Saturday, April 11, 2026

MAKAMU WA RAIS AFUNGUA KONGAMANO LA VIJANA KATIKA KUMBUKIZI YA KUZALIWA BABA WA TAIFA HAYATI MWL. J.K NYERERE








Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi ametoa wito kwa vijana kusimama imara na kulinda umoja, kujenga uadilifu, kutumia elimu na ubunifu katika kukuza maendeleo ya nchi ili kuweza kumuenzi Baba wa Taifa Hayati Mwl. Julius Kambarage Nyerere kwa vitendo.

Makamu wa Rais ametoa wito huo wakati akifungua Kongamano la Vijana katika Kumbukizi ya Miaka 104 ya Kuzaliwaa Baba wa Taifa, Hayati Mwl. Julius Kambarage Nyerere, lililofanyika Ukumbi wa Chimwaga mkoani Dodoma, leo tarehe 11 Aprili 2026. Amesema ni muhimu kwa vijana kutambua wajibu wa msingi wa kizazi hiki, kwa kuhakakikisha wanafanya kila jitihada kuimarisha misingi ya kujitegemea kiuchumi, kiakili na kimaamuzi ili kuijenga nchi.

Makamu wa Rais amesema Hayati Baba wa Taifa alikuwa kiongozi aliyeunganisha Taifa na kutoa mchango mkubwa katika ukombozi wa Bara la Afrika. Amesema Taifa la Tanzania lilipata bahati ya pekee kuwa na Hayati Mwl. Nyerere kwa kuwa alichukia rushwa, ubadhirifu na matumizi mabaya ya madaraka. Aliamini katika utu na uhuru wa mwanadamu ikiwemo msisitizo wa kuhakikisha kila wananchi anapata elimu.

Ameongeza kwamba Baba wa Taifa alitengeneza misingi ya amani, utulivu na mshikamano katika Taifa pamoja na kufundisha vitu vyote vinavyoweza kuleta mpasuko kama vile ukabila, dini, rangi, kupuuza maendeleo na usawa katika jamii.

Makamu wa Rais amesema ni dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kuendeleza mshikamano na umoja ambao Baba wa Taifa aliujenga.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Bodi wa Taasisi ya Kumbukumbu ya Mwal. Nyerere ambaye ni Waziri Mkuu Mstaafu Mhe. Mizengo Pinda ametoa rai kwa vijana kuhakikisha wanafanya jitihada za kujifunza historia ya Taifa ili kufahamu waliotoa mchango mkubwa katika historia hiyo.

Amewahimiza kusoma vitabu vilivyoandikwa kuhusu Hayati Mwal.Julius Kambarage Nyerere ili kufahamu mchango mkubwa aliyoutoa katika ukombozi wa Bara la Afrika na msisitizo alioutoa wa katika kuhakikisha umoja wa Afrika. Ameongeza Taasisi hiyo imejikita katika kutoa mchango kwa kuwasaidia viongozi vijana kuwa wazalendo na wanaowajibika.

Kongamano hilo limejadili mada mbalimbali zenye lengo la kuwajengea vijana uzalendo, uwajibikaji, matumizi sahihi ya mitandao na matumizi bora ya fursa zilizopo nchini.

Watumishi Tume ya Uchaguzi watakiwa kuepuka uchochezi, wajipanga uchaguzi Isimani

 








Na Mwandishi Wetu, Morogoro

Watumishi wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi wametakiwa kutekeleza majukumu yao kwa kuzingatia katiba, sheria, kanuni  na taratibu na kuepuka lugha zozote za uchochezi zinazoweza kuleta uvunjifu wa amani na kuhatarisha maisha ya Watanzania.

Hayo yamesemwa leo Aprili 11, 2026 na Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na wenye Ulemavu), Dkt. James Henry Kilabuko kwa niaba ya Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Dkt Jimmy Yonaz wakati akifungua kikao cha Baraza la Wafanyakazi la Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, katika kikao kilichoketi Mkoani Morogoro. 

“Napenda kuwaasa, kuzingatia katiba, sheria, kanuni  na taratibu mnapotekeleza majukumu ya Tume na kuepuka lugha zozote za uchochezi zinazoweza kuleta uvunjifu wa amani na kuhatarisha maisha ya Watanzania,”alisema Dkt Kilabuko.

Dkt. Kilabuko amesema, taasisi ina malengo yake, upo uwezakano wa kuepusha migogoro ya ndani na nje ya taasisi inayoweza kuathiri utekelezaji wa majukumu ya Tume kwa ufanisi.

