Monday, September 17, 2007

Salva Mkurugenzi wa Mawasiliano Ikulu



RAIS Jakaya Kikwete, amemteua Mwandishi Mwandamizi nchini, Salvatory Rweyemamu (pichani) , kuwa Mkurugenzi mpya wa Idara ya Mawasiliano Ikulu.

Salvatory anachukua nafasi hiyo ambayo iliachwa wazi na Balozi Peter Kallaghe, ambaye sasa ni balozi wa Tanzania, nchini Canada.

Taarifa ya Idara ya Habari (Maelezo), iliyotolewa jijini Dar es Salaam jana, ilisema uteuzi huo ulianza tangu Septemba 11.

Kabla ya uteuzi huo, Salvatory alikuwa anafanyakazi katika Kampuni binafsi ya ushauri wa masuala ya mawasiliano ya G na S Media Consultants.

Salvatory ni miongoni mwa waandishi wandamizi nchini, ambao wanafahamika kutokana na kazi zao za kitaaluma ambazo wamekuwa wakifanya.

Mkurugenzi huyo aliwahi kuwa Mhariri katika Kampuni ya Uhuru Publications, wachapishaji wa magazeti ya Uhuru na Mzalendo kabla ya kwenda kuanzisha kampuni nyingine akiwa na wanataaluma wengine waandamizi.

Kampuni hiyo ambayo aliazisha akiwa na waandishi wengine waandamizi ni Habari Corporation.

Wakati wa uchaguzi mkuu wa Rais mwaka 2005, Salvatory alikuwa ni miongoni mwa waandishi waliokuwa wakiandika makala mbalimbali zinazoingia kwa undani katika kuwachambua wagombea wa kiti hicho. Picha ya Magid Mjengwa.

No comments: