Mkurugenzi
Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge
akimkabidhi zawadi Mwenyekiti mpya wa Bodi ya Wadhamini ya Taasisi hiyo
Dkt. Hassan Mahmoud Mshinda alipotembelea JKCI kwa mara ya kwanza leo
kwaajili ya kuona utendaji kazi pamoja na kukutana na viongozi.Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge akimweleza utendaji kazi wa taasisi hiyo Mwenyekiti mpya wa Bodi ya Wadhamini ya JKCI Dkt. Hassan Mahmoud Mshinda alipotembelea taasisi hiyo kwa mara ya kwanza leo kwaajili ya kuona utendaji kazi pamoja na kukutana na viongozi. Uongozi wa Taasisi ya
Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) umepongezwa kwa maono ya mbali na uthubutu
mkubwa katika kuanzisha na kuendeleza upasuaji wa moyo wa aina mbalimbali,
hatua iliyoiwezesha Tanzania kuwa kitovu cha huduma za kibingwa na bobezi za
matibabu ya moyo katika Ukanda wa Afrika Mashariki na Kati.
Pongezi hizo zimetolewa na Mwenyekiti mpya wa Bodi ya Wadhamini ya
taasisi hiyo, Dkt. Hassan Mahmoud Mshinda wakati wa ziara yake ya kwanza JKCI kwaajili
ya kuona utendaji kazi pamoja na kukutana na viongozi wa taasisi hiyo.
Dkt. Mshinda alisema ameridhishwa na kasi ya maendeleo, ubunifu na
uthubutu uliofanywa na taasisi hiyo katika kuboresha huduma za moyo nchini.
“Nimejionea
kwa macho yangu ubora wa huduma na mipango mikubwa ya maendeleo inayoendelea
kutekelezwa. Si rahisi kwa taasisi nyingi kuwa na ujasiri wa kujaribu na kuwekeza
katika teknolojia za kisasa kama ilivyofanywa hapa, haya ni mafanikio
yanayostahili pongezi,” alisema Dkt. Mshinda.
Alisisitiza
kuwa Bodi ya Wadhamini itatoa ushirikiano wa karibu kwa uongozi wa taasisi hiyo
ili kuhakikisha malengo ya kuimarisha huduma za moyo yanatimia kwa ufanisi na
kwa manufaa ya Watanzania wote.
Akigusia
uzoefu wake binafsi, Dkt. Mshinda alisema aliwahi kupatiwa matibabu katika
taasisi hiyo na kushuhudia viwango vya juu vya huduma vinavyolingana na vya
mataifa yaliyoendelea.
“Nimewahi
kutibiwa hapa. Naweza kusema bila kusita kuwa huduma za hapa na za Switzerland
hazina tofauti kubwa. Hata wenzetu wa huko walishangaa kusikia kuwa Tanzania
ina taasisi ya kiwango hiki”, aliongeza.
Kwa
upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa JKCI, Dkt. Peter Kisenge alisema tangu
kuanzishwa kwa taasisi hiyo imechangia kwa kiasi kikubwa kupunguza rufaa za
wagonjwa wa moyo waliokuwa wakipelekwa nje ya nchi kwa matibabu maalum jambo
lililookoa fedha nyingi za Serikali na kupunguza adha kwa wagonjwa na familia
zao.
Alifafanua
kuwa taasisi hiyo imepanua wigo wa huduma kwa kuanzisha matawi sita katika
maeneo mbalimbali ya nchi, hatua iliyosaidia kupunguza msongamano wa wagonjwa
katika makao makuu na kuongeza ufanisi wa utoaji huduma.
“Mbali
na huduma za ana kwa ana, tumeanza pia kutoa huduma kwa njia ya mtandao hususan
kwa wagonjwa wa shinikizo la damu ili kurahisisha ufuatiliaji wa matibabu na
kupunguza gharama na muda wa safari”, alisema Dkt. Kisenge.
Alibainisha
kuwa JKCI ni miongoni mwa taasisi chache barani Afrika zenye uwezo wa kufanya
upasuaji wa moyo kwa kutumia teknolojia ya kisasa ya tundu dogo, pamoja na
kumiliki mtambo wa Carto 3 kwaajili ya matibabu ya umeme wa moyo ambao ni wa
kipekee katika Ukanda wa Afrika Mashariki na Kati.
Dkt.
Kisenge alimshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan,kwa kuendelea kuiunga mkono
taasisi hiyo na kwa kumteua Dkt. Mshinda kuiongoza Bodi ya Wadhamini huku
akieleza akieleza kuwa uzoefu wake katika utafiti utaongeza nguvu katika eneo
la tafiti za magonjwa ya moyo.
Katika
ziara hiyo Mwenyekiti huyo wa Bodi ya
Wadhamini ya JKCI alitembelea pia JKCI Hospitali ya Dar Group ambapo Mkurugenzi wa Hospitali
hiyo Dkt. Tulizo Shemu, alisema tangu hospitali hiyo ilipokabidhiwa kwa
JKCI mwishoni mwa mwaka 2022 imefanya maboresho makubwa ya miundombinu na utoaji
wa huduma.
Dkt.
Shemu alieleza kuwa idadi ya wagonjwa wa nje imeongezeka kutoka wastani wa 200
hadi kufikia 650 pia wamefanya ujenzi wa chumba cha kisasa cha upasuaji, wameboresho
eneo la OPD, ujenzi wa jengo la VIP, pamoja na ongezeko la vifaa tiba na uwepo
wa wataalamu mabingwa wa magonjwa mbalimbali.
Dkt. Shemu alisema Hospitali ya Dar
Group inatoa huduma za matibabu ya magonjwa mbalimbali ikiwemo matibabu za
moyo, huduma za upasuaji, matibabu ya magonjwa ya wanawake na watoto, matibabu
ya afya ya kinywa na meno, matibabu ya macho, huduma za mazoezi tiba, matibabu
ya mifupa, pamoja na huduma za dharura.
“Hospitali ya Dar Group ilianzishwa na Hayati Mwalimu Julius
Kambarage Nyerere kupitia azimio maalumu la mwaka 1981 na kusajiliwa na Wakala
wa usajili wa Biashara na Leseni (BRELA) mwaka 1997 chini ya sheria ya
makampuni ya mwaka 1967 ikihusishwa na dhamana isiyo mtaji”, alisema Dkt. Shemu.