Friday, October 05, 2012

KELVIN YONDANI AVUNJIKA, KUBAKI NJE YA UWANJA WIKI MBILI


Rafu aliyochezewa Kelvin Yondani na Haruna Moshi 'Boban'.


Mlinzi wa kati wa kutumainiwa wa klabu ya Young Africans na timu ya Taifa ya Tanzania (Taifa Stars) Kelvin Yondani anaendelea vizuri japo atakaa nje kwa muda wa wiki mbili mara baada ya kuanza kupata matibabu katika Hospitali ya Taifa Muhimbili kitengo cha mifupa (MOI)  jijini Dar es Salaam.
Akiongea na mtandao wa klabu www.youngafricans.co.tz, Daktari wa timu ya Young Africans Dokta Suphian Juma, amesema Yondani alipata mshtuko katika mfupa wake mkubwa, baada ya kuchezewa vibaya na kiungo wa timu ya Simba Haruna Moshi 'Boban'.
Dk. Suphian anawatoa wasiwasi wapenzi na washabiki wa Young Africans, kwamba Yondani anaendelea vizuri na anatazamiwa kurudi dimbani baada ya wiki mbili. "Unajua Yondani baada ya kukanygwa na Boban alipata mshituko katika mfupa wake mkubwa mguuni, hivyo anapata matibabu ya kumrejesha katika hali yake ya kawaida." Alisema Dk. Suphian.
Katika hali ya kushangaza mwamuzi wa mchezo huo wa watani wa jadi, Mathew Akrama alishindwa kumonyesha kadi nyekundu Boban kwa mchezo mbaya uliopelekea Yondani kutolewa nje na kushidwa kuendelea na mchezo.
Mechi hiyo ya Ligi Kuu ya Vodacom iliyowakutanisha watani wa jadi wakongwe Afrika Mashariki iliishia kwa sare ya mabao 1-1, mabao yaliyofungwa na Amri Kiemba Simba dakika ya 4 na Said Bahanunzi aliyesawazisha kwa upande wa Young Africans dakika ya 67.
Young Africans leo imeendelea na mazoezi katika uwanja wa shule ya sekeondari ya Loyola kujiandaa na mchezo unaofuata dhidi ya timu ya Kagera Sugar, mchezo utakaofanyika siku ya Jumapili katika uwanja wa Kaitaba mjini Bukoba. SOURCE: GLOBAL PUBLISHERS

No comments: