Monday, February 08, 2010

Majaji waipeleka puta serikali suala la mgombea binafsi




NAIBU Mwanasheria Mkuu wa Serikali jana alikuwa kwenye wakati mgumu mbele ya jopo la majaji saba wa Mahakama ya Rufaa wakati mabosi wa mhimili wa sheria hao walipohoji umakini wake katika kushughulikia rufaa dhidi ya uamuzi wa kuruhusu mgombea binafsi.

Wakiongozwa na Jaji Mkuu Augustine Ramadhani, majaji hao waliamua kuwa hukumu iliyotolewa na Mahakama Kuu ya kuruhusu mgombea huru ndiyo inayotambuliwa wakati wa uchaguzi mkuu wa Oktoba na baadaye hadi hapo itakapoamuliwa vinginevyo.

Ilifikia wakati Jaji Mkuu Ramadhan alisema: “Inasikitisha kuwa (Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali, George Masaju) unatoka kwenye ofisi ya AG (Mwanasheria Mkuu wa Serikali), lakini unalalamika kuwa hujasoma list of authorities. Sijui tunawapa mfano gani wengine!”

Mahakama Kuu iliruhusu mgombea binafsi baada ya mwenyekiti wa chama cha kisiasa cha DP, Mchungaji Christopher Mtikila kufungua kesi akidai kuwa sheria za nchi kuhusu haki ya kupiga kura na kupigiwa kura inapingana na katiba ya nchi kutokana na kutamka kuwa mgombea ni lazima apitishwe na chama.

Lakini tangu hukumu hiyo ilipotolewa mwezi Juni, 2006 ikitaka mchakato wa kutunga sheria ya kuruhusu mgombea binafsi ufanyike katika kipindi cha miezi sita, hakuna kilichofanyika na badala yake serikali ilikata rufaa ikipinga mamlaka ya Mahakama Kuu kutafsiri katiba. Imeandikwa na James Magai na Hussein Kauli

No comments: