinishiwa jumla ya Shilingi 1,800,262,058,000.00.

Waziri Mchengerwa amesema kati ya fedha hizo, Shilingi 652,236,871,000.00 sawa na asilimia 36 ya bajeti yote zimetengwa kwa matumizi ya kawaida, huku Shilingi 1,148,025,187,000.00 sawa na asilimia 64 zikielekezwa kwenye utekelezaji wa miradi ya maendeleo.

Ameeleza kuwa katika fedha za matumizi ya kawaida, kiasi cha Shilingi 516,323,356,000.00 kimetengwa kwa ajili ya mishahara ya watumishi wa Wizara, hospitali pamoja na taasisi zilizo chini yake, huku Shilingi 135,913,515,000.00 zikitengewa matumizi mengineyo.

Kwa upande wa fedha za maendeleo, Waziri huyo amesema Shilingi 789,458,609,000.00 ni fedha za ndani, wakati Shilingi 358,566,578,000.00 ni fedha kutoka vyanzo vya nje kwa ajili ya kuendeleza miradi mbalimbali ya afya nchini.

Aidha, Wizara ya Afya imekadiria kukusanya maduhuli ya Shilingi 747,200,091,299.81 katika mwaka wa fedha 2026/2027 kupitia Wizara, taasisi pamoja na hospitali zake.

Kwa mujibu wa Waziri Mchengerwa, kati ya fedha hizo, Shilingi 76,195,850,735.53 zinatarajiwa kukusanywa kutoka vyanzo vya ndani vya Makao Makuu ya Wizara, Shilingi 165,804,149,264.47 kutoka Hospitali za Rufaa za Mikoa, huku zaidi ya Shilingi bilioni 505 zikitarajiwa kukusanywa kutoka taasisi, Hospitali ya Taifa, hospitali maalum pamoja na hospitali za kanda.

Waziri huyo amesema fedha zinazoombwa zitawezesha Wizara ya Afya kuendelea kuboresha huduma za afya nchini, kuimarisha miundombinu ya matibabu, kuongeza upatikanaji wa vifaa tiba pamoja na kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma kwa wananchi.

SERIKALI YATOA BILIONI 48.8 BIMA YA AFYA KWA WOTE

 


Na Mwandishi Wetu , Dodoma

Serikali imeanza rasmi utekelezaji wa Mpango wa Bima ya Afya kwa Wote kwa kaya zisizo na uwezo kwa kutoa Shilingi bilioni 48.8 kwa ajili ya kuwawezesha wananchi wa makundi maalum kupata huduma za afya kwa uhakika.

Kupitia utekelezaji huo, jumla ya kaya 172,297 tayari zimefikiwa na kuingizwa kwenye mpango huo, huku wanufaika 463,228 wakianza kupata huduma mbalimbali za matibabu katika vituo vilivyosajiliwa nchini.

Akiwasilisha Hotuba ya Bajeti ya Wizara ya Afya Fungu 52 kwa mwaka 2026/27 Waziri wa Afya Mhe. Omary Mchengerwa amesema kuwa, utekelezaji huu unaonesha dhamira ya Serikali ya kuhakikisha kila Mtanzania anapata huduma bora za afya bila kujali hali yake ya kiuchumi, ikiwa ni sehemu ya safari ya kuelekea huduma jumuishi za afya kwa wananchi wote.

Katika kuimarisha sekta ya afya sambamba na utekelezaji wa mpango huo, mabaraza na bodi za kitaaluma yameendelea kusimamia ubora wa huduma kwa kusajili wataalam wa afya 14,310, hatua inayoongeza nguvu kazi muhimu kwa utoaji wa huduma nchini.

Amesema kuwa kuhusu upatikanaji wa huduma za matibabu, jumla ya maduka ya dawa 330 yamesajiliwa pamoja na watarajali 3,004, huku vituo vya kutolea huduma za afya 3,643 vikisajiliwa ili kuongeza upatikanaji wa huduma karibu na wananchi.

Katika kuhakikisha taaluma na maadili yanaendelea kuzingatiwa hususan wakati huu wa kuhudumia wananchi wengi zaidi kupitia mfumo wa Bima ya Afya, vituo binafsi vya afya 654 vimekaguliwa ili kuhakikisha vinakidhi viwango na kutoa huduma salama kwa wananchi.

Mafanikio hayo yanaakisi hatua kubwa ya Serikali katika kujenga mfumo imara wa afya unaojali usawa, ubora na upatikanaji wa huduma kwa wote, huku Bima ya Afya kwa Wote ikiendelea kuwa nguzo muhimu ya maendeleo ya kijamii na kiuchumi. 

WAZIRI KOMBO ASHIRIKI MKUTANO WA DHARURA WA KAMATI YA MAWAZIRI SADC

 

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo (Mb.), ameshiriki Mkutano wa Dharura wa Kamati ya Mawaziri wa Asasi ya Siasa, Ulinzi, na Usalama ya Jumuiya ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika (SADC-MCO), uliofanyika tarehe 10 Mei, 2026, Jijini Nairobi, Kenya.

Mkutano huo uliolenga kuimarisha misingi ya amani, umeongozwa na Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mhe. Dkt. George Chaponda, ambaye ni Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa wa Jamhuri ya Malawi.

Katika mazungumzo hayo, Mawaziri wamejadili changamoto mbalimbali za kiusalama zinazoikabili kanda hiyo ikiwemo Vurugu zinazoendelea nchini Afrika Kusini dhidi ya raia wa nchi nyingine za Afrika.

Kwa Upande wake Mwenyekiti Dkt. Chaponda amewahakikishia wajumbe wa mkutano huo kuwa mapendekezo yote yaliyofikiwa yatafanyiwa kazi kwa haraka na kwa ufanisi.

Hatua hii ni sehemu ya mikakati ya SADC kuhakikisha kuwa Kanda ya Kusini mwa Afrika inasalia kuwa kisiwa cha amani, utulivu, na ushirikiano wa kiuchumi.






SEKTA YA NYUMBA YAPATA MSUKUMO MPYA, NHC YATEKELEZA MIRADI YA MABILIONI NCHINI

Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Mhe. Dkt. Leonard Akwilapo a kiwasilisha  Bungeni Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ...