Monday, December 07, 2015

WATUMISHI WA UMMA KUSAINI KIAPO CHA AHADI NA UADILIFU


Katibu Mkuu Ofisi ya Rais-Utumishi Bw. HAB Mkwizu (kushoto) akizungumza na watumishi wa Ofisi ya Rais-Utumishi na Watendaji Wakuu wa ofisi zilizo chini yake katika kikao cha kuhimiza uwajibikaji kilichofanyika ofisini kwake.


Na Lilian Lundo-Maelezo

OFISI ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma imeanza rasmi kutekeleza Ahadi ya Uadilifu kwa watumishi wa Umma nchini ambao ulizinduliwa Agosti Mosi mwaka huu.

Akiongea na vyombo vya habari leo, Katibu Mkuu Hab Mkwizu amesema utekelezaji huo umeanza rasmi Disemba, 2015 ambapo kila mtumishi wa Umma ataweka saini ya kiapo kwa kuzingatia taratibu zilizowekwa na mazingira ya Taasisi husika.

“Utaratibu wa Utekelezaji wa Ahadi ya Uadilifu kwa watumishi wa Umma umetolewa kupitia waraka wa Mkuu wa Utumishi wa Umma Na. 2 wa mwaka 2015 kuhusu utekelezaji wa Ahadi ya Uadilifu kwa viongozi, watumishi wa Umma na sekta binafsi wa tarehe 1 Agosti, 2015.” Alisema Mkwizu.

Mkwizu aliongezea kwa kusema, uanzishwaji wa Ahadi ya Uadilifu ni muendelezo wa uundwaji wa vyombo vya kusimamia maadili baada ya ongezeko kubwa la ubadhirifu, utoro sehemu za kazi na kushuka kwa nidhamu katika kipindi cha miaka ya themanini na tisini.

Alivitaja vyombo vingine ambavyo vilianzishwa kusimamia ahadi na uadilifu kuwa ni Sekretariate ya Maadili ya Viongozi wa Umma, Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU).

Mkwizu alivitaja vipengele ambavyo mtoa ahadi anatakiwa kuvitamka ni, kuwa mzalendo wa nchi yake na kutii Serikali ya Jamhuri wa Muungano wa Tanzania, kuhudumia Umma na watumishi wenzake kwa heshima, kutimiza wajibu wa kutoa huduma bora kwa umma, kutoa huduma bora kwa usawa kwa watu wote na kutofanya ubaguzi wa dini, siasa, kabila, udugu, ukanda, jinsia, urafiki au hali ya mtu.

Vipengele vingine ni kutumia rasilimali za Umma kwa manufaa ya Umma, kutotoa siri za Serikali au mteja kwa watu wasiohusika isipokuwa kwa maslahi ya Umma, kufanya kazi kwa nidhamu ya hali ya juu, kutoomba kushawishi, kutoa wala kupokea rushwa na kutotumia madaraka kwa manufaa binafsi ya ndugu, rafiki au jamaa.

Aidha, Mkwizu ametoa wito kwa waajiri wote kuhakikisha kuwa utekelezaji wa Ahadi na Uadilifu unakamilika ifikapo tarehe 31/12/2015 na kuwasilisha Ofisi ya Rais – UTUMISHI kabla ya tarehe 25/02/2016 na utekelezaji wake kuwa kila ifikapo Juni 30 ya kila mwaka. Fomu za Ahadi ya Uadilifu zinapatikana katika tovuti ya Ofisi ya Rais – UTUMISHI yenye anwani www.utumishi.go.tz.

No comments: