Thursday, May 31, 2007

Breaking Newsss Flaviana





MWAKILISHI wa Tanzania kwenye mashindano ya Miss Universe, Flaviana Matata amewasili nchini leo na kupokewa kwenye Uwanja wa Ndege wa Mwalimu Nyerere jijini Dar es Salaam kwa nderemo, burudani kutoka kwa kikundi cha ngoma za asili cha Makumbusho Dancing Group.

Katika mashindano hayo, Flaviana alishika nafasi ya sita kati ya washiriki 77 kutoka nchi mbali mbali duniani.

Mratibu wa mashindano ya Miss Universe nchini, Maria Sarungi alikiri mashindano ya urembo ni bahati na kwamba pamoja na Flaviana kushika nafasi ya sita hakuwa na bahati ya kutwaa taji la dunia katika mashindano hayo.

Kutokana na kuingia 10 bora katika mashindano hayo, Flaviana ametwaa dola 500 za Marekani na kombe kutoka Kampuni ya Rogaska Crystal. Nachukua fursa hii kumpongeza Flavi huraaaaaa Mungu akujaalie usonge mbele zaidi na zaidi.

Mlimbwende wa Japan, Riyo Mori aliibuka kidedea katika mashindano hayo ambayo yalimalizika Jumatatu usiku mjini Mexico City, Mexico. PICHA IMEPIGWA FIDELIS FELIX

Wednesday, May 23, 2007

Flaviana aukaribia u-miss universe world

Mwakilishi wa Tanzania katika mashindano ya dunia ya Miss Universe, Flaviana Matata amezidi kung’ara katika mashindano hayo baada ya juzi kupewa nafasi ya kwanza ya kushinda kwenye mtandao wa Global Beauties (GB).

Flaviana ambaye aliwahi kushika nafasi ya pili akiwa na siku mbili tu tokea kuanza kwa zoezi hilo, mpaka sasa amekuwa gumzo kubwa miongoni mwa wawakilishi na wapenzi wa mashindano hayo duniani.

Mrembo huyo ambaye kwa sasa anashikilia taji la mrembo anayeonekana bora katika picha (Miss Photogenic) akiwa ni mshindi wa tano katika mtandao huo maarufu duniani katika masuala ya urembo.

Flaviana alifuatiwa na mrembo wa Venezuela katika nafasi ya pili na nafasi ya tatu ilikwenda kwa mrembo wa Hispania. Ugiriki ilishika nafasi ya nne, Serbia ya tano na Japan ya Sita na Marekani ya Saba.

Korea, Mexico na Russia zilishika nafasi ya nane, tisa na 10 katika upigaji kura huo. Nchi nyingine ya Afrika, katika 20 bora ilikuwa Angola ambayo ilifungana.

Wednesday, May 16, 2007

Jengo hili la walimu wasio na hadhi, inachekesha

KAMA kuna kitu ambacho pengine kimenipa faraja, lakini wakati huo huo kunipatia simanzi, basi ni lile jengo linaloitwa Mwalimu House, likibeba maana ya ‘Nyumba’ au ‘Jumba’ la mwalimu, ambalo lilizinduliwa wiki chache zilizopita.

Jengo hili la Mwalimu lilizinduliwa hivi karibuni na Rais Jakaya Kikwete, ni la kisasa na lenye kila kitu na hadhi kubwa, lakini bahati mbaya wamiliki wake wenyewe ni watu hohehahe, taabani, wanaoishi kwa taabu na shaka na yote inatokana na fani hiyo kukosa mwelekeo.

Matokeo yake, faini hiyo imepoteza heshima, haiheshimiki tena na hivyo kufanya kila anayehitimu chuo au elimu ya juu kufikiria mara mbili kabla ya kuichagua.

Sina budi kuanza kwa kuweka wazi kwamba kamwe siwaonei wivu wale wanaofaidi mavuno yaliyopandwa katika ghorofa hilo na wala lengo si kuwashambulia, wala sina nia mbaya na yeyote yue, bali ni kujaribu kufikiri kwa kina. Hivi, najiuliza, kwanini hali ya mwalimu inabakia kuwa hivi hadi leo.

