Monday, May 25, 2015

Edward Lowassa azungumza na waandishi wa habari Dodoma

Waziri Mkuu aliyejiuzulu Mh Edward Lowassa leo amezungumza na waandishi wa habari nyumbani kwake eneo la Area C mkoani Dodoma ambapo amebainisha dhamira yake ya kuchukua fomu ya kuwania Urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa tiketi ya Chama cha Mapinduzi(CCM).
Katika Mkutano huo na waandishi wa habari, Mh Lowassa amevunja ukimya kwa kusema kuwa tuhuma zinazoelekezwa kwake kuhusu sakata la Richmond si za kweli na hakuhusika.
Mbunge huyo wa Monduli amebainisha kuwa alishangaa kuona kamati ya Dr Harrison Mwakyembe haikuona sababu ya kumhoji.
Ameituhumu kamati hiyo kwa kushirikina na spika wa bunge wakati huo Mh Samwel Sitta kuwa ilikuwa na lengo la kumchafua ili aachie cheo cha uwaziri mkuu.
Mh Lowassa Amesisitiza kuwa hicho hakiwezi kuwa kikwazo kwake kuingia Ikulu.
Mh Lowassa ambaye anaonekana kujipanga vyema, amesema kuwa anaamini kila mtangaza nia ana makundi ya kumuunga mkono hivyo haoni tatizo kuwatambulisha baadhi ya watu wanaomuunga mkono.
Mbunge huyo wa Monduli pia amebainisha iwapo chama chake kitamteua na hatimae kushinda nafasi ya Urais, lengo kuu atakaloanza nalo ni Elimu.
Pia amesema kuwa anaamini atafanikiwa kutimiza ndoto yake ya kuingoza nchi hii na kuindoa kwenye dimbwi la umasikini huku akitoa shukrani kwa marafiki zake wanaomuunga mkono.
Amewataka wananchi kuwa tayari kwa mkutano mkubwa atakaoufanya jijini Arusha May 30, ambapo amesema katika mkutano huo ataanika kila jambo kuhusu mustakabali wa nchi na mipango yake ya kuiinua nchi kiuchumi katika miaka kumi ijayo.
Mh Lowassa pia amewaonya wapinzani wake kuwa wasitegemee kama atakihama chama cha Mapinduzi(CCM), ataendelea kuwa ndani ya CCM na harakati zake atazifanya CCM.

No comments: