Tuesday, August 30, 2016

Maonesho ya Biashara ya Afrika Mashariki yafunguliwa rasmi Jijini Mwanza

Mkuu wa Wilaya ya Ilemela mkoani Mwanza, Dkt.Leonard Massale, hii leo akifungua Maonesho ya Biashara ya Afrika Mashariki yanayofanyika Jijini Mwanza. 

Maonesho hayo yameandaliwa na Chemba ya Wafanyabiashara wenye Viwanda na Kilimo nchini TCCIA, yalianza Agosti 26,2016 na yanatarajiwa kufikia tamati Septemba 04,2016 katika viwanja wa Rock City Mall.
Mkuu wa Wilaya ya Ilemela mkoani Mwanza, Dkt.Leonard Massale, akizungumza kwenye Maonesho ya Biashara ya Afrika Mashariki yanayofanyika Jijini Mwanza. 
Mwenyekiti wa TCCIA mkoa wa Mwanza, Elibariki Mmari, akizungumza kwenye Maonesho ya Biashara ya Afrika Mashariki yanayofanyika Jijini Mwanza. 
Mwenyekiti wa TCCIA mkoani Mara, akizungumza kwenye Maonesho ya Biashara ya Afrika Mashariki yanayofanyika Jijini Mwanza. 
Viongozi mbalimbali wakiwa kwenye wa Maonesho ya Biashara ya Afrika Mashariki yanayofanyika Jijini Mwanza. 
Viongozi mbalimbali wakiwa kwenye wa Maonesho ya Biashara ya Afrika Mashariki yanayofanyika Jijini Mwanza. 
Viongozi mbalimbali wakiwa kwenye wa Maonesho ya Biashara ya Afrika Mashariki yanayofanyika Jijini Mwanza. 
Picha ya pamoja.

Wafanyabiashara katika nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki wamehimizwa kuchangamkia fursa za kibiashara na uwekezaji zilizopo katika soko la pamoja la nchi hizo kutokana na soko hilo kuwa na idadi kubwa ya wateja.
Akifungua maonesho ya 11 ya biashara ya Afrika Mashariki yanayofanyika kwenye viwanja vya Rock City Mall jijini Mwanza,Mkuu wa mkoa wa Mwanza John Mongela amesema soko lililopo kwenye nchi hizo lina zaidi ya wateja milioni 140 na hivyo likitumika vizuri litatoa fursa ya kuuziana bidhaa wenyewe kwa wenyewe.
Kwenye hotuba ya ufunguzi iliyosomwa na Mkuu wa wilaya ya Ilemela Dkt.Leonard Massale,mkuu huyo wa mkoa amesema badala  ya wafanyabiashara hao kutegemea masoko ya nje yanayofikika kwa gharama kubwa,wanapaswa kuuziana bidhaa ndani ya nchi za Afrika Mashariki na hivyo kuinua uchumi wa nchi hizo.
Aidha amewahimiza waandaaji wa maonesho hayo chemba ya wafanyabiashara, wenye viwanda na kilimo nchini, TCCIA, kuyatangaza zaidi ili yavutie makampuni mengi kutoka nchi zingine.
Katika hotuba yake Mwenyekiti wa TCCIA mkoa wa Mwanza, Elibariki Mmari, amesema licha ya kuandaa maonesho hayo kwa miaka 11 mfululizo bado wanakabiliwa na changamoto ya kutokuwa na eneo linalofaa kwa ajili ya maonesho hayo na hivyo kulazimika kuhama mara kwa mara na kuiomba serikali kuharakisha upimaji wa eneo la maonesho Nyamuhongolo ili kujenga majengo ya kudumu.
Maonesho ya mwaka huu yanashirikisha zaidi ya washiriki 300 kutoka nchi mbalimbali zikiwemo Kenya, Uganda, China na wenyeji Tanzania ambapo kuna mabanda ya bidhaa mbalimbali pamoja na wanyama hai.
Bonyeza HAPA Kujua Zaidi

Profesa Mbarawa: Serikali haijakurupuka kununua ndege za Bombadier Q400

index-60-768x512
Na Abushehe Nondo na Sheila Simba.
MAELEZO
Dar es Salaam
Serikali imesema kuwa iliamua kununua ndege mbili za abiria aina ya Bombadier Q400 kutoka nchini Canada kutokana na uhitaji wa huduma ya usafiri wa anga kwa safari za ndani ya nchi na mazingira halisi ya viwanja vya ndege vilivyopo nchini.
Hayo yamesemwa leo Jijini Dar es Salaam na Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa wakati wa ufunguzi wa mafunzo ya wakufunzi wa marubani katika chuo cha Taifa cha usafirishaji(NIT)  
Mbarawa alisema kuwa Serikali haikukurupuka katika kufanya maamuzi ya aina ya ndege za kununua badala yake imezingatia vigezo na malengo mahsusi ya kuhudumia usafiri wa ndani na kuboresha usafiri wa anga kupitia Shirika la Ndege Tanzania (ATCL).
“Serikali imeamua kununua aina hii ya ndege za Bombadier Q400 kutokana na hali halisi ya Viwanja vya ndege nchini kuwa vya Changarawe na lami kwa baadhi, huku lengo ni kutoa huduma za usafiri wa ndani” Alisema Profesa Mbarawa.
Mbarawa aliwataka Watanzania kuelewa nia ya Serikali yao ni kuhudumia wananchi hivyo watu wasipotoshe ukweli kuhusu ndege hizo kwani zimezingatia mambo mbalimbali ikiwemo suala la usalama na ufanisi katika uendeshaji wake.
Aliongeza kuwa ndege hizo zina uwezo wa kutua katika viwanja vingi hapa nchini kwani zinaweza kutua katika viwanja vyenye urefu wa kilomita 1.5 ambavyo ndio vingi nchini tofauti na aina nyingine ambazo hutua kwenye viwanja vyenye urefu zaidi ya kilomita mbili.
Prof. Mbarawa alibainisha sababu nyingine kuwa ni aliongeza uwezo mdogo wa ndege hizo katika kutumia mafuta ukilinganisha na aina zingine ambapo kwa safari ya kutoka Dar es Salaam hadi Mwanza zitakuwa zikitumia Tani 1.7 za mafuta tofauti na aina nyingine zinazotumia hadi Tani 2.8 kwa safari moja.
Waziri Mbarawa pia alitumia fursa hiyo kukanusha uvumi ulionezwa kuwa ndege hizo zimenunuliwa katika kampuni ndogo isiyokuwa na sifa na kubainisha kuwa suala hilo siyo la kweli kwani kampuni hiyo imefanya biashara na nchini nyingi ikiwemo Ethiopia yenye ndege t19 aina ya Bombadier Q400 zilizotengezwa na  Kampuni hiyo.
Mpaka sasa tayari Serikali imeshafanya malipo ya ununuzi wa ndege hizo kwa asilimia 40 ambapo ndege hizo zinatarajiwa kuwasili nchi tarehe 19 septemba mwaka huu ambapo zitaanza safari ya kutoka nchini Canada tarehe 15 septemba mwaka huu kupitia nchini Uingereza.
Akizindua mafunzo hayo ya wakufunzi wa  marubani, Waziri Mbarawa aliwaasa Marubani ambao watahitimu mafunzo hayo  kuhakikisha wanazingatia suala na nidhamu na uadilifu katika sekta hiyo ya usafiri wa anga.
“Hatutaki kuwa na marubani ambao wana uwezo wa kazi lakini sio waadilifu,hakikisheni mnawafundisha marubani wanafunzi kuzingatia nidhamu na uadilifu katika sekta hiyo ya anga ambapo wakati mwingine Rubani anajijua anakasoro lakini bado anang’ang’ania kurusha ndege” alisema Prof.Mbarawa.
Aidha amesema kuwa Serikali itashirikiana na chuo hicho katika kutoa kozi za urubani ili kuakabiliana na changamoto ya ukosefu wa marubani nchini.

WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII PROSESA MAGEMBE AZINDUA RIPOTI YA MAPENDEKEZO YA KUBORESHA UTAWALA WA MISITU NCHINI TANZANIA

Waziri wa Maliasili na Utalii, Profesa Jumanne Maghembe(katikati) akizindua ripoti ya matokeo ya utafiti pamoja na mapendekezo ya kuboresha utawala wa misitu nchini Tanzania, Wa kwanza kulia ni Mwakilishi wa Bodi ya Jumuiko la Maliasili Tanzania( TNRF), Charles Meshack na kulia ni Msaidizi wa Balozi wa Finland nchini Tanzania, Simo-Pekka Parviainen
Msaidizi wa Balozi wa Finland nchini Tanzania, Simo-Pekka Parviainen akizungumza jambo wakati wakuzindua ripoti ya uvunaji wa misitu pamoja na kujadili ripoti hiyo
  Mwakilishi wa Bodi ya Jumuiko la Maliasili Tanzania( TNRF), Charles Meshack akizungumza jambo wakati wa kongamano lililowahusisha wadau mbalimbali wa misitu ili kujadili ripoti ya uvunaji wa misitu nchini Tanzania.
Mtafiti na Mshauri wa masuala ya Misitu, Kihana Lukumbuzya akiwasilisha ripoti ya uvunaji wa misitu kwa waziri wa Maliasili na Utalii pamoja na wadau mbalimbali wa masuala ya misitu(hawapo pichani) katika ukumbi wa Utalii leo jijini Dar es Salaam
   Waziri wa Maliasili na Utalii Profesa Jumanne Maghembe(wa kwanza kushoto) pamoja na wadau mbalimbali wakifuatilia uwasilishwaji wa ripoti ya uvunaji wa misitu iliyokuwa ikiwasilishwa na Mtafiti na Mshauri wa masuala ya Misitu, Kihana Lukumbuzya.Baadhi ya wadau wakifuatilia mada
 
Mkurugenzi wa Jumuiko la Maliasili Tanzania( TNRF), Joseph Olila akizungumza na waandishi wa habari kuhusu mapendekezo yaliyopatikana katika utafiti pamoja na kuboresha utawala wa misitu nchini Tanzania.
Baadhi ya wadau wa misitu wakifuatilia mada kwenye kongamano hilo lililofanyika leo jijini Dar es Salaam
 
