Wednesday, June 03, 2026

KUSANYENI KODI NA MADENI BILA KUOGOPA MTU YEYOTE– WAZIRI AKWILAPO ASEMA AKIZINDUA BODI MPYA YA NHC

 

Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Dk. Leonard Akwilapo, akimkabidhi Mwenyekiti wa Bodi wa Shirika la Nyumba la Taifa (NHC), Dk. Sophia Kongela nyenzo za kazi wakati akizindua rasmi Bodi mpya ya Wakurugenzi ya Shirika la Nyumba la Taifa (NHC). Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Nyumba la Taifa, Hamad Abdallah anashuhudia. 

Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Dk. Leonard Akwilapo, akizungumza na Bodi Mpya wakati akizindua rasmi Bodi mpya ya Wakurugenzi ya Shirika la Nyumba la Taifa (NHC). 
Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Dk. Leonard Akwilapo, akimkabidhi Mjumbe wa Bodi, Eliud Betri Sanga nyenzo za kazi wakati akizindua rasmi Bodi mpya ya Wakurugenzi ya Shirika la Nyumba la Taifa (NHC).
Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Dk. Leonard Akwilapo, akimkabidhi Mjumbe wa Bodi Ali Laay nyenzo za kazi wakati akizindua rasmi Bodi mpya ya Wakurugenzi ya Shirika la Nyumba la Taifa (NHC).

Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Nyumba la Taifa, Hamad Abdallah akizungumza kumkaribisha Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Dk. Leonard Akwilapo, huku Mwenyekiti wa Bodi wa Shirika la Nyumba la Taifa (NHC), Dk. Sophia Kongela akishuhudia.

Na Mwandishi Wetu, Arusha

Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Dk. Leonard Akwilapo, amezindua rasmi Bodi mpya ya Wakurugenzi ya Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) na kuitaka kuimarisha usimamizi wa rasilimali za Shirika, kuongeza kasi ya ukusanyaji wa madeni pamoja na kusimamia utekelezaji wa miradi ya makazi nafuu ili kukidhi mahitaji ya Watanzania.

Akizungumza katika hafla ya uzinduzi iliyofanyika jijini Arusha, Dk. Akwilapo alisema NHC ni taasisi muhimu katika utekelezaji wa maono ya Serikali ya Awamu ya Sita ya kuhakikisha wananchi wanapata makazi bora, salama na yanayomudu gharama za maisha ya wananchi wa kipato cha kati na cha chini.

Waziri huyo alisisitiza kuwa pamoja na mafanikio makubwa ambayo Shirika limeendelea kuyapata katika uwekezaji na usimamizi wa miradi, bado kuna umuhimu wa kuimarisha nidhamu ya kifedha hususan katika ukusanyaji wa mapato na madeni yanayodaiwa na Shirika.

"Hakuna mdaiwa anayepaswa kuogopwa. Madeni yote halali yanapaswa kufuatiliwa na kulipwa kwa mujibu wa sheria na taratibu zilizowekwa. Uimara wa Shirika unategemea uwezo wake wa kusimamia rasilimali zake na kukusanya mapato yake kwa wakati," alisema Dk. Akwilapo.

Aliwaagiza NHC kutoogopa kudai malipo yao ambayo ni halali kwa shirika. "Msimuogope yeyote, hata akawa na cheo gani daini fedha za serikali na mimi nipo tayari kuwasaidia ili Shirika liendelee kutoa huduma bora."

Alibainisha kuwa Serikali ina matarajio makubwa kwa Bodi hiyo mpya katika kusimamia maandalizi na utekelezaji wa Mpango Mkakati mpya wa Shirika, ambao unapaswa kuendana na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, Mpango wa Taifa wa Maendeleo pamoja na ajenda ya makazi endelevu duniani.

Dk. Akwilapo pia aliitaka Bodi kuendelea kuhimiza matumizi ya teknolojia za kisasa za ujenzi, kuimarisha ubunifu katika upatikanaji wa mitaji ya miradi na kusimamia uwekezaji wa Shirika kwa tija zaidi ili kuongeza mchango wake katika uchumi wa Taifa.

Bodi hiyo mpya ya Wakurugenzi ya NHC inaongozwa na Dk. Sophia Kongela kama Mwenyekiti, huku wajumbe wake wakiwa ni Eliud Sanga, Profesa Wilbard Kombe, Dk. Ali Hussein Laay, Doroth Mwanyika, Ayoub Omari Kasuwi, Vupe Ligate na Elias Kisamo.

Akizungumza kwa niaba ya Bodi hiyo, Dk. Sophia Kongela alisema wajumbe wamepokea kwa heshima na uzito mkubwa dhamana waliyopewa na Serikali ya kuiongoza NHC katika kipindi hiki muhimu cha maendeleo ya sekta ya makazi nchini.

Alimshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, kwa kuendelea kuwaamini na kuwapa jukumu la kusimamia taasisi hiyo, akiahidi kuwa Bodi itafanya kazi kwa weledi, uwazi na uwajibikaji ili kuhakikisha NHC inafikia malengo yake.

"Tutatoa ushirikiano wa karibu kwa Serikali na Menejimenti ya Shirika ili kuhakikisha miradi yote ya maendeleo inatekelezwa kwa ufanisi, mapato yanaongezeka na NHC inaendelea kuwa taasisi ya mfano katika sekta ya makazi," alisema Dk. Kongela.

Awali, Mkurugenzi Mkuu wa NHC, Hamad Abdallah, alisema Shirika limeendelea kuimarisha nafasi yake kama taasisi ya kimkakati katika maendeleo ya makazi kupitia utekelezaji wa miradi mikubwa ya makazi, biashara na uwekezaji katika maeneo mbalimbali nchini.

Alieleza kuwa NHC imeendelea kuongeza thamani ya mali zake, kuimarisha mifumo ya kidijitali na kusimamia kwa ufanisi rasilimali zake za ardhi, nyumba na majengo ya biashara, hatua ambazo zimechangia kuongezeka kwa mapato na kuimarika kwa utendaji wa Shirika.

Hamad alisema Menejimenti iko tayari kushirikiana na Bodi mpya katika kutekeleza maelekezo ya Serikali na kuhakikisha NHC inaendelea kuwa chombo muhimu katika kutatua changamoto ya makazi nchini.

Katika hotuba yake, Dk. Akwilapo aliipongeza NHC kwa kuendelea kufanya vizuri kibiashara na kiutendaji katika kipindi ambacho baadhi ya mashirika mengi ya umma yaliyowahi kuwa nguzo za uchumi wa Taifa yalishindwa kuhimili ushindani na kutoweka.

Alisema mafanikio ya NHC yanaonesha kuwa taasisi za umma zinaweza kufanya vizuri ikiwa zitasimamiwa kwa nidhamu, uwajibikaji na maamuzi sahihi ya kiutawala na kibiashara.

Uzinduzi wa Bodi hiyo mpya unafungua ukurasa mpya wa utekelezaji wa majukumu ya Shirika la Nyumba la Taifa, huku matarajio makubwa yakiwekwa katika kuongeza upatikanaji wa makazi bora, kuimarisha uwekezaji wa kimkakati na kuchangia maendeleo endelevu ya miji na uchumi wa Tanzania.

Tuesday, June 02, 2026

RAIS SAMIA AANZA ZIARA YA KIHISTORIA URUSI, KUITANGAZA TANZANIA YA DIRA YA MAENDELEO 2050


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiagana na viongozi mbalimbali kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA) Jijini Dar es Salaam kabla ya kuondoka nchini, kuelekea Shirikisho la Urusi kwa ziara ya Kitaifa itakayoanza tarehe 3 hadi 5 Juni, 2026 kwa mualiko wa Rais wa Shirikisho la Urusi, Mheshimiwa Vladimir Putin



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, leo Juni 2, 2026 ameondoka nchini kuelekea Shirikisho la Urusi kwa ziara ya kitaifa ya kihistoria inayofanyika kufuatia mwaliko rasmi wa Rais wa Shirikisho la Urusi, Mhe. Vladimir Putin.

