Monday, March 20, 2006

Kumbe tunaweza, mkoloni hakukosea kutuchapa viboko

KADRI ninavyoendelea kutaabika kama walivyo Watanzania wengi, kusota na kuhofia kesho baada ya leo kupita kimkanda mkanda, ninakaribia kushawishika kuwa utawala wa kusukumana kwa viboko ndiyo hasa unafaa kusukuma maisha.

Naaamini ile hadithi kwamba, wakoloni hasa wa Kijerumani walikuwa wakiwashurutisha wasiotaka kufanya kazi kwa kuwatandika henzerani nyingi tena hadharani umeisikia na pengine imekuwa ikikugusa kwa namna moja au nyingine.

Kwa taarifa yako, hulka hiyo ya wakoloni ilipewa jina baya kabisa na ndiyo maana baada ya kupata uhuru ililaaniwa kwa nguvu zote, ingawa kwa mtazamo wangu ukweli unabaki pale pale kwamba, viboko viliwezesha mambo mengi kusonga mbele.

Hebu angalia, tulijengewa reli ambayo inatumika hadi leo, tulijengewa nyumba ambazo mpaka leo kila unapokwenda makao makuu ya karibu kila mkoa au wilaya utayakuta na yanatumika, miundombinu mingi kama barabara, madaraja, minara ya simu, mabomba ya maji yanatokea enzi hizo ingawa sikubaliani nao kwa ubabe wao, lakini walichofanyika kimeonekana.

Sijui hawa walikuwa wakifuata zile nadharia za baba wa menejimenti aliyevuma miaka ya sitini, Douglas McGregor aliyevumbua nadharia X na Y ambapo alijenga dhana kuwa kwa kawaida mwanadamu hapendi kufanya kazi na hujitahidi kukwepa kadri awezavyo.

Kutokana na binadamu kutopenda kazi akasema, watu wengi ni lazima wadhibitiwe na kutishwa kabla ya kuwa tayari kufanya kazi kwa ridhaa zao. Na kuwa mtu wa kawaida anapenda sana kuelekezwa, huchukia majukumu, ni mtata na hupenda sana kuhakikishiwa usalama wake.

Nadharia Y inadhania udhibiti, adhabu na vitisho siyo njia pekee inayowafanya watu kuchapa kazi na kwamba mtu atajielekeza mwenyewe kama atajituma kutekeleza malengo ya taasisi au kampuni husika.

Anaendelea kusisitiza kuwa, kama mazingira ya kazi yanaridhisha, basi matokeo yake itakuwa watu kujituma kwa kampuni, jumuiya. Kwa dhana hii kikawaida mtu anajifunza katika mazingira ya kawaida, fikra na utundu vinaweza kutumika kupata suluhisho la matatizo ya idadi kubwa ya waajiriwa.

Fikra zake hizi ndizo bila shaka zinatumika sasa, na bila shaka zinatoa mafanikio kwa pande zote mbili moja ikiwa ni ile inayotumia adhabu na udhibiti wa kina na ya pili ni ile inayovumilia uvivu na kutopenda kufanya kazi.

Ingawa zote hizi mbili zina upungufu wake sababu binadamu anahitaji mengi zaidi ya adhabu na vitisho, mathalani anahitaji motisha ya kipato cha fedha kazini na pia anahitaji kuenziwa.

Kwa kuzingatia hayo ya hapo juu, ninaposema viboko sina maana ya viboko halisi ninamaanisha maamuzi makali yasiyotania kuona aibu wala kutaka sifa kwa upande mmoja, yanayoangaliwa walala hoi wanapata nini wanaishi vipi na wanasikilizwa vipi.

Kipindi cha miezi michache iliyopita kuwapo katika ofisi ya juu kwa maana ya uwaziri, ukatibu mkuu au nafasi nyingine ilikuwa ni sawasawa na kuingia likizo, kula kuku, watu walijifanya mambo walivyoweza hawakuhofia lolote na hata kama walikuwa na hofu ya kuharibu basi walikuwa nayo kidogo mno.

Imefika kipindi cha Jakaya Kikwete huyu ndiye Rais wa sasa ambaye staili yake ya kuongoza ni tofauti kabisa na staili za viongozi waliopita kwa maana kwamba staili yake inazingatia kurekebisha hali za masikini.

Watu wale wale waliokuwa katika ofisi zile zile na waliopata mafunzo yale yale ya kazi wameibuka na kuanza kucharuka, dalili zinaanza kuonyesha kwamba kumbe watu wanaweza kufanya kazi. Wanaweza kutekeleza majukumu yao kama wakitiwa hofu, wakionyeshwa njia, wakielekezwa.

Ukijiuliza nini kimewafanya kuamka namna hii jibu lake bila shaka utakuwa na mlolongo wa visingizio, labda ni kwa sababu ya kuogopa uongozi au wanaogopa adhabu ya kupoteza unga unaowafanya kuishi mijini au wameridhishwa sana na mazingira.

No comments: