Sunday, September 20, 2009

Miss Tanzania waahidi nidhamu mtindo mmoja




Warembo wanaowania taji la Vodacom Miss Tanzania wameahidi kuonyesha nidhamu na kufuata maelekezo ya walezi wao  katika kipindi chote hiki walichopo kambini.
 
Wakizungumza baada ya kutembelewa na ndugu na jamaa zao katika kambi yao iliyoko katika hoteli ya Girrafe walisema kwamba wao wanaamini kwamba siku zote nidhamu ndiyo silaha kubwa ya mafanikio.
 
"Kwa kweli tutajitahidi kuwa na nidhamu ili tuweze kufanikisha malengo yetu ya kuwa mfano bora katika jamii," anasema Evelyn Gamasa mrembo kutoka Kanda ya Ilala.
 
Warembo hao wamemaliza ziara yao ya kutembelea vivutio vya utalii katika mikoa ya Arusha na Kilimanjaro na kufuatia ziara hiyo wamesema wamejifunza mengi kuhusu sekta ya utalii.
 
Wakizungumzia ziara hiyo wamesema wamebaini kwamba Tanzania ni nchi iliyobarikiwa na Mungu kuwa na vivutio vya kipekee Duniani na kwamba kama vitatumiwa ipasavyo vinaweza kuboresha maisha ya Watanzania wengi hasa kwa upande wa sekta ya ajira.
 
Kwa upande wao baadhi ya wazazi wameonyesha kufurahishwa na jinsi mdhamini wa shindano hilo Vodacom Tanzania anavyowasaidia vijana nao.
 
Wamesema mdhamini huyo amekuwa mstari wa mbele katika kuhakikisha kwamba maisha ya Watanzania wengi yanaboreka hasa kwa upande wa ajira.
 
"Kwa kweli mdhamini huyu Vodacom anastahili sifa, amewaweka vijana wetu katika hoteli nzuri na pia kuwapatia huduma bora, hii inatupa moyo," anasema mmoja wa wazazi hao.
 
Wazazi wamesema kwamba pia zawadi zinazotolewa na Vodacom ni nzuri na kwamba zinasaidia kuboresha maisha ya vijana wao.
 
Fainali ya Vodacom Miss Tanzania itafanyika tarehe mbili mwezi ujao na mshindi wa kwanza atapata zawadi ya gari Suzuki Grand Vitara lenye thamani ya sh. milioni 53 na fedha taslim shilingi milioni tisa.

No comments: