Monday, September 29, 2025

Mwili wa Hayati Askofu Mkuu Rugambwa wapokelewa Bukoba







Mwili wa Hayati Askofu Mkuu Novatus Rugambwa, aliyefariki hivi karibuni, uliwasili leo katika Kanisa Kuu la Bikira Maria wa Huruma, Jimbo Katoliki Bukoba, na kupokelewa kwa heshima kubwa na waumini pamoja na viongozi wa Kanisa Katoliki.

Waumini kwa mamia walijitokeza kuupokea mwili huo, huku ibada maalum ya kumuombea ikiongozwa na viongozi wa Kanisa, ikihudhuriwa pia na viongozi wa Serikali, wawakilishi wa madhehebu mbalimbali pamoja na wananchi.

Katika hotuba zao, viongozi wa dini walimsifu Hayati Askofu Mkuu Rugambwa kwa uongozi wake thabiti, hekima, na moyo wa utumishi uliogusa maisha ya wengi, si tu ndani ya Kanisa, bali pia katika jamii kwa ujumla.

Waumini waliendelea kumwombea marehemu apumzike katika amani ya Bwana, huku taratibu za mazishi zikitarajiwa kuendelea katika siku chache zijazo.

DKT. BITEKO AWAPA HEKO WACHIMBAJI WADOGO WA MADINI



Na Ofisi ya Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati

Serikali imeongeza ushirikishwaji wa Watanzania katika Sekta ya Madini ikiwa ni pamoja na shughuli zote za mnyororo mzima wa thamani wa madini nchini ambapo kwa Mkoa wa Geita pekee wachimbaji wadogo wamezalisha kilo 22,014.61 zenye thamani ya shilingi trilioni 3.443 na Serikali kukusanya mapato ya shilingi bilioni 2.5 katika kipindi cha mwaka 2021/2022 hadi 2024/2025.

Mchango wa wachimbaji wadogo wa madini umeongezeka kutoka asilimia 20 mwaka 2020 hadi kufikia asilimia 40 mwaka 2024 katika mapato yote ya sekta ya madini na mchango wa Sekta ya Madini katika Pato la Taifa umeongezeka kutoka asilimia 6.8 mwaka 2020 hadi kufikia asilimia 10 mwaka 2024.

Akizungumza Septemba 28, 2025 katika viwanja vya Dkt. Samia Suluhu Hassan Bombambili mkoani Geita wakati akifunga Maonesho ya Nane ya Teknolojia na Uwekezaji katika Sekta ya Madini, yenye kauli mbiu “Ukuaji wa Sekta ya Madini ni Matokeo ya Matumizi ya Teknolojia Sahihi na Uongozi Bora/Shiriki Uchaguzi Mkuu Oktoba 2025”. Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Mhe. Dkt. Doto Biteko amewapongeza wachimbaji wadogo na Wizara ya Madini kwa hatua hiyo.

“ Napenda kutoa pongezi maalum kwa Wizara ya Madini kwa usimamizi mzuri wa sekta hii pamoja na wachimbaji wadogo wa Tanzania. Ninyi ni sababu ya kusheherekea mafanikio haya mmekuwa shamba darasa na baada ya Serikali kuwapatia nafasi mmeonesha kwa vitu mlivyofanya mkipewa fursa mnaweza,” Amesema Dkt. Biteko.

Ameendelea “Mmepambana sana kuleta teknolojia ndani ya nchi na mmeonesha Watanzania wanaweza kufanya mambo makubwa na wakafanikiwa,”

Aidha, amesema kuwa tangu kuanza kwa maonesho hayo mwaka 2018 kumekuwepo na mabadiliko makubwa ya kiteknolojia yanayochangia kuongezeka kwa kasi ya uzalishaji madini hasa kwa wachimbaji madini wadogo. Ambapo katika uchenjuaji madini, zimekuwepo teknolojia mbalimbali za kisasa zikiwemo Carbon – In – Leach (CIL), Carbon – In – Pulp (CIP) na Froth Floatation (FF) ambazo zimekuwa na tija zaidi kuliko matumizi ya zebaki ambayo imekuwa na athari nyingi za kiafya na mazingira sambamba na kiwango kidogo cha uzalishaji. 

Dkt. Biteko amesema kufuatia usimamizi thabiti na mabadiliko makubwa ya teknolojia ambayo kwa kiasi kikubwa yamechangiwa na uwepo wa maonesho hayo ya teknolojia, Serikali kupitia Wizara ya Madini imefanikiwa kukusanya kiasi cha Shilingi trilioni 3.8 kwa kipindi cha miaka minne kuanzia mwaka 2020/2021 hadi 2024/2025.

Akizungumzia hatua mbalimballi za Serikali katika kuhamasisha uongezaji thamani madini, Dkt. Biteko amesema kumekuwepo na uanzishwaji wa viwanda vya uyeyushaji na usafishaji wa madini ya dhahabu, nikeli na shaba katika maeneo mbalimbali nchini ambapo kwa sasa kuna jumla ya viwanda nane vya uchenjuaji wa shaba na nickel katika Mkoa wa Dodoma, Kiwanda kimoja cha Uyeyushaji wa Shaba (Chunya) na Viwanda Sita vya Usafishaji wa Dhahabu katika Mikoa ya Geita, Mwanza na Shinyanga-Kahama.

“ Nitoe wito kwa wachimbaji na Wizara kuendelea kubuni na kuongeza uwezeshwaji wa Watanzania kuongeza thamani ya madini wanayozalisha. Mazingira haya yataongeza upatikanaji wa fedha za kigeni pamoja na kuwapatia watanzania ajira kwenye viwanda vya uongezaji thamani, STAMICO mmefanya kazi kubwa sana kubadilisha na kushiriki kwenye local content.” Amesisitiza Dkt. Biteko.

Amewahakikishia kuwa Serikali sikivu inayoongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, itaendelea kuweka mazingira wezeshi kwa ajili ya maendeleo ya sekta ya madini ikiwemo kufikisha huduma ya umeme katika maeneo yote muhimu.

Fauka ya hayo, Dkt. Biteko amewaasa washiriki wa maonesho hayo kushiriki kikamilifu katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2025 kwa kuwa hatua hiyo ni muhimu katika nchi ya kidemokrasia.

Naye, Mkuu wa Mkoa wa Geita, Martin Shigella amemshukuru Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa anayofanya ambapo mwaka jana aliagiza uwanja huo wa maonesho ujengewe miundombinu ya kudumu.

Amesema agizo hilo limetekelezwa na sasa uwanja huo una mabanda tisa ya kudumu ikiwa ni awamu ya kwanza ya ujenzi.

Amesema maonesho hayo kwa mwaka huu yamehudhuriwa na washiriki 930 wakiwemo washiriki kutoka nje ya nchi ikilinganishwa na washiriki 600 mwaka 2024.

Amesema “Rais Samia amewezesha kutoa leseni 9,000 kwa wachimbaji wadogo wakiwemo wa Pori la Kigosi na sasa tumeweza kuzalisha zaidi ya tani 22,000 za madini kwa wachimbaji wadogo,” 

Kwa upande wake, Katibu Mkuu Kiongozi wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, Mhandisi Zena Said amewashauri wadau wa sekta ya madini kwa ujumla kutumia fursa za taasisi za fedha ili kupata elimu kuhusu masuala ya fedha na uwekezaji.

Akimwakilisha Waziri wa Madini, Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini, Msafiri Mbibo amesema maonesho hayo yamekuwa na manufaa mbalimbali ikiwemo kuwa chachu hususan kwa wachimbaji wadogo na kuwaongezea elimu kuhusu uchimbaji hatarishi na matumizi ya zebaki.

Vilevile amesema Wizara ya Madini itahakikisha inasimamia sheria na taratibu zote ili kufanya sekta hiyo kutoa mchango mkubwa katika ukuaji wa uchumi wa nchi.

Mwenyekiti wa Tume ya Madini, Dkt. Janet Lekashingo amesema kuwa hivi sasa sekta ya madini nchini imefikia kiwango cha kushawishi viwanda vya kuzalisha vipuri kuja kuwekeza Tanzania ili vipuri hivyo vipatikane nchini na kufikia lengo la kuwa na Tanzania ya viwanda.

Amebainisha kuwa Tume ya Madini itaendelea kuwezesha sekta ya madini ili kuhakikisha madini yanawanufaisha Watanzania wote.

Mwenyekiti wa Wachimbaji Wadogo, Lenard Bugomola amesema kuwa Mkoa wa Geita umekuwa ukiongoza kwa uzalishaji wa dhahabu, aidha ameomba STAMICO iwapatie mitambo miwili ya uchimbaji madini.

