Friday, March 27, 2009

Marekani Yamtambua Anna Kilango Mwanamke Jasiri wa Kitanzania


Kaimu Balozi wa Marekani nchini Larry André jana alimkabidhi cheti Mbunge wa Jimbo la Same Mashariki mkoani Kilimanjaro, Mheshimiwa Anne Kilango Malecela, ambaye amechaguliwa na Ubalozi wa Marekani jijini Dar es Salaam kama Mwanamke Jasiri wa Kitanzania kwa Mwaka 2009.

Kwa mujibu wa taarifa kutoka katika Ubalozi wa Marekani, tuzo hiyo ya mwaka ilianzishwa kwa lengo la kutambua na kuthamini mchango wa mwanamke aliyeonyesha ujasiri wa kiwango cha juu na uongozi mzuri.

Aidha, Ubalozi wa Marekani nchini Tanzania ulimteua Bi. Malecela kuwa mmojawapo kati ya washiriki waliowania Tuzo ya Kimataifa ya Mwanamke Jasiri ya Mwaka 2009, kutokana na ujasiri aliounyesha katika kukosoa na kuupa changamoto uongozi wa chama chake ili uweze kushughulikia kikamilifu suala la rushwa.

Kwa kufanya hivyo alivunja utamaduni wa kisiasa uliokuwa umejengeka bila kujali vitisho kwa usalama wake binafsi. Bila kuchoka wala kutetereka, Bi Malecela alishikilia azma yake ya kupiga vita rushwa na kuuliza maswali mazito yaliyoibua mijadala iliyochangia sana katika jitihada za kuongeza uwazi na utawala bora ndani ya chama tawala. Kwa taarifa zaidi kuhusu suala hili hebu soma hapa