Mapema akimkaribisha Mgeni Rasmi, Mwenyekiti wa Baraza la Wafanyakazi INEC ambaye pia ni Mkurugenzi wa Uchaguzi wa Tume, Ndg. Ramadhani Kailima alisema kwa sasa Tume inaendelea na zoezi la uandishi wa Taarifa ya Uchaguzi Mkuu wa Rais, Wabunge na Madiwani ya Mwaka 2025.

“Tume imekamilisha Uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2025 ambao ulifanyika tarehe 29 Oktoba, 2025.  Kwa sasa Tume inaendelea na zoezi la uandishi wa Taarifa ya Uchaguzi Mkuu wa Rais, Wabunge na Madiwani ya Mwaka 2025. Taarifa hiyo baada ya kukamilika, itawasilishwa kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,”alisema Kailima.

Aidha, amesema Tume ipo katika maandalizi ya uchaguzi mdogo wa Ubunge katika Jimbo la Isimani mkoani Iringa kufuatia kifo cha aliyekuwa Mbunge wa Jimbo hilo, Mhe. William Lukuvi pamoja na uchaguzi wa udiwani katika Kata mbalimbali nchini ambazo madiwani wake walifariki.

Katika Kikao hicho cha siku moja pia kilitumika kwa kufanya uchaguzi wa Katibu wa Baraza hilo ambapo wajumbe walimchagua Ndg. Mwitaru Keboya kuwa Katibu mpya wa Baraza akichukua nafasi ya Ndg. Livini Avith ambaye amemaliza muda wake. 

Rais Samia Atunukiwa Shahada ya Uzamivu ya Heshima kwa Uongozi na Mchango wa Kijamii Afrika

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akitunukiwa Shahada ya Uzamivu ya Heshima kutoka Chuo Kikuu cha Jimbo la Nasarawa, Keffi nchini Nigeria kwa njia ya mtandao, tarehe 11 Aprili, 2026 Ikulu, Dodoma.

Mhe. Rais ametunukiwa Shahada hiyo ya Uzamivu ya Heshima kwa kutambua mchango wake kama Kinara wa Nishati Safi ya Kupikia, Afya ya Mama na Mtoto, Taswira nzuri katika masuala ya Uongozi kwa Wanawake Afrika na Kusimamia Masuala ya Biashara hususani kwa Vijana Afrika.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akizungumza kwa njia ya mtandao na Chuo Kikuu cha Jimbo la Nasarawa, Keffi nchini Nigeria ambacho kimemtunuku Shahada ya Uzamivu ya Heshima , tarehe 11 Aprili, 2026 Ikulu, Dodoma.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan, ametunukiwa Shahada ya Uzamivu ya Heshima na Nasarawa State University kwa njia ya mtandao, katika hafla iliyofanyika tarehe 11 Aprili 2026, Ikulu jijini Dodoma.

Tuzo hiyo imetolewa kwa kutambua mchango wake mkubwa katika kuendeleza ajenda za kijamii na kiuchumi barani Afrika, hususan katika maeneo ya nishati safi ya kupikia, afya ya mama na mtoto, pamoja na kukuza taswira chanya ya uongozi wa wanawake.

Aidha, Mhe. Rais ametambuliwa kwa juhudi zake za kusimamia na kuhamasisha maendeleo ya biashara, hasa kwa vijana, ambapo amekuwa kinara wa kuweka mazingira rafiki ya uwekezaji na ujasiriamali.

Kutunukiwa kwa heshima hiyo kunadhihirisha nafasi ya Tanzania katika ramani ya uongozi bora barani Afrika, pamoja na mchango wa Mhe. Rais katika kuleta mageuzi yenye tija kwa jamii na vizazi vijavyo.

MFUMO MPYA WA MAFUTA WAONGEZA MAPATO, WAFANYABIASHARA WAFURAHIA

 


KAMPUNI ya Uingizaji na Usambazaji wa mafuta Jamii ya Petrol nchini ya ‘MOIL Energies’ imesema imefurahishwa kwa kuanzishwa kwa mfumo mpya wa ulipaji kodi ya nishati hiyo kabla ya kuyatoa vituoni na kwenda sokoni (BIL)kwa kiasi kikubwa umesaidia kudhibiti ‘ujanja ujanja’ uliokuwepo hapo awali

Akizungumza Dar es Salaam Meneja Mkuu wa Kampuni hiyo nchini, Dkt Sajad Habib Rai amesema wao kama Kampuni ya kwanza nchini kutoa mapendekezo ya kuanzishwa kwa mfumo huo kwa EWURA na Wakala wa Uagizaji wa Mafuta kwa Pamoja (PBPA) na baadae kuanzishwa rasmi na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), wanajivunia kuona umetekelezwa kwa kuwa dhamira yao ilikuwa kuona huduma ya usambazaji wa mafuta nchini na nje ya nchi unaleta tija kwa Taifa.

“Tumefurahi kuona TRA wameusimamia kikamilifu mfumo huu kwa kuwa unazuia ukwepaji kodi ambao hapo awali ulikuwa ukifanywa na wafanyabiashara, hivi sasa TRA inapata kodi yake mapema kabla ya kuyaingiza mafuta sokoni” amesema Dk Sajad ambaye pia ni Meneja MKAZI wa ‘Mansoor Industry Limited’

Hivi karibuni Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) ilitangaza rasmi kuanza kutumika kwa mfumo huo ambao kwa kiasi kikubwa unalezwa kuleta tija kwa Serikali kwa kuwa umesaidia kudhibiti upotevu wa mapato unaotakana na Kodi za uingizaji wa mafuta hayo nchini.

Kupitia mfumo huo mpya na wa kisasa, kila mwagizaji au muingizaji wa mafuta atalazimika kutaja kiasi cha mafuta alichokiingiza nchini ambapo kupitia Shirika la Viwango Tanzania (TBS) watayataweka vinasaba kama alama ya kila mwagizaji kwa lengo la kuwatambua wahusika wote na kiasi alichoagiza ili kuwakadiria viwango vya Kodi wanavyopaswa kulipa.

“Nawapongeza TRA kwa kuona tija na umuhimu wa kuutumia mfumo huu, sisi kama wafanyabiashara tunaozingatia taratibu halali za uingizaji na Usambazaji wa mafuta tunaiona kuwa hatua hii ni kubwa na inayostahili kupongezwa kwa kuwa italeletea manufaa Taifa” ameongeza Dkt Sajad.

Utaratibu huo wa kikodi unawataka wamiliki wa mafuta hayo kuyalipia kodi kabla ya kuyaingiza sokoni ili yanapoingizwa sokoni yanaendelea na taratibu za uuzwaji hali ambayo inarahisisha usambazaji na kuwafikishia wateja huduma ya mafuta kwa wakati sambamba na kudhibiti kubaki nchini mafuta ambayo kimsingi yanapaswa kusafirishwa kwenda nje ya nchi.

Aidha akizungumza wakati wa ziara yake aliyoifanya hivi karibuni katika bohari za kuhifadhia mafuta zilizopo Jijini Dar es Salaam, Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Yusuph Juma Mwenda pamoja na mambo mengine alisema lengo la TRA kuweka utaratibu huo ni kuwezesha biashara kufanyika kwa urahisi na kuondoa changamoto zilizokuwepo hapo awali huku akitoa wito kwa wafanyabiashara watakaokutana na changamoto zozote kuwasiliana na TRA.

Pamoja na mambo mengine pia Kamishina Mwenda alisema Mamlaka hiyo pia umeweka utaratibu wa kufanya kazi kwa Saa 24 ili kuharakisha utolewaji wa huduma kwa walipakodi ambao ni waingizaji, wasambazaji na wauzaji wa mafuta hayo.



DKT. AKWILAPO AKUTANA NA MTENDAJI MKUU WA SHELTER AFRIQUE

 


Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo (Kushoto) na Mtendaji Mkuu wa Shelter Afrique Bw.Thierno-Habib Hann wakiwa katika picha ya pamoja mara baada ya kikao chao jijini Nairobi, Kenya, walipokutana pembezoni mwa Kongamano la pili la Miji Afrika lilofanyika nchini humo.

Na Munir Shemweta, WANMM Nairobi

Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Dkt Leonard Akwilapo, amekutana na kufanya mazungumzo na Afisa Mtendaji Mkuu wa Shelter Afrique Bw. Thierno-Habib Hann jijini Nairobi, nchini Kenya.

Viongozi hao wawili wamekutana pembezoni mwa Kongamano la Miji Afrika (2nd Africa Urban Forum) lililofanyika kuanzia Aprili 8 hadi 10, 2026 nchini Kenya, na kukutanisha mataifa mbalimbali Barani Afrika kwa lengo la kubadilishana uzoefu na suluhisho bunifu katika kukabiliana na changamoto za maendeleo ya miji na makazi.

Dkt Akwilapo na Bw.Thierno-Habib Hann katika kikao chao walijadili masuala mbambali yanayohusu uimarishaji wa upatikanaji wa makazi nafuu kwa wananchi pamoja na ushirikiano kati ya serikali na taasisi za kifedha katika kufanikisha azma hiyo. 

Shelter Afrique ni taasisi ya kifedha ya kimataifa inayolenga kusaidia maendeleo ya makazi Barani Afrika, huku makao makuu yake makuu yakiwa jijini Nairobi nchini Kenya.

Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo (Kulia) akizungumza na Mtendaji Mkuu wa Shelter Afrique Bw.Thierno-Habib Hann jijini Nairobi, Kenya walipokutana pembezoni mwa Kongamano la pili la Miji Afrika (2ND Africa Urban Forum) lilofanyika nchini humo.
Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo (Kulia) akitambulishwa baadhi ya maafisa wa taasisi ya Shelter Afrique alipokutana na Mtendaji Mkuu wa taasisi hiyo Bw.Thierno-Habib Hann pembezoni mwa Kongamano la pili la Miji Afrika (2nd Africa Urban Forum) lilofanyika jijini Nairobi nchini Kenya. (PICHA ZOTE NA WIZARA YA ARDHI)

MSD Yawanoa Watumishi Kanda ya Kilimanjaro Kuboresha Huduma za Afya

 






Watumishi wa Bohari ya Dawa (MSD) Kanda ya Kilimanjaro wanashiriki mafunzo maalum yenye lengo la kuimarisha uwajibikaji, mshikamano na ufanisi katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku—hatua muhimu katika kuboresha utoaji wa huduma kwa sekta ya afya nchini.

Mafunzo hayo yanafanyika mkoani Arusha, yakihusisha watumishi kutoka mikoa ya Kilimanjaro, Arusha na Manyara. Lengo kuu ni kuwajengea uwezo wa kufanya kazi kwa ufanisi zaidi kupitia misingi ya ushirikiano, umoja na maadili bora ya kazi.

Katika mafunzo hayo, washiriki wanapatiwa maarifa muhimu kuhusu mikakati ya utoaji huduma bora kwa wateja, maadili na uadilifu kazini, pamoja na uelewa wa kina wa mpango mkakati na mwelekeo wa taasisi. 

Aidha, wanajengewa uwezo wa kukabiliana na changamoto za msongo wa mawazo na namna ya kudumisha uwiano kati ya kazi na maisha binafsi—mambo yanayochangia kuongeza tija kazini.

Kanda ya Kilimanjaro ya MSD inahudumia takribani vituo vya afya 991 vilivyopo katika mikoa hiyo mitatu, hivyo juhudi hizi zinatarajiwa kuongeza ufanisi katika usambazaji wa dawa na vifaa tiba, na hatimaye kuboresha huduma kwa wananchi.

Sambamba na vipindi vya kitaaluma, mafunzo hayo pia yamejumuisha michezo na shughuli za kijamii zinazolenga kujenga timu imara, kuimarisha mawasiliano na kukuza mshikamano miongoni mwa watumishi.

Hatua hii inaonesha dhamira thabiti ya MSD ya kuwekeza katika rasilimali watu wake ili kuhakikisha huduma bora, za haraka na zenye viwango vya juu zinawafikia Watanzania wote.

Thursday, April 09, 2026

TUTABORESHA BAJETI YA ELIMU – WAZIRI MKUU




▪️Asema Serikali itaimarisha vitengo vya tathmini na ufuatiliaji kila wizara

Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba amesema Serikali itaendelea kuboresha bajeti ya elimu wakati ikitekeleza mtaala mpya wa elimu ili kuziba mianya ya mahitaji shuleni.

“Kwa kuwa tunaenda katika mtaala mpya wa elimu, tutaendelea kuboresha bajeti. Tutaendelea kuboresha bajeti kwa sababu mahitaji yanaongezeka kila wakati katika kumfanya mtoto asome vizuri,” amesema.

Waziri Mkuu ametoa kauli hiyo Bungeni jijini Dodoma, leo (Alhamisi, Aprili 9, 2026) wakati akijibu swali la Mbunge wa Segerea, Agnesta Lambert Kaiza, kwenye kipindi cha maswali ya papo kwa papo kwa Waziri Mkuu ambaye alitaka kujua kauli ya Serikali juu ya kukomesha michango holela inayotozwa shuleni.