Picha ya Pamoja

WAKWEPAKODI WANAIATHIRI SERIKALI-WAZIRI MKUU

index

WAZIRI MKUU, Kassim Majaliwa amesema wafanyabiashara wanaokwepa kulipa kodi wanaiathiri Serikali katika juhudi zake za kuboresha maisha ya Watanzania.
Amesema Serikali haina mgogoro na wafanyabiashara bali inawataka walipe kodi na kama kuna wanaonewa na watendaji wa chini kwa kubambikiziwa kodi watoe taarifa juu ya jambo hilo.
Waziri Mkuu ametoa kauli hiyo leo (Jumanne, 30 Agost, 2016) wakati akizungumza na Mkurugenzi Mtendaji wa Makampuni ya Mohamed Enterprises Tanzania Limited (MeTL), Mohamed Dewji, ofisini kwake jijini Dar es Salaam.
Amesema Serikali imedhamiria kuwaunga mkono wafanyabiashara katika shughuli zao ili waweze kulipa kodi itakayoifanya imudu kuwahudumia wananchi katika huduma mbalimbali za jamii.
“Sisi msisitizo wetu ni ulipaji kodi, wakwepa kodi wanatuathiri. Sekta nyingine zinashindwa kuendelea kwa sababu hazina mtaji na kodi hazipatikani vizuri,” amesema.
Amesema “Ninyi timizeni wajibu wenu kwa kulipa kodi stahiki, tutawasaidia katika kufanya biashara zenu. Tutawasaidia katika kusimamia mambo yenu ila mjue kwamba nchi hii bila viwanda hatuwezi kwenda,”.
Pia amewataka wafanyabiashara kwenda kujenga viwanda katika maeneo ambayo malighafi zinazalishwa ili kuwahamasisha wakulima kuzalisha zaidi na kuwapunguzia mzigo wa kusafirisha malighali hizo.
Kwa upande wake Dewji amemuhakikishia Waziri Mkuu kwamba wafanyabiashara wanaiunga mkono Serikali ya Awamu ya Tano na   hawana mpango wowote wa kuhamishia mitaji yao nje ya nchi kama inavyodaiwa na baadhi ya watu.
“Huu ni uongo na uzushi tu ambao watu wameamua kuusambaza, mfano mimi mwenyewe nimeanza kuongeza mitaji katika biashara zangu. Nimefufua kiwanda cha kuchambua pamba cha Chato. Nafungua biashara zingine mpya kubwa ikiwemo ya kufufua kiwanda cha nguo cha Musoma ambacho kitakuwa kinatengeneza jeans za kuuza nje ya nchi,” amesema.
Amesema yuko tayari kuwekeza kwenye ujenzi wa kiwanda cha sukari katika wilaya ya Rufiji mkoani Pwani. Kiwanda hicho kitakuwa na uwezo wa kununua miwa tani milioni 1.2 zitakazozalisha tani 120,000 za sukari kwa mwaka.
Mkurugenzi huyo amesema amepanga kuwekeza sh. bilioni 40 kwa ajili ya kukuza uzalishaji katika mashamba yake ya mkonge kwenye mikoa ya Pwani, Tanga na Morogoro.
Pia amewekeza sh. bilioni 70 katika viwanda vya kusaga unga wa ngano na sembe na anatarajia kununua tani laki moja za mahindi katika msimu wa mwaka huu.
Mbali na kuwekeza katika viwanda hivyo Dewji amesema anatarajia kujenga kiwanda kikubwa cha kutengeneza sabuni ya unga ambacho kitakuwa ni kikubwa kuliko vyote katika nchi za Afrika Mashariki na Kati.
“Tumeamua kuongeza uwekezaji katika viwanda ili kuunga mkono mkakati wa Serikali wa kuifanya Tanzania kuwa nchi ya viwanda. Vile vile nimefanikiwa kuishawishi kampuni kubwa na maarufu ya kutengeneza sigara duniani ya Marlboro kuingia nayo ubia na sasa tunajenga kiwanda cha sigara hizo mjini Mrogoro,” amesema.

MAKAMU WA RAIS MHE. SAMIA SULUHU AHUDHURIA UFUNGUZI WA MKUTANO WA 36 WA SADC MJINI MBABANE SWAZILAND

 Mfalme Mswati wa III (kushoto) akihutubia kwenye ufunguzi wa mkutano wa 36 wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa SADC kwenye ukumbi wa Mandvulo, Lozitha Swaziland.
 Binti akionyesha bendera ya Tanzania wakati wa kuimba shairi maalum ya ufunguzi wa mkutano wa 36 wa SADC
 Wakuu wa nchi na Serikali wa Jumuiya ya Maendeleo ya Nchi za Kusini mwa Afrika (SADC) wakiwa kwenye picha ya pamoja mara baada ya ufunguzi wa mkutano wa 36, Lozitha Swaziland.
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akisaini ubao wa kumbukumbu kwa niaba ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. John Pombe Magufuli wenye majina ya viongozi waliohudhuria mkutano wa 36 wa SADC uliofanyika Lozitha, Mbabane Swaziland.

NMB yawakumbuka watoto wenye usonji, yawapa msaada wa vifaa vya masomo

Pamoja na kuwa bora utoaji wa huduma za kibenki lakini pia benki ya NMB imejipanga kuhakikisha inakuwa pia bora katika kusaidia jamii na katika kudhihilisha hilo imetoa msaada wa vifaa vya kutumia darasani na vya michezo kwa watoto walio na usonji (autism) ambao wanasoma katika shule ya msingi Mbuyuni, iliyopo Manispaa ya Kinondoni, Dar es Salaam.

Akielezea kuhusu msaada huo, Meneja wa Kanda ya Dar es Salaam wa NMB, Bi. Vicky Bishubo alisema wameamua kutoa msaada kwa shule hiyo kwa ajili ya kuwasaidia watoto wenye usonji kusoma katika mazingira mazuri hasa kutokana na hali zao jinsi zilivyo.
Meneja wa Kanda ya Dar es Salaam wa NMB, Bi. Vicky Bishubo akizungumza wakati wa kukabidhi vifaa vya shuleni kwa wanafunzi wa usonji katika shule ya Msingi Mbuyuni.

"NMB kila mwaka tunatenga asilimia moja ya faida ambayo tunaipata katika kusaidia jamii, tumeshatoa misaada mingi kama madawati na sasa tuliona tuwasaidie watoto hawa na tunaamini msaada wetu utaweza kuwasaidia kwa kiasi kikubwa," alisema Bi. Bishubo.

Kwa upande wa mgeni rasmi katika makabidhiano ya msaada huo, Kamishna wa Ustawi wa Jamii kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu, Rabikira Mushi aliwashukuru NMB kwa msaada ambao wamewapatia shule ya Mbuyuni na kuwataka kuendelea kuwa na moyo huo kwa kutoa msaada katika shule zingine zilizo na mahitaji.
Mgeni rasmi katika makabidhiano ya msaada huo, Kamishna wa Ustawi wa Jamii kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu, Rabikira Mushi akiwashukuru NMB kwa msaada ambao wamewapatia ambao unakadiriwa kuzidi Milioni 7.

Alisema licha ya serikali kufanya jitihada mbalimbali lakini bado inahitaji wadau wengine wa kusaidiana na kama kunakuwa na wadau kama NMB ambao wanajitoa kusaidia jamii basi wanakuwa wadau wa ukweli ambao wanaunga mkono juhudi za serikali kuleta maendeleo.

"Kwa nia yenu ya kusaidia jamii basi nyie mnaipatia kabisa serikali sababu inajitahidi kuleta elimu bora na hata kwa watoto hawa ambao bado kuna changamoto ya vifaa kwahiyo sisi tuwashukuru kwa msaada wenu na msisite tena kutusaidia siku tukiwafata kwa kuomba msaada," alisema Mushi.

Na Rabi Hume, MO BLOG
Mwalimu Mkuu wa Shule ya Msingi Mbuyuni, Dorothy Malecela akitoa neno la shukrani kwani niaba ya uongozi wa shule na wanafunzi. (Picha zote na Rabi Hume - MO BLOG)

Mgeni rasmi katika makabidhiano ya msaada huo, Kamishna wa Ustawi wa Jamii kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu, Rabikira Mushi akimshukuru Meneja wa Kanda ya Dar es Salaam wa NMB, Bi. Vicky Bishubo kwa msaada ambao wamewapatia.
Mgeni rasmi katika makabidhiano ya msaada huo, Kamishna wa Ustawi wa Jamii kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu, Rabikira Mushi na Meneja wa Kanda ya Dar es Salaam wa NMB, Bi. Vicky Bishubo wakicheza na wanafunzi wa Shule ya Msingi Mbuyuni.

Mgeni rasmi katika makabidhiano ya msaada huo, Kamishna wa Ustawi wa Jamii kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu, Rabikira Mushi akipokea vifaa vya michezo kutoka kwa Meneja wa Kanda ya Dar es Salaam wa NMB, Bi. Vicky Bishubo ambavyo vitatumiwa na wanafunzi wa Shule ya Msingi Mbuyuni.
Mwonekano wa baadhi ya vifaa vya michezo ambavyo NMB imetoa msaada kwa Shule ya Msingi Mbuyuni.

RAIS DKT MAGUFULI AKUTANA NA MABALOZI WA CUBA NA INDIA IKULU DAR ES SALAAM LEO

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt John Pombe Magufuli akifanya  mazungumzo na balozi wa Cuba Mhe Jorge Lopez Tormo nchini Ikulu jijini Dar es salaam leo Agosti 30, 2016.

 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt John Pombe Magufuli akisalimiana na balozi wa India nchini Mhe.Sandeep Arya aliyekutana naye na kufanya mazungumzo Ikulu jijini Dar es salaam leo Agosti 30, 2016.
 Katibu Mkuu Wizara ya Viwanda na Biashara, Dkt. Adelhem Meru akisalimiana na balozi wa Cuba nchini Mhe Jorge Lopez Tormo kabla ya kufanya naye  mazungumzo Ikulu jijini Dar es salaam leo Agosti 30, 2016, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt John Pombe Magufuli (aliye nyuma).
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt John Pombe Magufuli akimsindikiza  balozi wa India nchini Mhe.Sandeep Arya aliyekutana naye na kufanya mazungumzo Ikulu jijini Dar es salaam leo Agosti 30, 2016.



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli amewaalika wafanyabiashara wa Cuba na Serikali ya nchi hiyo kuja hapa nchini kuwekeza katika uzalishaji wa sukari na kujenga viwanda vya kutengeneza dawa za binadamu.

Rais Magufuli ametoa mwaliko huo leo tarehe 30 Agosti, 2016 Ikulu Jijini Dar es Salaam alipokutana na kufanya mazungumzo na Balozi wa Cuba hapa nchini Mhe. Jorge Lopez Tormo.

Dkt. Magufuli amemhakikishia Balozi Jorge Lopez Tormo kuwa Serikali yake itatoa ushirikiano wa kutosha endapo mfanyabiashara yeyote wa Cuba au Serikali yenyewe ya Cuba itajitokeza kuwekeza katika uzalishaji wa sukari na utengenezaji wa dawa za binadamu, na kwamba licha ya Tanzania kuwa na mahitaji makubwa ya bidhaa hizo kuna nchi nyingi jirani na Tanzania zitanufaika.

"Mhe. Balozi ukiniletea huyo mwekezaji hata kesho nitamkabidhi shamba la kuzalisha miwa na kujenga kiwanda cha kuzalisha sukari mara moja ili uzalishaji uanze, tunataka kumaliza tatizo la sukari, uzalishaji wa sasa wa sukari hautoshelezi mahitaji yote ya Tanzania na pia majirani zetu wana upungufu wa sukari" Amesema Rais Magufuli na kuongeza kuwa yapo maeneo mengi yanayofaa kwa kilimo cha miwa likiwemo eneo la Bagamoyo ambako kuna hekta takribani 10,000.

Hali kadhalika Rais Magufuli amesema Serikali ipo tayari kutoa ardhi kwa mwekezaji yeyote kutoka Cuba atakayekuwa tayari kujenga kiwanda cha kutengeneza dawa za binadamu na vifaa tiba hapa nchini.

Kwa upande wake Balozi Jorge Lopez Tormo amempongeza Rais Magufuli kwa juhudi kubwa anazozifanya katika uendeshaji wa Serikali na amemhakikishia kuwa Cuba itaendeleza na kuimarisha uhusiano na ushirikiano mzuri na wa kihistoria uliopo kati yake na Tanzania, na ameahidi kufanyia kazi yote waliyoyazungumza.

Wakati huo huo, Rais Magufuli amekutana na kufanya Mazungumzo na Balozi wa India hapa Nchini Mhe. Sandeep Arya ambapo Balozi huyo ametoa taarifa ya hatua zinazoendelea kuchukuliwa baada ya ziara ya Waziri Mkuu wa India Mhe. Narendra Modi iliyofanyika Mwezi Julai mwaka huu.

Katika mazungumzo hayo Balozi Sandeep Arya amesema wawekezaji kutoka India wanaendelea na majadiliano na Shirika la Maendeleo ya Petroli (TPDC) juu ya utekelezaji wa mradi wa kusambaza gesi majumbani kwa ajili ya matumizi ya wananchi na pia wanajadiliana na Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi juu ya kuongeza uzalishaji wa mazao ya jamii ya kunde ili kulisha soko kubwa la mazao hayo nchini India.

Kuhusu ujenzi wa kiwanda cha magari cha Tata, Balozi Sandeep Arya amesema mchakato unaendelea na kwamba tayari wameoneshwa eneo la kujenga kiwanda hicho lililopo Kibaha Mkoani Pwani na matarajio ni kuwa ujenzi wa kiwanda hicho utakamilika mwaka ujao.

Kwa upande wake Rais Magufuli ameelezea kufurahishwa na uwepo wa miradi hiyo itakayoleta manufaa kwa pande zote mbili yaani Tanzania na India na ametoa wito kwa pande zote kuharakisha majadiliano ili utekelezaji wa miradi hiyo uanze haraka.

Aidha, Rais Magufuli amewakaribisha wawekezaji wa India kuja kujenga hospitali kubwa za matibabu ya binaadamu na kujenga viwanda vya kutengeneza dawa za binadamu huku akibainisha kuwa hatua hiyo itasaidia kupunguza gharama za matibabu kwa watanzania na wananchi wa nchi nyingine jirani na Tanzania wanaolazimika kusafiri hadi nchini India kufuata matibabu.

"Wambie wafanyabiashara wa India walio tayari kujenga hospitali kubwa, waje na mimi nitawapa ardhi ya kujenga hospitali, wasipoteze muda waje sasa" Amesisitiza Rais Magufuli. 


Gerson Msigwa 
Kaimu Mkurugenzi wa Mawasiliano, IKULU 
Dar es Salaam 
30 Agosti, 2016

MKURUGENZI MKUU AZUNGUMZA NA WAFANYAKAZI

Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Nyumba la Taifa, Nehemia Mchechu akizungumza na wafanyakazi wa NHC wa Makao Makuu na Matawi ya Mkoa wa Dar es Salaam kwa niaba ya wafanyakazi wote wa Shirika na kuzungumzia mambo mbalimbali ya maendeleo ya Shirika, masuala mbalimbali yanayohusu ufanisi wa Shirika, utendaji wa wafanyakazi pamoja na motisha kwa wafanyakazi.
 Mkurugenzi wa Rasilimaliwatu wa Shirika la Nyumba la Taifa, James Rhombo akizungumza na wafanyakazi wa NHC wa Makao Makuu na Matawi ya Mkoa wa Dar es Salaam.
Wafanyakazi wa NHC wa Makao Makuu na Matawi ya Mkoa wa Dar es Salaam wakifuatilia Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Nyumba la Taifa, Nehemia Kyando Mchechu akizungumzia masuala mbalimbali yanayohusu ufanisi wa Shirika, utendaji wa wafanyakazi pamoja na motisha kwa wafanyakazi.
 Wafanyakazi wa NHC wa Makao Makuu na Matawi ya Mkoa wa Dar es Salaam wakifuatilia Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Nyumba la Taifa, Nehemia Kyando Mchechu akizungumzia masuala mbalimbali yanayohusu ufanisi wa Shirika, utendaji wa wafanyakazi pamoja na motisha kwa wafanyakazi.
 Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Nyumba la Taifa, Nehemia Mchechu akizungumza na wafanyakazi wa NHC wa Makao Makuu na Matawi ya Mkoa wa Dar es Salaam akizungumzia masuala mbalimbali yanayohusu ufanisi wa Shirika, utendaji wa wafanyakazi pamoja na motisha kwa wafanyakazi.
Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Nyumba la Taifa, Nehemia Mchechu akizungumza na wafanyakazi wa NHC wa Makao Makuu na Matawi ya Mkoa wa Dar es Salaam akizungumzia masuala mbalimbali yanayohusu ufanisi wa Shirika, utendaji wa wafanyakazi pamoja na motisha kwa wafanyakazi.
 Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Nyumba la Taifa, Nehemia Mchechu akizungumza na wafanyakazi wa NHC wa Makao Makuu na Matawi ya Mkoa wa Dar es Salaam akizungumzia masuala mbalimbali yanayohusu ufanisi wa Shirika, utendaji wa wafanyakazi pamoja na motisha kwa wafanyakazi.
 Wafanyakazi wa NHC wa Makao Makuu na Matawi ya Mkoa wa Dar es Salaam wakifuatilia Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Nyumba la Taifa, Nehemia Kyando Mchechu akizungumzia masuala mbalimbali yanayohusu ufanisi wa Shirika, utendaji wa wafanyakazi pamoja na motisha kwa wafanyakazi.