Mhe. Dkt. Samia aliondoka katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA), Dar es Salaam, ambako alisindikizwa na viongozi mbalimbali wa Serikali kabla ya kuanza safari hiyo inayotarajiwa kufungua ukurasa mpya wa ushirikiano kati ya Tanzania na Urusi katika sekta za uchumi, biashara, uwekezaji, elimu, teknolojia, nishati na maendeleo ya miundombinu.

Ziara hiyo inakuja katika kipindi ambacho Tanzania inaendelea kutekeleza kwa kasi ajenda yake ya mageuzi ya kiuchumi na maendeleo jumuishi chini ya uongozi wa Rais Samia, huku nchi ikijipanga kufikia malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Katika ziara hiyo, Tanzania itapata fursa ya kuwasilisha mafanikio makubwa yaliyopatikana katika miaka ya hivi karibuni pamoja na mwelekeo wa maendeleo ya baadaye, hususan katika utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 inayolenga kuifanya Tanzania kuwa nchi yenye uchumi imara, shindani na unaotoa fursa kwa wananchi wote.

Aidha, mazungumzo kati ya viongozi wa Tanzania na Urusi yanatarajiwa kuimarisha zaidi uhusiano wa kidiplomasia uliodumu kwa miongo kadhaa na kufungua milango mipya ya uwekezaji, biashara na ushirikiano wa kimkakati unaolenga kukuza ustawi wa wananchi wa mataifa hayo mawili.

Ziara ya Rais Samia nchini Urusi pia inaonesha kuendelea kuimarika kwa nafasi ya Tanzania katika diplomasia ya kimataifa, ambapo taifa linaendelea kujenga mahusiano yenye manufaa ya pamoja na mataifa mbalimbali duniani sambamba na kutangaza fursa zake za kiuchumi na maendeleo.

Kupitia ziara hiyo, Tanzania inatarajia kuendelea kujifunza uzoefu wa kimataifa, kuvutia mitaji na teknolojia mpya, pamoja na kuimarisha ushirikiano utakaochangia utekelezaji wa vipaumbele vya maendeleo ya taifa kwa manufaa ya vizazi vya sasa na vijavyo.

Friday, May 29, 2026

Makamu wa Rais Dkt. Nchimbi Aungana na Waombolezaji Chato Katika Ibada ya Kumuaga Mama wa Hayati Dkt. John Magufuli

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi akiwa na waombolezaji mbalimbali kushiriki Ibada ya kumuaga na kumuombea Marehemu Bi. Suzana Ngolo Magufuli ambaye ni Mama wa aliyekuwa Rais wa Awamu ya Tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Hayati Dkt. John Pombe Magufuli, inayofanyika leo tarehe 29 Mei 2026.





Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi, amewasili katika Viwanja vya Kilimani vilivyopo Wilaya ya Chato mkoani Geita, ambapo ameungana na waombolezaji mbalimbali kushiriki Ibada ya kumuaga na kumuombea marehemu Bi. Suzana Ngolo Magufuli.

Marehemu Bi. Suzana Magufuli ni mama wa aliyekuwa Rais wa Awamu ya Tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Hayati Dkt. John Pombe Magufuli.

Ibada hiyo ya kuaga na kumuombea marehemu inafanyika leo tarehe 29 Mei 2026, ikiibua hisia za majonzi na heshima kubwa kutoka kwa viongozi wa Serikali, familia, pamoja na wananchi waliojitokeza kwa wingi kushiriki tukio hilo la maombolezo.

Thursday, May 28, 2026

SEKTA YA NYUMBA YAPATA MSUKUMO MPYA, NHC YATEKELEZA MIRADI YA MABILIONI NCHINI

Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Mhe. Dkt. Leonard Akwilapo akiwasilisha  Bungeni Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara kwa mwaka 2026/27
Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Nyumba la Taifa, Hamad Abdallah akisalimiana na Katibu Mkuu wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Injinia Anthony Sanga Bungeni Dodoma.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Injinia Anthony Sanga Bungeni Dodoma. akisalimiana na Mweyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Shirika la Nyumba la Taifa, Dk. Sophia Kongela
Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Nyumba la Taifa, Hamad Abdallah akiwa katika gallery ya Spika kufuatilia hotuba ya Bunge.

Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Nyumba la Taifa, Hamad Abdallah akiwa katika gallery ya Spika kufuatilia hotuba ya Bunge.

Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Nyumba la Taifa, Hamad Abdallah akijadiliana jambo na Bw. Deodatus Philip Mwanyika, Mbunge wa Jimbo la Njombe Mjini (CCM) na mmoja wa Wenyeviti wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Injinia Anthony Sanga Bungeni Dodoma. akisalimiana na Waziri wa Mstaafu  wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Dk. Angelina Lubala Mabula

DODOMA — Serikali kupitia Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi imeendelea kuonesha dhamira ya kuimarisha sekta ya makazi na biashara nchini kupitia utekelezaji wa miradi mikubwa ya Shirika la Nyumba la Taifa (NHC), huku miradi kadhaa ya kimkakati ikitarajiwa kukamilika ndani ya mwaka 2026 na mingine kuanza rasmi mwaka wa fedha 2026/27.

Akiwasilisha Bungeni Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara kwa mwaka 2026/27, Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Mhe. Dkt. Leonard Akwilapo amesema Serikali kupitia NHC imeendelea kusimamia utekelezaji wa miradi ya nyumba, biashara na uwekezaji inayolenga kuongeza upatikanaji wa makazi bora pamoja na kuchochea ukuaji wa uchumi wa miji mbalimbali nchini.

Katika hotuba hiyo, Mhe. Dkt. Akwilapo amesema ujenzi wa nyumba 422 katika mradi wa Kawe 711 jijini Dar es Salaam wenye thamani ya shilingi bilioni 169 umefikia asilimia 85 ya utekelezaji na unatarajiwa kukamilika ifikapo Juni 30, 2026. Aidha, mradi wa nyumba 196 wa Golden Premier Residence (GPR) wenye thamani ya shilingi bilioni 127 umefikia asilimia 50 huku ukitarajiwa kukamilika mwaka 2027.

Waziri huyo amesema Serikali pia inaendelea na maandalizi ya utekelezaji wa miradi mipya ya makazi kupitia mpango wa nyumba 5,000 wa Samia Housing Scheme katika maeneo ya Mtoni Kijichi na Kawe jijini Dar es Salaam pamoja na Medeli na Iyumbu jijini Dodoma.

“Katika mwaka 2026/27, Shirika litaendelea na ujenzi wa nyumba katika miradi ya Samia Housing Scheme sambamba na kuanza utekelezaji wa miradi mipya katika maeneo ya Njedengwa Dodoma, Urafiki Dar es Salaam, Makongoro Mwanza na Sokoine Complex Arusha,” amesema Mhe. Dkt. Akwilapo.

Kwa upande wa nyumba za gharama nafuu, Waziri Akwilapo amesema NHC limekamilisha maandalizi ya awamu ya kwanza ya ujenzi wa nyumba 800 katika maeneo ya Salama Creek Kigamboni, Sabasaba Morogoro, Iyumbu Dodoma na Buswelu Mwanza, ambapo utekelezaji rasmi utaanza mwaka 2026/27.

Mbali na sekta ya makazi, Waziri huyo amesema NHC linaendelea na utekelezaji wa miradi mbalimbali ya majengo ya biashara nchini, hatua inayochochea shughuli za kiuchumi pamoja na kuongeza thamani ya maeneo ya mijini.

Miradi hiyo ni pamoja na Meru View Shops Arusha iliyofikia asilimia 52, Tabora Commercial Complex asilimia 46, Singida 2F Plaza asilimia 85, Mkwakwani Commercial Complex Tanga asilimia 40, Kashozi Commercial Complex Kagera asilimia 65, Uluguru Plaza Morogoro asilimia 42 na Iringa Commercial Complex asilimia 40.

Aidha, Serikali imeeleza kuwa miradi ya biashara na ofisi katika maeneo ya Masasi, Mtanda Lindi na Zongomela Kahama imekamilika huku maandalizi ya mwisho ya miradi ya Usa River na Ngarenaro yakiendelea.

Katika eneo la ubia, Mhe. Dkt. Akwilapo amesema NHC linaendelea kusimamia miradi 21 ya ubia yenye thamani ya shilingi bilioni 351 ambapo miradi mitatu imekamilika na mingine ipo katika hatua mbalimbali za utekelezaji kwa wastani wa asilimia 56.

Amesema pia Shirika linaendelea kutwaa na kufufua miradi iliyokuwa imesimama kwa muda mrefu ili kuhakikisha uwekezaji huo unaleta tija kwa wananchi na Taifa kwa ujumla. Kati ya miradi 24 iliyokuwa imesimama, miradi 13 imekamilika huku mingine ikiendelea kushughulikiwa.

Katika hatua nyingine, Waziri huyo amesema NHC limeendelea kuimarisha utendaji wake wa kifedha ambapo hadi Mei 15, 2026 limefanikiwa kupunguza madeni kutoka shilingi bilioni 27.98 mwaka 2024/25 hadi shilingi bilioni 19 mwaka 2025/26.

Pia, Shirika limeendelea na mpango wa ukarabati wa nyumba zake ambapo nyumba 1,283 kati ya nyumba 1,600 zilizopangwa kukarabatiwa tayari zimekamilika sawa na asilimia 80 ya lengo.

Kwa upande wa miradi ya ukandarasi na ushauri elekezi, Waziri Akwilapo amesema NHC limekamilisha ujenzi wa majengo nane ya Ofisi za Serikali katika Mji wa Serikali Mtumba Dodoma pamoja na jengo la Soko la Madini la Tanzanite Mirerani Manyara.

Kadhalika, ujenzi wa majengo ya TCRA Dodoma umefikia asilimia 73 huku mradi wa Zanzibar ukiwa umefikia asilimia 50.

Hotuba hiyo imeendelea kuonesha nafasi ya NHC kama chombo muhimu cha Serikali katika utekelezaji wa miradi ya kimkakati ya makazi, biashara na huduma za ushauri elekezi nchini, huku Serikali ikiendelea kuweka mazingira bora ya uwekezaji na upatikanaji wa nyumba kwa Watanzania wa makundi mbalimbali.

Friday, May 22, 2026

MAKAMU WA PILI WA RAIS ZANZIBAR AMTEMBELEA MHE. FARIDA AMOUR MOH'D HOSPITALINI, AMTAKIA AFYA NJEMA






Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Mhe. Hemed Suleiman Abdulla, leo tarehe 21 Mei 2026 amemtembelea na kumjulia hali Mwakilishi wa Viti Maalum kupitia Chama cha ACT Wazalendo, Mhe. Farida Amour Moh’d, ambaye amelazwa katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Mjini Magharibi Lumumba kwa ajili ya matibabu.

Katika ziara hiyo, Mhe. Hemed alipata fursa ya kuzungumza na Mhe. Farida pamoja na madaktari wanaomuhudumia, ambapo alielezwa maendeleo ya afya yake na hatua zinazoendelea kuchukuliwa katika kumpatia huduma stahiki za matibabu.

Makamu wa Pili wa Rais alimtakia Mhe. Farida nafuu ya haraka na kurejea katika majukumu yake ya kuwahudumia wananchi, huku akisisitiza umuhimu wa kuendelea kumpatia huduma bora za afya hadi atakapopona kikamilifu.

Ziara hiyo imeonesha mshikamano, upendo na utamaduni wa viongozi kujali ustawi wa wenzao wakati wa changamoto za kiafya.

Imetolewa na Kitengo cha Habari (OMPR)
Tarehe 21 Mei 2026.