Dkt. Mwigulu amesema Serikali haina shida na michango ya chakula ambayo imekuwa ikitolewa shuleni lakini akasisitiza kuwa endapo kutatokea michango mingine yoyote, ni lazima ifuate miongozo ya serikali na ipate baraka za Wakuu wa Mikoa husika.

Akitoa mfano wa michango ambayo haikubaliki, Waziri Mkuu amesema akiwa ziarani mkoani Katavi, alipokea malalamiko ya Mama mmoja ambaye mwanaye alizuiwa kujiunga na shule ya sekondari hadi atoe sh. 50,000/- ya dawati.

“Nilielekeza yule mtoto arudishwe shuleni na nimpongeze Mkuu wa Mkoa ambaye amenijulisha kuwa yule mtoto amesharudi shuleni. Lakini pia nilielekeza yule mwalimu mkuu naye aitwe na mamlaka za nidhamu, ahojiwe kwa uzembe wa kuona mtoto anakosa masomo kwa miezi miwili na wao wakaendelea na maisha kana kwamba hakuna jambo lililotokea,” amesema.

Mbali na changamoto hiyo, Waziri Mkuu amewapongeza walimu nchini kwa kujitoa bila kuchoka ili kuhakikisha watoto wa Kitanzania wanapata elimu bora. “Sote tunatambua kuwa walimu wengi wamejitoa sana katika baadhi ya maeneo. Licha ya wingi watoto na uchache wa walimu, kwa juhudi zao wamehakikisha wanakamilisha syllabus zao ili watoto wetu wapate elimu bora.”

Akielezea kuhusu uwepo wa walimu wa kujitolea katika baadhi ya shule, Waziri Mkuu amesema alishatoa maelekezo kwamba malipo ya walimu wa aina hiyo yatoke kwenye mapato ya ndani ya Halmashauri husika badala ya kuwataka wazazi wachangie malipo yao.

“Wazo la kuwa na walimu wa kujitolea ni jema, na sisi wakati tunasoma tulipata mafunzo ya ziada (tuition) kwa walimu wa aina hii. Wazo la kuwa na walimu wanaojitolea ni jema lakini malipo yao yasilipwe na wazazi, badala ya kwenda kwenye michango, Mamlaka za Serikali za Mitaa watumie mapato ya ndani.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu amesema Serikali itaendelea kuimarisha vitengo vya tathmini na ufuatiliaji katika kila wizara ili viweze kufanya kazi kwa ufanisi zaidi. “Kwenye kila wizara, kuna hivi vitengo vya ufuatiliaji na tathmini. Tunapanga kuongeza bajeti zao ili viweze kutimiza wajibu wao katika ufuatiliaji wa miradi na shughuli zote za Serikali.

Alikuwa akijibu swali la Mbunge wa Monduli, Isack Joseph Copriano aliyetaka kujua  Serikali ina mkakati gani wa kuimarisha timu ya tathmini na ufuatiliaji ili kuharakisha majibu ya wananchi na hususan kero zao. 

Alisema katika kuimarisha mawasiliano na wananchi, Serikali imeanzisha kituo cha kupokea simu (Call Centre) yenye namba 190 ambapo mwananchi mwenye shida yoyote anaweza kupiga simu na kutoa kero yake na kwamba atajulishwa majibu yake kupitia kituo hicho.

Amesema Serikali inataka kurejesha utaratibu wa kila kiongozi kubeba hoja za wananchi kupitia rejesta ambazo zitakuwa zinatumika kwenye ofisi za viongozi kurekodi kero za wananchi na kutoa mrejesho serikalini kila mwisho wa mwezi.

“Utaratibu wa kupokea kero siyo wa kwenye ziara tu, kila mwezi viongozi watapaswa kutoa taarifa ya idadi ya wananchi waliowahudumia na majibu waliyowapa wakionesha hoja zipi walipokea, namba za simu za wananchi waliohudumiwa na hizo hoja zimetatuliwa vipi.” 

“Tunataka kurejesha utaratibu wa kila kiongozi kubeba hoja za wananchi na siyo kuacha wananchi waende kutafuta majibu kwa viongozi,” alisisitiza.


MAKAMU WA RAIS AFUNGUA KONGAMANO LA VIJANA KATIKA KUMBUKIZI YA KUZALIWA BABA WA TAIFA HAYATI MWL. J.K NYERERE

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi ametoa wito kwa vijana kusimama imara na kulinda umoja, ...