Jumuiya ya vikundi vya wenye viwanda na biashara ndogondogo Tanzania (VIBINDO) wamepongeza hatua ya ya Serikali kuwatembelea na kuchukua maoni yao, ikionyesha ushirikishwaji wa wananchi kuanzia hatua ya awali, kabla ya kuanza kutekelezwa kwa jambo lolote.
Hayo yamezungumzwa na Bw. Gaston Kikuwi mwenyekiti wa Jumuiya ya vikundi vya wenye viwanda na biashara ndogondogo Tanzania (VIBINDO), leo tarehe 16 Juni, 2024 wakati wajumbe wa Timu ya Kitaifa ya Wataalamu ya Kuandaa Mpango wa Pili wa Maboresho ya Mazingira ya Biashara (MKUMBI II) walipotembelea Jumuiya hiyo na kupata maoni na changamoto zinazohusu mazingira ya biashara nchini.
“Timu hii kufika katika maeneo yetu ya biashara, inatupa nafasi ya kutoa maoni yetu kwa uwazi, maana mnajionea hali halisi ilivyo. Tunawahakikishia changamoto na maoni tuliyoyatoa kuhusu mazingira ya biashara pamoja na mapendekezo ya namna ya kuyatatua kwa kushirikiana na serikali”. Amesema Bw. Kikuwi.
Itakubukwa kuwa Timu ya Kitaifa ya Wataalamu ya kuandaa MKUMBI II, iliundwa hivi karibuni na Mhe. Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa na kupewa jukumu la kufanya tathmini ya maendeleo yaliyopatikana kupitia MKUMBI I, na kutambua changamoto mpya zinazokabili sekta binafsi.
Katika kutekeleza hilo Timu hiyo imeanza kutembelea wadau wa sekta ya Umma na Binafsi ili kupata maoni yao katika hatua za awali ya maandalizi ya mpango wa Pili wa Maboresho ya Mazingira ya Biashara (MKUMBI II), pia kuhakikisha changamoto zote zinazoikabili sekta binafsi zinawekewa mikakati ya kupata ufumbuzi wa kudumu wa mazingira ya biashara na uwekezaji nchini.
No comments:
Post a Comment