KAMPUNI YA GEITA RESOURCES LIMITED YANADI FURSA





Vipo vifaa vya kisasa vya uchimbaji madini

GEITA

Kampuni ya Geita Resources  Limited inayojihusisha na utafiti, uchimbaji wa madini ya dhahabu, uuzaji wa kemikali za kuchenjua dhahabu na usambazaji wa vifaa vya uchimbaji wa madini kwenye Sekta ya Madini imekaribisha wadau  wa madini na wananchi kwa ujumla kujifunza na kujionea vifaa vya kisasa vya uchimbaji wa madini.

Akizungumza kwenye mahojiano maalum, mtaalam  kutoka kampuni hiyo, John Sililo leo Oktoba 7, 2024 kwenye Maonesho ya  Saba ya Teknolojia ya Madini katika Viwanja vya Bombambili  mkoani Geita, amesema kuwa kampuni hiyo iliyoanzishwa  tangu mwaka 2022 ilianza kutumia teknolojia ya kizamani katika kukamata dhahabu (Metal detector) ambapo kwa sasa wanatumia teknolojia ya kisasa zaidi ya (Shaking table/washing plant) ambayo inatumika kuzalisha dhahabu za vikole.

Katika hatua nyingine, Sililo ameishukuru Wizara ya Madini kupitia Tume ya Madini kwa miongozo na maelekezo kwa wachimbaji wadogo  hususan katika masuala ya kiusalama ambapo Tume ya Madini imekuwa ikiwatembelea na kuangalia usalama wa maeneo mara kwa mara sambamba na kutoa elimu kuhusu usalama kwenye shughuli za uchimbaji na uchenjuaji wa madini.

Vilevile amesema kuwa, wameweza kupiga hatua kutoka uchimbaji mdogo na kuwa wachimbaji wa kati, ambapo walikuwa wanachimba kwa kutumia duara za matimba na sasa wamefikia hatua ya kuchimba kwa kutumia duara za zege (Concrete Shaft) ambazo zinadumu mpaka miaka 100.

“Kutokana na jitihada za Mhe. Rais wa Jamhuri wa Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan alizozifanya kwenye Sekta ya Madini tumeweza kunufaika kwa kupelekewa nishati ya umeme kwenye maeneo ya uchimbaji ambapo imepunguza gharama za uzalishaji

Akieleza mipango ya Kampuni amesema kwa sasa wanaajiri watu wenye uzoefu katika masuala ya Utafiti, Uchimbaji na Uchenjuaji kwa lengo la kuongeza uzalishaji na kutengeneza ajira nyingi kwa Watanzania pamoja na kuendelea kuongeza migodi katika mikoa mingine.

Ameongeza  kuwa, wana Ofisi katika mikoa ya Geita, Mwanza, Simiyu, na Tabora na  wanapatikana kwa mawasiliano ya namba za simu +255742333345/0764 570579 na www.geitaresource.com

Comments