Monday, August 29, 2016

SERIKALI YAVIFUNGIA VITUO VIWILI VYA REDIO LEO JIJINI DAR


Na Zainab Nyamka, Globu ya Jamii.

WAZIRI wa Habari, Utamaduni , Sanaa na Michezo Nape Moses Nnauye amezifungia radio mbili kwa muda usiojulikana kwa makosa ya kuandaa vipindi ambavyo vimerushwa hewani vinavyoashiria uchochezi.

Akizungumza na waandishi wa habari, Waziri Nape amesema kuwa uamuzi wa kuvifungia vituo hivyo umefikiwa baada ya kujirdhisha kuwa kipindi cha Matukio kilichorushwa Agosti 25, 2016 muda wa saa 2 usiku hadi saa 3 na kituo cha utangazji cha Radio 5 pamoja na kipindi cha Morning Magic katika kipengele cha Kupaka Rangi Agosti 17 vilikuwa na maudhui ya uchochezi unaoweza kuleta uvunjifu wa Amani.

Nape amesema kuwa kufuatia hilo amevifungia kwa muda usiojulikana kwani wamekiuka masharti ya kanuni ya 5 (a, b, c na d) , kanuni ya 6 (2a, b na c) na kanuni ya 218 ya huduma za utangazaji ya mwaka 2005.

Wakati vituo hivyo vikifungiwa kwa muda usiojulikana kamati ya maudhui imepewa jukuu la kuviita na kusikiliza kwa kina Zaidi utetezi wao na ni hatua gani zaidi ya kuchukua dhidi yao kwa mujibu wa kanuni ya huduma za utangazaji.

Nape ameendelea kuvitahadhalisha vyombo mbalimbali vya habari kutoshawishika kuvunja sheria na kanuni zinazoongoza tasnia ya habari ili kulinda heshima ya tasnia yetu na wakati huo kuhakikisha nchi inabaki na Amani, Mshikamano na Umoja. 
Waziri wa Habari, Utamaduni , Sanaa na Michezo, Nape Moses Nnauye akizungumza na waandishi wa habari mapema leo, wakati akitangaza kuzifungia radio mbili kwa muda usiojulikana kwa makosa ya kuandaa vipindi na kuvirusha hewani ambavyo vinaashiria uchochezi. 

Waziri wa Habari, Utamaduni , Sanaa na Michezo Nape Moses Nnauye akitoa  ufafanuzi alipokuwa akijibu maswali mbalimbali ya Wanahabari,wakati alipokuwa akitoa taarifa ya kivifungia vituo viwili vya radio kwa muda usiojulikana kwa makosa ya kuandaa vipindi vyenye maudhui yenye viashiria vya uchochezi.
 Waziri wa Habari, Utamaduni , Sanaa na Michezo Nape Moses Nnauye akifafanua jambo kwa waandishi wa habari.Picha na Emmanuel Massaka,Globu ya jamii.