Awali Dkt. Biteko alitembelea mabanda ya mbalimbali yakiwemo Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini, Anglo Gold Ashanti, Shirika la Madini la Taifa (STAMICO), Chama cha Wanawake Wachimbaji Madini Tanzania (TAWOMA), Mwamba Mining ambapo alielezwa kuhusu teknolojia ya kisasa ya uchimbaji madini

WASTAAFU KUPATA HUDUMA MAALUM ZA KIBENKI NA BIMA


Baadhi ya wastaafu na wataalam wa kifedha wakimsikiliza Meneja Mwandamizi wa Mauzo wa Benki ya Stanbic, Priscus Kavishe kwenye kongamano la wastaafu lililoandaliwa na Benki ya Stanbic Tanzania lenye lengo la kutoa huduma za kifedha na bima kwa wastaafu nchini. Kongamano hilo lilifanyika jijini Dar es Salaam juzi.


…………….

Dar es Salaam, Septemba 26, 2025 – Wastaafu na wale wanaokaribia kustaafu nchini Tanzania wamehimizwa kujikita katika mipango thabiti ya kifedha, huduma za bima na uwekezaji ili kujihakikishia maisha yenye heshima na ustawi baada ya kumaliza muda wao wa kazi.

Ujumbe huu ulikuwa lengo kuu la Mkutano wa Wastaafu ulioandaliwa na Benki ya Stanbic, ambao uliwakutanisha wastaafu, wataalam wa kifedha na wadau wa sekta mbalimbali kujadili mbinu kwa vitendo ili kujiandaa kimaisha baada ya kustaafu. Tukio hili ni sehemu ya maadhimisho ya miaka 30 ya Benki ya Stanbic nchini Tanzania, yenye kaulimbiu ‘Miaka 30 ya Kukua Pamoja.’

Mjadala ulijikita zaidi katika akaunti ya Hekima Banking, akaunti maalumu iliyoanzishwa na Stanbic kwa ajili ya watu wenye umri wa miaka 55 na kuendelea. Akaunti hii inawapa wastaafu urahisi wa kufanya miamala, kuweka akiba, kupata mikopo na ushauri wa kifedha na uwekezaji.

Kwa mujibu wa Priscus Kavishe, Meneja Mwandamizi wa Mauzo wa Benki ya Stanbic, mpango huu umetengenezwa ili kuwapa wastaafu usalama na fursa. “Kwa Stanbic Bank, tunaamini kustaafu si mwisho, bali ni mwanzo wa fursa mpya. Kupitia Hekima Banking, tunawapa wastaafu suluhisho za vitendo zitakazowawezesha kuishi kwa heshima, kuwekeza na kuendelea kuchangia kwa maana katika familia na jamii zao,” alisema Kavishe.

Akaunti ya Hekima haina ada za kila mwezi, haina salio la chini, inapatikana kwa sarafu mbalimbali, na inatoa huduma za kidigitali saa 24/7. Wastaafu pia wanaweza kupata mikopo hadi TZS milioni 80 kwa masharti nafuu, huku mafao ya pensheni yakitumika kama dhamana. Aidha, wastaafu wanaweza kuomba bima ya afya pamoja na bidhaa nyingine za bima.

Umuhimu wa bima katika maisha ya kustaafu ulisisitizwa na Naphtal Ntangeki, Afisa wa Bima Stanbic, aliyebainisha kwamba bima ni nguzo muhimu ya mpango wa kifedha. “Kustaafu kwa usalama hakujengwi kwa akiba pekee. Bima inawapa wastaafu ujasiri wa kupanga maisha yao ya baadaye bila hofu ya misukosuko ya kifedha. Kwa Stanbic, tunaunganisha bima katika suluhu zetu ili wastaafu waweze kuishi miaka yao ya baadaye kwa uthabiti na heshima,” alisema Ntangeki.

Washiriki wa mkutano huo walipongeza hatua hii, wakibainisha kuwa imewapa maarifa na mbinu za moja kwa moja. Michael Liymbo kutoka KPMG, aliyeshiriki mkutano huo, alieleza tukio hilo kuwa na manufaa makubwa. “Mkutano wa leo umenifumbua macho. Nimejifunza jinsi akaunti ya Hekima Banking na huduma za bima zinavyoweza kusaidia wastaafu siyo tu kulinda fedha zao, bali pia kuishi maisha yenye heshima. Hatua hii ya Benki ya Stanbic kwa kweli inawanufaisha wataalamu na wastaafu wa baadaye,” alisema Liymbo.

Mkutano wa Wastaafu ni sehemu ya shughuli za mwaka mzima za Stanbic kuadhimisha miaka 30 ya shughuli zake nchini Tanzania. Zaidi ya kusherehekea historia yake, benki inatumia fursa hii kuanzisha suluhisho zinazooana na malengo ya Taifa ya Vision 2050 ya kukuza ujumuishaji wa kifedha, uthabiti na kuboresha maisha ya wananchi wote.

MWANAFUNZI APOKEA KITAMBULISHO CHA TAIFA, AISHUKURU NIDA





Careen Geofrey Erneo, mmoja wa wanafunzi wa Wilaya ya Ilala, ni miongoni mwa wananchi waliojitokeza katika Ofisi ya Usajili ya Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA) kuchukua Vitambulisho vyao, mara baada ya kupokea ujumbe mfupi wa maandishi (SMS) uliowataka kufika ofisini hapo mwishoni mwa wiki iliyopita.

Careen alieleza kuwa hatua hiyo ya kupata Kitambulisho chake kwa wakati ni jambo la kujivunia, kwani kitamrahisishia ushiriki wake katika shughuli mbalimbali za kijamii, kiuchumi na hata kielimu. Alisema kuwa Kitambulisho cha Taifa ni nyenzo muhimu kwa kijana wa kitanzania kwani ndicho kinachomtambulisha kisheria na kumfungulia fursa nyingi za kimaendeleo.

“Ninaishukuru sana NIDA kwa kuhakikisha napata Kitambulisho changu mapema. Hii imenipatia nafasi ya kuwa na uhakika katika masuala ya kitaaluma, kibenki na hata fursa za kijamii ambazo zinahitaji utambulisho rasmi. Kwa kweli, hii ni hatua kubwa kwangu kama kijana,” alisema Careen mara baada ya kukabidhiwa kitambulisho chake.

Aidha, aliwataka vijana wenzake, hususan wanafunzi, kujitokeza kuchukua vitambulisho vyao pale wanapopata taarifa kupitia SMS au tangazo lolote rasmi kutoka NIDA. Alisema kitambulisho hicho si tu kinahitajika kwa ajili ya shughuli za kila siku, bali pia ni nyenzo muhimu katika kujenga mustakabali wa maisha yao.

“Vijana wenzangu ambao bado hawajasajiliwa, nawahimiza wajitokeze kwa wingi ili wapate haki yao hii ya msingi. Kitambulisho cha Taifa ni cheti cha uraia wetu na ni sehemu ya msingi wa maendeleo yetu binafsi na ya taifa kwa ujumla,” alisisitiza.

Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA) kwa sasa inaendelea na jitihada za kuhakikisha wananchi wote wenye sifa wanapata Vitambulisho vyao, ikiwa ni pamoja na kuwasilisha SMS kwa wananchi walio tayari kukabidhiwa vitambulisho vyao, ili kuharakisha mchakato wa upatikanaji wa huduma na kupunguza msongamano katika ofisi zake.

TANAPA YASHIRIKI MAPOKEZI YA MWANARIADHA BINGWA WA DUNIA SAJINI TAJI SIMBU - ARUSHA.










Na. Jacob Kasiri - Arusha

Leo Septemba 29, 2025 TANAPA imeshiriki hafla ya mapokezi ya Bingwa wa Dunia mbio ndefu (Marathon) kilometa 42  Sajini Taji Alphonce Simbu yaliyofanyika  takribani wiki mbili jijini Tokyo - Japan, mapokezi yaliyofanyika katika Uwanja wa Ndege Kisongo jijini Arusha.

Katika mapokezi yaliyoandaliwa na Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), SGT Simbu aliwashukuru TANAPA kwa kushiriki mapokezi hayo na kumuandalia gari alilotumia Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan wakati wa maandalizi ya filamu ya “Tanzania:The Royal Tour”.

Simbu aliongeza kuwa licha ya heshima aliyoipata duniani ya kushinda medali ya Dhahabu katika mbio hizo za km 42, pia TANAPA imempa heshima isiyo kifani kutumia gari aliyotumia Mkuu wa nchi kama filamu yake iliyojizolea umaarufu ndani na nje ya Taifa letu.

Wakati wa kuhitimisha hafla ya mapokezi hayo yaliyofanyika katika uwanja wa mpira wa Sheikh Amri Abeid.

REA yauza majiko 1,500 kwa bei ya ruzuku kwenye maonesho ya Madini Geita



📌REA yapongezwa kwa kuuza majiko kwa bei ya ruzuku na kutoa elimu ya miradi ya wakala

📍Geita

Maonesho ya Nane ya Kitaifa ya Teknolojia ya Madini mkoani Geita yamehitimishwa rasmi na Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Mhe. Dkt. Doto Biteko ambayo yalifunguliwa Septemba 18 na kufikia kilele tarehe 28 Septemba, 2025

Wakala umeshiriki maonesho hayo kwa kutoa elimu ya nishati safi ya kupikia, kutoa elimu ya miradi inayotekelezwa na wakala wa nishati vijijini pamoja na fursa zinazopatikana kwa wakala kama vile vituo vidogo vya mafuta.

Sambamba na hayo Wakala unahamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia kwa kuuza kwa ruzuku mitungi ya gesi ya kilo 6 ambayo inauzwa kwa bei ya 50% ambayo ni kiasi cha shilingi 17,500 ambapo jumla ya mitungi 5,00 imeuzwa kwa ruzuku kwenye maonesho.

Pamoja na hayo, Wakala unafadhili uuzwaji wa majiko banifu yanayotumia mkaa mbadala pamoja na mkaa wa kawaida, majiko hayo yameuzwa kwa bei ya ruzuku ya 85% ambayo ni shilingi 6,195 ambapo bei yake ya kawaida ni shilingi 41,300 ambapo majiko banifu 1,000 yatauzwa kwa bei ya ruzuku katika maonesho hayo. 

Maonesho ya Nane ya Kitaifa ya Teknolojia ya Madini 2025  yamefanyika katika viwanja vya Dkt. Samia Suluhu Hassan, Bombambili mkoani Geita.

WITO WATOLEWA KWA WADAU KUENDELEA KUUNGA MKONO JITIHADA ZA KUPAMBANA NA CHANGAMOTO ZA LISHE NCHINI




Mkurugenzi Mtendaji Taasisi ya Chakula na Lishe Dkt. Germana Leyna  ametoa wito kwa wadu wa masuala ya lishe nchini kuendelea kuunga mkono jitihada za kupambana na changamoto zinazokabili masuala ya Lishe huku akisema kuwa Tanzania imepiga hatua kubwa katika kukabili changamoto hizo kwa kuwa na mikakati madhubuti.

Wito huo umetolewa  leo 29 Septemba, 2025 kwenye mahojiano maalumu katika kipindi cha Jambo Tanzania kinachorushwa na Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC)  Jijini Dar es Salaam katika kuelekea kwenye Mkutano Mkuu wa 11 wa Wadau wa Masuala ya Lishe. 

"Serikali imeendelea kuweka mikakati mbalimabli ikiwemo kuendelea kutoa elimu kwa umma na kuhakikisha jamii inakuwa na uelewa wa masuala ya lishe ili kuendelea kuwa na Taifa lenye watu wenye lishe bora na niseme apa kuwa wadau waje tunganishe nguvu katika kupambana na changamoto za maswala ya Lishe" amesema Dkt Germana Leyna. 

Pia ameongoza kuwa Serikali imejipanga kuhakikisha inawafikia wazalishaji hasa wakulima wawapo  katika shughuli zao za  kilimo na kuhakikisha wanapata elimu ya lishe bora na umuhimu wa kutunza chakula cha matumizi ya nyumbani badala ya kuuza chote.

Ametumia fursa hiyo kutoa rai kwa wadau kuendelea kujitokeza na kuendelea kuweka chachu katika masuala ya lishe nchini.

TANZANIA NA HUNGARY ZAIMARISHA USHIRIKIANO WA KIDIPLOMASIA NA KIMAENDELEO








Dar es Salaam, Septemba 29, 2025 – Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo, amempokea rasmi Waziri wa Mambo ya Nje na Biashara wa Hungary, Mhe. Péter Szijjártó, katika Ofisi Ndogo za Wizara jijini Dar es Salaam.

Katika mazungumzo yao, viongozi hao wawili walisisitiza dhamira ya nchi zao kuendeleza na kuimarisha uhusiano wa kirafiki, kidiplomasia na kiuchumi uliodumu kwa miaka mingi. Mazungumzo ya pande mbili yalihusisha pia mawaziri na wajumbe kutoka Tanzania na Hungary, ambapo maeneo ya ushirikiano katika biashara, elimu, teknolojia, kilimo, na uwekezaji yalijadiliwa kwa lengo la kuleta manufaa kwa wananchi wa nchi zote mbili.

Mhe. Szijjártó yupo nchini kwa ziara ya kikazi ya siku moja inayolenga kuimarisha mashirikiano ya kimaendeleo na kukuza fursa za kiuchumi baina ya Tanzania na Hungary. Ziara hii ni kielelezo cha uhusiano mzuri unaoendelea kujengwa na kuimarishwa baina ya pande mbili, huku ikitarajiwa kufungua njia mpya za ushirikiano endelevu kwa manufaa ya vizazi vya sasa na vijavyo.

Sunday, September 28, 2025

Dodoma kunoga kitalii: Serikali yajipanga kuifanya kitovu cha utalii Kanda ya Kati







Na Mwandishi Wetu, Dodoma

Serikali kupitia Wizara ya Maliasili na Utalii imeanza kutekeleza mkakati kabambe wa kuboresha vituo vya utalii vilivyopo jijini Dodoma na Kanda ya Kati kwa ujumla, ili kuviinua kufikia hadhi ya kimataifa.

Mkakati huo unalenga kuimarisha miundombinu na huduma za kitalii katika maeneo ya Mkungunero, Hifadhi ya Swaga Swaga na Kituo cha Michoro ya Miambani cha Irangi kilichopo Kolo, wilayani Kondoa.

Akizungumza wakati wa ziara maalumu ya kitalii katika Kituo cha Michoro ya Miambani Kondoa Irangi, Kaimu Mkurugenzi wa Sehemu ya Uendelezaji Utalii katika Wizara ya Maliasili na Utalii, Dainess Kunzugala, alisema utekelezaji wa mkakati huo unafanyika kwa ushirikiano na Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS), Bodi ya Utalii Tanzania (TTB) na wadau binafsi wa sekta ya utalii.

Alisema lengo ni kuhakikisha vituo hivyo vinatimiza vigezo vitano muhimu vya kimataifa ambavyo ni: miundombinu bora ya barabara, vifaa na huduma muhimu za utalii, hoteli za kisasa kuanzia nyota tatu, huduma kamili za kijamii na uwepo wa bidhaa pamoja na shughuli mbalimbali za kitalii zikiwemo burudani kwa familia na watoto.

*Ziara ya maadhimisho ya Siku ya Utalii Duniani*

Ziara hiyo, iliyopewa jina la “Nyama Choma Bata Pori”, iliratibiwa na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Dodoma kwa kushirikiana na kampuni ya Epic Adventures, TTB na TFS ikiwa sehemu ya maadhimisho ya Siku ya Utalii Duniani.

Mkurugenzi wa Epic Adventures, Joel Massai, alisema kampuni yake iliandaa ziara hiyo kuunga mkono jitihada za Rais Samia Suluhu Hassan katika kukuza sekta ya utalii nchini.

“Dodoma imebarikiwa vivutio vya kipekee vinavyohitaji jitihada za pamoja kati ya serikali na sekta binafsi ili kuviboresha na kuvitangaza,” alisema Massai.

*Wajibu wa TFS na TTB*

Kwa upande wake, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa TFS Kanda ya Kati, Mathew Kiondo, alisema Wakala unatekeleza mikakati mbalimbali kuboresha vivutio vya utalii vilivyopo katika kanda hiyo.

“Baadhi ya vivutio ikiwemo Mlima Hanang na michoro ya kale ya Kondoa Irangi vipo kwenye mapori ya akiba ambayo TFS inaendelea kuyaendeleza na kuyahifadhi ili kuchochea utalii wa mazingira,” alisema Kiondo.

Naye George Mwagane, Afisa Utalii Mwandamizi wa TTB Kanda ya Kati, alisema Bodi inatekeleza programu maalumu za kutangaza vivutio vya Dodoma kitaifa na kimataifa, huku miradi mikubwa kama Reli ya Umeme ya Mwendokasi (SGR) na uwanja wa ndege wa kimataifa wa Msalato ukiwa chachu ya kukuza utalii mkoani humo.

“Tunajipanga kuhakikisha dunia ya utalii inafika Dodoma,” alisema.

*Ongezeko la watalii Kondoa Irangi*

Meneja wa Kituo cha Michoro ya Miambani Kondoa Irangi, Zuberi Mabie, alisema uwekezaji wa serikali umechangia ongezeko kubwa la wageni wanaotembelea kituo hicho cha kihistoria.

Alisema idadi ya watalii wa ndani imeongezeka kutoka 1,287 mwaka 2018 hadi 7,654 mwaka 2024, huku watalii wa kimataifa wakipanda kutoka 171 mwaka 2020 hadi 541 mwaka 2024.

“Sababu kuu za mafanikio haya ni pamoja na kuboreshwa kwa barabara, huduma bora za kijamii na matangazo ya kitaifa na kimataifa,” alisema Mabie.

*Maadhimisho ya mwaka huu*

Siku ya Utalii Duniani kwa mwaka huu iliadhimishwa Septemba 27 kwa kauli mbiu “Utalii na Maendeleo Endelevu.” Zaidi ya washiriki 40 kutoka ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, TFS, TTB na taasisi binafsi walihudhuria ziara ya siku mbili katika kituo hicho cha kihistoria kilichopo Kolo, Kondoa.

MRADI WA TACTIC KUBDIDLISHA TASWIRA YA MANSPAA YA MOSHI-NURDIN BABU









 Ataka Kasi na Ubora katika utekelezaji wake 

Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro Mhe. Nurdin Hassan Babu amesema ni matarajio yake kuwa utekelezaji wa mradi wa uendelezaji Miji Tanzania TACTIC kwa Manispaa ya Moshi utaleta mabadiliko chanya kwa wananchi na wageni ambao watafaidi huduma za usafiri na usafirishaji pamoja na mazingira bora ya shughuli za kiuchumi kwa kuongeza thamani ya maeneo na kukuza pato la Halmashauri ya Manispaa ya Moshi.

Mkuu huyo wa Mkoa ameyaeleza hayo mara baada ya kushuhudia utiaji saini wa Mkataba wa ujenzi wa Miradi ya TACTIC katika Manispaa ya Moshi leo Septemba 27, 2025 kwenye Viwanja vya shule ya Msingi Msaranga, mradi ukihusisha ujenzi na uboreshaji wa miundombinu ya barabara, mitaro ya kutiririsha maji ya mvua pamoja na jengo la usimamizi, vyote vikigharimu Shilingi Bilioni 22.9.

"Jukumu letu ni kuitunza miundombinu hii itakayojengwa kwa gharama kubwa ili iweze kudumu kwa muda uliotarajiwa. Nitoe Rai kwa Mkandarasi kuhakikisha kazi hii inafanyika kwa haraka, ubora uliokusudiwa na kukamilika kwa wakati ili wananchi waanze kunufaika na miundombinu hii ambayo Serikali imewekeza katika Manispaa yetu." Amenukuliwa akisema Mhe. Babu.

Katika maelezo yake, Mhe. Babu amemuagiza Mkurugenzi Mkuu na Mameneja wa TARURA pamoja na Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji wa Moshi kusimamia kikamilifu miradi hiyo kwa kutumia rasilimali watu na vifaa vilivyopo, akitaka Mkandarasi kupewa ushirikiano wa karibu kwa kuzingatia muundo wa utekelezaji wa mradi wa TACTIC unaojumuisha wataalamu wa pande zote.

Babu ameeleza kuwa Serikali ya awamu ya sita imekuwa ikichukua hatua mbalimbali zenye lengo la kuboresha maisha ya wananchi kwa kupitia miradi mbalimbali ikiwemo TACTIC yenye kuboresha miundombinu ya usafiri na usafirishaji, ujenzi wa masoko na vituo vya Mabasi pamoja na utunzaji wa mazingira.

Jumla ya Gharama ya mradi huo ikiwa ni Dola za Marekani Milioni 410, ikitekelezwa kwenye Miji 45 ya Tanzania

Mwili wa Hayati Askofu Mkuu Rugambwa wapokelewa Bukoba

Mwili wa Hayati Askofu Mkuu Novatus Rugambwa, aliyefariki hivi karibuni, uliwasili leo katika Kanisa Kuu la Bikira Maria wa Huruma, Jimbo Ka...