Mmejenga jengo zuri, safi! Mnazungumzia matatizo yao, sawa. Lakini, kwanini hamsimamii haki za walimu hao wanaoishi kwa shida! Bonyeza hapa

Friday, May 11, 2007

Habari mpyaaaaaaa

Taarifa zilizotufikia muda si mrefu ni kwamba mrembo wetu flaviana matata anazidi kung'ara huko Mexico kwenye mashindano ya miss universe! amekuwa mshindi wa tano ktk Miss Universe-Photogenic ambayo ni hatua nzuri sana! Wadau Votes ziendelee..tunaweza kukawa na Miss Universe Jamani! bofya hapo chini kwa zaidi hapa

Tuesday, May 08, 2007

Soma interview ya Flaviana Matata Mexico

Flaviana Matata akiwa Mexico













Hii ni sehemu ya interview hiyo iliyotafsiriwa

Miss Universe: Ni kipi unachokipendelea na kipi kinakuvutia zaidi?

Flaviana: Napenda sana mitindo. Mitindo ndiyo kitu kikubwa kwangu. Muziki pia ni kitu kinachonivutia pia.

Miss Universe: Unatarajia kuwa nani maishani mwako?

Flaviana Matata: Matarajio yangu ni kuwa Mhandisi na pia kuwa mwanamitindo wa kimataifa na mbunifu wa mitindo.

Miss Universe: Elezea umezaliwa na kukulia wapi na maisha yako utotoni yalikuwaje.

Flaviana Matata: Nilizaliwa mjini Shinyanga katika familia ya kawaida . Shinyanga ni mkoa unaofahamika nchini kwetu kwa utajiri wa madini hasa almasi na pia mengine mengi kama dhahabu na kadhalika.

Maisha ya utotoni mwangu yalijaa furaha na vicheko na nilipenda sana kuthubutu kujifunza vitu vipya kila siku iendayo kwa Mwenyezi Mungu. Na mara nyingi nilitembelea migodi nikiwa mimi na familia yangu na hata na marafiki.

Miss Universe: Unataka kipi majaji wa mashindano haya wakifahamu kutoka kwako?

Flaviana Matata: Mimi ni mtaalamu wa masuala ya umeme kitaaluma na pia ni mwanamitindo nchini mwangu. Sipendi watu wanielezee vingine aidha kwa mavazi yangu au kwa nywele kwa kuwa naamini Mungu hakukosea kuniumba kama mwanamke wa kiafrika. Picha ni za mtandao wa miss universe kwa maelezo zaidi Bonyeza hapa au hapa hapa

Tuesday, May 01, 2007

Tucta: Serikali acheni kufanya anasa

KATIBU Mkuu wa Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi (Tucta), Nestory Ngulla, ameitaka serikali kupunguza matumizi ili iweze kuwalipa wafanyakazi wake mishahara minono itakayokidhi mahitaji yao.

Akihutubia katika sherehe za siku ya wafanyakazi katika uwanja wa Kirumba jijini Mwanza jana, Ngulla aliishauri serikali kupunguza safari za nje na za mikoani na kuacha kununua magari ya kifahari ili iongeze maslahi ya wafanyakazi.

Ngulla aliyasema hayo mbele ya Rais Jakaya Kikwete, aliyekuwa mgeni rasmi katika kuadhimisha sherehe hizo.

Alisema kwa kufanya hivyo, serikali itaweza kuongeza mshahara ya wafanyakazi kutoka kima cha chini cha Sh75,000 za sasa hadi Sh315,000 kwa mwezi.

Alisema serikali itafanikiwa kuongeza mshahara kwa wafanyakazi wake endapo pia itaacha kununua vitu vya samani, kupunguza semina na kuacha mpango wa misamaha ya kodi katika sekta mbalimbali na kuboresha hospitali ili watu waweze kutibiwa katika hospitali zetu na si kupelekwa nje.

Ngulla alisema endapo Serikali itafanya hivyo, itamudu mpango wa kuongeza mishahara ambayo itawawezesha wafanyakazi kumudu mahitaji yao ya kila siku. Pichani baadhi ya wafanyakazi wakiandamana kuadhimisha kilele cha sikukuu hiyo.