Thursday, May 21, 2026

Tanzania kudhibiti ujenzi holela pembezoni mwa miji kuepuka gharama za miundombinu










Na Mwandishi Wetu

WAKATI mataifa mengi ya Afrika yaliyo Kusini mwa Jangwa la Sahara yakishuhudia kasi kubwa ya ukuaji wa miji, Tanzania imechukua msimamo thabiti wa kudhibiti uendelezaji holela wa makazi pembezoni mwa miji ili kuepuka gharama kubwa za kurekebisha miundombinu baadaye.

Akizungumza katika Jukwaa la 13 la Miji Duniani (WUF13) jijini Cairo, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Prof. Riziki Shemdoe, ameeleza kuwa Tanzania imeweka mkakati madhubuti wa kitaifa wa kusuka upya mustakabali wa miji kabla ya ujenzi holela kushamiri.

Prof. Shemdoe amesema kuwa serikali imeamua kuelekeza nguvu zake katika maeneo ya pembezoni mwa miji, akibainisha kuwa Dar es Salaam, Dodoma, Mwanza, Mbeya na Arusha zinapanuka kwa kasi ya mlalo. 

Ameonya kuwa ukuaji wa miji bila mpango wa mapema unasababisha makazi yasiyo rasmi, ukosefu wa ajira na changamoto za huduma muhimu kama maji safi, umeme na usafi wa mazingira.

“Ukuaji wa miji unapotokea bila mipango ya mapema unatengeneza makazi yaliyotawanyika na ukosefu wa ajira. Kuweka miundombinu katika maeneo haya baada ya kuwa tayari yamejengwa ni gharama kubwa zaidi kuliko kuyapanga mapema kabla hayajajengwa,” amesema Prof. Shemdoe.

Serikali imezindua miongozo mipya ya mipango ya miji na udhibiti wa uendelezaji, pamoja na miongozo ya kuhifadhi mazingira ya kijani. 

Kupitia mifumo ya kidijitali na taarifa za kijiografia (GIS), serikali inarasimisha makazi ya pembezoni na kugawa viwanja vilivyopimwa ili kuhakikisha matumizi bora ya ardhi.

Prof. Shemdoe ametaja Programu ya Tanzania ya Kupandisha Kiwango cha Miundombinu na Ushindani wa Miji (TACTIC) inayotekelezwa katika miji 45, ikilenga barabara, masoko na udhibiti wa mafuriko. 

Aidha, ameeleza kuwa Mradi wa Maendeleo ya Jiji la Dar es Salaam (DMDP) Awamu ya Kwanza na ya Pili unalenga kuongeza miundombinu inayohimili mabadiliko ya tabianchi.

Serikali pia inawekeza katika miji ya kati na pembezoni kwa kujenga masoko ya kisasa 28, vituo vya usindikaji wa mazao ya kilimo na kuanzisha Ukanda wa Kiuchumi wa Kwala.

Hatua hizi zinahakikisha fursa za ajira zinapatikana karibu na wananchi na kupunguza shinikizo la ukuaji holela katika Dar es Salaam.

Prof. Shemdoe amesisitiza kuwa ujenzi wa masoko makubwa zaidi ya 15 na uboreshaji wa sekta isio rasmi, hususan kwa vijana na wafanyabiashara wadogo ni sehemu ya ajenda kuu ya kitaifa ya kupunguza tatizo la ajira na kuimarisha uchumi wa miji.

Kwa mkakati huu, Tanzania inalenga kujenga miji yenye usawa, yenye miundombinu imara na inayoweza kukabiliana na changamoto za tabianchi, huku ikiepuka gharama kubwa za kurekebisha makosa ya uendelezaji holela.

Wednesday, May 13, 2026

KASI YA UJENZI WA RELI YA SGR IMEONGEZEKA – PROF. MBARAWA

 

Wahudumu wa ndani (Train crew) wa shirika la reli Tanzania (TRC) upande wa Standard Gauge Railway (SGR) wamehudhuria Bungeni Jijini Dodoma kwa mwaliko maalum wa Waziri wa Uchukuzi Mhe. Prof. Makame Mnyaa Mbarawa ili kuweza kushuhudia uwasilishwaji wa hotuba ya bajeti ya Uchukuzi ya makadirio ya mapato na matumizi kwa mwaka wa fedha 2026/2027.









Waziri wa Uchukuzi, Makame Mbarawa amesema Serikali kupitia Shirika la Reli Tanzania inaendelea kuandika historia mpya katika sekta ya usafiri wa reli nchini kupitia utekelezaji wa mradi mkubwa wa reli ya kisasa ya Standard Gauge Railway (SGR), ambao umeendelea kuonesha mafanikio makubwa katika vipande mbalimbali vya ujenzi.

Akiwasilisha makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara ya Uchukuzi kwa mwaka wa fedha 2026/2027 bungeni jijini Dodoma leo Jumatano Mei 13, 2026, Profesa Mbarawa amesema Serikali imeongeza kasi ya utekelezaji wa mradi huo wa kimkakati ambao unatajwa kuwa miongoni mwa miradi mikubwa zaidi ya miundombinu barani Afrika.

Amesema hadi kufikia mwezi Machi mwaka huu, vipande vya kwanza vya reli kutoka Dar es Salaam hadi Morogoro pamoja na kutoka Morogoro hadi Makutupora vimekamilika kwa kiwango kikubwa na tayari huduma za usafiri zimeanza kutolewa kwa wananchi kupitia vipande hivyo.

Hatua hiyo imeendelea kutoa matumaini makubwa kwa wananchi na wadau wa maendeleo kutokana na mchango wa reli hiyo katika kurahisisha usafirishaji wa abiria na mizigo, kupunguza gharama za usafiri pamoja na kuchochea ukuaji wa uchumi wa Taifa.

Kwa upande wa kipande cha Mwanza hadi Isaka, Profesa Mbarawa amesema ujenzi umefikia asilimia 68.77 huku kazi zikiendelea vizuri na kwa kasi kubwa ili kuhakikisha mradi huo unakamilika kwa wakati.

Aidha, amesema Serikali inaendelea na utekelezaji wa kipande cha tatu kutoka Makutupora hadi Tabora pamoja na kipande cha nne kutoka Tabora hadi Isaka, ambapo shughuli mbalimbali za ujenzi zinaendelea katika maeneo hayo.

Profesa Mbarawa amesema pamoja na changamoto zilizojitokeza katika baadhi ya vipande vya mradi huo na kusababisha kuchelewa kwa utekelezaji katika hatua za awali, Serikali imefanikiwa kupata suluhisho la kudumu baada ya kupata mkopo wa masharti nafuu wenye thamani ya dola za Marekani bilioni 1.277, sawa na takribani Shilingi trilioni 3.32.

Amesema hatua hiyo inaonesha dhamira thabiti ya Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Samia Suluhu Hassan katika kuimarisha miundombinu ya reli nchini kwa lengo la kuongeza ufanisi wa usafiri, kukuza biashara na kuharakisha maendeleo ya uchumi wa Taifa.

Katika tukio hilo, wahudumu wa ndani wa treni (Train Crew) wa Shirika la Reli Tanzania upande wa SGR walihudhuria kikao hicho cha Bunge kwa mwaliko maalum wa Waziri wa Uchukuzi ili kushuhudia uwasilishwaji wa hotuba ya bajeti ya Wizara ya Uchukuzi kwa mwaka wa fedha 2026/2027, jambo lililoonesha heshima na kutambua mchango wao katika mafanikio ya sekta ya reli nchini.

Mradi wa SGR unaendelea kuwa alama ya mapinduzi makubwa ya miundombinu nchini Tanzania, huku ukitajwa kuwa chachu muhimu ya maendeleo ya uchumi, biashara na usafiri wa kisasa kwa kizazi cha sasa na kijacho.

KUSANYENI KODI NA MADENI BILA KUOGOPA MTU YEYOTE– WAZIRI AKWILAPO ASEMA AKIZINDUA BODI MPYA YA NHC

  Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Dk. Leonard Akwilapo, akimkabidhi Mwenyekiti wa Bodi wa Shirika la Nyumba la Taifa (NHC),...